UHURU 26.10.2005

 

Mkutano wa Mbowe Karatu wadorora

  • Wahudhuriwa na idadi ndogo ya wananchi
  • Ngome ya CHADEMA yadaiwa kumong’onyoka

Na Omar Shaaban, Karatu

MKUTANO wa kampeni wa Mgombea wa kiti cha Urais kupitia CHADEMA, Freeman Mbowe

katika jimbo la Karatu lililokuwa likishikiliwa na chama hicho, jana ulidorora

kwa kuwa na mahudhurio hafifu.

Wengi waliohudhuria mkutano huo ni watoto ambao walikuwa wakipiga kelele na

hivyo kumfanya mgombea huyo kukatisha hotuba yake mara kwa mara.

Mkutano huo, ulifanyika katika viwanya vya Halmashauri ya Manispaa ya Karatu.

Kelele hizo zilitokana na watoto hao kupinga hatua ya wazee wachache waliokuwa

wakiwakanyaga.

Mahudhurio hayo yameelezwa kuwa yameshindwa kuvunja rekodi ya mgombea wa kiti

cha urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete ambaye alizoa umati mkubwa wa watu

katika mkutano kama huo uliofanyika hivi karibuni.

Akizungumza katika mkutano huo, Mbowe alisema yuko radhi yeye na wagombea ubunge

kutoshinda ili kuhakikisha amani ya Tanzania isivurugwe.

Katika hotuba yake hiyo, Mbowe mbali ya kukiuka taratibu kwa kuzidisha muda

akiwa jukwaani kwa zaidi ya robo saa, alisisitiza umuhimu wa kudumisha amani

nchini.

Akisisitiza, Mbowe alisema yupo radhi apoteze ushindi wa kiti cha Urais na

wabunge wapoteze viti vyao kuliko amani ya Tanzania ipotee.

Mbowe ambaye katika kampeni amekuwa akitembea kwa Helkopta na kuvuta watu wengi,

alitarajiwa kupata mapokezi makubwa katika jimbo hilo ambalo chama chake

kilikuwa kikilishikilia kwa kipindi kilichopita.

Tifauti na matarajio hayo, jana watoto wa shule ndiyo waliojitokeza kwa wingi na

kuhudhuria mkutano huo, hali inayotafsiriwa kuwa ni dalili za dhahiri za

kuvunjika kwa kile kilichokuwa kinadaiwa kuwa Karatu ni ngome ya Chadema.

 

Tume ya Uchaguzi yafafanua kuhusu majina

  • Yasiyokuwepo vituoni kutopiga kura

Na Mwandishi Wetu

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema wapiga kura ambao majina yao

hayataonekana katika vituo walivyojiandikisha hawataruhusiwa kupiga kura.

Mwenyekiti wa Tume, Jaji Lewis Makame, aliwaambia waandishi habari jana wakati

akiwalezea hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya uchaguzi mkuu Jumapili ijayo.

Alisema uamuzi huo wa Tume unazingatia haja ya kuzuia

mkanganyiko katika suala zima la upigaji kura na kuongeza kuwa utaratibu wa kuwa

na daftari la kudumu la wapiga kura linaanza kutumika kwa mara ya kwanza mwaka

huu nchini, hivyo hakuna uzoefu wa kutosha.

Kuhusiana na wapiga kura ambao picha zao hazitakuwa zinaonekana vizuri, alisema

utafanyika uhakiki wa kulinganisha kitambulisho na ile iliyopo kwenye daftari na

msimamizi atakaporidhika ndiyo atamruhusu.

Aliwashauri watu wote ambao walihama na hawakutoa taarifa ya uhamisho wao kabla

ya Julai 31, mwaka huu kama ilivyotangazwa awali, wapige kura katika vituo

walivyojiandikisha mwanzo, vinginevyo hawataruhusiwa kupiga kura.

Awali, Tume ilikuwa na kikao na viongozi wa vyama vyote vyenye usajili wa kudumu

katika hoteli ya New Africa, kujadili maandalizi ya uchaguzi, ambapo baadaye

Jaji Makame, aliwaambia waandishi wa habari kuwa vyama vimeridhika na hatua

iliyofikiwa.

Uchaguzi utafanyika kati ya saa moja asubuhi na saa 10.00 jioni kwa Tanzania

Bara na Zanzibar itakuwa kati ya saa 1 asubuhi na saa 11 jioni.

Alisema tofauti ya muda inatokana na Zanzibar kuwa na watu watano wanaopigiwa

kura, ambao ni Rais wa Zanzibar na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na

wanaopigiwa kura kwa pande zote za Muungano, ni Rais wa Jamhuri ya Muungano,

Wabunge na Madiwani.

Mwenyekiti alisema kuwa wanawake wajawazito, wagonjwa wazee na walemavu watapewa

kipaumbele katika kuruhusiwa kupiga kura kwanza ili kuwandolea bughudha kutokana

na hali zao.

Jeshi la Polisi nalo jana lilitoa taarifa kuwataka wananchi kuepuka vitendo vya

ugomvi, matusi, kejeli pamoja na mikusanyiko ya aina yoyote wakati wa kupiga

kura na kwamba ni mawakala tu wa vyama vya siasa ndio watakaoruhusiwa kubakia

kwenye vituo.

Taarifa iliyotiwa saini na msemaji wa jeshi hilo, Aden Mwamunyange, ilisema

polisi itasimamia na kuhakikisha hakuna shughuli za kampeni siku ya kupiga kura.

