Mchango wa sekta ya madini kwa mauzo ya nje umeongezeka maradufu

 

KIPINDI cha miaka kumi iliyopita cha Serikali ya awamu ya tatu kimeshuhudia kufufuka na kukua kwa kasi kwa uzalishaji viwandani, ikiwemo migodi. Makala hii inafafanua mafanikio hayo yaliyochangiwa zaidi na utekelezaji wa sera ya taifa ya ubinafsishaji, na vilevile ufunguaji wa milango kwa mitaji kutoka nje ya nchi. 

Katika kipindi kilichopita, Serikali imetekeleza kwa dhati sera ya ubinafsishaji. Pia iliandaa Sera Endelevu ya Viwanda, Sera  ya Viwanda  Vidogo na Biashara Ndogo na Sera ya Utekelezaji ya Uwezeshaji  wa Wananchi Kiuchumi. Sera zote  hizo zilisaidia sana  kuimarisha  viwanda. Vilevile, yalianzishwa maeneo maalum ya uzalishaji kwa ajili ya kuuza bidhaa nje (EPZ).  Viwanda vingi vimepata wawekezaji wapya wenye uwezo  wa  kuingiza teknolojia mpya na uzoefu wa kuendesha viwanda kisasa.

Matokeo ya hatua hizo za ubinafsishaji wa viwanda ni pamoja na :-

Kuongezeka kwa uzalishaji wa bidhaa viwandani na hivyo  kukidhi  mahitaji ya wananchi. Kwa mfano, uzalishaji wa nguo uliongezeka kutoka  mita za mraba milioni 73.6 mwaka 2000 hadi mita za mraba milioni 109.8 mwaka  2004; usagishaji wa ngano kutoka tani 162,634 mwaka 2000 hadi 333,789 mwaka 2004 ; uzalishaji wa chuma kutoka tani 11,181 mwaka 2000 hadi tani 46,559 mwaka 2004. Ongezeko kubwa, la  uzalishaji  lilipatikana pia katika bia, sigara, mabati, saruji, biskuti na tambi, utengenezaji  wa kamba za katani, uuzaji nje wa samaki wa kusindikwa n.k.

Kuongezeka kwa ukuaji wa sekta ya viwanda kutoka asilimia 4.8  mwaka 2000 hadi asilimia 9 mwaka 2003.

Kuongezeka kwa thamani ya miradi iliyoidhinishwa  kutoka  sh. bilioni 123.8  mwaka 2000 hadi sh. bilioni  239.6 mwaka  2004, ongezeko la asilimia 93.5.

Kuongezeka kwa ajira viwandani kutoka 153,938 mwaka 2000 hadi 207,571 mwaka 2003, ongezeko la asilimia 34.8.

Madini

Serikali katika kutekeleza Ilani ya CCM ya 2000 katika sekta ya  madini iliongozwa na Sera ya Madini ya mwaka  1997 ; Sheria ya madini ya mwaka 1998 na  kanuni za mwaka 1999.  Sera hiyo ililenga kuvutia wawekezaji binafsi. Azma ya kuwavutia wawekezaji imefanikiwa kwa kiwango  kikubwa. Utafiti  wa madini uliongezeka  na migodi mikubwa ilifunguliwa. Ushiriki wa  sekta binafsi katika utafutaji na uchimbaji wa madini umewezesha kuwepo kwa migodi yenye hadhi ya kimataifa kama Geita Gold Mine, Kahama Mining, Buhemba Gold Mine (Musoma), Afrika Mashariki  Gold Mine (Tarime) na Tulawaka  Gold Mine (Biharamulo).

Kwa upande wa  wachimbaji wadogo wadogo, wamekuwa wakipatiwa mafunzo katika nyanja mbali  mbali kama uchimbaji salama wa madini, utunzaji wa mazingira, utafutaji  wa  madini, biashara ya madini, masuala ya afya n.k. Pia, wachimbaji wadogo wadogo  walifundishwa namna ya kupata  mikopo kutoka SIDO  na taasisi nyingine zinazotoa mikopo. Kutokana  na hatua hizo, sekta ya madini imeweza kupata mafanikio yafuatayo katika kipindi cha 2000-2005:-

Tanzania kwa sasa inazalisha takriban tani 50 za dhahabu kwa mwaka na kuifanya kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza katika uzalishaji wa  dhahabu Barani Afrika.

Sekta ya Madini imekuwa kati ya sekta zenye kasi kubwa ya ukuaji. Ukuaji uliongezeka  kutoka asilimia 13.9 mwaka  2000 hadi asilimia 14.1 mwaka 2004, ikiwa imefikia kilele cha asilimia 17 mwaka 2003.

Mchango wa sekta ya madini katika mauzo ya nje uliongezeka kutoka asilimia 26.9 mwaka 2000 hadi asilimia 51.4 mwaka 2004, na hivyo kuongoza katika muzo ya nje ikilinganishwa na mauzo  ya bidhaa nyingine.

