DK. A. KIGODA AELEZEA MAFANIKIO MAKUBWA YA UBINAFSISHAJI NCHINI TANZANIA
Mheshimiwa Mwenyekiti wa CCM Taifa – Rais Benjamin W.
Mkapa,
Waheshimiwa Makamu wa Mwenyekiti, Tanzania Bara na
Tanzania Zanzibar,
Waheshimiwa Viongozi wetu Wakuu wa Halmashauri Kuu ya
Taifa,
Waheshimiwa Wajumbe wa Halmashauri Kuu
ya Taifa.
Assalam Alheikum.
Nashukuru
sana kupewa heshima na fursa hii ya kuzungumza mbele ya Wajumbe wa Halmashauri
Kuu ya Taifa ya CCM ili nitoe Maelezo juu ya Sera ya CCM ya Ubinafsishaji. Mimi kama Waziri ninaesimamia masuala ya
Ubinafsishaji nafarijika kuwa maelezo nitakayoyatoa hapa yatasambaa Tanzania
nzima bila ya wasi wasi wowote, kwa vile ni ukweli usiopingika kuwa hadhara hii
inawakilisha uongozi wa juu kabisa wa nchi yetu katika Chama na vile vile ni
uongozi unaowakilisha Taifa zima.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, Sera ni Uamuzi. Katika
dunia, kila uamuzi una maana yake na unaweza ukawa na matokeo ambayo yanaweza
yasimfurahishe kila mwananchi. La
muhimu ni mizania ya matokeo hayo yatathminiwe na kubaini athari na mafanikio
yake. KWA MAANA KUPANGA NI KUCHAGUA
kama alivyotuasa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Iwapo mafanikio ndiyo mazito zaidi lazima
Chama kiwe jasiri kukubali kuendelea na utekelezaji endelevu. Na hivi ndivyo Serikali inavyofanya.
Kwanza
nikumbushie mwelekeo wa Sera za CCM katika miaka 2000 hadi 2010. Mwelekeo huu ulibuniwa mwanzoni wakati
ambapo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa bado yu hai. Nakumbushia hivyo kwa maksudi, maana wako
wanaohoji Sera zetu za CCM tena kwa kupotosha tu, au kupinga Sera za CCM na
mikakati yake, na wanatafuta uhalali huo kwa kutaja jina la Baba wa Taifa. Wanalitumia jina vibaya. Mwalimu, alitufundisha wazi kuwa mkakati wa
kujenga uchumi imara kwa kutumia mashirika ya umma ulikuwa umefikia ukomo. Wala hatukubadili mkakati na kukaribisha
Sekta Binafsi kwa vile tuna TATIZO la KIITIKADI na Sekta ya Umma au kwa vile
tuna mapenzi na Sekta Binafsi. UKWELI ni kwamba Mashirika ya Umma yametushinda,
hayangeweza kuhimili uendeshaji wa uchumi.
Hadi sasa kama tungeendelea na utaratibu ule robo tatu ya uchumi wetu
hivi sasa ungezimia au kufa na matatizo tele ambayo yangehatarisha maisha na
utawala wa Chama Chetu na Tanzania kudhalilika.
NJIA
sahihi na ya uhakika iliyobaki ni mkakati wa kutanguliza mbele SEKTA BINAFSI
kuwa mhimili wa uchumi. Nguvu zetu zote
tuzimalizie hapo.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, Kifungu cha 14 cha Mwelekeo wa Sera za CCM katika miaka ya 2000
hadi 2010 kinasema: nanukuu “Uchambuzi yakinifu wa hali ya Uchumi wa Tanzania
ni kuwa Uchumi wetu una sifa kuu mbili.
·
Ni
uchumi ulio nyuma.
·
Ni
uchumi ulio tegemezi.
Sifa hizi mbili za uchumi
wetu tusipoangalia tunaweza kuzilea kama vile tumepata watoto mapacha. Katika hali ya sasa ya Uchumi wa dunia nchi
haiwezi kujitegemea kiuchumi wakati uchumi wake uko nyuma, na pia uchumi wake
hauwezi kuwa ulioendelea kama haujitegemei.
Kadri uchumi unavyozidi kuwa wa kisasa (kama tufanyavyo sasa) ndiyo nchi
inavyoingia katika mkondo wa kujitegemea kiuchumi. TUSIDANGANYIKE Uchumi vile vile ni siasa.
Ilani
ya CCM ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2000
nayo inaongezea Ibara ya 2 …. Hivyo katika kipindi hiki cha mwaka 2000 hadi
2005, CCM itahakikisha kuwa Serikali zetu 2 zinazingatia mkakati wa
modenaizesheni katika Sekta zote za Uchumi wa Taifa kama mkakati wa pekee wa
kujenga msingi wa Uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea.
Uchumi
wa kisasa utajengwa kwa kuhakikisha kuwa Sayansi na teknolojia ya Kisasa
inapenyezwa katika sekta zote ili hatimaye kutokomeza umaskini nchini.
