Ni unafiki wapinzani kudai kumuenzi Mwalimu Nyerere wakati wanamchoma kwa matendo yao

 

Na Lucas Kisasa

Kampeni za uchaguzi mkuu ambao sasa umepangwa kufanyika Desemba 14, mwaka huu hivi

sasa zinaendelea kwa kasi kubwa huku vyama vya siasa na wagombea wao wakipitapita

huku na kule kujinadi ili wachaguliwe hii ikiwa ni katika ingwe ya pili ya kampeni

hizo.

Uchaguzi Mkuu ulikuwa ufanyike Oktoba 30, mwaka huu lakini ukaahirishwa kufuatia

kifo cha mgombea mwenza wa nafasi ya urais kwa tiketi ya CHADEMA, Jumbe Rajab

Jumbe, kilichotokea Oktoba 26, mwaka huu.

Kwa upande wa Zanzibar, uchaguzi ulifanyika hiyo Oktoba 30 kama ulivyopangwa kwa

nafasi ya Rais wa Zanzibar na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.

Uchaguzi wa Desemba 14 utakuwa kwa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa

Tanzania; wabunge na madiwani utakaohusisha nchi nzima ikiwemo Zanzibar ingawa

Zanzibar hawatahusika katika kuwachagua madiwani.

Kampeni hizi za sasa na hasa kwa nafasi ya urais wa Tanzania zimeanza kwa kasi

mpya, huku wagombea wote wa nafasi hiyo kutoka vyama 10 vya siasa wakiwa

wamejiandaa kutoa pigo kubwa la mwisho tayari kwa siku hiyo ya uchaguzi mkuu.

Siasa ni mchezo mchafu. Huu ni usemi ambao umezoeleka duniani kuhusiana na masuala

ya siasa na hasa siasa za uchaguzi. Huku vyama vya siasa vikiwa vinadi sera katika

kipindi hiki cha uchaguzi, lakini wakati huo huo wako wanasiasa ambao wanayo

mikakati ya "kupakaziana" kwa lengo la kudhoofisha upande mwingine katika

kinyang'anyiro cha madaraka.

Hivi sasa kwa mfano wako wanasiasa wanaopita huku na huko wakitumia jina la

Mwalimu Nyerere kwa lengo la kujinufaisha kisiasa. Wote tunafahamu umaarufu wa

jina la Mwalimu Nyerere, siyo katika nchi yetu tu, bali kimsingi kwa dunia nzima.

Mwalimu Nyerere ndiye mwasisi wa taifa letu, ni Baba wa taifa hili.

Kwa siasa za Tanzania mtu au tuseme mwanasiasa akitaka kujimaliza mwenyewe basi

amseme vibaya Mwalimu Nyerere. Ni kweli wako wanasiasa ambao hawakubaliani au

hawakukubaliana na Mwalimu Nyerere, wakiwemo akina Christopher Mtikila na wengine,

lakini kwa ujumla wake wanasiasa wengi wakiwemo wa upinzani hupenda kujipambanua

kuwa wao ndio wako msitari wa mbele katika kumuenzi Mwalimu Nyerere.

Hivi sasa, kwa mfano, wanasiasa kadhaa wa upande wa upinzani wakiwemo wagombea wa

nafasi ya urais katika mikutano yao ya kampeni wamekuwa wakijinadi kuwa wao ndio

wanaomuenzi Mwalimu Nyerere na kwamba Chama tawala, CCM, wamezitupa fikra zote za

Baba wa taifa.

Ni maoni ya safu hii kuwa wale wote , na hasa kwa upande wa upinzani, wanaojinadi

kuwa wao ndio wanaomuenzi Mwalimu Nyerere, ikiwa ndio mkakati wao wa kujipatia

kura, wanatenda kosa kubwa na kimsingi siyo tu kwamba kitendo hicho ni cha unafiki

mkubwa bali pia ni matusi kwa Baba wa taifa.

Katika kuchambua unafiki wa watu wanaolitumia jina la Mwalimu Nyerere ni muhimu

kwanza tukaainisha mambo yale muhimu ambayo Mwalimu Nyerere aliyaamini na

kuyasimamia wakati wa uhai wake.

