Kwa kuwa pamoja na wanaochochea vurugu Zanzibar, Marekani inazidi kulewa ubabe
Na Lucas Kisasa
ALHAMISI ya wiki iliyopita, ubalozi wa Marekani nchini Tanzania ulitoa taarifa
nzito na kali kuhusu uchaguzi wa Zanzibar, taarifa ambayo kimsingi imeweka wazi
kuwa serikali ya Marekani haiyatambui matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika Oktoba
30, mwaka huu ambapo CCM imeibuka mshindi kwa Rais Amani Abeid Karume kutetea tena
nafasi yake.
Taarifa hiyo ya ubalozi wa Marekani kwa vyombo vya habari imeainisha mambo kadhaa
inayodai kuwa yalikiukwa katika mchakato wa uchaguzi wa Zanzibar na kwamba
“inaiomba” serikali ya Tanzania kufanya uchunguzi wa kina na ulio wazi kuhusu
tuhuma za ukiukwaji huo.
Marekani inadai katika taarifa yake kuwa kulikuwepo na “vitendo kadhaa vya watu
kupiga kura zaidi ya mara moja, pamoja na hali iliyoashiria kwamba watu wa nje
waliruhusiwa kupiga kura kinyume na sheria. Vyombo vya usalama vilionekana
vikipiga kura, ingawa vidole vyao vilikuwa na alama ya wino usiofutika, hii
ikionyesha kuwa walikuwa tayari wamekwishapiga kura”.
Taarifa hiyo inaendelea kudai kuwa “daftari la kudumu la wapigakura halikutolewa
mpaka siku ya kupiga” na kwamba “hii ina maana kwamba Wazanzibari wengi hawakupata
fursa ya kuhakikisha kama majina yao yalikuwa kwenye orodha hiyo kabla ya siku ya
kupiga kura”.
Kutokana na madai hayo ya kinachoitwa ni ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi,
Marekani inaainisha katika taarifa hiyo kuwa ndiyo maana “Marekani bado inatiwa
wasiwasi na ukiukwaji huu na mwingine uliojitokeza, na inasita kutoa uamuzi kuhusu
uchaguzi huu kama ulikuwa huru na wa haki mpaka hapo athari zake juu ya matokeo
zimefafanuliwa. Kwa sababu hiyo Marekani haikuhudhuria sherehe ya kuapishwa Rais
iliyofanyika Zanzibar siku ya Jumatano”.
Kimsingi madai hayo ya Marekani, kupitia ubalozi wake wa hapa nchini, yanaoana na
madai ya chama cha upinzani cha CUF kilichoshindwa uchaguzi huo, na ambacho mara
tu baada ya upigaji huo wa kura kumalizika, na hata kabla ya Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar haijatoa matokeo, tayari kilijitangazia ushindi.
Kwamba Marekani, taifa kubwa pekee lililobaki duniani lenye nguvu kubwa za kijeshi
na kiuchumi, limetoa msimamo huo bila shaka hiyo imekuwa ni faraja kubwa kwa chama
cha CUF katika mikakati yake “ya kuifanya Tanzania nzima isikalike” kwa “kuleta
janga kubwa la kitaifa”.
Kwa ujumla wake ilichofanya Marekani kwa kutoa msimamo wa aina hiyo ni kuchochea
machafuko nchini, siyo kingine. Ilichofanya Marekani ni uchochezi.
Msimamo huo wa Marekani ndio ambao ulikuwa unaliliwa na CUF ili iwe ndiyo ngao ya
kufanya uasi nchini. Na wameanza uasi huo kwa kutoa “ultimatum” kwa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba wanataka katika muda wa siku 45 zijazo
matokeo ya uchaguzi Zanzibar yafutwe na ikibidi, eti uchaguzi huo urudiwe.
Kwa wachambuzi wa masuala ya siasa za kimataifa msimamo huo wa Marekani kuhusu
Zanzibar haushangazi kwani imekuwa ni hulka kwa taifa hili kubwa duniani kuingilia
mambo ya ndani ya nchi nyingine kinyume na taratibu na sheria za kimataifa.
