UHURU 12.11.2005
Maregesi asema uchaguzi si vita, bali ni demokrasia
Wanawake nchini watakiwa kubuni miradi ya maendeleo
TRA yaasa wafanyabiashara kuacha tabia za ‘kimachinga’
Nchi za Maziwa Makuu zapongezwa kwa kusuluhisha migogoro
Klabu za waandishi wa habari zatakiwa kuanza kuitenga CUF
Wana-CCM wote ni wagombea katika uchaguzi mkuu-Mangula
Maregesi asema uchaguzi si vita, bali ni demokrasia
Na Thomas Mtinge, Kilolo
MWENYEKITI wa Jumuia ya Wazazi Taifa, Abiud Maregesi, amesema kwamba uchaguzi si vita, bali ni sehemu ya kutimiza demokrasia kwa vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi wowote. Aliyasema hayo juzi kwa nyakati tofauti wakati akiwahutubia wananchi katika mikutano ya hadhara iliyofanyika katika vijiji mbalimbali vilivyoko katika Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa.Maregesi alisema mtu au chama kinaposhiriki katika uchaguzi Fulani, lazima
kikubali kushindwa au kushinda kwa kuwa huo ni utaratibu wa uchaguzi.
Alisema anasikitishwa na kauli ya CUF kukataa matokeo ya uchaguzi wa Zanzibar
wakati walijua kabisa kwamba katika uchaguzi huo wameshindwa na kuongeza
kuwa kukataa kwao kuutambua ushindi huo kuna lengo la kuwahadaa wananchi.
Alishangaa CUF kutoitambua serikali ya Rais Karume wakati huku tayari wajumbe wa
Baraza la Wawakilishi walioshinda katika uchaguzi huo wameapishwa na kuahidi
kuilinda katiba ya Zanzibar.
Kwa mujibu wa Maregesi, endapo CUF itakataa kukubali serikali ya Karume, basi
isingekubali wawakilishi wake kuapishwa.
Wanawake nchini watakiwa kubuni miradi ya maendeleo
Na Pendo Mangala, Dodoma
WANAWAKE nchini wametakiwa kuwa wabunifu katika kuanzisha miradi mbalimbali ya
maendeleo ambayo itawasaidia kuwaongezea vipato na kuondokana na umaskini.
Wito huo ulitolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Luteni mstaafu Shabani
Muyombo wakati alipokuwa akiongea na wafanyabiashara wa mkoa huo katika mafunzo
ya siku tano ya udhibiti wa ubora wa vyakula na uongozi wa biashara
yaliyoendeshwa na shirika la Viwanda Vidogo Vidogo (SIDO) yaliyofanyika mjini
hapa.
Muyombo alisema ni lazima wanawake wawe wabunifu katika kuanzisha miradi
mbalimbali ya maendeleo ambayo itawasaidia kuwaongezea kipato ikiwa ni pamoja na
kuondokana na umaskini.
Alisema miradi ambayo wanaweza kubuni na kuianzisha ni pamoja na kusindika
vyakula mbalimbali ambapo watajipatia soko zuri kwa ajili ya kuuzia bidhaa zao.
Hata hivyo, alifafanua kwamba hivi sasa mifugo ni moja ya rasilimali tosha, kwani
kuna mazao mengi yatokanayo na mifugo hiyo na mifugo yenyewe, hivyo wafanye
juhudi katika kuyanadi mazao hayo.
Alitoa mfano wa mazao yanayostawi vizuri kwa mkoa wa Dodoma ambayo ni zabibu,
mahindi uwele na alizeti na kuwataka wayatumie kwa kuanzisha viwanda vidogo kwa
kushirikina na taasisi mbalimbali na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali.
Mkuu huyo wa wilaya aliwashauri wanawake wa mikoa mingine kuanzisha miradi
kulingana na mazao yanayopatikana katika mikoa husika.
Naye Meneja wa SIDO mkoani Dodoma, Iskanda Tenga alisema kuwa mafunzo hayo
yanatolewa na shirika kwa lengo la kuwawezesha wajasiriamali wadogo waweze kupata
elimu ya kuweza kusindika vyakula mbalimbali vyenye ubora unaotakiwa kwa afya za
binadamu.
Tenga alisema mafunzo hayo ni mwendelezo wa mafunzo ambayo yamekuwa yakiyatolewa
kwa kipindi cha miaka mitatu na yameshatoa elimu hiyo katika wilaya zote za mkoa
wa Dodoma.
