HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA BENJAMIN WILLIAM MKAPA, KWENYE UFUNGUZI WA SEMINA YA VIONGOZI WA KITAIFA WA VYAMA VYA SIASA KUHUSU KUENDELEZA DHAMIRA YA MUAFAKA, HOTELI YA BWAWANI, ZANZIBAR, 19 FEBRUARI, 2005

 

 

Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la

            Mapinduzi;

Mheshimiwa Waziri Kiongozi;

Mheshimiwa Spika wa Baraza la Wawakilishi;

Mheshimiwa Jaji Mkuu wa Zanzibar;

Waheshimiwa Mawaziri;

Waheshimiwa Viongozi wa Dini;

Waheshimiwa Wenyeviti Wenza, Tume ya Rais ya Usimamizi;

Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa;

Washiriki wa Semina;

Wageni Waalikwa;

Mabibi na Mabwana:

 

            Nilipolihutubia taifa na kuwapa wananchi salamu za mwaka mpya, tarehe 31 Desemba 2004, nilizungumzia nia yangu isiyo na shaka ya kuhakikisha mwaka huu tunafanya Uchaguzi Mkuu wenye heri, wa haki na uhuru kamili, katika mazingira ya amani na utulivu, Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.

            Semina hii ni maandalizi mazuri ya kufikia lengo hilo lenye maslahi makubwa kwa kila raia mwema. Hivyo ninawashukuru sana walioandaa semina hii, na ninawapongeza kwa wazo la kuwa na semina hii.  Na ninashukuru sana kwa mwaliko wao kwangu kuja kuifungua semina hii; na hivyo kunipa fursa ya kurudia na kufafanua kauli hiyo niliyoitoa tulipokuwa tunaukaribisha mwaka mpya wa 2005, mwaka wa Uchaguzi Mkuu katika taifa letu. 

            Ipo asasi moja isiyokuwa ya kiserikali ambayo mwaka 2000, tulipokuwa tunajiandaa kwa Uchaguzi Mkuu, ilifanya semina mbalimbali na kuendesha elimu ya uraia kuhusiana na uchaguzi.  Hatimaye, katika kujumuisha matokeo ya semina hizo, waliorodhesha kile walichokiita wao Maadili Kumi ya Uchaguzi Huru na wa Haki.  Hayo ni:

 

(1)               Kushiriki

(2)               Mwafaka

(3)               Uwazi

(4)               Utawala wa Sheria

(5)               Haki za Binadamu

(6)               Ukweli

(7)               Utamaduni wa Ushindani

(8)               Elimu ya Uraia na Mpiga Kura

(9)               Uadilifu, na

(10)           Nafasi Sawa.

 

Ndugu Wana-Semina:

            Najua hapa Tanzania tunapozungumzia MUAFAKA, kinachokuja kichwani haraka ni Muafaka baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Wananchi (CUF) hapa Zanzibar.  Nami nitazungumzia Muafaka huo, lakini napenda nianze kwa kujenga hoja kuwa Tanzania nzima inahitaji muafaka mpana zaidi, muafaka unaojumuisha jamii nzima ya Watanzania. 

            Mageuzi ya kisiasa na kiuchumi tuliyoyafanya katika miaka karibu 20 iliyopita yamelegeza baadhi ya kamba zilizokuwa zimetufunga pamoja kama taifa moja, watu wamoja, ndugu wa familia moja.  Ninahofu kuwa bila kukubaliana na kuwa na muafaka juu ya aina ya jamii tunayotaka kuijenga, tutapoteza hata zile sifa ambazo kwa miaka mingi zilitutofautisha sisi na nchi nyingine za Kiafrika, ikiwemo baadhi ya majirani zetu.  Mimi naomba sana kuwa uchumi wa soko, au kwa jina jingine uchumi huru, pamoja na uhuru wa kisiasa na vyombo vya habari, usiwe mwanzo wa kudhoofisha umoja wetu, kulegeza mshikamano wetu, au kupunguza utaifa wetu, muungano wetu na udugu wetu.

