HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, MWENYEKITI WA CCM NA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE SHEREHE ZA MIAKA 31 YA KUZALIWA KWA CCM

03 FEBRUARI, 2008

 

 

Mheshimiwa Amani Abeid Karume, Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;

 

Mheshimiwa Ali Mohammed Shein, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

 

Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha, Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;

 

Waheshimiwa Wajumbe wa Sekretariat, Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa;

 

Waheshimiwa Waasisi wa TANU, ASP na CCM;

 

Wanachama wenzangu wa CCM;

 

Waheshimiwa Mabalozi;

 

Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;

 

            Nianze kwa kuwashukuru na kuwapongeza viongozi na wana-CCM walioandaa sherehe hii kwa kazi nzuri sana iliyofanywa.  Sherehe hizi zimefana sana. Inatia matumaini sana.  Nawashukuru kwa nyimbo za halaiki zimetukumbusha tarehe 05 Februari, 1977 pale Amani Stadium, CCM ilipozaliwa. Sisi tuliokuwepo nyakati hizo tunajikuta machozi yakitulenga lenga.

 

            Leo ninayo furaha kubwa kujumuika nanyi kuadhimisha miaka 31 ya kuzaliwa kwa chama chetu, Chama Cha Mapinduzi. Leo ni siku ya kuangalia tulikotoka, tulipo na tuendako katika uhai na ujenzi wa Chama chetu. Nawapongeza viongozi na wanachama wa CCM kwa mafanikio makubwa tuliyoyapata katika kukijenga, kukitunza na kukiimarisha Chama cha Mapinduzi katika uhai wake wa miaka 31. Kuweza tu kudumu kwa miaka 31, na nusu ya miaka hiyo ikiwa ni ndani ya ushindani wa vyama vingi, ni mafanikio makubwa ambayo wote hatuna budi kujivunia nayo. 

Lakini jambo linalitia faraja ni ule ukweli kwamba Chama chetu kimeiongoza nchi yetu vizuri na mafanikio yako wazi.  Mwenye macho haambiwi tazama.  Hata asiyetupenda hawezi kubisha kuwa tumefanya mengi mazuri na mazuri zaidi yanakuja. 

Ndugu zangu, viongozi wenzangu wana CCM wenzangu hatuna budi kujipongeza kwa yote tuliyoyafanya.  Na watani zetu nao wanapotupinga, nao wawe wakweli kwa kuyatambua mengi mazuri tuliyoyafanya.  Baniani mpigeni, upati wake mpeni”.  Nataka kuwahakikishia kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano wa Tanzania ni kitu kimoja. Tunashirikiana kwa karibu. Litakaloishinda Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Serikali ya Muungano ipo.  Likitushinda sote marafiki zetu tunao wengi duniani.            

Ndugu Wanachama wenzangu wa CCM;

            Wakati tunajivunia uhai na uimara wa Chama chetu kwa miaka 31 na mafanikio yaliyopatikana nchini chini ya uongozi wake hatuna budi kukumbuka kuwa kazi ya kukiimarisha Chama cha Mapinduzi ni inayoendelea, yaani ni kazi ya kudumu.

            Kila uongozi wa CCM uliopita, umechukua hatua muafaka, kulingana na mazingira ya kisiasa na kiuchumi ya wakati huo, kukiimarisha Chama chetu. Na sisi tuliopo sasa kwenye uongozi wa CCM, tunaendelea na pale uongozi uliopita uliishia. Tunachukua hatua thabiti za kuendelea kukiimarisha Chama cha Mapinduzi.

 

Kazi iliyo Mbele Yetu (2008)

 

Ndugu Viongozi, Wanachama, Wapenzi na Washabiki wa CCM;

            Katika mwaka huu mpya wa 2008, Chama chetu ni muhimu kijielekeze katika kufanikisha majukumu saba yafuatayo:

 

Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM

            Jukumu la kwanza, na kubwa zaidi, ni kuendelea kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Kazi hii tumekuwa tukiifanya tangu Serikali hii iingie madarakani, lakini ningependa sasa, katika mwaka huu wa 2008, Chama chetu kiongeze nguvu na umakini zaidi katika kuhakikisha kwamba Ilani na ahadi zake kwa Watanzania zinatekelezwa kwa ukamilifu na kwa kasi inayoridhisha. Sasa tumefikia katikati ya safari yetu ya miaka mitano ya uongozi wa Taifa letu. Wakati wa kurudi tena kwa wananchi hauko mbali.