TRA yaasa wafanyabiashara kuacha tabia za ‘kimachinga’
Ni kwa kufanya biashara bila leseni
Na Ghati Msamba, Tarime
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Mara imewataka wafanyabiashara kuachana
na tabia za kuendesha biashara za kimachinga bila lesseni.
Hayo yalisemwa katika warsha ya wafanyabiashara na Ofisa Elimu Kitengo cha
Walipakodi mkoa, John Mahundi katika kijiji cha Nyamongo wilayani Tarime.
Alisema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakifanya biashara zao kwa wasiwasi na
kuhamahama ili kukwepa kodi, jambo ambalo haliwanufaishi kibiashara.
Alisema njia pekee ya kumwezesha mfanyabiashara kufanya shughuli zake bila hofu
na kumnufaisha ni kulipa kodi, badala kukwepa kwa kuhamahama.
Kwa upande wa wafanyabiashara walidai kuwa wamekuwa wakiogopa kuchukua fomu za
kujiandikisha na kutambulisha biashara zao kutokana na kutokujua viwango na
gharama za ulipaji wa kodi.
Walisema hali hiyo ilitokana na ufahamu mdogo, na kwamba baada ya kuelimishwa,
wameahidi kukata leseni zao ili kuepuka usumbufu.
Warsha hiyo ilihusu ulipaji kodi, uanzishaji na uendeshaji biashara nchini,
uandikishaji majina ya biashara, kujua umuhimu wa kulipa kodi na utunzaji wa
kumbukumbu.
Iliandaliwa na TRA kwa kushirikiana na kampuni ya PLACER DOME na kuhudhuriwa na
wafanyabiashara 50 wanaouzunguka mgodi wa Nyamongo.
Nchi za Maziwa Makuu zapongezwa kwa kusuluhisha migogoro
Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Usalama la Umoja wa Mataifa limewapongeza viongozi wa nchi za Maziwa
Makuu kwa jitihada wanazofanya kusuluhisha migogoro katika nchi za Burundi,
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Rwanda.
Mwenyekiti wa Baraza hilo Balozi Jean Marc dela Sabliere alitoa pongezi hizo juzi
jioni alipojibu maswali ya waandishi wa habari kwenye Hoteli ya Moven Pick baada
ya kumaliza ziara ya siku 10 iliyowashirkisha wajumbe 15 wa Baraza hilo katika
nchi za Maziwa Makuu.
Ujumbe wa Baraza hlo ulianzia ziara yake katika nchi ya DRC na kufuatia katika
nchi za Rwanda, Burundi Uganda na Tanzania kwa lengo la kuangalia hali halisi.
Sabliere alisema katika ziara hiyo waligundua kwamba viongozi wa nchi za Maziwa
Makuu wakiongozwa na Rais Benjamin Mkapa walifanya kazi kubwa ya kusuluhisha
migogoro na kwamba mafanikio yanaonekana.
'Hali ya usalama ya mwaka juzi ni tofauti sana na usalama wa mwaka huu, hivyo
kuna mabadiliko makubwa,'' alisema na kuongeza kwamba ni jambo la kujivunia kuona
Burundi ilifanya uchaguzi na tayari wakimbizi wanakubali kurejea makwao kutoka
Tanzania.
Wakimbizi 15,000 wa Burundi waliopo Tanzania wamepangiwa kurudi nchini mwao kila
mwezi.
Hata hivyo alisema jitihada zaidi zinahitajika kuvishawishi baadhi ya vikundi
vinavyosita kushirikiana na serikali kama cha PALIPEHUTU -FNL na kikundi cha
waasi cha lililokuwa jeshi la Rwanda na kule Uganda.
Awali, ujumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ukiwa nchini ulifanya
mazungumzo na Rais Benjamin Mkapa ambaye alisisitiza kwamba kikundi cha
PALIPEHUTU kikiendelea kukaidi mazungumzo ataiambia serikali ya awamu ya nne
isikiruhusu kutumia ardhi ya Tanzania.
Ujumbe huo pia ulifanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa Jakaya Kikwete, na kuzungumza na wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam na uliondoka juzi hiyo usiku kuelekea New York Marekani.
