| |
Halmashauri
Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi imesema kwamba imepokea
kwa mshangao na masikitiko makubwa, uamuzi wa Serikali
ya Israel wa kutaka kumuondoa kutoka nchini mwake Rais
wa Palestina, Mheshimiwa Yassir Arafat.
Katika
tamko lililotolewa hivi karibuni Mjiji Dodoma, NEC ambayo
ilikutana chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Benjamin
Mkapa imesema kwamba uamuzi huo wa fedheha una shabaha
ya kuvuruga jitihada zinazoendelea sasa za kuleta amani
kati ya Israel na Palestina na katika Mashariki ya Kati
kwa jumla.
“Hii inathibitisha kwa mara nyingine tena jinsi
ambavyo Serikali ya Israel isivyokuwa na dhamira ya
dhati wala utashi wa kisiasa wa kupata ufumbuzi muafaka
na wa kudumu wa mgogoro baina yao na Wapalestina”,
tamko la NEC lilisema.
Aidha, uamuzi huo na matendo kadhaa ya kikatili yanayofanywa
na Israel dhidi ya Wapalestina vinadhihirisha wazi nia
mbaya ya Serikali ya Israel ya kutaka kukwamisha Mpango
wa sasa wa amani Mashariki ya Kati, maarufu kwa jina
la Road Map, Mpango ambao hatimaye ungewezesha kuzaliwa
kwa Taifa la Wapalestina lililo huru, na linaloishi
bega kwa bega na kwa amani na Taifa la Israel. |
|
| |
|
Katika
tamko lake NEC imeazimia kuwa: “Halmashauri Kuu
ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi inapenda kuelezea kutokufurahishwa
kwake na uamuzi huo, na kuulaani vikali. Kutekelezwa
kwa uamuzi huo hakutaongeza usalama kwa Israel bali
kutazidisha chuki na kuchochea ghasia zaidi. Hivyo basi,
Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi inaitaka
Serikali ya Israel kubadili uamuzi wake huo. Kimsingi
Halmashauri Kuu ya Taifa inaisihi Serikali ya Israel
kurudi kwenye mstari wa utekelezaji wa Mpango wa Amani
wa sasa na Mkataba wa Oslo”.
“Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi
inatoa wito kwa Jumuiya ya Kimataifa, hususan Umoja
wa Mataifa na nchi za Marekani, Urusi, Uingereza na
Ufaransa zilizotayarisha Road Map kufanya kila linalowezekana
kusimamia na kuhakikisha utekelezaji wake”.
“Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi
inapenda kukariri msimamo wake wa kuwaunga mkono watu
wa Palestina katika harakati zao za kujikomboa na kupata
Taifa lao lililo huru wanaloliendesha wenyewe”.
|
|