HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA BENJAMIN WILLIAM MKAPA, KWA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, DODOMA, 12 FEBRUARI 2004

 

 

Mheshimiwa Spika,

 

            Awali ya yote, napenda sote tuungane kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuweka hai tangu nilipohutubia Bunge hili Tukufu mara ya mwisho, tarehe 30 Januari 2002, hadi leo hii. Namshukuru pia kwa afya yangu inayoimarika siku hadi siku. Nanyi, Waheshimiwa Wabunge, nakushukuruni sana kwa salamu zenu za pole na dua kwa ajili ya afya yangu zilizowasilishwa kwangu na Mheshimiwa Spika wakati nikiwa nimelazwa hospitalini kule Uswisi.

 

Mheshimiwa Spika,

            Nilipohutubia wananchi, tarehe 31 Desemba 2003, niliwaambia kuwa ningependa katika kipindi cha uongozi wangu kilichobaki nielekeze nguvu zangu kwenye kuimarisha uendelevu wa mageuzi na mafanikio yetu, na unyumbulifu wa taifa letu kisiasa, kiuchumi na kijamii, pamoja na kuweka mkazo mpya kwenye kujenga uwezo wa Watanzania kutumia fursa za kujiendeleza ambazo mafanikio ya mageuzi yetu yanaziweka mbele yao.  Niliahidi pia kuwa, Inshallah, ningetafuta fursa ya kufafanua nini hasa nilichokuwa nazungumzia.

 

            Hakuna fursa iliyo bora kwa lengo hilo kuliko hii ya kuzungumza na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Bunge hili si tu mahali ambapo Watanzania wote wanawakilishwa, bali pia ni mshirika wangu mkuu katika kutekeleza yote ninayokusudia kuyafanya.  Na kwa vile nchi hii ni yetu sote, kiasi kwamba hata viongozi na wafuasi wa vyama vya upinzani nao hufaidi matunda ya kazi za Chama Tawala, na huhasirika tusipopiga hatua mbele, nimeomba viongozi hao wawe hapa kunisikiliza.  Kwa heshima naomba sasa niwatambulishe, na kuwaomba wasimame ili Waheshimiwa Wabunge nao wawatambue.

 

Mheshimiwa Spika,

            Napenda nianze kwa kurejea kwenye muhtasari nilioutoa kuhusu sura kuu za mwelekeo wa miezi 20 ijayo: 

 

·        Kwanza, kuongeza kasi ya kubadili mtazamo wa watumishi wa umma—kwenye Serikali Kuu na Serikali za Mitaa—ili wajue kuwa kazi yao ya msingi sasa ni kuwasaidia na kuwawezesha wananchi kujiendeleza.

·        Pili, kujenga na kuimarisha uwezo kitaifa wa udhibiti, uratibu na usimamizi wa uchumi wa soko.

 

·        Tatu, kufikiria upya haki za wanyonge wakiwemo wananchi walio katika sekta isiyo rasmi; hasa zile haki za kumiliki raslimali na mitaji, ikiwemo nguvu zao, na ardhi, kama mbinu ya kuwawezesha kuingia katika mfumo rasmi wa uchumi wa kitaifa.

 

·        Nne, kuweka kipaumbele kinachostahili kwenye mauzo nje ya nchi, ikiwemo kuongeza thamani yake kwa kuyasindika, na kukaribisha uwekezaji kwenye viwanda vitakavyotupatia haraka uwezo wa kufanya hivyo.

 

·        Tano, kuendelea kubainisha kero za wananchi, na kuondosha vikwazo vilivyo katika njia ya Watanzania walio tayari kujiendeleza.

 

Mheshimiwa Spika,

            Ningependa Waheshimiwa Wabunge waniunge mkono katika kuweka kipaumbele kwenye maeneo haya, na wawe wabia wa Serikali katika utekelezaji wake wa dhati. Nawaomba mambo mawili ya msingi kabisa:

 

·        Kwanza, nawaomba wazingatie wakati wote ukweli kuwa nchi yetu ni maskini, na kama alivyotuasa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tunapaswa kukimbia wakati wengine wakitembea.  Kwa kweli mimi nimechoka kila mara kusikia Tanzania inaitwa “moja ya nchi maskini kuliko zote”.  Inawezekana kuachana na sifa hiyo ya umaskini, lakini si kwa kasi yetu ya sasa.  Nchi nzima, ikiongozwa na Bunge hili, inapaswa kubadili gia, na tuonyeshe dunia kuwa baada ya kubuni sera na mwelekeo sahihi, sasa tunachochea mwendo kweli.  Sijengi hoja ya kugeuza Bunge hili kuwa muhuri wa Serikali.  Wala sithubutu.  Lakini najenga hoja ya mazingira ya kibunge yanayoiwezesha Tanzania kukimbia badala ya kutembea.  Najenga hoja ya “a sense of urgency”.

 

·        Pili, naomba katika kuzungumza na wananchi, na pamoja na Uchaguzi Mkuu ujao mwakani, sisi sote tusiwape matumaini kuwa ipo Serikali yenye majibu yote na uwezo wote.  Serikali ya aina hiyo haipo popote duniani.  Serikali haina muujiza wa peke yake.  Lakini inawezekana kupata muujiza wa kitaifa, kwa kushirikiana kutafuta ufumbuzi wa matatizo, kwa kujituma na kukubali wajibu wa kujiendeleza kama mtu binafsi, na kama jamii.  Dhana ya kwamba wajibu wa Serikali ni kutoa, na wajibu wa wananchi ni kushukuru, ni sawa na mbio za sakafuni, mwisho wake ni ukingoni. Dhana hiyo inaweza kumpatia mgombea kura, lakini haitotufikisha mbali kama taifa.

 

Hali ya Siasa

 

Mheshimiwa Spika,

              Baada ya miaka arobaini na mbili ya Uhuru wa Tanzania Bara, na miaka arobaini ya Mapinduzi ya Zanzibar, Tanzania imeuzatiti uhuru wake wa kisiasa, na kujenga umoja wa kitaifa usio na shaka, ambao kwa kiasi kikubwa umesaidia kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya amani na utulivu.

 

              Katika bara hili lenye historia ya vurugu za kisiasa na ghasia, Tanzania, iliyozaliwa mwaka 1964 kwa kuunganisha nchi mbili huru— Tanganyika na Zanzibar—hadi leo hii ndiyo Muungano pekee wa aina hiyo unaoendelea na kuweka hai matumaini ya umoja wa bara la Afrika.

 

              Serikali zetu zinabadilishwa kupitia sanduku la kura, kwa kuheshimu Katiba ya Taifa.  Hakuna Rais—Bara na Zanzibar—aliyeachia madaraka na kisha kulazimika kuikimbia nchi yake.  Wote wanaishi nasi, na wanaheshimiwa.

 

              Tanzania ni nchi ya kidemokrasia.  Serikali ya Awamu ya Tatu Tanzania Bara, na Awamu ya Sita Tanzania Zanzibar, zimefanya kazi kubwa kuimarisha misingi ya uhuru wa raia, demokrasia, haki na usawa, kwa mujibu wa Katiba.

 

              Siwezi kusema Tanzania sasa ni peponi.  Kote duniani vyama vya upinzani vinakuwa na malalamiko ya aina fulani dhidi ya Chama Tawala na Serikali yake.  Ni mambo ya kawaida kwenye ushindani wa kisiasa.

