TATHMINI YA HALI YA SIASA TANZANIA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA
MWAKA 2005
Na Philip J. Mangula, Katibu Mkuu wa CCM
1.0
UTANGULIZI
Itakapofika
Novemba mwaka 2005 Watanzania watapiga kura kwa mara ya tatu katika uchaguzi
utakaohusisha vyama vingi vya siasa.
Kwa mara nyingine tunategemea kubadilishana madaraka kwa amani kutoka
awamu moja kwenda nyingine. Uchaguzi wa
mwaka 2005 una mvuto na msisimko wa aina yake kwa sababu Rais aliyepo atatakiwa
kuachia madaraka kwa mujibu wa marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Hali hii inaleta ushindani si
tu ndani chama tawala bali pia hata ndani ya vyama vya upinzani. Tukirudi nyuma
kidogo ni muda mfupi tu tokea watanzania walipopiga kura mwaka 2000. Hiki ni
kipindi kizuri kwa wachunguzi wa masuala ya kisiasa kwa sababu mambo mengi
yanatokea au kufanywa ambayo huweza kutumika kama kigezo cha kupima demokrasia
nchini. Katika makala hii tutajitahidi kutathmini hali ya siasa za Tanzania
kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005. Tutachambua ahadi zilizotolewa wakati wa
uchaguzi wa mwaka 2000 na kuona ni jinsi gani zilitekelezwa au hazikutekelezwa
na athari zake kwa demokrasia, kwa kulinganisha na hali halisi ya sasa. Pamoja
na kuwa matukio muhimu ya kila siku yatachukuliwa katika kuelezea baadhi ya
mada tutakazojadili, si nia ya makala hii kujikita katika matukio ya kila
siku. Wakati tukielekea kipindi cha
uchaguzi mkuu wa 2005 ni muhimu tukafanya tafakuri za kina za nini kimefanyika
na maeneo ambayo bado kuna mapungufu.
Ni muhimu tukaeleza tokea awali kwamba tathmini itazingatia zaidi hali
ya siasa ilivyobadilika kuanzia mwaka 2000.
Lengo la tathmini ni kutoa mwanga wa mwelekeo wa kisiasa baada ya mwaka
2005.
Ili
kutuwezesha kuweka bayana tafakuri hii makala hii imegawanywa katika vipengele
vikuu vitatu:
(a) HALI YA SIASA BAADA YA
UCHAGUZI WA MWAKA 2000: MATARAJIO,
MAZURI NA MAPUNGUFU
·
Hali iliyojitokeza Zanzibar
·
Hatua za Kukabiliana na Rushwa ndani ya CCM na ndani ya
Serikali
·
Magomvi/Migogoro ndani ya vyama vya siasa na athari zake
katika ukuzaji wa demokrasia
·
Tathmini ya Imani ya Wananchi kwa Serikali
(b)
NAFASI YA VYOMBO VYA HABARI NA VYAMA VYA WANANCHI KATIKA KUKUZA DEMOKRASIA
·
Kushamiri kwa vyombo vya habari
·
Nafasi ya vyama vya wananchi kwenye ujenzi wa demokrasia
(c) KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2005 NA MUSTAKABALI WA TAIFA
● Umoja wa Kitaifa
● Mwelekeo wa wananchi Kisiasa
2. HALI YA SIASA
BAADA YA 2000
Uchaguzi Mkuu
wa Novemba 2000 ulijenga taswira mbili zinazokinzana Tanzania. Upande wa Tanzania Bara kwa ujumla uchaguzi
uliendeshwa kwa amani na utulivu na uvumilivu.
Hadithi, hata hivyo, ilikuwa tofauti kabisa upande wa Tanzania
visiwani. Uchaguzi ulileta utata mkubwa
na hata wasiwasi wa kutokea mgogoro wa kisiasa. Isingalikuwa ukomavu wa kisiasa uliokuja kuonyeshwa na wote
waliohusika, Tanzania ingaliwezaweza kuingia kwenye janga kama tunavyoshuhudia
nchi nyingine za Afrika. Kwa hakika
hali ya siasa ya Zanzibar na hofu ya siasa za vurugu ilikwishaainishwa na Tume
ya Nyalali[1]
ambayo iliona uwezekano wa chama kitakachoshindwa katika uchaguzi kuyakataa
matokeo.
Inatosha
kusema hapa kwamba haja ya muafaka ilionekana kuanzia awali kama ambavyo makala
zilizoandikwa na Prof. H. Othman, Bw. P. Mangula na Bw. S. S. Hamad[2]
zinaonyesha kwa namna tofauti umuhimu wa kukaa pamoja na kuzungumza. Muafaka II
wa mwaka 2001 ni kitu cha kujivunia na rekodi nzuri ya utatuzi wa migogoro
katika nchi za kiafrika. Matokeo ya
muafaka ni kama ifuatavyo:
(1) Kufanyika kwa
uchaguzi mdogo katika majimbo 16 ambayo awali Civic United Front (CUF) ilisusia
matokeo yake hivyo kuwawezesha kurejea tena kwenye siasa za ushindani bila
kupigana.
(2) Kuimarika kwa
amani na utulivu ambavyo vimeiwezesha nchi kupiga hatua za kimaendeleo. Kwa
mara ya kwanza CUF walishiriki kwenye sherehe za mapinduzi za mwaka 2003
kuonyesha kuwa wanaitambua serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
(3) Kuridhishwa kwa
wahisani na hali ilivyo Zanzibar na kuanza kutoa misaada kwa serikali iliyokuwa
imesitishwa. Hii imesaidia kuboresha hali ya uchumi na maisha ya wananchi kwa
ujumla.
(4) Kuundwa upya
kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ambayo itahusisha vyama vya siasa katika
uundaji wake.
2.1
Magomvi/migogoro
ndani ya vyama vya siasa
Kwa
bahati nzuri, Tanzania ina vyama 16 vya siasa vyenye usajili wa kudumu. Mojawapo ya mihimili ya siasa za kiliberali
ni kushindanisha sera za vyama vingi ili wananchi wapate fursa ya kuchagua
chama wanachoona kinafaa. Kwa vyovyote
vile mfumo wa siasa wa vyama vingi unahuishwa na uimara na uthabiti wa vyama
ambavyo vinakuwa tayari kuchukua fursa za kuongoza nchi kama chama tawala
kikidorora. Hali hii hukinyima usingizi
chama kinachotawala na hivyo kukifanya siku zote kitafute njia za kuboresha
utendaji wake – matokeo yake wananchi wanafaidika zaidi. Hali ni tofauti Tanzania, hasa Tanzania bara
kwa sababu bado haijafikia hatua chama tawala kikakosa usingizi kwa kuhofia
kupoteza madaraka kwa upinzani. Kama ripoti ya Profesa Mukandala[3]
ilivyoonyesha vyama vingi bado vinalegalega kwenye uchaguzi, havijajikita
mizizi vijijini, na bado havijajulikana sana ukiachilia mbali sifa za
waanzilishi. Kuna migogoro baina ya vyama na ndani ya vyama vyenyewe.