Maregesi ataka wanaohujumu CCM wazomewe
Na Thomas Mtinge, Iringa
MWENYEKITI wa Jumuia ya Wazazi Taifa, Abiud Maregesi
amewataka wana-CCM kuwazomea viongozi na wanachama wanaokihujumu Chama kwa
kuisaidia kambi ya upinzani ili CCM ishindwe katika uchaguzi mkuu unaotarajia
kufanyika Desemba 14 mwaka huu. Maregesi alitoa kauli hiyo wakati akihutubia
wananchi kwenye mkutano wa hadhara wa kampeni za CCM uliofanyika juzi katika
kijiji cha Mgoma, Wilaya ya Iringa Vijijini mkoani hapa.
Kauli hiyo ya Maregesi imekuja muda mfupi baada ya kupewa taarifa kwamba baadhi
ya viongozi na wanachama wa CCM akiwemo kiongozi mmoja wa kata ya Mgoma,
kumfanyia kampeni mgombea wa chama cha Jahazi Asilia badala ya Steven Galinoma wa
jimbo la Kalenga kupitia CCM.
Maregesi alionya kwamba viongozi na wanachama wa aina hiyo hawafai kuwemo ndani
ya CCM kwani ni hatari kwa Chama na kwamba hakiwezi kuwavumilia.
Alisema maendeleo ya kweli katika jimbo hilo yanaweza kupatikana kwa haraka
endapo wananchi hao wataichagua CCM na si vinginevyo, kwa kuzingatia ukweli
kwamba serikali ya CCM kamwe haitatupa nguvu zake katika majimbo au kata
zinazotawaliwa na wapinzani.
Maregesi alisema njia pekee ya wananchi hao kutatua kero zinazowakabili na
kujiletea maendeleo ya haraka ni kumchagua Steven Galinoma.
Kwa upande wake Galinoma alisema kwamba endapo atachaguliwa kushika wadhifa huo
atahakikisha kwamba anashirikiana na wananchi katika kuzitatua
kero zinazowakabili.
CUF mmeshindwa kwa kivuli chenu wenyewe
HIVI karibuni matukio makubwa kadhaa ya kisiasa yalijitokeza hapa nchini.
Miongoni mwa matukio hayo ni kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar ambapo licha
ya kushindwa chama cha CUF kilitangaza kupinga matokeo na lile la wafuasi wa
chama hicho kuwapiga waandishi wa habari waliokwenda makao makuu ya chama hicho
eneo la Buguruni, Dar es Salaam. Kutokana na matukio hayo wananchi wamekuwa
wakijiuliza kuhusu chama hicho na viongozi wake.
"Hatukubali matokeo. Tutaanzisha janga la kitaifa iwapo tutaibiwa kura. CUF
tumeshinda tena kwa kishindo," hizo ni baadhi ya kauli zilizosikika baada ya
kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar ambapo CCM iliibuka na ushindi wa jumla.
Katika uchaguzi huo, CCM imepata viti vya uwakilishi 30 na Civic United Front
(CUF) imeambulia viti 19 huku katika nafasi ya urais mgombea wa CCM Rais Amani
Abeid Karume akiwa ameibuka mshindi dhidi ya mpinzani wake wa karibu Seif Sharrif
Hamad wa CUF.
Siku chache baada ya matokeo ya urais Zanzibara kutangazwa, Baraza Kuu la chama
cha CUF lilikutana makao makuu ya chama hicho Buguruni, Dar es Salaam kwa ajili
ya kutoa tamko kuhusiana na uchaguzi huo.
Wakati 'vigogo' wa CUF wakiwa ndani wakiendelea na vikao, waandishi wa habari
kutoka vyombo mbalimbali waliokuwa, kama kawaida yao wakifuatilia mambo ili watoe
taarifa kwa umma, walianza kupata kipigo mithili ya wezi.
Matukio hayo na mengine, yamewaacha watu wakijiuliza maswali mengi kuhusu
uchaguzi na hatma ya Tanzania kutokana na mwenendo ulioonekana baada ya uchaguzi
wa Zanzibar kukamilika.
Kwa kuwa ni haki ya kila mtu kuzungumza yale anayoyaona yanafaa ili mradi havunji
sheria na taratibu zilizopo, nami nitalonga, kwani hiyo ni haki yangu.
Baada ya uchaguzi huo kumalizika, watu, vikundi na nchi mbalimbali zilitoa
maelezo yao kwa jinsi walivyoona uchaguzi wa Zanmzibar ulivyokwenda. Nchi na watu
wengi walisema uchaguzi huo ulikuwa huru na wa haki lakini wachache wakiongozwa
na Marekani walisema vinginevyo.