 

              Matatizo ya kisiasa Zanzibar, kufuatia Uchaguzi Mkuu uliopita, yametatuliwa kwa amani na majadiliano.  Matukio ya Januari 26 – 27, mwaka 2001, ambapo wenzetu walipoteza maisha yao, yamebaki kama kasoro na si hulka ya Watanzania.  Na kasoro ni kasoro—haifai kutukuzwa. Yaliyopita si ndwele, tugange yajayo.  Tunaandaa mfumo endelevu wa ushindani wa kisiasa ambao ni wa kistaarabu, huru na wa amani Zanzibar na Tanzania nzima.  Kwetu sisi, majadiliano ndiyo njia muafaka zaidi na ya uhakika ya kuendesha siasa huko tuendako. Kama alivyosema mshairi maarufu, Kahlil Gibran, “Tunapogeukiana na kushauriana tunapunguza idadi ya maadui zetu.” Mimi binafsi na Chama Cha Mapinduzi hatutaki uadui kwenye siasa. Tuko tayari kushauriana na kuelewana na wote wenye nia njema.

 

              Utayari wetu umedhihirika kwenye MWAFAKA baina ya vyama viwili vikuu, CCM na CUF, uliowekwa saini tarehe 10 Oktoba 2001 ambao umeendelea kuimarika, na umechangia kwa kiasi kikubwa utulivu wa kisiasa uliopo sasa Zanzibar, kielelezo kimojawapo kikiwa uchaguzi mdogo Mei 2003.  Naipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kutekeleza wajibu wake chini ya Mwafaka, na kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi yanayoonekana wazi. 

 

              Katika miezi ijayo tutapendekeza mabadiliko ya Katiba ambayo kwa maoni yetu yatasaidia kuimarisha demokrasia katika nchi yetu.  Tutatimiza pia ahadi yetu ya kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao.  Na tutazidi kuongeza nafasi na uwakilishi wa wanawake katika vyombo vya maamuzi. Kwa upande wa Bunge, ninakusudia idadi yao isipungue asilimia 30 ya Wabunge kabla sijaondoka madarakani.

 

              Lakini, Mheshimiwa Spika, yapo mambo mawili katika siasa nchini mwetu yasiyoniridhisha.  La kwanza, ni udhaifu wa vyama vya upinzani.  Miaka michache iliyopita nilielezea hofu hiyo kwa kofia yangu ya Urais.  Lakini nikajibiwa kuwa si kazi yangu kufikiria udhaifu wa vyama vya upinzani.  Mimi ninaamini wako Watanzania wengine walio na wasiwasi kama wangu, maana ama tunao ushindani wa kweli, wa timu zinazokaribiana kwa nguvu, au tunafanya mzaha.  Ni nia yangu CCM iendelee kutawala daima, lakini naelewa pia faida kwa taifa ya vyama vya upinzani makini vinavyoweza kutuamsha tusilale usingizi. Na CCM ikiwa macho, ni kwa faida ya wananchi na taifa.

 

Mheshimiwa Spika,     

              Jambo la pili linalonifadhaisha ni kauli za baadhi ya viongozi wa kisiasa na wanachama wao ambazo zinaonyesha kutojali thamani ya amani na utulivu nchini. Wapo hata wanaothubutu kuzungumzia damu kumwagika, japo sijasikia wakijitolea damu yao wenyewe, hata kwa jambo jema kama vile kutunisha akiba ya damu kwenye hospitali zetu!

 

              Pengine hakuna sifa muhimu kwa nchi yoyote kama sifa ya amani na utulivu.  Kiongozi, au mtu anayewania uongozi, lazima ajifunze kuheshimu thamani ya uhai wa raia.  Inachukua muda mrefu kwa nchi kujijengea sifa ya amani na utulivu, lakini ni rahisi sana kuibomoa, hasa ukipata viongozi wasiothamini uhai wa raia, walio tayari kuutumia kama ngazi ya kuingia madarakani. Katika nchi huru ya kidemokrasia hakuna uhalali wowote wa kutumia fujo na vurugu kutafuta madaraka.

 

              Naomba sana kuwa tunapoelekea kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa baadaye mwaka huu, na Uchaguzi Mkuu mwakani, tusithubutu hata kuwazia matumizi ya fujo na vurugu.  Na sisi Serikalini, wenye dhamana ya utulivu na usalama nchini, hatuwezi kuruhusu siasa za fujo na vurugu.  Ni wajibu wetu kikatiba kudumisha amani na usalama nchini kote.

           

Serikali za Mitaa

 

Mheshimiwa Spika,

              Tunataka kuhakikisha kuwa vikwazo dhidi ya ushiriki wa wananchi kwenye utawala na maendeleo ya nchi yao vinaondolewa.  Maana demokrasia si siasa tu, demokrasia ni uchumi vile vile.  Kwa asiye na chakula, demokrasia ni anasa. Kwa wananchi walio wengi demokrasia inayowagusa moja kwa moja, na inayohusu maisha yao ya kila siku na mustakabali wao, ni Serikali za Mitaa.  Demokrasia ni madaraka kwa wananchi.  Na ibara ya 146(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaeleza wazi kuwa “Madhumuni ya kuwapo Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi.”  Kwa sababu hiyo, Serikali ilibuni na inaendelea kutekeleza Mpango wa Uboreshaji wa Mfumo wa Serikali za Mitaa ili kuhakikisha kuwa Halmashauri za Wilaya na Miji zinawajibika kwa wananchi, pamoja na kutoa huduma bora zaidi kwao na kurahisisha jitihada zao za kujiendeleza.

 

Mheshimiwa Spika,

              Kielelezo cha utashi wa kisiasa kuimarisha Serikali za Mitaa ni kiasi cha fedha kinachokabidhiwa kwa Halmashauri.  Kumekuwa na ongezeko kubwa sana—mara 24—la ruzuku ya Serikali Kuu kwa Serikali za Mitaa kutoka Sh.12.3 bilioni mwaka 1995/96 hadi Sh. 292 bilioni mwaka huu wa fedha.  Huu ni uwezeshaji kimapato, utokanao na mafanikio ya mageuzi yetu ya uchumi. 

 

              Upo pia uwezeshaji kielimu.  Mafunzo ya kuimarisha utendaji yametolewa kwa Wakuu wa Mikoa wote, na baadhi ya Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tawala wa Mikoa.  Mpango wa mafunzo ya Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa, Vitongoji na Maafisa Watendaji wa Vijiji umeandaliwa.  Hadi sasa viongozi 72,000 wa Vijiji, Mitaa na Vitongoji wamepatiwa mafunzo ya kuimarisha utawala bora. Madiwani 3,447 na Maafisa Watendaji wa Kata 2,303 nao wamepatiwa mafunzo.  Aidha, Wakurugenzi wa Halmashauri zote wamepatiwa mafunzo kuhusu usimamizi wa mabadiliko.  Na yote hayo yanawezekana kutokana na mafanikio ya mageuzi yetu ya kiuchumi.

 

              Mafanikio hayo pia yamesaidia uwezeshaji kiutendaji.  Kwa mfano, Makatibu Tarafa wote wamepewa pikipiki ili kuwawezesha kusimamia vizuri shughuli za maendeleo.  Pikipiki hizo zisingepatikana kama si mageuzi ya uchumi tuliyoyafanya.

