HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, WAKATI WA MAZUNGUMZO NA WAZEE WA MKOA WA

DAR ES SALAAM, UKUMBI WA DIAMOND JUBILEE,

DAR ES SALAAM, TAREHE 14 FEBRUARI, 2008

 

 

 

 

Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa;

Waheshimiwa Wazee Wangu wote mliopo hapa;

Waheshimiwa Viongozi wenzangu;

Mabibi na Mabwana:

 

Wazee Wangu;

 

          Nawashukuru Wazee wa Chama na Serikali wa Mkoa wa Dar Es Salaam kwa mwaliko wenu.  Nimefurahi kwa uamuzi wenu wa mkutano huu wa Wazee na Halmashauri Kuu za CCM za Wilaya. Nawashukuru kwa maneno mliyosema kuhusu mimi, Serikali na Bunge letu.  Ni kweli kwamba kwa muda wa wiki nzima nchi yetu na hasa siasa na uongozi wa Taifa letu vimepata mtikisiko mkubwa. Ni hali ambayo hatukuitegemea.  Imetustukiza,  tumefanya maamuzi ambayo hatukuyapanga na kupata matokeo ambayo hatukuyategemea.  Tunamshukkuru Mwenyezi Mungu kwamba nchi yetu bado ni moja na watu wake ni wamoja.

 

          Nilikuwa na mawazo ya kufanya mabadiliko katika Baraza la Mawaziri, lakini siyo wakati huu.  Kwa fikra yangu tungefanya baada ya Bunge na baada ya mgeni wetu kuondoka. Yangekuwa mabadiliko ya kawaida.  Tumefikia miaka miwili, tulianza zoezi la kufanya tathmini ya hali ya utendaji ya kila mmoja wetu ili tujue turekebishe wapi na vipi!  Sikutarajia kufanya mabadiliko makubwa kiasi hiki. Lakini ya Mwenyezi Mungu huyajui.  Mwanadamu unakuwa na yako na Mwenyezi Mungu anakuwa na yake usiyoyajua wala kuyategemea.  Lakini kila linalotokea lina heri yake.

 

Wazee Wangu;

 

          Kama nilivyosema jana, nilikuwa nimepanga kikao changu cha Baraza la Mawaziri Jumanne tarehe 06 Februari, 2008 pale Dodoma.  Kwa kawaida tunafanya siku ya Alhamisi ya mwanzo wa mwezi na ya mwisho wa mwezi.  Lakini, siku ya Alhamisi ingekuwa tarehe 08 Februari, 2008 siku ambayo ndiyo tuliipanga kwa ufunguzi wa Kiwanda cha Vyandarua, Arusha.  Shughuli hiyo tuliipanga miezi kadhaa huko nyuma hivyo tukaona kikao chetu tukifanye tarehe 06 Februari, 2008 ili tarehe 07 mchana niende Arusha tayari kwa shughuli ya ufunguzi wa Kiwanda.

 

          Lakini, mtakumbuka kuwa katika kikao kilichopita cha Bunge, Wabunge waliamua kuunda Kamati Teule kuchunguza tuhuma zihusuzo utoaji wa zabuni kwa Kampuni ya Richmond ya Marekani ya kuleta mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura.  Hoja hiyo ilifikishwa Bungeni na Mhe. William Shelukindo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Biashara na Uwekezaji. Bunge liliafiki hoja hiyo na matokeo yake ni kuundwa kwa Kamati Teule ya Wabunge watano chini ya uongozi wa Mhe. Harrison Mwekyembe. Pengine ni muhimu kusisitiza kuwa kati ya Wabunge hao watano, wanne walikuwa wa CCM na mmoja alikuwa wa CUF.

 

          Nalitaja jambo hili kwa sababu nasikia watani zetu wanadai ati ya Richmond ni kazi yao.  Naambiwa juzi mkubwa mmoja alienda Kibaya, Kiteto na kusema ati wapinzani ndiyo walioangusha Serikali ya Kikwete.  Ni watu waajabu sana wanaotafuta sifa binafsi kwa jambo la wote.  Nilichokiona mimi na ambacho wote tumeshuhudia ni kuwa suala hili liliwahusu Wabunge wa pande zote.  Na pengine wa CCM walikuwa wakali zaidi hata kuliko wale wa upinzani. Hivi Mheshimiwa

Shelukindo ni wa CUF, hivi Mwakyembe ni wa CHADEMA?  Hivi Anne Kilango niwa TLP?  Au Seleli ni wa UMD.  Ukweli ni kwamba jambo  hili liliwahusisha Wabunge wa Pande zote.  Lilianzia kwa Mzee Shelukindo wa CCM kwa maana ya wazo  na uchunguzi ukafanywa na Dr. Mwakyembe wa CCM na wenzake wa CCM na mmoja wa CUF. Leo kugeuzwa la upinzani na siyo la CCM sielewi.

