TATHMINI YA HALI YA SIASA TANZANIA KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA MWAKA 2005  

Na Philip J. Mangula, Katibu Mkuu wa CCM

 

 

1.0            UTANGULIZI

Itakapofika Novemba mwaka 2005 Watanzania watapiga kura kwa mara ya tatu katika uchaguzi utakaohusisha vyama vingi vya siasa.  Kwa mara nyingine tunategemea kubadilishana madaraka kwa amani kutoka awamu moja kwenda nyingine.  Uchaguzi wa mwaka 2005 una mvuto na msisimko wa aina yake kwa sababu Rais aliyepo atatakiwa kuachia madaraka kwa mujibu wa marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Hali hii inaleta ushindani si tu ndani chama tawala bali pia hata ndani ya vyama vya upinzani. Tukirudi nyuma kidogo ni muda mfupi tu tokea watanzania walipopiga kura mwaka 2000. Hiki ni kipindi kizuri kwa wachunguzi wa masuala ya kisiasa kwa sababu mambo mengi yanatokea au kufanywa ambayo huweza kutumika kama kigezo cha kupima demokrasia nchini. Katika makala hii tutajitahidi kutathmini hali ya siasa za Tanzania kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2005. Tutachambua ahadi zilizotolewa wakati wa uchaguzi wa mwaka 2000 na kuona ni jinsi gani zilitekelezwa au hazikutekelezwa na athari zake kwa demokrasia, kwa kulinganisha na hali halisi ya sasa. Pamoja na kuwa matukio muhimu ya kila siku yatachukuliwa katika kuelezea baadhi ya mada tutakazojadili, si nia ya makala hii kujikita katika matukio ya kila siku.  Wakati tukielekea kipindi cha uchaguzi mkuu wa 2005 ni muhimu tukafanya tafakuri za kina za nini kimefanyika na maeneo ambayo bado kuna mapungufu.  Ni muhimu tukaeleza tokea awali kwamba tathmini itazingatia zaidi hali ya siasa ilivyobadilika kuanzia mwaka 2000.  Lengo la tathmini ni kutoa mwanga wa mwelekeo wa kisiasa baada ya mwaka 2005. 

 

 

 

Ili kutuwezesha kuweka bayana tafakuri hii makala hii imegawanywa katika vipengele vikuu vitatu:

 

          (a) HALI YA SIASA BAADA YA UCHAGUZI WA MWAKA 2000:  MATARAJIO, MAZURI NA MAPUNGUFU

 

·        Hali iliyojitokeza Zanzibar

·        Hatua za Kukabiliana na Rushwa ndani ya CCM na ndani ya Serikali

·        Magomvi/Migogoro ndani ya vyama vya siasa na athari zake katika ukuzaji wa demokrasia

·        Tathmini ya Imani ya Wananchi kwa Serikali

 

          (b) NAFASI YA VYOMBO VYA HABARI NA VYAMA VYA WANANCHI KATIKA KUKUZA DEMOKRASIA

 

·        Kushamiri kwa vyombo vya habari

·        Nafasi ya vyama vya wananchi kwenye ujenzi wa demokrasia

 

 (c) KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2005 NA MUSTAKABALI WA TAIFA

  Umoja wa Kitaifa

  Mwelekeo wa wananchi Kisiasa 

 

2.       HALI YA SIASA BAADA YA 2000

Uchaguzi Mkuu wa Novemba 2000 ulijenga taswira mbili zinazokinzana Tanzania.  Upande wa Tanzania Bara kwa ujumla uchaguzi uliendeshwa kwa amani na utulivu na uvumilivu.  Hadithi, hata hivyo, ilikuwa tofauti kabisa upande wa Tanzania visiwani.  Uchaguzi ulileta utata mkubwa na hata wasiwasi wa kutokea mgogoro wa kisiasa.  Isingalikuwa ukomavu wa kisiasa uliokuja kuonyeshwa na wote waliohusika, Tanzania ingaliwezaweza kuingia kwenye janga kama tunavyoshuhudia nchi nyingine za Afrika.  Kwa hakika hali ya siasa ya Zanzibar na hofu ya siasa za vurugu ilikwishaainishwa na Tume ya Nyalali[1] ambayo iliona uwezekano wa chama kitakachoshindwa katika uchaguzi kuyakataa matokeo.

