Ilani ya CCM Habari Mpya Historia ya TANU na ASP Kutoka Magazetini Hotuba

 

 

 

 

 

 

 

 

 

JARIDA LA MKEREKETWA

 
  Sio elimu, sio mali, sio dini; bali ni ...        
Na Muhammed Seif Khatib
 
 

Nnachojivunia. Ni kipi? Sio elimu. Sio utajiri. Sio dini. Sio kabila. Kwangu mimi, vyote sio muhimu. Kwa nini? Twahibu!, vyote ni pambo tu. Kama ni mali; mali yako. Wachache huipata. Wengi ni mafukara. Wachache wao hupata kihalali. Wengi wao chori chori! Ukiwa na elimu ni mali yako. Si yetu sote. Kumpa mwingine ni kupenda tu. Ni wewe ujinga utakayeutoroka. Naam! Nayo dini ni imani. Imani hutofautiana. Wapo wasioamini cho chote. Wao, wapo wapo tu! Huko paradise hao watakaokwenda hadi leo hawajijui! Kufika huko nako, sio kwa leo au kesho. Safari ni ndefu! Kujivunia kabila, ni ubozi na ubahaluli. Zinauzwa wapi kabila? Si unaikuta tu. Asokabila sio mtu?
Nnachojivunia nini? Uwanachama wa chama changu: Chama cha siasa chenye historia. Chama kilichofanya matendo makubwa Afrika. Ni chama hiki kilichotoka ndani ya mifupa na damu ya vyama vya ukombozi. Vipi hivyo, ni ASP na TANU. Naam! Vyama vya Waafrika. Vyama vya ukombozi. Vyama vilivyoona mbali. Vyama vya Nyerere na Karume. Viongozi waanzilishi. Viongozi waasisi wa taifa letu. Vyama vyao viliunganisha Waafrika. Viliwahamasisha. Vikawaamsha katika maruirui ya kutawaliwa. Walilemazwa ili kujiona sio watu kama watu. Waliamini kuwa wao ni watwana na wajakazi tu. Utu wao ulidhalilishwa! ASP na TANU, waasisi wa uanachama wangu, vikaweka mikakati ya kudai haki za Waafrika. Vikakataa katu kutawaliwa. Vikadai uhuru wa Tanganyika. Vikagombania uhuru wa Tanganyika. Vikagombania uhuru wa Zanzibar. Vilimkataa mkoloni. Vilimkataa Sultani. Mapambano yakapamba moto. Wakoloni wakasalimu amri Tanganyika. Masultani wakatimuliwa huko Zanzibar. Nchi zetu zikawa huru. Uhuru wa Mwafrika. Uhuru wa mtu mweusi. Hiki nnajivunia.
Nnachojivunia. Ni uwanachama wangu. Chama hiki kilichorithi historia hii ya ukombozi. Bila historia hii bado leo tungekuwa watwana na wajakazi katika nchi yetu ya asili. Naionea fahari historia hiyo. Nnachojivunia uwanachama wangu wa Chama Cha Mapinduzi. Chama kilichorithi heshima ya kuwa mkombozi. Hakuna chama kingine kinachoweza kujinasibisha na hilo. Huo ni ukweli. Hiyo nayo ni hoja nzito. Nnachojivunia kuwa mwanachama wa chama kikongwe. Sio ukongwe na kuishiwa au kukongoroka! La hasha. Ukongwe wenye busara na hekima. Chama kizoefu katika kuendesha nchi. Chama kiongozi. Chama kinachoongoza na vingine vinajikongoja! Chama kilichoonyesha na kubainisha umahiri wake. Kimeunganisha umma wa Tanzania kuwa kitu kimoja. Hakuna ufa wala mpasuko ndani ya Taifa. Kimefanikiwa kujenga umoja na utangamano wa kweli. Macho yanachukia kuona damu inamwagika ya binadamu! Tumezoea kununia mfarakano. Ni mfarakano wa dini, kabila ama rangi. Amani na upendo ni chaguo la watu wa nchi hii. Nnachojivunia mafanikio hayo yaloletwa na chama changu.
Nnachojivunia kuwepo kwa umoja thabiti wa kitaifa. Umoja wenye kukumbatisha makabila yote, dini zote, jinsia zote na maeneo yote. Umoja wa Waafrika wa nchi zetu mbili walioungana miaka arobaini iliyopita. Ni umoja wa Waafrika wa Tanganyika na Zanzibar. Lakini budi ifahamike umoja huo ulianza mwaka 1957. Ni pale African Association ya Zanzibar na Shiraz Association zilipounda Afro-shirazi Party. Mshikamano huo ukaimarika na kuongoza Mapinduzi halali ya mwaka 1964. Umoja huo ni wa kidugu na kihistoria. Kuuvunja itakuwa ni kosa kubwa. Nnajivunia kuwa chama changu kimerithi na kuendeleza umoja huo! Chama kipi kingine cha siasa nchini chenye historia ya kuunganisha umma wa Tanzania na kusimamia kwa dhati umoja huu? Hakuna zaidi ya chama changu. Hivyo budi nnajivunia hili.
Nnajivunia uhusiano mzuri uliojengwa na chama changu kati ya vyombo vya usalama ikiwemo Jeshi, Polisi na Usalama wa Taifa! Hili haliji wenyewe. Ni kazi ya busara na hekima iliyojengwa. Raia wanaheshimiwa na vyombo vinaheshimiwa. Utaifa unapewa umbele. Mipaka na majukumu ya kazi hayaingiliani. Uadilifu unapewa kipaumbele. Hakuna mfarakano. Hili katika nchi nyingine haliwezekani. Nnajivunia ufanisi wa chama changu katika kujenga kuaminiana huku katai ya vyombo vya usalama raia na vyombo vingine vikiwemo Serikali, Bunge na Mahakama!
Nnachojivunia chama changu kwa sera sahihi zinazokubalika na kutekelezeka! Sera zenye uhalisi wa mambo. Hazibuniwi kuwalaghai watu, la hasha! Hazibuniwi kufurahisha watu tu! Ila hilo. Zinabuniwa kuondolewa watu umasikini. Zinabuniwa kuwaletea watu maendeleo. Ni sera zinazosimamiwa vizuri na Serikali zetu. Zinawekewa mikakati ili zilete tija na fanaka. Ufanisi wa utekelezaji huo katika ngazi zote. Kila mwanachama miongoni mwetu aangalie kitongoji na kijijini pake nini kimetekelezwa. Hakuna shule iliyojengwa au kukarabatiwa? Nyumba za walimu, vyoo na kadhalika zimejengwa? Hakuna zahanati mpya? Hakuna soko au gulio? Hakuna kuboreka kwa huduma za madawa za mahospitali, huduma za wakunga na watoto? Mwanachama wa CCM kama mimi anayejivunia chama chake lazima atajivunia ufanisi wa utekelezaji wa sera zake. Yapo ya kusemea kifua mbele katika kitongoji au kijiji. Tena utayasemea kwa uhakika na mifano. Ikiwezekana utoe takwimu na gharama zote. Si hivyo tu ipo miradi katika kata, tarafa, wilaya na hata mkoa. Lakini ukiweza unaweza kuisemea miradi ya kitaifa kama ya barabara, madaraja, umeme, gesi, nyumba, hospitali na kadha wa kadha. Lakini sio lazima kama hauelewi.
Mimi Nnachojivunia, umahiri wa chama changu katika utendaji wake na uongozaji wake. Taifa hili linajizolea sifa kemkem duniani kote. Hilo wewe hujivunii? Mimi nnajivunia. Tujivuniye.