|
|
| JARIDA
LA MKEREKETWA
|
“CCM
ni Chama kinachotawala kwa uhakika, Tanzania Bara na
Tanzania Zanzibar; kwa nini hatusijisifu na tunawaachia
ukumbi wapinzani kutubeza?” - Mkapa |
| |
|
|
|
Alipokuwa
akifungua Mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM uliofanyika
Dodoma Septemba 13,2003, Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa
aliwataka wanachama wa CCM kujisifu na kutembea kifua
mbele kutokana na mafanikio yaliyopatikana katika kutekeleza
Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2003, badala ya kuwaachia
ukumbi wapinzani kutubeza. |
|
|
|
|
|
| |
Kwa
niaba ya Kamati Kuu, na wananchi wa Dodoma, nawakaribisheni
nyote, Waheshimiwa Wajumbe, kwenye mkutano wetu huu
wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi –
Chama kinachotawala kwa
uhakika, Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar!
Matarajio yangu ni kuwa nyote mmepokewa vizuri, mmepumzika
vya kutosha, na sasa mko tayari kwa kazi kubwa na muhimu
iliyo mbele yetu.
Sisi, kwenye Chama Cha Mapinduzi, tunao utaratibu mzuri
wa kidemokrasia wa kuchambua matatizo na Sera, wa kuchuja
wanaowania uongozi na uwezo wao wa kutekeleza Sera na
maamuzi ya Chama. Ni heshima kubwa kuwa Mjumbe wa Halmashauri
Kuu ya Chama Tawala; lakini heshima hiyo tunaipata kwa
kuchaguliwa kwenye uchaguzi huru na wa haki. Pili, tunafanya
vikao vyetu kwa mujibu wa Katiba ya Chama Cha Mapinduzi.
Vikao hivi, pamoja na mambo mengine, vinatoa fursa nzuri
ya kufanya tathmini ya hali ilivyo ndani ya Chama, na
nje ya Chama, kwa uwazi na ukweli. Tunafanya pia tathmini
ya utendaji ndani ya Chama, na utendaji wa Serikali
nje ya Chama. Kisha tunaeleweshana na kukubaliana ni
kazi gani iliyo mbele yetu, na mipango ya kwenda kuitekeleza
kazi hiyo ndani na nje ya Chama.
Mkutano huu unafanyika wakati ambapo tupo katikati ya
kipindi tulichokabidhiwa kuongoza nchi kabla ya taifa
kwenda kwenye Uchaguzi Mkuu mwingine. Hivyo, tathmini
yake lazima izingatie ukweli huo. Tunao wajibu wa kufanya
tathmini ya kina zaidi, kwa lengo la kuanza kujiandaa
kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwakani, na Uchaguzi
Mkuu mwaka 2005.
Hiki ni kipindi cha kubadili gia
katika utendaji wetu, katika Chama na katika Serikali;
ni kipindi cha kuchaji betri zetu kwa kazi kubwa inayokuja.
Sisi ni Chama makini, tena tumekabidhiwa na Watanzania
wenzetu wajibu na dhamana kuongoza nchi. Hivyo, hatupaswi,
na hatuwezi, kufanya mambo yetu kwa kubahatisha. Tunafanya
kwa mipango, kwa ratiba, na kwa kuzingatia vipaumbele.
Na hapa tulipo, katikati ya kalenda yetu ya miaka 5
iliyopo kutoka uchaguzi mmoja hadi mwingine, ni wakati
wa kurejea kwenye Ilani yetu, tuone tuliwaahidi nini
wananchi mwaka 2000; tuone tumefika wapi katika utekelezaji
wa ahadi hizo; tuone tumekwama wapi, kwa sababu gani;
na tuone tunajiandaa vipi kukamilisha kazi hiyo kabla
ya kurudi kwa wananchi.
|
|
|
|
|
| |
|
|
|
|
|
|
|
|
|
| |
|
|
|
“Swali
langu ni lile lile: Kwa nini hatujisifu zaidi na tunawaachia
ukumbi wapinzani kutubeza?” Mwenyekiti wa CCM,
Rais Mkapa
awauliza Wajumbe wa NEC. |
|
|
|
| |
|
|
Wakati
nikifunga Mkutano Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, tarehe
31 Oktoba 2002, niliorodhesha mambo manne ambayo, kwa
maoni yangu, tunapaswa kuyapa umuhimu wa pekee. Karibu
mwaka umepita tangu wakati huo. Hivyo mniwie radhi niyarudie
kwa ufupi, ili tuone tumefanya nini hadi leo kuyashughulikia.
