TATHMINI YA HALI YA SIASA TANZANIA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA
MWAKA 2005
Na Philip J. Mangula, Katibu Mkuu wa CCM
1.0
UTANGULIZI
Itakapofika
Novemba mwaka 2005 Watanzania watapiga kura kwa mara ya tatu katika uchaguzi
utakaohusisha vyama vingi vya siasa.
Kwa mara nyingine tunategemea kubadilishana madaraka kwa amani kutoka
awamu moja kwenda nyingine. Uchaguzi wa
mwaka 2005 una mvuto na msisimko wa aina yake kwa sababu Rais aliyepo atatakiwa
kuachia madaraka kwa mujibu wa marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Hali hii inaleta ushindani si
tu ndani chama tawala bali pia hata ndani ya vyama vya upinzani. Tukirudi nyuma
kidogo ni muda mfupi tu tokea watanzania walipopiga kura mwaka 2000. Hiki ni
kipindi kizuri kwa wachunguzi wa masuala ya kisiasa kwa sababu mambo mengi
yanatokea au kufanywa ambayo huweza kutumika kama kigezo cha kupima demokrasia
nchini. Katika makala hii tutajitahidi kutathmini hali ya siasa za Tanzania
kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005. Tutachambua ahadi zilizotolewa wakati wa
uchaguzi wa mwaka 2000 na kuona ni jinsi gani zilitekelezwa au hazikutekelezwa
na athari zake kwa demokrasia, kwa kulinganisha na hali halisi ya sasa. Pamoja
na kuwa matukio muhimu ya kila siku yatachukuliwa katika kuelezea baadhi ya
mada tutakazojadili, si nia ya makala hii kujikita katika matukio ya kila
siku. Wakati tukielekea kipindi cha
uchaguzi mkuu wa 2005 ni muhimu tukafanya tafakuri za kina za nini kimefanyika
na maeneo ambayo bado kuna mapungufu.
Ni muhimu tukaeleza tokea awali kwamba tathmini itazingatia zaidi hali
ya siasa ilivyobadilika kuanzia mwaka 2000.
Lengo la tathmini ni kutoa mwanga wa mwelekeo wa kisiasa baada ya mwaka
2005.
Ili
kutuwezesha kuweka bayana tafakuri hii makala hii imegawanywa katika vipengele
vikuu vitatu:
(a) HALI YA SIASA BAADA YA
UCHAGUZI WA MWAKA 2000: MATARAJIO,
MAZURI NA MAPUNGUFU
·
Hali iliyojitokeza Zanzibar
·
Hatua za Kukabiliana na Rushwa ndani ya CCM na ndani ya
Serikali
·
Magomvi/Migogoro ndani ya vyama vya siasa na athari zake
katika ukuzaji wa demokrasia
·
Tathmini ya Imani ya Wananchi kwa Serikali
(b)
NAFASI YA VYOMBO VYA HABARI NA VYAMA VYA WANANCHI KATIKA KUKUZA DEMOKRASIA
·
Kushamiri kwa vyombo vya habari
·
Nafasi ya vyama vya wananchi kwenye ujenzi wa demokrasia
(c) KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2005 NA MUSTAKABALI WA TAIFA
● Umoja wa Kitaifa
● Mwelekeo wa wananchi Kisiasa
2. HALI YA SIASA
BAADA YA 2000
Uchaguzi Mkuu
wa Novemba 2000 ulijenga taswira mbili zinazokinzana Tanzania. Upande wa Tanzania Bara kwa ujumla uchaguzi
uliendeshwa kwa amani na utulivu na uvumilivu.
Hadithi, hata hivyo, ilikuwa tofauti kabisa upande wa Tanzania
visiwani. Uchaguzi ulileta utata mkubwa
na hata wasiwasi wa kutokea mgogoro wa kisiasa. Isingalikuwa ukomavu wa kisiasa uliokuja kuonyeshwa na wote
waliohusika, Tanzania ingaliwezaweza kuingia kwenye janga kama tunavyoshuhudia
nchi nyingine za Afrika. Kwa hakika
hali ya siasa ya Zanzibar na hofu ya siasa za vurugu ilikwishaainishwa na Tume
ya Nyalali[1]
ambayo iliona uwezekano wa chama kitakachoshindwa katika uchaguzi kuyakataa
matokeo.