 

          Lakini, kabla ya kuletwa Bungeni na kuamuliwa Kamati Teule ya Bunge iundwe,  Kamati ya Uongozi ya CCM Bungeni ilikutana kulijadili suala hilo na kukubaliana Kamati Teule iundwe. Ndipo hoja hiyo ikakubalika Bungeni na ndipo Kamati ya Mwakyembe ikaundwa. Hivi kama hili jambo hlilikuwa ni la  Wabunge wa vyama vya upinzani na linapingwa na CCM lingefika popote.  Bunge letu hivi sasa lina jumla ya Wabunge 317 kati yao Wabunge wa CCM ni 272 na Wabunge wa upinzani kwa jumla yao ni 44. Hivi kwa tofauti hii kweli wangeweza kufanikiwa kama CCM ingelilipinga?  Nasema wasikilizeni lakini ukweli uwe vichwani na mioyoni mwenu.  Wapo watu wanatafuta umaarufu isivyo stahiki.  Lakini, tumewazoea.

 

Wazee Wangu; 

 

          Naomba mniruhusu nilizungumzie kidogo suala la Kamati ya Chama ya Bunge kwani kumekuwepo na upotoshaji kuhusu kuwepo kwake na kazi zake. Kwanza ipo kwenye Katiba ya CCM ibara 104(7) inasema  “Kutakuwa na Kamati ya Wabunge wote wa CCM” Ipo pia Kamati kama hiyo ya Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa Ibara  104(8)ya Katiba ya CCM. Lakini, pili ambalo ndilo jambo la msingi ni kuwa ndiyo utaratibu wa kuendesha siasa za vyama katika Mabunge yote duniani. Vyama vinakuwa nazo Kamati hizo kwa ajili ya kupanga mikakati ya kuendeleza sera na maslahi ya vyama vyao katika Taasisi hii muhimu ya kutunga sheria.

 

          Kuwa na Kamati ya Chama Bungeni ni jambo tulilorithi toka kwa waasisi wa Chama chetu na Taifa letu.  Tumekuwa nayo tangu wakati wa Chama kimoja mpaka sasa.  Ni jukwaa muhimu na mambo mengi makubwa yamefanywa kupitia kikao hiki.  Hatuna budi kuuenzi mfumo huo na kuuimarisha. Napenda kurudia tena pongezi zangu kwa Kamati ya CCM Bungeni kwa kazi nzuri inayoendelea kuifanya.  Inawezekana kuwepo mapungufu ya hapa na pale, ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wasisite, wazungumze kwa uwazi na kufanya marekebisho stahiki. Mimi naamini hakuna kasoro yoyote iwe ya muundo au ya watu binafsi ambayo haizungumziki na kurekebishika.  Wazungumzaji ni Wajumbe wenyewe wa kikao hicho ambao ni Wabunge wetu.  Ni watu makini na watu jasiri.  Katika kikao kilichopita cha Kamati Kuu, tulisisitiza umuhimu wa Kamati ya Chama kutumika ipasavyo.  Hakuna badala yake.  Vinginevyo itakuwa kuburuzana kwa maslahi binafsi ya watu Bungeni badala ya maslahi ya Chama na Taifa.

         

Wazee Wangu;

 

          Nilisema mwanzoni kuwa, nilipokwenda Dodoma tarehe 06 Februari, 2008 nilienda kwa ajili ya kikao cha Baraza la Mawaziri.  Lakini nilipofika nikapata taarifa kuwa baada ya Ripoti ya Tume ya Mwakyembe kuwasilishwa, Uongozi wa Wabunge wa CCM Bungeni umeamua kuitisha kikao cha Kamati ya Uongozi ya Chama mchana ule na usiku Kamati ya Wabunge wote wa CCM.  Mimi nilikuwa nimeamua kikao changu cha Baraza la Mawaziri nikifanye usiku lakini Mawaziri ni Wabunge wa Kamati ya Chama ya Bunge hivyo nikaamua niahirishe kikao changu.  Nilifanya hivyo kwa kuzingatia uzito wa suala lenyewe na unyeti wa hali pale Bungeni baada ya taarifa ile kutolewa.  Nilifurahi kuwa Kamati ya CCM ya Bunge itahusishwa kwa ukamilifu.