La kwanza, ni kuwa sisi wenyewe, viongozi na wanachama
wa CCM, tujitahidi kuelewa vizuri zaidi Sera zetu, Ilani
yetu, na Mwelekeo wa Chama chetu. Kisha tujielimishe
kuhusu kiwango cha mafanikio katika utekelezaji wake,
na sababu za mapungufu pale yanapojitokeza, pamoja na
mbinu za kushughulikia mapungufu hayo. Tukishaelewa,
twende kwa wananchi kuwaeleza mambo haya, kwa uwazi
na ukweli.
· La pili, ni kuwa lazima tukusanye nguvu za
Chama na Serikali kusukuma utekelezaji wa Ilani. Kutimiza
ahadi ni uungwana. Ni uungwana wetu ndio utawafanya
wananchi waendelee kutuamini na kutukabidhi dola ya
nchi hii. Na tuwakumbushe watumishi wa umma kuwa utekelezaji
wa Ilaniya CCM si jambo la hiari, au la kuchagua; ni
jambo la lazima na la haki.
· La tatu, ni kuwa tusionee haya ushindi wetu.
CCM ilishinda, kwa uhakika na kwa haki, kwa hiyo haina
sababu ya kusitasita kwenye kudai Ilani yake itekelezwe,
na kwenye kuhamasisha umma wa Watanzania uliotuweka
madarakani ushiriki kazi za maendeleo yao binafsi, na
ya taifa lao.
· La nne, ni kuhakikisha tunaendelea kuwa wamoja
ndani ya Chama. Migawanyiko, kwa sababu yoyote ile,
au kisingizio chochote kile, ni sumu kubwa. Tusiiachie
upenyo, na tusikubali wengine watengeneze ufa wa kupitishia
sumu yao ndani ya Chama Cha Mapinduzi.
Nasema, mwaka karibu unakwisha tangu nitoe orodha hiyo.
Je, tumefanya nini? Tufanye tathmini.
Lakini tathmini tutakayoifanya isiwe ya kulaumiana tu
– Chama kuilaumu Serikali, wala Serikali kukilaumu
Chama. Tunataka tathmini inayotambua, na kuzingatia,
kuwa CCM na Serikali zake zote mbili, ni kitu kimoja.
Tuelekeapo 2004 na 2005, nataka tuelewane kuhusu jambo
hili. CCM na Serikali zake ni watu wamoja, wenye lengo
moja, ila majukumbu mbalimbali.
Kama kweli sisi ni wamoja, tutashirikiana na tutaendelea
kupendwa na wananchi kwa umoja wetu. Lakini tukishindwa
kuonyesha umoja huo, tutadharauliwa na kupuuzwa kwa
kushindwa kutimiza matarajio ya wananchi kwetu.
Tukiwa peke yetu, kama hivi leo, tuna wajibu wa kuulizana,
kwa uwazi na ukweli, kwamba mbona wewe hujafanya hili,
au wewe mbona hujasema lile. Lakini tutawapa wananchi
matumaini zaidi tukionekana wazi mbele yao kuwa tu wamoja
– Serikali ya CCM, na CCM yenye Serikali. Chama
kina wajibu wa kufafanua na kutetea kazi za Serikali;
na Serikali nayo ina wajibu wa kufafanua na kutetea
nafasi na malengo ya Chama katika uongozi wa nchi yetu.
Kutoka kwenye Chama, Serikali imepewa Ilani na Mwelekeo.
Hili nalo napenda nilisisitize. Serikali yetu haina
dira nyingine nje ya dira tunayopewa na Chama Cha Mapinduzi.
Nasema hivyo kwa maana, nikiwa nimevaa kofia yangu ya
Urais, siwezi kukubali lawana kwa kazi ambayo Serikali
inaifanya katika kutekeleza Ilani na Mwelekeo. Kama
wapo miongoni mwetu, na kwenye uongozi wa Chama katika
ngazi zake zote, ambaye amesahau kazi na malengo tuliyopewa
na Chama, kupitia Ilani na Mwelekeo, basi namwomba akasome
tena miongozo yetu hiyo ya kazi za Serikali.