Ubabe (wa Marekani) hivi sasa ndio unaotawala dunia. Marekani imelewa ubabe ambapo
hivi sasa taifa hili limekuwa sawa na “mwendawazimu aliyepewa rungu”.
Marekani kwa namna yoyote ile haina haki yoyote kuingilia mambo ya Tanzania. Wala
hakuna mtu aliyeialika Marekani itoe tamko kuhusu uchaguzi wa Zanzibar.
Yako makundi kadhaa ya kimataifa yaliyoshiriki katika uangalizi wa uchaguzi wa
Zanzibar yaliyotamka wazi kuwa ukiacha kasoro ndogo ndogo zilizokuwepo kwa ujumla
wake uchaguzi huo ulifanyika kwa uhuru na haki.
Miongoni mwa makundi yaliyotamka kuwa uchaguzi wa Zanzibar ulikuwa huru na wa haki
ni Umoja wa Afrika (AU); Jumuia ya Madola; Jumuia ya Maendeleo ya nchi za Kusini
mwa Afrika (SADC) na kundi la waangalizi lililowakilisha makanisa.
Lakini kwa Marekani taarifa za makundi haya mengine zilikuwa ni za uongo isipokuwa
ile ya National Democratic Institute (NDI) na ambayo ripoti yake ndiyo iliyopewa
umuhimu na taifa hili. Kwamba Marekani imezingatia ripoti ya taasisi moja tu ni
jambo linaloshangaza mno na kimsingi ni kielelezo cha wazi kuwa taifa hilo lina
ajenda ya siri dhidi ya Tanzania.
Hoja zote zilizoainishwa na Marekani kuhusu uchaguzi wa Zanzibar zilishajibiwa na
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar wakati wa kutangaza matokeo ya uchaguzi huo ilipoanza
kwanza kwa kujibu madai ya CUF.
Kwa ufupi ni kwamba madai ya Marekani na CUF kuhusu kinachoitwa ukiukwaji wa
taratibu za uchaguzi hayana msingi, bali yamelenga katika kupotosha ukweli wa
kilichotokea Zanzibar wakati wa uchaguzi huo.
Marekani ina tabia moja mbaya nayo ni kwamba hutaka mataifa yote duniani yafuate
inachokitaka. Hujiita kuwa ni taifa la kidemokrasia, lakini ukweli ni kwamba
uongozi wa Marekani uko mbali na demokrasia kinyume kabisa na inavyohubiri.
Demokrasia ya Marekani ni ya ubabe na jeuri.
Bado tuna kumbukumbu ya kilichotokea huko Marekani katika uchaguzi wake mkuu wa
mwaka 2000 pale ukiukaji mkubwa wa taratibu ulipojitokeza ambapo watu wengi kwa
maelfu walinyimwa haki ya kupiga kura, huku pia kukiwepo na wapigakura
waliobainika kuwa walikuwa ni marehemu.
Kimsingi kulikuwa na wizi mkubwa wa kura katika uchaguzi huo wa mwaka 2000 mpaka
mahakama kuu ya taifa hilo duniani ikaamua kuingilia kati kwa kumtangaza George
Bush kuwa rais na kumtupa kando mpinzani wake kutoka chama cha Democrat, Al Gore.
Kama wizi huo wa kura wa mwaka 2000 haukutosha, tatizo hilo lilijitokeza tena
katika uchaguzi wa mwaka jana ambapo taratibu nyingi za uchaguzi zilikiukwa na
kuleta aibu kubwa kwa taifa hilo kubwa duniani.
Pamoja na ukiukwaji huo mkubwa wa taratibu za uchaguzi wa Marekani kwa mwaka 2000
na 2004, hakuna kiongozi wa nchi nyingine duniani aliyeingilia kati suala hilo kwa
kutangaza kutoyatambua matokeo hayo. Viongozi wengi wa nchi nyingine hawakufanya
hivyo kwa kuwa walielewa kuwa kufanya hivyo ingekuwa ni kuingilia mambo ya nchi
nyingine.