            Najua ninyi nyote ni Waheshimiwa, lakini muafaka wa kwanza ninaoutaka katika nchi yetu ni wa kukubaliana kuwa sisi sote ni ndugu. Uchumi wa soko utawafanya baadhi yetu watajirike kuliko wengine. Uhuru wa kisiasa umetuletea vyama vingi na Waheshimiwa viongozi wake wengi. Lakini hii isiwe sababu ya kujiona wengine ni bora kuliko  wenzao.  Lazima Watanzania tubakie ndugu. Udugu wetu ndio unatufanya tujione sisi sote ni binadamu sawa, wenye utu sawa, haki sawa na mahitaji ya msingi sawa.  Hivyo japo wengine wetu tunaitwa Waheshimiwa, naomba mkubali  na tuafikiane kuwa katika nchi yetu sisi sote bado ni ndugu, na wala “ndugu” hii si ya itikadi, ni ya utamaduni wetu wa Kiafrika. Kwa kusisitiza jambo hilo, mtaniwia radhi leo nitakuiteni nyote, “Ndugu-Wanasemina”.

 

Kushiriki na Nafasi Sawa

Ndugu Wana-Semina:

            Naomba mnikubalie tuwe na muafaka wa kitaifa kuwa kila raia anayo haki sawa kushiriki siasa, na kupata fursa sawa za kijamii, kiuchumi na kitamaduni katika nchi yetu.  Na leo napenda nizungumzie haki sawa ya kisiasa.  Si kila raia anatamani uongozi wa kisiasa.  Lakini ninaamini kuwa kila raia anapenda ashiriki kuchagua viongozi wake, pamoja na kuchagua chama cha siasa kitakachokabidhiwa uongozi wa taifa. Hivi sasa tunaendelea kuandikisha wananchi, wenye sifa zinazotakiwa, kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.  Kazi hiyo inakwenda vizuri, na ninawapongeza sana wanaoifanya kazi hiyo.  Lakini inaonekana kama vile bado hatuna muafaka wa kitaifa, miongoni mwa baadhi ya vyama vya siasa, kuhusu haki sawa ya raia wetu kujiandikisha, na hivyo kushiriki Uchaguzi ukifika.

            Naomba sana kwenye semina hii tukubaliane sote, na tutoke na kauli moja, kuwa kila raia, mwenye sifa zilizobainishwa wazi kisheria, anayo haki sawa ya kujiandikisha na hatimaye kupiga kura.  Nasema hivyo maana ninasikia kuwa wapo wanaofanya jitihada kubwa kuzua kila aina ya vikwazo kuwazuia wenzao wasijiandikishe, na kwa maana hiyo, kuwazuia wasishiriki. Jambo hilo si sahihi, na ni vema tulirekebishe kama sehemu ya muafaka mpana zaidi wa kitaifa.  Vipo vizuizi vya haki.  Hivyo tuendelee navyo.  Lakini visivyo vya haki tuachane navyo.

 

MUAFAKA

Ndugu Wana-Semina:

            Nimekwisha kuzungumzia dhana ya muafaka katika jamii.  Lakini kabla sijazungumzia Muafaka wa Zanzibar, napenda kusema kuwa muafaka wowote ni maridhiano baina ya watu au makundi ya watu katika jamii.  Mambo manne ni muhimu kabisa katika muafaka wa kweli. Kwanza ni dhamira.  Muafaka wa kweli hauwezi kupatikana na kuwa endelevu kama wahusika na wadau wote hawana dhamira ya kweli ya kufikia, kufanikisha na kuendeleza muafaka. Naomba semina hii ifafanue vizuri jambo hili. Muafaka usionekane kama vile ni jambo la kushurutishwa, ambapo kwa kisingizio chochote kile, mhusika anajivua wajibu ndani ya muafaka.  Muafaka hauwezi kufanikiwa ikiwa badala ya kushirikiana kurekebisha kasoro zinazojitokeza, tunatafuta visingizio vya kukwepa majukumu, au kulaumiana. Nasema, lazima tukiri na kudumisha dhamira ya kweli ya kutaka muafaka wa kisiasa, kijamii na kiuchumi katika nchi yetu.

