Ilani ya CCM Habari Mpya Historia ya TANU na ASP Kutoka Magazetini Hotuba

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JARIDA LA MKEREKETWA

Serikali zatakiwa ziandae sherehe kabambe za miaka 40 ya Mapinduzi na Muungano mwakani kwani
 
  • Muungano wetu ndio mfano pekee Barani Afrika
  • Kauli mbiu ya MAPINDUZI DAIMA iendelezwe
   
  Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM imezitaka Serikali zote mbili za CCM za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ziandae sherehe kubwa za aina yake kuadhimisha miaka 40 ya Mapinduzi ya Zanzibar hapo tarehe 12 Januari, 2004 na miaka 40 ya Muungano wa Tanzania zitakazofikia kilele chake tarehe 26 Aprili, 2004.  
     
     
   
Mwalimu Nyerere akichanganya udongo wa Tanganyika na Zanzibar kudhihirisha muungano wa nchi hizo mbili hapo tarehe 26 Aprili, 1964
     
 
Katika kikao chake cha siku mbili kilichofanyika mjini Dar es Salaam hivi karibuni chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Benjamin William Mkapa, Kamati Kuu ilizingatia ujasiri wa Afro-Shiraz Party wa kuikomboa Zanzibar kutoka katika makucha ya wakoloni wa Kiingereza na utawala wa Masultani walowezi tarehe 12 Januari, 1964.
Wajumbe wa Kamati Kuu waliuthamini na kuuenzi mchango mkubwa wa mashujaa wa Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi thabiti wa Rais wa Chama cha Afro-Shiraz, Mzee Abeid Amani Karume, ambao walijitoa mhanga wa maisha yao kwa ajili ya uhuru wa kweli wa Wazanzibar na kuutokomeza kabisa utawala mkongwe wa Kisultani.
Katika kikao chake hicho, Kamati Kuu ilitamka kwamba Chama Cha Mapinduzi kina fahari kubwa kuona kwamba ASP na hatimaye CCM baada ya kuungana na TANU imeweza kuyalinda, kuyaendeleza na kuyadumisha Mapinduzi ya Zanzibar kwa karibu miako 40 sasa na kuyawekea msingi imara wa kuyadumisha milele.
Kutokana na ukweli huu, Kamati Kuu imesisitiza kwamba kauli mbiu ya MAPINDUZI DAIMA iendelee kutumika kama kielelezo cha dhamira ya kweli ya kuyadumisha mapinduzi hayo na matunda yake ambayo kila Mzalendo wa kweli wa Zanzibar na Tanzania nzima anapaswa kujivunia.
Aidha, Kamati Kuu ilitafakari pia ujasiri wa TANU na ASP chini ya Baba wa Taifa, Marehemu Mwalimu Julius Nyerere na Jemedali Mkuu wa Mapinduzi ya Zanzibar wa kuziunganisha nchi mbili za Tanganyika na Zanzibar na kuwa Tanzania tarehe 26 Aprili, 1964. Karibu miaka 40 sasa, Muungano wa Tanzania ndio mfano pekee Barani Afrika wa mafanikio ya utekelezaji wa dhamira ya Waafrika kuungana kikweli.
Kamati Kuu ina fahari kubwa kwamba vyama vya TANU na ASP na hatimaye CCM vimeweza kudumisha Muungano wetu kwa kipindi chote cha miaka 40 na kuujengea msingi imara wa kudumu milele, licha ya juhudi zinazofanywa na maadui wa Muungano za kutaka kuudhoofisha na kuusambaratisha ambazo zimegonga ukuta.
Kwa kuzingatia na kuthamini mafanikio hayo makubwa na kuwapa heshima wanayostahili waasisi wa Mapinduzi na Muungano, Kamati Kuu ya CCM imezitaka Serikali zote mbili za CCM ziandae sherehe kubwa za kuadhimisha miaka 40 ya Mapinduzi ya Zanzibar hapo tarehe 12 Januari, 2004 na miaka 40 ya Muungano wa Tanzania hapo tarehe 26 Aprili, 2004.
Kamati Kuu ya CCM inawataka wananchi wote bila kujali tofauti zao za kisiasa kushiriki katika sherehe hizo muhimu na kamwe wasikubali kurubuniwa na wezi wa fadhila wanaotaka tarehe hizo muhimu katika historia ya nchi yetu zisahaulike.
 
       
       
        Rais Nyerere anamvisha nishani ya uaminifu na ushujaa Rais wa ASP Mheshimiwa Abeid Amani Marume tarehe 19/2/1967 kwenye jengo la
Makao Makuu ya ASP Kisiwandui