Lakini Marekani haina aibu. Ni taifa linaloongozwa kwa misingi ya ukandamizaji, si
tu kwa mataifa mengine bali hata kwa watu wake. Haki za Wamarekani weusi zimeanza
kuwepo nchini mwao kuanzia miaka ya 1960 tu.
Kabla ya hapo Marekani ilikuwa sawa na Afrika Kusini katika suala la ubaguzi wa
rangi. Wamarekani weusi walikuwa ni raia daraja la mwisho katika nchi yao wenyewe.
Walikuwa wana shule zao; mabasi yao; baa zao; na kadhalika, huku wakiwa
hawaruhusiwi kugombea madaraka bali waendelee katika “taaluma” yao katika muziki
na michezo kama mbio, ngumi na mpira wa kikapu.
Kati ya mataifa yote, Marekani ndiyo inayonuka damu kwa kuua mamilioni ya watu
duniani wasio na hatia yoyote. Iliua maelfu ya watu huko Vietnam katika miaka ya
1960. Hivi sasa inaendelea kuua watu kwa maelfu Irak, huku wachambuzi wa masuala
ya kisiasa duniani wakiainisha kuwa mpaka sasa zaidi ya watu 150,000 wamekufa
katika nchi hiyo ya Mashariki ya Kati.
Marekani ni taifa linalokataza nchi nyingine zisiwe na silaha za maangamizi
zikiwemo za nyuklia, lakini yenyewe imejilimbikizia silaha lukuki za maangamizi
ambapo zinaweza kuiangamiza dunia mara 20. Na si suala la kujilimbikizia silaha
tu, bali Marekani ndiyo nchi ya kwanza duniani kutumia silaha za nyuklia. Mabomu
ya Atomiki yaliyotupwa katika miji ya Hiroshima na Nagasaki huko Japan wakati wa
vita vya pili vya dunia, Agosti 1945, na kuua zaidi ya watu 200,000 ilikuwa kazi
ya Marekani.
Katika vita vya Vietnam, Marekani ilitumia silaha za maangamizi, yakiwemo mabomu
ya sumu ya ‘napalm’, kuwaua wananchi wa Vietnam na wengine bado wanaendelea kufa
pole pole kwa magonjwa kutokana na sumu hizo. Picha ya mtoto wa kike wa Vietnam
akiwa uchi wa mnyama na akikimbia, huku akiwa ameunguzwa vibaya na mabomu, bado
iko katika kumbukumbu za watu wengi duniani.
Marekani imekuwa ikisema kuwa inaendesha mapambano dhidi ya ugaidi duniani. Sawa,
lakini ugaidi uliopo duniani hivi sasa unazalishwa na nani? Unazalishwa na
Marekani yenyewe kwa kuendesha vitendo vya kibabe na uonevu kwa baadhi ya nchi
duniani.
Marekani ndiyo iliyoongoza majeshi ya kimataifa katika kuishambulia nchi iliyokuwa
ikiitwa Yugoslavia na hatimaye kumkamata Rais wa nchi hiyo, Slobodan Milosevic,
ambaye sasa anahukumiwa na kinachoitwa mahakama ya kimataifa.
Marekani hiyo hiyo ndiyo iliyoivamia Irak kwa kisingizio kuwa nchi hiyo ilikuwa na
silaha za maangamizi, jambo ambalo limekuja thibitika kuwa ni uongo. Aliyekuwa
Rais wa Irak, Saddam Hussein, alikamatwa na majeshi ya Marekani na sasa
anashitakiwa na kinachoitwa mahakama ambayo imeundwa na Marekani.
Jenerali Noriega wa Panama alikamatwa akiwa katika ikulu yake na hivi sasa yuko
jela Marekani. Ni Marekani ndiyo iliyoishambulia nchi ndogo ya Grenada na kuuondoa
uongozi wa nchi hiyo.
