Ilani ya CCM Habari Mpya Historia ya TANU na ASP Kutoka Magazetini Hotuba

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JARIDA LA MKEREKETWA

Tumeachana na Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea? La hasha
 
[Na Omar R. Mapuri]
   
 
Tokea mwanzoni mwa miaka ya tisini, Tanzania imo katika mageuzi makubwa ya kisiasa, kiuchumi na kijamii ambayo yanakwenda sambamba. Mageuzi ya kisiasa yametuingiza katika mfumo wa vyama vingi vya siasa baada ya zaidi ya miaka 40 ya mfumo wa chama kimoja. Mageuzi ya kiuchumi yametutoa katika uchumi hodhi uliokuwa ukimilikiwa na dola na kutuingiza katika mfumo wa uchumi wa soko unaotoa nafasi ya ushiriki wa sekta ya binafsi. Mageuzi ya kijamii ni pamoja na kupanuka kwa uhuru wa vyombo vya habari pamoja na mambo mengine mengi ambayo aghlabu ni matokeo ya mageuzi ya kiuchumi na kisiasa.
Kama ilivyo kawaida ya mageuzi, mageuzi haya makubwa na mengi yanayokwenda sambamba yamewa-fadhaisha na hata kuwababaisha wananchi wengi
wakiwemo wana CCM. Ilivyokuwa mageuzi hayo yameletwa, yanaendeshwa na kusimamiwa na CCM, wapo wana CCM wanaojiuliza kama CCM imeachana na sera zake za msingi, hasa Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea na dira ya utekelezaji wake ambayo ni Azimio la Arusha. Wapo pia wanachama wa CCM wachache, wakiwemo hata viongozi, ambao hawajiulizi tena, bali wanaamini hasa kwamba CCM imekwishaachana na sera zake. Katika nyakati fulani wapo hata viongozi wa CCM waliosikika wakitoa kauli kama vile: “tulipokuwa tukijenga ujamaa ….” au “enzi zile za Azimio la Arusha ….” kama vile ujenzi wa ujamaa haupo tena au enzi za Azimio la Arusha zimekwisha. Yupo hata kiongozi mkubwa wa CCM aliyewahi kutamka mwanzoni mwa vuguvugu la mageuzi kwamba eti CCM haina dira. Aidha, wapo wasomi wanaojaribu kuonyesha kwamba CCM imeachana na ujamaa na kwamba sasa inaendesha sera wanazoziita za kiliberali. Zaidi ya yote, vipo hata vyama vya upinzani vilivyodiriki kujinasibu kwamba eti vyenyewe ndivyo sasa vyenye sera za ujamaa eti kuziba pengo lililoachwa na CCM iliyoutelekeza ujamaa.
 
         
     
       
“Siasa ya Ujama na Kujitegemea ipo pale pale,” Katibu Mwenezi wa CCM Taifa, Ndg. Omar R. Mapuri akiwaeleza waandishi wa habari hivi karibuni
   
 

