Mzumbe wamkumbuka Baba wa Taifa
Waandaa kongamano kuzungumzia maadili na uongozi
Washauri jamii imuenzi kwa kufuata maadili na haki
Wanaotuhumiwa kwa rushwa na ukiukaji maadili Wajiengue katika uongozi
CHUO Kikuu cha Mzumbe, Morogoro, juzi kiliandaa kongamano la kumbukumbu ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere ikiwa ni miaka sita tangu kufariki kwake mwaka 1999. Katika makala hii Mwandiashi Wetu EPSON LUHWAGO aliyehudhuria kongamano hilo amaelezea yaliyojiri na ushauri uliotolewa katika kumuenzi kiongozi huyo mwasisi wa taifa la Tanzania.
KWA mara ya nne mfululizo, Chuo Kikuu cha Mzumbe kilichoko Morogoro, juzi kiliandaa kongamano la nne la kumkumbuka Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere lililofanyika chuoni hapo, kilomita 25 kutoka Morogoro mjini.
Katika kongamamo hilo, washiriki walipata uhondo wa mada mbalimbali zilizotolewa na wasomi wakiwemo wanazuoni bingwa waliobobea katika taaluma mbalimbai kama vile siasa, utawala, elimu na sosholojia.
Waliohudhuria kongamano hilo ni pamoja na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe na mwanasiasa mkongwe nchini, Ibrahim Kaduma; Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Sokoine, Profesa David Mwayusa; Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Profesa Moses Warioba.
Wengine ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Profesa Joseph Kuzilwa; Mrajisi wa Chuo, Profesa Hamisi Mahigi; Mrajisi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Profesa Uswege Mwinga na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kiislamu Morogoro, Profesa Saidi Iddi.
Pia walikuwepo maporofesa, wahadhiri waandamizi na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, wanafunzi na wanajamii ya chuo kikuu hicho kwa jumla.
Katika kongamano hilo lililokuwa na kaulimbiu “Uongozi na Maadili kwa Mtazamo wa Nyerere”, jumla ya mada tano ziliwasilishwa na kujadiliwa.
Mada hizo na waliotoa kwenye mabano ni Mfumo wa Siasa wa Vyama Vingi na Maendeleo ya Uongozi wa Demokrasia Tanzania (Profesa Gaudens Mpangala), Mwalimu Nyerere Kiongozi Mwenye Shujaa na Mfano wa Kuigwa (Dk. Christopher Sotta), na Maadili na Uongozi kwa Mtazamo wa Kijinsia: Wajibu wa Mashirika ya Kijamii iliyowasilishwa na Dk. Simeon Mesaki.
Zingine ni Mchango wa Mwalimu Nyerere katika Kuimarisha Maadili kwenye Utumishi wa Umma Tanzania (Dk. Mujwahuzi Njunwa) na Nyerere Kielelezo katika Maadili Duniani iliyowasilishwa na Profesa Matthew Chao.
NENO LA AWALI
Kabla ya kuanza kwa mada hizo, kilitolewa hotuba ya ufunguzi iliyotolewa na Msaidizi Maalum wa Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyeyrere, Gallus Abedi.
Abedi ni mwanasiasa mkongwe tangu enzi za uongozi wa Nyerere na aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali kama vile mkuu wa Mkoa wa Singida na Kilimanjaro, Katibu wa CCM Mkoa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Hata hivyo, kabla ya Abedi kutoa hotuba yake, Profesa Mwakyusa ambaye alikuwa daktari wa Mwalimu Nyerere hadi anafariki, alimkaribisha kwa kutoa maneno machache yaliyobeba ujumbe mzito.
Katika maneno hayo, Profesa Mwakyusa alisema yapo mambo mengi ambayo Watanzania hawana budi kumkumbuka kiongozi huyo mwasisi wa taifa kutokana na kuifanya Tanzania kuheshimika ndani na nje ya nchi.
"Hii inawafanya hata baadhi ya watu walioko huko vijijini kuamini kwamba Nyerere bado yuko hai.
Wahadzabe wanaamini hivyo na wamekuwa wakisema wanamsikia kila siku kwenye redio.
Si hivyo tu hata baadhi ya watu unapofika wakati wa uchaguzi hutaka kumpigia kura Nyerere au chama cha Mwalimu Nyerere. Hii inaonyesha wazi kuwa Nyerere ni kielelezo cha taifa kutokana na mambo mengi aliyoyafanya," alisema.
Kutokana na hali hiyo, alisema Watanzania hawana budi kuyaenzi kwa vitendo mambo aliyoyafanya wakati wa uhai na uongozi wake kwa jumla.
Kubwa katika hayo, Profesa Mwakyusa alisema Nyerere amewaachia watanzania urithi wa kudumu ambao uko katika vitabu na machapisho yake mbalimbali, hivyo hawana budi kuyasoma ili kuelewa alichokuwa akimaanisha kulinganisha na hali halisi ya maisha ya sasa ya Watanzania.