            Jambo la pili ni umuhimu wa kuvumiliana, kustahimiliana na kusahau yaliyopita. Muafaka wa kweli unaanza na methali:  “Yaliyopita si ndwele, tugange yajayo.” Muafaka wowote wa kijamii hauwezi kudumu iwapo kila siku mtakuwa mnakumbushana au kutishana kwa mambo ambayo yamepita.  Kiini cha muafaka ni ujasiri na kuachana na yaliyopita; ni kuacha kutonesha vidonda, maana vidonda vinavyotoneshwa kila mara kamwe haviwezi kupona.

            Jambo la tatu ni kuaminiana.  Muafaka wowote hauwezi kudumu iwapo wahusika watakuwa kila mara hawaaminiani, na kila mara wanatafuta sababu ya kutupiana lawama na kutoana kasoro.

            Jambo la nne ni kukubaliana juu ya mgawanyo wa majukumu ndani ya muafaka, vigezo vya utekelezaji wa majukumu hayo, na namna bora ya kusuluhisha matatizo yanayojitokeza, bila kuvunja muafaka wala kuzua magomvi.

            Mambo haya manne ni muhimu katika kufikia muafaka, na ni ya lazima iwapo tunataka tuwe na utulivu na uvumilivu wa kisiasa, ambalo ni sharti muhimu la maendeleo ya nchi, na ya wenye nchi.  Ndio maana ni muhimu sana tunapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu, tukubaliane kuwa kwa vyovyote vile lazima Muafaka wa CCM na CUF hapa Zanzibar ulindwe, utetewe, uenziwe, na uheshimiwe.

            Nimesikia wenzetu wa CUF wakisema kuwa hakutakuwa na Muafaka mwingine.  Nakubaliana nao, iwapo nia yao ni kuhakikisha muafaka uliopo hauvunjiki. Lakini kama wanachosema kinaashiria vurugu na fujo, sikubaliani nao hata kidogo, maana hapo sasa ni kuchezea moto.  Lakini kwa dhati kabisa nasema lazima tuhakikishe kuwa muafaka uliopo unadumu. Hatuna ruhusa ya kurudi nyuma.

            Napenda kuamini kuwa Muafaka huu baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Wananchi (CUF) ni kielelezo cha dhamira ya kweli ya kuondoa dosari mbalimbali zilizojitokeza wakati na mara baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000. Na kila mwenye nia njema atakiri kuwa zimefanyika juhudi kubwa za kutekeleza Muafaka huu katika mazingira magumu kisiasa na kiuchumi.

Katika Muafaka ule, sehemu kubwa ya utekelezaji tuliibebesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), ambayo sote tunajua ilipata ugumu wa kisiasa katika kuwashawishi Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa CCM kupitisha Marekebisho ya Nane na ya Tisa ya Katiba ya Zanzibar na Sheria nyingine. Itakumbukwa kuwa marekebisho hayo yalipitishwa na Baraza la Wawakilishi wakati huo likiwa na Wajumbe wa CCM peke yao.

Sisi kwenye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivi majuzi tulishindwa kupitisha Bungeni baadhi ya mapendekezo yetu ya Marekebisho ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Lakini Marekebisho ya Nane na Tisa ya Katiba ya Zanzibar yalifanywa na kuwezesha utekelezaji wa mambo mengi mengine makubwa na ya msingi yaliyotakiwa na Muafaka.  Hayo ni pamoja na Marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar, kuundwa upya kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, kuanzishwa kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka, kufanyika—kwa mafanikio makubwa—Uchaguzi Mdogo kule Pemba mwaka juzi, kuanzishwa kwa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, na mengine mengi. Haya ndiyo mambo ya msingi kabisa yanayohakikisha uchaguzi huru na wa haki.

Mimi, kwa dhati kabisa, mbele yenu nampongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Ndugu yetu Amani Abeid Karume, na Serikali yake, kwa kazi kubwa waliyoifanya kuwezesha mambo haya kutekelezwa.

