KATIBU MKUU WA CCM, NDUGU PHILIP J. MANGULA AELEZEA  MAAMUZI YA KIKAO CHA  HALMASHAURI KUU YA TAIFA (NEC) YA CHAMA CHA MAPINDUZI KWA WAANDISHI  WA  HABARI TAREHE 31/01/2004

 

 

1.0     UTANGULIZI:

 

Kama mnavyofahamu, Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi ilikutana mjini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa kuanzia tarehe 27-29/01/2004.

 

Kikao cha NEC kilijadili masuala mbali mbali yaliyowasilishwa kwake na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ambayo nayo ilikutana mapema mjini Dar es Salaam kuanzia tarehe 20-22/01/2004.

 

Mkutano ulianza na Semina kuhusu Ubinafsishaji ambayo ilihudhuriwa na Wajumbe wa NEC na nyinyi Wanahabari mlikaribishwa kuhudhuria wakati wa ufunguzi na ufungaji wa Semina hiyo ambayo ilikuwa ya mafanikio sana.

         

2.0     AGENDA ZA NEC:

         

Dondoo za agenda ambazo miongoni mwa mengine, zilihusiana na mambo yafuatayo:-

 

          (a)      Hali ya Siasa nchini,

          (b)     Uteuzi wa wagombea nafasi za uongozi katika Jumuiya za CCM za WAZAZI na VIJANA,

 


          (c)      Kuweka utaratibu bora zaidi wa kuwapata wagombea wa CCM katika vyombo vya Dola,

          (d)     Uhuishaji wa Muundo wa Chama Cha Mapinduzi.

 

3.0     HALI YA KISIASA:

 

Halmashauri Kuu ya Taifa ilipokea taarifa ya uchaguzi mdogo wa Madiwani uliofanyika tarehe 11/01/2004 katika Kata 41 Tanzania Bara.

 

Tume ya Uchaguzi (NEC) imekwisha tangaza rasmi kwamba katika chaguzi hizo, CCM imeshinda katika Kata 39 kati ya Kata 41.  Maana ya matokeo haya ni kwamba CCM tumeweza kushinda tena katika Kata zote 37 zilizokuwa zikishikiliwa na Madiwani wetu ambao walifariki dunia na kuziacha wazi.

 

Aidha, CCM tumefanikiwa kuzinyakua Kata mbili kati ya nne zilizokuwa zikishikiliwa na upinzani kabla ya uchaguzi mdogo huo uliofanyika tarehe 11/01/2004.  Kata tulizowapokonya wapinzani ni za Nkome, Wilaya ya Bariadi Mkoani Shinyanga na ile ya Masama Rundugai iliyopo katika Wilaya ya Hai, Mkoa wa Kilimanjaro.

 

Matokeo haya ni kielelezo dhahiri cha jinsi CCM inavyokubalika kwa Watanzania kutokana na sera zake sahihi na zinazotekelezeka.

         

Ushindi huu wa asilimia 95% ni ushahidi tosha kwamba CCM inaendelea kuwa NAMBARI WANI nchini.  Aidha, ni ushindi wa wazi wa jinsi sera za wapinzani za vitisho, matusi na upotoshaji zinavyokataliwa na wananchi wanaoitakia mema nchi yetu.

 

Hivyo basi, Halmashauri Kuu ya Taifa imetoa pongezi kwa Madiwani wote wa CCM walioshinda katika uchaguzi huo, na viongozi wa ngazi zote za uongozi walioongoza mapambano hayo.  Aidha, imewapongeza na kuwashukuru wana-CCM na wananchi waliokiunga mkono Chama Cha Mapinduzi na kutuwezesha kupata ushindi huo mkubwa na wa kishindo.  ALUTA CONTINUA.

 

4.0     UTEUZI WA WAGOMBEA WA NAFASI ZA UONGOZI KATIKA JUMUIYA ZA WAZAZI NA VIJANA

 


Kama tulivyokwisha watangazieni hapo awali Halmashauri Kuu ya Taifa katika kikao chake hiki ilifanya uteuzi wa mwisho wa wanachama walioomba kugombea nafasi mbali mbali za uongozi katika Jumuiya za WAZAZI na VIJANA, ngazi ya Mkoa na Taifa.

