HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, NA MWENYEKITI WA CCM, KWENYE UFUNGUZI WA MKUTANO WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA YA CCM, BUTIAMA – MARA, 28 MACHI, 2008

 

Mhe. Ali Mohammed Shein, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

 

Mhe. Amani Abeid Karume, Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;

 

Mhe. Mhe. Pius Msekwa, Makamu Mwenyekiti wa CCM

 

Makamu Mwenyekiti Mstaafu, Mzee Rashid Mfaume Kawawa;

 

Mwenyeji wetu hapa Butiama, Mama Maria Nyerere;

 

Wajumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa;

 

Wajumbe Wenzangu wa Halmashauri Kuu ya Taifa;

 

          Nianze kwa kuwashukuru wenyeji wetu, wanakijiji wa hapa Butiama, wakiongozwa na Mama yetu, Mama Maria Nyerere, kwanza, kwa kutukubalia tufanye mkutano wetu huu hapa kijijini kwao; na, pili, kwa kutupokea na kutukaribisha vizuri sana. Tunawashukuru sana wewe Mama Maria Nyerere na familia na ukoo mzima wa Nyerere na wanakijiji wa Butiama kwa ukarimu na upendo wenu.  Mimi si mgeni hapa Butiama.  Nilikuja hapa mara ya kwanza mwaka 1980 na mara kadhaa baada ya hapo.  Lakini safari hii mmetia fora.  Ahsanteni sana!

 

Nawashukuru na kuwapongeza wanachama na viongozi wa CCM wa Mkoa wa Mara kwa mapokezi mazuri na kwa maandalizi mazuri ya mkutano huu. Mmetupokea vizuri na mmetupangia ratiba nzuri.  Wajumbe wa NEC wamepita maeneo mengi, wameona mambo mengi ya maendeleo ya Chama na Mkoa yanayotia moyo.  Wameona juhudi kubwa wazifanyazo wanachama, wapenzi na washabiki wa CCM mkoani Mara za kujiletea maendeleo na kujenga Chama chao.  Tumeona raha zenu na karaha zenu.  Tunawapongeza kwa mafanikio na kuwahakikishia kuwa tumeona, tumesikia, tuko pamoja nanyi. 

Napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi mahsusi kwa Mhe. Nimrod Mkono, Mjumbe mwenzetu wa NEC na Mbunge wa Musoma Vijijjini, kwa kazi kubwa aliyoifanya na mchango wake muhimu uliowezesha kufanikisha mkutano huu kufanyika kwa kiwango hiki.  Amesimamia kwa ufanisi mkubwa ujenzi wa ukumbi huu.  Ahsante sana.  Pia, naipongeza Kamati nzima ya Maandalizi ya Mkutano wetu huu kwa jitihada kubwa waliyoifanya katika kufanikisha mkutano huu. Kuna kila dalili kwamba mkutano wetu huu utakuwa wa mafanikio makubwa.

 

Ndugu Wajumbe wenzangu wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Ndugu Wageni Waalikwa,

 

Tulipoamua kufanya mkutano wetu huu hapa Butiama, sikujua kwamba uamuzi huo ungezua mjadala na matumaini makubwa kuliko matarajio halisi ya sisi tulioamua. Kwangu mimi na wenzangu katika Halmashauri Kuu ya Taifa, tulitaka kurudia utaratibu mzuri wa zamani ambapo vikao vya NEC vilikuwa vinafanyika mikoani kwa mzunguko.  Yaani, Mkoa ambao ulikuwa tayari kuwa mwenyeji uliwaalika Wajumbe wa NEC kwenda kufanya mkutano wao kule.  Hapo katikati, kwa sababu mbalimbali, utaratibu huo ukaachwa na vikao vyote vikawa vinafanyika Dodoma, Makao Makuu ya CCM.

 

Tuliona ni busara sasa turudie kwenye ule utaratibu wetu wa zamani.  Tuliamua hivyo baada ya kupima manufaa makubwa tutakayoyapata ya kuhamasisha uhai wa Chama katika Mikoa mwenyeji.  Pia ni fursa ya kuwafanya viongozi wa ngazi ya juu wa Chama chetu wakijue vizuri zaidi Chama na waijue kwa undani zaidi nchi ambayo wana dhamana ya kuiongoza.  Ni kutokana na shabaha hiyo, karibu kwa muda wa siku tatu, Wajumbe wa NEC wametembelea Wilaya zote za Chama za Mkoa huu kukagua uhai wa Chama, kuzungumza na viongozi na wanachama wa CCM.  Aidha, wamekagua shughuli za maendeleo na kuzungumza na wananchi.  Ni ukweli ulio dhahiri kwamba ziara hizo za Wajumbe wa NEC zitakuwa zimepanda mbegu itakayochipua mmea mzuri wa kudumisha na kuendeleza uhai wa Chama chetu siku za usoni.

 

Baada ya NEC kuamua hivyo, Mkoa wa Mara ulikuwa ndiyo Mkoa wa kwanza kuwa tayari kuwa mwenyeji wa mkutano wa NEC katika utaratibu huu mpya.  Naambiwa Mkoa wa Dar es Salaam wameonyesha nia ya kufuatia, na wapo wengine wanataka kuelezea nia yao hiyo.  Naomba tuelewane juu ya utaratibu kwamba kila baada ya kufanya mkutano mmoja mikoani, mkutano unaofuatia tunaufanyia Makao Makuu.