Nitaelezea kidogo.
Migogoro
imeshamiri ndani na baina ya vyama vya siasa hali inayowaacha wananchi njia
panda. Hapa tutazungumzia migogoro
katika baadhi ya vyama vikubwa vyenye wabunge na madiwani. Tumeshuhudia mgogoro mkubwa wa kugombea
madaraka ndani ya UDP. Ilianza kwa
kamati kuu ya chama hicho kumtimua Mwenyekiti Bwana John Cheyo. Baadaye msajili akabatilisha maamuzi ya
kamati kuu na kumrudisha Mwenyekiti Cheyo.
Kilichofuata ni timua-timua.
Baadhi ya wabunge waliotuhumiwa kushirikiana na Bwana Amani
Jidulamabambasi kumpindua Mwenyekiti wakawa wa kwanza kutimuliwa. Matokeo:
Aliyekuwa Mbunge wa UDP na Madiwani 9 walihamia CCM na wanachama 1,147 wa wilaya ya Bariadi walihamia CCM pia.
TLP
sasa hivi kunafuka moshi na kuna kila dalili ya mlipuko hali ikiachwa iendelee
ilivyo. Madiwani matano wa wilaya ya
Moshi Vijijini walihamia CCM na hivi
sasa kuna kampeni za uchaguzi mdogo zinaendelea. Tarehe 24/4/2004 Mwenyekiti wa TLP Mkoa wa Dar es Salaam ambaye
alikwua pia mfadhili wa chama Bw. Saab
Ally na Mwenyekiti wa Umoja wa
Vijana wa chama hicho wamehamia CCM.
Athari
za migogoro katika vyama vya siasa ni nyingi, na kwa ujumla wake zinachangia
kudorora kwa demokrasia. Panapokosekana
chama chenye upinzani wa kweli na nguvu ya siasa, hutokea chama kilichoshika
dola kikalala usingizi na kujisahau kabisa.
Wananchi ndio waathirika wakubwa wa hali hii.
Ni
jukumu la kila mmoja wetu na kila mdau kikiwemo chama tawala kuhakikisha kuwa vyama vya upinzani vinaimarika Tanzania. Hali ya vyama vya siasa Tanzania kama
inavyoonyeshwa kwenye jedwali lifuatalo inaonyesha kupungua nguvu kwa vyama vya
upinzani ukilinganisha na CCM.
Idadi ya kura ambazo vyama vilipata katika uchaguzi wa Bunge
2000
|
CHAMA |
IDADI YA
KURA |
ASILIMIA |
ONGEZEKO
TOKA 1995 |
|
|
1. 2. 3. 4. 5. 6. 7. 8. 9. 10 11. 12. 13. |
CCM NCCR-MAGEUZI CHADEMA CUF UDP TADEA NRA UMD TLP NLP UPDP PONA TPP |
4,634,047
258,591
99,461
792,378
315,357
9,647 70
7,550 652,535
2,507
14,818
11,789 10,206 |
65.3 3.6 4.2 11.2 4.4 0.1 0.001 0.1 9.2 0.04 0.2 0.2 0.1 |
+6
-18 - 2 - 6
+1.1
+ 1 0. 0. + 9 0 0 0 0 |
|
|
JUMLA |
|
100 |
|
Chanzo: Tume
ya Taifa ya Uchaguzi (NEC): Uchaguzi Mkuu wa 2000
NB: Taarifa hii haihusu uchaguzi katika majimbo
25 ambamo CCM ilipita bila kupingwa.
Tunaona
katika jedwali hapo juu kuporomoka kwa vyama vikubwa kama NCCR-Mageuzi ambacho
kilitawaliwa na migogoro iliyoishia kukigawa chama. Hapa nigusie tu kwamba CCM
kutokana na ukomavu wake kisiasa kimeweza kudhibiti migogoro kila
ilipojitokeza. Kipindi cha kuelekea
uchaguzi mkuu kitatawaliwa na migogoro ndani ya vyama na ni vyema vyama viweke
mikakati ya kukabiliana nayo.
2.2
Tathmini ya
kukubalika kwa serikali na chama
Uchaguzi
mkuu kwa kawaida ni tathmini ya kukubalika kwa chama kwa wananchi wapiga kura
(na hivyo serikali kitakayoiunda).
Hutokea umaarufu wa chama ukaporomoka ghafla mara baada ya uchaguzi mkuu
kwa sababu kadha wa kadha. Katika
utafiti uliofanyika hivi karibuni[4]
asilimia 63 ya wasailiwa wanakataa mfumo wa siasa wa chama kimoja. Asilimia 73 wanakataa utawala wa mtu mmoja
(personalized rule) hasa machifu au wazee (wa makabila). Asilimia 87 wanakataa kabisa utawala wa
kijeshi. Asilimia 86 wanapinga mawazo
ya kufuta bunge na kumpa rais madaraka yote.
Tafsiri mojawapo ya matokeo haya ni kwamba watanzania wanahitaji sana
mfumo wa demokrasia wa vyama vingi (yaani uliopo).
Kukataa udikteta (Asilimia)
|
|
Nakubali
Kabisa/Sana |
Nakubali |
Yote sawa |
Sikubali |
Sikubali
Kabisa |
Sijui |
|
Chama
kimoja tu kiruhusiwe kusimama kwenye uchaguzi |
12.0 |
17.0 |
7.0 |
25.0 |
38.0 |
1.0 |
|
Maamuzi
yote yafanywe na Mchifu au Baraza la Wazee |
4.0 |
9.0 |
10.0 |
33.0 |
40.0 |
4 |
|
Jeshi
litawale nchi |
2.0 |
4.0 |
5.0 |
28.0 |
59.0 |
2.0 |
|
Chaguzi
zisiwepo ili Rais aamue kila kitu |
2.0 |
4.0 |
6.0 |
28.0 |
58.0 |
2.0 |
Chanzo: “Results from Round II OF Afrobarometer
Survey”
2.2.1 Ukuaji wa Demokrasia
Katika jamii
nyingi demokrasia imehusishwa na maendeleo ya nchi kisiasa, kiuchumi na
kijamii. Kadri nchi inavyokuwa ya
kidemokrasia zaidi ndivyo inavyoongeza uwezekano wa kupata maendeleo. Hivyo kuna ulazima wa kuifanya demokrasia
kuwa sera ya taifa. Wananchi lazima
waridhishwe na kiwango cha demokrasia ili waunge mkono. Katika utafiti uliofanyika mwaka 2003
wahojiwa waliulizwa ni kwa kiasi gani Tanzania inafuata demokrasia. Kwa ujumla
asilimia 81 walisema Tanzania ni nchi ya kidemokrasia. Hata hivyo walisema demokrasia Tanzania bado
ina matatizo madogo. Asilimia 12 tu
walisema Tanzania ina demokrasia kamili, ambapo asilimia 19 walisema demokrasia
ya Tanzania ina matatizo makubwa.