Inatosha
kusema hapa kwamba haja ya muafaka ilionekana kuanzia awali kama ambavyo makala
zilizoandikwa na Prof. H. Othman, Bw. P. Mangula na Bw. S. S. Hamad[2]
zinaonyesha kwa namna tofauti umuhimu wa kukaa pamoja na kuzungumza. Muafaka II
wa mwaka 2001 ni kitu cha kujivunia na rekodi nzuri ya utatuzi wa migogoro
katika nchi za kiafrika. Matokeo ya
muafaka ni kama ifuatavyo:
(1) Kufanyika kwa
uchaguzi mdogo katika majimbo 16 ambayo awali Civic United Front (CUF) ilisusia
matokeo yake hivyo kuwawezesha kurejea tena kwenye siasa za ushindani bila
kupigana.
(2) Kuimarika kwa
amani na utulivu ambavyo vimeiwezesha nchi kupiga hatua za kimaendeleo. Kwa
mara ya kwanza CUF walishiriki kwenye sherehe za mapinduzi za mwaka 2003
kuonyesha kuwa wanaitambua serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
(3) Kuridhishwa kwa
wahisani na hali ilivyo Zanzibar na kuanza kutoa misaada kwa serikali iliyokuwa
imesitishwa. Hii imesaidia kuboresha hali ya uchumi na maisha ya wananchi kwa
ujumla.
(4) Kuundwa upya
kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ambayo itahusisha vyama vya siasa katika
uundaji wake.
2.1
Magomvi/migogoro
ndani ya vyama vya siasa
Kwa
bahati nzuri, Tanzania ina vyama 16 vya siasa vyenye usajili wa kudumu. Mojawapo ya mihimili ya siasa za kiliberali
ni kushindanisha sera za vyama vingi ili wananchi wapate fursa ya kuchagua
chama wanachoona kinafaa. Kwa vyovyote
vile mfumo wa siasa wa vyama vingi unahuishwa na uimara na uthabiti wa vyama
ambavyo vinakuwa tayari kuchukua fursa za kuongoza nchi kama chama tawala
kikidorora. Hali hii hukinyima usingizi
chama kinachotawala na hivyo kukifanya siku zote kitafute njia za kuboresha
utendaji wake – matokeo yake wananchi wanafaidika zaidi. Hali ni tofauti Tanzania, hasa Tanzania bara
kwa sababu bado haijafikia hatua chama tawala kikakosa usingizi kwa kuhofia
kupoteza madaraka kwa upinzani. Kama ripoti ya Profesa Mukandala[3]
ilivyoonyesha vyama vingi bado vinalegalega kwenye uchaguzi, havijajikita
mizizi vijijini, na bado havijajulikana sana ukiachilia mbali sifa za
waanzilishi. Kuna migogoro baina ya vyama na ndani ya vyama vyenyewe.
Nitaelezea kidogo.
Migogoro
imeshamiri ndani na baina ya vyama vya siasa hali inayowaacha wananchi njia
panda. Hapa tutazungumzia migogoro
katika baadhi ya vyama vikubwa vyenye wabunge na madiwani. Tumeshuhudia mgogoro mkubwa wa kugombea
madaraka ndani ya UDP. Ilianza kwa
kamati kuu ya chama hicho kumtimua Mwenyekiti Bwana John Cheyo. Baadaye msajili akabatilisha maamuzi ya
kamati kuu na kumrudisha Mwenyekiti Cheyo.
Kilichofuata ni timua-timua.
Baadhi ya wabunge waliotuhumiwa kushirikiana na Bwana Amani
Jidulamabambasi kumpindua Mwenyekiti wakawa wa kwanza kutimuliwa. Matokeo:
Aliyekuwa Mbunge wa UDP na Madiwani 9 walihamia CCM na wanachama 1,147 wa wilaya ya Bariadi walihamia CCM pia.
TLP
sasa hivi kunafuka moshi na kuna kila dalili ya mlipuko hali ikiachwa iendelee
ilivyo. Madiwani matano wa wilaya ya
Moshi Vijijini walihamia CCM na hivi
sasa kuna kampeni za uchaguzi mdogo zinaendelea. Tarehe 24/4/2004 Mwenyekiti wa TLP Mkoa wa Dar es Salaam ambaye
alikwua pia mfadhili wa chama Bw. Saab
Ally na Mwenyekiti wa Umoja wa
Vijana wa chama hicho wamehamia CCM.
Athari
za migogoro katika vyama vya siasa ni nyingi, na kwa ujumla wake zinachangia
kudorora kwa demokrasia. Panapokosekana
chama chenye upinzani wa kweli na nguvu ya siasa, hutokea chama kilichoshika
dola kikalala usingizi na kujisahau kabisa.
Wananchi ndio waathirika wakubwa wa hali hii.
Ni
jukumu la kila mmoja wetu na kila mdau kikiwemo chama tawala kuhakikisha kuwa vyama vya upinzani vinaimarika Tanzania. Hali ya vyama vya siasa Tanzania kama
inavyoonyeshwa kwenye jedwali lifuatalo inaonyesha kupungua nguvu kwa vyama vya
upinzani ukilinganisha na CCM.
