UCHUKUAJI WA FOMU ZA UBUNGE, UWAKILISHI WA MAJIMBO NA WA  VITI MAALUM (WANAWAKE) KWA TIKETI YA CCM

 

Chama Cha Mapinduzi kimeweka utaratibu wa ndani ya Chama wa namna ya kuwapata wana-CCM watakaogombea nafasi za Ubunge na Uwakilishi wa Majimbo na wa Viti Maalum Wanawake katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 30, 2005.

 

Kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa, siku ya Jumatatu tarehe 1/08/2005 ndiyo mwanzo wa kuchukua fomu kwa wanachama wa CCM wote wanaotaka kugombea Ubunge na Uwakilishi wa aina zote kwa tiketi ya CCM.  Mwisho wa kurudisha fomu hizo ni tarehe 3/08/2005 kabla ya saa 10 jioni.

 

Utaratibu mzima utakaotumika kuwapata watakaogombea nafasi hizo ni kama ifuatavyo:-

 

KUCHUKUA NA KURUDISHA FOMU

 

MWAKA

NAFASI YA UONGOZI

MWANZO WA KUCHUKUA FOMU

MWISHO WA KURUDISHA FOMU

 

2005

Ubunge

1/08/2005

3/08/2005 kabla ya saa 10.00 jioni

Uwakilishi

1/08/2005

3/08/2005 kabla ya saa 10 .00 jioni

 

UTEUZI WA WABUNGE/WAWAKILISHI/VITI MAALUM WANAWAKE

 

MWAKA 2005

TUKIO

4-6 Agosti 2005

Kura za maoni katika Majimbo

7 Agosti 2005

Mikutano Mikuu ya UWT ya Mikoa kupendekeza wagombea 5 kwa kila mkoa

8 Agosti

Kamati za Siasa za Wilaya

9 Agosti 2005

Kamati za Siasa za Mikoa zitajadili wagombea Ubunge, Uwakilishi na Viti Maalumu-Wanawake.

10 Agosti 2005

Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa kuwajadili wagombea Ubunge na Uwakilishi wa aina zote.

11 Agosti 2005

Baraza Kuu la UWT kuandaa orodha ya wagombea wote nchini

12-13 Agosti 2005

Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa.

15 Agosti 2005

Kamati Kuu Maalumu

16 Agosti 2005

Halmashauri Kuu ya Taifa kuteua wagombea Ubunge na  Uwakilishi wa jimbo na Viti Maalumu-Wanawake

Mapitio na uthibitishaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005

17 Agosti 2005

Kutangaza Uteuzi

20 Agosti 2005

Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuteua wagombea

21 Agosti 2005

Kuanza kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu kwa Tanzania Bara

03 Septemba 2005

Tume ya Uchaguzi Zanzibar kuteua wagombea

05 Septemba 2005

Kuanza kampeni kwa upande wa Zanzibar

29 Oktoba 2005

Kumalizika kwa Kampeni za Uchaguzi Mkuu nchi nzima

30 Oktoba 2005

Siku ya Uchaguzi (Kupiga Kura)

 

Fomu za Ubunge na Uwakilishi wa Majimbo zinatolewa na Makatibu wa CCM wa Wilaya na zile za Viti Maalum (Wanawake) zinatolewa na Makatibu wa UWT wa Mikoa.

 

Gharama za uchukuaji wa fomu hizo ni Sh. 100,000/= tu; si zaidi, wala si kasoro.  Fomu zinatakiwa kurejeshwa katika ofisi zilizochukuliwa.

 

INDHARI KWA WATAKAOCHUKUA FOMU ZA UBUNGE NA UWAKILISHI KUPITIA CCM

 

Wanachama  wa CCM wote wanaokusudia kujaza fomu za kuomba uteuzi wa kugombea Ubunge na Uwakilishi kwa tiketi ya CCM wanatahadharishwa dhidi ya kujihusisha na vitendo vya kuvunja maadili ya Chama.  Vitendo  hivyo ni pamoja na kupakana matope, kutoa rushwa na kutumia udini, ukabila, rangi na ubaguzi mwingine katika kujilabu.  Inasisitizwa kwamba ye yote atakayethibitika kukiuka maadili hasa kuhusiana na rushwa, ataweza kukosa uteuzi hata kama ataongoza katika kura za maoni.

 

Kanuni ya 10(1) ya Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM Katika Vyombo vya Dola iko wazi katika hilo kama ifuatavyo:-

 

10(1)    Mgombea yeyote wa CCM anayetaka kuingia katika chombo cha Dola, atateuliwa kwa kuzingatia kura za maoni zilizopigwa.  Mgombea atakayeteuliwa ni yule aliyepata ushindi kwa wingi wa kura za maoni alizopata.

 

            Isipokuwa kwamba endapo itathibitika kuwa kura hizo za ushindi alizipata kwa njia ya rushwa, kikao cha uteuzi wa mwisho hakitamteua kugombea nafasi anayoiomba.

 

Aidha, Kanuni ndogo za (1) hadi (6) za Kanuni ya 20 ya Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM Katika Vyombo vya Dola zinabainisha miiko ya shughuli za uchujaji na uteuzi wa wagombea.  Kanuni ndogo ya (7) ya Kanuni hiyo ya 20 inabainisha adhabu kwa viongozi na wagombea watakaokiuka miiko hiyo.  Kanuni hiyo inasomeka ifuatavyo:-

 

            20(7)    Adhabu za kuvunja miiko iliyotajwa katika Kanuni hii ni hizi zifuatazo:-

 

(a)               Kiongozi yeyote atakayethibitika kuvunja miiko hiyo atavuliwa uongozi wake.

 

(b)        Mwanachama anayeomba kugombea nafasi yoyote atakayethibitika kuvunja miiko hiyo hatateuliwa kugombea nafasi anayoiwania.

 

Ni dhahiri kwa hivyo kwamba kujiingiza katika mitego ya rushwa na kuvunja miiko na maadili mengine kunaweza kugeuka balaa kwa mgombea.  Ni vyema wajichunge.

 

IDHARI KWA VIONGOZI WATAKAOSIMAMIA MAZOEZI YA KURA ZA MAONI NA UCHUJAJI

 

Viongozi watakaosimamia mazoezi ya kura za maoni na uchujaji nao wanafungika na miiko na maadili yanayobainishwa katika Kanuni ya 20 ya Kanuni za Uteuzi wa Wagombea wa CCM Katika Vyombo vya Dola.  Miiko na maadili hayo kimsingi yanawataka watende haki bila ya kumpendelea mgombea fulani na kumuonea mwingine.  Kama ilivyoelezwa hapo awali, kiongozi yeyote atakayethibitika kukiuka miiko na kuvunja maadili hayo, ataweza kuvuliwa uongozi.  Kwa hivyo, na wao wanapaswa kujichunga.