 

Kwa kuwa Uchaguzi Mkuu wa Jumuiya za CCM hufanyika kila baada ya miaka mitano kuanzia ngazi ya chini hadi Taifa, Halmashauri Kuu ya Taifa imezipongeza Jumuiya za WAZAZI na VIJANA kwa kukamilisha uchaguzi hadi kufikia ngazi ya Wilaya, na imezihimiza Jumuiya hizo kuendelea kukamilisha chaguzi hizo katika ngazi zilizobaki za Mkoa na Taifa.

 

Aidha, Halmashauri Kuu ya Taifa imetoa pongezi maalum kwa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT) kwa kukamilisha uchaguzi wa viongozi wake kuanzia ngazi ya chini hadi Taifa.  Imewapongeza pia viongozi wote waliochaguliwa katika ngazi mbali mbali za Jumuiya hiyo.

                                               

 

 

5.0     UTARATIBU WA KUWAPATA WAGOMBEA WA CCM KATIKA CHAGUZI ZA VYOMBO VYA DOLA


 

A.      Utaratibu wa kumpata Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

 

                   Halmashauri Kuu ya Taifa baada ya kupokea na kutafakari juu ya Mapendekezo ya Kamati ya Kupendekeza Namna Bora Zaidi ya Kuwapata Wagombea wa CCM Katika Chaguzi za Vyombo vya Dola, imeamua katika maeneo mbali mbali kama ifuatavyo:-

 

         


·        Wanachama wote wanaopenda kuwania nafasi ya Urais na wanazo sifa zinazotakiwa wajaze fomu na kuziwasilisha kwa Katibu Mkuu wa CCM katika muda utakaokuwa umewekwa, kupata wadhamini na kulipa ada kwa viwango vilivyowekwa katika Kanuni za sasa.  Utaratibu wa sasa unasema kwamba kila mgombea wa nafasi ya Urais kwa tiketi ya CCM anatakiwa apate wadhamini 250 kutoka mikoa isiyopungua 10, angalao miwili kati ya hiyo iwe ni mikoa ya Tanzania Zanzibar.

 


·        Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa itawachuja wagombea wote kwa kupitia sifa zao na kutoa maoni na mapendekezo yake kwa Halmashauri Kuu ya Taifa ya majina yasiyozidi matano.

         

·        Halmashauri Kuu ya Taifa itafikiria na hatimaye kupiga kura za siri za kupendekeza majina yasiyozidi matatu na kuyawasilisha mbele ya Mkutano Mkuu wa Taifa kwa uteuzi wa mwisho.

                                                         

·        Mkutano Mkuu wa Taifa utapiga kura za siri kumchagua mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano kwa tiketi ya CCM.

                            


          B.       Utaratibu wa kumpata Mgombea Urais wa Zanzibar

         

                   Kuhusiana na namna ya kumpata Mgombea Urais wa Zanzibar, Halmashauri Kuu ya Taifa imeamua utaratibu ufuatao:-

 

·        Wanachama wote wanaopenda kuwania nafasi hiyo na wanazo sifa zinazotakiwa, wajaze fomu na kuziwasilisha kwa Katibu Mkuu wa CCM katika muda uliowekwa, pamoja na kupata wadhamini na kulipa ada kwa viwango vilivyowekwa katika Kanuni za sasa.

 


·        Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa itawachuja wagombea wote kwa kupitia sifa zao na kutoa maoni na mapendekezo yake mbele ya Kamati Kuu, bila kuwapigia kura wagombea hao.

 

·        Kamati Kuu itafikiria na kupendekeza majina yasiyozidi matatu na kuyawasilisha mbele ya Halmashauri Kuu ya Taifa kwa uteuzi wa mwisho.

 

·        Halmashauri Kuu ya Taifa itapiga kura za siri za kuchagua jina moja la mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM.