Asilimia 8 walisema hakuna demokrasia kabisa Tanzania.
2.2.2 Ushiriki katika siasa
Demokrasia
inaweza tu kushamiri pale ambapo watu wanashiriki katika siasa. Watanzania wanapenda sana siasa na hii
inajidhihirisha kwamba asilimia 67 ya wahojiwa walisema hujadili masuala mbali
mbali ya kisiasa, asilimia 36 walisema hujadili sana siasa. Asilimia 83 ya wahojiwa wanasema
wanahudhuria mara nyingi mikutano ya kijamii.
Hata hivyo asilimia 34 ya wahojiwa wanaona mambo ya siasa na serikali
kuwa ya utatanishi (complicated). Hii
inapunguza nguvu ya ushiriki katika siasa.
Lakini hata hivyo, inashangaza kidogo kwamba asilimia 76 wanasema
wanaweza kuwafanya viongozi wao wawasikilize.
Tabia hii ni muhimu kwa demokrasia kwa sababu inaonyesha wananchi
wanaweza kuwawajibisha viongozi wao.
Ushiriki
mkubwa wa kisiasa huwasaidia Watanzania kujiunga katika kupigania haki
zao. Hivyo kiasi kikubwa cha wahojiwa
(karibu asilimia 69) walionyesha kwamba hujiunga na wenzao kudai haki zao. Hata hivyo asilimia kubwa hawajishirikishi
na siasa za kupinga (protest politics) na hawashiriki kwenye maandamano. Hata
hivyo wanaunga mkono demokrasia.
Asilimia 81 wanasema hawawezi kamwe kutumia nguvu kwa madai yoyote ya
kisiasa. Hii inaonyesha kuwa watanzania
walio wengi ni wapenda amani na hawawezi kutumia nguvu kwa ajili ya madai ya
kisiasa.
Njia nyingine
ya ushiriki katika siasa ni kuonana na viongozi wao. Ni muhimu wananchi kuwaona na kushauriana na viongozi wao wa serikali
kama watataka kuwa karibu na serikali yao na kuunga mkono maamuzi yake. Hivyo utafiti ulitaka kujua ni kiasi gani
wananchi wanashauriana na viongozi wao.
Waliulizwa; “Katika mwaka uliopita, ni mara ngapi uliwaona hawa wafuatao
ili wakusaidie kutatua matatizo yako?
Jedwali hapa chini linaonyesha watanzania wengi wanawaona viongozi wa
ngazi za chini kuliko wa ngazi za juu (asilimia 33). Hii ni ongezeko la asilimia 4 ukilinganisha na mwaka 2001. Hata hivyo watanzania wengi (asilimia 56)
wako radhi kuwaona viongozi wa dini kuliko kuwaona viongozi wa kisiasa
(Asilimia 34 tu ndiyo waliowaona viongozi wa vyama vya siasa).
Ni Kiasi gani
unawaona wafuatao kwenye matatizo?
|
|
2001 |
2003 |
|
Viongozi wa serikali za
mitaa/madiwani |
29 |
42 |
|
Watu wengine mashuhuri |
26 |
32 |
|
Viongozi wa dini |
49 |
56 |
|
Mbunge |
12 |
19 |
|
Kiongozi wa jadi |
12 |
27 |
|
Kiongozi wa chama |
13 |
34 |
|
Kiongozi wa serikali kuu |
9 |
34 |
Chanzo: “Results from Round II of Afrobarometer
Survey”
2.2.3 Uhuru wa Kisiasa
Uhuru wa
kisiasa ni kipimo cha kiwango cha ukomavu wa demokrasia katika jamii. Uhuru finyu unamaanisha demokrasia finyu
pia. Hapa ni tathmini ya uhuru wa
kisiasa kwa kuangalia uhuru wa kujieleza, uhuru wa kujiunga kwenye vikundi na
kutokushtakiwa ovyo, na usawa mbele ya sheria.
Uhuru wa
Kisiasa (Asilimia)
|
|
Mzuri |
Mzuri sana |
Sawa tu |
Mbaya |
Mbaya sana |
Sijui |
|
Uhuru wa kuongea unachofikiri |
53 |
23 |
11 |
8 |
3 |
4 |
|
Uhuru
wa kujiunga na chama chochote |
52 |
29 |
11 |
3 |
1 |
4 |
|
Hofu
ya kufungwa kwa kuonewa |
42 |
16 |
19 |
13 |
3 |
7 |
|
Uhuru wa kupiga kura |
46 |
31 |
13 |
6 |
2 |
2 |
|
Uwezo wa kuishawishi serikali |
35 |
13 |
19 |
19 |
8 |
6 |
|
Usalama
kutokana na uhalifu na fujo |
34 |
9 |
18 |
26 |
10 |
3 |
|
Usawa kwa wote |
37 |
10 |
23 |
18 |
8 |
4 |
2.2.4 Kiwango cha kukubalika/uhalali kwa sherikali/chama
Serikali
ambayo inatimiza ahadi zake za demokrasia na kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa
na huduma muhimu kwa kawaida huungwa mkono na wananchi. Uhalali wa serikali ni ishara ya uzuri wa
utendaji kazi wake. Watu lazima waone
kuwa serikali inawakilisha mawazo na ndoto zao. Serikali ya namna hii inaweza kufanya maamuzi ambayo wananchi wote
watayaheshimu.[5] Utafiti
ulitaka kupima kiwango cha uhalali wa serikali kwa kuangalia vyombo vya
serikali kama katiba, polisi, mahakama na idara ya kodi. Hivi ni vyombo vya serikali ambavyo
vinahitaji imani ya wananchi ili serikali iweze kufanya kazi sawasawa.