Katika makala haya tutajaribu kusahihisha dhana hizo ambazo tunaamini kwa kiasi kikubwa ni matokeo tu ya ubabaikaji uliosababishwa na mageuzi. Tutajitahidi kuonyesha kwamba CCM haijaachana na siasa yake ya Ujamaa na Kujitegemea, bali ambacho kimekuwa kikibadilika kulingana na wakati na mazingira, ni mikakati tu ya kufikia lengo hilo kuu la muda mrefu.
UCHANGANUZI WA MANENO ”FALSAFA”, “IMANI”, “SIASA”, “SERA”, “ILANI” n.k.
Kabla ya kuitazama kwa undani siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, inafaa kwanza kuchanganua maneno ya “falsafa”, “imani”, “siasa”, “itikadi”, “sera”, “maamuzi” na “ilani” ambayo yanatumika sana katika kuielezea dhana nzima ya ujamaa na kujitegemea katika mikutadha mbali mbali.
Falsafa:
Falsafa inayosarifu dhana na nadharia za Chama Cha Mapinduzi, na nchi nzima kwa jumla ni usawa wa binadamu na mtu kuthaminiwa kwa utu wake. Falsafa hii inabeba dhana za uhuru, demokrasia, haki, udugu na amani. Falsafa hii inaashiriwa katika Ahadi ya Kwanza ya Mwanachama wa CCM isemayo: “Binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja”. Falsafa hii ndiyo pia iliyoweka misingi ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar. Katika Utangulizi wa Katiba zote mbili unapata maneno yafuatayo: “… tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayozingatia misingi ya uhuru, haki, udugu na amani.” Pia Katiba hizo zinaendelea: “…. Misingi hiyo yaweza tu kutekelezwa katika jamii yenye demokrasia …” Ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haikuvunga vunga maneno katika kuibainisha falsafa hii ya msingi. Ibara hiyo inasomeka kama ifuatavyo:-
“12. - (1) Binadamu wote huzaliwa huru, na wote ni sawa.
(2) Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.
Ibara ya 11 ya Katiba ya Zanzibar ina maneno hayo hayo.
Inathibitika kwa hivyo kwamba falsafa hii si ya CCM peke yake, bali ni ya nchi nzima. Hatujapata kusikia chama hata kimoja cha siasa kinachoipinga falsafa hii.
Imani/Siasa/Itikadi:
Ni imani ya CCM kwamba ujamaa na kujitegemea ndiyo njia pekee ya kujenga nchi ya watu walio sawa, huru na wanaoheshimiana. Kwa hivyo, hiyo ndiyo siasa au itikadi ya msingi ya CCM. Ibara ya 4 ya Katiba ya CCM inaweka bayana imani ya CCM kama ifuatavyo:-
4. CCM kinaamini kwamba:
(1) Binadamu wote ni sawa
(2) Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.
(3) Ujamaa na kujitegemea ndiyo njia pekee ya kujenga jamii ya watu walio sawa na huru
Kwa upande wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sehemu ya Utangulizi imeelezea madhumuni ya kutungwa kwa Katiba hiyo kuwa ni kujenga jamii yenye demokrasia na pia kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Tanzania inaongozwa na Serikali yenye kufuata misingi ya demokrasia na ujamaa. Maneno kama hayo yamerejewa pia katika Katiba ya Zanzibar.
Ibara ya 3(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaitangaza rasmi Tanzania kuwa ni nchi ya kidemokrasia na ya kijamaa, yenye kufuata mfumo wa vyama vingi vya siasa. Ibara ya 8(1) ya Katiba ya Zanzibar nayo imeitangaza hivyo hivyo Zanzibar isipokuwa tu imetumia maneno “haki za kijamii” badala ya neno “ujamaa”. Hata hivyo madhumuni ni yale yale.