Kwanza kabisa Mwalimu Nyerere aliipenda nchi yake. Aliipenda Tanzania kwa moyo wa

dhati kabisa na bila unafiki wowote. Katika matendo yake yote kamwe Mwalimu

Nyerere hakuisaliti nchi yake. Aliitetea kwa vitendo. Mwalimu Nyerere hakuwa

tayari kuona Tanzania inadhalilika. Aliitetea hata mbele ya mataifa makubwa na

hasa ya kibeberu. Ni katika enzi za Mwalimu Nyerere ambapo heshima ya Tanzania

ilikuwa juu kutokana na msimamo wake usioyumba.

Sasa hebu tujiulize ni akina nani hao kwa upande wa upinzani wanaodai kuwa

wanamuenzi Nyerere na ambao wanaipenda Tanzania? Hivi kweli kama wanaipenda

Tanzania watathubutuje kutamka hadharani kuwa ikiwa hawatapata madaraka kwa kile

wanachodai kuwa ni kutokana na mizengwe watahakikisha kuwa kunakuwepo na janga la

kitaifa?

Kama kweli wapinzani wanaipenda Tanzania watawezaje kwenda nchi za nje kupiga

kampeni ili Tanzania itengwe na jumuia ya kimataifa na hata kunyimwa misaada ya

kiuchumi? Kama wanaipenda Tanzania kwanini waamue kwa moyo wao wa dhati kabisa, na

siyo kwa bahati mbaya, katika kuchochea maasi Tanzania?

Jambo la pili aliloliamini na kulisimamia Mwalimu Nyerere ni kwamba aliwapenda

wananchi wake. Mwalimu Nyerere aliwapenda Watanzania, na alifanya hivyo kikweli

kweli na kwa moyo wa dhati kabisa. Ajitokeze mpinzani hapa na atuambie kwa moyo

wake wa dhati kama kweli anawapenda Watanzania!

Kwa ujumla, vitendo vya wanasiasa wengi ni kuwa wanawapenda wananchi kwa nadharia

tu, lakini matendo ya wanasiasa hao ni kinyume kabisa na wanachohubiri kwenye

majukwaa ya kisiasa.

Mwalimu Nyerere aliwapenda wananchi na alipenda Watanzania wawe na maendeleo.

Mwalimu alipenda maendeleo ya wananchi na alikuwa msitari wa mbele kuhakikisha

kuwa wananchi wanaondokana na unyonge.

Sasa basi waje hao wanaojidai kuwa wanamuenzi Mwalimu Nyerere na watufahamishe

namna wanavyomuenzi kwa kupenda wananchi na hata maendeleo yao. Watueleze

wamewafanyia nini wananchi. Katika hili wapinzani wanaweza wakaja na hoja kuwa

hawajawafanyia lolote wananchi kwa kuwa hawajapata madaraka. Sawa, lakini je,

wameshawahi kwenda huko vijijini kuhimiza maendeleo ya wananchi? Je, wamekwenda

huko vijijini au hata katika maeneo ya mijini kuishi na wananchi na kuhimiza

miradi ya kuondokana na umaskini?

Ambacho tumekuwa tukikishuhudia kutoka kwa wanasiasa wengi wa upinzani ni pita

pita zao na za hapa na pale huku wakipiga kelele za kwamba eti CCM ni wezi wa kura

kwa hiyo wasipewe madaraka. Wapinzani ni kama wamerogwa. Wanadhani kuwa kelele za

uongo dhidi ya Chama tawala kwamba eti kinapata madaraka kwa hadaa zitawasaidia

wapinzani hao kuingia Ikulu.

Wanachofanya wapinzani ni kulalamika na siyo kuchochea maendeleo. Tena basi wako

baadhi wanakwenda mbali zaidi kwa kuhujumu hata mali, majengo, viwanda na miradi

mbalimbali iliyopo kwa ajili ya wananchi. Hivi watu wa namna hiyo kweli

wanawapenda wananchi?

Katika mgomo huu wa madaktari wa Hospitali kubwa nchini, Muhimbili, ambao umeacha

baadhi ya wananchi wakikosa huduma za matibabu na hata kuhatarisha maisha yao,

wako wanasiasa uchwara waliounga mkono mgomo huo. Wamefanya hivyo kwa sababu za

kisiasa. Wanachojali wanasiasa hao ni maslahi yao na siyo uhai wa wananchi.