Ninachosema
ni kwamba katika hali ya sasa ya Uchumi, na mazingira ya utandawazi hatuwezi
kuendesha uchumi wetu kama tulivyokuwa tunafanya zamani. Lazima tubadilike. Tunahitaji, mitambo ujuzi, teknolojia mpya ili tuongeze
uzalishaji na tija. Lazima tuwe jasiri
na kubadilika, kwa maana tusipobadilika uchumi wetu utabaki nyuma na utabaki
kuwa tegemezi.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, mkakati wa jumla wa kuondoa uchumi wetu katika uduni na
utegemezi wake nao upo wazi ndani ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Kifungu cha 4. Nanukuu “Sera ya CCM ya
urekebishaji wa uchumi ulioanza tangu zama za awamu ya pili na kuendelezwa
katika kipindi cha 1995 na 2000 itaendelea kutekelezwa kwa nguvu na kasi mpya
katika miaka 2000 na 2005.”
Na Sehemu ya Mwisho ya
Kifungu cha 5 Cha Ilani nayo inasema “Katika Kipindi kijacho, CCM itahakikisha
kuwa Serikali itaendelea na zoezi la Urekebishaji na Ubinafsishaji wa mashirika
na makampuni yaliyosalia”. Tujiulize
zoezi hili linaendelea au limesitishwa?
La bado linaendelea.
Kwa
hiyo basi Sera hii ni yetu lazima CCM tuilinde, na tuitetee bila ya aibu. Hatuwezi kubabaika na kuangalia nyuma na
tukakaa tu tukisikia ikipotoshwa.
Kujenga hisia kuwa Sera hizi na mikakati hii ni Shinikizo la Mashirika
ya Fedha ya Kitaifa ni upotoshaji. Sera
hizi ni za CCM na ndizo zilizotupatia idhini ya Chama chetu kutawala kwa
ushindi mkubwa na ridhaa isiyo na shaka.
Ni
kweli CCM imezungumza na kukubaliana na Mashirika ya Fedha ya Kimataifa, ya
Kikanda, nchi wahisani juu ya ratiba ya utekelezaji wa malengo yetu. Hali hii imetujengea heshima dunia
nzima. Madeni tunasamehewa na nchi
inakopesheka. Hii ni Sera yetu, sisi
sote Wana CCM na Watanzania. Kwa mantiki
hii Sera ya Ubinafsishaji si Sera ya Mwenyekiti wetu wa Taifa, au ya
Halmashauri Kuu ya Taifa, ya Waziri yeyote au mtu yeyote. Hii ni Sera ya CCM iliyofafanuliwa vizuri
katika Ilani zote za Uchaguzi za CCM za mwaka 2000 na 2005 pamoja na
kusisitizwa katika mwelekeo wa CCM kuelekea mwaka 2005, kama nilivyoelezea hapo
awali.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, utaratibu na mwelekeo tunaousikia na kuuona hivi sasa katika
kuelezea Sera ya Ubinafsishaji, unaofanywa hususan na baadhi ya Wanasiasa
Wapinzani wanapoona mafanikio ya Sera za CCM, kwa vile hawapendi wanayakejeli
na kuyakebehi bila ya sababu zozote zile, ila ile ya UPOTOSHAJI. Upotoshaji huo unaofanywa umefikia kiwango
cha wapotoshaji hao hata kushindwa kutofautisha kati ya Sera ya Ubinafsishaji
na ile ya Uwekezaji. Hali hii
inasikitisha na ni bahati mbaya. Hali
hii vile vile inadhihirisha mtazamo finyu wa wale wapinzani kupinga jambo au
fanikio lolote lile kwa sababu tu ni wapinzani. Kwa wanasiasa hawa kufanya hivi wanafikiria kuwa watapata afueni
za kisiasa. Hili haliwezi kutokea kwa
sababu popote pale ukweli unaposimama uongo hujitenga. Kutokana na hali ya maendeleo ya uchumi
duniani ilivyo hivi sasa, itakuwa ni vigumu sana kuwashawishi Wananchi kwa
kutumia propaganda ya upotoshaji wa
kutoa habari ambazo si sahihi.
Kwa
upande mwingine inashangaza vile vile kusikia na kuona kuwa hata baadhi ya
wasomi wetu nchini nao wanatumia taaluma na elimu zao walizozipata kuwapotosha
Wananchi aidha kwa kukidhi dhana, matakwa na maslahi yao binafsi au kwa malengo
ya kupaka matope siasa nzuri za CCM.
Sote tunafahamu kuwa mchakato wa kuleta maendeleo yawe ya kiuchumi au
kijamii, pamoja na mambo mengine, unahitaji tujenge fikra zilizo sahihi na
kubadilisha mtazamo wetu ili twende kwa wakati kwa kukubali kuwa dunia sasa
hivi inapambana na mabadiliko makubwa ya kijamii na Uchumi. Wanasiasa na wasomi hawa wamekuwa wakitumia
baadhi ya vyombo vya habari kama vile Radio, TV, Magazeti kueneza propaganda
hizo za upotoshaji mkubwa wa Sera nzuri za CCM, hususan hii ya
Ubinafsishaji. Nadhani hali hii ni
kupoteza wakati mzuri tunaouhitaji katika kupambana na Umaskini.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, hapa ningependa kusema wazi kuwa hata hivyo vyombo vya habari
wanavyovitumia kwa upotoshaji huo, hivi sasa vimeshamiri sana nchini kutokana
na Sera hii hii ya Ubinafsishaji. Wito
wangu kwa baadhi ya vyombo vya habari visaidie kuwaelimisha Wananchi na
kuelezea ukweli wa mafanikio ya Sera za CCM na pale penye matatizo vikiri mbinu
na ufumbuzi unaofanywa na Serikali yetu
inayoongozwa na Chama Tawala cha CCM.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, ni vema sasa nielezee Sera ya Ubinafsishaji kwa mantiki ya
kupima mafanikio yetu na matatizo yetu kulingana na dhamira ya Sera yenyewe
kama ilivyoainishwa katika madhumuni ya Sera ya Urekebishaji wa Mashirika ya
Umma.