 

          Baadae usiku nilipokea taarifa ya vikao hivyo viwili vya Chama chetu.  Baada ya  kufuatilia mjadala Bungeni siku iliyofuata  na kusikiliza  hisia za watu nchini ndipo tukafikia kwenye maamuzi yale magumu na mazito tuliyofanya. Maamuzi ambayo yalipelekea kuvunjwa kwa Baraza la Mawaziri.  Ni maamuzi magumu, lakini yalikuwa hayana budi kufanyika kwa maslahi ya utangamano wa taifa letu.  Uamuzi mwingineo tofauti  ulikuwa unaliingiza taifa letu kwenye matatizo makubwa zaidi.  Ni uamuzi mgumu kwa sababu unawahusu watu ambao ni wenzangu wa karibu kimaisha na kikazi kwa miaka mingi. Na pia kwa sababu unaona wazi kuwa  kama mambo fulani fulani yangefanyika mambo yasingefikia kuwa yalivyo.  Lakini, ndiyo imeshafikia hapo.  Imeshakuwa na fursa ya kufanya vinginevyo kwa maslahi ya taifa haikuwepo. Kama ilikuwepo ni finyu sana na haingeleta hatima tofauti na ile tuliyoifikia.

 

Wazee Wangu;

Wananchi Wenzangu;

 

          Napenda kuitumia nafasi hii kumshukuru sana Mhe. Edward Lowassa kwa moyo wake wa uzalendo na kwa utumishi wake kwa taifa letu.  Ameitumikia nchi kwa jitihada kubwa katika nyadhifa mbalimbali mpaka kufikia kuwa Waziri Mkuu.  Katika miaka hii miwili amefanya kazi kubwa ya kusukuma mbele gurudumu la maendeleo la taifa letu.  Ameacha alama za kudumu za kipindi chake cha miaka miwili.  Yaliyotokea ni ajali katika maisha ya siasa,  lakini naamini historia itamhukumu kwa haki stahiki. 

 

          Nawashukuru sana Mawaziri na Naibu Mawaziri tuliokuwa nao kwenye Baraza la Mawaziri lililopita, ambao hawakuteuliwa tena, kwa mchango wao kwa taifa.  Nitoe shukrani kwa kaka zangu walioamua kupumzika.  Sina maneno ya kuelezea furaha yangu na shukrani zangu zaidi ya kusema wao ni mfano wa kuigwa.

 

Wazee wangu;

 

          Ni ukweli ulio wazi kuwa hiki kipindi cha wiki moja kilikuwa kigumu sana kwa nchi yetu.  Nchi yetu ilipata  mtikisiko mkubwa na wananchi wengi walikuwa katika hali ya mkanganyiko, wakati mwingine  walikuwa wakijiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu kuhusu hatma ya taifa letu. Kwangu mimi ilikuwa kipindi cha mtihani mkubwa sana.  Hivyo hivyo kwa Makamu wa Rais.  Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia rehema zake zilizotuvusha salama katika kipindi hiki kigumu. Tuzidi kumuomba Mwenyezi Mungu atujalie karama zake nchi yetu izidi kutulia na atuepushe na misukosuko ya namna hii tena.

 

          Nawashukuru sana wananchi wenzangu kwa utulivu wenu na uelewa wenu wakati wote nchi yetu ilipokuwa katika mazingira hayo magumu.   Halikuwa jambo dogo hata kidogo. Ulikuwa mtihani mkubwa kwetu sote. Utulivu wenu  na uelewa wenu wakati wote wa kipindi hicho kigumu ndiyo uliotuwezesha kuvuka salama.  Nawashukuruni nyie wazee wangu kwa sala na dua zenu.  Watanzania tumeonyesha ukomavu mkubwa wa kisiasa.  Mshikamano na umoja tuliouonyesha ni jambo la kujivunia sisi sote.

 

          Hali iliyojitokeza na jinsi tulivyoishughulikia pia ni kielelezo cha wazi cha kukomaa kwa demokrasia ya nchi yetu.  Licha ya hofu na  msukosuko mkubwa tulioupata tumeweza kuvuka salama.  Nchi yetu tayari imerudia hali yake ya kawaida na kila mmoja wetu anaendelea na shughuli zake.  Hili nalo ni jambo jema la kujivunia kama taifa.  Nawaombeni nalo tuliendeleze.

