HOTUBA YA MWENYEKITI
WA CHAMA CHA MAPINDUZI NA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA
BENJAMIN WILLIAM MKAPA, KWENYE MKUTANO WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA YA CHAMA CHA
MAPINDUZI, DODOMA, 15 FEBRUARI 2005
Waheshimiwa
Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM;
Waheshimiwa
Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM;
Mabibi na
Mabwana:
Baada ya Kamati Kuu ya CCM jana kuamua kuleta Taarifa
mliyoizungumza, niliamua kuwa nifunge mjadala wake kwa maelezo ya maandishi.
Waheshimiwa Wajumbe:
Chama chetu Tawala,
CCM, lazima kiendelee kutawala kwa sababu ya usahihi wa sera zake, kwa ubora wa
uongozi wake na kwa vile, kwa sifa hizo, hakina mbadala!
Leo tena, kama ilivyokuwa kwenye Mkutano wetu wa tarehe
25 Agosti mwaka jana, nimeamua kufunga mjadala huu kwa hotuba inayoendeleza
hoja ya msingi niliyoijenga wakati ule ya “Ushupavu wa Uongozi”. Maana ushupavu huo ndio utahakikisha kuwa
Taifa letu haliyumbi, kwamba Taifa letu litapata uongozi bora linalostahili, na
kwamba CCM itabakia kwenye usukani wa merikebu ya Taifa letu la Tanzania, na
kuivusha salama kwenye mawimbi yote.
Mwezi Agosti mwaka jana nilizungumzia hofu ya wananchi,
hofu ya wahisani na hofu ya wawekezaji tunapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu. Nikataka tujiulize kwa nini wawe na hofu
wakati wanao uhakika kuwa CCM itashinda.
Nikasema hofu hiyo inatokana na wao kuwa na wasiwasi kuwa pengine sisi
wenye jukumu muhimu la kuteua wagombea wa CCM hatutakuwa makini vya kutosha, na
hivyo kuweka wagombea wasiofaa lakini watakaoshinda kwa nguvu tu ya CCM.
Leo nataka nizungumzie hofu nyingine, nayo ni hofu ya
baadhi ya viongozi wenyewe ambayo nayo ningependa niitulize. Maana haifai kufanya maamuzi mazito kama haya
katika hali ya hofu. Tujiandae kufanya
maamuzi katika hali ya kujiamini, tukiwa na uhakika wa umakini wetu, busara
zetu, uadilifu wetu na uwezo wetu wote.
Kipindi hiki tunapoelekea kwenye uteuzi wa wagombea
Urais, wapo viongozi wenzetu wenye hofu.
Wapo wanaohofia Chama chetu, hasa wanapoona bidii isiyo ya kawaida ya
wanaowania kuteuliwa. Wanaona kuwa bidii
hiyo isipodhibitiwa mapema inaweza kukigawa Chama kwa misingi mbalimbali,
ikiwemo misingi ya ukabila, kanda, na dini.
Hofu na hatari hiyo ni jambo la msingi kabisa, na wala si
jambo la kupuuzwa. Halmashauri Kuu hii itapata nafasi ya kuchuja wagombea
wakati wa kufanya hivyo ukifika. Kwa
sababu hiyo, naamini tunao wajibu wa sisi wenyewe kujikumbusha na kuwakumbusha
wanaokusudia kuwania nafasi hizi za juu kabisa katika uongozi wa taifa letu,
kuwa kutumia rushwa, na kutumia mambo yanayotugawa kama vile ukabila, udini na
ukanda katika kutafuta kuteuliwa, si mojawapo ya sifa za kuteuliwa; badala yake
ni sababu ya kutosha ya kukataliwa.
Narudia. Halmashauri Kuu hii ina wajibu wa
kujikumbusha yenyewe, na kuwakumbusha wanaokusudia kuwania kuteuliwa kuwa
wagombea kupitia CCM, kuwa kwetu sisi wana-CCM, rushwa, ukabila, udini na
ukanda si sifa hata kidogo ya kuteuliwa; na badala yake ni sababu ya kutosha
kukataliwa. Nikiwa Mwenyekiti wa CCM,
ninao wajibu wa kukumbusheni jambo hili mara kwa mara mpaka dakika ya mwisho.
Aidha, nikiwa
Mwenyekiti, nitahakikisha haki inatendeka kwenye jambo hili la msingi
kabisa. Na haki hiyo ina pande
mbili. Upande wa kwanza ni kuwa kila
anayethibitika kuvunja maadili ya CCM kwa kutumia, au kuendekeza, rushwa,
maovu, ukabila, ukanda, na udini hapenyi hata kidogo kwenye mchujo wetu. Upande wa pili ni kuwa asiyethibitika kuvunja
maadili hayo naye haonewi wala kusingiziwa.
