TAMKO LA
KAMATI KUU YA HALMASHAURI KUU YA TAIFA YA CCM KUHUSU UCHAGUZI MKUU WA ZANZIBAR
ULIOFANYIKA TAREHE 30 OKTOBA, 2005
- Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi imekutana katika kikao cha
dharura tarehe 7 Novemba, 2005 mjini Dar es Salaam kuzingatia miongoni mwa
mengine, Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar uliofanyika tarehe 30 Oktoba, 2005.
- Katika kikao
hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa CCM, Ndugu Benjamin William Mkapa,
Kamati Kuu imempongeza kwa dhati Ndugu Amani Abeid Karume kwa kuchaguliwa
na wananchi wa Zanzibar kuendelea kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi kwa kipindi cha pili. Ushindi wa asilimia 53.2
alioupata Ndugu Karume katika uchaguzi huo ni mkubwa na wa kujivunia hasa
ukizingatia mazingira ya kisiasa ya Zanzibar.
- Ushindi huo wa Ndugu
Karume ni kielelezo stahiki cha kukubalika kwake na jinsi wananchi
wanavyotambua na kuthamini mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi
cha miaka mitano ya uongozi wake. Aidha, ni uthibitisho wa kukubalika kwa
Chama Cha Mapinduzi na sera zake za amani, umoja, utulivu na maendeleo. Ni
ukweli ulio wazi kwamba, chini ya uongozi thabiti na shupavu wa Rais Amani
Abeid Karume, wananchi wa Zanzibar na Zanzibar kwa ujumla imepata utulivu
wa kuridhisha na maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii. Katika pembe
zote za Visiwa vya Unguja na Pemba upo ushahidi wa kutosha wa mafanikio
makubwa yaliyopatikana katika kuendeleza miundo mbinu na kuboreshwa kwa
huduma za jamii kama vile Elimu, Afya, Umeme, Maji, n.k. Uchumi umekuwa
unakua vizuri na kusababisha kuongezeka kwa ajira na kukua kwa pato la
watu.
- Aidha, Kamati Kuu
imewapongeza na kuwashukuru wananchi wa Unguja na Pemba kwa imani yao kwa
Chama Cha Mapinduzi na kukipa ridhaa ya kuongoza Zanzibar kwa kipindi cha
miaka mitano ijayo. Pamoja na kumchagua Ndugu Amani Abeid Karume, wananchi
wa Zanzibar wamewachagua wana-CCM 30 katika majimbo 50 kuwa Wajumbe wa
Baraza la Wawakilishi. Imani huzaa imani, CCM inawaahidi wananchi wa
Zanzibar na Watanzania kwa ujumla kwamba itahakikisha Serikali yake
inafanya vizuri zaidi ya ilivyokuwa miaka mitano iliyopita. Wakati huo
huo, Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa inatoa pongezi kwa wana-CCM 30
waliochaguliwa kuwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na wanawake 9 walioteuliwa
kuwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kupitia Viti Maalum.
- Kamati Kuu
imeipongeza pia Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa kwa kutoa
uongozi sahihi na Kamati ya Kampeni ya CCM Zanzibar kwa kuendesha kampeni
kwa ustaarabu, umahiri mkubwa na ufanisi wa hali ya juu. Mambo hayo ndiyo
ambayo yameleta ushindi. Katika mtiririko huo huo, Kamati Kuu imewapongeza
viongozi wa CCM wa ngazi zote na wanachama wote wa CCM wa Zanzibar kwa
uvumilivu wao, mshikamano na bidii kubwa, mambo ambayo yamekuwa chachu ya
ushindi huo.
- Kamati Kuu
imeridhika na kufurahishwa na jinsi zoezi zima la Uchaguzi Mkuu Zanzibar
lilivyoendeshwa. Hivyo basi, CCM inaungana na Waangalizi wa uchaguzi wa
kutoka ndani ya nchi na wenzao wa kimataifa kuipongeza Tume ya Uchaguzi
Zanzibar (ZEC) kwa kuendesha vizuri zoezi zima la Uchaguzi wa Rais,
Wawakilishi na Madiwani huko Zanzibar. Safari hii, maandalizi, uendeshaji,
utawala na mwenendo mzima wa uchaguzi vilikuwa bora zaidi kuliko wakati wa
chaguzi zilizopita. Kamati Kuu ya CCM imeridhika kuwa uchaguzi ulikuwa
huru na wa haki.
- Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM imefurahi kwamba Wapiga kura wengi sana
walijitokeza vituoni kupiga kura (zaidi ya asilimia 90) na upigaji kura
ulikuwa wa amani na utulivu. Watu walipiga kura kwa uhuru bila vitisho
wala shinikizo. Haki yao ya kupiga kura ya siri iliheshimiwa na kutimizwa
kwa ukamilivu. Mawakala wa vyama walikuwepo katika kila kituo cha kupigia
kura, jambo lililohakikisha kuwa maslahi ya vyama yanalindwa na
wasiostahili kupiga kura hawakuruhusiwa kupiga kura. Kila aliyepiga kura
alipakwa wino usiofutika kumzuia asipige kura tena. Vituo vya kupigia kura
vilifunguliwa kwa wakati na vifaa husika vilipatikana kama ilivyopasa.