UKUZAJI
WA PATO LA TAIFA
(a)
Dhumuni
la kwanza ni kuongeza ufanisi wa uzalishaji katika sekta zetu mbalimbali ili
ziweze kuchangia zaidi katika Pato la Taifa na kupunguzia Serikali na walipa
kodi mzigo wa ruzuku na mikopo kwa mashirika ya umma. TUJIULIZE dhumuni hili tumelifikia au la? Hivi sasa uchumi wetu unakua kwa asilimia
takribani kati ya 6.2 na 7 na kuifanya Tanzania nchi ya 3 kwa Kukuza uchumi
wake katika nchi 14 za SADC mwaka 2003.
Mfumko wa bei umepungua na mapato ya Serikali sasa yameongezeka kuanzia
sh. 25 bilioni hadi kufikia zaidi ya sh. 100 bilioni kwa mwezi hivi sasa. Kabla ya Ubinafsishaji Serikali ilikuwa
ikitoa ruzuku kuyabeba Mashirika ya Umma kwa kiasi cha dola 100 milioni kila
mwaka na mashirika haya yalikwisha ingizia Serikali hasara ya dola 300
milioni. Hivi sasa kwa eneo la KODI
Serikali inalipwa kodi badala ya kutoa ruzuku.
Mifano ni viwanda vya sukari Mtibwa, Kilombero; Mbeya Cement, Tanga
Cement, Tanzania Portland Cement, NBC, CRDB, Canvass Mill, Handico, Blankets na
Textile Manufacturers Ltd., TBL, TCC, DAHACO, Sabuni Detergents Ltd, nk. Mtibwa ililipa VAT ya zaidi ya Tsh. 800/=
mwaka 2001. Ilipobinafsishwa mwaka 1998
ililipa malimbikizo ya kodi ya Tshs. 400 mil.
Kabla ya hapo malipo ya kodi hayakuwa ya kuaminika. TBL mwaka 2002 ililipa kodi ya sh. Bilioni
43.5 na gawio kwa wanahisa sh. Bilioni 34.5.
Kabla ya kubinafsishwa mwaka 1993, TBL haikuwahi kupata mapato (total
revenue) zaidi ya Tsh. 15 bilioni na hivyo kodi ilikuwa ndogo sana. Handico haikuwa ikilipa kodi kabla ya
kubinafsishwa mwaka 1996 kwa sababu ilikuwa ikiendeshwa kwa hasara. Hivi sasa inalipa wastani wa Sh. 2 milioni
kwa mwaka kama kodi mbalimbali.
Blankets and Textile Manufactures Ltd. inalipa wastani wa kodi ya sh.
200 milioni kwa mwaka. Wakati
kinabinafsishwa mwaka 1997, kiwanda kilikuwa kimefungwa kwa miaka kadhaa na
hivyo kilikuwa hakilipi kodi. TTL
(Zamani Kibo Paper) ililipa kodi ya Tsh. 460 milion mwaka 1999 na Tsh. 662
mwaka 2000. Kabla ya kubinafsishwa
mwaka 1977 kiwanda kilikuwa kikiendeshwa kwa hasara. Canvass Mill ilifungwa kwa muda wa miaka minne kabla ya
hakijabinafsishwa mwaka 1998. Mwaka
2002 ililipa Tsh. 109.7 milioni kama kodi mbalimbali. Sigara (TCC) inalipa Serikalini wastani wa kodi Tsh. 40.9 bilioni
kwa mwaka. Mwaka 1999 ililipa Tsh. 34
bilioni kama kodi mbalimbali. Kabla ya
ubinafsishaji kiwango cha kodi kilikuwa kidogo kwa sababu ya uzalishaji mdogo
uliombatana na biashara ya magendo ya sigara.
Tanzania Portaland Cement ililipa Serikalini kodi ya Tsh. 3.4 bilioni
mwaka 2002. Tanga Cement ililipa
Serikalini kodi ya Tsh. 1.9 bilioni mwaka 2002. Kiwanda kinaongoza katika kulipa kodi mkoani Tanga. Mbeya Cement ililipa Serikalini kodi ya Tsh.
847.5 milioni mwaka 2002. Kabla ya
ubinafsishaji mwaka 1997 Kampuni iliendeshwa kwa hasara. NBC ililipa kodi Tsh. 3.2 bilioni mwaka
2002. Kabla ya ubinafsishaji mwaka 1999
Benki ilikuwa inapata hasara ya wastani wa Tsh. 1.5 bilioni kila mwezi. NBC pia ilikuwa na mtaji hasi (negative
capital) wa Tsh. 39,517 bilioni hapo Desemba 1999.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, inaonekana Wanasiasa Wapinzani, wasomi hawa na wanapropaganda
wanatatizo kubwa la USAHAULIFU au KUSAHAU.