Maoni ya
wananchi kuhusu uhalali wa serikali
|
|
Nakubali
Sana |
Nakubali |
Yote Sawa |
Sikubali |
Sikubali
Kabisa |
Sijui |
|
Katiba
yetu inaeleza matarajio na ndoto za watanzania |
14 |
43 |
10 |
10 |
5 |
18 |
|
Mahakama
zina haki ya kufanya maamuzi yatakayoheshimiwa na watu wote |
19 |
49 |
14 |
10 |
4 |
4 |
|
Polisi
wana haki siku zote ya kufanya watu waheshimu sheria |
20 |
46 |
15 |
11 |
6 |
3 |
|
Idara
ya kodi ina haki ya kutoza kodi na kuhakikisha watu wanalipa |
16 |
41 |
15 |
14 |
9 |
5 |
Tukiangalia
jedwali hapo juu, kiasi kikubwa cha wahojiwa (asilimia 57) wanaona katiba
inaelezea mawazo na ndoto zao. Hata
hivyo idadi hii bado ni kidogo. Wasomi
na wanasiasa hapa Tanzania wameendelea kusisitiza umuhimu wa kuwa na mjadala wa
kitaifa wa katiba. Serikali inaonekana
inalifanyia kazi hili kwa sababu karibu itapeleka muswada wa mabadiliko ya
katiba bungeni. Mahakama zinaonekana
kupata uungwaji mkubwa wa mkono (uhalali) kwa kuwa na theluthi mbili (asilimia
68) ya wananchi wanaokubali kuwa mahakama zinatoa maamuzi yenye
kufuatwa/kutekelezwa. Watu wengi kiasi
(asilimia 66) wanaona polisi wana haki ya kuhakikisha wananchi wanafuata
sheria. Kwa ujumla wananchi wanaipa
uhalali serikali iliyopo lakini wanaona umuhimu wa mabadiliko kwenye nyanja
fulani za uongozi.
3.1
Hali ya Vyama vya Habari
Katika mfumo
wa siasa ambao Tanzania inaujenga, uhuru wa kuzungumza ni mhimili mmojawapo wa
siasa. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania katika Ibara ya 18(1) na (2) inazungumzia uhuru wa mawazo na
inasomeka:
(i)
Bila ya kuathiri sheria za nchi, kila mtu yupo huru kuwa na
maoni yoyote au kutoa vyema mawazo yake, na kutafuta, kupokea na kutoa habari
na dhana zozote kwa chombo chochote bila kujali mipaka ya nchi; na pia ana
uhuru wa mawasiliano yake kutoingiliwa kati.
(ii)
Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu
matukio muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, na juu ya masuala muhimu kwa
jamii.[6]
Umuhimu
wa vyombo vya habari kama nyenzo muhimu katika kuimarisha uhuru wa kujieleza/kuzungumza
hauwezi kusisitizwa zaidi hapa. Ni
vigumu kuifikiria hata hiyo demokrasia yenyewe kama uhuru wa vyombo vya habari
utakuwa umefinyangwa. Hapa Tanzania
uhuru wa vyombo vya habari na nafasi yake katika ukuzaji wa demokrasia umekuwa
ukiimarika na wakati mwingine umetumika vibaya.
Bado kuna madai kwamba sheria nyingi
kandamizi zimeendelea kubaki katika
vitabu vya sheria licha ya Tume ya Jaji Nyalali kupendekeza zifutwe. Sheria zinazodaiwa kukwaza uhuru wa habari
ni kama zifuatazo: Sheria ya Usalama wa Taifa (National Security Act, N. 3);
Sheria ya Magazeti (Newspaper Act, No. 3) ya 1976; na Kanuni za Utumishi wa
serikalini (Civil Service Regulations and Standing Orders). Inadaiwa kwamba sheria hizi ni kama
zinachukua kwa mkono wa kushoto haki ambayo ilikwishatolewa kwa mkono wa kulia
na katiba ya nchi.
Hatua
ambayo imechukuliwa hivi karibuni na serikali ya kurekebisha sheria ya
utangazaji wa mwaka 1993 ya kuruhusu Radio na Television binafsi zitangaze nchi
nzima inahitaji kuungwa mkono na wapenzi wa uhuru wa habari na demokrasia
nchini. Sheria zingine ambazo inadaiwa
ni kandamizi zinafanyiwa kazi.[7]
3.2 Hali ya Vyama vya Wananchi Tanzania
Vyama
vya wananchi (Civil Society Organizations – CSOs) ni mhimili muhimu katika
kujenga demokrasia na kuleta maendeleo ya jamii kwa ujumla.[8] Vyama vya wananchi viliendelea kukua na
kujiongezea uwezo tangu uchaguzi mkuu uliopita. Mpaka mwaka 2000 takwimu za utafiti zinatoa mwelekeo ufuatao wa
idadi ya vyama vya wananchi.
3
Jumla ya vyama vyote vya wananchi vilivyoandikishwa ni 2,700
kati ya hivyo 93 viko Zanzibar na Pemba
4
Mikoa inayoongoza ni Dar es Salaam (808), Arusha (158),
Morogoro (113), Kagera (87), na Kilimanjaro (86).
5
Mikoa ya kati ni pamoja na Mbeya (56), Mwanza (54), Dodoma
(53), Songea (52), Tanga (51) na Iringa (48).
6
Mikoa ya chini ni pamoja na Mtwara (32), Kigoma (29), Rukwa
(26), Shinyanga (17), Singida (15) na Lindi (10).
Hili ni
ongezeko kubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma. Tafsiri ya haraka ya ongezeko hili ni kuwepo kwa mazingira rafiki
kwa vyama vya wananchi pamoja na mwamko wa kisiasa wa wananchi.
Idadi ya NGOs
kwa mkoa, jinsia na kaz zake (Baadhi ya Mikoa)
|
|
MIKOA |
||||||
|
KAZI ZA NGO |
DSM |
MWANZA |
ARUSHA |
||||
|
|
WOTE |
WAKE |
JUMLA |
WOTE |
WAKE |
JUMLA |
WOTE WAKE JUMLA |
|
Starehe na Utawala |
5 |
- |
5 |
- |
- |
- |
1 - 1 |
|
Elimu na Utafiti |
87 |
2 |
89 |
7 |
1 |
8 |
16 - 16 |
|
Afya |
35 |
2 |
37 |
1 |
- |
1 |
7 1 8 |
|
Huduma za Jamii |
22 |
- |
22 |
- |
- |
- |
3
- 3 |
|
Mazingira |
48 |
1 |
49 |
16 |
- |
16 |
11 1 12 |
|
Maendeleo ya jamii |
460 |
63 |
528 |
23 |
10 |
33 |
95 6 101 |
|
Uhamasishaji |
7 |
- |
7 |
- |
- |
- |
2 1 3 |
|
Kimataifa |
34 |
- |
34 |
3 |
1 |
4 |
4 - 4 |
|
Dini |
3 |
- |
- |
- |
- |
- |
1 - 1 |
|
Jumla |
701 |
68 |
769 |
50 |
12 |
62 |
140 9 149 |
Chanzo: Mchanganuo wa “Directory of Tanzania
Non-Governmental Organizations – 2000”
Pamoja na
idadi ya vyama vya wananchi kuongezeka tunapaswa kujiuliza kama ufanisi wake
pia umeongezeka. Kwa ujumla vyama vingi
vya wananchi vinakabiliwa na matatizo mengi, mengine ya kiutendaji, na mengine
ya miundo mibovu na ukosefu wa utaalam na uzoefu. Ni vigumu kupitia kazi na michango ya vyama vyote lakini
tutaangalia tu baadhi.