Tukizilinganisha Katiba za nchi na ile ya CCM katika muktadha wa siasa ya ujamaa na kujitegemea, inadhihirika kwamba neno “kujitegemea” halikutumika katika Katiba za nchi. Tafsiri yetu ya tofauti hiyo ni kwamba katika siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, ncha ya ujamaa ni ya nchi nzima lakini ncha ya kujitegemea inatoa fursa kwa vyama vya siasa kutofautiana kwa sera. Ingawa kuna vyama vya upinzani ambavyo husikika vikitaka kipengele cha Ujamaa kiondoshwe katika Katiba ya nchi, lakini ukizitazama kwa undani sera za vyama hivyo, utagundua kwamba zimejengwa juu ya msingi huo huo wa ujamaa. Na vipo vyama ambavyo hujinasibu kwa wananchi kwamba eti ndivyo vyenye uwezo mkubwa zaidi wa kuzitekeleza sera za CCM kuliko CCM yenyewe. Vyama kama hivyo vinakiri usahihi wa siasa ya Ujamaa lakini vinadai kuwa eti CCM haina uwezo wa kuitekeleza. Lakini zaidi ya yote, hatujapata kusikia chama cho chote cha siasa nchini Tanzania kinachojitambulisha na ubepari.
Sera na Dira:
Baada ya kubainisha siasa yake ya Ujamaa na Kujitegemea iliyojengwa juu ya msingi wa falsafa ya usawa wa binadamu na mtu kuthaminiwa kwa utu wake, TANU mnamo mwaka wa 1967 ilipitisha Azimio la Arusha lililoandaa mazingira na kuweka dira ya utekelezaji wa siasa hiyo. Sera ni mkakati wa utekelezaji wa siasa kwa kipindi fulani kulingana na uchambuzi wa dira uliofanywa kwa ajili ya kipindi hicho. Sera huweza kubadilika kulingana na mahitaji ya wakati. Kwa hivyo, wakati siasa ya Ujamaa na Kujitegemea ni ya kudumu na Azimio la Arusha kama dira yake ya utekelezaji nalo ni la kudumu kwa kiasi fulani, sera na mikakati ya utekelezaji huweza kubadilika kila baada ya muda, kulingana na mabadiliko ya mahitaji ya wakati. Na kweli uzoefu katika TANU na ASP na baadaye CCM unaonyesha kwamba baada ya kila kipindi cha wastani wa miaka 10, Chama kimekuwa kikitathmini utekelezaji wa siasa ya Chama na kuzitazama upya sera zake za msingi kwa lengo la kuzifanya zikidhi mahitaji ya wakati. Baada ya kufanya mapitio hayo Chama huja ama na mwongozo unaojikita katika ufafanuzi na kuyawekea mkazo maeneo fulani au huja na sera mpya kabisa, lakini lengo kuu likiwa ni lile lile la kutekeleza siasa ya Ujamaa na Kujitegemea kwa kuzingatia misingi ya Azimio la Arusha. Ndiyo maana katika kipindi cha toka 1971 hadi sasa, CCM imetoa nyaraka nne zifuatazo za kisera za msingi:-
(1) Mwongozo wa TANU wa 1971 ambao ulijenga hamasa ya utekelezaji wa Azimio la Arusha.
(2) Mwongozo wa CCM wa 1981 ambao ulijielekeza katika kukabiliana na mmong’onyoko wa maadili uliokuwa unasababishwa na hali ngumu ya uchumi iliyochangiwa na vita vya nduli Idi Amin.
(3) Mwelekeo wa Sera za CCM katika Miaka ya Tisini uliozingatia haja ya kujihami na taathira za upepo wa mageuzi makubwa ya kiuchumi na kisiasa uliokuwa ukivuma Duniani na kuziangusha dola kubwa za kijamaa za Ulaya ya Mashariki likiwemo la Urusi yenyewe ya Kisovieti.
(4) Mwelekeo wa Sera za CCM katika Miaka ya 2000-2010 unaozingatia zaidi suala la matumizi ya teknolojia (modenaizesheni) katika ujenzi wa uchumi wa kisasa.
Kwa jumla, chimbuko la sera zote za CCM ni Azimio la Arusha na zinapoandaliwa, yanazingatiwa pia malengo na madhumuni ya CCM yaliyobainishwa katika ibara ya 5 ya Katiba ya CCM.