 

Mgombea wa CUF Shinyanga ahojiwa polisi

  • Adaiwa kuhamasisha vurugu siku ya uchaguzi

Na Anthony Komanya, Shinyanga

MGOMBEA Ubunge kwa tiketi ya CUF, Shinyanga Mjini Lutalosa Yemba, anahojiwa na

polisi kwa tuhuma za kuhamasisha vurugu siku ya uchaguzi.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Abdallah Mssika, akiongea na waandishi wa habari

ofisini mwake jana, alisema, mgombea huyo alitumia lugha yenye kuashiria

uvunjifu wa amani wakati akihutubia mkutano wake wa kampeni katika eneo la

Nguzonane juzi.

Mssika, alisema, mgombea huyo aliwataka wapiga kura kutokuondoka kwenye kituo

cha kupiga kura baada ya kutumbukiza kura zao kwa kile alichodai kulinda wizi wa

kura.

Kamanda Mssika, alisema kauli kama hiyo inaweza kuhamasisha uvunjifu wa amani

siku ya upigaji kura endapo kila chama kitawataka wafuasi wake kubaki kwenye

vituo baada ya kupiga kura.

Mssika, alisema kinachotafutwa kutoka kwa mgombea huyo ni ufafanuzi wa kina juu

ya maana halisi ya kauli yake ya Nguzonane ya Oktoba 21, na vituo vya kupigia

kura.

 

 

 

Kinana asema Kikwete anafaa kuwa rais

Na Rodrick Makundi, Vunjo

SPIKA wa Bunge la Afrika Mashariki, Abdurahman Kinana, amemmwagia sifa mgombea

wa kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi, Jakaya Kikwete, na

kumwelezea kuwa ana sifa zinazomstahili kuwa rais.

Kinana ambaye anaongoza timu ya kampeni za CCM kanda ya Kaskazini, alitoa sifa

hizo katika mikutano ya kampeni iliyofanyika juzi katika kata za Kahe, Kirua

Vunjo Kusini, Makuyuni na Mwika Kaskazini.

Alisema mgombea huyo wa kiti cha urais amekuwa waziri ndani ya serikali ya awamu

ya kwanza, ya pili na ya tatu kwa kipindi cha zaidi ya miaka 20, tofauti na

wagombea wa vyama vya upinzani aliodai wengi wao hawana hata ofisi.

Alisema kutokana na uzoefu huo ndani ya serikali, Kikwete ameweza kuzitembelea

nchi mbalimbali duniani na kufahamiana na marais wengi, ambao wengi wao

walimtumia salamu za pongezi baada ya kuchaguliwa na chama kuwania kiti hicho.

Ziara hiyo ya Kinana imefufua matumaini makubwa kwa Chama cha Mapinduzi kuweza

kuyanyakua majimbo manne yanayoshikiliwa na wapinzani kutokana na mikutano yake

kuvuta mamia ya watu.

Aliwaponda wabunge wa vyama vya upinzani akidai kuwa hawana mchango wowote ndani

ya bunge, na kazi yao kubwa ni kupingana na serikali huku wakiendelea kulipwa

mishahara yao ya ubunge.

Alisema wabunge hao wa upinzani hawana uwezo wowote wa kutunga sera wala

hawawezi kuwaletea maendeleo wananchi, na kuwataka wana Kilimanjaro wabadilike,

na wafanye mkataba na serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Katika ziara hiyo ambayo Kinana anafuatana na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa

ya Chama cha Mapinduzi, Grace Soka, ambaye pia ni mratibu wa kampeni za uchaguzi

kanda ya Kaskazini, alifanikiwa kuzoa wanachama wengi kutoka vyama vya upinzani.

Alisema serikali ya Chama cha Mapinduzi itatekeleza kwa vitendo ahadi zake zote

alizotoa mgombea wa urais, ikiwemo kuboresha elimu na kuwatengenezea mazingira

mazuri ya kupata ajira vijana wengi.

Wakati huo huo wagombea wawili wa udiwani katika kata ya Uru Kaskazini katika

jimbo la Moshi vijijini kupitia vyama vya TLP na CHADEMA, wametangaza kujitoa

kuwania nafasi hizo.

Hatua hiyo ni pigo kwa vyama hivyo ambapo sasa mgombea wa kata hiyo kupitia CCM,

Evarist Mombuli, amebaki peke yake na anasubiri kuapishwa baada ya kufanyika kwa

uchaguzi mkuu Jumapili ijayo.

Waliojiengua ni Blasi Mchau (CHADEMA) na Patrick Tarimo (TLP), amabao wote kwa

pamoja wamemwandikia barua msimamizi wa uchaguzi katika jimbo hilo, Robert

Kitimbo, kumuelezea uamuzi wao huo.

 

Elizabeth Minde aahidi utekelezaji wa sera za maendeleo Moshi Mjini

Na Rodrick Makundi, Moshi

MGOMBEA ubunge katika jimbo la Moshi mjini, Elizabeth Minde, amesema iwapo

atachaguliwa katika uchaguzi wa mwaka huu atatoa msukumo kwa chama na serikali

itekeleze sera zinazolenga kuleta maendeleo kwa wananchi wa jimbo hilo.

Aliyasema hayo jana wakati wa mahojiano maalum mjini hapa, ambapo pamoja na

mikakati mingine alisema CCM imelenga kuboresha maisha ya wakazi wa Moshi, kwani

miongoni mwa sera zilizoko kwenye ilani ya CCM imewalenga wananchi wa jimbo hilo

katika kuwaletea maendeleo.