            Mimi nimeshiriki katika juhudi nyingi za usuluhishi katika nchi zetu za Kiafrika.  Ni nadra sana kwa Serikali kukaribia, wacha kufikia, kiwango cha utekelezaji wa makubaliano kilichofikiwa na SMZ.  Hivyo, ninashangaa sana ninaposikia kauli za kubeza utekelezaji huu, kana kwamba wakosoaji hao hawafurahii hatua hii kubwa ya utekelezaji iliyofikiwa.  Wengine wanathubutu hata kutoa picha ya kama vile hakuna lililofanywa kutekeleza Muafaka. Najiuliza. Lengo la kauli kama hizo ni nini?  Kuikatisha tamaa SMZ?  Kampeni ya kuichafulia jina?  Au kuendelea kujenga mazingira ya kuja kukataa matokeo ya uchaguzi na kujikosha? Kwa hakika utekelezaji wa Muafaka uliofanywa hadi sasa unatoa fursa nzuri kwa vyama vyote vya siasa kuzitumia ipasavyo taasisi na sheria zilizowekwa sasa kuendesha siasa za kistaarabu badala ya kulalamika tu, na wakati mwingine hata kupotosha ukweli.  Narudia.  Muafaka wa kweli unahitaji dhamira ya kweli ya pande zote.  Bila hivyo tunajisumbua bure.

            Najua kuwa yapo mambo machache ambayo hayajatekelezwa na Serikali.  Lakini, kila mwenye nia njema, ataona kwamba mambo hayo aghalabu ni yale yanayohitaji fedha nyingi ambazo sote tunajua Serikali hainazo.  Kwa mfano, katika eneo la fidia kwa waathirika wa matukio mbalimbali ya kisiasa, hata wahisani wetu ambao hapo mwanzo walituahidi kwa hamasa kubwa kwamba wangesaidia, hawajafanya hivyo, na sasa wengine wamebadili kauli.

            Wapo waliosema kuwa hawana fedha.  Wapo pia waliosema kwamba hawawezi kufidia madhara yanayompata mtu baada ya kuvunja Sheria za nchi.  Hayo ndiyo mazingira inayokabiliana nayo Serikali katika kutekeleza Muafaka.  Hata hivyo, ni jambo la faraja kwamba eneo hili la Muafaka, ambalo utekelezaji wake bado haujawezekana kwa ukamilifu, linahusu kunufaika kwa mtu mmoja mmoja.  Yale yanayohusu manufaa kwa wote, karibu yote yametekelezwa.  Naamini SMZ bado inatafuta njia nyingine mbadala za kutafuta fedha kwa ajili ya fidia hizo.  Lakini hilo litachukua muda.  Muhimu ni kwamba dhamira ya utekelezaji bado ipo. Tuwe waungwana basi, na tusikimbilie kuihukumu SMZ kwa umaskini wa nchi yetu na utegemezi wetu. 

Ndugu Wana-Semina:

            Nasikitika kuwa zipo dalili kwamba dhamira na ari ya Muafaka inaonekana kupungua.  Hii inadhihirishwa na kauli za baadhi ya viongozi wa kisiasa zinazoashiria kujenga chuki, kuleta shari, na kueneza uchochezi. Tulikubaliana katika Muafaka kuachana na kauli kama hizi.  Tulikubaliana pia katika Muafaka kuheshimu Sheria za nchi.  Tuliweka utaratibu wa mashauriano patokeapo kutoelewana au matatizo.  Sasa kwa nini mwaka huu mambo haya yamezidi?

Kuendelea kutolewa kwa kauli kama hizi na vitendo vya kuvunja Sheria ni ukiukaji wa Muafaka na dhamira yake.  Jukumu la utekelezaji wa Muafaka si la Serikali peke yake, bali pia ni la Vyama vya Siasa vinavyohusika. Viongozi wa Vyama vya Siasa wana nafasi kubwa kwa sababu wana uwezo wa kuonana na kubadilishana mawazo na wanachama wao, na wana ushawishi mkubwa kwao.  Wakipenda, viongozi hao wanaweza kuimarisha imani ya wafuasi wao juu ya Muafaka. Wakipenda pia wanaweza kufifisha imani hiyo kutegemeana na ujumbe wanaoufikisha kwa wanachama wao na wananchi.  Kila chama kijiulize kipo upande upi:  Upande wa kuimarisha dhamira na imani juu ya Muafaka au upande wa kuidhoofisha na hivyo kuhujumu utekelezaji wake.