 
         
       
   
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere katika “Kujitawala ni Kujitegemea” aliyaelezea ifuatavyo mahusiano baina ya Azimio la Arusha na Sera za Chama:-
Azimio la Arusha ndilo linaloeleza itikadi ya chama chetu. Ndiyo kauli kuu ya lengo letu na misingi yetu; ndilo msingi wa maamuzi yote ya sera za Chama na Serikali.
Aidha Mwalimu alitambua haja ya kupitia upya sera kila mara na kurekebisha Azimio. Alisema tena katika “Kujitawala ni Kujitegemea:-
Kila miaka inavyopita, kauli yo yote muhimu kupitiwa mara kwa mara kuona kama misingi yake bado inahitajiwa katika mazingira mapya … Hata mimi nakubali kwamba (Azimio la Arusha) linahitaji marekebisho.
Maneno hayo yanatosha kuwasuta wale wanaodai kwamba eti Mwalimu hakutaka mabadiliko ya Azimio na Sera.

Maamuzi:
Ndani ya utekelezaji wa sera ya msingi, Chama huweza kupitisha maamuzi yenye lengo la kutoa msukumo wa utekelezaji wa jambo fulani mahsusi au kukabili tatizo fulani la utekelezaji. Ni kwa msingi huo ndio TANU na baadaye CCM ilipitisha maamuzi mengi yakiwemo yafuatayo:-
(1) Siasa ni kilimo (Azimio la Iringa) (1972) kwa lengo la kutoa msukumo katika suala zima la kilimo.
(2) Mpango wa Elimu kwa Wote (UPE) (Azimio la Musoma), (1974) uliotoa msukumo wa kuharakisha kufikisha elimu kwa wote ikiwa ni pamoja na suala la elimu ya watu wazima.
(3) Mtu ni Afya (1976): Kutoa msukumo kwa sera ya kinga kuliko tiba.
(4) Mpango wa Kujihami Kiuchumi (1980/81) ili kukabiliana na hali ngumu ya uchumi wa nchi.
(5) Maamuzi ya Zanzibar (1991) ambayo yaliwaondolea wanachama wa kawaida wa CCM masharti ya uongozi yaliyoainishwa katika Azimio la Arusha. Maamuzi hayo yalikuwa na lengo la kuwawezesha wanachama wa CCM kushiriki katika harakati za kiuchumi katika mazingira mapya yaliyokuwa yanaingia ya uchumi wa soko. Masharti ya uongozi yalibaki kwa viongozi tu kama ilivyokuwa imekusudiwa katika Azimio la Arusha.
Ilani:
Kama ilivyokwishabainishwa, sera za msingi huchukua upeo wa muda mrefu kidogo, na kwa uzoefu wa CCM, ni kama miaka 10 hivi. Ndani ya kipindi hicho, Chama huchambua sera na kujipangia malengo ya utekelezaji kwa vipindi vifupi vifupi, aghlabu vya miaka mitano mitano. Hapo ndipo tunapopata ilani za uchaguzi ambazo huwasilishwa kwa wananchi kwa ajili ya kuombea kura katika chaguzi za dola ambazo hufanywa kila baada ya miaka mitano.
Baada ya uchanganuzi huo wa maneno “falsafa”, “siasa”, “itikadi” “sera”, “maamuzi” na “ilani” kama yanavyotumika katika msamiati wa CCM, imedhihirika kwamba falsafa na siasa ni vitu vya kudumu, au ni malengo ya muda mrefu, lakini sera, maamuzi na ilani ni vitu vinavyobadilika kila baada ya muda. Na hapa ndipo penye siri ya mafanikio ya CCM. Ingawa CCM ni chama kikongwe, lakini kila baada ya muda hujirekebisha kwa mujibu wa mazingira ya wakati, lakini bila ya kupoteza lengo. Kwa ufupi, CCM inafuata kanuni ya mwezi ambao katika mzunguko wake huanza na uchanga (ukiwa na umbo la hilali), ukafikia upevu (ukiwa na umbo la sahani) na kurejea tena uchanga ambapo unakuwa tunu tena. Ni kutokana na kanuni hiyo ndiyo maana wananchi hawaichoki CCM pamoja na ukongwe wake, kwani wakati wote inawaletea matumaini mapya.