Alieleza kuwa ilani imeainisha majukumu ya serikali ya kuwavutia wawekezaji

ambao watakuja kuwekeza na kutoa ajira kwa vijana na kinamama, na kuongeza kuwa

hatua hizo zimeanza kuonekana ambapo kituo cha uwekezaji cha kanda na mkoa

kimezinduliwa mkoani hapa kwa ajili ya kuainisha maeneo ya kuwekeza.

Minde aliongeza kuwa mji wa Moshi umeshuka kiuchumi na hilo limetokana na

kushuka kwa zao la kahawa ambalo lilitegemewa na wakazi wa Moshi, na kuongeza

kuwa sera za CCM zimeeleza mipango ya kufufua zao hilo.

Pia alisema pamoja na mipango hiyo ya serikali na kwa mujibu wa ilani ya CCM,

jukumu kubwa ni la kuwakomboa wananchi katika umasikini kwa kuwawezesha kujikimu

kimaisha, na hali hiyo inaweza kutatuliwa kwa kufufua viwanda vilivyokufa ili

kuwezesha wananchi kupata ajira.

Minde alisema viwanda ndio kitovu cha maendeleo kwa wananchi kwani uchumi

utapanuka zaidi iwapo viwanda vitafanya kazi.

"Hapa Moshi katika kipindi cha hadi mwaka 1995, tulikuwa na viwanda vinane

vilivyokuwa vikifanya kazi, lakini viwanda hivi vimekufa na hili limesababisha

uchumi wa mkoa kuanguka na wananchi wengi wameshindwa kujiendesha, maana hata

zao la kahawa nalo lilikuwa linashuka. Hivyo tuna kazi kubwa ya kuweka mikakati

ya kufufua vitu vyote hivi ili kuinua upya uchumi wa mkoa," alisema mgombea

huyo.

Azungumzia nafasi za wanawake kujitokeza kugombea nafasi mbali mbali alisema

mfumo dume bado unaonekana kuwatatiza wanawake kujitokeza kugombea katika

uchaguzi mbali mbali, akatoa wito wanawake wapambane na mfumo huo kwa kujitokeza

kwa wingi kuwania nafasi mbali mbali za uongozi siyo wa siasa tu, bali hata wa

sehemu za kazi.

"Wanawake wako wengi wenye uwezo na wanaojieleza vizuri, lakini wanahofia maneno

ya kashfa na kejeli ambayo yanajitokeza wakati wa kampeni. Hili limekuwa tatizo

na pia ili mwanamke aweze kuongoza inabidi awe na uwezo mara mbili ya mwanamme

ndio atapewa nafasi," alisema.

Kwa upande wa huduma za kijamii aliipongeza serikali kwa kuboresha huduma hizo

ambazo ni afya kwa kufanya ukarabati wa hospitali ya mkoa Mawenzi, kuongeza

zahanati kwa takribani kata zote mkoani Kilimanjaro, kusambaza huduma za maji

kwa wananchi, na kusema serikali itaendelea kuwahudumia wananchi kwa kuboresha

huduma hizo na kukamilisha utekelezaji wa huduma nyinginezo.

Aliwataka wana-CCM mjini Moshi kuwahamasisha wananchi kuipigia kura CCM katika

uchaguzi wa Oktoba 30 mwaka huu, ili kutekeleza ahadi zilizotolewa kwa wananchi

na ambazo zimo kwenye ilani ya ucahguzi wa mwaka huu.

 

 

Mgombea ubunge wa CUF Gairo asalimu amri na kurejea CCM

Na Stanslaus Likomawagi, Kilosa

Ikiwa zimebaki siku ne kuhitimisha kampeni na kufanyika Uchaguzi

Mkuu, mgombea ubunge katika jimbo la Gairo kwa tiketi ya CUF, Dk. Stanley

Lemnyambwa, amejing’atua kutoka chama hicho na kujiunga na CCM.

Lemnyambwa aliikimbia CUF baada ya kukabidhi kadi yake ya uanachama wa chama

hicho namba 0850506 ya mwaka 2000, kwa mgombea mwenzake wa ubunge kwa tiketi ya

CCM katika jimbo la Gairo, Ahmed Shabiby.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukabidhi kadi kwa Shabiby, mgombea

huyo alizitaja sababu za kujitoa kwake katika kuwania ubunge kwa tiketi ya CUF,

ni kutelekezwa na uongozi taifa wa chama hicho katika kaMpeni zake za kuwania

ubunge.

Alisema tokea kuanza kwa kampeni za ubunge uongozi wa taifa wa chama

alichokihama umemtelekeza na haujampa msaada wa kikampeni katika jimbo alilokuwa

akiwania la Gairo.

Alisema alishangazwa na uongozi wa taifa wa CUF kumpa Sh. 250,000 kwa ajili ya

kununulia vifaa vya kampeni bila kujali Angeishi vipi katika mizunguko yake ya

kampeni hizo.

Alieleza kuwa kampeni siyo vifaa pekee, bali ni pamoja na kula na kulala katika

maeneo mbali mbali anayotembelea katika jimbo lake, ambako ni mbali na nyumbani

kwake.

Dk. Lemnyambwa alisema alishangazwa kuona kuwa pamoja na kuamua kuiwakilisha CUF

jimboni Gairo, amekuwa akipata ushirikiano mdogo kutoka uongozi wa taifa, kiasi

cha kushindwa kuteua meneja wake wa kampeni.