Narudia. Serikali haina mwongo-zo wake au dira yake
tofauti na Ilani na Mwelekeo. Kazi yetu ni moja tu:
kutekeleza. Tukikwama tutakuja kusema hapa, na kueleza
kwa nini. Lakini pale tunapotekeleza mliyotutuma msitu-funge
kamba. Na kwa kweli tunatazamia kuwa mtakuwa mstari
wa mbele kuwaelezea wananchi, na wana CCM wengine, kuwa
hivyo ndivyo hasa mlivyoituma Serikali kwenda kufanya.
Tunayo haki pia kutarajia Chama kiwe mwangwi wa kueneza
pembe zote sifa nzuri, na utendaji mzuri, wa Serikali
ya Chama Cha Mapinduzi. Kazi mliyotutuma ni yenu. Tukiifanya
vizuri sifa ni kwa Chama.
Na sasa nikivaa kofia yangu ya Mwenyekiti wa Chama,
ninamhimiza kila kiongozi wa CCM, kuanzia tuliomo humu
ndani, na wengine wote, tuone ni wajibu wetu wa msingi
kukumbuka kila mara Ilani inasema nini, na Mwelekeo
unasema nini, na kisha kufuatilia kwa makini utendaji
wa Serikali.
Tunahitaji kujituma zaidi ili kuelewa, kutetea na kutangaza
mafanikio ya Serikali zetu mbili; ndani ya Chama na
nje ya Chama. Kwenye Mkutano Mkuu uliopita Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar, kila moja ilitoa taarifa yake ya utendaji.
Mkutano Mkuu ukakasimu kwetu kazi ya kuchambua na kujadili
taarifa hizo, ili hatimaye zitumike kujenga hoja kwa
wananchi kwa nini tunastahili kuendelea kukabidhiwa
uongozi wa nchi hii.
Naomba mkazisome tena taarifa hizo ili mjiridhishe wenyewe
na kazi tuliyoifanya. Mafanikio hayo, na mengine ambayo
yametajwa kwenye Kikao cha Bunge la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania kilichopita, sambamba na kwenye Kikao cha
Baraza la Wawakilishi Zanzibar, yanatosha kabisa kutufanya
tutembee kifua mbele tunapoelekea 2004 na 2005.
|
|
|
| |
|
|
|
|
|
|
|
|
| |
|
|
Lakini
badala yake unasikia zaidi kelele za wapinzani, badala
ya nyimbo za ushindi za Chama Cha Mapinduzi. Tunawaachia
nafasi wapinzani kujaribu kupuuza, au kukebehi, rekodi
ya usahihi wa Sera, na umakini wa utekelezaji. Hili
si sahihi, na lazima tujirekebishe tuelekeapo kwenye
uchaguzi. Tusikubali wapinzani wajipe nafasi wasiyostahili,
nafasi kubwa kuliko yetu katika majukwaa ya kisiasa.
Maana, siasa ni mapambano ya kudumu ya kuvutia nyoyo
na fikra za wananchi, wapiga kura. Kamwe tusisahau jambo
hili. Kutetea rekodi yetu ni silaha katika uchaguzi
ujao. Na kuelewa na kisha kueleza tunafanya nini, kwa
namna gani, na mipango ijayo ikoje, nayo ni silaha.
Kwenye siasa tusione haya kujisifu, na wala tusingoje
tu kila mara wengine nje ya nchi ndio watusifu kama
ilivyo sasa.
· Uchumi wa taifa umekua kutoka ongezeko la asilimia
3.3 kwa mwaka 1997 hadi asilimia 6.2 mwaka jana; kwa
nini tusijisifu?
· Wastani wa kukua kwa uchumi barani Afrika katika
miaka 3 iliyopita ni asilimia 3.4 kwa mwaka. Wastani
wetu sisi Tanzania kwa miaka hiyo 3 ni asilimia 5.6;
kwa nini tusijisifu?
· Mfumuko wa bei ulifika chini ya asilimia 10
mwaka 1999, na tangu wakati huo unaendelea kushuka kila
mwaka, hadi kufikia chini ya asilimia 5 hivi sasa; kwa
nini tusijisifu?