Mwalimu Nyerere alipenda na kusimamia amani, umoja na utulivu nchini. Mwalimu

Nyerere alifanya hivyo kwa vitendo. Alikuwa mkali kwa wale wote waliokuwa

wakihatarisha amani, utulivu na umoja wa kitaifa. Baba wa taifa pia alipenda

utawala wa sheria.

Sasa basi asimame mwanasiasa, na hasa wa upande wa upinzani, anayejidai kuwa

anamuenzi Mwalimu Nyerere atueleze ni namna gani anatekeleza aliyoamini Mwalimu

kuhusu suala la amani, umoja, utulivu nchini na utawala wa sheria.

Wanasiasa wengi wa upande wa upinzani wanakwenda kinyume na aliyoamini Baba wa

taifa. Wanachochea vurugu nchini. Wanawahamasisha wanachama na wafuasi wa vyama

vyao walale barabarani eti "mpaka kieleweke". Wanawachochea wafuasi wao waendeshe

vitendo vya hujuma. Na kweli, baadhi ya wafuasi wao wamekuwa wakitekeleza

maelekezo hayo ya wanasiasa wa upinzani katika "kuifanya nchi isitawalike".

Tumeshuhudia mauaji ya kisiasa yakitokea nchini mwetu. Kada wa CCM wa Tawi la

Chama (CCM) la Midizini, Manzese, Dar es Salaam yeye na wanafamilia wake wanne

waliuawa katika tukio la kutisha baada ya nyumba yao kuchomwa moto usiku.

Waliochoma moto nyumba hiyo ni akina nani? Ni wafuasi wa chama kimojawapo cha

siasa nchini. Kosa la kada huyo wa CCM aliyeuawa ni nini? Ni kuipenda na

"kuifagilia" CCM.

Huko Tanga nako katika kijiji kimojawapo mkoani humo kada wa CCM akiwa amevalia

sare zake za "Ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya" na akipita njiani akiimba nyimbo

za "kuifagilia" CCM, alishitukia akidakwa na kundi la vijana wa chama cha siasa

cha upinzani ambapo walimsulubu na kumuua.

Baada ya kitendo hicho kiovu maiti ya Mtanzania huyo ikafungiwa ndani ya ofisi na

kuenezwa habari za uongo kuwa kada wa CCM amejinyonga. Baadhi ya waandishi wa

habari wakaidaka habari hiyo kama walivyolishwa na kuandika kwenye magazeti yao

yanayodaiwa ni huru kwamba kada wa CCM akutwa amejinyonga.

Hatujasahau kilichotokea katika kijiji cha Piki huko Pemba mara baada ya uchaguzi

mkuu wa Oktoba 30, mwaka huu huko Zanzibar. Askari wawili wa Jeshi la Kujenga

uchumi la Zanzibar wakiwa katika pikipiki yao wakadakwa na wafuasi wa chama

wanaojiita wao ni ngangari. Mmoja wa askari hao akateleza kama samaki na kukimbia

lakini mwenzake hakusalimika.

Askari huyo wa Jeshi la Kujenga Uchumi la Zanzibar akasulubiwa na "wana-ngangari"

na kuuawa. Baada ya kitendo hicho kiovu wanakijiji wote wa kijiji hicho wakaingia

msituni kukimbia mkono wa dola. Lakini ikapigwa propaganda na kudakwa na vyombo

kadhaa vya habari kwamba wanakijiji wa Piki wamewakimbia polisi ili

wasiwanyanyase. Kitendo cha baadhi yao kumuua kikatili polisi huyo ikawa siyo hoja

ya msingi isipokuwa mazungumnzo sasa yakawa ni namna wanakijiji waovu

walivyowakimbia polisi "wanyanyasaji".

Katika matukio yote haya ya mauaji ya kisiasa viongozi wa chama cha siasa ambacho

wafuasi wake walihusika hawakuomba radhi hata kidogo. Walifanya hivyo tu pale

waandishi wa habari walipopigwa katika ofisi ya chama kimoja cha upinzani kwa

kuogopa kuwa kama wasingefanya hivyo habari za chama hicho zingesusiwa.

Kwa wanasiasa wasioamini katika umoja wa kitaifa, amani na utulivu wala utawala wa

sheria ni matusi makubwa kusema kuwa eti wanamuenzi Baba wa taifa. Wanyamaze.

Wasipotoshe historia, wasimdhalilishe Mwalimu Nyerere huko aliko.

Simu: 0744-309858

E.mail: kisasa2000@yahoo.com