Mara hii wamekwishasahau kuwa tulikuwa tukisimama mistari mirefu
(foleni) kutafuta chumvi, sukari, mafuta, sabuni za kufulia, nguo nk. Wanakumbuka kuwa wakati ule utawala bora ni
kwa viongozi kugawa sabuni au mafuta? Taifa
lilitumbukia katika dimbwi la aibu, ulanguzi na rushwa na tulikata tamaa. Hali hii tuizungumzeni kwa ukweli kabisa na
tuwahamasishe Wananchi waelewe vyema kuwa baada ya Ubinafsishaji kupitia
menejimenti bora, ujuzi mzuri na teknolojia ya kisasa, sekta zetu za kuzalisha
uchumi moja kwa moja zilifufuka na kuongeza bidhaa, ajira na mapato kwa
Serikali kwa faida ya kujenga uchumi wa Taifa letu. Ngoja nitoe mifano michache ifuatavyo: Viwanda/mashirika mengi yaliyobinafsishwa yameongeza uzalishaji
wa bidhaa mbalimbali zenye ubora wa kimataifa.
Hii imewezekana kutokana na uwekezaji katika teknolojia ya kisasa na
mbinu bora za uendeshaji (management/business skills). Kilombero uzalishaji wa sukari umepanda
kutoka tani 29,000 wakati wa ubinafsishaji mwaka 1997 hadi tani 98,000 mwaka
2002/2003. Mtibwa tani 29,000 wakati wa
ubinafsishaji mwaka 1998 hadi tani 49,700 sasa. Katumba kilo 1,042,000 mwaka 2001 hadi kilo 2,194,000 za chai
mwaka 2002. kabla ya ubinafsishaji
ukulima wa chai ulisimama na viwanda vya Katumba na Mwakaleli kufungwa. Tanga Cement mwaka 1999 tani 340,000 hadi
tani 400,000 mwaka 2002/2003. Sabuni
Detergent (FOMA); Kiwanda hiki kilibinafsishwa kwa utaratibu wa kufilisiwa
kupitia LART mwaka 1995. Baada ya
ukarabati, uzalishaji wa sabuni ulianza upya mwezi Machi 1996 na sasa
umeshamiri. Sabuni zinazotengenezwa ni
aina mbalimbali za Foma za unga na maji, Foma Limao, Foma Dazzle, nk. Gombamwenga Sisal Estate uzalishaji
umeongezeka kutoka tani 481 mwaka 1998 hadi tani 535 mwaka 2002. Kabla ya ubinafsishaji shamba liliota majani
na kusitisha uzalishaji mkonge. Viwanda vingi vya Nguo kama
Mwatex, Mutex nk. sasa vimeendelea kuzalisha nguo nchini baada ya kusimama kwa
muda mrefu. Ajira imeongezeka sana na
taarifa tulizonazo hivi sasa karibu asilimia 75 ya pamba yetu ghafi,
inasindikwa na viwanda vyetu.
SUALA
LA AJIRA, MISHAHARA NA MENEJIMENTI.
Dhumuni
la pili ni kuongeza ajira na kuboresha menejimenti. TUJIULIZE dhumuni hili tunalifikia au la? Inafaa izingatiwe kwamba Ubinafsishaji si
lazima usababishe upunguzaji wa ajira.
Wafanyakazi wengi walipoteza ajira zao hata kabla ya Sera ya
Ubinafsishaji haijaanza kutekelezwa kwani mashirika yapatayo 78 yalikwishafunga
shughuli zake na hivyo wafanyakazi husika kujikuta hawana kazi/ajira. Baadhi ya mashirika haya sasa yamefufuliwa
na yanafanya kazi vizuri. Mifano ni
Kiwanda cha Mablanketi, Kiwanda cha Viatu (Bora), Kiwanda cha Sabuni cha Tanga
nk. na yameajiri upya wafanyakazi.
Mashirika mengine yalilazimika kupunguza wafanyakazi baada ya ubinafsishaji
kwa vile yaliajiri wafanyakazi zaidi ya waliokuwa wanahitajika. Kwa sasa ajira katika mashirika
yaliyobinafsishwa ni yenye uhakika na endelevu. Ajira zaidi zimeongezeka nje ya viwanda/mashirika ambayo sasa
yanafanya kazi vizuri na kwa ufanisi mkubwa.
Kwa mfano viwanda vyote vya saruji sasa vimeongeza uzalishaji. Hali hii imechangia kuongezeka kwa haraka
shughuli za ujenzi na biashara ya kufyatua matofali; usafirishaji wa saruji pia
umetoa ajira kwa wenye vyombo vya usafiri, n.k. Viwanda vya sukari vimeongeza ajira ya wakata miwa, wakulima
wadogo wadogo (outgrowers), watengezaji wa bidhaa mbalimbali zinazotumia
sukari, nk. Wakulima wa mazao mengine
kama tumbaku, nao wameongeza uzalishaji baada ya kuhakikishiwa soko kutoka
kwenye viwanda ambavyo vimefufuliwa baada ya ubinafsishaji. Inakadiriwa kwamba mapato/maisha ya zaidi ya
Watanzania 300,000 hutegemea sana usambazaji na ugawaji wa bidhaa za Kampuni ya
bia (TBL) na Kampuni ya sigara (TCC).