 

Inatosha kusema hapa kwamba haja ya muafaka ilionekana kuanzia awali kama ambavyo makala zilizoandikwa na Prof. H. Othman, Bw. P. Mangula na Bw. S. S. Hamad[2] zinaonyesha kwa namna tofauti umuhimu wa kukaa pamoja na kuzungumza. Muafaka II wa mwaka 2001 ni kitu cha kujivunia na rekodi nzuri ya utatuzi wa migogoro katika nchi za kiafrika.  Matokeo ya muafaka ni kama ifuatavyo:

 

(1)     Kufanyika kwa uchaguzi mdogo katika majimbo 16 ambayo awali Civic United Front (CUF) ilisusia matokeo yake hivyo kuwawezesha kurejea tena kwenye siasa za ushindani bila kupigana.

 

(2)     Kuimarika kwa amani na utulivu ambavyo vimeiwezesha nchi kupiga hatua za kimaendeleo. Kwa mara ya kwanza CUF walishiriki kwenye sherehe za mapinduzi za mwaka 2003 kuonyesha kuwa wanaitambua serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

 

(3)     Kuridhishwa kwa wahisani na hali ilivyo Zanzibar na kuanza kutoa misaada kwa serikali iliyokuwa imesitishwa. Hii imesaidia kuboresha hali ya uchumi na maisha ya wananchi kwa ujumla.

 

(4)     Kuundwa upya kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ambayo itahusisha vyama vya siasa katika uundaji wake.

 

2.1            Magomvi/migogoro ndani ya vyama vya siasa

Kwa bahati nzuri, Tanzania ina vyama 16 vya siasa vyenye usajili wa kudumu.  Mojawapo ya mihimili ya siasa za kiliberali ni kushindanisha sera za vyama vingi ili wananchi wapate fursa ya kuchagua chama wanachoona kinafaa.  Kwa vyovyote vile mfumo wa siasa wa vyama vingi unahuishwa na uimara na uthabiti wa vyama ambavyo vinakuwa tayari kuchukua fursa za kuongoza nchi kama chama tawala kikidorora.  Hali hii hukinyima usingizi chama kinachotawala na hivyo kukifanya siku zote kitafute njia za kuboresha utendaji wake – matokeo yake wananchi wanafaidika zaidi.  Hali ni tofauti Tanzania, hasa Tanzania bara kwa sababu bado haijafikia hatua chama tawala kikakosa usingizi kwa kuhofia kupoteza madaraka kwa upinzani. Kama ripoti ya Profesa Mukandala[3] ilivyoonyesha vyama vingi bado vinalegalega kwenye uchaguzi, havijajikita mizizi vijijini, na bado havijajulikana sana ukiachilia mbali sifa za waanzilishi. Kuna migogoro baina ya vyama na ndani ya vyama vyenyewe. Nitaelezea kidogo.

 

Migogoro imeshamiri ndani na baina ya vyama vya siasa hali inayowaacha wananchi njia panda.  Hapa tutazungumzia migogoro katika baadhi ya vyama vikubwa vyenye wabunge na madiwani.  Tumeshuhudia mgogoro mkubwa wa kugombea madaraka ndani ya UDP.  Ilianza kwa kamati kuu ya chama hicho kumtimua Mwenyekiti Bwana John Cheyo.  Baadaye msajili akabatilisha maamuzi ya kamati kuu na kumrudisha Mwenyekiti Cheyo.  Kilichofuata ni timua-timua.  Baadhi ya wabunge waliotuhumiwa kushirikiana na Bwana Amani Jidulamabambasi kumpindua Mwenyekiti wakawa wa kwanza kutimuliwa.  Matokeo: 

Aliyekuwa Mbunge wa UDP na Madiwani 9 walihamia CCM na wanachama 1,147 wa wilaya ya Bariadi walihamia CCM pia.

 

TLP sasa hivi kunafuka moshi na kuna kila dalili ya mlipuko hali ikiachwa iendelee ilivyo.  Madiwani matano wa wilaya ya Moshi Vijijini  walihamia CCM na hivi sasa kuna kampeni za uchaguzi mdogo zinaendelea.  Tarehe 24/4/2004 Mwenyekiti wa TLP Mkoa wa Dar es Salaam ambaye alikwua pia mfadhili wa chama Bw.  Saab Ally na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa chama hicho  wamehamia CCM.

 

Athari za migogoro katika vyama vya siasa ni nyingi, na kwa ujumla wake zinachangia kudorora kwa demokrasia.  Panapokosekana chama chenye upinzani wa kweli na nguvu ya siasa, hutokea chama kilichoshika dola kikalala usingizi na kujisahau kabisa.  Wananchi ndio waathirika wakubwa wa hali hii.