Kutokana na kauli ya ubalozi wa Marekani kulijitokeza watu mbalimbali waliowaunga
mkono na wengine kuwapiga, nilikuwa mmojawapo wa waliowapinga na nilieleza sababu
zangu hivyo sina haja ya kuzitaja tena. Lakini kama tukifuata misingi ya
demokrasia ambayo inatoa nafasi ya ushindi kwa walio wengi, kundi la Marekani na
wenzake wameshindwa!
Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2000 nilipata bahati ya kuwepo Zanzibar ambapo kwa
kiasi kikubwa nilishuhudia na kuzungumza na watu mbalimbali kuhusiana na siasa za
CUF.
Yupo bwana mmoja (jina namhifadhi) alisema katika siku zijazo chama cha CUF
kitapoteza umaarufu na hatimaye kusambaratika kabisa kwa kuwa kimekuwa kikiwapo
matumaini makubwa wafuasi wake kuliko hali halisi ilivyo.
Baada ya matukio ya hivi karibuni, nilikumbuka kauli ya bwana huyo na nina imani
chama hicho kitapoteza umaarufu na hatimaye kusambaratika kabisa. Lakini baada ya
matukio ya hivi karibuni kuna kila dalili sasa CUF itakwenda na maji.
Picha inayojengeka sasa kwa jamii ni kuwa CUF ni chama cha watu wenye vurugu na
ambao wana malengo binafsi ambayo ni zaidi ya siasa za kawaida kwa maana hiyo na
kwa malezi tuliyopewa Watanzania ya kupenda amani na utulivu kuwa mwanachama wa
CUF ni kama kuamua vurugu. Je kwa malezi yetu nani atakubali kuwa mwanacahama wa
chama hicho?
Inashangaza kuona CUF wanakataa kukubalia kushindwa katika uchaguzi wa Zanzibar
ili hali wanajua nguvu walizonazo sio kubwa kama za CCM ambayo katika kipindi
chote imekuwa mstari wa mbele kujiimarisha katika maeneo mbalimbali.
Akihutubia mikutano ya kampeni kabla ya kampeni, mgombea uraia wa Tanzania
kupitia CCM Jakaya Kikwete alikuwa akisisitiza kuwa vyama vya upinzani hasa
Zanzibar vilianza kuona dalili za kushindwa ndiyo maana wafuasi wake walikuwa
wanabeba mawe kwenye malori.
Kikwete alisema vyama ambavyo vimeanza kutoa matusi majukwaani dhidi ya CCM ni
dalili kuwa vimekata tamaa ya kupata ushindi na kuwa vile ambavyo vinajihusisha
na kuzomea ni sawa na kukubali kushindwa. Alisema siasa si kutukana wala kuzomea.
Siasa ni hoja.
Kikwete aliwasisitiza wananchi kuwa amani na utulivu wa Tanzania hautokani na
hulka bali misingi mizuri iliyojengwa na waasisi wa TANU na ASP na hatimaye CCM
waliosisitiza umoja na mshikamano wa kitaifa.
Alitanabahisha kuwa tangu mwanzo viongozi wa CCM wangeendekeza ubaguzi wa rangi,
ukabila, chuki kati ya kabila na kabila au ugawaji wa rasilimali kutokana na
maeneo, nchi ingejaa vurugu.
CUF ikumbuke na kutambua kuwa kwa misingi ya kauli za Kikwete, ambazo Watanzania
wengi wanakubaliana nazo uwezekano wa kushinda Zanzibar ulikuwa mdogo kwa kuwa
badala ya kuashiria amani na utulivu, chama hicho kilijikita kwenye ubabe zaidi.
Chukulia mfano kauli ya kuwataka wafuasi wa CUF wasikae mbali na vituo baada ya
kupiga kura, iliashiria nini? Achilia mbali kauli mbiu za wanaumeee, mapanga na
ngangarii!
Pia kuna propaganda zinazopandikizwa hivi sasa na hata kwa baadhi ya wana habari
kuwa siku ya kupiga kura watu kwa makundi walikuwa wakipelekwa kwenye vituo vya
kupiga kura na kufanya hivyo bila hatua zozote kuchukuliwa. Inashangaza.
Hivi pamoja na teknolojia ya habari kupiga hatua kubwa mbele, alikosekanaaliyeona
hilo na kupiga picha hasa zile za televisheni, ukitilia maanani walikuwepo wana
habari wengi hata wale wa kutoka nje ya nchi ambao sasa CUF mmedai ndiyo
mnawaamini zaidi ya wa hapa nchini!