 

              Sera zetu na mageuzi yetu vimetujengea mahusiano mazuri na wahisani wanaotusaidia kutekeleza Mpango huu wa Uboreshaji Serikali za Mitaa.  Aidha, mapato ya Serikali ambayo yameongezeka sana baada ya mageuzi hayo ndiyo yamewezesha Serikali Kuu kugharamia uwezeshaji wa Halmashauri nilioutaja hapa. Ni mafanikio ya mageuzi hayo ndiyo vile vile yaliyoipa Serikali uwezo wa kufuta kodi mbalimbali zilizokuwa kero kwa wananchi kwa miaka mingi. Wanaokebehi mageuzi waulizwe, ingewezekanaje?

 

Mabadiliko ya Fikra na Usimamizi wa Uchumi wa Soko

 

Mheshimiwa Spika,

              Jambo jingine ambalo nitalitilia mkazo katika kipindi changu kilichobaki ni mabadiliko ya fikra ya viongozi na watendaji wa Serikali, pamoja na Serikali za Mitaa, kuhusu nafasi ya sekta binafsi.  Kila kiongozi na mtumishi wa Halmashauri anapaswa kujua kuwa maslahi yake binafsi, na maendeleo ya wilaya au mji unaohusika, vinategemea sana mafanikio ya uwekezaji, uzalishaji, huduma na biashara.  Wakati umefika sasa kwa Halmashauri kushindana kwa dhati miongoni mwao katika kuvutia wawekezaji na wafanyabiashara. Watumishi wa umma waelewe kuwa nyakati zimebadilika, na tunahitaji mbinu mpya kukabiliana na changamoto za leo na zijazo.

 

              Ipo hadithi ya bwana mmoja aliyekuwa anatembea barabarani. Akamsimamisha mtu mmoja na kumuuliza wakati. Mtu yule akaangalia saa yake na kumjibu, “Hivi sasa ni saa 10:00.” Yule bwana aliyeuliza akakuna kichwa na kusema, “Unajua, ninyi wenye saa mnanichanganya kweli. Siku nzima ya leo nimekuwa nauliza watu wakati, na kila mara ninapewa jibu tofauti!”

 

              Na mimi nawaambia watumishi wa umma kuwa wasiwalaumu wenye saa, wala wasichanganyikiwe. Ukweli ni kuwa nyakati zinabadilika haraka, na majibu lazima yabadilike.

 

Mheshimiwa Spika,

              Hivi sasa ni kama vile kila mmoja anakubali kwa wepesi kuwa uwekezaji mkubwa na biashara mahali pake ni Dar es Salaam.  Hivi leo Mkoa wa Dar es Salaam, na hususan Jiji la Dar es Salaam, huchangia karibu asilimia 82 ya mapato yote ya Serikali.  Hali hii si nzuri hata kidogo.  Chanzo cha maendeleo ni uwekezaji, uzalishaji, huduma na biashara.  Kwa kadri mambo hayo yanavyofanyika Dar es Salaam, ndivyo maendeleo yatakavyoelekea Dar es Salaam, na kuzidi kuwavuta vijana toka pande zote za nchi kuja Dar es Salaam kwa matumaini kuwa huko ndiko kwenye uwekezaji, na hivyo kwenye ajira; na kwamba huko ndiko kwenye maendeleo na hivyo maisha bora.  Bila Halmashauri kwenye mikoa mingine kufanya bidii kuvutia uwekezaji huko waliko, tatizo hili haliwezi kwisha na hakutakuwa na usawa wa kijiografia kwenye maendeleo ya taifa.

 

            Ndio maana nachukua fursa hii kuupongeza Mkoa wa Kilimanjaro kwa kuwa mstari wa mbele kujiandaa kuvutia wawekezaji, na kuitisha Kongamano la Uwekezaji Kilimanjaro lililofanyika tarehe 14-15 Agosti 2003.

 

Lakini, Mheshimiwa Spika, uchumi wa soko lazima udhibitiwe kwa maslahi ya taifa na walaji. Ili kuwalinda wateja na kuhakikisha kunakuwa na ushindani wa haki kwenye biashara, Serikali imeanzisha mashirika manne ya usimamizi ambayo ni: Mamlaka ya Usimamizi wa Huduma za Maji na Nishati (Energy and Water Utilities Regulatory Authority -EWURA), Mamlaka ya Usimamizi wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Surface and Marine Transport Regulatory Authority- SUMATRA), Mamlaka ya Usimamizi wa Huduma za Mawasiliano (Tanzania Communication Regulatory Authority-TCRA), na Mamlaka ya Serikali ya Tanzania ya Usimamizi wa Usalama wa Usafiri wa Anga (Tanzania Government Aviation Regulatory Authority-TGARA). Mamlaka hizi na nyingine zote zitahitaji kuimarishwa sana katika siku zijazo.

 

Hali ya Uchumi

 

Mheshimiwa Spika,

            Kwa ujumla, uchumi wa Tanzania umeendelea kuboreka katika miaka ya hivi karibuni, kufuatia utekelezaji wa kina uliofikiwa katika marekebisho mbalimbali ya uchumi na sekta ya fedha.  Viashiria vya mafanikio ya hivi karibuni, yaliyoleta kutengamaa kwa uchumi mpana, ni pamoja na kuongezeka kwa mitaji katika sekta za umma na sekta binafsi, na kuongezeka kwa akiba ya fedha za kigeni na kujenga uwezo wa kutosha kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa miezi 7 – 8 hivi sasa ukilinganisha na miezi 6.3 katika mwaka 2001.

 

            Kuanzia mwaka 1990 hadi Desemba 2003, Kituo cha Uwekezaji (TIC) kimeidhinisha jumla ya miradi 2,527, inayokadiriwa kutoa nafasi za ajira 497,539.  Kati ya miradi hiyo, miradi 1,809 ilikuwa mipya, na miradi 718 ni ya upanuzi na ukarabati. Miradi 1,113 (asilimia 44) inamilikiwa na wawekezaji wa ndani ya nchi, miradi 609 (asilimia 24) ni ya wawekezaji wa nje, na miradi 805 (asilimia 32) ni ya ubia kati ya wawekezaji wa ndani na wa nje.

 

            Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa imeendelea kuongezeka, kutoka asilimia 3.3 katika mwaka 1997 hadi kufikia asilimia 6.2 mwaka 2002.  Wastani wa ukuaji huu wa kiuchumi wa asilimia 5.6 kwa mwaka kwa miaka mitatu mfululizo unatia moyo, hasa ukilinganishwa na wastani wa ukuaji wa uchumi barani Afrika wa asilimia 3.4 katika kipindi hicho. 

 

            Kwa sababu ya ukame uliotupata, inakadiriwa kuwa mwaka 2003 uchumi umekua kwa asilimia 5.7, na mfumuko wa bei umeongezeka kidogo kutoka wastani wa asilimia 4.5 mwaka 2002 hadi asilimia 4.6 mwezi Desemba 2003. Kwamba ukame huu haukuathiri sana utulivu wa uchumi mkuu ni ishara ya mafanikio makubwa ya mageuzi yetu ya uchumi.   Tutaendeleza mageuzi hayo, na tutayaimarisha ili kamwe tusirudi nyuma tulikotoka.

 

Mheshimiwa Spika,

              Sababu kubwa ya Azimio la Arusha kusema “Fedha si msingi wa maendeleo”, ni kwa vile tulikuwa hatuna fedha.  Likasisitiza kuwa huwezi kupanga maendeleo kwa kutegemea kitu ambacho huna.  Ni hoja nzito, na ya haki kabisa.

