UHURU 11.09.2005

 

Mwana-CCM apigwa na wafuasi wa CUF


Na  Mwandishi  Wetu
MKAZI wa kijiji cha Magole, wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro, Ahmed Muya (50) amewalalamikia wafuasi wa chama cha CUF kwa kumpiga na kumjeruhi  kwa tuhuma za kuwa mwanachama wa CCM.
Muya alitoa malalamiko hayo jana alipofika ofisi za gazeti hili, mtaa wa Lumumba, mjini Dar es Salaam,  akitokea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili alikopata matibabu ya kurekebishwa uso wake baada ya kupigwa na wafuasi wa chama hicho, nao wakazi wa kijijini hapo, Septemba 4, mwaka huu.
Pamoja na kulalamika, aliiomba serikali kupitia polisi, kuwashughulikia kwa karibu wanachama wa CUF wanaotaka kuharibu amani nchini kwa kuanzisha vita “vya visu na nondo’.
Alisema siku ya tukio, saa 2 asubuhi alikuwa akihangaikia maandalizi ya harusi ya mtoto wake, Zuhura Ahmed na kwamba alipita eneo ambalo wanachama wa CUF walikuwa wanafanya matayarisho ya mkutano wao.
''Wafuasi wa CUF waliikamata baiskeli yangu kwa nyuma na kudai kwamba mimi nilisababisha wakose umeme kutoka kwa mtu waliyekuwa wakimwomba ili wautumie kwenye mkutano wao,'' alisema.
Muya alisema kabla hajajibu hoja alipigwa usoni kwa nondo iliyosababisha aanguke na baadaye kusaidiwa na wananchi wema kupelekwa kwenye vyombo vya dola.
Alisema wana-CUF hao walijigamba kwa kutamka maneno ya ''wanaume, yeee, mapanga, shashasha''  na kwamba hata hivyo wanakijiji walijitokeza na kumpeleka Polisi kituo cha Dumila alikopata PF3 ili kutibiwa kwenye zahanati ya Dumila.
Zahanati ya Dumila walishauri aende hospitali kubwa kwa vile alikuwa amevunjika mataya na kwamba ndipo alipoamua kufika Dar es Salaam ambako ndugu yake anafanya kazi hospitali ya Temeke.
Hata hivyo, alisema, madaktari wa Temeke walishauri apelekwe moja kwa moja Muhimbili ambako alichunguzwa na hatimaye kufanyiwa upasuaji wa kurekebisha taya kwa saa 3.50 mfululizo.
Alisema taarifa alizopata kutoka Dumila ni kwamba watuhumiwa walikamatwa na kufikisha mahakamani, na kwamba wameachiwa kwa dhamana.
''Pamoja na kunipiga, pia waliiba simu yangu, '' alisema.


Salma Kikwete ahimiza kura kwa CCM
Prosper Kulita na Latifa Ganzel, Morogoro
MKE wa wa mgombea urais wa Tanzania kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi, Mama Salma Kikwete amesema sera nzuri zinazotekelezeka kwa urahisi ni sababu kubwa inayowafanya wanachama wa vyama vya upinzani kujirudi na kujiunga na CCM.
Salma  aliyatamka hayo mjini hapa juzi  wakati wa ziara yake ya siku ya moja ambayo iliandaliwa na UWT makao makuu  kuwahamasisha wanawake kukipigia debe Chama Cha Mapinduzi katika uchaguzi mkuu wa  rais, wabunge na madiwani, mwezi ujao.
Akizungumzia uchaguzi mkuu, Salma  amewataka wanawake wa Morogoro kuungana na kuwa kitu kimoja ili kuipatia CCM  ushindi mkubwa na kuendelea kuongoza nchi.
Mke wa mgombea urais alikumbusha kwamba  wanawake ndiyo nguzo namba moja katika mapambano ya CCM na ndiyo maana hata viongozi wakuu wa Chama  wameandaa ziara hiyo.
Akizungumzia  mikopo ya wanawake,  alieleza matumaini yake kwamba  serikali ya CCM awamu ya nne itaandaa  utaratibu mzuri zaidi ambao utawawezesha wanawake kukopa na riba kupunguzwa ili  iwasaidie katika kupunguza umaskini.
Mwenyekiti wa UWT, mkoa wa Morogoro, Hawa Mbaruk, awali alimtaka Salma kutambua kuwa uwingi wa wanawake waliojitokeza kukutana naye kwenye mkutano huo  ni dalili ya kuwepo kwa  ushindi mkubwa wa CCM katika uchaguzi mkuu.
Alisema kuwa mapokezi makubwa kama hayo yanadhihirisha kuwa CCM ina wapenzi, mashabiki na wakereketwa ambao wako nyuma katika kila tukio ambalo linafanyika.
Mama Salma alikuwa amefuatana na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Zakia Meghji, na wagombea ubunge viti maalum, wakiwemo  Shamim Khan, Lucy Mayenga, Lucy Nkya na Margareth Mkanga.
 


CCM Tabora ‘yawapigia debe’ wagombea ubunge
Na El-hadji Yuusuf, Kaliua
CHAMA Cha Mapinduzi kimesema kuwa kinatarajia kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi mkuu ujao kutokana na CCCM kukubalika kwa Watanzania wengi.
Mwenyekiti wa CCM mkoani Tabora, Juma  Nkumba, aliyasema hayo juzi  mjini Kaliua, alipokuwa akizindua kampeni za uchaguzi mkuu katika jimbo la Urambo Magharibi.
Alisema kuwa CCM imekuwa ikitekeleza ahadi zake kwa wananchi, kila inapoahidi kufanya jambo na kuwa uamuzi huo umewezesha kuondoa matatizo mengi yaliyokuwa yakiwakabili wananchi katika jimbo hilo.
Nkumba alisema  kutokana na msimamo huo wa CCM, wananchi katika jimbo hilo wanatakiwa waendelee kuiamini na kuwachagua wagombea wake katika ngazi zote ili waweze kutekeleza sera nzuri za CCM ambazo lengo lake ni kuleta maendeleo.
Aliwataka wananchi wamchague Profesa Juma Kapuya kuwa mbunge wa jimbo hilo, kutokana na uwezo mkubwa wa kuhimili kazi anazopewa na  Rais, ambazo zimekuwa fahari ya Tanzania na wakazi wa jimbo hilo.
Mwenyekiti alionya kwamba   kuchagua kiongozi wa majaribio ni hatari, kwa sababu wakazi wa jimbo hilo wanaweza kujikuta wakiwachagua watu ambao hawana sifa na hivyo kurejesha nyuma maendeleo yaliyokwisha patikana.
“Wapinzani bado ni wachanga na wanahitaji kulelewa kwanza, hivyo kuwakabidhi madaraka ni sawa na kukubali mtoto wa miaka 13 aongoze nyumba yenye baba na mama,” alisema Mwenyekiti.
Nkumba alikumbusha kwamba  serikali ya CCM inatarajia kujenga barabara ya lami itakayopita katika  jimbo hilo, kupeleka huduma za maji safi katika mji wa Kaliua na kupeleka simu za mkononi kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano kwa wakazi wa jimbo hilo.
Mwenyekiti pia aliwataka wakazi wa jimbo la Urambo Mashariki wamchague Samwel  Sitta, kuwa mbunge wa jimbo hilo, kwa kuwa  ni kiongozi mwenye uwezo, mbunifu na mwaminifu ambaye anaweza kuwatumikia wakazi wa jimbo hilo kwa uaminifu mkubwa.
Alisema kuwa rekodi ya utendaji wa Sitta ni nzuri, hivyo kumpoteza ni sawa na kupoteza lulu ambayo Mwenyezi Mungu amewatunukia watu wa wilaya hiyo.
 

Masasi wasema sera za CUF ni kivuli cha za CCM
Na Godfrey Mhando, Masasi
BAADHI ya wananchi mjini Masasi, mkoani Mtwara,  wamesema kwamba mgombea urais kwa tiketi ya CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, hana sera mpya .
Wamesema pamoja na Profesa Lipumba kupinga sera za CCM, lakini  imebainika kwamba sera anazozitangaza  kwamba atazitekeleza chama chake kikiingia madarakani ni marudio ya sera ambazo CCM hivi sasa inazitekeleza.
Mpaka sasa hakuna chama cho chote cha siasa  ambacho kimetoa mgombea urais mwenye uwezo, nguvu ya umma na  sera bora zenye kuzingatia maslahi ya umma
kama Jakaya Kikwete, wamesema.
Mwana-CCM aliyejitambulisha kwa jina moja la Ndumbaro,  alisema Lipumba pamoja na uprofesa wake, hakuna kipya katika sera anazozinadi kwa kuwa ni kurejea sera ambazo CCM hivi sasa inazitekeleza.
Ndumbaro alisema sera za elimu ya msingi na afya bora kwa jamii ndizo ambazo CCM inazitekeleza sasa hivi, na hakuna kitu kipya ambacho CUF itawaletea Watanzania.
Mwananchi  mwingine  aliyetambulika kwa jina moja la Clitus alisema kwamba hadi sasa sera za CUF  zina mwelekeo wa kutaka madaraka kwa nguvu kutokana na chama hicho kutamka kwamba hakitayapokea matokeo ya kushindwa katika uchaguzi mkuu ujao.
Alisema  hali hiyo inaonyesha kwamba chama hicho, ambacho Lipumba anakiongoza hakiafiki muafaka, na kuna hatari kwamba kikipata madaraka kitaingiza nchi katika machafuko.
Akiwa mjini Mtwara juzi  watu waliojitokeza katika mkutano kwenye uwanja wa Mashujaa  walionyesha kutoshangazwa na hoja alizotoa katika mkutano wake wa kampeni na wengine wakisema 'hana jipya'.
Jana mchana Lipumba aliondoka mjini Mtwara  kwenda Lindi  ambapo alisimama katika vijiji vya Mnolela na Mnazi Mmoja katika tarafa ya Mingoyo. Jioni  alitarajiwa kuhutubia mkutano katika viwanja vya  Ilulu.
Leo anatarajiwa kuendelea na kampeni zake katika maeneo mbali mbali ya Lindi Vijijini na wilaya ya Kilwa kabla ya kesho kuendelea na ziara yake katika wilaya ya Rufiji na Mkuranga, mkoani Pwani.



UVCCM yateua makatibu
Na  Mwandishi  Wetu
UMOJA wa Vijana wa CCM (UVCCM), umefanya uteuzi wa makatibu wapya wa mikoa na wilaya nchini, taarifa kwa vyombo vya habari iliyopatikana jana imeeleza.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotiwa saini na Katibu Uhamasishaji na Chipukizi ya UVCCM, Dk. Diodorus Kamala, Kamati ya Utekelezaji imewateua Abdubakari Ghati kuwa katibu wa mkoa wa Mwanza na Saad Kusilawe, Mbeya.
“Pamoja na uteuzi huo, kamati ya Utekelezaji pia imempangia kituo cha kazi Barnabas Essau mkoa wa Singida,” ilisema  taarifa .
Kwa upande wa wilaya, walioteuliwa na wilaya zao katika mabano ni Judith Mlela (Tabora Mjini), Said Yasin Said (Kisarawe) na Philbert Ngemela (Muleba).    
Umoja huo  Alhamisi na Ijumaa iliyopita, ulikuwa  na semina maalum kwa watendaji wake, chini ya Mwenyekiti wa Taifa, Dk. Emmanuel Nchimbi, juu ya mikakati ya kuipatia CCM ushindi katika uchaguzi mkuu ujao.
Kamala aliwataja washiriki wa semina hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam, kuwa ni wenyeviti na makatibu wa UVCCM wa mikoa na wilaya zote za Tanzania na wajumbe wa Baraza Kuu la Taifa la Umoja huo.


Majambazi yaua Katibu wa UVCCM
Na Esther Katua
KATIBU  wa UVCCM wilaya ya Mkoa Kusini Pemba, Rajab Kheri Rajab, amefariki baada ya kujeruhiwa kwa risasi ubavuni na majambazi waliovamia nyumba ya  wageni ya Bondeni, iliyopo Magomeni Morocco, Dar es Salaam, usiku wa kuamkia juzi.
Taarifa kutoka Umoja huo zilisema tukio hilo lilitokea saa saba na nusu usiku wakati Rajab na wenzake wakiwa katika nyumba hiyo wakiangalia televisheni.
Kwa mujibu wa taarifa, majambazi  yalivamia  na kuanza kurusha risasi zilizompata Rajab ubavuni wakati mjumbe wa kamati ya Utekelezaji  ya vijana Taifa, Mohamed Abrahamani Mwinyi, alijeruhiwa  mkono wa kulia.
Alisema walikimbizwa hospitali ya Muhimbili, lakini Rajabu alifariki juzi  mchana wakati Mwinyi alitibiwa na kuruhusiwa.
Maiti ya Rajab, ambaye alikuwa mjini Dar es Salaam kwa semina ya UVCCM,   ilisafirishwa juzi  kupelekwa Zanzibar.