            Kwa upande wa Serikali, ninaridhika na juhudi za dhati zinazofanywa kuweka mazingira mazuri ya kufanikisha Muafaka. Mimi mwenyewe nimekuwa nikisisitiza katika mikutano yangu mbalimbali, ndani na nje ya nchi, kwamba nimekusudia katika kipindi changu cha uongozi kilichobaki kuhakikisha kwamba juhudi zinachukuliwa kufanikisha Muafaka na kuiona Tanzania inaendesha siasa za ushindani bila ya kugombana.  Tukiwa sote na dhamira ya kweli ya Muafaka, tofauti za mawazo tuliyonayo haziwezi kuwa chanzo cha kugombana.  Tuufanye umoja wetu, na udugu wetu, kuwa jambo muhimu zaidi.

Aidha, tuhakikishe kwamba vyombo na maadili yanayohusiana na demokrasia ya uchaguzi hasa wakati wa kampeni na uchaguzi wenyewe vinaimarishwa. Tuwe na muafaka miongoni mwa vyama vyote juu ya maadili ya kisiasa na namna ya kuhakikisha yanafuatwa na kila chama cha siasa.

 

Uwazi na Ukweli, na Elimu ya Uraia na Mpiga Kura

Ndugu Wana-Semina:

            Ipo hisia iliyojengeka kwa wananchi kuwa siasa ina ulaghai kiasi fulani ndani yake.  Mimi naamini kuwa si lazima iwe hivyo, lakini hiyo haiondoi wajibu wetu wanasiasa kuongeza uadilifu wetu ili kufuta hisia hizo.  Na tusisahau kuwa wakati mwingine mbio za mwongo huwa fupi kweli kweli kwenye siasa.

            Mgombea mmoja wa Ubunge, tumwite Masanja, alikuwa anazungukazunguka kwenye jimbo analowania akimchangamkia kila anayemkuta. Akakuta watoto kadhaa wanacheza nje ya nyumba, na mama mmoja akiwaangalia.  Akamwendea yule mama, akamsabahi, na kisha akasema:  “Watoto wazuri sana hawa, mama.  Naweza kuwabusu?”  “Endelea tu,” akajibu yule mama.

Baada ya kuwabusu, Mheshimiwa Masanja akarejea kwa yule mama, na kusema, “Haki ya Mungu sijawahi kuona watoto wazuri kama hawa.  Ni wako sio?” Kabla yule mama hajajibu, Mheshimiwa Masanja akaendelea, “Lazima watoto hawa ni wako.  Hebu ona macho yao mazuri, nyuso angavu, na sauti kama tausi.  Wanafanana na wewe kwa kila hali.” Yule mama akabaki anamkodolea macho Mheshimiwa Masanja, aliyeendelea kusema: “Tafadhali mama yangu. Nakuomba mume wako akirejea nyumbani umwambie kwamba Bwana Masanja alipita hapa kumsabahi.”  Yule mama akaamua kumtolea uvivu. “Tazama Bwana Masanja.  Sina muda na ulaghai wenu wanasiasa.  Kwa taarifa yako mimi sina mume, na hapa ni kituo cha watoto yatima!”

Ndugu Wana-Semina:

Naomba pia tuwe na muafaka wa kitaifa wa kuendesha shughuli za kisiasa kwa uwazi na ukweli.  Tuache udanganyifu.  Kwa mfano nimeambiwa kuwa kuna sehemu ya nchi yetu ambapo wazee walidanganywa na wanasiasa wa chama fulani kuwa wao hawana haja tena ya kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura eti kwa vile tayari wamekamilisha mchango wao kwa taifa hili na hivyo wanayo haki kupumzika!!

            Huko nyuma katika mojawapo ya chaguzi kipo chama fulani kilichowadanganya wananchi kuwa baada ya kufikia Muafaka mwaka 2001, basi vyama vyote vya siasa ni sawa tu, na ukipigia kura mgombea wa upinzani ni sawa tu na kumpigia kura mgombea wa Chama Tawala.

            Na mifano ya namna hii ipo mingi.  Nasema, hatuwezi kuimarisha demokrasia ya vyama vingi kwa udanganyifu.  Na kwa hili naomba sana vyombo vya habari vitusaidie kuwaumbua wanaowadanganya wananchi.