 

              Lakini dunia inabadilika, na mahitaji ya maendeleo nayo hubadilika.  Kwenye orodha ya mambo ambayo Azimio lilituambia ni muhimu kwa maendeleo—yaani ardhi, watu, siasa safi, na uongozi bora—napenda niongeze jingine, nalo ni mitaji.  Ipo mitaji ya aina nyingi.  Mtaji wa maskini ni nguvu zake.  Lakini wakati umefika pia kutumia siasa safi na uongozi bora kuongeza upatikanaji wa mitaji ya fedha.

 

              Sote tutakumbuka hali ya uchumi ilivyokuwa mwaka 1995.  Na wala sisemi hivyo kwa kulaumu.  Nimlaumu nani wakati mimi pia nilikuwa sehemu kamili ya Serikali zilizopita nikiwa Waziri kwa miaka mingi? 

 

            Lakini ukweli ni kuwa wakati ule ukuaji wa Pato la Taifa ulikuwa chini ya asilimia 3 kwa mwaka, mfumuko wa bei ulikuwa karibu asilimia 30, akiba ya fedha za kigeni ilikuwa ndogo isiyotosha hata miezi minne ya thamani ya bidhaa na huduma kutoka nje, Serikali ilikuwa inakusanya mapato yasiyozidi wastani wa Sh. 25 bilioni kwa mwezi, nidhamu ya matumizi ya Serikali na usimamizi wa fedha za umma ilikuwa ndogo sana, uwajibikaji Serikalini na katika Sekta ya Umma kwa ujumla ulikuwa mdogo, na Serikali ilikuwa inadaiwa kulia na kushoto, nje na ndani ya nchi.  Aidha, ushirikiano kati ya Serikali na Sekta Binafsi ulikuwa wa kiwango cha chini, na uwekezaji ulikuwa unasuasua.  Misaada ya nje ilikuwa michache na ilipatikana kwa masharti magumu. Kweli yupo anayetaka turudi huko? Kiongozi, msomi au mwandishi habari aliye makini atakosaje kulinganisha tulikotoka na tulipo leo?  Ni kweli bado kuna kazi kubwa ya kufanya. Lakini hiyo si sababu ya kupuuza yaliyofanyika.

 

Mheshimiwa Spika,

            Mojawapo ya mambo ya mwanzo yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tatu ilikuwa kubuni sera na mikakati itakayoongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani ili Serikali iweze kuboresha huduma za uchumi na za jamii na hivyo kusaidia jitihada za kupunguza umaskini.  Tuliimarisha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kuipa madaraka kamili ya kukusanya mapato bila kuingiliwa na Serikali.  Aidha, Serikali ilianzisha utaratibu thabiti wa majadiliano na wadau, hasa walipa kodi wakubwa, kuhusu sera za kodi na utawala wa ukusanyaji wa kodi. Matokeo yake leo TRA inakusanya wastani wa Sh. 108 bilioni kwa mwezi, ikilinganishwa na Sh. 25 bilioni mwaka 1995.  Hadi mwisho wa mwezi uliopita, pamoja na matatizo ya ukame, TRA ilikuwa imeshavuka lengo lake la miezi 7 ya kwanza ya mwaka huu wa fedha kwa kukusanya Sh. 788.3 bilioni ikilinganishwa na lengo la Sh. 757.4 bilioni. Yaani wamevuka lengo kwa karibu Sh. 30.9 bilioni. Naomba Bunge hili liungane nami kuwapongeza kwa dhati kabisa viongozi na watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kazi nzuri, na kuwataka waendelee mbele. Tuna kazi ya kupiga vita umaskini.

 

Jambo la pili lilikuwa kurejesha mahusiano mazuri na nchi wafadhili na mashirika ya fedha ya kimataifa.  Leo tunapata misaada yenye thamani zaidi ya mara nne ya ile tuliyokuwa tunapata kabla ya 1996.  Aidha, Tanzania ilikuwa moja ya nchi nne za kwanza kufuzu mtihani wa kufutiwa madeni chini ya mpango wa HIPC, jambo ambalo limetuongezea uwezo wa kutoa huduma za uchumi na za jamii.  Fedha zinazotolewa kwa sekta za kipaumbele kwenye vita dhidi ya umaskini, ikiwemo elimu, afya, barabara, maji, vita dhidi ya UKIMWI na kilimo, sasa ni mara nne zaidi ya kiwango cha mwaka 1996.

 

Tumeimarisha nidhamu katika matumizi ya fedha za Serikali, kwa kuamua kutumia kile tu tulichonacho.  Nalishukuru Bunge hili Tukufu kwa kupitisha sheria mbili muhimu kwa nidhamu na usimamizi bora wa fedha za Serikali: Sheria ya Fedha za Umma (Public Finance Act 2001), na ile ya Ununuzi wa Umma (Public Procurement Act 2001).  Sheria hizi mbili zimeimarisha nidhamu na utawala bora kiasi kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi maskini zinazosifiwa sana kwenye eneo hili.

 

Mheshimiwa Spika,

Uchumi mpana tulivu ni nyenzo muhimu sana ya kuvutia uwekezaji, kuchochea ukuaji wa uchumi, kupanua nafasi za ajira, kuongeza mauzo ya nje, kuongeza mapato ya Serikali na kuongeza misaada ya nje pamoja na mikopo yenye masharti nafuu.  Uwezeshaji wananchi kimitaji nao unahitaji ushindani kwenye sekta ya fedha.  Tumepiga hatua kubwa ukizingatia tulikotoka. Benki za biashara sasa ziko 26, taasisi nyingine za fedha ziko 6, kuna kampuni za bima zaidi ya 10, tumeanzisha Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF) unaoongezea kwenye huduma inayotolewa na mifuko iliyopo ya PPF, NSSF na LAPF, soko la mitaji limeanzishwa na linakua, ipo sera mpya ya mikopo midogo midogo, umeanzishwa mfuko wa kudhamini mikopo kwa sekta za kipaumbele ambazo ni pamoja na vyama vya ushirika na kampuni zinazozalisha bidhaa maalum kwa ajili ya kuuza nje, na umebuniwa mfuko wa hisa za pamoja (Unit Trust of Tanzania). Maeneo haya yote yana mchango mkubwa katika kukua kwa uchumi, na kuwawezesha Watanzania kimitaji.  Nitakazania sana eneo hili katika siku zijazo.

 

Mheshimiwa Spika,

              Tusisahau tulikotoka, na wala tusione haya kujivunia mafanikio yetu.  Lakini kamwe tusiridhike, maana ukweli ni kuwa bado ipo kazi kubwa mbele yetu, na matatizo bado ni mengi.  Lakini tumeweka msingi mzuri, na hakuna sababu ya kukosa ujasiri na kuanza kuangalia nyuma.  Katika miaka michache ijayo, tutaweka mkazo katika maeneo yafuatayo:-

 

1.      Kuchochea uwekezaji na ukuaji wa uchumi kwa kasi kubwa zaidi. Asilimia 6 haitoshi.  Tunataka kufika asilimia 8 na kuzidi.  Huduma za benki na vyombo vya fedha zitatakiwa kurahisisha upatikanaji mitaji na kushiriki kuvutia wawekezaji wa ndani na nje. Marekebisho ya Sheria ya Ardhi yatasaidia. Bajeti ya Serikali nayo itatumika kuboresha miundombinu na kuondosha vikwazo vingine vya uwekezaji na biashara.

 

2.      Tutatumia bajeti ya Serikali kuchochea upatikanaji wa ajira kwa kutumia sera za mapato na matumizi, hasa kupitia mifuko ya udhamini wa mikopo kwa wawekezaji wadogo na wa kati.