Vyama vya
wananchi vilivyoonekana kutoa hamasa kubwa ni vile vya uhamasishaji. Tumeshuhudia kwa mfano TAMWA (Tanzania Media
Women’s Association) ikifanya kazi kubwa ya uhamasishaji dhidi ya ukandamizaji
wa haki za wanawake na watoto. Tafiti
zao mbali mbali zinaleta upeo mpya wa kuyaendea matatizo haya ambayo yalianza
kuonekana kama sehemu ya kawaida ya jamii. TAMWA kwa kushirikiana na TGNP
ilishinikiza kupitishwa kwa muswada wa sheria uliotoa adhabu kali kwa
wanaonyanyasa watoto na akina mama.[9] Katika hali isiyo ya kawaida, katika Mkoa
wa DSM UONGHOZI wa TAMWA ulikwenda
POLISI na kufanikiwa kuzuia Msichana wa
umri mdogo kuolewa. Kulitokea tafrani
na mjadala mkali lakini iliwezekana.
4.0 KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2005 NA
MUSTAKABALI WA TAIFA
Tunapoelekea uchaguzi, mkuu na sasa ikiwa imebaki chini ya
miezi kumi na minane kabla ya uchaguzi homa ya uchaguzi imeanza kupanda. Vichwa
vya habari vya magazeti vinapambwa na picha za wale ambao wanatarajiwa kushika
wadhifa mkuu wa seriakali (yaani urais).
Vichwa vya habari vya aina hiyo vinafanya magazeti yauzike. Katika
mijadala inayoendelea sasa hivi ni ule wa wale wanaosema mgombea urais lazima
ajulikane mapema kwa wapiga kura ili waweze kupata nafasi ya kutosha ya
kumtafakari kama kweli anafaa kuwa rais wa nchi. Hoja ni kwamba rais hana chama cha siasa, akishachaguliwa anakuwa
rais wa wote na hakuna wanaosema iwe mapema kwa kiasi gani. Hata hivyo utaratibu wa kumpata mgombea urais kutoka CCM utaanza 2005 mwezi
Machi kwa kuchukua fomu na kutafuta Wadhamini wasiopungua 250 kutoka Mikoa isyopungua
10 ikiwemo miwili
ya Zanzibar (Unguja 1/Pemba 1). Hapa chini nitazungumzia nyanja chache
zinazogusa uchaguzi na mambo yanayopaswa kufanyika ili kuondoa uwezekano wa
kuwa na uchaguzi usioleta muafaka wa kitaifa
4.1 Mfumo wa uchaguzi
Mfumo
wa uchaguzi wa Tanzania ni ule wa kiti kwenda kwa aliyepata kura nyingi (first
past the post). Mfumo huu una mapungufu yake kwa kuwa unavifungia nje ya
uongozi vyama vidogo na hivyo kuvifanya vikate tamaa.[10]
Mfumo wa sasa unavifanya vyama vidogo pamoja na wale wanaovipigia kura kukata
tamaa na hasa baada ya kujaribu kupata viti kwa muda mrefu na kushindwa. Mfumo wa uchaguzi ambao unampa kiti
aliyepata kura nyingi hautoi nafasi ya kustawi kwa vyama vidogo na unajenga
mazingira ya nchi kuwa na vyama vikubwa viwili na vingine hubaki havina nguvu
wala uwezo wa kubadilisha chochote katika siasa za nchi. Mfumo huu una
mapungufu. Kunakosekana uwiano wa kura
na idadi ya viti ambavyo chama kinapata. Kwa mfano, mwaka 1995 CCM ilipata
asilimia 59.2 ya kura zote lakini ilipata asailimia 80.2 ya viti vyote bungreni.
CUF ilipata asilimia 5 ya kura lakini ikapata viti asilimia 10.3 na NCCR
Mageuzi ilipata kura aslilimia 21.8 lakini ikapata asilimia 6.9 tu ya viti
vyote. Kwa jinsi hali ilivyo hapa Tanzania mfumo wa uchaguzi unampa kiti yule
mwenye kura nyingi na unaonekana kama utoaji zawadi kutokana na ushindi kwa
mgombea wa chama tawala. Sasa hivi ukishashinda kura za maoni na ndani ya CCM
unakuwa umeshashinda kiti cha ubunge kwa sababu hakuna upinzani wenye
nguvu. Hata hivyo zipo faida nyingi tu
za kuwa na mfumo unaompa kiti yule aliyepata kura nyingi. Moja kubwa ni kwamba
ni rahisi kuutekeleza na huwezesha kuundwa kwa serikali iliyo imara. Ili
kujaribu kupunguza athari za mfumo huu Halmashauri Kuu ya taifa imependekeza
Serikalini kwamba kuwe na kura za uwiano kwa wabunge wanawake ambao
hawatapungua 30% ya Wabunge wote 247 waliomo Bungeni. Uwiano huo tayari unatekelezwa Baraza la Uwakilishi
Zanzibar. Aidha kutakuwa na kundi la
pili la Wabunge watakaopatikana kwa uwiano wa kura. Kundi hili ni la jinsia zote.
Jumla ya Wabunge watakaopatikana kwa utaratibu huu watakuwa 103 ambayo
ni asilimia 29.4 ya Wabunge wote (350).
Kama muswada huu utapitishwa utaboresha kwa kiwango kikubwa mfumo wa
sasa wa uchaguzi.
4.2 Asasi za
kusimamia uchaguzi
Asasi muhimu
za kusimamia na kuamua katika ushindani zimekwishaundwa na kusimikwa katika
uwanja wa ushindani. Asasi kuu tatu ni
Msajili wa Vyama vya Siasa, Tume ya Uchaguzi (NEC na ZEC) na Mahakama. Asasi hizi zinakubalika na wadau walio wengi
kwa kiasi kikubwa, lakini bado kuna matatizo madogo madogo.