 

Ni jukumu la kila mmoja wetu na kila mdau kikiwemo chama tawala kuhakikisha  kuwa vyama vya upinzani vinaimarika Tanzania.  Hali ya vyama vya siasa Tanzania kama inavyoonyeshwa kwenye jedwali lifuatalo inaonyesha kupungua nguvu kwa vyama vya upinzani ukilinganisha na CCM.

 

Idadi ya kura ambazo vyama vilipata katika uchaguzi wa Bunge 2000

 

CHAMA

 

IDADI YA KURA

 

ASILIMIA

 

ONGEZEKO TOKA 1995

 

1.

2.

3.

4.

5.

6.

7.

8.

9.

10

11.

12.

13.

 

CCM

NCCR-MAGEUZI

CHADEMA

CUF

UDP

TADEA

NRA

UMD

TLP

NLP

UPDP

PONA

TPP

 

4,634,047

  258,591

   99,461

  792,378

  315,357

     9,647

        70

    7,550

 652,535

    2,507

  14,818

  11,789

10,206

 

65.3

3.6

4.2

11.2

4.4

0.1

0.001

0.1

9.2

0.04

0.2

0.2

0.1

 

+6

  -18

 - 2

 - 6

     +1.1

     + 1

             0.

0.

          + 9

               0

0

0

0

 

JUMLA

 

100

 

Chanzo: Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC): Uchaguzi Mkuu wa 2000

NB:  Taarifa hii haihusu uchaguzi katika majimbo 25 ambamo CCM ilipita bila kupingwa.

 

Tunaona katika jedwali hapo juu kuporomoka kwa vyama vikubwa kama NCCR-Mageuzi ambacho kilitawaliwa na migogoro iliyoishia kukigawa chama.   Hapa nigusie tu kwamba CCM  kutokana na ukomavu wake kisiasa kimeweza kudhibiti migogoro kila ilipojitokeza.  Kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu kitatawaliwa na migogoro ndani ya vyama na ni vyema vyama viweke mikakati ya kukabiliana nayo.

 

2.2            Tathmini ya kukubalika kwa serikali na chama

Uchaguzi mkuu kwa kawaida ni tathmini ya kukubalika kwa chama kwa wananchi wapiga kura (na hivyo serikali kitakayoiunda).  Hutokea umaarufu wa chama ukaporomoka ghafla mara baada ya uchaguzi mkuu kwa sababu kadha wa kadha.  Katika utafiti uliofanyika hivi karibuni[4] asilimia 63 ya wasailiwa wanakataa mfumo wa siasa wa chama kimoja.  Asilimia 73 wanakataa utawala wa mtu mmoja (personalized rule) hasa machifu au wazee (wa makabila).   Asilimia 87 wanakataa kabisa utawala wa kijeshi.  Asilimia 86 wanapinga mawazo ya kufuta bunge na kumpa rais madaraka yote.  Tafsiri mojawapo ya matokeo haya ni kwamba watanzania wanahitaji sana mfumo wa demokrasia wa vyama vingi (yaani uliopo).

 

  Kukataa udikteta (Asilimia)

 

Nakubali Kabisa/Sana

Nakubali

Yote sawa

Sikubali

Sikubali Kabisa

Sijui

Chama kimoja tu kiruhusiwe kusimama kwenye uchaguzi

 

12.0

 

17.0

 

7.0

 

25.0

 

38.0

 

1.0

Maamuzi yote yafanywe na Mchifu au Baraza la Wazee

 

4.0

 

9.0

 

10.0

 

33.0

 

40.0

 

4

 

Jeshi litawale nchi

 

2.0

 

4.0

 

5.0

 

28.0

 

59.0

 

2.0

Chaguzi zisiwepo ili Rais aamue kila kitu

 

 

2.0

 

4.0

 

6.0

 

28.0

 

58.0

 

2.0

Chanzo:  “Results from Round II OF Afrobarometer Survey”

 

 

 

 

2.2.1 Ukuaji wa Demokrasia

 

Katika jamii nyingi demokrasia imehusishwa na maendeleo ya nchi kisiasa, kiuchumi na kijamii.  Kadri nchi inavyokuwa ya kidemokrasia zaidi ndivyo inavyoongeza uwezekano wa kupata maendeleo.  Hivyo kuna ulazima wa kuifanya demokrasia kuwa sera ya taifa.   Wananchi lazima waridhishwe na kiwango cha demokrasia ili waunge mkono.  Katika utafiti uliofanyika mwaka 2003 wahojiwa waliulizwa ni kwa kiasi gani Tanzania inafuata demokrasia. Kwa ujumla asilimia 81 walisema Tanzania ni nchi ya kidemokrasia.  Hata hivyo walisema demokrasia Tanzania bado ina matatizo madogo.  Asilimia 12 tu walisema Tanzania ina demokrasia kamili, ambapo asilimia 19 walisema demokrasia ya Tanzania ina matatizo makubwa.  Asilimia 8 walisema hakuna demokrasia kabisa Tanzania.