Majina ya wapiga kura wa kila kituo yalibandikwa ukutani pembeni mwa kituo
wazi kwa kila mmoja kuona. Kura zilihesabiwa vituoni baada ya kukamilika
upigaji kura na vituo kufungwa. Zoezi la kuhesabu kura lilifanywa kwa
uwazi na kushuhudiwa na mawakala wa vyama vya siasa pale kituoni. Kwa
baadhi ya vituo, hata waangalizi wa uchaguzi waliokuwepo waliweza
kushuhudia. Kwa ajili hiyo, kila wakala aliondoka kituoni na matokeo
kamili. Isitoshe, matokeo ya kila kituo yalibandikwa ukutani nje ya kituo
kwa yeyote anayependa kujua aweze kuona. Mambo yalifanywa kwa uwazi wa
hali ya juu. Ni kutokana na ukweli huu CCM inaridhika kuwa uchaguzi
ulikuwa huru, haki na wa amani.
- Aidha, Kamati Kuu
inatambua kujitokeza kwa matatizo ya hapa na pale katika baadhi ya vituo,
hasa katika eneo la Mji Mkongwe. Tumeridhika kama walivyoridhika
Waangalizi wa Uchaguzi kuwa kasoro hizo ndogo ndogo katika maeneo machache
hazikuathiri mwenendo na matokeo ya uchaguzi mzima. Kamati Kuu inawasihi
wale wanaoitakia mema Zanzibar na Tanzania kwa ujumla wasizichukulie
kasoro zilizojitokeza katika vituo hivyo vichache vya eneo la Mji Mkongwe
kama ni kielelezo cha hali ilivyokuwa katika uchaguzi mzima wa Zanzibar.
- Kamati Kuu
imevipongeza vyombo vya dola kwa kusimamia vizuri hali ya usalama kiasi
cha kuwapa wananchi wa Zanzibar, waliokuwa wamegubikwa na vitisho vingi
vya viongozi na wafuasi wa CUF wakati wa kampeni, imani iliyowafanya
kujitokeza kwa wingi na kupiga kura zao kwa uhuru siku ya uchaguzi. Ukweli huu unathibitishwa na wingi wa
wanawake waliojitokeza kupiga kura vituoni.
- Kamati Kuu
imevipongeza vyombo vya habari, hasa vya ndani ya nchi, kwa jitihada kubwa
vilivyofanya kutoa taarifa za uchaguzi huo kwa uwazi, usahihi na bila
upendeleo.
- Kamati Kuu inatoa
wito kwa Chama cha CUF kukubali matokeo ambayo ni kauli halali ya uamuzi
wa wananchi wa Zanzibar. Vilevile, Kamati Kuu imesikitishwa na tabia
ambayo sasa inaelekea kuwa hulka ya Bwana Seif Shariff Hamad na Chama cha
CUF ya kukataa matakwa ya wananchi walio wengi. Hulka hii inadhoofisha
jitihada za kujenga na kuendeleza demokrasia nchini. Aidha, Kamati Kuu
imeelezea kufadhaishwa kwake na tabia na vitendo vya viongozi na wanachama
wa CUF vya kuchochea ghasia na kuvunja amani. CCM inatoa wito kwa viongozi
na wanachama wa CUF kuachana na muelekeo usiokuwa na maslahi kwa taifa
letu changa na watu wake.
- Kamati Kuu imetoa
wito kwa marafiki wa kweli wa Tanzania kuisadia nchi yetu iendelee kuwa na
umoja, amani na utulivu. Rafiki wa kweli wa Tanzania atajiepusha kufanya
vitendo au kuonekana anafanya vitendo au kutoa kauli zitakazochangia
kuleta mgawanyiko badala ya umoja na mshikamano au itakayochochea ghasia
katika jamii badala ya kuleta amani na utulivu. Tunawaomba marafiki zetu
wa kweli wasifanye vitendo au kutoa kauli zitakazowatia moyo na kuwapa
hamasa watu, vyama au vikundi vyenye nia mbaya ya kuchochea ghasia na tofauti
na mifarakano miongoni mwa Watanzania. Marafiki wanaotaka kuiona Zanzibar
na Tanzania kwa ujumla katika hali ya migogoro, hawawezi kujigamba kuwa ni
marafiki wa kweli wa nchi yetu.
- Wakati huo huo,
Chama Cha Mapinduzi kinatambua kwamba upo umuhimu wa kuendeleza jitihada
za kuleta umoja na kutafuta mustakabali wa kisiasa na kijamii Visiwani.
CCM inatambua kuwa hakuna majawabu ya mkato katika kufikia azma hiyo. Kama
vile ambavyo Muafaka umekuwa hatua muhimu katika kuwasogeza Wazanzibari
kuelekea kwenye azma hiyo, Chama Cha Mapinduzi hakitachoka kuendelea na
jitihada za kupata mustakabali endelevu kwa manufaa ya amani, utulivu na
maendeleo ya Zanzibar na nchi yetu kwa ujumla.
- Kwa mara nyingine
tena, Kamati Kuu imewashukuru wananchi wa Zanzibar kwa kuipa tena ridhaa
CCM kuendelea kuongoza. Kwa uamuzi wao huo, wamechagua sera za maendeleo
na kuzikataa sera za chuki na visasi. Kamati Kuu inawaomba wananchi wa
Zanzibar, bila kujali itikadi zao za kisiasa, watoe ushirikiano kwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa manufaa yao. Uchaguzi umekwisha na
uongozi umepatikana. Kilichobaki sasa kwa Wazanzibari ni kushikamana na
kukusanya nguvu zao kujenga nchi na kupambana na umaskini.
- Mwisho, Kamati
Kuu imeitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Ndugu
Amani Abeid Karume iendeshe shughuli zake za kuwatumikia na kuwaletea
maendeleo wananchi wa Zanzibar kwa kujiamini ikiwa na uhakika wa uhalali
kamili unaotokana na ridhaa ya wananchi.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI
Philip J. Mangula
KATIBU MKUU