 

Ndugu zangu, Wazee Wangu;

 

          Kule  kwenye shaka tulikokuwa tayari tumeshapita.  Baraza jipya la Mawaziri limeshapatikana. Kazi iliyo mbele yetu kama Serikali ni nikuwatumikieni.  Nampongeza na kumshukuru tena Mhe. Mizengo Pinda kwa kukubali uteuzi wangu na kuthibitishwa kwa kishindo na Bunge.  Nimelielekeza Baraza la Mawaziri kuchapa kazi kwa kasi ili kuleta maendeleo ya haraka ya nchi yetu. Pia nimewasisitiza na kuwakumbusha Mawaziri wetu hao haja ya kufanya kazi zao kwa uadilifu ili yaliyotokea yasijirudie tena. Kwani mimi naamini kabisa kuwa hali iliyojitokeza imetokana na ulegevu wa baadhi yetu  katika utendaji na  suala zima la uadilifu.  Lazima tondokane na udhaifu huo.

 

          Ripoti ya Kamati ya Mhe. Mwakyembe ina mapendekezo mazuri.  Bunge letu linaendelea kuijadili taarifa hiyo.  Tunayasubiri kwa hamu mapendekezo ya Bunge mwishoni mwa mjadala.  Nia yangu kuwa yale yanayoihusu Serikali tuyafanyie kazi mapema iwezekanavyo.

 

Ndugu Wananchi, Wazee Wangu;

 

          Kabla ya kumaliza naomba kurudia niliyoyasema.  Nimesema nchi yetu imepita kipindi kigumu, kipindi kilichotuletea mtikisiko mkubwa.  Lakini kwa dua zenu na sala zenu tumevuka salama. Kazi iliyo mbele yetu sasa ni kuwatumikieni kwa uwezo wetu wote ili kutimiza ahadi zetu kwenu.

 

          Daima tujitahidi kuwa watumishi wenu makini.  Kila mara tutahakikisha kuwa tunafanya maamuzi yenye manufaa na tija kwa taifa na wananchi wetu.  Hatutasita kuchukua hatua kwa mambo yote yanayopingana na maslahi ya watu wetu.

 

          Nawashukuru tena kwa utulivu wenu, uelewa wenu na mshikamano wenu mliouonyesha. Nawaomba tuendeleze moyo huo wa uzalendo na mapenzi makubwa kwa nchi yetu. 

 

          Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitamshukuru Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein kwa ushirikiano mkubwa alionipa katika kipindi chote kigumu tulichopita.  Ni kutokana na msaada wake huo kwangu ndiyo maana tumeweza kufanikisha kazi ngumu ya kuliongoza taifa kwa salama na amani.  Tumeweza kumteua Waziri Mkuu mpya na kuunda Baraza jipya la Mawaziri.  Namshukuru sana.

 

Ndugu Wananchi;

 

          Aidha, namshukuru Waziri Mkuu wetu mpya, Mheshimiwa Pinda kwa kukubali kubeba jukumu hilo zito na kwa ushirikiano wake.  Ni mtu hodari na mchapa kazi.  Nawaombeni sote tumpe ushirikiano wetu wa karibu ili aifanye kazi yake kwa ufanisi na mafanikio makubwa.

 

          Naomba mniruhusu pia nitumie fursa hii kuwataarifu tena kuwa keshokutwa  tunao ugeni mkubwa na wa kihistoria wa kutembelewa na Rais wa Marekani, Mheshimiwa George W. Bush.  Rais Bush na Mkewe mama laura Bush na Ujumbe wake watawasili hapa nchini kesho kutwa siku ya Jumamosi Februari 16.  Ujio wake ni heshima kubwa kwa nchi yetu.  Hii ni mara ya pili kwa nchi yetu kutembelewa na Kiongozi wa taifa hilo kubwa duniani kwa ziara ya kitaifa.  Mwaka 2000 tulibahatika kutembelewa na Rais Bill Clinton kwa ziara ya kikazi. wakati wa usuluhishi wa mgogoro wa Burundi kule Arusha.

 

          Hivyo kupitia kwenu Wazee wangu naomba sote tujitokeze kumlaki mgeni wetu huyo kwa furaha na ukarimu wa Watanzania. Tumuonyeshe kuwa sisi Watanzania ni watu wema na wakarimu, tunaojali na kuthamini urafiki wetu na mataifa mengine.  Tuhakikishe kuwa mgeni wetu huyo awapo hapa nchini yupo salama na anarejea salama.

 

          Mwisho kabisa  nawashukuruni tena Wazee wangu kwa kuacha kazi zenu na kuja kuzungumza nami. Niliona ni busara tubadilishane mawazo   kuhusu hali iliyojitokeza na jinsi tulivyoikabili sote kama taifa.  Tumevuka salama na wote tuendelee na shughuli zetu kama kawaida.

 

Asanteni  kwa kunisikiliza.