KANUNI ZA UCHAGUZI WA CCM NA KANUNI ZA UTEUZI WA WAGOMBEA WA CCM KATIKA VYOMBO VYA DOLA

 

Katika kikao chake cha tarehe 15-16/02/2005, Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM iliyokutana mjini Dodoma chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Benjamin William Mkapa imezifanyia marekebisho Kanuni za Uchaguzi wa CCM na Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM katika Vyombo vya Dola.

 

Kuhusu Kanuni za Uchaguzi wa CCM, marekebisho makubwa yaliyofanywa yapo katika maeneo makuu yafuatayo:-

 

1.      Utaratibu wa kupiga kura

 

          Katika chaguzi za ngazi zote za CCM, upigaji kura utaendelea kuwa wa siri, lakini sasa litatengwa eneo wazi kwa ajili ya kupigia kura badala mtu kupiga kura pale pale alipokaa.  Lengo la utaratibu huu ni kuondoa uwezekano wa majirani kushawishiana wakati wa kupiga kura.

         

2.      Uteuzi wa Wagombea wa Ngazi ya Mtaa na Kijiji Wanaoomba kushika Nafasi za Muda Wote Zaidi ya Moja

         

Katika hali ya kawaida, mgombea hatakiwi kuomba nafasi ya muda wote kama tayari anayo nyigine ya aina hiyo, isipokuwa kama Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa itaruhusu kwa mazingatio maalumu.  Hata hivyo, sasa Kamati Kuu imeruhusiwa kukasimu madaraka yake hayo kwa Kamati za Siasa za Mikoa kwa nafasi ya ngazi ya Mtaa/Kijiji.

 

3.     Ushughulikiaji wa Malalamiko ya Uchaguzi

 

Kabla ya marekebisho,  Kanuni zilitoa utaratibu wa kushughulikia malalamiko kwa kipindi cha baada ya uchaguzi tu.  Marekebisho sasa yameweka pia utaratibu kwa ajili ya kipindi cha kabla na baada ya Uchaguzi.  Utaratibu huu utawezesha kufuatilia nyendo za wagombea na ikibidi kuchukua hatua zipasazo katika kipindi hicho hicho bila kusubiri uchaguzi kumalizika.  Kamati za Siasa za ngazi husika na Kamati Kuu kwa ngazi ya Taifa ndizo  zitakazokuwa Mamlaka za Udhibiti.  Hata hivyo, kwa chaguzi zinazofanywa na Mkutano Mkuu, Halmashauri Kuu ya Taifa ndicho kitakachokuwa chombo cha udhibiti.

 

4.     Vitendo Ambavyo ni Makosa Katika Uchaguzi

 

Miiko mingi tayari imeorodheshwa katika Kanuni za sasa.  Lakini marekebisho yamebainisha vitendo vya rushwa kuwa ni kosa kubwa ambalo adhabu yake ni kufutiwa uteuzi.  Makosa mengine yaliyoongezwa kwa msisitizo katika Kanuni ya Uchaguzi ambayo tayari yamo katika Kanuni za Maadili ni pamoja na matumizi ya mabango na vipeperushi kinyume cha utaratibu uliowekwa na Chama, kampeni chafu, vurugu za wapambe au wapiga debe, matusi na upotoshaji wa makusudi wa sifa za wagombea wengine wanaoshindana nao.

 

5.     Marufuku Kampeni Siku ya Uchaguzi

 

Kuanzia sasa, siku ya uchaguzi itakuwa ni ya uchaguzi tu.  Aina yoyote ya kampeni haitoruhusiwa siku hiyo.

 

Kwa upande wa  Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM Katika Chaguzi za Vyombo vya Dola, yamefanywa marekebisho katika maeneo makuu yafuatayo:-

 

1.     Tathmini za Wabunge, Wawakilishi na Madiwani Waliopo

 

Sasa, karibu na Uchaguzi Mkuu, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani waliopo watatathminiwa na Chama kwa utaratibu utakaowashirikisha na wao wenyewe.  Tathmini hizo zitasaidia vikao husika vya uteuzi kama mhusika ateuliwe tena au la.

 

2.     Kura za Maoni Kupigwa Katika Mikutano Mikuu ya Jimbo kwa Wabunge na Wawakilishi na Kata/Wadi kwa Madiwani

 

        Marekebisho ya Kanuni yanaondoa utaratibu wa kura za maoni za kuhama hama na badala yake kuzihamishia kwenye Mkutano Mkuu mmoja tu.  Wagombea Ubunge/Uwakilishi watapigiwa kura za maoni na Mkutano Mkuu wa Jimbo na wagombea Udiwani watapigiwa kura za maoni katika Mkutano Mkuu wa Kata/Wadi.

 

3.     Kuondoa Utata Kuhusu Kutangaza Nia ya Kugombea

 

Kabla ya marekebisho, Kanuni zilipiga marufuku kampeni kabla ya kipindi kilichowekwa rasmi ambacho aghalabu ni baada ya kuchukua fomu.  Lakini zilikuwa kimya kuhusu kipindi mwanachama anachoweza kutangaza nia yake ya kutaka kugombea.  Marekebisho sasa yameondoa utata huo kwa kuruhusu mtu kutangaza wakati

wowote apendao nia yake ya kugombea, lakini marufuku ya kampeni kabla ya muda yanaendelea na yamesisitizwa.

 

4.     Udhamini wa Wagombea Urais

 

Kanuni zinapiga marufuku Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa na Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa kuwadhamini wagombea Urais kwa tiketi ya CCM.  Hii ni kwa sababu wao tayari wana majukwaa ya maamuzi na kuwapigia kura wagombea, na hivyo ni vyema kuwaachia wanachama wengine fursa ya kushiriki katika mchakato wa uteuzi wa wagombea hao.