CUF imefika wakati wa kuamua kama ni kufanya siasa na ifanyike kwa njia ya amani
na utulivu, ujanja ujanja na kuwajaza matumaini yasiyokuwepo wafuasi wenu
hautawafikisha mbali. Mwanzo wa mwisho CUF huenda ukawa baada ya uchaguzi mkuu na
tusubiri tuone.
Kwa maana halisi ya kamusi ya kiswahili neno 'kivuli' lina maana ya giza
linalofanywa na kitu kuwa mbele ya mwanga. Lakini pia kivuli ina maana kumfanyia
mtu mambo ya kumdhuru na kumuendea kinyume na hali wakati mbele ya macho yake
unamuonyesha kuwa ni mwema. CUF mmeshindwa kwa kivuli chenu wenyewe.
Mafunzo kuhudumia wagonjwa wa majumbani yanahitajika
Na Rodrick Makundi, Moshi
MAFUNZO kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wa majumbani yanahitajiwa zaidi ili
kuwezesha ubora wa huduma za kiafya kwa wagonjwa hao.
Kutokana na hali hiyo, serikali imeshauriwa kutoa mafunzo ya kuwahudumia wagonjwa
wa majumbani hasa wenye virusi vya ukimwi, ikilinganishwa na idadi kubwa ya
wagonjwa hao wanaopatiwa huduma majumbani mwao.
Akiwakabidhi vyeti wahudumu wa afya wapatao 26, waliohitimu mafunzo yao ya huduma
za afya katika hospitali mbalimbali mkoani hapa, Mganga Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro, Hubert Bwana alisema ametoa ushauri huo kwa serikali ili kuona
uwezekano wa utoaji wa mafunzo hayo kwa wataalamu wa afya walio karibu na jamii.
Alisema hivi sasa idadi ya wagonjwa wa ukimwi mkoani hapa imekuwa kwa kasi hali
inayosababisha wagonjwa wengi kupatiwa huduma majumbani kutokana na wingi wa
wagonjwa katika vituo vya afya na hospitalini.
Akitoa takwimu za wanaopima damu, Mganga Mkuu alisema kuwa kila watu 100, tisa
wamekutwa na virusi vya ukimwi, hali ambayo inaashiria kukua kwa ongezeko la
wagonjwa wa ukimwi.
Kwa mujibu wa takwimu wagonjwa 650 wa ukimwi wanapatiwa tiba katika hospitali ya
mkoa ya Mawenzi, huku wengi wao wakirejeshwa majumbani ili kupunguza msongamano
unaokuwepo.
Kwa upande wake Mratibu wa Shirika la Mildmay International lililoendesha mafunzo
hayo, Lightness Kaale amesema lengo la mafunzo ni kuiwezesha jamii kupata mafunzo
ya utunzaji wa wagonjwa wa ukimwi majumbani.
Shirika hilo hadi sasa limetoa mafunzo kwa wauguzi 1000 tangu kuanzishwa kwake
mwaka jana hapa nchini, zikiwa zimetumika sh. milioni 178 katika utaoji wa
mafunzo hayo.
Wauguzi waliopata mafunzo na waliohitimu mafunzo hayo ni kutoka katika hospitali
za Kilema, KCMC, Kibosho, Marangu, Mwika, Umbwe na Mawenzi mjini hapa.
UVCCM yakata wananchi kuiadhibu CUF kwa kuinyima kura Desemba 14
Ni kwa wafuasi wake kuwapiga waandishi wa habari
Na Mwandishi Wetu
UMOJA wa Vijana wa CCM (UVCCM) umelaani kitendo kilichofanywa na wafuasi wa CUF
cha kuwashambulia waandishi wa habari na umewaomba wananchi kukiadhibu chama
hicho kwa kukinyima kura kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Desemba 14, mwaka
huu.
Tamko hilo la UVCCM lilitolewa jana na Naibu Katibu Mkuu wake, Amos Makala
alipozungumza na viongozi wa Umoja huo wa ngazi mbalimbali kuanzia matawi
wilayani Kinondoni, Dar es Salaam.
Makala alisema kitendo kilichofanywa na wanachama na wafuasi hao mbele ya Ofisi
za Makao Makuu ya chama chao, Buguruni, Dar es Salaam kimeudhihirishia umma
kwamba hakistahili ridhaa ya wananchi kuliongoza taifa.
