Ilani ya CCM Habari Mpya Historia ya TANU na ASP Kutoka Magazetini Hotuba

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JARIDA LA MKEREKETWA

Uchaguzi Mkuu wa CCM wa mwaka 2002 ulikuwa halali na wa mafanikio makubwa
 
  • Walioshindwa wakubali kwamba kuna kushinda na kushindwa katika uchaguzi
   
 

Katika mkutano wake wa mwezi uliopita wa Septemba, Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM miongoni mwa mengine ilipokea taarifa ya Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu maamuzi iliyofanya baada ya kusikiliza na kuyajadili malalamiko yaliyotolewa na baadhi ya wagombea wa nafasi mbali mbali za uongozi katika ngazi ya Mkoa katika Uchaguzi Mkuu wa CCM uliofanyika mwaka jana (2002).
Kamati Kuu haikupata lalamiko hata moja kuhusiana na uchaguzi wa Ngazi ya Taifa uliofanyika Chimwaga mwezi Oktoba, 2002.
Kuhusiana na chaguzi za Ngazi ya Mkoa, Kamati Kuu ilipokea malalamiko kutoka Mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Iringa, Kagera, Mara, Mbeya, Mwanza, Rukwa na Singida.
Kwa jumla, malalamiko mengi yalijikita juu ya tuhuma za rushwa. Walalamikaji na walalamikiwa wote walipewa fursa ya kutosha ya kujieleza katika vikao husika na Kamati Kuu yenyewe kupitia Kamati ya Maadili ya CCM ilifanya uchunguzi wa kina wa kila tuhuma katika kipindi cha karibu mwaka mzima. Lakini hakuna hata tuhuma moja iliyothibitika.
Kilichobainika kwa malalamiko yote ni uchungu tu wa kushindwa ulioambatana na ugumu wa kukubali kushindwa. Lakini hayo ndiyo maisha katika ushindani wowote; kuna kushinda na kushindwa.
Kwa hiyo, uamuzi wa Kamati Kuu ni kwamba matokeo ya uchaguzi yaliyotangazwa katika mikoa yote iliyolalamikiwa ni halali na yanabaki yalivyo. Kwa mujibu wa Ibara ya 29 ya Kanuni za Uchaguzi wa CCM, uamuzi huo ni wa mwisho.
Halmashauri Kuu ya Taifa imeridhika kwamba si uchaguzi wa ngazi ya Taifa tu ambao haukuathiriwa na rushwa, bali pia hata chaguzi za ngazi ya Mkoa. Kwa hivyo, Halmashauri Kuu ya Taifa imeungana na kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Rais Benjamin Mkapa aliyoitoa katika hotuba yake ya ufungaji wa Mkutano Mkuu pale Chimwaga ambapo aliutangaza uchaguzi mkuu wa Chama kuwa na mafanikio makubwa. Kwa maneno yake Mwenyekiti, “mafanikio hayo makubwa yameonyesha pia kuwa CCM si mali ya mtu, ni mali ya watu, ambao ni wanachama.”
Halmashauri Kuu ya Taifa imeridhika pia kwamba mjadala kuhusu rushwa ndani ya Chama ambao umekuwa ukikuzwa sana na magazeti na vyombo vingine vya habari kwa kiasi kikubwa ni mkakati tu wa wapinzani wa CCM kukichafulia jina Chama wakati wakijiandaa kwa Uchaguzi Mkuu wa 2005.
CCM inawataka wanachama wake na wananchi wote kwa jumla wasimame kidete kufichua vitendo vya kweli vya rushwa (siyo dhana tu), lakini wasikubali kuingizwa katika mtego wa mikakati ya uchaguzi ya wapinzani.

Buriani Mzee Ibrahim Raha Jongo
  • CCM itakukumbuka daima

  • Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Mzee Ibrahim Raha Jongo (66) amefariki dunia tarehe 29/8/2003 usiku mjini Dar es Salaam.
     
     
     
    Enzi za uhai wake, Mzee Jongo akiwa jukwaani huko Shinyanga akiifanyia kampeni CCM
    Mzee Jongo ambaye alifariki dunia katika Hospitali ya Tumaini ambako alikuwa amelazwa kutokana na kusumbuliwa na afya yake alizikwa tarehe 31/8/2003 kijijini kwake Chamazi, katika Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam.
    Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Philip Mangula aliongoza maelfu ya viongozi wa CCM, Serikali na wanachi kwenye mazishi ya Mzee Jongo ambaye alizikwa kwa heshima zote za Chama.
    Katika salaam zake za rambirambi kwa niaba ya Halmashauri Kuu ya Taifa, wanachama wa CCM na wananchi kwa ujumla, Ndugu Mangula aliusifu mchango wa marehemu kwa kutumia kipaji chake cha usanii katika kukitetea na kukiimarisha Chama.
    Aidha, Katibu Mkuu wa CCM alimueleza marehemu kuwa alikuwa mtu wa watu na ni mtu aliyetoa mchango mkubwa sana wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Serikali wa mwaka 1995 na 2000.
    Marehemu alishika nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya CCM na katika Jumuiya ya CCM ya Wazazi.
    Mzee Jongo alikuwa Mjumbe wa NEC tangu mwaka 1997 hadi umauti wake ulipomfika.
           
         
             
    Marehemu Mzee Jongo