 

3.      Bajeti ya Serikali pia itatumika kama kichocheo cha kuinua uzalishaji wa kilimo kwa njia za udhamini na uwezeshaji, hasa kuhusu upatikanaji wa pembejeo na mbegu.

 

4.      Tutaendelea kuboresha usimamizi wa fedha za Serikali ili mapato yanayoongezeka kutokana na mafanikio ya mageuzi yetu yatumike kwa ufanisi katika vita dhidi ya umaskini na kuwezesha wananchi kujiendeleza.

 

5.      Kwa kadri uchumi unavyokua, na ukusanyaji kodi unavyoboreshwa, tuna lengo la kuongeza mapato ya Serikali kutoka asilimia 12 ya Pato la Taifa hivi sasa hadi asilimia 15 ifikapo mwaka 2006, na asilimia 18 ifikapo 2008. 

 

6.      Tutaanzisha mpango wa kubainisha na kutambua kisheria mitaji na raslimali za watu walio katika sekta isiyo rasmi, pamoja na kubaini na kuondoa vikwazo vinavyofanya iwe vigumu kwao kuingia kwenye sekta rasmi, inayotambuliwa kisheria.

 

Vita Dhidi ya Umaskini

 

Mheshimiwa Spika,

              Umaskini una sura nyingi—upo umaskini wa kukosa kauli katika masuala yanayomhusu mtu; na upo umaskini wa kipato, miongoni mwa sura nyingine za umaskini.

 

              Nimekuwa Rais kwa zaidi ya miaka 8 sasa.  Na mambo mawili kuhusu umaskini yananitatiza sana kinadharia.

 

              La kwanza, ni namna ya kupima umaskini.  Wengi wanapenda kutumia kigezo cha mapato, tena kwa dola za marekani, kwa siku.  Lakini hicho ni kigezo finyu sana, na kisicho sahihi hata kidogo.  Ni kipimo kinachokazania umaskini wa kipato tu, wakati umaskini hauna sura ya mapato peke yake.  Isitoshe, kwa uchumi uliojikita kwenye sekta isiyo rasmi, kuna uhakika gani kuwa takwimu zetu zinabeba ujumla wa mali na raslimali za jamii zetu? Mfugaji wa Kitanzania anaweza kuwa anahama kila baada ya miezi michache, nyumba yake wala haistahili kuitwa nyumba, na mfukoni hana pesa.  Lakini anao ng’ombe 500.  Halafu anaambiwa anaishi kwa chini ya dola moja kwa siku!

 

              Mimi nafikiri wakati umefika tuwe na tafsiri ya umaskini inayozingatia mazingira yetu.

 

              Jambo la pili linalonitatiza linahusu swali la msingi kabisa.  Hivi hasa vita dhidi ya umaskini inapiganwaje?  Na, ni nani hasa mwenye wajibu wa msingi kupigana na umaskini?  Maana huishi kusikia au kusoma kwenye vyombo vya habari kuwa Serikali haipigi vita umaskini, au mageuzi hayasaidii kupiga vita umaskini.

 

              Ninyi, Waheshimiwa Wabunge, ni wawakilishi halali wa wananchi.  Naomba mnisikilize vizuri.  Umaskini wa kauli unapigwa vita kwa kuwapa watu kauli.  Lakini umaskini wa kipato haupigwi vita kwa kuwagawia watu pesa!

 

              Mtaniwia radhi, lakini lazima niweke jambo hili wazi, maana utakuta mtu mzima, mwenye akili timamu, anauliza:  “Kama mageuzi yamefanikiwa mbona sina pesa mfukoni?  Serikali ina mpango gani?  Serikali hii haipigi vita umaskini.”

 

              Ukweli ni kuwa anayekuahidi kuwa Serikali inaweza kukuondolea umaskini wa kipato anakudanganya.  Nchi hii haiwezi kushinda umaskini wa kipato kwa hadaa kama hizo, hadaa zinazowafanya wananchi wabweteke, wasijitume vya kutosha wakingojea msaada.  Serikali makini haifanyi hivyo.

 

              Yapo mambo makuu manne niliyoyaahidi kwa nyakati mbalimbali kama mkakati wa vita dhidi ya umaskini:

 

·      Kwanza, ni kuwapa watu kauli juu ya mambo yanayowagusa, ikiwemo ushirikishwaji wa kidemokrasia katika kupanga, kusimamia na kutekeleza miradi ya maendeleo, hususan ile ya kuondoa kero zao.  Miradi mikubwa kama TASAF na MMEM imejengwa imara juu ya dhana hii, kama ulivyo mpango wa kuboresha Serikali za Mitaa.

 

·      Pili, ni kuweka mazingira bora ya uchumi kukua na ajira kupatikana, ikiwemo mazingira yanayovutia uwekezaji na kurahisisha biashara.

 

·      Tatu, ni kupeleka kiasi kikubwa zaidi cha bajeti ya Serikali kwenye maeneo muhimu kwa vita dhidi ya umaskini, ambayo tumekubaliana kitaifa kuwa ni elimu, afya, maji, barabara za vijijini, na UKIMWI. 

 

·      Nne, ni kuweka mazingira mazuri kwa wananchi kujiendeleza, ikiwemo kwa kubaini na kisha kuondosha vikwazo vyote kwa wananchi wanaotaka, na walio tayari, kujiendeleza.

 

 

Mheshimiwa Spika,

              Nafurahi wanapojitokeza wananchi kutathmini vita dhidi ya umaskini niliyoahidi kuiongoza.  Lakini wafanye tathmini ya haki, kwa yale niliyoahidi.  Niliyoyataja hapa niliyaahidi, na niko tayari kupimwa nayo. Lakini sikuahidi, wala Chama changu hakikuahidi,  kuweka fedha mifukoni mwa watu.  Tuliahidi fursa, na fursa zinawafaa wanaozitumia. Haziwezi kuwafaa wasiozitumia.

                  

Ushirika

 

Mheshimiwa Spika,

              Idadi kubwa ya Watanzania ni wakulima, wafugaji na wavuvi.  Kwa hawa, na kwa hali halisi ya nchi yetu, ipo njia moja tu ya uhakika ya kuwawezesha kutumia fursa za kujiendeleza katika mazingira ya uchumi wa soko.  Njia hiyo ni ushirika.  Pamoja na matatizo yote yaliyovisibu vyama vya ushirika bado ukombozi wa uhakika wa wakulima, wafugaji, wavuvi na wafanyabiashara ndogondogo ni umoja kupitia ushirika.  Nguvu ya mnyonge ni umoja. 

 

              Mwaka 2000 niliitisha kongamano kuhusu ushirika kule Mwanza kuchambua matatizo ya ushirika, na kuyatafutia ufumbuzi ili ushirika ukidhi matarajio yetu ya kuimarisha umoja wa wanyonge, umoja ambao ndio uwezeshaji wao.

 

              Ninalishukuru Bunge hili Tukufu kwa kupitisha Sheria mpya ya Ushirika mwezi Novemba 2003 ambayo inaweka mazingira mazuri ya kuimarisha ushirika, na kuwapa wanachama kauli kubwa zaidi ya kidemokrasia katika uendeshaji wa vyama vyao.  Sheria hii pia itasaidia kudhibiti wizi na ubadhirifu, mambo ambayo huko nyuma yalihujumu ushirika kwa kuwavunja moyo wanachama.