Viongozi wa CCM ni lazima wajue Chama chao kiliahidi mambo gani katika maeneo yao na Serikali inafanya nini kutekeleza ahadi hizo. Hili ni jambo la msingi sana kwani mwaka 2010, watakaorudi kwa wananchi kuomba ridhaa mpya ya kuliongoza Taifa letu ni viongozi wa CCM. Kwahiyo, viongozi wa Chama katika ngazi zote ni lazima watoe uongozi makini na mahiri kwenye kufuatilia utekelezaji wa Ilani na ahadi za CCM. Viongozi wa Serikali hawana budi kutoa ushirikiano kwa viongozi wa Chama wanapofanya kazi hiyo.

            Katika Ilani ya CCM kuna yale mambo ya kawaida, tunayoyaongelea  siku, yanayohusu ustawi wa kiuchumi, kisiasa na kijamii wa Tanzania na Watanzania, ambayo lazima tuendelee kuyasimamia. Lakini vilevile, Sura ya Tisa ya Ilani ya CCM, inakihusu Chama chenyewe. Ilani inatoa maelekezo mahsusi kwa viongozi wa CCM kuhusu wajibu na majukumu yao kwa wananchi wote.

Na, hapa kuna wajibu wa kimsimamo na kimtazamo, lakini vilevile kuna wajibu wa vitendo, ambapo Ilani inawataka viongozi wa CCM waongoze kwa kuonyesha njia. Tunapopiga vita rushwa inapendeza zaidi sisi wenyewe tukiwa waadilifu. Tunapohimiza mapinduzi ya kilimo, na sisi viongozi, ambao tunalima, tuwe na mashamba ya mifano. Ilani inawahimiza viongozi na wanachama wa CCM kuwa mfano wa kuigwa kwa uchapakazi na kujitegemea katika maisha.

Ndugu zangu, tukizingatia haya, na maagizo mengine ya Ilani kwa viongozi na wanachama wa CCM, Chama chetu, sio tu kitakuwa kinaongoza mapambano dhidi ya umaskini, bali kitakuwa kinatoa uongozi madhubuti katika maisha na ustawi wa watu wa nchi yetu.

 

Maandalizi ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa

Ndugu Wanachama wenzangu;

            Jukumu la pili la Chama chetu kwa mwaka huu mpya wa 2008, ni maandalizi ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika mwaka ujao, wa 2009. Pia kuanza matayarisho ya Uchaguzi Mkuu wa 2010.

            Kama mnavyojua, mwaka ujao wa 2009, kutakuwa na uchaguzi wa Serikali za vijiji na vitongoji nchi nzima. Ni lazima mwaka huu tuutumie vizuri na kujiandaa vya kutosha kuhakikisha tunapata ushindi wa kishindo na kushika dola katika ngazi ya chini kabisa, lakini iliyo muhimu sana, ya uongozi wa Serikali. Ushindi huu wa ngazi hii ni nguvu kubwa ya kukihakikishia Chama chetu ushindi mnono katika Uchaguzi Mkuu wa 2010. Ni mtaji na msingi muhimu kisiasa.

            Na, katika kutafuta ushindi wa Serikali za Vijiji na Vitongoji, matumaini yetu yapo kwa viongozi na watendaji wa CCM katika ngazi za mashina, matawi na kata. Bahati nzuri mwaka wa jana Chama chetu kilikamilisha kuunda safu ya uongozi katika ngazi hizo. CCM imejitengenezea mtandao mkubwa katika ngazi zote za utawala nchini mwetu, ambao wahimili wake ni wanachama wake na wapenzi wake. Tuhakikishe kwamba tunautumia mtandao huu kushinda katika chaguzi zilizo mbele yetu. Nawaomba viongozi wa CCM ngazi za Wilaya, Mikoa na Taifa, tuhakikishe kwamba tunazo orodha za vijiji na vitongoji vyote katika maeneo yetu. Aidha, tuhakikishe kuwa safu za uongozi katika ngazi za vijiji na vitongoji zimekamilika na tunawapatia viongozi hawa mafunzo yapasayo. Chama cha Mapinduzi lazima kishiriki uchaguzi katika kila kijiji na kitongoji nchini. Hivyo tuanze pia kuwatambua na kuwashawishi wanachama na makada kujiandaa kwa uchaguzi.