            Na hili linanifikisha kwenye umuhimu wa elimu ya uraia, na elimu ya mpiga kura.  Ni dhahiri udanganyifu unaofanywa na baadhi ya wanasiasa unachangiwa na kutoelewa kwa wananchi juu ya haki zao katika siasa na katika demokrasia ya vyama vingi.  Jambo hili ni muhimu, na ni la kutiliwa mkazo.  Na, kwa kadri inavyowezekana, ni vizuri elimu hiyo itolewe na Tume ya Uchaguzi ya Taifa, na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.

            Lakini viongozi wa kisiasa, wa vyama vyote, nao wanayo nafasi nzuri ya kutoa elimu ya uraia, lakini pale tu ambapo wamekuwa wawazi na wakweli, na waadilifu, wasiotumia fursa hiyo kupigia kampeni vyama vyao au kuhujumu vyama vya wenzao.  Vivyo hivyo Asasi Zisizokuwa za Serikali zina nafasi nzuri ya kutoa elimu ya uraia, na elimu kwa wapiga kura.  Na kwa kweli wengine wamefanya kazi nzuri huko nyuma.  Lakini narudia.  Elimu hiyo isiwe fursa ya kupigia kampeni chama kimoja, na kuponda chama au vyama vingine, au isitumike kama mbinu ya kuhujumu nchi yetu kutoka kwa watu wa nje.

Viongozi wa vyombo vya habari pamoja na vyombo vyao wana nafasi kubwa katika kutoa elimu ya uraia na kuendeleza dhamira ya Muafaka.  Wana uwezo mkubwa pia wa kuvuruga dhamira hiyo kama watataka kufanya hivyo. Lakini wajue wazi kuwa wanapotoa taarifa za kuchonganisha wanasiasa, au za kushabikia kauli za uchochezi na za kutishia amani zinazotolewa na baadhi ya wanasiasa, au za kupotosha ukweli, wanadhoofisha dhamira za Muafaka.

Mimi nawaomba wachague kuendeleza dhamira ya Muafaka na si kuidhoofisha, wajenge udugu wa Watanzania badala ya kufarakanisha jamii. Watakuwa wanachangia katika kuendeleza dhamira ya Muafaka ikiwa watatoa uzito na kipaumbele kwa habari zinazoonyesha kukerwa na uchochezi, zinazoheshimu haki ya kuelezea msimamo wa pande zote zenye mawazo yanayotofautiana, na pia habari zenye ukweli uliothibitishwa na utafiti.

Nawaomba sana waandishi wa habari wasikubali kununuliwa na wanasiasa, kwa madhumuni ya kuwapaka matope washindani wao, na kuwatukuza waliowanunua.  Hivi sasa yapo magazeti nchini ambayo kila uchao, hawakosi baya la kuandika kuhusu wanasiasa fulani.  Na yapo magazeti ambayo mabaya ya wanasiasa fulani kamwe hayaandikwi, na yakiandikwa wahusika wataandamwa sana, na pengine kutishwa.

            Sisemi mabaya ya wanasiasa yasiandikwe; nasema uwepo uwiano mzuri isionekane kuwa wapo watakatifu daima na wapo waovu daima.

            Mgombea Urais katika nchi moja tajiri alikasirishwa sana na yaliyoandikwa kuhusu yeye na gazeti moja kubwa katika mji wake.  Akaenda kwa hasiri kumwona mhariri wa gazeti hilo.  “Unaandika uwongo kabisa kuhusu mimi kwenye gazeti lako, na unajua hivyo!” Yule mhariri akatabasamu na kumjibu, “Mheshimiwa, unishukuru kwa kuandika uongo.  Hebu fikiri kampeni yako ingeishia wapi iwapo tungeandika ukweli kuhusu wewe?”

Ndugu Wana-Semina:

            Nimefurahishwa pia na ushirikishwaji wa viongozi wa kijamii katika semina hii.  Viongozi wa kijamii, hasa wa kidini wana nafasi ya pekee kabisa katika kuendeleza dhamira ya Muafaka. Katika dini, madhehebu na taasisi zao wanazoziongoza wanakutana na wafuasi wa vyama mbalimbali vya kisiasa.  Nawaomba wafikishe ujumbe wa upendo, amani, umoja na uungwana kwa waumini wa dini zao. Aidha, wanapoendesha ibada, ningependa waendelee kuiombea nchi yetu na watu wake ili tufaulu mtihani wa uchaguzi mkuu unaotukabili mwaka huu.