Kabla ya ubinafsishaji Watanzania karibu 100,000 walikuwa wanapata ajira
kutokana na usambazaji wa bidhaa za TBL na TCC. Mishahara na maslahi ya wafanyakazi wa mashirika mengi
yameongezeka na kuboreshwa. Kwa mfano: Kabla ya kubinafsishwa, kima cha chini
pamoja na marupurupu Tanga Cement kilikuwa sh. 150,000/= kwa mwezi. Sasa ni zaidi ya sh. 450,000/=. TBL ilikuwa inalipa kima cha chini sh.
9,000/- kabla ya ubinafsishaji. Sasa
kiasi ni zaidi ya sh. 120,000/= mbali ya marupurupu yanayotolewa nk. Aidha kiwanda cha Tanga Cement hutumia sh.
100 milioni kwa mwaka kugharamia elimu kwa wafanyakazi; TBL imetenga zaidi ya
saa 100 za mafunzo ya kompyuta kwa kila mfanyakazi kwa mwaka nk.
TEKNOLOJIA
YA KISASA.
Dhumuni
la tatu ni lile la kupata teknolojia ya kisasa. TUJIULIZE dhumuni hili tunalifikia au la? Hivi sasa ni vigumu kupata nafasi muhimu
viwandani na hata katika maeneo ya menejimenti bila ujuzi au elimu ikizingatiwa
na pale zamani. Teknolojia ya kisasa
imeanzishwa katika uzalishaji mali na utoaji wa huduma muhimu kwa jamii. Umwagiliaji mashamba ya miwa Kilombero
hutumia mitambo ya kisasa. TBL pia
hutengeneza bia kutumia kompyuta nk.
UPATIKANAJI
WA MITAJI NA MASOKO.
Dhumuni
la nne lilikuwa ni lile la kupata mitaji ya ndani na nje na kupata masoko ya
ndani na nje ya bidhaa zetu. TUJIULIZE
dhumuni hili linafikiwa au la? Hivi
sasa saruji yetu, huuzwa nchi jirani za Malawi, Zambia, Rwanda, Burundi
nk. Bia pia huuzwa Kenya, Uganda na
nchi nyingine za jirani. Maturubai ya
Canvas Mill yanauzwa katika majeshi ya NATO nk. Sabuni zetu zimepata soko DRC Kongo, Malawi, Msumbiji na hata
Kenya. Aidha Sigara, chai na Tumbaku
tunayozalisha tunaziuza nje. Hivi sasa,
ubora wa bidhaa za viwanda vingi vilivyobinafsishwa umeongezeka na vingine
vimeweza kuthibitishwa, kutambuliwa na kukubaliwa na asasi za kimataifa zinazodhibiti
ubora wa bidhaa na usimamizi wa mzingira kama ISO, NOSA nk. na hivyo kukubalika
katika masoko yetu ya ndani na nje. Hii
ni moja ya sababu ya kuongezeka kwa akiba yetu ya fedha za kigeni zinazoweza
kuhimili miezi 7 hadi 8 badala ya wakati ule ambapo akiba yetu isingeweza
kuhimili hata kipindi cha miezi 2.
KUIPA
NAFASI SEKTA BINAFSI.
Dhumuni
la tano ni lile la kuipa Sekta binafsi nafasi ya kuendesha uchumi ili Serikali
ielekeze nguvu zake katika kuimarisha shughuli za jamii, miundombinu, ulinzi,
usalama na utawala bora. TUJIULIZE
dhumuni hili linafikiwa au la?
Kuainishwa kwa Baraza la Wafanyabiashara, Taasisi ya kuendeleza Sekta
binafsi nchini ni vigezo tosha kwa upande wa dhamira ya Serikali ya
kubadilishana mawazo na Wawekezaji, wafanyabiashara binafsi ili kujenga
mazingira bora ya utendaji kazi. Aidha
watanzania wengi wamepata fursa ya kuwa wawekezaji katika mashirika yapatayo
138 kwa asilimia 100 na wengine zaidi wameingia ubia na wageni katika kumiliki
mashirika 123 yaliyobinafsishwa, kati ya Mashirika zaidi ya 266
yaliyobinafsishwa. Vile vile zaidi ya
Wananchi 98,000 wamenunua hisa katika mashirika yaliyobinafsishwa na wanapata
gawio kila mwaka. Katika hawa, wanawake
wanaongoza (55%).
Aidha
ili sasa kuendeleza zao la Korosho, Serikali imeamua kufuata utaratibu wa
kubinafsisha viwanda vya kubangulia Korosho kwa misingi ya kuangalia Mpango wa
Uwekezaji na Uendeshaji, badala ya kung’ang’ania fedha za kununulia viwanda
hivi. Utaratibu wa kutoa fedha
umekwamisha kuendelea kwa viwanda hivi kwa vile baada ya kununua viwanda
inabidi mwekezaji aingie gharama kubwa ya kubadilisha teknolojia iliyopitwa na
wakati ili wazalishe kwa ufanisi na tija.
Umuhimu na kipaumbele katika kubinafsisha viwanda hivi utatolewa kwa
Watanzania ili waendeleze viwanda hivi.