 

Ushiriki katika Zoezi la Kuboresha Daftari la Wapiga Kura

Ndugu Wananchi,

            Chama cha Mapinduzi, katika mwaka huu, ni lazima kijielekeze katika kuwahamasisha wananchi washiriki kwenye zoezi la Kuboresha Daftari la Wapiga Kura. Hili ni jukumu la tatu kwa mwaka wa 2008.

            Katika chaguzi zote, siri mojawapo kubwa ya ushindi wa Chama chetu ni kuhakikisha kwamba wanachama, wapenzi na washabiki wa CCM wanajiandikisha kupiga kura na siku ya kupiga kura wanajitokeza vituoni na wanapigia kura wagombea wa CCM. Hii ni siri ya ushindi ambayo hatuna budi kuikumbuka na kuifanyia kazi.

            Sasa hivi kote nchini, Tume ya Uchaguzi inaendesha zoezi la Kuboresha Daftari la Wapiga Kura. Wale ambao hawakuwa wameandikishwa mara ya mwisho sasa wana nafasi hiyo. Na wale ambao walikuwa hawajafikia umri wa kupiga kura kwenye uchaguzi uliopita, na sasa wamefikisha umri stahiki, pia wana fursa ya kujiandikisha sasa na kushiriki kwenye chaguzi zijazo kuanzia sasa. Lakini pia wapo wenzetu wengine ambao wamepoteza kadi zao za kupigia kura, nao pia wajitokeze kujiandikisha wapewe kadi mpya.

            Ndugu zangu, suala la kuhimiza wananchi kujitokeza kujiandikisha ni jambo lenye maslahi makubwa kwa Chama chetu. Nasisitiza kuwa tuhakikishe wanachama wetu, wapenzi na washabiki wa CCM wanajiandikisha. Pamoja na hayo, hili ni jambo lenye maslahi mapana kwa kwa nchi yetu pia. Demokrasia inasimama kwenye msingi wa wananchi kuchagua viongozi wao. Na, kwa mujibu wa sheria ya nchi yetu, mtu huwezi kuchagua kiongozi ambaye kama huna sifa ya kupiga kura. Sifa kubwa ni kwamba ni lazima uwe umeandikishwa kwenye Daftari la Wapiga Kura.

            Chama cha Mapinduzi ni lazima kitoe uongozi kwenye zoezi hili muhimu kwa maendeleo ya demokrasia nchini mwetu.

Kuimarisha Uhusiano Baina ya CCM na Vyama vya Upinzani

Ndugu Wanachama wenzangu;

            Mwaka huu pia ni mwaka wa kuimarisha mahusiano baina ya Chama chetu na vyama vya upinzani nchini. Kwenye kuendesha mfumo wa siasa za vyama vingi, kuna sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni ushindani. Na sehemu ya pili ni ushirikiano. Ushindani ni wakati wa uchaguzi, na uchaguzi unapokwisha, kwa kuwa wote tunajenga nchi moja, hatua inayofuata ni ushirikiano.

Kuimarisha ushirikiano na mahusiano baina ya CCM au Serikali na vyama vya upinzani imekuwa ni dhamira yangu tangu mnipe heshima ya kuliongoza taifa letu mwaka 2005.

Na, ndio maana niliunda Wizara mahsusi katika Ofisi yangu, Wizara inayoongozwa na Mzee Kingunge Ngombale Mwiru kwa ajili hiyo, pamoja na mambo mengine.