· Hivi leo tunayo akiba ya fedha za kigeni kuliko
wakati wowote tangu tuwe taifa huru; kwa nini tusijisifu?
· Hivi leo washirika wetu katika maendeleo, yaani
wahisani, wana imani na Serikali yetu pengine kuliko
katika miaka mingi iliyopita. Wengi sasa wanaanza kupitishia
misaada yao moja kwa moja kwenye bajeti ya Serikali
wakiwa na uhakika kuwa hazitatumiwa isivyopaswa. Aidha,
wengi wao wametuhakikishia fedha hadi 2005. Kwa nini
tusijivune kwa kuaminiwa kiasi hicho?
· Hivi leo wawekezaji kutoka nje wanatuamini
kuliko miaka iliyopita, na ndio maana wanaendelea kuwekeza
katika nchi yetu ambayo ni miongoni mwa nchi zinazoongoza
barani Afrika kwa kuvutia mitaji. Sasa kwa nini tusijisifu?
· Nchi chache sana hadi sasa zimepewa
msamaha wa madeni kwa nchi maskini sana. Tanzania ni
mojajwapo, kwa vile tunaaminika kuwa tuko makini kupiga
vita umaskini, na kuepuka madeni makubwa mno siku zijazo.
Sasa kwa nini tusijisifu?
· Mapato ya Serikali yameongezeka mara nne katika
miaka 7 iliyopita. Ndio maana tumeweza kufuta kodi za
kezo kwa wananchi, ndio maana kasi ya kujenga barabara
na madaraja imeongezeka, na ndio maana mishahara imeongezwa.
Sasa kwa nini tunaogopa kujisifu?
· Mwaka jana sekta ya kilimo ilikuwa kwa asilimia
5; sekta ya madini kwa asilimia 15; sekta ya utalii
kwa asilimia 9.3; sekta ya viwanda kwa asilimia 8; sekta
ya ujenzi kwa asilimia 11; sekta ya mawasiliano na uchukuzi
kwa asilimia 6.4; sekta ya fedha kwa asilimia 4.8; na
nyingine nyingi zimeongezeka. Sasa kwa nini tusijisifu?
· Mauzo ya nje yameongezeka kutoka USD 543.3
mwaka 1999 hadi USD 902.5 mwaka jana, sawa na ongezeko
la asilimia 66 kwa miaka 3 tu. Sasa kwa nini hatujisifu?
· Tumeongeza bajeti ya elimu kwa asilimia 151.6
katika miaka 3 iliyopita. Uandikishaji watoto kwenye
shule za awali umeongezeka kwa asilimia 87 kwa mwaka
mmoja tu uliopita. Uandikishaji watoto darasa la kwanza
umefikia asilimia 98.6 ya watoto wa rika la elimu ya
msingi mwaka 2002, na walioko shuleni ni asilimia 80.7.
Mwaka huu, 2003, kulikuwa na ongezeko la asilimia 23
katika kuandikisha watoto darasa la kwanza. Mwaka jana
tumeongeza idadi ya shule za msingi za Serikali kwa
asilimia 4.8, na walimu kwa asilimia 5.8. Wanafunzi
wanaoingia katika Shule za Sekondari waliongezeka kwa
asilimia 11.6 mwaka jana, na idadi ya walimu wa sekondari
iliongezeka kwa asilimia 10. Kwa nini hatujisifu vya
kutosha?
Ningeweza kuendelea, na kuendelea, na kuendelea, kutaja
mafanikio, Bara na Visiwani. Lakini nawaachia Mawaziri
wa Serikali zetu mbili ambao watatoa maelezo zaidi.
Swali langu ni lile lile: kwa nini hatujisifu zaidi,
na tunawaachia ukumbi wapinzani?