Hoja hii ya kusema nchi inauzwa kwa wageni inatoka wapi kama si
upotoshaji tu? Kwa upande wa kuboresha
huduma za jamii hivi sasa tunashuhudia juhudi kubwa za Serikali katika
kuboresha mashule, vituo vya afya, mabarabara nk. Mikakati ya kupambana na rushwa inaendelezwa na vile vile mpango
wa kurekebisha Serikali za Mitaa na Miji unaendelea kama njia mojawapo ya
kuboresha utawala bora.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, si kweli kuwa mikataba inayoingiwa na Serikali na Wawekezaji
katika ubinafsishaji ni ya siri na ni vyema ikajadiliwa na umma. Utaratibu huu utakiuka haki na Sheria za
Kimataifa na vile vile utaondoa mantiki ya ushindani baina ya Wawekezaji pale
ambapo wale wanaowania kununua kiwanda fulani, mipango yao ya Uwekezaji na
Uendeshaji, pamoja na bei walizotoa zinapokuwa bayana kwa kila mtu.
Hata
mtu anaponunua baiskeli haitawezekana atangaze katika mitaa yote juu ya mkataba
wake wa kununua baiskeli hiyo.
Utayarishaji wa Mikataba hii huhusisha Serikali, Ofisi ya Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Wizara ya Sheria na Katiba pamoja na Mnunuzi baada ya
makubaliano ya uuzaji kufuata utaratibu niliokwisha uelezea. Hi inatosha.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, mashirika yaliyobinafsishwa hayajauzwa kwa bei poa. Yale yaliyonunuliwa na Watanzania
yamegharimu takriban sh. 60 bilioni, yale ya wageni takriban sh. 23 bilioni na
yale yaliyonunuliwa kwa ubia yamefikia takriban sh. 400 bilioni. Hii hoja inayozungumzwa siku zote na
wahusika kuwa mashirika haya yameuzwa bei poa imetoka wapi. Misingi ya uuzaji inayozingatia aina ya
teknolojia, madeni ya shirika kutokana na mikopo inaeleweka kabla ya kutoa hoja
hizi. Kiwanda maana yake si majengo
tu. Huu ni upotoshaji.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, Wanasiasa wapinzani, baadhi ya wasomi na watu wengine wamekuwa
wakiuliza na kuhoji, kwa kujifanya kwa maksudi, eti hawajui Ubinafsishaji
umemfaidishaje Mtanzania wa kawaida.
Nimeshaonyesha kuwa Serikali sasa haitoi ruzuku na kufidia madeni ya
mashirika haya yaliyolimbikiza hasara ya dola takriban 400 milioni kabla ya
Ubinafsishaji. Badala yake Serikali
sasa inapata mapato kupitia kodi na gawio kutoka viwandani ambazo zinaingia
moja kwa moja katika mfuko wa Serikali.
Tunashuhudia sasa ujenzi wa mabarabara uboreshaji wa huduma za jamii:
elimu, afya, maji n.k. Haitawezekana na
wala haiwezekani kiwanda kikiuzwa waitwe wananchi wote wagawiwe fedha
mifukoni! Swala la kupunguza umaskini
lina mtazamo wa aina mbili: kupunguza umaskini usio wa kipato na kupunguza
umaskini wa kipato. Bila ya kuelewa
dhana hii tutabaki kuoegelea kwenye propaganda ya upotoshaji kama vile
inavyoshabikiwa na Wanasiasa Wapinzani na baadhi ya wasomi. Hakuna njia ya panda katika ajenda hii na
CCM iko katika mstari sahihi.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, sera hii ya Ubinafsishaji inayozungumziwa na Wanasiasa
wapinzani kwa upotoshaji na kupakana matope, ni kama vile sera hii inatekelezwa
Tanzania peke yake. Hii siyo
sahihi. Nchi zile zilizoikataa sera hii
pale awali sasa zinaitekeleza. Afrika
ya Kusini, Kenya n.k. Aidha nchi nyingi
za Afrika, Ulaya na Asia zinaendeleza kutekeleza sera hii hadi hivi sasa ili
kuipa nguvu sekta binafsi. Aidha
Malawi, Rwanda na Burundi pamoja na Kenya na Uganda zimeshaleta wajumbe wao
hapa nchini kujifunza taratibu za ubinafsishaji kutokana na mafanikio
tuliyoyapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, si sahihi kusema kuwa
ubinafsishaji haujali malipo ya mafao ya wafanyakazi. Serikali imelipa mafao yote ya kisheria ya wafanyakazi
walioachishwa kazi kutokana na viwanda vyao kufungwa kwa kushindwa kufanya kazi
na hatimae kubinafsishwa. Tatizo lipo
katika malipo ya mafao chini ya utaratibu wa Mikataba ya Hiari. Mikataba hii hutekelezeka wakati kiwanda au
shirika husika likitengeneza faida.
Kama shirika limefilisiwa au limefungwa kwa kushindwa kufanya kazi,
faida hiyo na hususan malipo hayo ya mkono wa kheri yatatoka wapi au yatatokana
na nini? Wanasiasa Wapinzani na baadhi
ya Wasomi wanajifanya hili hawalijui au hawalielewi. Mafao yanayotokana na mikataba ya hiari ni makubaliano kati ya
menejimenti ya wafanyakazi, na wala Serikali haihusiki.
Mafao
yanayotokana na makato ya Pensheni, mengi yalikuwa hayawasilishwi kwenye
taasisi husika na mashirika mengi ya umma.
Fedha hizi zilipokatwa kutoka mishahara ya wafanyakazi hazikufikishwa
kwenye taasisi husika; zilitumika.