 

              Lakini, sera na sheria zitakuwa na maana tu iwapo wanachama wenyewe watakuwa jasiri kudhibiti viongozi wao na mwenendo wa ushirika wao. Hivyo, tumeanzisha Mpango wa Elimu ya Ushirika Shirikishi ili kuwajasirisha wanachama, kuwapa mbinu za ujasiriamali, na mbinu za kusimamia vizuri zaidi vyama vyao. 

 

Mheshimiwa Spika,

              Sera ni muhimu.  Sheria ni muhimu.  Na uwezeshaji kielimu ni muhimu.  Lakini mitaji nayo ni muhimu.  Hali ya mitaji ya vyama vingi vya ushirika, hasa vya mazao ya kilimo, ni mbaya sana.  Hivyo, Serikali imeamua kuvisaidia na kuviwezesha vyama hivyo kimitaji kupitia utaratibu wa Udhamini wa Mikopo kwa Mauzo ya Nje (Export Credit Guarantee Scheme) unaoviwezesha kukopa fedha za kununulia mazao ya wakulima, na kuyauza nje ya nchi.  Kwa utaratibu huu, vyama vya ushirika vilikopeshwa Sh.10.1 bilioni na CRDB mwaka 2002/03. Mwaka huu, 2003/04, vyama vimekopeshwa Sh.16.3 bilioni na CRDB na Benki ya Ushirika Kilimanjaro (Kilimanjaro Cooperative Bank).  Nazishukuru Benki hizi kwa kushirikiana nasi, na navionya vyama vya ushirika visithubutu tena kutumia mikopo hii nje ya makusudio yake, na wahakikishe wanailipa kwa wakati.

 

Mheshimiwa Spika,

              Huu ni ufumbuzi wa muda mfupi wa matatizo ya mitaji.  Ufumbuzi wa kudumu ni kujenga uwezo wa mitaji ndani ya vyama vyenyewe.  Huo ndio utakuwa uwezeshaji wa kudumu.  Vyama vya ushirika vya kuweka na kukopa ni jibu la uhakika la tatizo la mitaji.  Tumeweka mkazo mkubwa sana kwenye jambo hili, na mafanikio yameanza kuonekana.  Vyama vya Akiba na Mikopo vimeongezeka kutoka 803 mwezi Juni 2000 hadi 1,264 mwishoni mwa 2003, sawa na ongezeko la asilimia 57 katika kipindi cha miaka 2½ tu.  Hisa na akiba kwenye vyama hivyo nazo zimeongezeka kutoka Sh.14.0 bilioni hadi Sh.25.7 bilioni, ongezeko la asilimia 83.  Mikopo nayo ikaongezeka kutoka Sh.11.5 bilioni hadi Sh.28.5 bilioni, sawa na ongezeko la asilimia 117. Huu ndio uwezeshaji wanyonge kimitaji, na utawanufaisha walio tayari kushirikiana na wenzao. Wasiotaka kushirikiana watabaki kulalamika.

 

Mheshimiwa Spika,

              Pamoja na kuviwezesha vyama vya ushirika kwa kuviwekea mazingira bora ya kisera na kisheria, na pamoja na kuviwezesha kielimu na kimitaji, tutaweka mkazo pia kwenye ukaguzi ili kuhakikisha kuwa mali na fedha za vyama zinatumika vizuri, kwa ufanisi, kwa manufaa ya wanachama badala ya manufaa binafsi ya viongozi.

 

Mheshimiwa Spika,

              Wapo wanaouliza faida ya mageuzi yetu ya kiuchumi ni nini kwa wananchi wa kawaida.  Nasema, utashi wa wazi wa kisiasa wa kuwasaidia wanyonge kupitia ushirika, mapato ya Serikali yalioongezeka na kutuwezesha kugharamia uwezeshaji kwenye  ushirika kama nilivyoelezea hapa, na mageuzi kwenye sekta ya fedha yaliyowezesha vyama vya ushirika kukopeshwa, ni faida za wazi kwa wanyonge na ni uwezeshaji wao katika uchumi wa soko, na utandawazi. Lakini ili wafaidike, wanyonge lazima wajiunge kwenye ushirika, lazima wausimamie vizuri ushirika wao, lazima wawe wajasiriamali, wabunifu na wenye kuthubutu na kujiamini.  Sifa hizo zinatokana na wananchi wenyewe. Serikali haiwezi kuzishurutisha kwao.  Waheshimiwa Wabunge mnayo nafasi nzuri, na ni wajibu wenu, kujenga sifa hizo miongoni mwa wananchi kwenye kila jimbo la uchaguzi, na ni vema muwaambie wananchi ukweli huu.

 

              Unajua, Mheshimiwa Spika, wasiotupenda wanadai kuwa sisi wanasiasa ni walaghai, wasiosema ukweli wote. Si sifa nzuri hata kidogo na inaweza kuwa na madhara baadaye. Siku moja basi lililojaa wanasiasa liliacha njia na kugonga mti kwenye shamba la mkulima mmoja mzee. Mzee yule akaenda kuchunguza. Kisha akachimba kaburi na kuwazika wanasiasa wote. Siku chache baadaye akaja askari polisi. Akamuuliza yule mzee, “Je, wote walikufa?” Mzee akajibu, “Ah!, wengine walisema hawajafa, lakini unajua tena jinsi wanasiasa walivyo hodari wa kudanganya!”

Mungu apishie mbali!

 

Elimu ya Msingi

 

Mheshimiwa Spika,

            Ulimwengu, kupitia Umoja wa Mataifa, ulijiwekea malengo 8 ya kufikiwa ifikapo 2015 ili kupunguza umaskini kwa nusu duniani. Yanaitwa Malengo ya Maendeleo ya Milenia.  Lengo la 2 kwenye orodha hiyo linahusu elimu, kwamba ifikapo mwaka 2015 kila mtoto, wa kike na wa kiume, apate elimu kamili ya msingi.  Benki ya Dunia inasema ifuatavyo kuhusu lengo hilo:

 

“Elimu ni maendeleo.  Inawapa watu uwezo wa kuchagua na inawapa fursa, inawapunguzia mizigo miwili ya umaskini na maradhi, na inampa mwenye nayo kauli nzito zaidi kwenye jamii.  Inafanya nchi ziwe na nguvukazi yenye elimumwendo (dynamic) na raia waelewa wanaoweza kushindana na kushirikiana na wengine duniani—ikifungua milango ya mafanikio ya kiuchumi na kisiasa.”

 

Mheshimiwa Spika,

            Serikali inakubaliana kabisa na kauli hiyo.  Ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tatu imeweka mkazo mkubwa sana kwenye elimu ya msingi; na tukaona kuwa mwaka 2015 ni mbali mno kufikia lengo muhimu kama hili.

 

            Tukabuni Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi, (MMEM), 2002-2006, kuhakikisha lengo hili linafikiwa ifikapo mwaka 2006.  Yapo mafanikio mengi ya mpango huu katika miaka yake miwili ya kwanza.  Nitataja machache tu.

 

1.      Tumefikia usawa wa kijinsia kwenye shule za msingi;

 

2.      Idadi ya wanafunzi kwenye shule za msingi imeongezeka kwa asilimia 50;

 

3.      Tumeongeza uwiano wa watoto wanaoandikishwa shule kwa rika ya wanaopaswa kuwepo shuleni (GER) kutoka 77.6% mpango ulipoanza hadi 105.2% hivi sasa;

 

4.      Tumeongeza kiasi cha wanafunzi wanaobakia shuleni mpaka mwisho (NER) kutoka 58.8% tulipoanza hadi 88.5% hivi sasa.