Hata hivyo, alisema kuwa kikubwa zaidi kilichomkatisha tamaa ni uongozi wa CUF

kutokuwa wakweli katika suala zima la ruzuku kwa wagombea wake wa nafasi

mbalimbali.

“Tangu kuanza kwa nyimbo za kupewa ruzuku kwa ajili ya kampeni, mpaka leo

(jana), hakuna chochote nilichopewa pamoja na kuwa zimebakia dakika za

majeruhi,” alisema Dk. Lemnyambwa. Mgombea huyo alisema ameshangazwa na mgombea

wa urais kwa tiketi ya CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, kufika katika jimbo lake

kumnadi akiwa ameongozana na magari zaidi ya 10, wakati yeye akitumia baiskeli

na wakati mwingine kulazimika kutembea kwa miguu kusaka kura katika baadhi ya

vijiji na kata.

Alidai kitendo hicho kimemuonesha kuwa CUF ianajali maslahi ya ubinafsi zaidi

kuliko maslahi ya chama kama ilivyo katika Chama cha Mapinduzi.

Dk. Lemnyambwa alisema hakuwa na sababu ya kuendelea kukaa kwenye chama chenye

ahadi za uongo kwa wagombea wake, hali ambayo alidai itamuwia vigumu kutimiza

ahadi anazotoa kwa wananchi wakati wa kuomba kura.

Wakati huo huo mgombea wa jimbo la Gairo kwa tiketi ya CCM, Ahmed Shabiby na

timu yake, wamesambaratisha ngome ya CUF katika kijiji cha Dumila jimbo la

Kilosa.

Timu hiyo ya wana-CCM ilikwenda jimboni Kilosa kumuunga mkono mgombea wake wa

ubunge Mustafa Mkullo.

Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja wa kampeni za CCM jimbo la Gairo, Dan

Mwenegoha, alisema timu hiyo ya wana-CCM ilimwaga sera na ilani ya CCM, kiasi

cha kuisambaratisha ngome hiyo ya CUF na wanachama wake 45 kurudisha kadi na

kujiunga na CCM.

 

Njama za kufanya vurugu zagunduliwa

Na Fadhili Abdallah, Kigoma

Serikali mkoani Kigoma imegundua njama zinazopangwa na chama kimoja cha siasa

katika wilaya ya Kigoma, zenye lengo la kufanya vurugu siku ya kupiga kura.

Mkuu wa wilaya Kigoma, Henry Clemence, aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa

jana, kuwa serikali imegundua njama za chama hicho ambacho kimepanga

kuwavisha sare za CCM wafuasi wake ili ionekane wanaofanya fujo ni wafuasi wa

CCM.

Clemence alisema kamati ya ulinzi na usalama wilayani imekutana na imeweka

mkakakti wa kuhakikisha wote wenye lengo la kufanya vurugu siku hiyo

wanadhibitiwa, na kuchukua hatua zinazostahili.

Mkuu huyo wa wilaya amewaonya wananchi wilayani humo wasikubali kutumiwa na watu

wanaotaka kuanzisha vurugu ambazo zitahatarisha usalama na amani wa watu

wilayani humo.

Pia aliwataka wananchi wote siku ya kupiga kura kwenda kupiga kura na baadaye

kuendelea na shughuli zao nyingine, badala ya kukaa vituoni bila kuwa na

shughuli yoyote jambo ambalo linaweza likawa chanzo cha kuzuka kwa vurugu.

Pia alitoa wito kwa wapiga kura kufuata maelekezo ya wasimamizi wasaidizi katika

vituo vya kupigia kura, ili kuepusha ugomvi usio wa lazima na kuchangia

kuvurugika kwa upigaji kura.

Sambamba na hayo, mkuu huyo wa wilaya aliwataka wananchi wilayani humo matokeo

yatakapotolewa, kusherehekea ushindi wa mgombea atakayeshinda kwa amani, bila

kuathiri shughuli za watu wengine na kuanzisha vitendo ambavyo vinaweza

kusababisha ugomvi na uvunjifu wa amani.

 

 

Aonya vyama vya upinzani vidhibiti wanachama wao wasifanye fujo

Na Mwandishi Wetu, Moshi

MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Hilda Ngoye, amevitaka vyama vya siasa vinavyowania

uongozi mkoani humo, kuwadhibiti wanachama wao na kufanya kampeni za kistaarabu

ili kuepusha vurugu zinazowaathiri wananchi na wanachama wa vyama hivyo.

Hilda alisema serikali mkoani humu haitovumilia vitendo vinavyofanywa na baadhi

ya vyama vinavyolenga kuhatarisha hali ya amani.

Kauli ya mkuu wa mkoa imetolewa kufuatia vurugu zinazotokea katika baadhi ya

mikutano ya kampeni za vyama vya siasa kwenye maeneo mbali mbali ya mkoa wake.

Alisema kila vurugu zinazopotokea kila chama kinachodaiwa kufanya kinakataa

kuhusika na vurugu hizo, jambo ambalo linasumbua serikali.

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro alikutana na viongozi wa vyama vya siasa ngazi ya

mkoa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi na vyombo vya dola, ambapo aliwapa kazi wadau

hao kuhakikisha wanaepusha vitendo vinavyoashiria kuvuruga amani wakati huu wa

kampeni na siku ya uchaguzi.