 

          C.       Suala la Wakati Muafaka wa Kuteua na Kutangaza Wagombea wetu wa Urais wa Jamhuri ya Muungano pamoja na Wagombea Urais wa Zanzibar

 

Halmashauri Kuu ya Taifa ilikubali kwamba utaratibu unaotumika katika kuteua wagombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano na wa Zanzibar ufanyike ifuatavyo:-

 

                   (a)      Kwamba zoezi zima la uteuzi wa wagombea wa ngazi hiyo lifanyike na kukamilika, angalau miezi sita kabla ya siku ya Uchaguzi wenyewe.


                  

                   (b)     Kwa kuwa Uchaguzi Mkuu hufanyika mwishoni mwa mwezi Oktoba wa mwaka husika, zoezi la uteuzi wa wagombea wa ngazi hiyo liwe limekamilika ifikapo tarehe 30 Aprili ya mwaka wa Uchaguzi Mkuu.

 

          D.      Utaratibu wa Kuwapata Wagombea Ubunge/Uwakilishi:

 

                   Halmashauri Kuu ya Taifa imeamua kuweka utaratibu mpya ufuatao wa kuwapata wagombea Ubunge/Uwakilishi katika hatua ya kura za maoni:

                  

                             Kura za maoni zipigwe na Mkutano Mkuu wa Jimbo la Uchaguzi utakaowashirikisha Viongozi wengi zaidi wa CCM kutoka katika Kata/Wadi, pamoja na Matawi.

 


          E.       Utaratibu wa Kuwapata Wagombea Udiwani:

         

                   Halmashauri Kuu ya Taifa imeamua uendelee utaratibu wa sasa ambapo wagombea wanapigiwa kura za maoni katika Mikutano ya Wanachama wote wa Matawi ya Kata/Wadi inayohusika.


         


6.0      KUHUISHA MUUNDO WA CHAMA CHA MAPINDUZI


 

Halmashauri Kuu ya Taifa baada kupokea taarifa ya Kamati ya Kuhuisha Muundo wa Chama Cha Mapinduzi na kuzingatia mapendekezo ya Kamati Kuu, ilipitisha maamuzi yafuatayo ya msingi kuhusiana na uhuishaji wa muundo wa Chama Cha Mapinduzi:

 

 

 

 

 

          A.      CCM Kuendelea kuwa Chama cha Umma (Mass Party):

 

                    Chama Cha Mapinduzi kiendelee kuwa Chama cha Umma kama ambavyo kimekuwa siku zote tangu enzi za TANU na ASP.

 

          B.       Marekebisho ya Idara za Makao Makuu

 

                    Yamefanywa marekebisho ya Idara za Makao Makuu ya Chama ambapo sasa zitakuwapo Idara zifuatazo:-

 

                   (a)      Organaizesheni (badala ya Mipango),

                   (b)     Itikadi na Uenezi (badala ya Uenezi),

                   (c)      Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (Idara mpya),

                   (d)     Uchumi na Fedha (badala ya Fedha),

                   (e)      Utawala na Uendeshaji.

         

                   Katika ngazi za Mikoa hadi Tawi, Idara hizo zitakuwa na sura zifuatazo:-

 

                   (a)      Organaizesheni (itaongozwa moja kwa moja na Katibu wa CCM wa ngazi husika),

                   (b)     Siasa na Uenezi,

                   (c)      Uchumi na Fedha.

         

7.0     PONGEZI MAALUMU:

 

Halmashauri Kuu ya Taifa ilitoa pongezi zake kwa Kamati ya Kuhuisha Muundo wa Chama Cha Mapinduzi na Kamati ya Kupendekeza Namna Bora zaidi ya kuwapata wagombea wa CCM katika chaguzi za vyombo vya Dola kwa kukamilisha kazi zao kwa ufanisi mkubwa.