Kwanza,
imekuwepo migongano kati ya vyama vya upinzani na Msajili wa Vyama vya Siasa
tangu mwanzo wa mpito. Vyama vya
upinzani vinaona kama Msajili anaweka mkazo mkubwa zaidi juu ya wajibu wa kukosoa
na kuadhibu kuliko wajibu wa kulea na kuvikuza vyama.
Pili, Tume ya
Taifa ya Uchaguzi (NEC) imekwishaonyesha uwezo wa kusimamia uchaguzi kwa
ufanisi na ushirikiano na vyama huku Tanzania Bara, lakini wajibu wake na
mahusiano yake na ZEC huko Zanzibar bado vina utata. ZEC ilikuwa moja ya asasi zilizotakiwa kurekebishwa na Muafaka wa
2001.
Tatu, tangu
mwanzo wa mpito mahakama zimejihusisha na kesi za uchaguzi, kwa mfano, kesi ya
Mchungaji Mtikila kuhusu wagombea binafsi, kesi ya Mtei/Marando kuhusu matumizi
ya vyombo vya habari vya umma (hasa RTD) wakati wa kampeni za uchaguzi, kesi ya
Mkuu wa Wilaya (DC) kutoa vibali vya mikutano ya vyama vya siasa, malalamiko
mbalimbali dhidi ya uchaguzi, kesi kuhusu kuweka shilingi milioni tano kwa
ajili ya kufungua kesi ya uchaguzi, n.k.
Nne, kuna
mjadala miongoni mwa vyama vya upinzani pia
kama wakuu wa mikoa (RCs) na wakuu wa wilaya (DCs) waendelee kuwa
waamuzi na wachezaji wa “mchezo wa
siasa”. Viongozi hawa ni wanasiasa na
huteuliwa na Rais kwa msingi wa uanachama wa chama tawala.
Tano, kiwango cha kujivua ushabiki wa chama tawala
(delinking) kwa watumishi wa serikali (wanaotumiwa na tume za uchaguzi wakati
wa uchaguzi na katika makao makuu yake), na vyombo vya dola vinavyosimamia
usalama katika mikutano ya vyama ya
kawaida na ya kampeni za uchaguzi unatiliwa mashaka na vyama vya upinzani. Kwa mujibu wa ripoti za ufuatiliaji
uchaguzi, ushabiki wa chama tawala ulikuwa mkubwa katika uchaguzi wa 1995 na
kisha kupungua kiasi katika uchaguzi wa 2000 (isipokuwa Zanzibar).[11] Ushabiki huu utaendelea kupungua kadri
ambavyo utamaduni mpya wa kisiasa wa vyama vingi unavyozoeleka miongoni mwa
wadau mabalimbali.
Kumekuwapo
vuguvugu kwenye duru za vyama vya kisiasa na jamii kwa ujumla kutaka suala la
mgombea binafsi liruhurisiwe. Hili linaendena na upeo wa siasa za
kiliberali ambazo hutoa vikwazo vyote katika kushiriki siasa. Hali ilivyo sasa
hivi mtu asiyekuwa na ushabiki wa vyama vya siasa hawezi kabisa kuchaguliwa
kuwa kiongozi katika ngazi yoyote ile.
Tume ya Jaji Kisanga ilionyesha matokeo yafuatayo: Kati ya washiriki 17,891 waliohojiwa
Zanzibar 17,577 (98.24%) walitaka
wagombea binafsi wasiruhusiwe na 309 (1.73%) walitaka waruhusiwe. Kwa Tanzania Bara washiriki 31,574 kati ya 35,459 (89.4%) waliotoa maoni walikataa wagombea binafsi na
3,743 (10.6%) walitaka wagombea binafsi
waruhusiwe.
4.3 MUAFAKA WA
KITAIFA
Uchaguzi
katika nchi yoyote ile ni njia nzuri ya kuleta muafaka wa kitaifa. Wananchi
wanapopiga kura wanaonyesha imani yao kwa vyama na watu wanaowachagua.
Wanaochaguliwa wanakuwa na jukumu zito la kuwatumikia wananchi na kuhakikisha
kuwa wanatimiza ahadi walizotoa wakati wa uchaguzi.
Baada ya
uchaguzi 1995 na ule wa 2000 tulishuhudia vurugu kule Zanzibar kutokana na
kukosekana Muafaka wa Kitaifa. Hapo
palikuwa hakuna kuelewana. Sera za
chama Tawala zilikuwa hazitekelezeki kwa sababu ya upinzani kutoka kwa
wasiokubaliana na matokeo. Nchi
ilishindwa kutawalika. Wahisani
waliamua kusitisha misaada yote na hivyo kuifanya hali ya uchumi kuwa mbaya na maendeleo
kudorora. Kimsingi shughuli za utalii
zilipungua na kwa hiyo kupunguza pato la serikali. Hali hii tunaweza kuiita kulikuwa na mzunguko wa siasa za chuki
katika nchi.
Kijamii watu
waligawanyika makundi makundi. Tulishuhudia watu wa familia moja kugawanyika
mara mbili kwa sababu ya tofauti za kisiasa. Watu waliacha hata kuzikana kama
wanapishana mitazamo ya kisiasa! Shule na zahanati zilisusiwa. Vurugu na wingu
zito likatanda na kila mmoja akashindwa kuelewa mustakabali wa taifa.
Mwisho
ni vitendo vya hujuma dhidi ya
serikali. Hali iliyofuatia uchaguzi mkuu wa Zanzibar mwaka 2000 ilikuwa ya
kutatanisha. Ususiaji wa uchaguzi uliendana na vitendo vya hujuma vikihusisha
kulipua mabomu mali za serikali. Hatuna haja ya kurudia kwamba kwa mara ya
kwanza Tanzania ilizalisha wakimbizi mwaka 2001.
Tunapoelekea
uchaguzi wa 2005 kuna vitu viwili ambavyo lazima tuvitilie mkazo ili
mustakabali wa taifa letu uwe ni wa kutabirika. Kwanza ni kuendelea kupambana
na rushwa ambayo ilijitokeza kwa nguvu
mwaka 2000 na pili haja ya kukamilisha uamuzi wa kuwa na daftari la kudumu la wapiga kura. Nitaelezea kwa kifupi.