Mzigo huu si wa Serikali. Hata hivyo
Serikali inajitahidi kulipa baadhi ya malipo haya ambayo hayakuwakilishwa hapo
awali kwa sababu ya uzembe na ubadhirifu uliotokea. Hivi sasa Serikali inatafuta sh. 18 bilioni ili kufidia uzembe
huu.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, mada yangu haisemi kuwa Sera yeyote katika nchi inaweza
kutekelezwa kikamilifu kwa asilimia moja.
Hili halijapata kutokea dunia nzima.
Kwa mantiki hii hata utekelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji haujaendelea
bila ya matatizo.
Matatizo yaliyojitokeza:
·
Baadhi
ya wananchi kutoelewa dhana nzima ya Sera ya Ubinafsishaji na kujenga
hisia/imani kwamba mali yao inauzwa kwa wageni.
·
Mashirika
mengi kuwa na malimbikizo makubwa ya madeni na hivyo kuwa vigumu kuwavutia
wawekezaji.
·
Baadhi
ya mashirika/viwanda yalikuwa katika hali mbaya sana katika vitendea kazi
muhimu, yaani mitambo na miundombinu yake ilikuwa imechakaa na teknolojia yake
kupitwa na wakati.
·
Baadhi
ya wawekezaji kushindwa au kuchelewa kufufua mashirika waliyokabidhiwa. Mifano ni: Moshi Hotel, Kiwanda cha Ngozi
Morogoro, Tegry Plastics, viwanda vya magunia, mashamba ya mkonge, nk.
·
Baadhi
ya wawekezaji/wabia kutoa taarifa za uwekezaji zisizo sahihi na kutokuwa na
uwezo wa kifedha wa kuendesha taasisi zilizobinafsishwa.
·
Watanzania
wengi kukosa mitaji ya kumiliki na kuendeshea mashirika yanayobinafsishwa.
·
Mashirika
mengi kuwa na kesi Mahakamani, nk. Sasa
hivi kuna kesi zaidi ya 170 Mahakamani dhidi ya mashirika ya umma.
·
Kukosekana
kwa hati miliki karibu 700 za mashirika.
PSRC imeweza kuzipata hati 400.
Zilizobaki (300) zinafuatiliwa.
Hatua zilizochukuwa:
Serikali imechukua hatua
zifuatazo ili kukabiliana na matatizo yaliyojitokeza:-
·
Kuimarisha
ufuatiliaji wa utendaji wa mashirika yaliyobinafsishwa kwa kushirikiana na
Wizara zinazohusika.
·
Kutumia
wataalam kukusanya madeni kutoka kwa wadaiwa sugu.
·
Kuwafanyia
tathmini wawekezaji wote wanokusudia kuwekeza kwenye mashirika ili kubaini
uwezo wao kiutendaji, kibiashara na kifedha.
·
Kuendelea
kuwaelimisha wadau mbalimbali kuhusu Sera ya ubinafsishaji na umuhimu wake
katika jitihada za kufufua uchumi na kupiga vita umaskini.
·
Kuanzisha
utaratibu wa dhamana za benki (bid bonds) kwa nia ya kuwaengua/kuwadhibiti
madalali na wawekezaji wasio waaminifu.
·
Kuchukua
hatua za kisheria dhidi ya wawekezaji walioshindwa kutekeleza mikataba ya ubinafsishaji. Mifano: Mikumi Wildlife Lodge na Katani
Ltd., nk.
·
Kuajiri
wanasheria kushughulikia kesi zilizo Mahakamani.
·
Kuajiri
mtaalam wa masuala ya ardhi kufuatilia hati miliki zenye matatizo nk.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, utaratibu huu wa upotoshaji na propaganda unaoendelea hivi sasa juu ya Sera ya
ubinafsishaji ni dhaifu. Kutokuwaeleza
ukweli na kuwapotosha Wananchi si mkakati ambao utazuia hata kidogo kuendelea
na Sera ya Ubinafsishaji na sera nyingine za CCM zenye lengo la kuboresha
uchumi na maisha yetu, hasa katika kipindi hiki tunachopambana na mabadiliko
makubwa ya uchumi duniani pamoja na hili la sasa la utandawazi. Nawasisitiza Wana CCM, Wakereketwa na
Watanzania wenzangu tufanye kazi kwa bidii ili kuendeleza mafanikio haya
tuliyokwishayapata sasa kupitia Sera ya ubinafsishaji ili tusije tukarudi
katika zama zile za kukosa huduma muhimu za kibinadamu. Ndio maana hivi sasa
Serikali ya CCM, Bunge la Jamhuri ya Muungano linalowakilisha Watanzania wote,
tumefikia muafaka wa jinsi ya kubinafsisha Benki ya NMB ili ifanye kazi kwa
tija na ufanisi zaidi kuliko inavyofanya kazi hivi sasa. Aidha mikakati ya kubinafsisha mashirika
makubwa yatoayo huduma za miundo mbinu kama vile TANESCO, TTCL, THA,
TRC, NIC itaendelea kama vile tulivyokwisha binafsisha Shirika la Ndege na DAWASA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanapropaganda hawa wanapozungumzia Sera
ya Ubinafsishaji wanatengeneza picha ya kuwafanya Wananchi kuona kuwa matatizo
yote ya kiuchumi Tanzania yanaletwa na Ubinafsishaji. Hii si kweli. Uchumi
hujengwa na utendaji bora wa sekta zote zinazozalisha moja kwa moja. Aidha, ufumbuzi wa matatizo ya jamii kama