Sisemi vita dhidi ya umaskini
imekwisha. Ninachosema ni kuwa takwimu hizi zinaonyesha
wazi kuwa tuko katika njia sahihi; kilichobaki ni kuongeza
kasi, maana tuna uhakika wa tuendako, na tuna uhakika
wa njia ya kupita. |
|
|
| |
|
 |
|
| |
|
Daraja
la Mto Rufiji ambalo sasa linaitwa la DARAJA
LA MKAPA ni moja ya miradi mikubwa iliyokamilika
ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM |
|
| |
|
|
Ni
muhimu pia katika kufanya tathmini ya utendaji wetu
kuzingatia mazingira tunayofanyia kazi, ndani na nje
ya nchi. Sisi wana-CCM, ambao ndio wenye Serikali, lazima
tuelewe jambo hili, tulizingatie na kisha kuwaelimisha
wengine. Bei ya kahawa au pamba inapoanguka kwenye soko
la dunia si kwa sababu ya CCM. Kauli ya nchi maskini
kama zetu ni ndogo sana, na ni kama vile haipo kabisa,
katika kupanga bei ya mazao kwenye soko la dunia. Na
siamini kipo chama kingine cha siasa nchini hapa chenye
uwezo mkubwa wa kujenga hoja ya mfumo wa haki zaidi
wa biashara duniani kuliko CCM. Tutafanya hivyo pia
kule Cancun, Mexico, ambako Mkutano wa Mawaziri wa Biashara
Duniani unaendelea hivi sasa. Kwa kushirikiana na nchi
nyingine zinazoendelea tutajenga hoja. Tatizo si kujenga
hoja. Tatizo ni utashi wa kisiasa wa wakubwa waliobuni
na wanaofaidi mfumo uliopo sasa.
Wapo watu wanaofanya mzaha na utandawazi. Wanasema huyu
Mkapa naye kazidi na mambo yake ya utandawazi. Lakini
hili si jambo la mzaha hata kidogo. Utandawazi umeweka
mbele yetu fursa, na umeweka pia mbele yetu hatari kubwa.
Kazi yetu ni kupanua uwanja wa fursa, na kuupunguza
ule wa hatari. Si kazi rahisi; lakini lazima tuifanye.
Tuendelee kulaani na kupinga mfumo wa utandawazi ambao
si wa haki. Lakini, penye fursa, kama za AGOA zinazotuwezesha
kuuza bidhaa zetu nchini Marekani kwa upendeleo maalum
utolewao na nchi hiyo kwa nchi za Kiafrika, na EBA itoayo
fursa kama hizo hizo za upendeleo tunapouza barani Ulaya,
tuzitumie kwa ukamilifu fursa hizo. Ukweli ni kuwa hivi
sasa hatuzitumii vya kutosha fursa hizo. Tunaona ni
rahisi zaidi kulalamika tu. Lazima tubadilike.
Mwisho, napenda, kama nilivyofanya kwenye kufunga Mkutano
Mkuu mwaka jana, nizungumzie umuhimu wa kupanga matumizi
ya Chama kulingana na mapato yetu. Hii ni hekima ya
kawaida tu. Tushone koti letu kulingana na kitambaa
kilichopo. La sivyo tufanye bidii kupata kitambaa zaidi.
Nilisema Oktoba mwaka jana, na leo narudia changamoto
hizi mbili.
· Kwanza, tuhakikishe kwamba kinakuwa na vyanzo
vya uhakika vya mapato yetu wenyewe ili kujinusuru na
hatari ya kuishi kwa utegemezi, au kuwa Chama cha matajiri
peke yao; na
· Pili, tupunguze matumizi, ikiwemo kwa kupitia
tena muundo wa mfumo wa Chama chetu; lakini bila kuathiri
ulazima wa kisiasa na kijamii wa kujenga utaifa, uzalendo,
na umoja.
Nimezungumza vya kutosha. Inapasa tuendelee na kikao.
Nimalizie kwa kuwakumbusha nilivyosema mwanzo: Tufanye
tathmini na tusione haya kujisifu. Na kisha, tujue tumekuja
kuchaji betri zetu kwa kazi kubwa iliyo mbele yetu.
Mwanafalsafa mmoja (Friedrich Nietzsche) aliwahi kusema,
“Ukipoteza lengo, umepoteza njia.” Na bila
shaka ukipotea njia huwezi kufika unakokusudia. Katika
kuchaji betri zetu, tukumbushane lengo letu la msingi,
nalo ni kushika dola. Lolote tufanyalo, mmoja mmoja
na kwa ujumla wetu, tusisahau lengo kuu hilo: Kushika
Dola!!
|
|
|
|
| |
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|