Inawezekana ni kweli Milosevic, Saddam Hussein na Jenerali Noriega walikuwa na
makosa yao, lakini pamoja na hayo Marekani haikuwa na haki kuzishambulia nchi hizo
na kuwakamata viongozi wake.
Hivi sasa Marekani na Uingereza zimemvalia njuga Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe
kwa kumuita ni dikteta na king’ang’anizi wa madaraka. Kosa la Mugabe ni nini? Ni
uamuzi wake wa kuongoza mageuzi makubwa ya ardhi ya nchi hiyo kwa kuwanyang’anya
ardhi walowezi wa kizungu na ardhi hiyo kugawiwa kwa wananchi wazalendo waliokuwa
hawana ardhi katika nchi yao wenyewe.
Wakati Marekani inajidai kupinga ugaidi duniani, taifa hilo kubwa ndilo
linaloongoza kwa kuendesha ugaidi wa dola kwa kuzishambulia nchi nyingine na
kukamata viongozi wake.
Mwanamapinduzi na kiongozi wa Chile, Salvador Allende, aliuawa katika miaka ya
1970 kutokana na njama za Marekani. Tunafahamu kilichotokea huko Congo pale
mwanamapinduzi Patrice Lumumba alipouawa katika miaka ya 1960 kutokana na
kinachosadikiwa kuwa ni njama za Marekani na nchi nyingine za magharibi.
Watu kwa maelfu waliuawa nchini Angola kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe
ambavyo vilikuwa vinachochewa na Marekani kwa kumuunga mkono gaidi Jonas Savimbi.
Kwa hiyo ni dhahiri Marekani inanuka harufu ya damu, inanuka damu za maelfu ya
raia wasio na hatia wanaouawa katika nchi mbalimbali kutokana na njama za taifa
hilo kubwa.
Viongozi wa Marekani ndio kwa hakika wanaostahili kushitakiwa kwenye mahakama za
kimataifa kwa dhambi za serikali yao dhidi ya mataifa mengine duniani. Katika
kumshitaki Milosevic na Saddam kwenye mahakama zinazoitwa ni za kimataifa pengine
Rais George Bush naye alistahili kushitakiwa katika mahakama hizo kwa unyama wa
nchi yake dhidi ya nchi nyingine duniani.
Ubabe huu wa Marekani ndio unaowafanya Wamarekani wengi kuchukiwa katika nchi
mbalimbali duniani. Imefika wakati katika baadhi ya nchi duniani Wamarekani
huogopa na kushindwa kujitambulisha utaifa wao. Wanawindwa mithili ya panya
walioingia ndani ya nyumba.
Marekani haipendi nchi na viongozi wenye msimamo. Marekani ni nchi ambayo hupenda
kuleta uchochezi na yenyewe kunufaika kiuchumi kutokana na machafuko katika nchi
mbalimbali yaliyojitokeza kwa uchochezi wake.
Kwa msimamo wa kuiunga mkono CUF kuhusiana na uchaguzi wa Zanzibar ni dhahiri
Marekani inataka kuiona Tanzania ikiathirika na machafuko. Ni jambo linaloudhi
kuona kuwa Marekani inayojifanya kuwa ndiye kinara wa demokrasia duniani na
inayoendesha mapambano dhidi ya ugaidi ndiyo inakuwa na msimamo wa kukiunga mkono
chama cha siasa chenye mwelekeo wa ugaidi.
CUF wameshatangaza kuwa watahakikisha kuwa Tanzania inakumbwa na janga la kitaifa.
Wanachomaanisha hapa bila shaka ni kuhakikisha kuwa yanakuwepo machafuko nchini
yanayoandamana na umwagaji wa damu, ambayo kwa msimamo wa sasa, yatakuwa
yamebarikiwa na Marekani. Na hii ikitokea damu ya Watanzania watakaouawa kutokana
na vurugu zitakazotokea iwe pia mikononi mwa Wamarekani wa kizazi hiki na vizazi
vyao vyote vijavyo.
Simu: 0744-309858
E. mail:
kisasa2000@yahoo.com