 

2.2.2 Ushiriki katika siasa

Demokrasia inaweza tu kushamiri pale ambapo watu wanashiriki katika siasa.  Watanzania wanapenda sana siasa na hii inajidhihirisha kwamba asilimia 67 ya wahojiwa walisema hujadili masuala mbali mbali ya kisiasa, asilimia 36 walisema hujadili sana siasa.  Asilimia 83 ya wahojiwa wanasema wanahudhuria mara nyingi mikutano ya kijamii.  Hata hivyo asilimia 34 ya wahojiwa wanaona mambo ya siasa na serikali kuwa ya utatanishi (complicated).  Hii inapunguza nguvu ya ushiriki katika siasa.  Lakini hata hivyo, inashangaza kidogo kwamba asilimia 76 wanasema wanaweza kuwafanya viongozi wao wawasikilize.  Tabia hii ni muhimu kwa demokrasia kwa sababu inaonyesha wananchi wanaweza kuwawajibisha viongozi wao.

 

Ushiriki mkubwa wa kisiasa huwasaidia Watanzania kujiunga katika kupigania haki zao.  Hivyo kiasi kikubwa cha wahojiwa (karibu asilimia 69) walionyesha kwamba hujiunga na wenzao kudai haki zao.  Hata hivyo asilimia kubwa hawajishirikishi na siasa za kupinga (protest politics) na hawashiriki kwenye maandamano. Hata hivyo wanaunga mkono demokrasia.  Asilimia 81 wanasema hawawezi kamwe kutumia nguvu kwa madai yoyote ya kisiasa.  Hii inaonyesha kuwa watanzania walio wengi ni wapenda amani na hawawezi kutumia nguvu kwa ajili ya madai ya kisiasa.

 

Njia nyingine ya ushiriki katika siasa ni kuonana na viongozi wao.  Ni muhimu wananchi kuwaona na kushauriana na viongozi wao wa serikali kama watataka kuwa karibu na serikali yao na kuunga mkono maamuzi yake.  Hivyo utafiti ulitaka kujua ni kiasi gani wananchi wanashauriana na viongozi wao.  Waliulizwa; “Katika mwaka uliopita, ni mara ngapi uliwaona hawa wafuatao ili wakusaidie kutatua matatizo yako?  Jedwali hapa chini linaonyesha watanzania wengi wanawaona viongozi wa ngazi za chini kuliko wa ngazi za juu (asilimia 33).  Hii ni ongezeko la asilimia 4 ukilinganisha na mwaka 2001.  Hata hivyo watanzania wengi (asilimia 56) wako radhi kuwaona viongozi wa dini kuliko kuwaona viongozi wa kisiasa (Asilimia 34 tu ndiyo waliowaona viongozi wa vyama vya siasa).

 

Ni Kiasi gani unawaona wafuatao kwenye matatizo?

 

2001

2003

Viongozi wa serikali za mitaa/madiwani

29

42

Watu wengine mashuhuri

26

32

Viongozi wa dini

49

56

Mbunge

12

19

Kiongozi wa jadi

12

27

Kiongozi wa chama

13

34

Kiongozi wa serikali kuu

 9

34

 

Chanzo:  “Results from Round II of Afrobarometer Survey”


2.2.3 Uhuru wa Kisiasa

 

Uhuru wa kisiasa ni kipimo cha kiwango cha ukomavu wa demokrasia katika jamii.  Uhuru finyu unamaanisha demokrasia finyu pia.  Hapa ni tathmini ya uhuru wa kisiasa kwa kuangalia uhuru wa kujieleza, uhuru wa kujiunga kwenye vikundi na kutokushtakiwa ovyo, na usawa mbele ya sheria.

 

Uhuru wa Kisiasa (Asilimia)

 

Mzuri

Mzuri sana

Sawa tu

Mbaya

Mbaya sana

Sijui

Uhuru wa kuongea unachofikiri

53

23

11

8

3

4

Uhuru wa kujiunga na chama chochote

52

29

11

3

1

4

Hofu ya kufungwa kwa kuonewa

42

16

19

13

3

7

Uhuru wa kupiga kura

46

31

13

6

2

2

Uwezo wa kuishawishi serikali

35

13

19

19

8

6