VIGONGO VYA ABEDI
Baada ya maneno hayo ya ukaribisho, Abedi ambaye wakati wa utawala wa mkoloni alikuwa mkalimani wa mahakama, alianza kwa kusema: “Watanzania hawana budi kumuenzi Mwalimu Nyerere kutokana na mchango wake katika kueleleza, kufafanua na kusisitiza imani yake katika haki, usawa, heshima, uhuru na maendeleo ya binadamu”.
Alisema Mwalimu alisisitiza suala la uongozi na maadili kwa viongozi wa ngazi zote. Katika kusisitiza kwake, alisema Mwalimu alikuwa akiweka bayana kuwa uongozi una asili mbili ambazo ni haki na watu.
Katika hilo, kwa mujibu wa Abedi, Mwalimu Nyerere siku zote alikuwa akisisitiza kwamba uongozi wa nchi katika ngazi zote lazima utokane na watu na mtu anapokuwa kiongozi hana budi kuternda haki.
Abedi alimnukuu Mwalimu akisema: "Uongozi wetu hauna budi utokane na watu wa nchi hii bila hila, bila rushwa, bila vitisho na bila ujanja wa aina yoyote. Tunapokuwa katika hali ya uongozi kwa kupitia mlango wa hila, rushwa, vitisho au ujanja wa aina nyingine yoyote, basi hatukutokana na watu wenyewe".
Katika hali hiyo, Nyerere alikuwa akihimiza na kusisitiza kwamba kiongozi yeyote hawezi kuwa kiongozi kamili kama atakuwa hajishughulishi na shida za wananchi hususan watu waliomchagua.
Kwa upande wa haki, Abedi alisema Nyerere alikuwa kiongozi wa mstari wa mbele kutaka haki itendeke kwa watu wote bila kujali nafasi au hali aliyo nayo mtu fulani.
Alisema Nyerere hata baada ya kuondoka madarakani, hakusita kutoa msimamo wake alipokuwa akiona mambo ndani ya serikali au Chama yanaendeshwa bila kufuata utaratibu.
Alitoa mfano wa mwaka 1994 alipotunga kitabu cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania. Alifanya hivyo baada ya kuona kuna hatari ya nchi kuyumba kutokana na mambo mbalimbali yakiwemo ya ukiukwaji wa sheria na katiba ya nchi.
Kiongozi huyo wa siku nyingi serikalini hakuishia hapo. Alisema Nyerere alikuwa mkali pindi alipokuwa akiona maadili yanakiukwa kwa viongozi wake. Alisema hakuwa na huruma kwa mtu aliyekuwa akienda kinyume na maadili.
VIONJO VYA MADA
Profesa Mpangala kutoka Taasisi ya Taaluma ya Maendeleo (IDS) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika
mada yake alisema Nyerere alikuwa kiongozi aliyekuwa akisisitiza demokrasia na utawala bora.
Profesa Mpangala alitoa mfano wa Mwalimu alivyosisitiza juu ya misingi ya demokrasia, uongozi bora na kuwa mtu asiyependa rushwa wala kujinufaisha.
Alisema Mwalimu Nyerere alisisitiza suala la demokrasia na uongozi bora hata wakati wa mfumo wa chama kimoja ambapo uchaguzi ndani ya chama na serikali ulikuwa ukifuata misingi hiyo. Alisema Mwalimu alikuwa akisisitiza uongozi bora lazima utokane na watu.
"Ingawa Mwalimu alikuwa kiongozi na mwanzilishi wa mfumo wa chama kimoja, busara zake zilimfanya kukubali kwamba mawimbi yaliyoikumba Afrika na dunia nzima juu ya mabadiliko ya kisiasa yalikuwa hayakwepeki na hivyo kushauri Tanzania pia kubadilika na kuingia katika mfumo wa vyama vingi mwanzoni mwa miaka ya 1990," alisema.
Dk. Simeon Mesaki wa Idara ya Sosholojia ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika mada yake juu ya Maadili na Uongozi katika Mtazamo wa Jinsia, alisema Mwalimu Nyerere alikuwa mfano wa viongozi walioongoza kwa kufuata misingi ya maadili na uadilifu.
Kwa masuala ya kijinsia, Dk. Mesaki alisema tangu wakati wa kupigania uhuru, Mwalimu Nyerere alikuwa mstari wa mbele katika kupigania haki za wanawake.
Alisema katika Azimio la Arusha, mathalan, Mwalimu alielezea usawa baina ya wanawake na wanaume na kusisitiza kuwa wanawake hasa waishio vijijini wanafanya kazi kwa muda mrefu kuliko mtu yeyote nchini.
Hata katika maendeleo, kwa mujibu wa Dk. Mesaki- Mhadhiri Mwandamizi wa Socholojia, Nyerere alisisitiza kama ifuatavyo juu ya suala la usawa hasa kwa wanawake;
“ Kama tunataka nchi yetu iwe na maendeleo ya haraka, ni muhimu wanawake wakaishi katika hali ya usawa sambamba na raia wenzao ambao ni wanaume”.