Na nitahakikisha pia kuwa tunao uwezo wa kuthibitisha
penye hatia, au tuhuma nzito, na wa kuthibitisha pasipo na hatia au tuhuma
nzito. Uwezo huo unatokana na mfumo na
mtandao wa Chama Cha Mapinduzi, ikiwemo kuanzia ngazi ya mkoa, wilaya hadi
tarafa, kata na kijiji. Kazi ya kuhakiki
usafi au uchafu wa mgombea si yangu peke yangu; ni ya kila mwana-CCM na kila
kiongozi wa CCM ambaye yeye mwenyewe kwanza ni msafi, na pili ambaye hataki
kanuni na maadili ya chama chetu yapuuzwe au kuchezewa.
Uvunjaji wowote wa
maadili, taratibu na kanuni haufanyiki hewani; unafanywa ndani ya jamii
zetu. Na ninyi Wajumbe wa Halmashauri
Kuu ya Taifa ya CCM ndiyo wasimamizi wakuu wa maadili ya uongozi ndani ya Chama
chetu. Mkijituma, mkitambua uzito wa
nafasi na wajibu wenu, na mkiwa wenyewe ni waadilifu, mtasaidia sana
kuhakikisha CCM inaendelea kuwa imara, na kuongoza taifa imara.
Narudia. Kwanza, ninyi wenyewe wote mnapaswa muwe
waadilifu, msiokubali kununuliwa kwa fedha, kwa ahadi za vyeo, au kwa jambo
lolote lile. Pili, mtambue umuhimu wa
kupata wagombea safi – safi kwa tabia na mienendo, na safi kwa upeo na uwezo wa
kutekeleza Ilani ya CCM kwa uaminifu. Na
tatu, mjue na kuzingatia uzito wa dhamana mliyonayo. Nyote mkitekeleza wajibu wenu, haki
itatendeka ndani ya Chama, na Chama kitalitendea taifa haki kwa kulipatia
viongozi bora. Tukiazimia kufanya hivyo hatuna sababu ya kuwa na hofu juu ya
Chama chetu. Ni rahisi mkiwa kwenye makundi ya fitina kupuuza ushauri wangu,
lakini siku moja kila mtu atakuwa peke yake, na ndipo umuhimu wa ushauri huu
utakapobainika kwa kila mtu.
Waheshimiwa Wajumbe:
Lakini najua pia kuwa wapo miongoni mwetu wenye hofu— si
hofu ya Chama—bali hofu binafsi. Nataka nao niwatulize. Uongozi wenye heshima,
uongozi ambao unapewa na wenzako kwa vile umechomoza kwa usafi, upeo na uwezo,
si uongozi wa kuhuzunika usipoupata.
Maana uongozi wa aina hiyo, unaoweka Chama na Taifa mbele, ni mzigo
mzito. Nimekuwa Rais, huu ni mwaka wa 10
sasa. Najua ninachosema, naelewa
alichosema Baba wa Taifa, na bila shaka Mzee Mwinyi atakubaliana nami. Uongozi wa juu wa taifa ni heshima kubwa
sana, na dhamana kubwa mno. Lakini ni
mzigo mzito. Mwalimu hakuukimbilia. Mzee Mwinyi hakuukimbilia. Na mimi mwenyewe sikuukimbilia kwa wepesi
kama mwelekeo wa mwaka huu unavyoashiria.
Kulikoni?
Hivyo, nawaomba sana wanaowania kugombea uongozi mwaka
huu, tangu ngazi ya Rais, mpaka Wabunge, Wawakilishi na Madiwani, wasiwe na
hofu binafsi ya kusema, “Itakuwaje nisipoteuliwa na Chama?” Wengi mtashindana.
Nafasi za Rais, Wabunge, Wawakilishi, na Madiwani zitakuwa zote wazi, na kila
mwenye sifa anayo ruhusa kugombea. Na mimi nitafanya kila lililo ndani ya uwezo
wangu kuhakikisha taratibu, kanuni na Katiba ya CCM vinazingatiwa kwa
ukamilifu, ili demokrasia ndani ya Chama itimie, haki itendeke, na ushindani
uwe huru na wa haki. Na pale vigezo vya kuteuliwa vinapokuwa wazi, jambo la
msingi si uhodari wa kujenga makundi ya fitina, bali kufikia vigezo hivyo kwa
namna ambayo kila mtu atakiri kuwa huyu ndiye anayestahili kuteuliwa.