 

Utawala wa Sheria na Haki za Binadamu

Ndugu Wana-Semina:

            Hakuna haki isiyokuwa na mipaka.  Nasi wachanga kwenye demokrasia ya vyama vingi lazima tuwe tayari kukubali mipaka ya haki zetu ndani ya mfumo huu wa siasa.  Maana wapo ambao kwa vitendo na kauli zao ni kama vile hawadhani ipo mipaka katika uhuru wao wa kisiasa na uhuru wa maoni.  Na zaidi sana tusisahau kuwa sisi ni Waafrika, wenye utamaduni wetu, na maadili yetu.

            Ukweli ni kuwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nao una maadili yake ambayo lazima tuyazingatie.  Mojawapo ni hayo ya uwazi na ukweli niliyoyasema. Si ruhusa, kwa makusudi, kuwadanganya wananchi na wapiga kura.  Jingine ni umuhimu, na kwa kweli ulazima, wa kufuata sheria.

            Kwa mfano, sheria inasema kuwa kabla ya kufanya mkutano wa hadhara au kufanya maandamano upate kibali cha Polisi.  Lengo lake si kuzuia, bali ni kuratibu na kuwapa Polisi muda na nafasi ya kusimamia mikutano na maandamano ili amani idumishwe. Lakini utakuta mwanasiasa ambaye, akiulizwa, anasema anapenda siasa za amani, huyo huyo anakerwa sana akiambiwa apate kwanza kibali cha Polisi.  Hebu fikiri.  Kitoke Chama “A” kifanye maandamano bila kuiarifu Polisi, halafu njiani kikutane na maandamano ya Chama “B” ambacho nacho hakitaki kupata kwanza kibali cha Polisi, unafikiri kutatokea nini kama si mlipuko wa fujo, na pengine kuumizana au hata kutoana roho?

            Napenda vyama vya siasa vyote vielewe kuwa kazi ya Polisi ni kuratibu na kuhakikisha usalama wakati wa shughuli za kisiasa.  Hawako kupendelea chama chochote, na wala hawana ruhusa kuzuia mkutano wa kisiasa au maandamano bila sababu ya msingi, na siku zote wataeleza wazi sababu hiyo.  Na ni wajibu wetu sote wanasiasa kufuata sheria na kuheshimu utawala wa sheria.  Na pale unapoona umezuiwa kwa sababu ambazo si za msingi utaratibu wa kukata rufaa upo.  Ufuatwe huo, maana siku zote tabia ya kuvunja sheria haina mwisho mwema.

            Na, kama nilivyosema, ni vizuri pia kuzingatia mila na desturi zetu.  Uhuru wa kisiasa, na uhuru wa maoni, usiwe uhuru wa matusi na lugha chafu, na usiwe uhuru wa uchochezi.  Majukwaa ya siasa yawe ya kuuza sera na mikakati, si ya kuchochea fujo na uvunjifu wa sheria.

            Kila chama cha siasa kina vijana, wenye damu inayochemka.  Unapochochea vijana wa chama chako ujue wengine nao wanaweza kuchochea vijana wao.  Hapo itakuwa zahama kubwa.  Na mimi napenda kuweka wazi kuwa wakati mwingine nina kazi kubwa kuwazuia vijana wa CCM, ambao ndio wengi, wasilipize visasi.  Sasa nasema, tafadhali sana tuwe na muafaka wa kitaifa kuhusu jambo hili.  Majukwaa ya siasa kamwe yasiwe fursa ya kutukana, au kuchochea fujo na vurugu.

            Na pia ni vema tujenge tabia ya kuheshimu vyombo vya dola.  Hawa tumewafunza na kuwapa silaha kihalali ili walinde amani na usalama katika nchi yetu.  Na pamoja na semina zote tunazowapa kuhusu haki za binadamu tujue kuwa na wao ni binadamu, wenye hisia.  Ni vema sisi wanasiasa tuwatendee haki kwa kuwachukulia kama binadamu wenzetu ambao nao hawapendi kutukanwa.

            Na pia, kama nilivyowahi kusema, utulivu wa kisiasa ni matokeo ya vyama vyote kukubaliana kuwa tuwe na ushindani wa kisiasa wa kistaarabu.  Na wala si kweli kuwa kila panapotokea matatizo au fujo kwenye siasa, wa kulaumiwa ni Chama Tawala peke yake, na Serikali.  Wazungu wana msema:  “It takes two to tango”.   