Idadi ya kura ambazo vyama vilipata katika uchaguzi wa Bunge
2000
|
CHAMA |
IDADI YA
KURA |
ASILIMIA |
ONGEZEKO
TOKA 1995 |
|
|
1. 2. 3. 4. 5. 6. 7. 8. 9. 10 11. 12. 13. |
CCM NCCR-MAGEUZI CHADEMA CUF UDP TADEA NRA UMD TLP NLP UPDP PONA TPP |
4,634,047
258,591
99,461
792,378
315,357
9,647 70
7,550 652,535
2,507
14,818
11,789 10,206 |
65.3 3.6 4.2 11.2 4.4 0.1 0.001 0.1 9.2 0.04 0.2 0.2 0.1 |
+6
-18 - 2 - 6
+1.1
+ 1 0. 0. + 9 0 0 0 0 |
|
|
JUMLA |
|
100 |
|
Chanzo: Tume
ya Taifa ya Uchaguzi (NEC): Uchaguzi Mkuu wa 2000
NB: Taarifa hii haihusu uchaguzi katika majimbo
25 ambamo CCM ilipita bila kupingwa.
Tunaona
katika jedwali hapo juu kuporomoka kwa vyama vikubwa kama NCCR-Mageuzi ambacho
kilitawaliwa na migogoro iliyoishia kukigawa chama. Hapa nigusie tu kwamba CCM
kutokana na ukomavu wake kisiasa kimeweza kudhibiti migogoro kila
ilipojitokeza. Kipindi cha kuelekea
uchaguzi mkuu kitatawaliwa na migogoro ndani ya vyama na ni vyema vyama viweke
mikakati ya kukabiliana nayo.
2.2
Tathmini ya
kukubalika kwa serikali na chama
Uchaguzi
mkuu kwa kawaida ni tathmini ya kukubalika kwa chama kwa wananchi wapiga kura
(na hivyo serikali kitakayoiunda).
Hutokea umaarufu wa chama ukaporomoka ghafla mara baada ya uchaguzi mkuu
kwa sababu kadha wa kadha. Katika
utafiti uliofanyika hivi karibuni[4]
asilimia 63 ya wasailiwa wanakataa mfumo wa siasa wa chama kimoja. Asilimia 73 wanakataa utawala wa mtu mmoja
(personalized rule) hasa machifu au wazee (wa makabila). Asilimia 87 wanakataa kabisa utawala wa
kijeshi. Asilimia 86 wanapinga mawazo
ya kufuta bunge na kumpa rais madaraka yote.
Tafsiri mojawapo ya matokeo haya ni kwamba watanzania wanahitaji sana
mfumo wa demokrasia wa vyama vingi (yaani uliopo).
Kukataa udikteta (Asilimia)
|
|
Nakubali
Kabisa/Sana |
Nakubali |
Yote sawa |
Sikubali |
Sikubali
Kabisa |
Sijui |
|
Chama
kimoja tu kiruhusiwe kusimama kwenye uchaguzi |
12.0 |
17.0 |
7.0 |
25.0 |
38.0 |
1.0 |
|
Maamuzi
yote yafanywe na Mchifu au Baraza la Wazee |
4.0 |
9.0 |
10.0 |
33.0 |
40.0 |
4 |
|
Jeshi
litawale nchi |
2.0 |
4.0 |
5.0 |
28.0 |
59.0 |
2.0 |
|
Chaguzi
zisiwepo ili Rais aamue kila kitu |
2.0 |
4.0 |
6.0 |
28.0 |
58.0 |
2.0 |
Chanzo: “Results from Round II OF Afrobarometer
Survey”
2.2.1 Ukuaji wa Demokrasia
Katika jamii
nyingi demokrasia imehusishwa na maendeleo ya nchi kisiasa, kiuchumi na
kijamii. Kadri nchi inavyokuwa ya
kidemokrasia zaidi ndivyo inavyoongeza uwezekano wa kupata maendeleo. Hivyo kuna ulazima wa kuifanya demokrasia
kuwa sera ya taifa. Wananchi lazima
waridhishwe na kiwango cha demokrasia ili waunge mkono. Katika utafiti uliofanyika mwaka 2003
wahojiwa waliulizwa ni kwa kiasi gani Tanzania inafuata demokrasia. Kwa ujumla
asilimia 81 walisema Tanzania ni nchi ya kidemokrasia. Hata hivyo walisema demokrasia Tanzania bado
ina matatizo madogo. Asilimia 12 tu
walisema Tanzania ina demokrasia kamili, ambapo asilimia 19 walisema demokrasia
ya Tanzania ina matatizo makubwa.