Alisema serikali haitovumilia vitendo vya uvunjaji wa amani, na atakayebainika

kushiriki katika kupanga au kufanya vurugu atawajibishwa kwa mujibu wa sheria za

nchi.

Vyama vya siasa mkoani hapa vimekuwa vikiendelea na mikutano ya kampeni, ambapo

baadhi yake imekuwa ikiripotiwa kutokea vurugu zinazosababishwa na wanachama

huku malalamiko yakiangukia kwa wagombea kuhusika katika kupanga vurugu hizo.

Wakati serikali ikitoa tamko hilo mgombea urais wa TLP, Augustine Mrema,

amedaiwa kufanya mikutano katika jimbo la Vunjo kinyume na mwongozo wa ratiba za

kampeni.

Akihojiwa kwa njia ya simu jana, msimamizi wa uchaguzi wa majimbo ya Vunjo na

Moshi vijijini, Robert Kitimbo, alisema kulikuwa na hali ya vurugu baada ya

Mrema kuhutubia wananchi wa eneo la Himo.

Alisema Mrema alipaswa kuendesha kampeni zake katika wilaya ya Hai, na akadai

kuwa baada ya kuzuiwa alichukua jukumu la kuhamishia mkutano huo eneo jingine

ndani ya jimbo hilo la Vunjo.

Hata hivyo, alidai polisi wanaoongozwa na mkuu wa kituo cha Himo wamefuatilia

eneo hilo la mkutano ili kuzuia mkutano huo uliokiuka ratiba.

Alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo, Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro, Dk.

Mohammed Chicco, alidai kuwa hana taarifa kamili za tukio hilo ambalo polisi

inafuatilia kupata taarifa sahihi kuhusiana na kuvurugwa ratiba za kampeni.

 

 

 

Rais Mkapa atetea msimamo wa Mugabe kuwapatia ardhi wananchi

  • Asema ni wa haki na unalenga kuwajali watu wake

Na Mwandishi Wetu

RAIS Benjamin Mkapa amesema msimamo wa Rais wa Zimbabwe juu ya kuwapatia

wananchi ardhi isiyotumika ni wa haki na unalenga kuwajali wananchi wake.

Mkapa alitoa msimamo huo juzi nchini Zimbabwe wakati wa chakula cha jioni

kilichoandaliwa kwa heshima yake na Rais Robert Mugabe.

Katika hotuba ambayo nakala ilipatikana mjini Dar es Salaam, Rais alisema

haikubaliki na wala haingii akilini kuona Waafrika wanakosa ardhi ya kulima

wakati watu wachache wanayo ardhi ya kutosha lakini hawaitumii.

“Kwa kipindi kirefu Afrika imefundishwa masuala ya siasa, uchumi na haki za

binadamu, sasa muda umefika kwa Afrika kujipanga upya na kutetea haki, tuchukue

madaraka ya kujiamulia mambo yetu na siyo kushinikizwa na nchi za nje,” alisema.

Alisema uongozi mpya wa Afrika hautakubali kuongoza nchi kwa matakwa ya watu wa

nje na kwamba uongozi mpya utasikiliza mawazo ya viongozi wa Afrika wazoefu ili

wafanye kazi kwa manufaa ya Afrika.

Alisema Afrika itafanikiwa ikiwa Waafrika watakuwa na msimamo mmoja na

kusaidiana na kwamba nchi za Afrika hazina budi kuunga mkono msimamo wa Zimbabwe

kuhusu umuhimu wa kuwapatia ardhi wananchi.

Zimbabwe imekuwa na mgogoro na baadhi ya nchi za Ulaya kwa madai ya kukiuka haki

za binadamu kufuatia kitendo cha nchi hiyo kugawa ardhi iliyokuwa ya wazungu kwa

wananchi wasio na ardhi.

Lakini pia wazungu walidai uchaguzi wa Zimbabwe haukuwa huru na wala haukuwa wa

haki.

Rais Mkapa alimhakikishia Rais Mugabe na wananchi wa Zimbabwe kwamba Tanzania

itasimama daima upande wa Zimbabwe na kwamba vitendo vya nchi za Ulaya kuiwekea

vikwazo Zimbabwe vitakwama ikiwa Afrika itaendelea kuwa na umoja.

Katika Ukanda wa Kusini mwa Afrika, tunayo Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za

Kusini mwa Afrika (SADC) ambayo kwa kweli inaweza kuzisaidia sana nchi wanachama

ikiwa tutaimarisha,” alisema

Alisema SADC haina budi kuimarisha teknolojia ya habari na mawasiliano (ICT),

ili kuboresha masuala ya biashara na mawasiliano baina ya nchi wanachama wa

Jumuia hiyo.

Rais Mkapa alisema nchini za Tanzania na Zimbabwe zina uwezo wa kila kitu na

kwamba kinachotakiwa ni kuangalia uwezekano wa kampuni za ndani ya nchi hizo

namna ya kufanya biashara.

 

Wapambe wa Murji wadai ni ndumilakuwili

  • Ni baada ya kutaka kuhama CCM, kisha akaghairi

Mwandishi Wetu, Mtwara

KIGUGUMIZI kilichompata Hasnein Murji mbunge aliyemaliza muda wake cha kutangaza

nia ya kuhama Chama cha Mapinduzi na baada ya muda kughairi kumemfanya aonekane

ndumilakuwili mbele ya wapambe wake.