 

5.      Tumejenga madarasa 31,825, na nyumba za walimu 7,530 kwa kushirikiana na wananchi;

 

6.      Tumejenga shule mpya za msingi 1,081;

 

7.      Walimu wapya 17,851 wameajiriwa, na 14,852 kupatiwa mafunzo ya kujenga uwezo wao na kujiendeleza;

 

8.      Upatikanaji wa vitabu umeongezeka kutoka uwiano wa kitabu 1 kwa wanafunzi 8 (1:8) katika madarasa ya I-IV hadi kufikia 1:3, na kutoka 1:10 hadi 1:6 kwa madarasa ya V-VII;

 

9.      Kiwango cha kufaulu mtihani wa kumaliza elimu ya msingi kimeongezeka kutoka 22% mwaka 2000 hadi 40.1% mwaka 2003;

 

10.Kamati za shule 12,689 zimepatiwa mafunzo ya kujenga uwezo wa kusimamia miradi ya shule na shule zenyewe.

 

 

Mheshimiwa Spika,

            Mafanikio ya MMEM yameonyesha usahihi wa mwelekeo ambao tunaamini ndiyo njia pekee ya kufikia Malengo ya Maendeleo ya Milenia.  Mimi ninaamini kuwa malengo hayo yatafikiwa iwapo tu kuna ushirikiano wa kimataifa unaozingatia mambo matatu yafuatayo:

 

·        Kwanza, utashi wa kisiasa na utawala bora katika nchi maskini.

 

·        Pili, mipango-shirikishi kwenye kila jamii.

·        Tatu, mazingira nje ya nchi yanayosaidia jitihada za nchi maskini kama vile kusamehe madeni, kuongeza misaada badala ya mikopo, na kutoa fursa za uwekezaji na biashara.

 

            Haya mambo matatu ndiyo yametuwezesha kupata mafanikio yetu, na kutupa matumaini kuwa malengo ya elimu ambayo dunia ilifikiri yatafikiwa mwaka 2015, sisi tutayafikia mwaka 2006, yaani miaka 9 kabla ya tarehe iliyowekwa na Umoja wa Mataifa!!

 

            Lakini narudia kibwagizo changu. Ni mageuzi yetu ya uchumi ndiyo yaliyosaidia kukua kwa uchumi na kuongezeka kwa mapato ya Serikali, na hivyo kutuwezesha kufuta ada kwenye shule za msingi.  Ni mageuzi yetu ndiyo yalitufanya tuwe na mahusiano mazuri na wahisani, na kusamehewa kiasi fulani cha madeni ya nje na kuelekeza unafuu tulioupata kwenye sekta muhimu kwenye vita dhidi ya umaskini kama ilivyo elimu.  Ni mageuzi yetu ndiyo yametufanya tuaminiwe na wahisani na kupewa misaada zaidi na mikopo ya masharti nafuu.  Na ni utashi wa kisiasa uliotuwezesha kuongeza sehemu ya bajeti ya Serikali iendayo kwenye sekta za kipaumbele kwenye vita dhidi ya umaskini.

 

Mheshimiwa Spika,

            Mafanikio ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi yametupa uzoefu na dhamira ya kuwa na Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari utakaoongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondari kutoka asilimia 22 ya waliomaliza elimu ya msingi mwaka 2003 hadi asilimia 50 ya watakaomaliza elimu hiyo mwaka 2009, tena kwa kuzingatia jinsia na mtawanyiko kijiografia ndani ya nchi.  Lengo pia ni kuongeza kiwango cha kufaulu mtihani wa kidato cha IV ili wanaopata Daraja la I – III wafikie asilimia 70 ya wanafunzi wafanyao mtihani ifikapo 2009.

 

Mheshimiwa Spika,

            Yote haya yamewezekana, na yataendelea kuwezekana kutokana na mafanikio ya mageuzi yetu, ili mradi tusirudi nyuma wala kupunguza kasi. Mageuzi yanafungua milango na fursa kwa wengi, ukianzia na hawa wapatao elimu. Baadhi yao wamefanya vizuri sana katika shule zetu za Serikali na za binafsi, na kututia moyo.

 

            Leo, mbele yenu, Waheshimiwa Wabunge, napenda niwatambulishe vijana wetu wanafunzi, mmoja wa kike na mwingine wa kiume, waliofanya vizuri kuliko wenzao wote Tanzania kwenye mitihani iliyopita ya Darasa la VII, Kidato cha IV, na Kidato cha VI.

 

            Katika mtihani uliofanyika Septemba 2003 wa kumaliza elimu ya msingi, binti wa Kitanzania, Mbuke Solomoka, aliyekuwa anasoma Shule ya Kanawa, Wilaya ya Shinyanga Vijijini, alikuwa msichana wa kwanza; na kijana wa Kitanzania, Kesy Fulano, kutoka Shule ya Bumanji, Wilaya ya Geita, naye alikuwa wa kwanza kwa upande wa wavulana.

 

            Katika mtihani wa Kidato cha IV uliofanyika Oktoba 2003, binti mwingine wa Kitanzania, Sara A. Cheche, aliibuka cheche kweli kweli na kuwa wa kwanza kwa upande wa wasichana Tanzania nzima.  Yeye alikuwa anasoma St. Mary, Mazinde Juu.  Kwa upande wa wavulana, kijana wa Kitanzania, Mosses Mwizarubi aliyekuwa anasoma Ilboru alikuwa wa kwanza.

 

            Katika mtihani wa kumaliza Kidato cha VI uliofanyika mwezi Mei 2003, binti wa Kitanzania, Alice Edward, kutoka St. Mary, Mazinde Juu alikuwa msichana wa kwanza, na kijana Emil Patrick aliyekuwa anasoma Mzumbe alikuwa wa kwanza.

 

            Vijana wetu hawa wako katika ukumbi huu, na naomba wasimame Bunge hili liwatambue ipasavyo. Naomba tuwapigie makofi wanayostahili.

 

Mheshimiwa Spika,

            Nataka Bunge liwatambue maana hawa na wenzao wengi ndilo tumaini la Tanzania ya kesho.  Uendelevu na ustawi wa Tanzania unawategemea hawa.  Lazima kama wazazi na kama taifa tuwekeze sana kwenye vijana wetu kama hawa.  Dunia ijayo ni ya ushindani mkubwa sana.  Walioelimika vizuri ndio wenye uhakika wa kuhimili ushindani huo, iwe kwenye ajira au kwenye biashara.

 

            Kupitia kwa vijana hawa napeleka ujumbe kwa wenzao wote wa Kitanzania.  Ujumbe wangu ni mfupi sana.  Tutafanya kila tuwezalo kuwapeni elimu.  Lakini uamuzi wa kutumia elimu hiyo ni wenu.  Tambueni kuwa upo mzigo mkubwa wa kuendesha nchi hii ambao unawasubiri.  Jiandaeni vizuri.  Someni kwa makini.  Msituangushe.  Na zaidi sana msipate UKIMWI.  Thamani yenu ni kubwa sana na ni ya kudumu.  Msiipoteze kwa tamaa za mwili zipitazo.