Asilimia 8 walisema hakuna demokrasia kabisa Tanzania.
2.2.2 Ushiriki katika siasa
Demokrasia
inaweza tu kushamiri pale ambapo watu wanashiriki katika siasa. Watanzania wanapenda sana siasa na hii
inajidhihirisha kwamba asilimia 67 ya wahojiwa walisema hujadili masuala mbali
mbali ya kisiasa, asilimia 36 walisema hujadili sana siasa. Asilimia 83 ya wahojiwa wanasema
wanahudhuria mara nyingi mikutano ya kijamii.
Hata hivyo asilimia 34 ya wahojiwa wanaona mambo ya siasa na serikali
kuwa ya utatanishi (complicated). Hii
inapunguza nguvu ya ushiriki katika siasa.
Lakini hata hivyo, inashangaza kidogo kwamba asilimia 76 wanasema
wanaweza kuwafanya viongozi wao wawasikilize.
Tabia hii ni muhimu kwa demokrasia kwa sababu inaonyesha wananchi
wanaweza kuwawajibisha viongozi wao.
Ushiriki
mkubwa wa kisiasa huwasaidia Watanzania kujiunga katika kupigania haki
zao. Hivyo kiasi kikubwa cha wahojiwa
(karibu asilimia 69) walionyesha kwamba hujiunga na wenzao kudai haki zao. Hata hivyo asilimia kubwa hawajishirikishi
na siasa za kupinga (protest politics) na hawashiriki kwenye maandamano. Hata
hivyo wanaunga mkono demokrasia.
Asilimia 81 wanasema hawawezi kamwe kutumia nguvu kwa madai yoyote ya
kisiasa. Hii inaonyesha kuwa watanzania
walio wengi ni wapenda amani na hawawezi kutumia nguvu kwa ajili ya madai ya
kisiasa.
Njia nyingine
ya ushiriki katika siasa ni kuonana na viongozi wao. Ni muhimu wananchi kuwaona na kushauriana na viongozi wao wa serikali
kama watataka kuwa karibu na serikali yao na kuunga mkono maamuzi yake. Hivyo utafiti ulitaka kujua ni kiasi gani
wananchi wanashauriana na viongozi wao.
Waliulizwa; “Katika mwaka uliopita, ni mara ngapi uliwaona hawa wafuatao
ili wakusaidie kutatua matatizo yako?
Jedwali hapa chini linaonyesha watanzania wengi wanawaona viongozi wa
ngazi za chini kuliko wa ngazi za juu (asilimia 33). Hii ni ongezeko la asilimia 4 ukilinganisha na mwaka 2001. Hata hivyo watanzania wengi (asilimia 56)
wako radhi kuwaona viongozi wa dini kuliko kuwaona viongozi wa kisiasa
(Asilimia 34 tu ndiyo waliowaona viongozi wa vyama vya siasa).
Ni Kiasi gani
unawaona wafuatao kwenye matatizo?
|
|
2001 |
2003 |
|
Viongozi wa serikali za
mitaa/madiwani |
29 |
42 |
|
Watu wengine mashuhuri |
26 |
32 |
|
Viongozi wa dini |
49 |
56 |
|
Mbunge |
12 |
19 |
|
Kiongozi wa jadi |
12 |
27 |
|
Kiongozi wa chama |
13 |
34 |
|
Kiongozi wa serikali kuu |
9 |
34 |
Chanzo: “Results from Round II of Afrobarometer
Survey”
2.2.3 Uhuru wa Kisiasa
Uhuru wa
kisiasa ni kipimo cha kiwango cha ukomavu wa demokrasia katika jamii. Uhuru finyu unamaanisha demokrasia finyu
pia. Hapa ni tathmini ya uhuru wa
kisiasa kwa kuangalia uhuru wa kujieleza, uhuru wa kujiunga kwenye vikundi na
kutokushtakiwa ovyo, na usawa mbele ya sheria.
Uhuru wa
Kisiasa (Asilimia)
|
|
Mzuri |
Mzuri sana |
Sawa tu |
Mbaya |
Mbaya sana |
Sijui |
|
Uhuru wa kuongea unachofikiri |
53 |
23 |
11 |
8 |
3 |
4 |
|
Uhuru
wa kujiunga na chama chochote |
52 |
29 |
11 |
3 |
1 |
4 |
|
Hofu
ya kufungwa kwa kuonewa |
42 |
16 |
19 |
13 |
3 |
7 |
|
Uhuru wa kupiga kura |
46 |
31 |
13 |
6 |
2 |
2 |
|
Uwezo wa kuishawishi serikali |
35 |
13 |
19 |
19 |
8 |
6 |