 

Kamati ya Kuhuisha Muundo wa Chama Cha Mapinduzi iliyoteuliwa na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ilikuwa na Wajumbe wafuatao:-

 

          (a)      Ndugu Kingunge Ngombale-Mwiru         -        Mwenyekiti

          (b)     Ndugu Omar R. Mapuri                         -        Mjumbe

          (c)      Ndugu Jackson Msome                         -        Mjumbe

          (d)     Ndugu Anna Abdallah                          -        Mjumbe

          (e)      Ndugu Yussuf Mohamed Yussuf             -        Mjumbe


          (f)      Ndugu Amina Salum Ali                       -        Mjumbe

          (g)     Ndugu Juma S. Nkumba                       -        Mjumbe


           (h)     Ndugu Emmanuel John Nchimbi           -      Mjumbe

         

Kamati ya Kupendekeza namna bora zaidi ya kuwapata wagombea wa CCM katika chaguzi za vyombo vya Dola ilikuwa na Wajumbe wafuatao:-

 

 

1.                                      Ndugu Pius Msekwa                      -        Mwenyekiti

2.                                      Ndugu Abdulrahaman Kinana         -        Mjumbe

3.                                      Ndugu Omar R. Mapuri                 -        Mjumbe


4.                                      Ndugu Jackson Msome                  -        Mjumbe

5.                                      Ndugu Mohamed Seif Khatib          -        Mjumbe

6.                                      Dr. Maua Daftari                           -        Mjumbe

7.                                      Ndugu Chrisant Mzindakaya           -        Mjumbe

8.                                      Dr. Mary Nagu                              -        Mjumbe

9.                                      Ndugu Amina Salum Ali                -        Mjumbe

10.                                  Ndugu Pancras Ndejembi               -        Mjumbe

11.                                  Ndugu Haji Omar Kheri                 -        Mjumbe

12.                                  Ndugu Juma S. Nh’unga                -        Mjumbe

 

 

NB:             SIFA ZA MSINGI KUHUSU WAGOMBEA URAIS ZILIZOWEKWA  NA NEC MWAKA 1992

 

1.     Awe na uzoefu mkubwa wa kuongoza Taifa kwa kuzingatia uzoefu wake katika uongozi wa shughuli za Serikali, umma na Taasisi.

 

2.     Awe Mwadilifu, mwenye Hekima na Busara.

 

3.     Awe na angalau kiwango cha Elimu ya Chuo Kikuu au elimu inayolingana na hiyo.

 

4.     Awe mwenye upeo na uwezo mkubwa wa kudumisha, kuimarisha na kuendeleza Muungano wetu, Umoja wetu, Amani na Utulivu wetu na Mshikamano wa Kitaifa.

 

5.     Awe mtu mwepesi wa kuona mbali, asiyeyumbishwa na mwenye uwezo wa kufanya uamuzi wa busara kuhusu masuala nyeti na muhimu ya Taifa kwa wakati unaofaa.

 

6.     Awe na upeo mkubwa na usiotiliwa shaka kuhusu masuala ya Kimataifa ili aweze kuwa kiungo imara kati ya nchi yetu na Dunia yote kwa jumla.

 

7.     Asiwe mtu mwenye hulka ya udikteta au ufashisti bali awe mtu anayeheshimu na kulinda Katiba ya Nchi, Sheria, Utawala Bora, Kanuni na Taratibu za Nchi.

 

8.     Awe mtetezi wa wanyonge, wa Haki za Binadamu, mzingatiaji makini wa maendeleo ya raia wote na asiwe na tamaa ya kujitafutia umaarufu wa mtu binafsi.

 

9.     Awe mstari wa mbele katika kuzifahamu, kuzieleza, kuzitetea na kuzitekeleza sera za CCM na Ilani ya CCM ya Uchaguzi.

 

10. Awe mpenda haki na awe mtu jasiri katika kupambana na dhuluma       

      na maovu yote nchini.

 

11. Asiwe ni mtu ambaye anatumia nafasi yake ya uongozi kujilimbikizia   

     mali.

 

12. Kwa ujumla awe ni mtu anayekubalika na wananchi.

 

13. Awe mtu makini katika kuzingatia masuala ya uwajibikaji wa  

Viongozi/Watendaji na asiyevumilia uzembe katika utekelezaji wa    majukumu/wajibu waliokabidhiwa ili kuinua Nidhamu ya Kazi, Tija na Ufanisi.