UHURU 21.11.05

 

Wamiliki wa boti Pemba wavusha watu kiitikadi

Na Khatibu Suleiman, Zanzibar

WAMILIKI wa boti na ngalawa zinazovusha watu katika maeneo mbali mbali ya visiwa vidogo kisiwani Pemba, wameanzisha mgomo wa kuwavusha watu wanaotofautiana nao kiitikadi.

Habari zilizopatikana hapa jana kutoka Pemba, zilisema kuwa wenye boti hao hawataki kuwavusha wananchi wasiyo wanachama wa chama wanachokishabikia. Inaaminika wengi wa wamiliki hao ni wana CUF.

Kufuatia mgomo huo, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, Kassim Tindwa, ametoa siku siku mbili kurejesha huduma bila ubaguzi wa kiitikadi, vyenginevyo atafuta leseni za biashara za vyombo vinavyobagua watu wa kuwavusha.

Kisiwa cha Pemba kina visiwa vidogo vidogo kadhaa ambavyo wakazi wake wanalazimka kuvuka kwa kutumia vyombo hivyo vya usafiri kutoka ama kuingia kwenye visiwa hivyo. Miongoni mwa visiwa hivyo ni Kisiwa Panza, Fundo na Kojani.

“Natoa muda wa siku mbili wamiliki wa vyombo vya usafiri wa baharini kusitisha mgomo wao huo mara moja, vyenginevyo nitafuta leseni zao za kutoa huduma ya usafiri,” Tindwa alikaririwa na Sauti ya Tanzania Zanzibar akisema.

Mgomo huo huo wa wenye vyombo vinavyovusha watu kwenda ama kutoka kwenye visiwa vidogo, inaaminika umeanzishwa baada ya chama cha CUF kushindwa katika uchaguzi mkuu wa Zanzibar, uliyofanyika Oktoba 30, mwaka huu. Wengi wa wanaoathirika ni wafuasi wa Chama cha Mapinduzi.

Hali hiyo katika kisiwa cha Pemba inaashiria kuibuka tena kwa siasa za chuki na uhasama, ambazo miaka mitano iliyopita zilichukuwa nafasi kubwa kiasi ya watu wa familia moja kushindwa kuzikana ama kuhudhuria shughuli za kifamilia.

Hali hiyo iliondoka baada ya kutiwa saini Muafaka wa kisiasa mwaka 2001, kati ya vyama vya CCM na CUF, ambapo wananchi wa Pemba walishiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na maendeleo bila kujali itikadi zao za kisiasa.

Hali ya kuwepo kwa mgomo huo wa vyombo vya baharini umewakumba wananchi wanaoishi katika kisiwa Panza ambao kwa muda wa siku tatu wameshindwa kuja ng’ambo ya pili kupata huduma mbali mbali zikiwemo matibabu, kufuatia mgomo huo.

Kisiwa cha Pemba ni moja ya ngome kubwa ya chama kikuu cha upinzani Zanzibar cha CUF, ambacho katika uchaguzi wa Oktoba 30, kilizoa viti

vyote 18 vya ujumbe wa Baraza la Wawakilishi kisiwani humo.

 

 

 

TAZARA, DAWASCO zakubaliana kutafuta ufumbuzi wa maji machafu

Na Mbazigwa Hassan

MAMLAKA ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) imekubali kufanya mazungumzo na Kampuni ya Majisafi na Majitaka mkoa wa Dar es salaam (DAWASCO) ili kutafuta ufumbuzi wa tatizo la uchafuzi wa mazingira katika eneo la Temeke-Sokota jijini Dar es Salaam.

Hatua hiyo inafuatia mgogoro uliopo kati ya DAWASCO inayodaiwa kutaka kulipwa sh. milioni moja kila mwezi kutokana na TAZARA kumwaga kinyesi katika kituo cha Sokota, kutoka kwenye nyumba zake zilizopo Temeke kwa Maganga jijini.

Meneja wa Fedha na Uhusiano wa TAZARA, Pascal Mulenga, alisema wameomba kulizungumzia suala hilo kutokana na DAWASCO kushindwa kutoa huduma hiyo kwa zaidi ya miaka miwili.

Alisema DAWASCO wanadai sh. milioni 40 kwa madai ya kutoa huduma ya majitaka ya nyumba hizo, lakini ukweli ni kwamba kampuni hiyo haijatoa huduma kwa zaidi ya miaka miwili sasa.

Mulenga alisema huduma huyo inakosekana kwa sababu pampu ya kusukuma majitaka iliharibika siku nyingi.

“Ni kweli suala hilo lipo na sisi hatupati huduma kutokana na kuharibika kwa mashine ya kusukuma majitaka, hivyo kulazimika kutumia gari letu la majitaka. Hata hivyo, tunafikiri jambo zuri ni kukaa nao ili tupate muafaka,” alisema.

Mulenga alisema wanafanya utaratibu wa kuzungumza na wafanyakazi walionunua baadhi ya nyumba zao katika eneo la Temeke-Maganga ili baadaye wahusike moja kwa moja kulipia ankara za majitaka badala ya TAZARA, kwa sababu nyumba wanazoishi ni mali yao binafsi.

Alisema utaratibu huo utafanywa baada ya kulipa deni la DAWASCO ili wasiwalipishe watu hao deni lisilowahusu, na kuongeza kwamba baadhi ya nyumba wanazoishi askari wao ndizo zitakazolipiwa.

Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Shyrose Bhanji, alipoulizwa kuhusu kuwepo kwa uchafuzi huo wa mazingira alikiri na kuongeza kuwa tatizo ni TAZARA ambao imekuwa hailipi deni kwa muda mrefu na kuwafanya washindwe kutoa huduma kama inavyopaswa.

Wananchi wa eneo la Temeke -Sokota walilalamika kwamba kinyesi cha binadamu kinafurika katika mfereji ulio kando ya barabara ya Mandela na kusababisha harufu kali, jambo linaloweza kusababisha kuenea kwa magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu.

 

Acheni kuchoma mapori, DC Iringa awaasa Watanzania

Na Mwandishi Wetu, Iringa

MKUU wa wilaya ya Iringa, Tatu Ruta, amewataka Watanzania kuacha tabia ya kuchoma moto mapori ili kuepusha usumbufu kwa wanyamapori na wadudu wanaoishi kwenye mapori hayo.

Tatu alitoa wito huo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Ofisa Wanyamapori wa Halmashauri ya Iringa, wakati wa kuzindua maonyesho ya picha za wanyamapori yaliyodhaminiwa na mtaalamu wa wanyamapori, Godwin Van Lawick.

Alisema Watanzania lazima waheshimu mapori na misitu kwamba ni makazi ya viumbe wengi walio hai, na kwamba kitendo cha kuchoma moto misitu ni sawa na kuchoma moto nyumba anayoishi mtu.

Aliwasihi wachoma mkaa nchini kutafuta ajira nyingine badala ya kuangamiza miti kila siku na kusababisha kero kwa viumbe wengine.

Mdhamini wa maonyesho hayo ya siku 20, Van Lawick, alisema Tanzania ina utajiri mwingi wa maliasili, hususan miti na wanyama, lakini asilimia kubwa ya Watanzania hawana upendo kwa wanyamapori.

Alisema wanyamapori ni viumbe wanaostahili kuishi kwenye mapori yao bila bughudha na kwamba iwapo mapori yataharibiwa, wanyama watavamia makazi ya watu.

Alisema wapo watu wazima ambao hawajawahi kumwona mnyama wa porini kama tembo, ingawa wapo tele hapa Tanzania.

"Nimeamua kuwaonyesha picha mbalimbali za wanyama na kuwapa mafunzo ya kuwatambua wanyama na kufahamu faida zao ili wawatunze na kupata faida mbalimbali," alisema

 

Watakiwa kuenzi ushindi wa Rais Karume

Na Mwandishi Wetu, Mtwara

WANANCHI wametakiwa kuuenzi ushindi wa Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, kwa kuichagua CCM katika uchaguzi mkuu wa Jamhuri ya Muungano unaotarajiwa kufanyika Desemba 14, mwaka huu, ili iweze kuendelea kuwaletea maendeleo.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Jumuia ya Wazazi Taifa, Abiud Maregesi, wakati akiwahutubia wananchi katika mkutano wa hadhara wa kampeni uliofanyika mwanzoni katika Kijiji cha Mkangaula, Masasi mkoani hapa.

Maregesi alisema matokeo ya uchaguzi wa Zanzibar ni kielelezo tosha kwamba wananchi wa Zanzibar wanaziamini serikali za CCM kutokana na utekelezaji makini wa ahadi zake zinazotolewa kupitia Ilani za Uchaguzi.

Alisema CCM ndicho chama pekee kinachotekeleza ahadi zake kwa wananchi na kikichaguliwa tena kitahakikisha kinawaletea mafanikio makubwa zaidi kwa kushirikiana na wananchi, na marafiki wa nje na ndani ya nchi.

Maregesi alisema vyama vya upinzani kikiwemo CHADEMA na CUF bado vinajifunza uongozi ndani ya vyama vyenyewe na havifai kupata kura za kuongoza nchi.

Aliwataka wananchi wasidiriki kuwachagua wapinzani, kwani kuwachagua wapinzani ni sawa na kujifunga kitanzi cha kuua maendeleo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Mwenyekiti huyo alisema vyama vya upinzani havina sera inayolenga kuwaletea maendeleo wananchi wake na badala yake vimehubiri matusi na kuvuruga amani nchini.

Maregesi alisema pamoja na vurugu za mara kwa mara zinazofanywa na vyama vya upinzani, hususan CUF kuelekea uchaguzi mkuu ujao, CCM itaendelea kuendesha kampeni zake kwa ustaarabu, kuheshimu sheria, amani na utulivu na kuwataka wananchi kuhudhuria kwa wingi katika mikutano yake ya kampeni, lakini kura iende kwa wagombea wa CCM.

Kwa upande wake mgombea ubunge wa jimbo la Nanyumbu, Masasi mkoani Mtwara, Steven Mkapa, alisema endapo atachakuliwa kushika wadhifa huo atashirikiana na serikali kuharakisha maendeleo.

Alisema uwezo anao, nia anayo ya kuwaletea maendeleo wananchi wa jimbo hilo na kwamba anachosubiri sasa ni ridhaa ya wananchi kumchagua ili aweze kuwatumikia kwa moyo wa dhati kabisa.

Mkapa alisema kwamba maendeleo ya jimbo hilo yatapatikana endapo wananchi wataipigia kura CCM kuanzia mgombea wake wa urais wa Tanzania Jakaya Kikwete, wabunge na madiwani.

Alifafanua kuwa akiingia madarakani atahakikisha kwamba anashirikiana kikamilifu na wananchi wake katika kuhakikisha maendeleo hayo yanapatikana haraka.

Alisema maendeleo katika jimbo hilo yatapatikana kwa njia ya ushirikiano na mshikamano na si kwa mtu mmoja.

“Maendeleo katika jimbo letu yatapatikana kwa njia ya kushirikiana, kwani yeye pekee hawezi kufanikisha chochote hata kama angekuwa na uwezo wa kifedha,” alisema.

 

 

Vodacom yazindua promosheni kamambe

Na Esther Katua

KAMPUNI ya simu za mkononi ya Vodacom imezindua kampeni ya ijulikanayo kama VodaMOTO ikiwa ni ofaa maalumu kwa wateja wake kwa kipindi cha mwisho wa mwaka.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa kupokezana kwenye viwanja vya Karimjee Jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Masoko wa Vodacom Junaid Munshi na Meneja Masoko Eprahim Mafuru walisema lengo la VodaMOTO ni kuwapa zawadi wateja wao kwa kuwa nao kwa kipindi hiki cha mwisho wa mwaka.

Kwenye VodaMOTO kutakuwa na vitu vinne ambavyo ni droo la shinda mamilioni na Vodataarifa, punguzo la mawasiliano ya ujumbe usiku, nyongeza ya asilimia tano kwa kila ongezo la fedha zitakazoingizwa kwenye simu na siku ya kufurahi na familia.

Wakifafanua kuhusu ofa hizo, walisema nyongeza ya asilimia tano ya fedha unazoingiza kwenye simu za muda wa maongezi zimeanza jana, ambapo kila kiwango cha fedha utakazoingiza kwenye simu yako utaongezewa muda wa maongezi wa asilimia tano.

Wakizungumzia droo la shinda mamilioni na Vodacom walisema mteja anapaswa kutuma ujumbe kwenye voda taarifa kwa gharama ya sh. 150 iikiwemo VAT kwenda namba 155, ambapo ataingizwa kwenye droo la kushindaniwa.

Walisema kila wiki kutaendeshwa droo la washindi wa wiki ambapo shindano la mwisho litafanyika baada ya wiki sita na watachaguliwa washindi sita ambao kila mmoja atapewa sh. milioni tano.

Wakizungumzia punguzo la utumaji wa ujumbe mfupi walisema kuanzia saa sita usiku hadi asubuhi wateja wataweza kutumia sh. 30 kwa kutuma ujumbe badala ya sh. 45 ofa ambayo itaanza leo.

Kuhusu siku ya familia walisema kampuni ya Vodacom imeamua kuandaa matamasha kwenye mikoa ya Arusha, Mbeya, Mwanza, Dar es Salaam kwa lengo la kufurahi na wateja wao na familia zao, hasa watoto yatima.

Wakizungumzia kuhusu watoto yatima walisema Vodacom iliamua kutenga sh. laki tano kwa kila kituo cha watoto yatima, ambapo wanatoa msaada kulingana na mahitaji ya kituo au watatoa fedha taslimu.

 

 

Rais Mkapa kuzindua rasmi Ubungo Plaza

Na Mwandishi Wetu

RAIS Benjamin Mkapa leo anatarajia kuzindua rasmi jengo jipya la Ubungo Plaza lilipo karibu na kituo cha mabasi yaendayo mikoani, jijini Dar es Salaam.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mwenyekiti wa Bodi ya Ubungo Plaza, Margaret Ikongo, ilisema jengo hilo linamilikiwa kwa ubia na Shirika la Bima la Taifa (NIC), Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF).

Alisema jengo hilo linatoa huduma mbalimbali kwa wakazi wa Dar es Salaam kama vile hoteli, sehemu za kufanyia mikutano, ofisi, maduka na upangaji wa ofisi.

Margaret alisema katika sehemu ya hoteli kutakuwa na vyumba 154, wakati ukumbi wa mikutano una uwezo wa kuingiza watu 800 wakati kwa wapangaji wa ofisi tayari wameingia kwenye jengo hilo toka Mei mwaka jana.

Baada ya uzinduzi huo kesho, Rais Mkapa anatarajiwa kuzindua majengo ya Mahakama Kuu, Mahakama ya Mkoa wa Iringa na Mahakama ya wilaya ya Iringa.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Sam Rumanyika, ilisema shughuli hiyo itaenda sambasamba na kuwaaga majaji wote wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania.

 

Wanawake watia fora mahafali Chuo cha Ustawi wa Jamii

Na Mwandishi Wetu

WANAWAKE walitia fora kwa kuwa wahitumu wengi kuliko wanaume katika mahafali ya 29 ya Chuo cha Ustawi wa Jamii, kilichoko Kijitonyama, Dar es Salaam.

Katika mahafali hayo ambayo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana na Michezo, Profesa Juma Kapuya, kati ya wahitimu 217, wanawake walikuwa 151. Hata hivyo wahitimu 15 wa kozi ya cheti cha kompyuta hawakuainishwa jinsia zao.

Dk.Hosea Rwegoshora, Kaimu Mkuu wa Chuo hicho, alitaja idadi ya wahitimu na kozi zao katika ngazi ya cheti ni: Rasilimali Watu (40), Uongozi wa Kazi (6) na Ustawi wa Jamii (62).

Katika ngazi ya Stashahada za juu kwenye fani ya Usatwi wa Jamii (40), Uongozi wa Kazi (8), Rasilmali Watu (30) na Stashahada ya Uzamili ya Ustawi wa Jamii (5).

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya chuo hicho, Ibrahim Marwa, alifafanua kuwa idadi hiyo ya wahitimu mwaka huu imeongezeka kwa asilimia 26, kwani mwaka jana ilikuwa 171 na kila mwaka imeendelea kuongezeka.

Marwa alisema, chuo hicho sasa hivi kinatarajia ifikapo mwakanai kitaanza kutoa shahada katika fani zilizopo chuoni hapo, baada ya Mamlaka ya Elimu nchini kuidhinisha mitaala yake na ndiyo hatua kuelekea kuwa chuo kikuu ndani ya miaka mwili ijayo.

Kwa mujibu wa Marwa, nafasi ya kozi za Stashahada za juu zitachukuliwa na kuanzishwa kwa mafunzo ya diploma katika fani hizo, pia katika mwaka wa masomo 2007/8 chuo kinatarajia kuanza kutoa shahada ya juu na kuwa maandalizi yote yamekamilika.

Alilalamika hali mbaya ya makataba ya chuoni hapo kuwa ni ndogo yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 31 tu, jambo ambalo halikidhi haja na kuomba Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana na Michezo iingilie kati.

Kuhusiana na kampeni dhidi ya ugonjwa wa ukimwi, Marwa alisema chuo kimefanya utafiti kujua hali ya ukimwi chuoni hapo na taarifa zake karibu zitachapishwa na kuwa wanatarajia kuanzisha kituo cha ushauri nasaha.

Kwa upande wake, Waziri Kapuya ameunga mkono juhudi hizo na kuongeza kuwa wizara yake inalenga kuendesha mkakati kama huo kwa kutimia wataalamu wa chuoni hapo.

Alisema asilimia 68 ya vijana kitaifa ndio nguvu kazi ambayo pia ndiyo inaathirika zaidi na ukimwi na ametaka juhudi zifanyike kulinusuru taifa na janga hilo.

Sambamba na hilo, chuo kinatarajia kuanzisha kozi ya usuluhishi wa migogoro sehemu za kazi na Waziri Kapuya, ameunga mkono mpango huo.

 

Afrika Mashariki wakubaliana kutangaza utalii kwa pamoja

Na Omari Shaaban.

BODI za utalii za nchi za Jumuia ya Afrika Mashariki, Kenya, Uganda na Tanzania, zimekubaliana kuutangaza utalii kwenye nchi hizo kwa pamoja katika masoko ya kimataifa.

Makubaliano yaliifikiwa Novemba 14 mwaka huu, kwenye soko la kimataifa la jijini London, Uingereza ambapo wakurugenzi wa bodi hizo walikutana katika shughuli za kutangaza utalii wa nchi zao.

Taarifa iliyotolewa na Ofisa Uhusiano wa jumuia hiyo, Magaga Alot, ilisema makubaliano hayo hayatahusiana na utekelezeji wa masuala ya ndani ya utalii wa nchi wanachama.

Hata hivyo, alisema makubaliano hayo yataanza mwakani na katika kipindi kilichobakia, kila nchi itakwenda kivyake kwenye masuala yanayohusiana na utalii.

Alisema katika maonyesho ya utalii ya kimataifa ambayo yatafanyika hivi nchini Ujerumani, nchi za Afrika mashariki zitashiriki kwenye banda moja litakaloitwa "East African Village" lakini kila nchi itajitangaze kivyake.

Ofisa huyo alisema makubaliano hayo ya pamoja yatatengenezewa kanuni zake na kwamba mkutano wa kwanza wa kujadili mambo mbalimbali ya muungano huo utafanyika mwakani na ambao utajadili masuala ya kisheria na mikataba.

Wakurugenzi wa bodi za utalii waliokuwepo kwenye mkutano huo, nchini Uingereza ni Dk. Ongonga Ochien wa Kenya, James Bahinguza wa Uganda na Peter Mwenguo wa Tanzania.

Wengine waliohudhuria mkutano huo ni mchumi mwandamizi wa EAC kuhusu utalii, Dk. Nyamajeje Weggoro, Mkurugenzi wa Utalii nchini, Selehe Pamba na Mkurugenzi wa utalii nchini Kenya, Wanjiru Munene.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Weggoro alisema kuwa muungano huo ni mzuri kwa kuwa utaleta ongezeko la utalii kwa nchi za Afrika Mashariki na kukua kwa ajira.

 

Madaktari rejeeni kazini, komeni kujiona bora kuliko fani nyingine

MGOMO wa madaktari katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) leo umeingia katika siku ya tano, huku wakiwa wameshawarubuni hata wafamasia kuwaunga mkono. Madaktari wanashiriki mgomo huo kwa wanachosema ni kuishinikiza serikali iwaongeze mishahara kufikia sh. milioni 1.2 kwa kima cha chini, yaani kwa wanaoanza kazi.

Madaktari hao wameahidi kuendelea na msimamo wao huo hadi serikali itakapokubali kutekeleza madai yao kwa kuwawekea kwenye akaunti zao za benki fedha hizo, kulingana na viwango vya kila mmoja vitakavyokuwa vinazingatia kima hicho cha chini. Wanasema hivi sasa wanalipwa kima cha chini sh. 200,000 ambazo hazitoshi kukidhi mahitaji.

Inawezekana kabisa madai ya madaktari hao yakawa ya msingi na ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi ili kuwapunguzia makali ya maisha, na tunakubali kuwa kazi ya udaktari inahitaji watu wenye utalaamu wa kutosha kwa maana kuwa waliokwenda shule.

Lakini kinachoshangaza ni msimamo mkali uliochukuliwa na madaktari wetu hao wa kutaka fedha kwanza, vinginevyo wataendelea kukaa wakishuhudia wagonjwa wakifa bila msaada kutoka kwao. Inavyoeleweka ni kwamba katika mambo yanayohusu ugonjwa, madaktari wana nafasi kubwa ya kuokoa maisha pale roho ya binadamu inapokuwa haijafikia hatima yake kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu.

Pamoja na kuwa wameitisha mgomo, lakini tunaamini hali halisi ya maisha ya binadamu inafanya hata hao madaktari wasutwe na hatua hiyo waliyoichukua kwa kuona au kuendelea kusikia taarifa za vifo vya wagonjwa wanaofikishwa hospitalini hapo. Watuambie: Hivi kweli wanafurahia na kupiga vigelegele wanapopata taarifa kwamba wagonjwa wengi wanazidi kupoteza maisha Muhimbili kutokana na mgomo wao?

Madaktari hao watambue kuwa katika nchi yetu si wao pekee ambao taaluma yao ni muhimu kwa jamii. Zipo kada nyingi za taaluma zilizo muhimu. Kwa kutambua kwamba kuna uduni wa maslahi katika sekta karibu zote, je, sasa fasheni iwe kama hiyo ya mgomo inayotumiwa na madakri wetu?

Mathalani, kuna walimu waliowafundisha hata hao madaktari. Wapo polisi wanaofanya kazi kwa saa 24 kuhakikisha wanalinda mali na usalama wa raia, wakiwemo hao madaktari. Wapo wanajeshi ambao ni mahiri katika ulinzi wa usalama wa mipaka ya nchi yetu. Wapo wahandisi wa fani mbalimbali, zikiwemo za ujenzi wa miundombinu kama barabara na madaraja.

Pamoja na kutambua mchango wa Watanzania wote hao, na wengine, katika kutoa huduma na kuijenga nchi yetu, vipi madaktari ndio sasa wajione ndio bora zaidi na kutoa masharti ambayo lazima kwanza yatekelezwe bila kujali roho za watu zinazotoweka kutokana na hatua yao hiyo?

Tunavyofahamu ni kwamba katika nchi inayojali kuzingatiwa kwa taratibu na utawala wa sheria, utekelezaji wa mambo mbalimbali daima hufuata kanuni.

Na serikalini ambako ajira ya madaktari wanaogoma sasa huangukia, utoaji wa maslahi ni jambo linalozingatia bajeti. Je, ndugu zetu hawa madaktari wasomi, wanaelewa kwamba fedha wanazotaka wawekewe benki mara moja kabla ya kuendelea na kazi zao, zimeshaidhinishwa kwa mujibu wa taratibu? Kama hawaelewi, na kama hazijaidhinishwa, shinikizo lao hilo ambalo tayari linaathiri uhai wa watu ni la nini?

Wimbi la sasa la madai haya ya madaktari si la kwanza. Mara zote ni madai yanayoandaliwa kwa uongozi wa madaktari hao. Pengine tujiulize: Hivi uelewa wa viongozi wa madakari hao na madaktari wenyewe ni finyu kiasi cha kutofahamu taratibu zinazohusu utoaji wa malipo ya serikali zinavyofanya kazi?

Kwa sababu baada ya kuanza kwa mgomo wa sasa, serikali ilijitahidi kueleza hatua iliyokuwa imefikiwa katika utekelezaji wa madai hayo, lakini madaktari wakasema hakuna watakachokielewa isipokuwa tu kukuta fedha zao benki. Hoja gani isiyokuwa na mantiki hii? Au ndugu zetu hawa wana ajenda ya siri wasiyotaka kuiweka wazi, wakitumia unyeti wa taaluma yao, likiwa ni tishio kwa uhai wa watu? Hivi iwapo hizo fedha wanazoziota hazipo, huu ndiyo sasa utakuwa mwisho wa utekelezaji wa taaluma yao Muhimbili?

Tujuavyo, kulingana na uwezo wake katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali, Serikali kwa upande wake imejitahidi kuwawekea mazingira mazuri wananchi wake, ikiwemo kutoa fursa za kusoma bure au kwa gharama nafuu kwa watu mbalimbali, wakiwemo hao madaktari. Nani asiyejua kwamba madaktari wamekuwa wakifaidika na mambo mengine kama kusamehewa kodi wanapoingiza vitu, yakiwemo magari? Hivi hatua yao hiyo ya kugoma ndiyo ielezeke pengine kwamba ni ‘shukrani ya punda ni mateke’ kiasi cha kupuuza kuokoa roho za watu?

Madaktari waangalie tena uamuzi wao na kurejea kazini huku matatizo yao yakiendelea kushughulikiwa. Hakuna fedha ambazo mtu akipewa anaweza kusema zinatosha. Madaktari wetu wasidhani wao ni tofauti na watendaji wa fani zingine.

Wakishaelewa hivyo hawatathubutu kila kukicha kuiona fani yao kama silaha ya kuonyeshana ubabe na serikali, kwa kugoma kufanya kazi, hali ambayo inasababisha kero kubwa kwa wagonjwa, huku wengi wao wakipoteza uhai kwa sababu tu wataalamu wetu hao wa tiba wanataka kima chao cha chini mishahara kiwe sh. milioni 1.2.