HOTUBA YA MWENYEKITI
WA CHAMA CHA MAPINDUZI NDUGU BENJAMIN
WILLIAM MKAPA, AKIFUNGUA MKUTANO MKUU MAALUM WA SABA WA CCM; CHIMWAGA, DODOMA,
24 JUNI 2006
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete;
Makamu
Mwenyekiti wa CCM, Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Ndugu Amani
Abeid Karume;
Makamu
Mwenyekiti wa CCM,
Ndugu John Samwel Malecela, Mb;
Makamu wa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Dkt. Ali Mohamed Shein;
Mwenyekiti
Mstaafu wa CCM na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mzee Ali Hassan Mwinyi;
Katibu Mkuu
wa Chama Cha Mapinduzi,
Ndugu Philip Japhet Mangula;
Makamu
Mwenyekiti Mstaafu wa CCM, Zanzibar na
Rais Mstaafu wa Zanzibar, Dkt. Salmin Amour
Muasisi Wetu
Mzee Rashid Mfaume Kawawa;
Wajumbe wa
Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi,
Wajumbe wa
Halmashauri Kuu ya Taifa,
Wajumbe wa
Mkutano Mkuu,
Wazee na
Waasisi wa TANU, ASP na CCM,
Mabibi na
Mabwana.
1. Napenda kukukaribisheni
wote katika Mkutano Mkuu wa Taifa wa Saba wa Kawaida wa Chama Cha
Mapinduzi. Mkutano huu umekuwa wa
kawaida baada ya Mkutano Mkuu wa Taifa kufanya marekebisho kwenye Katiba ya
Chama hapo mwaka jana. Kwa mujibu wa marekebisho
hayo, Mkutano Mkuu wa Taifa sasa utakutana mara tatu katika kipindi cha miaka
mitano badala ya mara moja tu kama ilivyokuwa huko nyuma.
2. Mwaka mmoja uliopita
tulikuwa hapa Chimwaga kuhitimisha kazi muhimu ya kuteua wagombea wa Chama
chetu kwa uongozi wa Taifa letu kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2005. Ushindi wa
kihistoria tulioupata ni kielelezo kwa mara nyingine cha imani ya Watanzania
kwa historia na uzoefu wetu; kwa ubora na usahihi wa sera zetu; kwa matumaini
ya amani na maendeleo tunayoendelea kuwapa wananchi; na kwa ubora na uzoefu wa
wagombea wetu.
Nauliza kama nilivyouliza tena na tena kwenye
kampeni: Nani kama CCM? Nani kama CCM?
Ndugu Wajumbe,
3. Katika mkutano wetu wa
tarehe 4 Mei, mwaka jana tulifanya kazi kubwa ya kuteua Mgombe Mgombea Urais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama chetu. Kwa njia ya uchaguzi kama Katiba na Kanuni
zetu zinavyotaka, tulimteua ndugu Jakaya Mrisho Kikwete kwa wingi mkubwa wa
kura. Tulipompeleka kwa wananchi,
aliibuka na ushindi mkubwa wa kishindo wa asilimia 80.28, na hivi sasa ndiye
Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Nne. Ni wajibu wetu sote kutumia fursa ya Mkutano
huu kumpongeza kwa dhati Ndugu Kikwete kwa ushindi huo mkubwa wa aina yake
alioupata na kukipatia Chama Cha Mapinduzi.
4. Tumpongeze pia Ndugu
Amani Abeid Karume kwa kupata ushindi wa asilimia 53.18 ambao umemwezesha
kuendelea kuwa Rais wa Zanzibar kwa kipindi chake cha pili na cha mwisho. Kwa mazingira ya Zanzibar, ushindi huo nao ni
wa kishindo.
5. Pongezi zetu
hazitokamilika bila ya kuzielekeza pia kwa Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wa
CCM kwa kupata imani za wapiga kura.
Ndugu Wajumbe,
6. Wabunge, Wawakilishi na
Madiwani. Mlifanya kazi kubwa sana ya kutetea rekodi ya Chama chetu kwenye
uongozi wa Taifa, na kujenga hoja ya kutosha kwa nini tuendelee kupewa dhamana
ya uongozi wa Taifa. Sifa zenu zilikutangulieni. Maana ushindi kwenye uchaguzi
unasimama kwa miguu miwili. Sifa za Chama kwa upande mmoja na sifa za wagombea
kwa upande wa pili. Miguu yetu yote miwili katika CCM ilikuwa imara na ushindi
ulikuwa stahili yetu.
7. Wengi wenu hapa
mlishiriki mchakato wa uteuzi wa wagombea katika ngazi zote. Nakupongezeni sana
kwa kazi nzuri mliyoifanya. Nakushukuruni sana. Yapo maamuzi mengine magumu
ilibidi tuyafanye. Kuna wakati na mahali tulijikuta tuna wagombea wawili au
zaidi ambao wote wana sifa kubwa sana, na wote wanatosha na kustahili kubeba
bendera ya CCM. Kwa moyo mzito ilibidi tuchague mmoja na kumwacha mwingine, si
kwa vile hafai bali kwa vile hatuwezi kuwachukua wote.
Nafasi ya Wanawake
Ndugu Wajumbe:
8. Tukiwa Chama kikubwa
kuliko vyote, Chama Tawala, tulikuwa pia na wajibu wa kuhakikisha kuwa baada ya
uchaguzi tunakuwa na Bunge na Mabaraza ya Halmashauri yenye uwiano wa kijinsia
unaotimiza dhamira yetu na makubaliano ya nchi za SADC kuwa angalau asilimia
thelathini ya Wabunge wawe wanawake. Ilibidi tufanye juu chini kupata wagombea
wanawake wa kutosha kwenye majimbo. Iibidi wakati mwingine tuwasihi wagombea
wakiume walioongoza kwenye kura za maoni waridhie uamuzi wetu wa kuwachukua
wagombea wanawake. Nafurahi kuwa walielewa, wengi hawakununa sana, na
waliwasaidia hao wagombea wanawake hadi wakashinda. Nauliza tena. Nani kama
CCM? Nani kama CCM?