            Na mwisho, kwa kuzingatia maadili ya Kiafrika, ni vema heshima ya nafasi kuu za uongozi katika nchi yetu ziheshimiwe.  Leo mimi ni Rais.  Mwaka kesho sitakuwa Rais.  Heshima ya ofisi hii si yangu binafsi, ni heshima ya ofisi.  Hivyo hata kama hunipendi binafsi, unao wajibu kuheshimu ofisi hii.  Yapo mengi mema tunayoweza kuiga kutoka nchi tajiri. Naomba tusiige dharau.  Tusiige kushusha heshima ya viongozi wetu katika jamii.  Hili pia naomba tuwe na muafaka nalo katika nchi yetu.

 

Utamaduni wa Ushindani na Uadilifu

Ndugu Wana-Semina:

            Nitashukuru pia iwapo semina hii itahimiza muafaka wa kitaifa kuhusu uadilifu katika siasa na utamaduni wa ushindani.  Wahenga walisema:  “Asiyekubali kushindwa si mshindani”.  Hivyo kwenye siasa, kwenye chaguzi ndani ya kila chama, na vile vile kwenye chaguzi zinazoshindanisha chama na chama, lazima kuwe na uchaguzi huru na wa haki, lakini baada ya hapo kila mgombea, awe mtu binafsi au chama, akubali kuwa kuna kushinda, na kuna kushindwa.

            Uchaguzi ukiisha tuendelee kujenga nchi badala ya kushinda mahakamani kufungua kesi baada ya kesi kila baada ya uchaguzi.  Pale ambapo ni lazima, sawa.  Lakini ninaamini kesi nyingi zinazofunguliwa zinatokana na kukataa kushindwa tu, badala ya kuonewa.

            Na kama nilivyosema uadilifu ni muhimu katika vyama vyote.  Tusiwape wananchi hisia kuwa siasa ni mahali pa ulaghai, rushwa, wizi na matumizi mabaya ya fedha.  Kila chama cha siasa kiwe tayari kupimwa uadilifu wake kwa vigezo vile vile ambavyo Chama Tawala na Serikali yake inapimwa navyo. Maana wasipokuwa waadilifu, wawazi na wakweli wakati wakiwa kwenye upinzani, kwa hakika wataendelea kuwa vivyo hivyo wakibahatika kuingia madarakani.

 

Hitimisho

Ndugu Wana-Semina:

            Kwa kumalizia naomba nikumbushe kidogo tu kwamba Tanzania imekuwa moja miongoni mwa nchi chache Barani Afrika iliyo na utulivu mkubwa wa kisiasa na yenye utamaduni wa kuvumiliana na kusaidiana. Tofauti zetu za kabila, dini na itikadi hazikuruhusiwa kudhoofisha udugu, umoja, na mshikamano wetu. Utamaduni huu hauna budi kuenziwa na kuimarishwa.  Naomba sote tukubaliane kuwa tofauti za kisiasa hazitaruhusiwa kuwa chanzo cha kufarikiana na kuhasimiana.  Tukidumisha utulivu na ustahamilivu tutaondoa shaka ya kutoaminiana baina yetu. Tukiimarisha dhamira ya muafaka tutaona mema zaidi kuliko mabaya. Ni vizuri watu wakaishi kwa upendo na umoja na kukabili matukio yoyote ndani ya Taifa letu kwa pamoja, tukijua sote ni wadau kamili wa hatma ya nchi yetu. Wanasiasa tukumbuke kuwa watu wetu ni kama watu wengine duniani, wanaweza kubadilika kwa mujibu wa mazingira yalivyo, hivyo tusiwafanye wakabadilika kwa mivutano isiyokuwa na maana. Badala yake tuwawekee mazingira ya kimaendeleo na ya kujenga upendo na umoja wa Kitaifa.

            Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa Semina hii ya Viongozi wa Kitaifa yenye Dhamira ya Kuendeleza Ari ya Muafaka wa CCM na CUF imefunguliwa rasmi.

            Ahsanteni kwa kunisikiliza.