Mchango wa sekta ya madini kwa mapato ya fedha za kigeni umekua  kutoka dola za Marekani  milioni 178.2 mwaka 2000 hadi dola milioni 543 mwaka 2004. Hili ni ongezeko la asilimia  204.8.

Watafutaji na wachimbaji madini wakubwa na wadogo hulipa ada  za  leseni na mrabaha kwa madini wanayouza. Tangu mwaka 2000, maduhuli  ya Serikali yaliyokusanywa na Wizara yaliongezeka kutoka sh. bilioni 7.441 mwaka 2000/01 hadi sh. bilioni 22.786 mwaka 2003/04, likiwa  ni ongezeko  la asilimia 206.2

Migodi mikubwa imekuwa ikisaidia katika utekelezaji wa miradi ya jamii  kama vile afya, elimu, maji na barabara. Huduma hizo huvinufaisha vijiji vinavyozunguka migodi hiyo. Baada ya uchimbaji madini kufikia kikomo, majengo ya migodi  hiyo yatatumika kwa huduma za jamii kama kuanzisha shule au huduma nyingine kulingana na vipaumbele  vya wanajamii katika eneo husika.

Ajira rasmi katika migodi mikubwa imeongezeka kutoka 1,781  mwaka 1997 hadi 7,082 mwaka 2003, likiwa ni ongezeko la asilimia  297.6. Pia, mwaka 2003 inakadiriwa kuwa zilizalishwa nafasi 42,000 za  ajira  nje ya   migodi kutokana na kuwapo  kwa migodi  hiyo. Kwa upande wa kujiajiri, inakadiriwa walikuwapo wachimbaji wadogo zaidi ya 500,000 waliokuwa wamejiajiri.

Biashara

Biashara ni muhimu sana katika jitihada za kuongeza pato la wananchi na kuendeleza uchumi. Dunia ya sasa ya utandawazi imeegemea sana kwenye biashara ya kimataifa. Kwa kutambua hilo, Serikali imeweka msukumo wa pekee  katika kukuza mauzo ya bidhaa zetu nje na kuongeza wingi na ubora wa bidhaa katika soko la ndani. Kutokana na msukumo huo, hatua zifuatazo zilichukuliwa katika kipindi kilichopita :-

Kuondoa kero ya ulipaji wa kodi ya makisio kabla ya hata kuanza biashara yenyewe. Serikali iliweka wazi masharti ya kuanzisha biashara, viwango vya ada kwa aina mbali mbali za biashara na hivyo kupunguza vishawishi vya rushwa.

Kushiriki katika majadiliano kuhusu mfumo wa biashara kimataifa. Julai, 2001, Tanzania iliandaa mkutano wa mawaziri wa biashara kutoka nchi maskini sana  uliofanyika Zanzibar. Tamko Rasmi la Zanzibar liliweka msimamo wa pamoja katika mikutano ya Shirika la Biashara la Dunia (WTO) ya Doha, Qatar, Novemba, 2001 na Cancun, Mexico, Septemba 2003. Ushirikiano huo ulizuia upitishaji wa ajenda ambazo zingeendeleza na kuimarisha maslahi ya nchi kubwa dhidi ya nchi changa. Mchango wa Tanzania katika kujenga nguvu hii ulikuwa mkubwa.

Ili kukuza maendeleo ya kiuchumi, na hasa viwanda na biashara, Serikali iliendelea kushirikiana na nchi jirani, hasa za Afrika Mashariki kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).

Kutunga Sheria ya kudhibiti uingizaji holela wa bidhaa kutoka nje ili kulinda nchi yetu isigeuzwe kuwa dampo la bidhaa hafifu kutoka nje.

Kuanzisha maeneo huru ya biashara

Kuwasaidia wafanyabiashara wadogo wadogo katika taaluma za ujasiriamali, namna ya kupata mikopo kutoka mifuko mbali mbali na benki, na kurahisisha taratibu za kupata mikopo chini ya Mkakati wa Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.

Kupunguza mlolongo wa leseni kabla ya kuanzisha biashara.

Kutungwa sera na mikakati ifuatayo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika kuwezesha ukuaji wa biashara kubwa na ndogo:-

(i) Sera ya Utekelezaji ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.

(ii) MKUKUTA

(iii) MKURABITA

Kutokana na hatua hizo na nyinginezo, mafanikio makubwa yamepatikana yakiwemo yafuatayo:

Ukuaji wa sekta ya biashara uliongezeka kutoka asilimia 6.5 mwaka 2000 hadi asilimia 7.4 mwaka 2004.

Mauzo ya nje yaliongezeka kutoka dola milioni 663.3 mwaka 2000 hadi dola milioni  1,142 mwaka 2003, likiwa ni ongezeko la asilimia 72.2

Biashara imechangamka zaidi nchini.