Tumeongelea
katika makala hii kwamba rushwa ilikuwa ni kero namba moja ambayo serikali ya
CCM chini ya Rais Mkapa imedhamiria kupambana nayo. Juhudi hizi zinaungwa mkono
na kila anayelitakia mema Taifa hili. Bahati mbaya baadhi ya wagombea
waliingiza mchezo mchafu katika siasa.
Watu ambao hawana sifa za kutosha za kugombea na kushinda hujiingiza katika
njia za makato za kutafuta ushindi – walijaribu kuwarubuni wapiga kura kwa
kuwapa rushwa. Athari yake ni kuwa mtu anayepata uongozi kwa rushwa
ataiendeleza rushwa mara baada ya kuchaguliwa kushika wadhifa wake hivyo
kuendeleza mzunguko wa rushwa. Lakini mbaya zaidi ni kwamba hata kama kutakuwa
na kiongozi mzuri maadam tu hawezi kutoa rushwa basi hawezi kuchaguliwa. Mwishowe
ni kuwa na taifa linaloongozwa na matajiri watoa rushwa. Hawa asilani hawawezi
kutekeleza matakwa ya wananchi na wanawafanya wananchi kukata tamaa na mfumo
uliopo wa uongozi. Wananchi wakikata tamaa watatafuta mbinu zozote hata kama ni
za vurugu kuiondoa madarakani serikali.
Halamshauri
Kuu ya Taifa ya CCM ilifuta matokeo ya
kura za maoni kwenye majimbo matatu kwa tuhuma na ushahidi wa mazingira ya
rushwa. Katika majimbo manne waliachwa
waliiongoza katika kura za maoni akateuliwa mgombea aliyeshika namba tatu. Katika majimbo matatu waliachwa walioongoza
katika kura za maoni wakateuliwa walioshika nafasi ya pili.
Kwa hiyo
katika uteuzi wa wagombea ndani ya CCM tulishuhudia baadhi ya matokeo ya kura za maoni yakitenguliwa na kuteuliwa
wengine walioonekana na sifa zinazofaa na ambao hawakukiuka maadili ya chama.
CCM inaandaa utaratibu mpya wa kura za maoni ili, pamoja na mambo mengine,
kupunguza uwezekano wa rushwa. Tuna uhakika kuwa elimu ya uraia pia itapunguza
kiasi kikubwa cha matumizi ya rushwa kujipatia madaraka. Kadri wananchi
wanvyokuwa na uelewa mkubwa wa mambo ya kisiasa ndivyo ambavyo wataepa kuwapa
madaraka watoa rushwa. Mifano ipo mingi .
Kitu kingine
ambacho kimeonekana kuwa muhimu ni
kuwepo kwa daftari la kudumu la wapiga kura.
Hivi sasa kila uchaguzi wapiga kura hujiandikisha na baada ya kupiga
kura orodha hiyo haitunzwi kwa ajili ya uchaguzi mwingine. Katika uchaguzi wa mwaka 2000 yalijitokeza
malalamiko mengi ya watu kujiandikisha na kupiga kura mara mbili au zaidi. Watu
wengine pia kwa kukosa muda huwa hawajiandikishi kupiga kura hivyo kuwanyima
nafasi hii muhimu. Kule Zanzibar hii ilikuwa ni moja ya makubaliano ya Muafaka
II. Kwa kutambua umuhimu wake serikali imeazimia kuwa mpaka ifikapo uchaguzi
mkuu wa 2005 daftari la kudumu la wapiga kura liwe tayari. Tunaambiwa
maandalizi yote muhimu yamekamilika na zoezi litaanza wakati wowote. Daftari la
kudumu la wapiga kura lazima liaminiwe na wadau wote na liwe bora.
Pamoja na
mambo mengine yanayohusu daftari hilo
kuna mjadala juu ya utaratibu wa nani
anastahili kuandikishwa na nani hastahili. Baada ya kuandikishwa panatakiwa
kuwa na utaratibu mzuri wa kulifanyia marekebisho daftari hilo. Wananchi wana
uwezo wa kuweka pingamizi kwa mtu
wanayedhani hastahili kuwemo kwenye daftari la kudumu. Kwa kawaida orodha hiyo
huchapishwa na kuwekwa bayana kwa ajili ya kuikagua. Hata hivyo elimu bado
inahitajika kwa ajili ya kuwafahamisha wapiga kura umuhimu wa daftari la
kudumu. Pia lazima waelimishwe mapungufu yake ili wasije wakadhani daftari la
kudumu la wapiga kura ndio muarobaini
wa matatizo yote ya uchaguzi.[12]
5.0 MATARAJIO BAADA
YA 2005
5.1 Kujenga umoja
wa kitaifa
Kama taifa
lengo la kuingia katika uchaguzi mkuu ni kutaka kutafuta uhalali wa kuongoza
kutoka kwa wananchi ambao ndio wenye uamuzi wa mwisho wa nani ashike hatamu za
uongozi wa nchi. Sio lengo la makala hii kutabiri nini kitatokea mwaka 2005
baada ya uchaguzi. Katika sehemu hii ya mwisho tutajaribu kwenda mbele zaidi na
kuangalia yanayoweza kutokea baada ya 2005.
Katika uchaguzi
wa mwaka 2000 na chaguzi ndogo zilizofanyika Mei mwaka 2003 CCM iliendelea
kupata ushindi na hivyo kuonyesha imani ya wananchi kwa chama na serilkaili
yake. Kwa hali ilivyo sasa tunaweza kusema bado CCM ni chama chenye nguvu na
kinachoweza kutoa ushindani mkali kwa vyama vingine. Ndiyo sababu lilipozuka
suala la kupokezanan urais kati ya bara na visiwani, watu wote hata viongozi wa
vyama vya siasa ya upinzani walitoa maoni yao ya nini kifanyike ndani ya CCM
ili kufikia muafaka juu ya jambo hili. Kifupi tu hapa kinachoonekana dhahiri ni
kwamba vyama vingine vinaona vina uwezekano finyu wa kuitoa CCM madarakani.
Lakini ni
lazima tuseme kwamba siasa mara nyingi huwa hazitabiriki. Tukiangalia chaguzi
zilizowahi kufanyika katika nchi jirani na yetu vyama tawala viliweza kutolewa
madarakanai na vyama ambavyo awali havikuwa vikijulikana kabisa. Je hii inaweza
kutokea Tanzania? Kiashiria kimojawapo
kikubwa ni mbio za urais ndani ya CCM.
Utaratibu wa CCM wa kumpata mgombea wake wa Urais ni wa kidemokrasia sana. Aidha ushindi wa kishindo wa 1995 (61.7%) na
wa 2000 (71.4%) ni tofauti na ushindi wa 30 – 35% wa mgombea Urais wa KANU
ambaye utaratibu usio wa kidemokrasi wa kuteuliwa kwake ulisababisha baadhi ya
watu maarufu kujitoa ndani ya chama hicho na kujiunga na kambi ya upinzani na
hivyo kuimarisha safu ya upinzani.