UJAMAA NA KUJITEGEMEA
KAMA SIASA YA CHAMA:
Kama siasa ya Chama, Ujamaa na Kujitegemea ni lengo la kudumu. Ni kwa msingi huo ndiyo tunasema kwamba Chama Cha Mapinduzi bado kabisa hakijaachana na siasa hiyo. Katiba na sera za CCM zinabainisha wazi wazi msimamo huo kama ilivyokwishaelezewa. Baada ya kuuelewa msimamo huo, ni muhimu pia kuelewa tunapozungumzia Ujamaa na Kujitegemea tunakusudia nini. Tutajaribu kwa kutumia lugha nyepesi kabisa, kutoa ufafanuzi huo katika sehemu hii ya makala haya. Kama inavyojieleza yenyewe, siasa ya Ujamaa na Kujitegemea ina ncha mbili, yaani ya Ujamaa na ile ya Kujitegemea. Katika Azimio la Arusha, umefanywa uchanganuzi wa kina ambapo Sehemu ya Pili ya Azimio hilo inachambua Siasa ya Ujamaa na Sehemu ya Tatu inachambua Siasa ya Kujitegemea. Kwa maneno mengine siasa yetu hii ni siasa mbili ndani ya moja. Nasi kwa ufupi kabisa tutafanya uchanganuzi kama huo.
Siasa ya Ujamaa:
Siasa ya Ujamaa imechambuliwa na wanafalsafa wengi wakubwa waDunia hii wakiongozwa na Karl Marx na Vladmir Lenin. Pia imechambuliwa kwa kina na Mwalimu Julius K. Nyerere kwa mazingira ya Tanzania katika vitabu vyake mbali mbali, ambapo majumuisho yake yaliwekwa katika Azimio la Arusha. Sisi katika makala haya hatukusudii kurejea uchambuzi wa kifalsafa bali tu tunajaribu kumwelezea mwananchi wa kawaida maana pana na nyepesi inayokusudiwa katika Siasa ya Ujamaa. Kwetu sisi Ujamaa maana yake ni kugawana utajiri wa nchi kwa usawa na kwa haki katika misingi ya kuheshimiana. Jitihada zetu za kiutekelezaji katika kufikia lengo hilo kama zinavyoongozwa na Azimio la Arusha zimekuwa zikichukua sura za kusambaza huduma za jamii (elimu, afya, maji n.k.) kwa wote, kujenga misingi ya fursa sawa za kujiendeleza, kuondoa unyonyaji, kupiga vita kila aina ya ubaguzi na dharau, kuwatetea wanyonge na kuwasaidia kujikwamua na kadhalika. Uamuzi wa kuanzisha vijiji vya ujamaa katika miaka ya sabini ulikuwa na lengo la kurahisisha utekelezaji wa juhudi hizi. Pamoja na matatizo ya hapa na pale ya utekelezaji, tunaamini Watanzania walio wengi hasa wanyonge, bado wanapenda kufikiwa kwa malengo hayo. Ndiyo maana tunasema Siasa ya Ujamaa ni ya kudumu.
Kugawana au kusambaza kwa wote utajiri wa nchi (si kwa kugawana fedha bali kwa kuhakikisha upatikanaji wa huduma za kijamii kwa wote) ni sura moja tu ya Ujamaa. Lakini pia kuna sura ya pili ambayo ni ya kuuchuma huo utajiri wenyewe wa kugawana. Katika Azimio la Arusha, unafafanuliwa utaratibu wa kuchuma utajiri bila ya kunyonyana. Mkakati uliowekwa ni wa njia kuu za uchumi wa nchi kuwekwa chini ya wakulima na wafanyakazi kupitia vyombo vya Serikali
Siasa ya Kujitegemea:
Siasa ya Kujitegemea imechambuliwa kwa kina katika Sehemu ya Tatu ya Azimio la Arusha. Siasa hii inajikita katika kuleta maendeleo ya kweli ya nchi na ya wananchi wenyewe hasa wanyonge. Hoja inajengwa kwamba huwezi kuzungumzia maendeleo ya kweli kama maendeleo hayo ni ya vitu tu na si ya watu wenyewe na kama maendeleo hayo yamejengwa juu ya msingi wa utegemezi wa fadhila za nje. Inasisitizwa kwamba fedha si msingi wa maendeleo bali ni matokeo ya maendeleo. Kwa hivyo mkakati unaotiliwa mkazo ni wa kujituma katika kujiletea maendeleo bila ya kusubiri fedha kwanza au misaada na mikopo kutoka nje. Vitu hivyo kama vitapatikana vije tu kusaidia juhudi zetu za kujitegemea na kamwe visiruhusiwe kuhatarisha uhuru wetu.
Kwa mnasaba huo, Siasa ya Kujitegemea inasisitiza kwamba: Maendeleo ya nchi huletwa na watu, hayaletwi na fedha. Fedha ni matokeo siyo msingi wa maendeleo. Ili tuendelee twahitaji vitu vinne: (i) Watu; (ii) Ardhi; (iii) Siasa safi na (iv) Uongozi bora. Kwa kuzingatia ukweli kwamba nchi yetu ina watu wengi na eneo kubwa la ardhi, mkakati wa siasa ya kujitegemea unabainisha kwamba maendeleo yataletwa na kilimo na hivyo pia unamjali zaidi mkulima vijijini.
Siasa ya Kujitegemea imebainisha masharti mawili ya maendeleo. Masharti hayo ni Juhudi na Maarifa. Juhudi inaashiria kufanya kazi kwa kujituma na Maarifa ni kiashirio cha matumizi ya utaalamu na teknolojia kwa lengo la kuziongezea tija juhudi.
Kwa jumla, mtu hahitaji utafiti wa kina kubaini kwamba karibu yote yaliyoelezewa kuhusiana na Siasa ya Kujitegemea yalikuwa na ukweli mwaka 1967 na bado yana ukweli hadi leo. Aidha, yote hayo yanaendelea kupendwa na Watanzania waliowengi ambao siyo tu wameyakubali, bali pia wanajitahidi kuyatekeleza. Kwa mfano Watanzania pamoja na unyonge wao, hawakubali kuonewa wala kunyanyaswa. Pia, Watanzania wamejiletea maendeleo mengi (shule, zahanati, visima, njia, maji n.k.) kwa kujitegemea bila ya kusubiri fedha. Na zaidi ya yote, Watanzania wanajituma kwa bidii kubwa. Kwa kuzingatia ukweli huo, mtu hapaswi kupata taabu sana kuelewa kwa nini Siasa ya Kujitegemea inaendelea kuwa siasa ya CCM.
Kama ilivyo katika siasa ya ujamaa, bila shaka yamejitokeza hapa na pale matatizo ya kiutekelezaji. Yapo matatizo yaliyo nje ya uwezo wetu kama vile matatizo ya kiuchumi ya dunia ambayo yalipotukumba na sisi yaliathiri utekelezaji wetu. Lakini pia yapo matatizo yaliyotokana na kasoro zetu wenyewe kama vile kuweka mkazo mdogo katika maarifa na badala yake kukazania tu juhudi ambapo matokeo yake yamekuwa ni tija ndogo katika uzalishaji hasa katika kilimo. Maeneo kama haya ya matatizo na kasoro ndiyo yanayotoa fursa ya kuzipitia upya baadhi ya sera za Chama kama tutakavyobainisha baadaye.
Mwandishi wa Makala hii ni Katibu Mwenezi wa CCM Taifa, Ndugu Omar R. Mapuri ambaye katika toleo lijalo la jarida hili atamalizia Makala yake kwa kueleza juu ya:-
Baadhi ya maeneo yaliyohitaji marekebisho ya Sera
Shabaha ya Ujamaa katika kipindi
hiki.
Masharti na miiko ya Uanachama