Hai hiyo inaonyesha bayana kwamba Nyerere alikuwa mtu anayezingatia suala la usawa wa kijinsi hata kabla harakati za watu mbalimbali duniani hazijaanza na kuota mizizi.
Dk. Sotta, Mhadhiri Mwandamizi wa Kitivo cha Utawala na Uongozi cha Chuo Kikuu cha Mzumbe alimwelezea Nyerere kuwa alikuwa kiongozi shujaa na aliyejitoa kuwatumikia watu wake.
Alisema sifa nyingine inayomfanya Nyerere kuonekana tofauti na wengine ni uwezo mkubwa wa kuchambua mambo kwa kutumia nadharia mbalimbali ambazo zilikuwa na mantiki.
Katika suala la maadili, Profesa Chao wa Taasisi ya Taaluma ya Maendeleo ya Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema Nyerere alikuwa kielelezo cha maadili mema duniani.
Alizitaja sababu zilkizomfanya kuwa na sifa hiyo kuwa ni uwezo wake wa kujifunza kwa kina matatizo yanayoikabili jamii, kusikiliza masuala mbalimbali, utekelezaji katika kutatua matatizo ya kijamii na kushiriki kwake katika mgawanyo wa madaraka.
Sifa ya ziada ya Mwalimu Nyerere, kwa mujibu wa Profesa Chao, katika mambo hayo ni kuwa mbunifu katika kukabiliana na chanamoto za matukio na itikadi zilizokuwa zikitokea kila wakati.
Dk. Njunwa kwa upande wake alisema Nyerere alikuwa mstari wa mbele kuhakikisha maadili katika utumishi wa umma yanazingatiwa na kufuatwa ipasavyo.
ALIKUWA MKAMILIFU?
Kama ilivyo kwa binadamu yeyote asivyo mkamilifu, washiriki walieleza kwamba Nyerere alikuwa na udhaifu wake katika dhana na mambo aliyoyaanzisha, kutekeleza na hata kuyaamini. Pamoja na udhaifu huo, washiriki hao walikubaliana kwamba mambo mengi aliyoyaanzisha yameleta mafanikio tofauti na yale ambayo yameonekana kuwa hayakufaa kwa mtazamo wa watu mbalimbali.
Kutokana na hali hiyo, walisema Nyerere hana budi kuenziwa kwa mambo aliyoyafanya kwa taifa hili na yale ambayo yalikuwa na udhaifu yachukuliwe kama changamoto katika ujenzi wa taifa linalofuata haki, usawa, maadili na uongozi bora kama alivyokuwa akisisitiza juu wakati wa uhai wake.
MAMBO YAKE YANAFUATWA?
Tofauti na alivyohimiza Nyerere katika maadili na uongozi, viongozi wengi wa sasa, kwa mujibu wa washiriki, wameshindwa kufuata maadili ya uongozi na hivyo kwenda kinyume na dhana ya Nyerere.
Baadhi ya washiriki waliochangia kwenye kongamano hilo walieleza wazi kwamba hivi sasa watu wengi wanaingia madarakani siyo kuwatumikia wananchi bali kwa manufaa binafsi.
Walisema hali hiyo inajionyesha nyakati za uchaguzi ambapo mamalamiko mengi yamekuwa yakijitokeza juu ya watu kutumia fedha kuingia madarakani. Hali hiyo, kwa mujibu wa washiriki inaashiria kwamba maadili ya taifa yanamomonyoka kwa kasi kubwa.
Michango hiyo ya washiriki pia ilihanikizwa na igizo lilionyesha watu wanavyogombea kuingia madarakani huku wakitumia mbinu mbalimbali za kuchafuana na kupigana vita vya maneno baina yao.
WANG’ATUKE
Abedi katika hotuba wyake alitoa ‘ushuri wa bure’ kwamba waliopewa dhamana katika nafasi mbalimbali hawana budi kujiuzulu nyadhifa zao pindi wanapotiliwa shaka kuwa wamekiuka maadili ya uongozi, ikiwa ni pamoja na kujihusisha na vitendo vya rushwa.
Abedi alisema viongozi katika ngazi mbalimbali wamekuwa wakituhumiwa kukiu kamaadili, zikiwemo tuhuma za rushwa, lakini hakuna hatua zinazochukuliwa ikiwa ni pamoja na kuamua kujiuzulu.
Alisema kwa viongozi kujiuzulu pindi wanapotuhumiwa watakuwa wanatekeleza dhana halisi ya kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa vitendo.
"Umefika wakati watu wakafufua utamaduni wa kung'atuka kama tuhuma za ukiukaji maadili zinawaandama. Suala siyo kusubiri upatikane ushahidi kwani kiongozi anatakiwa wakati wote kuwa mfano wa kutokutiliwa shaka juu ya matendo yake," alisema.