Sasa nitamshangaa
sana yule ambaye baada ya demokrasia kutumika, baada ya haki kutendeka, baada
ya kanuni, taratibu na katiba kuzingatiwa, bado atasononeka na kununa
asipoteuliwa. Nitashangaa vilevile
akitokea yule ambaye baada ya kuteuliwa na kushinda atajiona bora sana na
kupuuza wenziwe. Maana, wenye sifa na
uwezo ni wengi. Hawawezi kuteuliwa wote. Watakaoteuliwa na wale ambao hawatateuliwa
wote wana wajibu kwa Watanzania wenzetu kuendelea kushirikiana, kuimarisha
umoja wa Chama, na kuwa mhimili mkuu wa umoja wa taifa. Ikiwa hivyo ndivyo, hofu binafsi ni ya nini? Hofu hiyo itaendelea kuwapo iwapo tu mhusika
ni mbinafsi, aliye tayari kutoa kafara maslahi ya CCM na taifa ili kunusuru
maslahi yake binafsi.
Najua wapo pia wenye hofu binafsi kwa vile wameingia,
kabla ya wakati, kwenye makundi ya kampeni zisizo rasmi na za fitina za
wanaowania uongozi katika ngazi mbalimbali.
Wapo walioingia kwa kuamini usafi na uwezo wa wanaowaunga mkono. Lakini najua kuwa wapo pia wanaojiunga na
yeyote yule anayewaahidi vyeo na fadhila mbalimbali. Sasa hiyo ni hatari kubwa; na kwa kweli hao
wana kila sababu ya kuwa na hofu, na ninawaonea huruma.
Nyote mnajua. Nilipowania kuteuliwa kugombea Urais mwaka
1995 sikumwahidi mtu yeyote fadhila wala cheo.
Kwa upande mwingine hiyo ilikuwa ndiyo salama yao. Maana ukishakuwa Rais
unaweza kubadili mawazo kulingana na hali halisi utakayokabiliana nayo kwenye uongozi.
Na leo pia nisingependa wana-CCM, na hasa viongozi, wawe watu wa kununuliwa kwa
fedha au kwa ahadi za vyeo, ambavyo wala hawana uhakika wa kuvipata baada ya
uchaguzi.
Na mambo hayo
hayawezi kufichika daima. Tena najua wapo wanaowania kuteuliwa ambao kwa cheo
kimoja wanawaahidi watu wengi. Ndio
maana nasema kuwa hao wanaokubali kununuliwa kwa ahadi hizo wana kila sababu ya
kuwa na hofu: hofu ya kujulikana, na
hofu ya kutotimiziwa ahadi hizo. Lakini
dawa yake ni nyepesi. Ni
kujirekebisha. Ni kuacha kuufanya
uchaguzi uwe wa kutafuta maslahi binafsi, na badala yake kuweka mbele maslahi
ya Chama na maslahi ya nchi yetu Tanzania, na wananchi wenzetu wanaokiamini
Chama Cha Mapinduzi. Ni kuwakataa
wanaogawa fedha na ahadi za vyeo.
Waheshimiwa Wajumbe:
Nimezungumza sana kuhusu kupiga vita rushwa, ukabila na
ukanda. Leo napenda nikemee, kwa nguvu
zote, tabia inayoanza kuonekana ya wanaowania kuteuliwa kujipendekeza na
kujinadi kwa viongozi wa dini; jambo hatari sana hilo!
Ninaamini kuwa kila anayewania kuteuliwa kuwa mgombea wa
CCM anaijua vema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania—Katiba ambayo
akichaguliwa ndiyo atakayoapa kuilinda, kuihifadhi na kuitetea kwa moyo wake
wote na nguvu zake zote. Katiba hiyo inatenganisha
mambo ya kidini na mambo ya kiserikali.
Kila raia anao uhuru wa imani ya dini na ibada; lakini Serikali haina
uhuru wa kuwa na dini wala ibada maalum.
Sisi tumefanya kazi kubwa sana kuwataka viongozi wa dini
wasitumie mimbari zao kuwashawishi waumini wao kuchagua chama fulani, au
mgombea fulani. Hili ni suala la msingi
kabisa kabisa—la msingi kikatiba na la msingi kimaadili ndani ya Chama Cha
Mapinduzi. Sasa, baada ya kazi hiyo,
viongozi hao wa dini watatushangaa sana iwapo wagombea wetu wataanza tena
kuwafuatafuata, kwa kisingizio kimoja au kingine. Viongozi wa dini si wajinga. Ni wasomi na wanazuoni. Wana busara.
Wanajua wale wanaowafuata wanataka kuwashawishi ili watumie nyadhifa zao
za dini kuwasaidia kuungwa mkono na wafuasi wa dini zao.