 

Elimu ya Juu

 

Mheshimiwa Spika,

            Mafanikio ya mageuzi ya uchumi yametuwezesha pia kupanua elimu ya juu, kwa kushirikiana na sekta binafsi na mashirika ya dini.  Matokeo yake katika miaka 4 iliyopita (1998/99 – 2002/03) idadi ya wanafunzi katika vyuo vya ufundi, vyuo vikuu binafsi na vyuo vikuu vya umma iliongezeka kutoka 18,829 hadi 30,602, sawa na ongezeko la asilimia 62.5.  Cha kutia moyo zaidi ni kuwa ongezeko kubwa lilikuwa la wanafunzi wa kike ambao wameongezeka kutoka 3,889 hadi 10,137, sawa na ongezeko la asilimia 160.7.  Miaka 4 tu iliyopita wanawake walikuwa asilimia 20.7 ya wanafunzi wote kwenye vyuo hivi.  Leo wapo asilimia 33.1.  Nawapongeza sana wanawake waliojitokeza kutafuta elimu ya juu.  Maana Serikali inaweza kutoa fursa, lakini uamuzi wa kutumia fursa hizo ni wa mtu binafsi.

 

Mheshimiwa Spika,

            Uwezeshaji kwa njia ya elimu ni sehemu muhimu ya mkakati wa kitaifa wa kukabiliana na changamoto za utandawazi.  Bado tunayo kazi kubwa ya kufanya.  Lengo la Serikali ni kuwa ifikapo mwaka 2008 wawepo wanafunzi 55,000 katika vyuo vya ufundi, vyuo vingine vya elimu ya juu, na vyuo vikuu.  Mambo matatu ni muhimu sana ili tufike hapo.  Kwanza, Bunge hili liendeleze utashi wa kisiasa wa mkakati huu.  Pili, uchumi ukue kwa kasi zaidi na kuipa Serikali mapato ya kutekeleza mipango yetu, na Bunge hili lichochee ukuaji huo. Tatu, elimu ya sekondari ipanuke na iboreke, kupitia mpango ambao nimeuzungumzia, ili tupate wahitimu bora wa kutosha kudahiliwa kwenye vyuo vyetu.

 

            Napenda nilishukuru Bunge hili Tukufu kwa kukubali kupitisha Sheria Na. 8 ya 2001 iliyoanzisha Mfuko wa Elimu, ambao kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge watakumbuka una malengo matatu makuu:

 

·        Kwanza, kuhakikisha elimu yetu katika ngazi zote ni bora zaidi;

·        Pili, kuhakikisha upo mfumo endelevu wa kugharamia elimu nchini; na

·        Tatu kuhakikisha mfumo wa elimu unatoa fursa sawa kwa wote, bila ubaguzi wowote.

 

            Mfuko umeanza kazi, na tayari Mamlaka ya Elimu Tanzania inayousimamia imetoa Sh.3.4 bilioni kwa vyuo vya ufundi na vyuo vikuu vya umma Tanzania Bara na Zanzibar, pamoja na vyuo vikuu binafsi na vya mashirika ya dini.  Narudia.  Mfuko huu ni wa kuwezesha elimu kwa Watanzania wote, bila ubaguzi.  Popote Mtanzania anapopata elimu, ujumla wake ni ongezeko la wasomi nchini ambayo ni hazina ya taifa.  Tutaendeleza ushirikiano huu kati ya Serikali zetu mbili, ya Muungano na ya Zanzibar, na taasisi binafsi za elimu nchini kwa lengo moja la kuongeza idadi na ubora wa nguvukazi ya taifa.

 

 

Afya

 

Mheshimiwa Spika,

            Sekta ya afya ni muhimu sana katika vita dhidi ya umaskini.  Lakini ni wazi pia kuwa mafanikio yake hayategemei utashi na maamuzi ya Serikali peke yake.  Hatimaye afya ya mtu ina gharama, ambayo mwenyewe lazima awe tayari kuibeba.  Ipo gharama ya kuzuia usiumwe – kwa kula chakula bora, kwa kuweka mazingira ya pale unapoishi na kufanya kazi kuwa safi, kwa kufanya mazoezi, kwa kuzuia magonjwa kwa chanjo pale palipo na chanjo, au kwa kuepuka kuambukizwa kwa magonjwa kama UKIMWI yasiyo na chanjo, na  kwa kuchangia gharama za matibabu.

 

            Mafanikio ya mageuzi yetu, na mahusiano mazuri na wahisani na sekta binafsi, yote yametusaidia kuleta mabadiliko makubwa ya mfumo wa huduma za afya, ukarabati wa taasisi za afya na upatikanaji wa chanjo. Bajeti ya afya imekuwa ikiongezeka kwa miaka 3 mfululizo.  Hili nalo limewezekana kwa sababu ya mafanikio ya mageuzi yetu ya kiuchumi.

 

            Hali ya chanjo imeboreka na kufikia asilimia 83, kuzidi kiwango cha asilimia 80 ambacho kimataifa kimekubalika kuwa ni kiwango kizuri.  Hivi sasa tumeanza kutoa chanjo ya Hepatitis ambayo imechanganywa na chanjo iliyopo ya DPTT bila malipo ya ziada.  Hii itasaidia kuokoa maisha kati ya 20,000 – 25,000 yanayopotea kwa mwaka hivi sasa.

 

            Tanzania ipo mstari wa mbele duniani katika vita dhidi ya malaria.  Lakini tunaomba uelewa na ushirikiano wa wananchi.  Tumefuta kodi kwenye vyandarua na bidhaa zinazosaidia vita dhidi ya malaria.  Tumepata msaada wa Mfuko wa Kimataifa wa Kudhibiti UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria.  Hivyo tumeweza kufidia baadhi ya gharama za vyandarua vilivyotiwa dawa ambavyo imedhihirika vinasaidia sana kupunguza maambukizo ya malaria hasa kwa kina mama waja wazito na watoto wachanga.  Lakini jitihada zetu hizo ni bure iwapo wananchi hawatatumia utaratibu uliowekwa.

 

Mheshimiwa Spika,

            Duniani kote bima ya afya ndiyo kinga thabiti, hasa kwa wanyonge, ya kukabiliana na gharama za tiba.  Kwa wananchi wa kawaida tumeanzisha Mifuko ya Afya ya Jamii.  Pale ambapo mifuko hii inafanya kazi yapo mafanikio makubwa ambayo siri yake ni ushirikiano mzuri kati ya Serikali na wananchi.  Mifuko hiyo imewapunguzia mzigo na hofu wananchi, na kuzipatia hospitali uwezo wa kujiendesha.  Tunataka mifuko hii ianzishwe katika wilaya zote zilizobaki katika miaka michache ijayo.

 

            Kwa wafanyakazi wa sekta ya umma, tumeanzisha bima ya afya ambayo huchangiwa kati ya mfanyakazi na mwajiri.  Matatizo mengi ya awali kutokana na uchanga wa mfuko yamepatiwa ufumbuzi, na kazi iliyo mbele yetu ni kuimarisha mfuko huo, na kuboresha taratibu zake.

 

            Tumeendelea pia na ukarabati mkubwa wa vituo vya huduma za afya, kuanzia Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo kazi inaendelea, mpaka hospitali za wilaya.  Kwa mfano, kwa kushirikiana na Serikali ya Uholanzi, tayari tumefunga mashine za eksirei na mashine nyingine katika hospitali za wilaya, mikoa na rufaa.  Kazi iliyo mbele yetu ni kuvitumia vifaa hivyo vizuri, na kuvitunza, ili viendelee kutumika kwa miaka mingi ijayo na kuboresha uwezo wa madaktari kutibu wagonjwa kwa usahihi na uhakika zaidi.