KAMATI KUU YA CCM YAIPONGEZA SMZ NA RAIS KARUME KWA KUFANIKISHA SHEREHE ZA MIAKA 40 YA MAPINDUZI
Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imeipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuandaa na kufanikisha sherehe kabambe za kuadhimisha miaka 40 ya Mapinduzi ya Zanzibar ambazo zilifikia kilele chake Januari 12, mwaka huu.
Aidha, Kamati Kuu ya CCM imetoa pongezi maalum kwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Amani Abeid
Amani Karume kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa siku ya kilele cha sherehe hizo
zilizofanyika katika Uwanja wa Amani, Zanzibar ambayo ilielezea kwa kina
mafanikio ya Mapinduzi na juhudi zinazofanywa na Serikali kuijenga Zanzibar.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Dar
es Salaam leo na Katibu Mwenezi wa CCM Taifa, Ndugu Omar R. Mapuri ilisema
kwamba pongezi hizo zilitolewa katika siku ya kwanza ya kikao cha siku tatu cha
Kamati Kuu ya CCM ambayo inakutana chini ya Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Rais
Benjamin William Mkapa.
Ndugu Mapuri alisema kwamba Kamati Kuu ya CCM pia
iliwapongeza viongozi wa Chama na Serikali wa Tanzania Zanzibar kwa
kuwahamasisha na kuwashirikisha wananchi, bila kujali tofauti zao za kisiasa
kushiriki katika sherehe za Mapinduzi ambayo ndiyo yaliyoikomboa Zanzibar
kutoka katika makucha ya wakoloni wa Kiingereza na utawala wa Masulani walowezi
tarehe 12 Januari 1964.
Wanachama wa CCM, wakereketwa, wana-maskani, wapenzi
wa CCM na wananchi kwa ujumla pia walipongezwa kwa wingi ambao haujawahi
kuonekana kwa muda mrefu katika Uwanja wa Amani siku ya kilele cha sherehe.
Kamati Kuu ya CCM imesema kwamba itaendelea
kuuthamini na kuuenzi mchango mkubwa wa mashujaa wa Mapinduzi ya Zanzibar chini
ya uongozi thabiti wa Rais wa Chama cha Afro-Shirazi na Rais wa Kwanza wa
Zanzibar huru, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, ambao walijitoa mhanga wa
maisha yao kwa ajili ya uhuru wa kweli wa Wazanzibar.
Kamati Kuu ilisisitiza kwamba CCM ina fahari kubwa
kuona kwamba ASP na hatimaye CCM baada ya kuungana na TANU imeweza kuyalinda,
kuyaendeleza na kuyadumisha Mapinduzi ya Zanzibar hadi kutimiza miaka 40 sasa
na kuyawekea msingi wa kuyadumisha milele.
Kutokana na hali hii, Kamati Kuu ya CCM imesisitiza
tena kwamba kauli mbiu za MAPINDUZI DAIMA iendelee kutumika kama kielelezo cha
dhamira ya kweli ya kuyadumisha Mapinduzi hayo na matunda yake ambayo kila
mzalendo wa kweli wa Zanzibar na Tanzania nzima anapaswa kujivunia.