Niliwaahidi Watanzania kwenye salamu zangu za mwaka mpya wa 2008 kwamba mwaka huu tutaongeza juhudi katika kutimiza azma hii. Ningependa CCM ionyeshe uongozi kwenye suala hili na pia kuonyesha njia kwamba siasa za upinzani hazina maana ya uadui, chuki na kutokushirikiana.

Kwa sasa, nchi yetu ina taasisi mbili ambapo vyama vya siasa vinaweza kuzitumia kushirikiana vizuri. Kwanza, lipo Bunge, ambapo Wabunge wa vyama vyote vya siasa wanaweza kuongeza ushirikiano katika shughuli za Bunge, zikiwemo kutunga sheria na kupitisha maamuzi mbalimbali yenye maslahi kwa Taifa.

Lakini pia ipo taasisi ya Kituo cha Demokrasia Tanzania (Tanzania Centre for Democracy), ambapo vyama vyote vyenye Wabunge ni wanachama, lakini pia vyama visivyo na Wabunge vimealikwa kuwa Wanachama Shirikishi (Associate Members). Kwa mwaka huu, CCM imeazimia kuendelea  kushiriki kikamilifu katika shughuli za taasisi hii. Serikali tumeitikia wito wa Mwenyekiti wa taasisi hii Mhe. John Cheyo wa kutaka tuchangie taasisi hiyo. Tumefanya hivyo mwaka huu na tutaendelea kufanya hivyo kwa miaka ijayo kwa kutenga fedha katika bajeti ya Serikali.

 

Ndugu zangu;

Kwa hapa Visiwani, ambapo kwa muda mrefu sasa, mahusiano ya kisiasa baina ya CCM na CUF yamekuwa sio mazuri, naomba niseme mambo yafuatayo;

 

Kwanza, kuwahakikishia wananchi kuwa, katika mahusiano hayo yasiyoridhisha, CCM siyo chanzo.  Haina chuki na CUF. Ni kwa msingi huo, CCM iliamua kuzungumza na wenzetu wa CUF. Dhamira kuu ya mazungumzo yanayoendelea sasa baina ya CCM na CUF ni kubadilisha aina ya mahusiano kati ya vyama hivi viwili, yatoke kuwa ya mahusiano ya chuki, uhasama na uadui, yawe mahusiano ya kupingana kwa hoja na kushirikiana katika kuijenga Zanzibar na Tanzania kwa ujumla, pale uchaguzi unapokwisha. Dalili zote zinaonyesha kwamba mazungumzo haya yatafanikiwa katika azma hii adhimu. Tumefikia pazuri. Inshallah tutafanikiwa. Ninachowasihi wapenzi na washabiki vya vyama vya CCM na CUF ni kuendelea kuvuta subira kidogo kwani nia ya makubaliano ipo na imedhihirika kwa pande zote.

 

Kuendelea Kusimamia Maadili ya Viongozi na Uongozi

Ndugu Wanachama wa CCM;

            Jukumu jingine kubwa lililo mbele yetu kama Chama ni kuendelea kusimamia maadili ya uongozi, hasa kupambana na tatizo la rushwa na ubadhirifu ndani ya Chama na katika taifa tunaloliongoza. Ni muhimu sana tulisisitize suala la maadili kwa viongozi. Suala la viongozi kutokuwa waadilifu linasumbua na kuudhi sana jamii. Mambo yanapokithiri watu wanapoteza imani kwa viongozi na uongozi wa Chama.

            Kimsingi, suala la maadili limesisitizwa na Chama chetu ndani ya Ilani yake ya Uchaguzi wa 2005. Ibara ya 110 ya Ilani hiyo, pamoja na mambo mengine, inazitaka Serikali na CCM “kuongeza juhudi za kuendelea kuchukua hatua za kisheria, kiutawala na kinidhamu kwa wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa”.

            Kwa maana hiyo, hatua ambazo Serikali na CCM imekuwa inazichukua kupambana na rushwa, wizi na ubadhirifu wa nchi ni utekelezaji thabiti wa maagizo hayo ya Chama kupitia Katiba ya Chama na Ilani ya CCM.