Afya, Elimu, Maji husaidia sana kukua kwa uchumi. Ni vyema tukaelewa kuwa Ubinafsishaji ni moja ya mbinu za kurekebisha uchumi wa nchi ambao kwa Tanzania
ni asilimia 2 tu ya mikakati yote ya urekebishaji inayofanyika. Upo urekebishaji wa sekta ya fedha, sekta ya
barabara, sekta ya uchukuzi, sekta ya sheria, sekta ya utumishi nk. Ubinafsishaji unagusa sekta nyingi za uzalishaji wa moja kwa
moja. Mimi naamini kwa dhati kuwa kama
mafanikio ya uchumi na jamii tuliyokwisha kuyapata hivi sasa kutokana na
matokeo ya utekelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji, kama tutajitahidi kuyafanya
endelevu, tutapata ufumbuzi wa kimsingi wa matatizo yetu ya kujenga uchumi imara. Kinachohitajika sasa ni kuendeleza
uendeshaji wa mashirika yaliyobinafsishwa hasa kwa Watanzania kwa kuwajengea
utamaduni na mazingira ya kuendesha mashirika hayo; na kuwajengea utamaduni wa
kutayarisha vyema michanganuo ya kuombea mitaji kutoka taasisi na vyombo vyetu
vya fedha. Utaratibu wa sasa wa
Serikali wa uwezeshaji wa wananchi, kuheshimu na kuthaminisha mali za wananchi
ki haki, na sheria za ardhi zinazowezesha ardhi kuwa dhamana ya kuchukulia
mikopo itasaidia sana katika kuimarisha shughuli za kiuchumi za Watanzania.
Mheshimiwa
Mwenyekiti, ningependa Chama cha Mapinduzi kupitia Halmashauri Kuu ya Taifa
ya CCM kiwatahadharishe wale wapotoshaji wa maksudi wa Sera ya Ubinafsishaji
kwa sababu zao tu za kisiasa. Wananchi
tuwahamasishe na tuwaelimishe. Nami
naamini penye ukweli wataelewa na nina hakika hivi sasa wameshagundua
upotoshaji huu wenye malengo ya kisiasa hasa tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu
wa mwaka 2005. Kama Mataifa mengine
yanaiongelea na kupongeza ufanisi wa uchumi tuliokwisha upata kwa nini CCM
tusijigambe na kuongeza juhudi zetu za kuimarisha uchumi. Ubinafsishaji si suala tu la kuuza Mashirika
ya umma, bali ni mfumo unaojenga mashirikiano ya kudumu baina ya wawekezaji wa
nje, Serikali na Wawekezaji wa ndani kwa nia ya kuongeza ufanisi, kuboresha
utendaji kupanua uwigo wa ajira, kuongeza ubora wa bidhaa na kuyapatia mitaji
na utaalam mashirika yaliyobinafsishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu tumekuwa
tukijigamba Tanzania ni nchi ya amani na usalama, mazingira mazuri, hali nzuri
ya hewa n.k. Haya tunayo. Tuongelee sasa yale ambayo hatuna, kama vile
teknolojia, mitaji, ujuzi, menejimenti bora nk. Haya yote tutayapata ikiwa mafanikio na matokeo ya Sera ya
Ubinafsishaji kwa uchumi wetu tutayafanya endelevu. Nina imani ya dhati kabisa Wanasiasa Wapinzani, wanapropaganda,
baadhi ya wasomi na wale wanaowapotosha wananchi kwa maksudi juu ya Sera ya
Ubinafsishaji, kwa mtazamo wa kisiasa, hususan Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2005
watashindwa hivi karibuni tu. Mhe.
Mwenyekiti, kama nilivyosema, siasa hivi sasa ni Uchumi, na Mazingira ya Uchumi
yanabadilika haraka haraka. Huko
tunakoelekea hatutaweza hata kidogo kuepukana na mabadiliko haya. Tulianza na Uchumi funga; tukaingia Uchumi
huria ulioandamana na mipango mingi ya kurekebisha muundo na mfumo wa uchumi,
tunashuhudia zoezi la ubinafsishaji na uwekezaji; hivi sasa tumeingia katika
kuimarisha Sekta Binafsi na Uwekezaji, na kama vile hili halitoshi tunapambana
sasa na Sera ya Utandawazi. Mabadiliko
haya yanaweza kueleweka na wachache wetu sisi hapa ndani kama viongozi, lakini
kwa wananchi haya mabadiliko ni ya kasi kubwa.
Inawezekana yasieleweke vizuri.
Hali hii sasa inatulazimisha kama Chama, kinachotegemea kutawala kwa
muda mrefu ujao kuandaa mpango kabambe wa kuandaa Makada wa Uchumi wa CCM
kufundishwa mabadiliko haya ya Uchumi yanayotokea hivi sasa kwa haraka ili
waeneze hali hii kwa Wanachama, Wakereketwa na Wananchi wote kwa ujumla
wanaokitakia mema Chama cha Mapinduzi ili nao waelewe tunakoelekea. Nadhani kwa nguvu za Chama chetu hili
linaweza kufanikishwa, sambamba na kuwakomesha wapotoshaji wa maksudi wa Sera
zetu nzuri za Uchumi za CCM.
Nawashukuru
kwa kunisikiliza Kidumu Chama cha
Mapinduzi.
Ahsanteni sana !