Wapambe ndani ya kambi yake imemshtukia na kumwambia kuwa anawapeleka pabaya.

Habari za kuaminika zinadai kuwa wapambe wengi wamemtosa kutokana na kugundua

kuwa maamuzi yake siyo ya busara na ameweka mbele zaidi maslahi yake kuliko ya

Chama na wananchi.

Kambi ya mbunge huyo wa zamani ambaye aliwahi kuwa wa Jimbo la Mitema,

Tandahimba na akatoka kugombea jimbo la Newala ambako alikuwa mbunge katika

bunge lililopita, inadaiwa imeisumbua sana kampeni ya Chama katika jimbo hili

kutokana na undumakwili wake.

Kwa mujibu wa watu walio karibu yake ambao baadhi yao walikuwa waratibu wa

mikakati yake ya kumwezesha kunyakua ubunge wa jimbo hili, Murji alipata wakati

mgumu siku aliyotishia kutaka kuondoka CCM baada ya kugundua wengi waliokuwa

wanamshabikia walikuwa wanafikina kwamba hawakuwa tayari kuungana naye kwa hatua

hiyo.

"Unajua huyu jamaa alipiga hesabu vibaya na kuona kuwa akiingia upinzani atavuna

watu, hasa viongozi wa CCM na wagombea wa udiwani aliowasaidia kushinda kura za

maoni," alidai mmoja wa watu muhimu katika kundi lake.

"Alikuwa hajui kuwa watu wamebadilika na baada ya kutafakari na kuona

anatupeleka pabaya huyu jamaa anaonekana kuwa na staili za Mrema," alisema

mpambe huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa kuhofia usalama wake.

"Hawa watu wa Murji wanataka kutufanya watu wajinga, watuburute kwa manufaa yao,

tunajua kuwa wao wana mikataba, sasa sisi wananchi tukimbilie tu," alisema

mwananchi mmoja katika baa moja maarufu mjini hapa kufuatia habari zilizokuwa

zimezagaa kuwa amehama Chama Cha Mapinduzi.

Habari kutoka maeneo mbali mbali ya mji zinadai kuwa wengi walisema heri aondoke

CCM kutokana na kambi yake kuwasumbua watu kwa kuwashawishi wapigie upinzani,

kuandaa vijana wa kuzomea mikutano ya CCM bila sababu.

Murji aliyekuwa amepambana na Mohamed Sinani katika kura za maoni ya CCM katika

kinyang'anyiro cha ubunge Mtwara Mjini na kuongoza kwa kuzoa kura 314 na

kumwacha mbali mwenzie aliyepata kura 92 alienguliwa na Halmashauri Kuu ya Taifa

ambayo ilimpendekeza Sinani.

Tangu uteuzi huo ufanyike kumekuwa kukijitokeza matukio mengi mabaya katika

kampeni ya CCM yanayodaiwa kufanywa na kambi yake inayodaiwa kukataa kuivunja,

ingawa alinukuliwa mara mbili na gazeti hili akidai kuvunja kambi hiyo.

Lakini katika hatua ambayo haikutarajiwa wiki hii alitaka kula matapishi yake

alipotangaza kukihama Chama na kuingia upinzani, lakini juzi alibadili msimamo

kwa kudai ilikuwa uamuzi huo ulitokana na hasira.

 

 

Shirika la Umeme Z’bar lakamilisha matengenezo ya laini kubwa

Na Khatib Suleiman, Zanzibar

SHIRIKA la Umeme la Zanzibar limesema kazi ya kuzifanyia matengenezo laini kubwa

za kupitisha umeme kutoka Bara yamekamilika ambapo sasa umeme huo hautapotea

tena njiani wakati ukitoka katika gridi ya taifa.

Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme la Zanzibar, Suleiman Juma alisema kwamba

matengenezo hayo muhimu yamekuja baada ya kuwepo kwa uchakavu mkubwa wa vikombe,

bolti pamoja na minara ambayo ilikuwa tayari imeanza kuota kutu huku ikiwa

katika hatari ya kuanguka.

Minara hiyo ambayo tangu kuwekwa kwake katika mwaka 1979 ilikuwa haijafanyiwa

matengenezo yeyote makubwa, na kuwepo katika hali mbaya ambapo kama ingelianguka

basi shirika hilo lingepata hasara kubwa.

“Sasa tunao uhakika wa kuitumia minara hii kwa muda mrefu bila ya kuifanyia

matengenezo, kwani ukarabati umefanywa kwa kutumia teknolojia ya kisasa ambapo

umeme haukuzimwa katika kipindi chote cha matengenezo,” alisema Juma.

Matengenezo hayo yaliyofanywa na kampuni ya MACDONALD kutoka Tanzania Bara

ambapo walifanya kazi za kuweka nati na bolti pamoja na kubadilisha vikombe

vilivyoharibika katika kipindi chote bila ya kuzima umeme.

Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya MACDONALD, Donald Mwakemela alisema kazi ya

kuifanyia ukarabati minara 20 ilikuwa kubwa, kutokana na baadhi ya vifaa

vilivyomo ndani yake kuwa vimeharibika kabisa na hivyo kulazimika kutafuta

vipuri vingine nje ya nchi.

Alililitaka Shirika la Umeme la Zanzibar kuwatumia vijana waliofanya matengenezo

hayo ambao ni kutoka Visiwani ili kuepuka shirika kutafuta mafundi wengine

wakati wanapotaka kufanya matengenezo mengine madogo madogo.