 

Ndugu Wajumbe;

NEC ilipoamua kuwa Mkoa wa Mara uwe wenyeji wa kikao hiki, tuliona ni vyema mkutano huu tuje kuufanyia hapa Butiama, kwa sababu nzuri.  Hapa ndipo alipozaliwa na kuzikwa muasisi wa Chama hiki na Taifa letu.  Hii ni mara ya kwanza NEC nzima inakuwa Mkoani Mara kwa pamoja tangu alipotutoka mzee wetu huyu kipenzi.  Ni mahali muafaka kabisa kuja kufanyia mkutano.  Tuwape nafasi wasiopajua Butiama wapajue.  Watu wapate nafasi ya kuzuru kaburi lake.   Lakini pia tulitaka kuiweka hai kumbukumbu ya mahali muhimu kwa Chama chetu na Taifa letu.  Kwa kufanya hivyo, tunaiweka hai kumbukumbu ya Mzee wetu hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

 

Pamoja na hayo, tutumie nafasi hii kujikumbusha juu ya mema mengi ambayo Mwalimu amelifanyia taifa letu na Chama hiki alichokiasisi.  Tujikumbushe kuhusu moyo wa kujitolea kwa ajili ya wengi na moyo wa uzalendo kwa nchi.  Tujikumbushe wajibu wa viongozi kuzingatia misingi ya uadilifu na uaminifu.  Rais wa zamani wa Marekani, John F. Kennedy, alisema: “mifano ya watu mashuhuri huzaa watu wa kiwango hicho”.  Kuja hapa kutatupa ari ya kuishi na kutumikia taifa na watu wake kwa mfano wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

 

Ndugu Wajumbe, huu ni mwanzo tu wa hatua za kuiweka kumbukumbu ya Baba wa Taifa.  Tutafanya mambo mengine ambayo yatafanya watu wawe wanamkumbuka Baba wa Taifa na wanaikumbuka Butiama.  Kwa mfano, mwenge wa Uhuru utazimwa Butiama mwakani.  Pia, siku za usoni, hapo tutakapofikia uamuzi wa kuigawa wilaya ya Musoma kiserikali, nitapenda, kama itawezekana makao Makuu ya Wilaya itakayojumuisha eneo la Musoma vijijini yawe hapa Butiama.

 

Matumaini Makubwa

 

Ndugu Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa;

Kwetu sisi tulioamua mkutano huu ufanyike hapa, tuliona kuwa tumefanya uamuzi wa kawaida tu kwa ajili ya kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Taifa. Kumbe hatukujua kuwa kwa sababu ya uhusiano wa Baba wa Taifa imejengeka imani kuwa kikao hiki ni maalum kwa ajili ya kufanya maamuzi mazito.  Kwa namna fulani, wanaofikiria hivyo hawajakosea, kwani NEC ni kikao kikubwa sana cha Chama chetu na kila kinapokutana maamuzi mazito yahusuyo Chama chetu na Taifa hufanywa.

 

Na hata kwenye kikao hiki, yatakuwepo maamuzi muhimu yatakayofanyika.  Tutatoa taarifa mwisho wa kikao.  Lakini napenda kusema kuwa maamuzi hayo hayatahusu mageuzi ya kisera au kiitikadi.  Nalisema hili kwa sababu wapo watu wanaotumaini au wenye hofu kuwa hapa Butiama kutatokea tamko la kurudia tena kutaifisha mali na kuziweka njia kuu za uchumi mikononi mwa dola.  Wapo pia wanaodhani tutatoa tamko la kulirudisha nyuma gurudumu la mageuzi ya kisiasa yaliyoleta demokrasia ya vyama vingi na uhuru mkubwa wa watu kutoa maoni yao. 

 

Napenda kuwahakikishia kuwa hili halitatokea na wala siyo makusudi ya kikao cha Butiama kuja na maamuzi ya kugeuka nyuma kwenye mageuzi ya kisiasa na kiuchumi tuliyoyafanya.  Mageuzi ambayo pamoja na matatizo ya hapa na pale yameliweka taifa letu katika msingi mzuri wa maendeleo ya sasa na siku za usoni.

 

Ndugu Wajumbe,

Kama ilivyo kawaida yetu, tutatumia fursa ya kikao hiki kutafakari hali ya kisiasa, kiuchumi na kiusalama katika Chama na Taifa.  Katika vipengele mbalimbali vya kuzungumzia mambo hayo, yapo masuala makubwa yatakayojitokeza na kufanyiwa maamuzi.  Kama nilivyosema awali, na kama ilivyo kawaida yetu, tutatoa taarifa kwa ukamilifu mwishoni mwa kikao kuhusu nini kimezungumzwa na nini kimeamuliwa.   Hivyo basi, nawasihi wana-CCM wenzangu na wananchi wote kwa ujumla kuwa na moyo wa subira.  Subira yavuta heri.

 

Nawashukuru sana. Asanteni sana.  Nawatakia mkutano mwema.

 

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI