Kikwete awataka wapinzani wasione haya kuipigia CCM

  • Asema ni yeye ndiye atakayeshinda Urais

Na Rashid Zahor, Mkuranga

MGOMBEA Urais wa Jamhuri ya Muungano kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete amewataka

wafuasi wa vyama vya upinzani wasione aibu kukipigia kura chama hicho kwa vile

hakuna mgombea urais wa vyama hivyo atakayeweza kushinda wadhifa wa urais.

Kikwete alitoa rai hiyo juzi na jana alipokuwa akihutubia mikutano ya kampeni

iliyofanyika Utete na Mkuranga mkoani Pwani.

"Hakuna mgombea urais wa upinzani akayemshinda mgombea wa CCM. Kama hivyo ndivyo,

mpe kura yako mgombea urais wa CCM, wabunge na madiwani ili uharakishe maendeleo

ya jimbo lako," alisema.

"Kura ni jambo la siri, hawezi kuja Lipumba akakuuliza umempigia kura nani, na

hata kama atakuuliza unamdanganya tu kwa kumwambia. mwaka huu tutashinda kwa

kishindo, lakini ukweli unabaki kuwa nao mwenyewe moyoni mwako," alisema.

Mgombea wa CCM aliwatahadharisha Watanzania wawe macho na viongozi wa vyama vya

upinzani wanaotangaza matokeo ya uchaguzi kwamba wanafanya makosa kwa vile kazi

hiyo ni ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

Alitoa mfano wa matokeo ya uchaguzi mkuu wa Rais na Wawakilishi wa Zanzibar

yaliyotangazwa na CUF kwamba hayakuwa sahihi na yalilenga kuwapotosha Watanzania.

"CUF wanadai kwamba Maalim Seif alishinda kwa asilimia 50.6 na Karume alishinda

kwa asilimia 49.3. Ukijumlisha asilimia hizi unapata asilimia 100.

"Kule Zanzibar wagombea walikuwa sita na wote walipata kura. Sasa unapotoa takwimu

za kura za CCM na CUF ambazo ukizijumlisha unapata asilimia 100, kura za wagombea

wengine ziko wapi? Kama huu siyo uongo ni nini?" Alihoji.

Wakati huo huo,  akihutubia mkutano mkubwa wa kampeni Mburahati Barafu jijini Dar

es Salaam jana, Kikwete, ameahidi kuwa serikali ya awamu ya nne itahakikisha

walimu nchini wanajengewa nyumba bora za kuishi.

Alisema katika mkutano huo uliohudhuriwa na mamia ya wananchi na wapenzi wa CCM

kuiwa, baada ya serikali ya awamu ya tatu kukamilisha ukarabati wa shule za

msingi, katika awamu ijayo, serikali itatoa kipaumbele kwa walimu.

"Huko vijijini nyumba za walimu zinatisha. Wanafanya kazi kwa moyo. Tumeanza na

madarasa, sasa itakuwa zamu ya nyumba za walimu.

"Kama tumeweza kujenga shule nzuri, sasa ni zamu ya walimu nao kulala na kuamka

kwenye nyumba nzuri," aliongeza.

Kikwete pia aliahidi kuwa serikali ijayo ya CCM itatilia mkazo ajira kwa vijana

kwa vile ukosefu wa ajira ni bomu la kutega, ambalo yeye binafsi linamtisha.

Alisema karibu kila mwaka vijana 800,000 wanamaliza vyuo na shule za msingi, hali

inayoonyesha kuwa tatizo hilo linaongezeka kila mwaka, lakini aliahidi kuwa

serikali ijayo itapambana nalo.

 

 

Wananchi Bukoba Mjini wasusia mkutano wa Seif

  • l Alikuwa akimpigia kampeni Lwakatare

Na Angela Sebastian, Bukoba

WANANCHI wa Bukoba Mjini wamesusia mkutano wa kampeni wa chama cha CUF uliokuwa

ukihutubiwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Shariff Hamad.

Tofauti na mikutano ya chama hicho kujaa mamia ya mashabiki, juzi hali ilikuwa

tofauti ambapo Maalim Seif alijikuta akiwahutubia viongozi wa wilaya wa chama

chake, wafuasi wachache na watoto.

Wananchi wengi waliususa mkutano huo uliyofanyika juzi katika viwanja vya Uhuru

mjini hapa, ambapo wengi waliamua kusikiliza sera za kumnadi mgombea ubunge wa CCM

katika jimbo la Bukoba Mjini, Khamis Kagasheki, uliofanyika katika viwanja vya

Bunena mjini hapa.

Hali hiyo imetafisiriwa na wakazi wengi wa hapa kuwa ni dalili inayoonyesha

kupungua kwa umaarufu wa CUF mjini hapa, jimbo ambalo lilikuwa likishikiliwa na

mbunge wa chama hicho, Wilfred Lwakatare. Hali hiyo inatoa nafasi nzuri zaidi ya

ushindi katika uchaguzi wa Desemba 14, mwaka huu, kwa CCM kuchukua jimbo hilo.

"Hivi huyu mtu aliyeshindwa Zanzibar anawezaje kupiga kampeni wakati hana sera,

hii ni kama kipofu kumwongoza kipofu mwenzake," walisema wananchi waliokuwa katika

mkutano wa CCM.

Hali hiyo ya wananchi kuukimbia mkutano wa Seif, inasemekana kumechangiwa na

kiongozi huyo kukosa ushindi huko Zanzibar, na kitendo cha wafuasi wa CUF kuwapiga

waandishi wa habari, ambapo wananchi walidai hawawezi kupoteza muda wao kwenda

kusikiliza sera zinanopalilia matusi, kashfa na vurugu.

Kundi moja lililokuwa pembeni mwa uwanja huo wa Bunena llililokuwa likiongozwa na

mzee mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Salimu Swahibu mkazi wa mjini Bukoba

lilisikika likisema “sera za CUF ni kujenga chuki ndani ya mioyo ya wananchi,

kashfa na sasa wamecheza ngoma wasiyoijua".

"Itikadi ya vyama vingi si mapanga, marungu na fujo bali ni kuboresha demokrasia

na maendeleo ya Taifa la Tanzania,” waliongeza wananchi hao.

Walisema kuwa siku hizi watu wameelewa kwa hiyo wanatafuta  viongozi bora

watakaoweza kutatua matatizo yao, na siyo kupata uongozi na kuutumia kwa maslahi

binafsi.

Wananchi hao walisema kuwa matusi yanayotolewa na viongozi wa CUF hayatawafaidisha

wananchi, bali viongozi watoa matusi nia yao ni kutaka kuvunja amani ya Tanzania.

Wakati huo huo, Mgombea ubunge kupitia tiketi ya CCM Khamisi Kagasheki alipokuwa

akihutubia katika mkutano wake wa kampeni jana uliofanyika katika kata ya

Rwamishenye, alisema kuwa nia ya kugombea ubunge katika jimbo hilo si kupata cheo,

bali kutaka kushirikiana na wananchi wa Bukoba kuleta maendeleo na kuwatumikia.

Mkutano huo ambao ulikuwa mkutano wa uzinduzi wa kampeni kwa mara ya pili

ulihudhuriwa na maelfu ya wananchi na wakazi wa mji wa Bukoba wakiimba nyimbo za

kuwanadi wagombea wa CCM.

 

 

Msome aasa kuendelezwa kwa amani na utulivu

Na Mwandishi Wetu

CHAMA cha Mapinduzi kimewataka viongozi  na wafuasi wa vyama vya siasa nchini

kujiepusha na vitendo vya fujo, chuki na uhasama wakati wa kampeni za uchaguzi

mkuu zinazoondelea ili kudumisha na kuendeleza umoja, amani, utulivu na mshikamano

wa taifa.

Wito huu umetolewa na Katibu wa Organaizesheni wa Chama Cha Mapinduzi, Jackson

Msome katika mikutano ya kampeni za uchaguzi iliyofanya katika wilaya za Uyui na

Tabora, wiki hii.

Msome alisema hayo kufuatia mfululizo wa matukio ya kuhatarisha amani yaliyotokea

mkoani Tabora na sehemu kadhaa nchini ambayo yanaaminika kufanywa na  wafuasi wa

vyama vya upinzani.

Akitoa mfano wa vitendo vya uvunjaji wa amani, Msome alivitaja vitendo vya hivi

karibuni vya ushambuliaji wa wana- CCM, uchomaji wa nyumba, uwekaji wa vinyesi

katika kuta za nyumba na visima vya maji na upigaji wa watu wakiwemo waandishi wa

habari  ni baadhi ya mambo ambayo  hayana  budi kukemewa na jamii.

Msome alisema Watanzania wanachotaka kuona na kusikia ni sifa za wagombea, ubora

wa sera na rekodi ya vyama, wala si vitendo vinavyokiuka sheria za uchaguzi na

kuhatarisha misingi ya taifa.

Aliwakumbusha wananchi kuwa mfumo wa vyama vingi vya siasa haukuanzishwa ili

kuvunja misingi ya utaifa ambayo imejengwa kwa muda mrefu na waasisi wa Taifa letu

ambao  ni Baba  wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid   Amani Karume,

bali kuiendeleza na kuiboresha kwa maendeleo ya Taifa.

"Kwa maana hiyo, chama chochote cha siasa kinachotishia misingi hiyo kikataliwe na

kunyimwa nafasi ya kuongoza nchi yetu," alisema

Msome ambaye pia  ni Mjumbe wa kamati Kuu ya CCM, amewaomba Watanzania kuendelea

kukiunga mkono Chama cha Mapinduzi ambacho kimekuwa daima mtetezi mkubwa wanyonge,

udumishaji na uendelezaji wa umoja, amani na maendeleo ya taifa.

Msome amemaliza ziara ya siku nne mkoani Tabora ambayo ilikuwa ya lengo la

kuwanadi wagombea wa CCM wa nafasi za urais, ubunge na udiwani. Baadaye wiki hii

ataanza ziara kama hiyo katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa.

 

RPC Mbeya aagizwa kuondoa tofauti na wana habari

Na Mohammed Mhina, wa Jeshi la Polisi

MAKAO Makuu ya Jeshi la Polisi nchini limemuagiza kamanda wa Polisi wa Mkoa wa

Mbeya Kamishna Msaidizi wa Polisi Suleimani Kova, kudumisha na kuendeleza uhusiano

mwema na waandishi wa habari mkoani humo kwa manufaa ya jamii inayowazunguka.

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Aden

Mwmaunyange, alisema jana uongozi wa polisi umeshtushwa na kusikitishwa na taarifa

ya chama cha waandishi wa habari wa mkoa wa Mbeya kuwa wametishia kususia kufanya

kazi na kamanda wa polisi wa mkoa huo kwa sababu za kutoaminiana.

Mwamunyange alisema Jeshi la Polisi kwa maana ya Makao Makuu na makamanda wa

polisi wa mikoa na vikosi, wakati wowote wanakuwa na uhusiano mwema na wa karibu

na wa moja kwa moja na waandishi ama vyombo vya habari kwa nia ya kuelimisha umma

juu ya masuala ya uhalifu na usalama.

Alisema hakuna haja ya kutofautiana ama kulumbana kati ya pande hizo mbili kwa

masuala ya kiutendaji kwani wote ni wadau katika suala la kuhakikisha kwamba

ulinzi na usalama na elimu kwa jamii inawanufaisha wananchi katika maeneo yao.

Jeshi hilo pia limewakumbusha wanahabari na wamiliki wa vyombo vya habari nchini,

kutojenga tabia ya kutishia ama kususia kutoa taarifa za viongozi ama taasisi ya

mtu binafsi, taasisi au idara ya serikali kwani kwa kufanya hivyo kunawakosesha

wananchi haki yao ya msingi ya kupashwa habari, kuelimishwa na kuburudishwa kwa

njia ya habari.

Msemaji huyo alisema hakuna haja ya baadhi ya waandishi ama vyombo vya habari

kujenga chuki na viongozi wa serikali ama taasisi kutokana na kuhitilafiana au

kutiliana mashaka kwani kwa kufanya hivyo hasara kubwa ni kwa jamii.

Mwamunyange alisema kwa vile makamanda wa polisi wa mikoa na wakuu wa vikosi vyote

vya polisi hapa nchini wapo chini ya Mkuu  wa Jeshi la Polisi ni vema mtu ama

taasisi ikiona inahitalifiana na mmoja wa makamanda kutoa taarifa makao makuu

kabla ya kuchukua hatua dhidi ya mhusika kwa ushauri na maelekezo zaidi.

Jeshi hilo pia limewaagiza makamanda wa polisi wa mikoa akiwemo wa Mbeya

kuhakikisha usalama wa waandishi wa habari katika kazi zao, maisha yao na  mali

zao ukiwa pia ni wajibu wa msingi katika jamii nzima ya Kitanzania.

 

'Ondoeni dhana ya dawa ya jino kuling'oa'

Na Mwandishi Wetu

WIZARA ya Afya imewataka madaktari wa meno nchini kuondoa dhana iliyojengeka kwa

wananchi kwamba dawa ya jino ni kuling'oa.

Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi wa Huduma za Hospitali katika Wizara ya Afya Dk.

Zacharia Berege ambaye alitoa hotuba ya ufunguzi wa mkutano kwa niaba ya Katibu

Mkuu wa Wizara ya Afya Mariam Mwaffisi kwenye warsha ya siku tatu ya Chama cha

Madaktari wa Meno Tanzania unaofanyika kwenye hoteli ya Golden Tulip.

Berege katika hotuba hiyo alisema changamoto waliyonayo madaktari hao kutoka

sehemu mbalimbali za Tanzania na nchi jirani ni kutafuta namna ya kuimarisha mfumo

wa meno ya binadamu kama alivyozaliwa badala ya kuona suluhisho la matatizo ni

kung'oa.

Aliwataka madaktari pia kulizungumzia kwa kina suala la maambukizi ya ukimwi kwa

mate na njia ya damu.

Berege aliwataka madaktari hao kutilia manaani changamoto wanazopata ili

kurekebisha sehemu zinazoonekana zina kasoro.

Alisema suala la msingi kwa binadamu ni pamoja na mazungumzo na mazungumzo

yanakuwa mazuri pale harufu inayotoka mdomoni inakuwa nzuri.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania Dk. Flora Fabian katika

hotuba yake ya kumkaribisha mgeni  alisema kuwa wanatarajia katika mkutano huo

watatoka na maazimio ya kuendeleza afya ya meno.

 

 

Ukata wasababisha mgombea ubunge kupitia TLP Handeni kushindwa kufanya kampeni

Na Mwandishi Wetu, Handeni

MGOMBEA ubunge wa Jimbo la Handeni kwa tiketi ya Tanzania Labour (TLP) Mwajabu

Sufiani Mhina ameshindwa kufanya kampeni kutokana na kukosa fedha.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Ofisini kwake mjini hapa, Mwajabu alisema

mbali na uwezo wake mdogo wa kifedha pia amekosa ushirikiano na uongozi wa TLP

mkoa  wa Tanga.

"Nimeshindwa kufanya kampeni sababu uwezo wangu wa kifedha ni mdogo...lakini

sikupata ushirikiano wala kutembelewa na viongozi wa mkoa, sielewi ni kwanini,

wakati niliteuliwa kihalali kugombea nafasi hiyo," alisema Mwajabu.

Mwajabu aliendelea kusema alifuata taratibu zote za kisheria hadi kuteuliwa,

lakini kinachomshangaza ni uongozi wa mkoa huo kutomjali.

Mgombea huyo ambae ni Mwenyekiti wa chama hicho wilayani hapa na ni Mjumbe wa

Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama hicho, alisema mgombea uraisi kupitia TLP

Augustine Mrema ilikuwa afanye ziara ya kampeni wilayani hapa miezi miwili

iliyopita lakini alishindwa kufanya hivyo.

"Sio uongo mgombea wetu (Mrema) ilikuwa aje na nilipigiwa simu kutoka makao makuu

nifanye maandalizi ya ugeni huo, tulishirikiana na uongozi wa wilaya na kata,

tulifanya maandalizi makubwa tuliandaa mabango, bendera na vipeperushi vya kila

aina tukatangaza ujio wa Mwenyekiti," alisema Mwajabu na kuwa pamoja na yote

hakutokea.

"Wakati maandalizi hayo yakiwa yamekamilika usiku wa ujio wa mgombea wetu

nikapigiwa simu na Katibu wa Vijana wa chama hicho mkoa Omari Chombo kuniambia

Mrema hatokuja Handeni," alisema Mwajabu.

Aliendelea kuwa: "Nilipata ugonjwa wa moyo, nilijiuliza nitawaambia nini wananchi

je wale waliopo njiani itakuaje, kulipokucha nilipata wakati mgumu sana

nilijifungia ndani chumbani nilishindwa kutoka."

Mgombea huyo alifafanua kua kutokana na kutokufika kwa Mrema baadhi ya ngome za

chama hicho zimevunjika kutokana na watu kukasirika.

Mwajabu katika kinyang'anyiro hicho cha ubunge anachuana na Mjumbe wa Kamati Kuu

ya CCM Taifa ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mipango na Ubinafsishaji)

Dk. Abdallah  Kigoda na Saidi Mbweto wa CUF. 

 

Tawi  la TLP Kitunda lavunjika

L Wanachama wajiunga CCM

Na Nashon Maingu

TAWI la chama cha TLP liitwalo Ngurwi katika kata ya Kitunda, Manispaa ya Ilala

lenye wanachama 59, limevunjika baada ya wanachama wake kukihama na kujiunga na

Chama cha Mapinduzi.

Kufa kwa tawi hilo kumesababishwa na waliokuwa wanachama wake, kuzikubali na

kuzielewa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo inatangazwa katika kampeni zinazoendelea

za uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Tawi hilo lilikuwa na wanachama 33 wakiwemo viongozi wa kata, ambao wote

walikabidhiwa kadi za CCM na mgombea wa udiwani kata ya Kitunda, Johannes Kisano

(Jaluo). Mwezi uliopita katibu wa CUF wa kata hiyo alijiunga na CCM.

Akikabidhi kadi hizo, Kisano aliwataka wananchi wengine waingie CCM na kuachana na

vyama vya ubabaishaji kama vile TLP na CUF.

Akijibu hoja hiyo ya mgombea udiwani, Mwenyekiti wa tawi jipya la CCM,

lililofunguliwa baada ya kufungwa la TLP, Hussein Mkukila, alisema walikuwa

wanachama wa CCM,  lakini baada ya kulaghaiwa mwaka jana, walijiunga na TLP na

kuwa sasa wanakiri kuwa  mtoto akimkosea mzazi wake na kuondoka nyumbani, iko siku

atarudi tu.

Katibu wa Tawi hilo, F. Waziki alimponda Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema kwa

kutowatembelea. Pia alisema hakuna kiongozi yeyote wa wilaya ama mkoa aliyewahi

kulitembelea tawi hilo tangu kufunguliwa kwake.

Mwandishi wa habari hizi alipomhoji Katibu wa siasa na uenezi CCM, kata ya

Kitunda, Francis Kalokola, kuhusu mwenendo wa kampeni na matumaini ya CCM katika

kata hiyo, alisema wagombea wa CCM wanakubalika kutokana na sera nzuri za chama na

wana uhakika wa kupata ushindi  wa zaidi ya asilimia 90.

"Ni kweli lilikuwepo kundi la wanachama na viongozi waliokuwa wakipinga chama

kutokana na matokeo ya kura za maoni, lakini mambo sasa ni shwari na ndiyo maana

tunatamba kwa jeuri kuwa tutapata ushindi zaidi ya asilimia 90," alisisitiza

Katibu huyo wa siasa na uenezi .

Kata ya kitunda ina matawi 16 na lengo ni kufikisha matawi 20 kabla ya mwisho wa

mwaka huu.

 

Dk. Sheni: Umoja na mshikamano ndiyo siri ya ushindi uchaguzi ujao

Na Mwandishi Wetu, Korogwe

Mgombea mwenza wa urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Ali Mohammed Sheni, amesema umoja

na mshikamano miongoni mwa wanachama na wapenzi wa CCM ndio silaha kubwa

itakayowezesha kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi mkuu ujao.

Dk. Sheni aliyasema hayo alipokuwa akihutubia mkutano wa kampeni uliofanyika Mombo

wilayani Korogwe.

"Sote tushikamane, walio wanachama, wapenzi, wakereketwa wa CCM na wapenda amani,

letu liwe moja, ifikapo Disemba 14 tuipigie CCM  kura zote za ndiyo za urais kwa

Jakaya Kikwete, wabunge na madiwani wote wa CCM.

"Umoja na mshikamano wetu ndio utatuwezesha kukata 'kilomolomo' chao

wapinzani...tuwanyoe kwa wembe ule ule kama ilivyotokea Zanzibar. Tuwaonyeshe

hakuna chama mbadala katika nchi hii zaidi ya CCM," alisema.

Dk. Sheni alisema wananchi wana kila sababu ya kuichagua CCM kwa kuwa ina historia

kubwa ya ukombozi na ujenzi wa nchi kiasi kwamba maendeleo yanaonekana katika

sekta mbalimbali zikiwemo za uchumi na huduma za jamii.

Mgombea Mwenza huyo amebainisha kuwa muda wa upinzani umekwisha na kilichobaki

wakusanye nguvu waipigie kura CCM, maana wapinzani watake, wasitake CCM itashinda

kwa kuwa inapendwa na watu wengi na ndio wanaokiweka madarakani.

"Waambieni hao wapinzani muda wa kukaa huko umekwisha wajikusanye nguvu waipigie

kura CCM maana watake wasitake CCM itashinda kwa sababu inawekwa madarakani na

nyinyi wananchi." alifafanua.

Dk. Sheni alikamilisha ziara yake ya kampeni mkoani Tanga kwa kupokea wanachama

164 wa kutoka vyama vya upinzani wilayani Korogwe wakiwemo 107 TLP, 27 CUF, 28

CHADEMA na wengine wawili kutoka NCCR-MAGEUZI na UDP.

Akiwa njiani kwenda Arusha, ambako alianza ziara ya kampeni jana, Dk Sheni

alisalimiana na wananchi wa Hedaru, Same, Mwanga, njia panda Himo na Hai mkoani

Kilimanjaro, ambapo aliwakumbusha juu ya uchaguzi mkuu ujao na kuwataka kupiga

kura kwa utulivu na wala wasibabaike na wapinzani.

Aliwataka wananchi wasikosee waendelee kuichagua CCM kwa kuwa viongozi wake wana

uwezo na uzoefu mkubwa wa kuongoza nchi tofauti na viongozi wa vyama vingine ambao

amewaelezea kuwa bado ni wachanga.

 

Hongera Tibaigana kwa kuwaepusha madaktari wahuni kupigwa mawe

NIMEMSIKIA  na kumwona Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Dar es Salaam, Alfred

Tibaigana, akiwaeleza madaktari kuacha mpango wao wa kuandamana kwenda eti Ikulu

kuwasilisha malalamiko yao kwamba wanalipwa kiduchu.

Sababu alizotoa Afande Tibaigana kuwazuia madaktari hao, hasa wa hospitali kubwa

ya Muhimbili, kutoandamana ni kwamba ofisi yake haijapokea taarifa kutoka Ofisi

Kuu (Ikulu) kwamba maandamano yao yatapokewa huko.

Kutokana na hatua yake hiyo, Tibaigana akawaambia madaktari hao kwamba iwapo

wanaona upo umuhimu wa kuendelea na maandamano yao, basi wako huru kufanya hivyo

kuelekea kiwanja chochote, lakini si Ikulu.

Nakiri kwamba uamuzi  wa afande huo umeonyesha anavyoweza kutumia kichwa chake

kuepusha shari na dhahama ambazo zinaweza kutokea panapofanyika maandamano holela

na kutaka kuingia Ikulu bila kufuata taratibu zilizopo.

Hata hivyo, Afande Tibaigana ameshindwa kuwaeleza madaktari sababu nyingine muhimu

zaidi hata ya hiyo ya kufuata utaratibu wa kuingia Ikulu, kwamba ‘nguvu ya umma’

ingeweza kabisa kusababisha maafa kwa madaktari hao kutokana na hatua yao ya

kugoma kuwahudumia wagonjwa, na kuacha wengine wakipoteza maisha yao kirahisi

rahisi iwapo wangeandamana.

Nasema amewaepusha na ‘nguvu ya umma’ kutokana na ukweli kwamba, baada ya

madaktari kutangaza mgomo wao kutokana na sababu wanazoeleza kuwa ni ujira mdogo,

ikiliganishwa na majukumu yao, wananchi wengi wamekasirishwa na hatua hiyo na

kuielezea kuwa ni ya kinyama.

Kugoma kwa madaktari maana yake ni kuruhusu vifo vinavyoweza kuzuiwa kutokea

kutokana na wagonjwa kukosa huduma zinazohitajika kwa haraka kuokoa maisha.

Hata hivyo, serikali baada ya kukiri kuwepo kwa malipo kidogo, si kwa madaktari

tu, bali kwa kada zote za ajira za serikali na hata kwa watu binafsi, iliamua

kupandisha mishahara ya madaktari kwa viwango tofauti, huku waliokuwa wakipokea 

zaidi ya sh. 200,000 kwa mwezi wakiongezewa hadi sh. 400,000 na ushei.

Madaktari waligoma wakiishinikiza serikali kuwalipa zaidi ya  sh. milioni 1.2 ili

eti waweze kuishi kwa raha, huku wakitoa huduma  kwa wagonjwa kwa ufanisi mkubwa.

Hao madaktari cha kushangaza, baada ya kutangazwa kwa nyongeza hiyo, ‘wakakaza

kamba’ kwamba hawawezi kuendelea na kazi hadi watakapohakikishiwa malipo ya sh.

milioni 1.2, kima cha chini, kwa mwezi, tena kwa kuanza kulipwa mara moja, si

kusubiri hadi Januari, mwakani kama serikali ilivyoahidi.

Wakielezea msimamo wao huo, madaktari hao walionekana wakiselebuka kwa ‘magoma

motomoto’ ndani ya viwanja vya hospitali ya Muhimbili eti wakifurahia kuendelea na

mgomo wao huku wagonjwa wakiendelea kufa na wengine wakichukuliwa na ndugu zao

kwenda hospitali binafsi.

Kitendo cha madaktari kuendelea na mgomo, huku wakionyesha kejeli kwa wagonjwa 

kwa kucheza muziki na kuwapiga madaktari wenzao wenye moyo na huruma, waliokuwa

wakiendelea kutoa huduma, ni kitendo ambacho kimewakasirisha mno wananchi.

Wananchi wanashindwa kabisa kuwaelewa wasomi hao, wengi wao wakiwa wametumia kodi

za wananchi hao hao wanaowasusa kuwapa tiba leo baada ya kuwa wamepata kazi.

Kitendo cha madaktari kugoma na kuruhusu vifo zaidi ni cha kinyama na hakina

chembe ya ubinadamu wala Utanzania ambao tumeuzoea kwa miaka mingi.

Madaktari wamekuwa kimbilio la wagonjwa miaka nenda rudi, lakini leo vijana wa

kileo walioidandia fani hiyo sasa wanaonekana sawa na mashetani wekundu ambao wao

kutoa roho siyo ‘issue’. Ni kazi ya dakika moja tu ilimradi wanapata ujira wao.

Iweje madaktari hao wajione kwamba ndio wanastahili kupata malipo makubwa zaidi

eti kwa kuwa tu wamesomea taaluma yao kwa muda mrefu au kwa kuwa tu wanahusika kwa

njia fulani na uhai wa binadamu na kusahau kwamba kada zote ni muhimu na

zinazotegemeana katika kuendesha maisha ama maendeleo ya nchi?

Ni wasomi wa namna gani ambao wanajitanabaisha kwa ujinga wa mambo ambayo hata

watoto wa chekechea wanaweza kuelewa baya na zuri kabla ya kuchukua uamuzi wa

hovyo kama huo unaochukuliwa na madaktari, tena Watanzania wenzetu!

Uhakika ni kwamba kama si busara za Afande Tibaigana, madaktari hao wangeandamana

kwenda Ofisi Kuu na wakiwa njiani lazima wangekumbana na dharuba ya mawe na

marungu yanayokwenda sambamba na bakora kwani hakuna mwananchi anayekubaliana na

watoa roho’ (baada ya kugoma) hao ambao wanajali zaidi ubinafsi wa matumbo yao na

ya wategemezi wao na kupuuza uhai wa ndugu zao unaopotea kutokana na uamuzi wa

kijinga.

Taarifa ambazo nadhani hata Afande Tibaigana hakuwa nazo ni kwamba baadhi ya

wananchi walikuwa tayari wameandaa bakora kuwacharaza madakatari hao wakiwa njiani

kuelekea Ikulu kuwasumbua viongozi wetu ambao wako katika mchakato mzito wa

kupambanua mustakabali wa nchi hii.

Kejeli zaidi zilijitokeza juzi kwa madaktari hao kudai kwamba hawana wasiwasi na

ajira zao kwani  serikali haina ubavu wala thubutu ya kuwafuta kazi. Kwamba hakuna

wa kufanya kazi zao ikiwa watafukuzwa! Kumbe watu hao wanajua umuhimu wao kwa

maisha ya Watanzania, sasa iweje waendekeze maamuzi ya hovyo na kijinga namna hiyo

huku wakicheza muziki nje ya wodi za wagonjwa?

Wengi tunafahamu kwamba ingekuwa enzi za ujamaa uliokomaa na ukomunisti uliofikia

kikomo, madaktari hao wasingekuwa na thubutu hiyo kwani kufumba na kufumbua

wangemwagika’ Wachina na Wacuba kama mvua kuwatibu wagonjwa wetu na kuwatupilia

mbali hao wanaojidai na taaluma yao. Bahati yao mambo yamebadilika.

Ninachowaomba madaktari ni kwamba, pamoja na kuwa na hoja zenye mwangwi wa uhalali

wa madai yao, lakini kugoma kwao kunawaumiza wananchi wa kawaida, zaidi ya pengine

wao wanavyodhani kwamba wanaikomoa serikali ambayo kimsingi haiumwi. Wanaoumwa ni

binadamu kama wao.

Wanapaswa kufikiria upya njia nzuri zaidi za kudai ujira mkubwa badala ya kuvaa

roho ya paku na kuruhusu binadamu wenzao kufa eti kwa kuwa wanaomba mlo zaidi kwa

matumbo yao.

Mijadala ndiyo daima imekuwa njia ya kistaarabu kwa watu wasomi kama madaktari

waungwana kutafuta suluhu ya matatizo yao; si migomo, tena migomo yenye kufanywa

huku wahusika wakishuhudia watu wakiteseka na kufa, huku wagomaji wakicheza dansi.

Unyama gani huo mlionao nyie mnaoitwa madaktari!

 

Bodi iondoe adha hii ya wanafunzi kuhemea mikopo

KWA mara nyingine katika kipindi kisichozidi miezi miwili, Bodi ya Mikopo kwa

Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini imelazimika kushinikizwa na wanafunzi ndipo

iwapatie mikopo yao kuwawezesha kuendelea na masomo kwa utulivu.

Baada ya lililowahusu wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, karibu miezi

miwili iliyopita, tukio la hivi sasa ni la juzi ambapo baadhi ya wanafunzi wa Chuo

cha Uhasibu Arusha (IAA) walisafiri kwa mabasi madogo manne waliyokodi kutoka

chuoni kwao mjini Arusha hadi katika ofisi za bodi hiyo mjini Dar es Salaam

kufuatilia mikopo yao.

Walipowasili eneo la ofisi hizo juzi alfajiri, walianza ufuatiliaji kwa maofisa

husika baada ya saa za kazi kuanza, huku wakiahidi kukesha hapo mpaka baada ya

kukamilishiwa malipo yao na ya wanafunzi wenzao waliobaki chuoni. Ilielezwa kuwa

kila mwanafunzi alichangia msafara huo sh. 3,000, na kwamba wanafunzi wapatao 100

ndio waliotumwa Dar es Salaam kuwawakilisha wenzao waliobaki chuoni.

Tunafarijika kwa taarifa iliyotolewa na uongozi wa Bodi hiyo kwamba suala hilo

lilikuwa tayari linashughulikiwa baada ya kuwasiliana na wanafunzi hao, na kwamba

lengo lilikuwa ni kuhakikisha fedha hizo, kiasi cha sh. milioni 168, zinalipwa

jana na hivyo wanafunzi kurejea chuoni.

Lakini pamoja na kufarijika kwa taarifa hiyo, inashangaza kwa nini utaratibu wa

utoaji mikopo hiyo uwe ni wa kusuasua namna hiyo, ambapo hatima yake ni kuwapa

usumbufu wanafunzi ambao wanastahili kuwa vyuoni wakiendelea na masomo bila ya

bughudha kama hizo zilizowasibu wanachuo wa Arusha.

Wakati utekelezaji wa utaratibu huu mpya wa kuwapatia mikopo wanafunzi wa elimu ya

juu unaanza Septemba, mwaka huu, Bodi ilieleza katika taarifa yake namna uitikiaji

wa wanafunzi kujaza na kuwasilisha fomu ulivyokuwa ukienda taratibu mno, na

kulazimika kuwahimiza kuharakisha kujaza fomu hizo ili kuepuka usumbufu.

Lakini kinyume kabisa na taarifa hiyo ya awali ya Bodi, uongozi hivi sasa unaeleza

kwamba wanafunzi wengi mno wamejitokeza katika vyuo mbalimbali kuomba mikopo zaidi

ya ilivyokuwa imekisiwa. Waliojitokeza wanatajwa kuwa ni 37,500 ambapo waliokisiwa

ni 35,194, hali ambayo imeelezwa kuwa inahitaji maandalizi ya ziada kufanikisha

utoaji wa mikopo.

Haja ya kuwepo maandalizi ya ziada ni sawa, lakini maandalizi hayo yazingatie hali

halisi ya umuhimu wa mikopo hiyo kwa mahitaji ya wanafunzi. Fedha zinazotolewa ni

pamoja na za chakula kwa muda ambao wanafunzi watakuwa vyuoni, ada na vitabu.

Yote hayo ni mahitaji muhimu, mengine yakiwa ni ya lazima na ya msingi kwa

binadamu kama chakula, na malazi yanayoangukia katika ada. Hivyo wanafunzi wengi

hawatarajiwi kufanya miujiza kujitosheleza katika mahitaji hayo, hasa ikizingatiwa

halisi ya uduni wa mapato ziliyonayo familia nyingi katika nchi yetu. Matokeo yake

ni kuwaweka wanafunzi katika uwezekano wa kubangaiza huku na kule, wakati mwingine

kuwa katika hatari ya kujiingiza katika vitendo visivyofaa.

Kwamba Bodi inakiri idadi ya wanafunzi waliojitokeza kuomba mikopo ni zaidi ya

ilivyotarajiwa, tulidhani ingekuwa busara kwa Bodi hiyo kuwa na mkakati maalum wa

kutekeleza majukumu yake, ikiwa pamoja na kufanya kazi kwa wakati wa ziada.

Ushughulikiaji maombi mengi namna hiyo lazima ukabiliwe kwa kukusanya nguvu zaidi

na muda mrefu zaidi kwa watendaji wake ili kuwaondolea matatizo wanafunzi. Bila

kufanya hivyo tutazidi kushuhudia ofisi za Bodi zikifurika wanafunzi kutoka chuo

kimoja hadi kingine kila kukicha. Wanafunzi waepushwe na adha hii.