9. Nawapongeza wagombea
wetu wanawake kwa ujasiri wao mkubwa na kwa kuitikia wito wetu kuwa wajitokeze
kwa wingi kugombea. Binafsi
wamestahimili mengi. Familia zao zimevumilia mengi. Wamefanya kazi kubwa kwa
niaba ya Chama. Nawashukuru sana.
10. Namshukuru pia Rais wetu
wa Jamhuri ya Muungano na Rais wa Zanzibar kwa uamuzi wao wa busara wa kuteua
wanawake wengi kuliko zamani kushika nafasi muhimu katika uongozi wa nchi.
Nionavyo mimi, kama ilivyokuwa kwa wale niliowateua mimi wakati wangu, kinamama
hawa wameonyesha uelewa na uwezo wa uongozi. Wameonyesha wako tayari. Swali la
msingi ni kiasi gani wanaume wako tayari kutoa nafasi zaidi kwa wanawake siku
zijazo, si katika Serikali tu, bali pia katika familia, katika jamii, katika
biashara na katika vyama vingine vya siasa. Kama mjuavyo uamuzi wa Umoja wa
Afrika ni kuwa hatimaye, mapema iwezekanavyo, uwepo usawa wa kijinsia katika
uongozi wa nchi zetu na Umoja wetu. Ni vema Tanzania ijiandae na ijiweke mahali
pazuri kuwa miongoni mwa nchi za kwanza barani Afrika kufikia lengo hilo.
11. Ushindi mkubwa
tulioupata katika uchaguzi Mkuu wa 2005 tulipewa na wananchi kwa imani
yao. Hatuna budi kuwashukuru kwa imani
hiyo kubwa. Ushindi huo mkubwa waliotupa
umeambatana na matarajio makubwa kwa Serikali za CCM zilizoundwa mara tu baada
ya Uchaguzi Mkuu. Kwa kujiamini kabisa,
tunawahakikishia Watanzania kwamba matarajio yao yatakidhiwa. Kujiamini kwetu huko kumeimarishwa na jinsi
Serikali ya Awamu ya Nne ya Jamhuri ya Muungano na ile ya Awamu ya Sita
inayoendelea kule Zanzibar zilivyoanza kazi kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi
mpya.
Ndugu Wajumbe
12. Mkutano huu ni wa
kazi. Kazi ya kutathmini tulivyofanya
huko nyuma katika kazi za Chama na za Serikali, hususan utekelezaji wa Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya 2000. Lakini pia kazi
ambayo ni ya msingi zaidi ni ya kutafakari majukumu yaliyo mbele yetu, hasa
kuhusiana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2005. Nakuombeni kazi hizo tuzifanye kwa umakini
mkubwa kama unavyotarajiwa Mkutano wa hadhi kubwa kama huu wetu.
Ndugu Wajumbe,
13. Katika mkutano huu
tutafanya pia Uchaguzi wa Mwenyekiti kwani kama wote mnavyofahamu, nitang’atuka
baadaye katika Mkutano huu. Nakuombeni
kama kawaida yetu katika CCM wakati utakapofika tufanye uamuzi thabiti.
Ndugu Wajumbe,
14. Mengi nakusudia kuyasema
kesho wakati nitakapong’atuka. Lakini
siyo siri kwamba miongoni mwa mambo yaliyochangia ushindi wetu mkubwa katika
Uchaguzi Mkuu uliopita, ni kutekelezwa kwa kiwango kikubwa yale tuliyoahidi
katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya 2000.
Tuliwapa wananchi programu nzuri ya maendeleo kwa kipindi cha 2000 hadi
2005, na tukaitekeleza. Na wao
wakatuchagua tena. Kama ambavyo Ndugu
Rais amekuwa akisisitiza kwamba kumalizika kwa Uchaguzi wa 2005 ni kuanza kwa
maandalizi ya Uchaguzi wa 2010. Sasa
tuna Ilani ya uchaguzi ya 2005.
Changamoto yetu kubwa ni kuitekeleza.
Na hakuna cha kusubiri kuanza kuikabili changamoto hiyo.
15. Kwa hilo, napenda
kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Nne kupitia ndugu Rais
Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuianza kazi hiyo kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi
mpya. Ni dhahiri kabisa bajeti ya
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejielekeza katika utekelezaji wa
Ilani. Na alipokuwa akiiwasilisha bajeti
hiyo Bungeni, Waziri wa Fedha alisisitiza mara kwa mara na kuonyesha jinsi
bajeti hiyo ilivyojikita katika utekelezaji wa Ilani.
16. Pongezi zangu pia ziende
kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi mahiri na makini wa Rais
Karume. Na wenzetu huko Zanzibar nao
wameanza utekelezaji wa Ilani kwa ile ile ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya.
17. Utakelezaji wa Ilani si
wa Serikali peke yake. Nasi katika Chama
ni jukumu letu pia. Tuhamasishwe na
fursa ya Mkutano Mkuu huu wa Taifa kujipangia mikakati ya utekelezaji wa jukumu
hilo. Lengo ni kuhakikisha kwamba mwaka
2010 utukute tukiwa tumetekeleza yote tuliyoahidi katika Ilani. Nitafurahi sana kama majadiliano yetu katika
Mkutano huu yatachukua mkondo huo kwa sehemu kubwa.
Ndugu Wajumbe, Tuanze kazi.
Mkutano umefunguliwa.