Jumla ya mafundi 20 wa hapa walishirikiana na kampuni ya MACDONALD chini ya

Mwakemela katika kufanya matengenezo ya minara hiyo ambapo katika kipindi cha

miezi sita ya kazi hiyo umeme haukuzimwa hali ambayo imewafanya wananchi kufanya

shunguli zao bila ya usumbufu.

 

Sumaye awataka waandishi wa habari kujiendeleza kitaaluma

Asifu mkakati wa TAMWA kusomesha wanachama wake

Na Mwandishi Wetu

WAZIRI Mkuu Frederick Sumaye amewakumbusha waandishi wa habari umuhimu wa

kujiendeleza na wamiliki wa vyombo vya habari kuweka mkakati wa kutoa mafunzo

kwa wafanyakazi wao.

Sumaye alitoa ushauri huo juzi jioni alipozungumza na waandishi wa habari kutoka

vyombo mbalimbali aliowaandalia chakula nyumbani kwake Oysterbay jijini Dar es

Salaam kwa lengo la kuwaarifu rasmi kustaafu kwake.

“Tabia ya kunyang'anyana waandishi wachache waliosoma ni mbaya na ina mwisho

wake, hivyo ni jukumu la kila mwaajiri kusomesha waandishi wake ili chombo chake

kiheshimike,” alisema.

Waziri Mkuu alipongeza mkakati wa Chama cha Waandishi Wanawake Tanzania (TAMWA)

wa kuchangisha fedha za kuwasomesha wanachama wake kwamba ni wa kuigwa na kila

taasisi ya habari.

Akizungumza maendeleo ya habari nchini, Waziri Mkuu aliwashauri waandishi wa

habari kuacha tabia ya kuikashifu nchi yao na kutangaza mabaya kwa wageni.

Sumaye alisema serikali imefanya mambo mengi mazuri, lakini vyombo vya habari

vimekuwa vikiripoti mambo madogo madogo ambayo hayana msingi, na kwamba mambo

hayo yamechangia kupotosha nchi za nje.

"Nchi ni yetu na ninyi ni yenu… hivyo ni yetu sote,” alisema na kuongeza kwamba

waandishi wa habari nchini hawana budi kujenga tabia ya uzalendo kwa kutangaza

mazuri yanayohusu Tanzania kwa wageni.

Alisema serikali ya awamu ya tatu imejitahidi kuweka misingi mizuri ya utawala

bora, kufuata sheria na kutekeleza mipango ya maendeleo kwa uhakika, lakini mara

nyingi habari zilizotawala ni zile zinazokebehi jitihada hizo na

zinazodhalilisha taifa.

Akizungumzia janga la ukimwi, Sumaye ameonya kwamba ugonjwa wa ukimwi una uwezo

wa kuangamiza ukoo au kabila, endapo tu wahusika wataendekeza vitendo

vinavyosababisha kuenea kwa virusi vya ugonjwa huo.

Alisema takwimu za maambukizo zinatisha na kwamba mara nyingi wanaokumbwa ni

watu wanaotegemewa na familia au serikali kwa jumla, jambo ambalo aliwasihi

waandishi wa habari kuongeza kasi ya kuandika athari za ugonjwa huo ili wananchi

wabadili tabia.

Kuhusu uchaguzi mkuu ujao, Waziri Mkuu aliwataka waandishi wa habari kutoa

taarifa zinazotoa matumaini kwa wananchi kwa nia ya kuimarisha umoja wa kitaifa

na siyo kusambaratisha.

Alisema ni hatari kutoa taarifa za uchochezi, bali vyombo vya habari viendelee

kukemea vurugu zinazochochewa na wanasiasa uchwara.

Kwa upande wao, waandishi wa habari walimpongeza Waziri Mkuu Sumaye kwa uwazi na

kushirikiana vizuri na vyombo vya habari katika kipindi chote cha uongozi wake.

 

 

NBC Ltd waendelea na kazi

Na Mwandishi Wetu

WAFANYAKAZI wa benki ya NBC Ltd nchini jana waliendelea na kazi baada kusitisha

mgomo wao tangu juzi mchana kufuatia ombi la menejimenti kushughulikia tatizo la

kutiwa saini mkataba wa hali bora kabla ya Ijumaa ya wiki hii.

Juzi, wafanyakazi wa benki hiyo matawi mbalimbali yakiwemo ya Arusha, Dodoma,

Zanzibar na Dar es Salaam waligoma kazi ili kushinikiza menejimenti ikubali

kutia saini mkataba wa hiari na hali bora ya mafao.

Hata hivyo kuanzia saa saba juzi hadi jana, wafanyakazi wa matawi karibu yote

yaliyohusika na mgomo waliendelea na kazi kama kawaida baada ya kukubali ombi la

menejimenti.

Menejimenti iliwaomba wafanyakazi suala la kutiwa saini au kutotiwa litajulikana

siku ya Alhamisi na iliomba wachukue hatua yoyote baada ya siku hiyo.

Katibu wa chama cha wafanyakazi wa viwanda na biashara, taasisi za fedha, huduma

na ushauri (TUICO) Generose Beatus jana aliendelea kuwa mzito wa kutoa habari,

lakini habari zilizopatikana zilisema TUICO na menejimenti walifanya kikao

ambacho kilikubaliana kwamba suala la kutiwa saini lifanyike siku ya alhamisi.

Tukio hilo litafuatiwa na taarifa rasmi itakayotolewa kwa ujumla na pande zote

mbili.

