CHAMA CHA MAPINDUZI

 

OFISI  NDOGO YA MAKAO MAKUU  S.L.P. 9151 DAR ES SALAAM F2180108


Barua zote zipelekwe kwa Katibu Mkuu                        Fax: 255-022-2185245; 022-2184580; 022-2183275

 

Kumb. Na.      

Tarehe       

 


KIKAO CHA KAMATI KUU YA HALMASHAURI KUU YA

TAIFA YA CCM CHA TAREHE 19-20 MACHI, 2004,

 DAR ES SALAAM

 

1.       Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi ilifanya kikao chake cha kawaida cha siku mbili tarehe 19-20 Machi, 2004 mjini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake, Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa.  Kama kawaida, Kamati Kuu ilijadili mambo mbali mbali yaliyokuwamo katika agenda iliyowasilishwa kwake na Sekretarieti ya Chama na kuyatolea maamuzi na maelekezo.

 

2.       Awali ya yote, Kamati Kuu iliwapongeza na kuwapokea wajumbe wake wawili wapya wanaoingia kwa nyadhifa zao za Uwenyekiti wa Jumuiya za CCM walizozipata kwa kuchaguliwa hivi karibuni.  Wajumbe hao wapya ni Ndugu Emmanuel Nchimbi, Mwenyekiti wa UVCCM na Ndugu Abioud Maregesi, Mwenyekiti wa Jumuiya ya WAZAZI.  Ilimpongeza pia Mheshimiwa Getrude Mongella (Mb.) kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Kwanza wa Bunge la Afrika.

 

3.       Kamati Kuu pia ilitoa Tamko la kulaani vitendo vya vitisho vinavyofanywa huko Zanzibar dhidi ya Watanzania wenye asili ya Bara wanaoishi huko.

 


4.              Ililaani pia vitendo vya uvunjaji wa amani vinavyofanywa huko huko Zanzibar kwa kutumia kisingizio cha dini.  Kamati Kuu imezitaka Serikali zote mbili zividhibiti vitendo hivyo kwa manufaa ya amani na utulivu wa nchi.

 

5.       Aidha, katika kikao chake hicho, Kamati Kuu imeamua kushiriki kikamilifu katika chaguzi ndogo za:-


 

          (a)     Ubunge - Jimbo la Bariadi Mashariki, na

                              (b)     Udiwani - katika jumla ya Kata zote 20 zitakazogombewa katika mikoa ya Lindi (Kata 1), Mbeya (Kata 2), Tabora (Kata 1), Tanga (Kata 1), Mwanza (Kata 1), Shinyanga (Kata 8), Kilimanjaro (Kata 5) na Kagera (Kata 1).

 

CCM imepania na ina uhakika wa kupata ushindi mkubwa katika chaguzi zote hizo zinazotarajiwa kufanyika tarehe 30 Mei, 2004.  Kamati Kuu imetoa wito kwa wananchi wote wanaotimiza masharti, wa Jimbo la Bariadi Mashariki na wa Kata zote zitakazofanya uchaguzi, wajitokeze kwa wingi kuanzia tarehe 21 Machi hadi 10 Aprili 2004 kujiandikisha kupiga kura.

 

6.       Kamati Kuu pia imethibitisha uamuzi uliofanywa na uongozi wa Chama wa Mkoa wa Kagera wa kumvua uanachama wa CCM, Ndugu Hassan Milanga, aliyekuwa Diwani na Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Muleba, baada ya kuridhika kwamba amepungukiwa na sifa za uanachama.

 

7.       Aidha, Kamati Kuu imeelekeza kwamba uandaliwe utaratibu wa kuieneza dhana ya utandawazi ndani ya mfumo mzima wa Chama Cha Mapinduzi.  Hii inafuatia hatua ya Mwenyekiti Mwenza wa Tume ya Kimataifa kuhusu Masuala ya Kijamii katika Utandawazi, Mheshimiwa Rais Benjamin Mkapa kukikabidhi Chama Cha Mapinduzi nakala za Ripoti ya Tume hiyo kama alivyofanya kwa vyama vingine vya Siasa mara tu baada ya kuizindua hapa nchini tarehe 16 Machi, 2004, katika Hoteli ya Royal Palm, Mjini Dar es Salaam.

 

                              Omar R. Mapuri (Mb.),

KATIBU MWENEZI WA CCM TAIFA

21/03/2004