Kazi kubwa
kwa CCM ni kujitahidi kuzuia makundi ndani ya CCM yanayotokana na ushabiki kwa
mgombea fulani kabla ya wakati. Tujiulize, NARC inawezekana Tanzania? Mazingira ya siasa za Tanzania ni tofauti
sana na siasa za Kenya ukiangalia hasa ufuasi wa vyama vya siasa, hivyo
hapaonekani kuwepo uwezekano wa
kilichotokea Kenya kutokea pia Tanzania. Kama mgombea ataonekana dhahiri
anapendwa na watu wengi atachaguliwa na
Mkutano Mkuu wa CCM. Kama anayeshindwa
kwenye Mkutano Mkuu ataamua kujitoa na timu yake na kujiunga na chama cha
upinzani, anaweza kutoa upinzani mkali lakini hawezi kushinda. Ndiyo sababu tunasema itahitajika busara na
ukomavu wa hali ya juu ili kuweza kumpata mgombea wa uraisi wa mwaka 2005 ndani
ya CCM bila kuitikisa CCM yenyewe wala misingi ya umoja wa kitaifa.
5.2 Utamaduni wa Kisiasa
Watanzania wanasifika kwa kuwa na sifa ya amani na utulivu.
Lakini amani na utulivu vinaendana kwa karibu sana na uvumilivu wa kisiasa. Kwa
kadri ambavyo wananchi wanakuwa na imani na serikali yao ndivyo wanavyokuwa
wavumilivu zaidi wakitumaini kuwa serikali inafahamu matatizo yao na
inayashughulikia. Kama wananchi wanakuja kugundua kuwa uvumulivu wao
haokuonyesha dalili zozote za mafanikio wanaanza kukosa subira. Mtafuruku
utafukuta ndani ya nchi. Hicho kitakuwa kiashiria cha mgogoro. Wakati wa
uchaguzi mkuu ujao wananchi itabidi waoyeshe subira na ukomavu wa hali ya juu
ikiendana na imani kwa taasisi za kusimamia uchaguzi. Tuna kila sababu za kusema
uchaguzi ujao utafanyika kwa amani.
Ni dhahiri
kwamba umaskini unaweza kutoa cheche za kisiasa. Lakini utafiti unaonyesha pia kwamba
wananchi wa Tanzania wanao uvumilivu mkubwa na kiwango cha juu cha kuaminiana
kijamii na kisiasa. Chapisho moja lina
kichwa cha habari kinachowaelezea Watanzania kuwa “Raia Wasiolalalmika na
Walengwa Wavumilivu.”
6.0 HITIMISHO
Tukirejea
yale tuliyoyasema kwenye makala hii, Tanzania imekuwa na utamaduni wa
kubadilishana madaraka kwa njia za amani na za kikataba. Hali haitakuwa tofauti
mwaka 2005. Tumetoa viashiria vya migogoro kama sheria, taratibu na miongozo ya uchaguzi haitafuatwa kama
inavyotakiwa. Tumegusia mfumo wa uchaguzi na haja ya kuweka uwiano kati ya
mifumo miwili ya uchaguzi ili kupunguza tofauti kubwa kati ya kura na idadi ya
viti kwa chama. Pamoja na yote haya tunabakia kuwa Taifa moja. Kwa hiyo wakati tukiwa katika ushindani wa kisiasa,
tubaki na misingi yetu ya utaifa.
Dira ya Taifa
ya Maendeleo 2025 kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na 2020 kwa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ni makubaliano ya mwelekeo uliopata ridhaa ya
wananchi wote. Katika dibaji Rais
Benjamin William Mkapa anaandika,
“Amani,
Utulivu na Usalama wa Raia na Mali zao ni mazingira ya lazima kabisa na ya
msingi kwa maendeleo. Bila mazingira
hayo dira hii haitakuwa na maana na wala hatutapata maendeleo. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kuepuka
kila linaloweza kuwagawa Watanzania kama vile kubaguana kwa msingi wa dini,
kabila, rangi, jinsia au eneo analotoka mtu.
Ni wajibu wa kila mmoja wetu pia kumtenga na kumsuta ye yote
anayeleta, kushabikia, au kuleta
dharau, mifarakano, chuki na kutoaminiana katika nchi yetu.”
REJEA
[1] Tazama Haroub Othman, (2002) “Hali ya Zanzibar Baada ya Uchaguzi Mkuu”, Katika Uimarishaji wa Demokrasia na Utawala wa Kidemokrasia Tanzania. Vitabu Vya Programu ya REDET. Uk. 184
[2] Makala hizi kwa pamoja zinapatikana katika kitbu cha REDET (2002) Uimarishaji wa Demokrasia na Utawala wa Kidemokrasia Tanzania. Uk 169 - 205
[3] Tazama Mukandala (2003) Hali ya Siasa Tanzania: Tathmini ya Miaka Kumi ya Vyama Vingi, 1992 – 2002. Makala iliyowasilishwa kwenye Semina ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa na Makda wa CCM, Dodoma 29/1 – 2/2/2003
[4] Tazama Amon Chaligha and Yul Derk Davis 2004 “Results from Round II Afrobarometer Survey. REPOA 9th Annual Research Workshop
[6] Kama ilivyonukuliwa kutoka Lawrence Kilimwiko na Gervas Moshiro (2000)“Nafasi ya vyombo vya habari katika kukuza demokrasia, Utamaduni wa Siasa na Hatma ya Demokrasia Tanzania. REDET
[7] Tazama pia Makala ya Mukandala, op. cit na Anthony Ngaiza (2002) Hali ya vyombo vya habari nchini katika Uimarishaji wa Demokrasia na utawala wa Kidemokrasia Tanzania
[8] Andrew Kiondo (2002) “Hali ya vyama vya Wananchi” katika Uimarishwaji Demokrasia na Utawala wa Kidemokrasia Tanzania. Vitabu vya REDET
[9] Kiondo, A (2002) Hali ya Vyama vya Wananchi katika Madumulla, J.S Uimarishaji Demokrasia na Utawala wa Kidemokrasia Tanzania. REDET, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
[11] Tazama, kwa mfano, Max Mmuya (2002) “Hali ya Taasisi na Wananchi: Hali za Vyama vya Siasa” katika Uimarishaji wa Demokrasia na Utawala wa Kidemokrasia Tanzania. REDET Publications