Nafurahi sana kuwa
tunazo kauli za wazi za viongozi wa dini zetu kuu zote kuwa hawatatumia
ushawishi wao mkubwa kwenye jamii kupigia debe chama fulani, au mgombea fulani.
Ninawaomba waendelee na msimamo huo, na wawafukuze wanaojipendekeza kwao kwa
sababu hizi. Lakini sisi tuonyane wenyewe
pia. Asitokee mtu tena kuwafuatafuata
viongozi hao wa dini. Tutagawa watu,
tutagawa chama, na hatimaye tutagawa taifa, na kupoteza kabisa sifa za
kukabidhiwa dhamana ya uongozi wa taifa hili.
Waheshimiwa Wajumbe,
Namalizia kwa kumtaka kila kiongozi na kila mwanachama wa
Chama Cha Mapinduzi asiwe na hofu; awe jasiri na mkakamavu. Kila mmoja wetu akiwa mwadilifu, awekaye
mbele maslahi ya Chama na Taifa, hana sababu ya kuwa na hofu. Tuondoe hofu
maana tunao, miongoni mwetu, uwezo na madaraka kuhakikisha tunapata mgombea
bora wa Urais, wa Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Hofu pekee inayoweza kuwepo ni pale wagombea
wanapokuwa wadaiwa wa fadhila na vyeo wanavyonadi wakitafuta fedha au kuungwa mkono.
Hofu nyingine ni kwa wale wanaokubali kuahidiwa fadhila hizo na vyeo
hivyo. Lakini, kwa wote wanaoweka
maslahi ya Chama na Taifa mbele, ambao ninaamini ndio wengi, hawana sababu ya
kuhofu.
Tutafanya kila lililo ndani ya uwezo wetu kuhakikisha
haki inatendeka, demokrasia inaimarika ndani ya Chama, na taifa linapata
viongozi bora kwa tabia njema, kwa maadili mema, na kwa uwezo mkubwa wa
kusukuma taifa mbele kimaendeleo—sio kurudi nyuma, kupunguza kasi, au kubakia
pale pale tulipo. Kwa wasioweka mbele
ubinafsi, hawataona taabu kujipanga nyuma ya wale tutakaowateua, na kuwasaidia,
ili kweli sifa ya Tanzania nje ya nchi, na mafanikio ya maendeleo na vita dhidi
ya umaskini, viendelee mbele chini ya uongozi wa CCM. Mimi siamini kabisa kuwa Rais atakayepita
kwenye mchujo thabiti wa CCM, atakuja kutaka kuangamiza watu, kulipiza visasi
au kuwaandama wasiokubaliana naye. Sisi, Tanzania, na hasa Chama Cha Mapinduzi,
tumeshavuka huko. Hatutoi wala kulea
viongozi wa aina hiyo.
Kwa hiyo, narudia.
Tuondoe hofu. Tujisafishe
wenyewe, sisi Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi, ili
tuwe na uhalali na ushupavu wa dhamira kusimamia maadili, haki na demokrasia
ndani ya Chama Cha Mapinduzi tunapoelekea kufanya maamuzi mazito kwa maendeleo,
utulivu, na hatma ya taifa letu. Natarajia kuwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka
huu wa 2005 itatupa mwelekeo na kigezo muhimu cha kisayansi cha kubainisha nani
miongoni mwetu – aliyetangaza kuwania au ambaye bado hajajitokeza – anazo sifa
za kutufanya sisi sote tuseme huyu mwenzetu ndiye anastahili kuliko wengine
kukabidhiwa utekelezaji wa Ilani yetu.
Nakuhakikishieni, kwa wale wenye shaka, kuwa mimi
Mwenyekiti wenu sina mgombea wangu, na wala sijamtuma mtu yeyote akawanie
kuteuliwa kwa baraka zangu. Narudia.
Sina mgombea wangu. Ninayo kura
yangu wakati wa uteuzi ukifika.
Nitaitumia kwa makini sana, kwa kulinganisha sifa, uadilifu, na uwezo wa
wagombea watakaojitokeza. Lakini hatimaye nitaheshimu ushindi wa
atakayechaguliwa kwa haki, na kwa mujibu wa kanuni, taratibu, na Katiba ya
CCM. Na huyo ndiye nitakayemnadi kwa
bidii zangu zote kwa Watanzania wenzangu, ili wamchague na kunipa mimi idhini
isiyo na shaka ya kumkabidhi yeye usukani wa taifa letu.
Tumuombe Mwenyezi Mungu atupe busara na hekima
tunapoelekea kilele cha mchakato huu mzito na adhimu.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI!
MAPINDUZI DAIMA!
Ahsanteni kwa kunisikiliza.