            Ndugu zangu, kwahiyo basi, mwaka huu wa 2008, uwe ni mwaka wa kuimarisha juhudi za kusimamia maadili ya viongozi wa Chama na Serikali. Hivi majuzi, nimeelezea nia ya Serikali ya Muungano kuweka utaratibu utakaowawezesha Wabunge na Mawaziri kutenganisha shughuli za biashara na uongozi. Katika nchi kama yetu, baada ya kuondoa masharti ya uongozi ambayo yalikuwa na misingi ya kijamaa, palihitajika pawepo masharti muafaka yanayoendana na mfumo wa uchumi wa soko tunaoufuata sasa. Wenzetu kama sisi wanao utaratibu unaoitwa kwa Kiingereza “Blind Trust”. Yaani wakati ukiwa kwenye nafasi ya uongozi wa umma, hujihusishi moja kwa moja na shughuli  zako za biashara. Unakabidhi shughuli hizo kwa wadhamani  wanaoziendesha kwa niaba yako. Haki zako zinahifadhiwa mpaka siku ukiacha uongozi wa umma unachukua na kuendelea. Ni utaratibu mzuri ambao unaosaidia kumuondolea kiongozi migongano ya kimaslahi na kutiliwa shaka na jamii kuhusu uadilifu wake.

Kutekeleza Mradi wa Kuimarisha Chama

Ndugu zangu;

            Mwaka 2006, Chama chetu kilizindua Awamu ya Tatu ya Mradi wa Kuimarisha Chama. Na, mwaka jana, tulizindua shughuli za utekelezaji wa mradi huo kwa hapa Pemba.

            Lakini mwaka jana, tulijielekeza zaidi kwenye kufanikisha zoezi la uchaguzi wa ndani ya Chama nchini, kwahiyo hatukutumia muda wa kutosha kutekeleza Miradi hii ya kuimarisha Chama.

            Ningependa kuona mwaka huu na kuendelea tunatoa msukumo  maalum wa kuhakikisha kuwa madhumuni ya Mradi yanafikiwa. Kubwa zaidi katika kutekeleza mradi huu ni kuhakikisha kwamba wanachama wa CCM na jumuiya zake wanaongezeka. Wanachama ambao ni imara kukitetea na kukilinda Chama chao. Wanaolipa ada zao kwa wakati na kuchangia maendeleo ya Chama chao. Nafurahi leo kupokea wanachama wapya wengi. Kume inawezekana. Mtaji wetu unazidi kukua. Pili, kuhakikisha kuwa Chama chetu kinao viongozi walio madhubuti: yaani waaminifu kwa Chama, waadilifu, wachapakazi hodari na jasiri katika kukipigania Chama chao; viongozi waliopatikana kidemokrasia. Na kwa hapa, kuwa na viongozi wenye sifa hizo ni muhimu sana.  Tatu, vikao vya ngazi zote vinafanyika, wanachama wanalipa ada na kushiriki kwenye shughuli za Chama. Kadhalika, tuhakikishe Jumuiya za Chama ziko imara, na ari na hamasa ya wapenzi, washabiki na wanachama wa CCM ipo juu wakati wote. 

Naomba tukubaliane kwa dhati sasa kwamba viongozi wa Chama wanapofanya ziara katika maeneo yao ya uongozi, moja ya kazi ambazo wanapaswa kufanya ni kukagua kazi za Chama na hasa maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Kuimarisha Chama.

Uchaguzi wa Jumuiya

Mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi wa Jumuiya.  Nawatakia kila la heri, mambo yaende kwa mafanikio.  Hata hivyo, niwaombe viongozi  wenzangu kutambua wajibu wao wa kuhakikisha kuwa chaguzi hizi zinafanikiwa.  Pia nawaomba wanajumuiya kuzingatia maadili ya uchaguzi.  Kasoro zilizokuwepo uchaguzi uliopita tuziepuke.  Ni jambo lisilokubalika.  Tuwe waadilifu. 

Ndugu zangu, kama nilivyosema mwanzoni, Chama chetu ni imara. Lakini kazi ya kuendelea kukiimarisha ni kazi ya kila siku na ni kazi ya kudumu. Shime wote tushirikiane kuhakikisha kwamba Chama chetu kinaendelea kutamba kama Chama bora na imara nchini.

