Katibu
Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Ndugu Philip Mangula, amesema sababu kubwa ya CCM
kuendelea kukubalika nchini licha ya kuwepo utitiri wa vyama vingine vya siasa
ni uwezo kilionao katika kuoanisha nadharia na vitendo vinavyoendana na
mahitaji ya wakati husika.
Ndugu
Mangula amesema hayo leo mjini Dar es Salaam alipokutana ofisini kwake na
ujumbe wa wabunge Saba kutoka Bunge la
Marekani.
Amesema
mara kwa mara Chama Cha Mapinduzi kimekuwa kikifanya mapitio ya sera zake na
wakati fulani kimediriki hata kutoa tafsiri mpya kuhusu falsafa inayohimidi
itikadi yake ili kuona kama bado inaendana na matarajio ya umma.
Kwa
mfano amesema katika nyanja ya uchumi CCM
ilitafsiri upya dhana ya uchumi wa nchi kumilikiwa na umma ambapo
ulazima wa serikali pekee kuwa ndio imiliki njia kuu za uchumi wa Taifa lkwa
niaba ya wananchi uliondolewa.
Amesema
hivi sasa wananchi mmoja mmoja , vikundi, vyama vya ushirika na hata mashirika
yasiyo ya kiserikali wanaruhusiwa kushiriki katika kuendesha na kumiliki uchumi
wa nchi yao.
Hata
hivyo amesema pamoja na kuitafsiri upya dhana hiyo ya uendehsaji uchumi, itikadi ya CCM bado ni ile ile ya
Ujamaa na Kujitegemea na kwamba
serikali zote mbili zinatekeleza sera zenye mwelekeo wa itikadi hiyo.
Katibu
Mkuu wa CCM alitoa maelezo hayo baada ya wabunge hao kutaka kuelewa mazingira
yanayoifanya CCM iendelee kukubalika nchini licha ya kuwepo changamoto
anuwai za dunia ya utandawazi ambazo
zimeyalazimisha baadhi ya mataifa kuzitelekeza hata itikadi zao.
Akitaja
sababu nyingine ya CCM kuendelea kukubalika, Ndugu Mangula amesema ni ile tabia
ya chama na viongozi wake kupenda kusikiliza maoni ya umma.
Ndugu
Mangula amesema hata msimamo wa sasa wa CCM na serikali yake kuendelea
kusisitiza muundo wa muungano wa serikali mbili umetokana na kubaini kuwa hayo
ndiyo matakwa ya Watanzania walio wengi.
Amesema
kwa maongozi ya Chama Cha Mapinduzi, Serikali iliunda kamati ya jaji Kisanga
ili kukusanya maoni ya wananchi kuhusu jambo hilo. Amesema ripoti ya Kamati ilionyesha kuwa Watanzania walio wengi
wanapendelea Muungano wa Taifa la
Tanzania uwe wa serikali mbili na wala siyo muungano wa shirikisho lenye
serikali tatu.
Katibu
Mkuu wa CCM amewaambia Wabunge hao kwamba hakuna muujiza kwa mtu au chama
kukubalika na umma isipokuwa siri pekee ni kufanya mambo yanayowapendeza na
kutarajiwa na watu.
Wabunge
hao kutoka majimbo saba wanaowakilisha vyama tofauti vya siasa nchini Marekani
wakiwa wamefuatana na maofisa toka serikali za majimbo na serikali ya Marekani
walikuwepo nchini kwa ziara ya siku kumi inayomalizika leo na walikuja kwa
mwaliko wa Taasisi ya Bunge (Bunge Foundation).
Imetolewa
na:
Ofisi
ya Katibu Mkuu CCM
Ofisi
Ndogo Makao makuu DSM
18/5/2004