Wakati huo huo, menejimenti ya NBC Ltd iliwaomba radhi wateja wake kwa tukio la

kukosa huduma baada ya wafanyakazi kugoma juzi.

Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo Christo De Vries alisema jana tukio hilo

lilitokea kwa bahati mbaya na kwamba halitatokea tena.

Vries alisema juhudi zinafanyika kwa nguvu zote ili kuepusha tukio kama hilo

lisitokee tena na kwamba menejimenti na TUICO wana uhakika watamaliza mambo hayo

kwa maelewano mazuri.

 

Kasi ya mageuzi ya uchumi yaongezwa

Na Solomon Mwansele, Mbarali

SERIKALI imeamua kuongeza kasi ya mageuzi ya kiuchumi kwa kuandaa mipango ambayo

itachochea ukuaji endelevu wa uchumi na maisha ya wananchi vijijini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera), William Lukuvi

wakati akifungua mfumo wa utumiaji wa stakabadhi za mazao kwenye maghala

unaosimamiwa na Programu ya Uendelezaji Mfumo wa Masoko ya Mazao ya Kilimo

(AMSDP), katika kata ya Chimala wilayani Mbarali.

Lukuvi alisema mojawapo ya mazingira hayo ni kuwepo kwa masoko ya kuaminika

vijijini ambako ndiko kuna shughuli za kilimo.

Alisema wafanyabiashara na wakulima wadogo wanafanya shughuli zao mmoja mmoja na

hivyo kukosa uwezo wa kunadi bidhaa zao katika masoko kwa sababu ya ufinyu wa

soko.

"Siyo hivyo tu, wakulima hawa pia hawana habari zozote kuhusu soko hili ikiwa ni

pamoja na kutofahamu bei za bidhaa katika masoko hayo na kushindwa kupata mikopo

itakayowawezesha kuhifadhi mazao yao hadi wakati wa bei nzuri," alisema.

Aliongeza kuwa hali hii kwa kiasi kikubwa inamwathiri mkulima mdogo kwa sababu

hulazimika kulipia gharama za kusafirisha mazao yake kwenda kwenye soko na kuwa

katika baadhi ya vijiji hakuna maghala ya kuaminika.

Pia alibainisha kuwa mfumo wa stakabadhi za mazao kwenye maghala unaweka

utaratibu wa kisheria wa kuainisha na kutoa leseni kwa waendeshaji wa maghala ya

kuhifadhia mazao.

"Utaratibu huu huwapa uwezo wa kisheria watunza maghala hayo kutoa stakabadhi

kwa wakulima au wafanya biashara wa mazao ya kilimo watakaotunza mazao yao

kwenye maghala" alisema Lukuvi.

Alisema stakabadhi hizo ambazo hujulikana kama 'Stakabadhi za Maghala', zina

hadhi na thamani kama zilizonazo nyaraka za fedha kama vile hundi.

Lukuvi alisema kwa kutumia stakabadhi hizo, wakulima watapata mikopo kwenye

asasi za fedha kwa kuziweka rehani.

Naye mratibu wa wa Programu ya AMSDP, Nathaniel Katinila alisema madhumuni ya

programu hiyo ni kumuongezea kipato mkulima ili kupunguza makali ya umasikini na

hatimaye kuuondoa kabisa.

Katinila aliongeza kuwa utekelezaji wa programu hiyo utagharimu kiasi cha sh.

bilioni 48 na utatekelezwa katika halmashauri za wilaya 38 katika mikoa minane.

Aliitaja mikoa hiyo kuwa ni Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Mbeya, Iringa,

Ruvuma na Rukwa.

 

Amuua kwa kumchoma kisu 'bwana wa nje' wa dada yake

Na Pendo Mangala, Dodoma

POLISI Mkoani hapa inamshikilia Mazengo Chigonela (45) mkazi wa kijiji cha

Kiterela katika manispaa ya Dodoma kwa tuhuma ya kumuua kwa kumchoma kisu Ali

Simoni (37) wa kijiji hicho.

Hayo yalisemwa jana na kamanda wa polisi wa mkoa wa Dodoma Omari Mganga

alipokuwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake mjini hapa.

Mganga alisema tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki katika kijiji hicho baada

ya kuzuka ugomvi baina ya Nyerere Seif na Semeni Mazengo ambao ni mtu na mkewe.

Alisema ugomvi huo ulizuka kati ya wanandoa hao ambao walikuwa wakinywa pombe

katika klabu na kuanza kutoleana matusi.

Mganga alisema baada ya ugomvi huo, marehemu Simoni ambaye anadaiwa kuwa ni

'bwana' wa Semeni, aliposikia ugomvi huo akiwa ndani ya klabu alikwenda

kuwaamulia wanandoa hao.

Chigonela ambaye ni kaka wa Semeni naye alikuwa ndani akipata kinywaji,

alikwenda kuamulia ugomvi huo na alipowafikia alitoa kisu na kumchoma Simon

ubavuni na kusababisha kifo chake papo hapo.

Alifafanua kwamba, awali kulikuwa na uhusiano wa kimapenzi kati ya marehemu huyo

na Semeni na kwamba uhusiano huo umekuwa ukichangia kuwepo kwa ugomvi kati ya

ndoa ya Nyerere Seif na mkewe.

Kutokana na tukio hilo, polisi mkoani hapa inatarajia kumfikisha mahakamani hivi

karibuni mtuhumiwa Chigonela.