Mwisho

Ndugu viongozi na wanachama wa CCM;

            Mimi naamini tukiyatekeleza kwa ukamilifu majukumu haya saba katika mwaka huu wa 2008, tutakuwa tumepiga hatua kubwa katika kukiimarisha Chama chetu na kuzidisha imani ya wananchi kwa CCM.

            Mwisho, ndugu viongozi, naomba niongelee kwa kifupi jambo moja muhimu na la kihistoria ambalo tumeamua ndani ya Chama tuliadhimishe kwa pamoja na sherehe za miaka ya 31 ya kuzaliwa kwa CCM.  Mwaka huu ni Jubilei (Miaka 50) ya Uamuzi wa Busara wa Tabora, ambapo TANU iliamua kushiriki uchaguzi wa kura tatu. Uamuzi ule, ambao ulipingwa sana na baadhi ya wana-TANU na kufikiwa kwa ugumu, ndiyo uliobadilisha muelekeo wa historia ya nchi yetu.

            Lakini uamuzi ule una mafundisho makubwa sana kwetu sote leo.  Labda tuikumbuke historia kidogo. Kwa kifupi, wakati wote wa kupigania uhuru, TANU ilikuwa na msimamo thabiti kwamba Baraza la Kutunga Sheria ni lazima litokane na wajumbe waliopigiwa kura na watu wote wazima nchini (universal suffrage) kwa misingi ya haki na usawa.

Hata hivyo, Serikali ya Kikoloni ya Uingereza ilipanga uchaguzi wa Baraza la Kutunga Sheria ufanyike kwa namna na misingi ambayo ni kinyume na imani hii ya msingi ya TANU.  Wakaloni waliamua watu wa Tanganyika wapige kura tatu: kwa Mzungu, Muasia, na Mwafrika

Kwahiyo, mjadala ukaletwa mbele ya Mkutano Mkuu wa TANU mjini Tabora, tarehe 21 Januari 1958. Je, TANU ishiriki kwenye uchaguzi ambao utaendeshwa kwa namna ambayo TANU yenyewe na vyama  vingine vya ukombozi Barani Afrika vimekuwa vinaupinga hadharani siku zote?   

Baada ya mjadala mrefu na mkali, TANU, pamoja na kukiri kwamba mfumo wa kura tatu ni mbaya, iliamua kushiriki uchaguzi ule. TANU ilishinda viti karibu vyote vilivyogombaniwa na hivyo kuweza kutawala na kudhibiti mwelekeo na shughuli za Baraza la Kutunga Sheria, hivyo kuwezesha kutungwa Sheria na kupitishwa kwa maamuzi yenye tija na maslahi kwa Watanganyika. Hata kupatikana kwa uhuru wa Tanganyika mapema kuliko ilivyotarajiwa, kulitokana na kuwepo kwa TANU kwenye Baraza la Kutunga Sheria. Kama TANU ingegoma kushiriki uchaguzi ule, na ikawa nje ya Baraza la Kutunga Sheria, Baraza hilo lisingesimamia shughuli ya kutunga sheria na historia ya nchi yetu ingekuwa tofauti na ilivyo sasa.

Fundisho kubwa tunalopata kutokana na uamuzi ule ni kwamba wakati mwingine viongozi wa siasa tunawajibika kufanya maamuzi magumu, ambayo wakati mwingine yanaendana kinyume na tunayoaamini na kuyahubiri. Cha msingi ni kwamba maamuzi yoyote ya kisiasa ni lazima yaangalie manufaa mapana zaidi ya Taifa.

Vilevile, kwetu sisi katika CCM tunajivunia urithi wa viongozi na uongozi wa busara ambao siku zote, yanapokuja maamuzi makubwa, maslahi ya Taifa yanawekwa mbele. Huu ni urithi ambao hatuna budi kuuenzi na kuutafsiri kwa vitendo na kuupitisha kwa vizazi vijavyo vya viongozi wa Chama chetu na Taifa letu.

 

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI!

MAPINDUZIII!

 

Asanteni sana kwa kunisikiliza!