|
Halmashauri
Kuu ya Taifa imempongeza kwa dhati Mheshimiwa Benjamin
William Mkapa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi kwa kuchaguliwa
kuwa Mwenyekiti wa SADC kwa mwaka 2003/2004. Imempongeza
pia kwa kufanikisha kwa kiwango kikubwa Mkutano wa Wakuu
wa Nchi za SADC uliofanyika Mjini Dar es Salaam tarehe
26-27 Agosti, 2003.
Halmashauri Kuu ya Taifa imeendelea kumpongeza Rais
Mkapa kwa uwezo wake mkubwa wa uongozi ambao umeijengea
heshima kubwa Tanzania na Chama Cha Mapinduzi ndani
na nje ya nchi yetu.
Rais Mkapa amejibainisha waziwazi kwa sasa kuwa tegemeo
kubwa la kuzisemea nchi za Kiafrika na nyingine za Dunia
ya Tatu katika medani za Kimataifa, hasa katika wadhifa
wake wa heshima kubwa wa Mwenyekiti Mwenza wa Tume ya
Utandawazi Duniani.
Lakini pia, kwa haiba yake ya uongozi, Rais Mkapa amejitokeza
kuheshimika sana hata mbele ya macho ya nchi zilizoendelea.
Kutokana na kuheshimika huko, ameweza kujenga imani
kubwa ya nchi hizo siyo kwake yeye binafsi tu bali hata
kwa nchi yetu. Imani hiyo inajidhihirisha katika mambo
makuu yafuatayo miongoni mwa mengi mengine:-
(1) Tanzania ni miongoni mwa nchi chache sana zilizofanikiwa
kuingia katika mpango wa kuzifuatia madeni nchi maskini
duniani (HIPC).
(2) Tanzania hivi sasa inapokea misaada mingi na mikubwa
ya wahisani kuliko wakati mwingine wowote; na tena misaada
hiyo inaingizwa moja kwa moja katika bajeti ya Serikali
ukiwa ni ushahidi wa kutosha wa jinsi wahisani wanavyotuamini
kuwa tunazitumia vizuri fedha zao.
(3) Hivi sasa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoongoza
katika kuvutia vitega uchumi vya nje katika Bara la
Afrika.
Halmashauri Kuu ya Taifa ilijadili pia hotuba ya ufunguzi
wa Mwenyekiti ambayo ilibainisha mafanikio makubwa ya
jumla katika maeneo ya siasa, uchumi na huduma za jamii
wakati tukiwa tumemaliza nusu ya kipindi cha utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000-2005.
Katika hotuba hiyo ambayo imechapishwa katika ukurasa
wa pili wa jarida hili , Mwenyekiti alitoa changamoto
kwa viongozi na wanachama wa CCM kuwa mstari wa mbele
kutetea rekodi nzuri ya Chama na Serikali zake badala
ya kuwaachia wapinzani wanaojaribu kupuuza au kukebehi
rekodi hiyo, usahihi wa Sera za CCM na umakini wa utekelezaji
wake.
Halmashauri Kuu ya Taifa imempongeza pia Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Amani Abeid
Karume kwa kazi nzuri anayoifanya Zanzibar ambayo matunda
yake yanaonekana. Uchumi wa Zanzibar hivi sasa umekua
kutoka aslimia 3.2 mwaka 2000 hadi asilimia 5.6 mwaka
2002.
Mfumko wa bei umeshuka kutoka aslimia 6.2 mwaka 2000
hadi kufikia aslimia 5.2 mwaka 2002. Miundombinu hasa
ya barabara na mawasiliano pamoja na shule imekuwa bora
zaidi hivi sasa kote Unguja na Pemba na mabadiliko yanaonekana
kwa kila mtu.
Tangu Serikali ilipozundua mpango wa kupunguza umaskini
mwezi Mei 2002 imekuwa ikiweka mkazo mkubwa katika uimarishaji
wa sekta ya elimu, mawasiliano, afya na maji.
Aidha, Rais Karume ameirejeshea Zanzibar heshima mbele
ya Jumuiya ya Kimataifa kama inavyodhirishwa na kurejeshwa
kwa misaada ya wahisani.
Kutokana na mafanikio hayo makubwa, Halmashauri Kuu
ya Taifa ya CCM imezipongeza Serikali zote mbili, yaani
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Mapinduzi
ya Zanzibar kwa kutekeleza vizuri Ilani ya Uchaguzi
ya CCM ya mwaka 2000 na kuwataka Watanzania wajivunie
mafanikio hayo.
Pia Serikali zote mbili zimepongezwa kwa juhudi zake
za kuondoa kero mbali mbali za wananchi. |
|