Alisema kitendo cha kuwapiga, kuwajeruhi na kuharibu vifaa vya waandishi
wakitekeleza majukumu yao ya kutafuta habari siyo tu kimewanyima wananchi uhuru
wa kupata habari ni uvunjaji wa sheria za nchi na kimedhihirisha hawaitakii amani
Tanzania.
Makala pia amewapongeza wananchi wa Zanzibar kwa uamuzi wao wa Oktoba 30, mwaka
huu wa kuichagua CCM kuendelea kuongoza kwa kipindi kingine cha miaka mitano
ijayo. Katika uchaguzi huo wananchi hao walimchagua kwa kura nyingi Amani Abeid
Karume kuwa Rais na wagombea wa majimbo 30 wa CCM kati ya 49 kuwa Wawakilishi.
Kwa uamuzi huo wa Wazanzibari, Makala alitoa mwito kwa Watanzania wote kuwa
matokeo hayo yawe changamoto kwao kwa kuendelea kuichagua CCM katika Uchaguzi
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Desemba 14, mwaka huu.
Uchaguzi Mkuu wa Desemba 14, mwaka huu, ambao Watanzania wote wa Bara na Zanzibar
watapiga kura kumchagua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wabunge na
Madiwani.
Aliwataka wana-CCM kuendeleza zaidi umoja, amani na mshikamano, hususan katika
kipindi hiki cha kampeni kwa kushindana na vyama vingine kwa hoja kwa kunadi sera
na ilani ya CCM badala ya kutumia nguvu, ghilba na vitisho kama vinavyofanya
baadhi ya vyama vya upinzani.
Mapema, Mwenyekiti wa CCM wa wilaya ya Kinondoni, Aaron Mwaikambo akimkaribisha
Makala kuzungumza na vijana hao alitoa mwito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi
kwenda kupiga kura Desemba 14, mwaka huu.
Mwaikambo alisema Desemba 14 itakuwa Jumatano ambayo serikali imeamua kuwa siku
ya mapumziko, hivyo wananchi hawana sababu za kushindwa kwenda kupiga kura
isipokuwa kwa wagonjwa mahututi.
Alisema hata kwa waumini wa dini ambao wengi wao siku za Ijumaa, Jumamosi na
Jumapili ni siku mahsusi kwa sala hawatakuwa na kizuizi cha kuwafanya kushindwa
kwenda kupiga kura.
Klabu za waandishi wa habari zatakiwa kuanza kuitenga CUF
Na Solomon Mwansele, Mbeya
KLABU za Waandishi wa habari nchini zimetakiwa kuacha kushirikiana na chama cha
CUF na kukataa mialiko yao.
Hayo yamo katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na rais wa Umoja wa
Klabu za waandishi wa habari nchini (UTPC) Ulimboka Mwakilili.
Rais huyo wa UTPC alisema CUF wasusiwe hadi hapo watakapokuwa wametekeleza yote
yaliyoagizwa na vyama vya waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari
(MOAT), asasi za kisheria na wadau wengine wote waliopatwa na majonzi.
Katika taarifa hiyo, Mwakilili alisema CUF wanatakiwa wawajibike kikamilifu
kugharamia matibabu ya waandishi hao na kulipa fidia zote za vifaa na mali
zilizopotea na athari mbalimbali.
Imeongeza kuwa viongozi wa CUF wamekuwa wakipanda mbegu mbaya za fujo, migogoro
na vurugu kwa wanachama wake kwa muda mrefu kwa kupinga juhudi zote zinazofanywa
hadi wao waingie madarakani na mbegu hiyo imeanza kuzaa matunda kwa madhara
yanayojitokeza sasa.
"Tunauagiza uongozi wa CUF ukubali na kukiri hadharani, kujutia na kutoa
ushirikiano wote kwa vyombo vya dola kuwasaka walioshiriki kutenda kitendo hicho
cha kinyama na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria," alisema Mwakilili katika
taarifa yake.
Iliongeza kuwa CUF wameendelea kuwaita na kuwatumia waandishi wa habari wakati
wote kwa kufikisha taarifa za mafanikio yao na matatizo kila inapobidi kwa vyombo
vya kitaifa na kimataifa na mambo yao kufanikiwa, lakini sasa wanawafanya
waandishi kuwa 'mbuzi wa kafara'.
Mwakilili alisema uongozi wa kitaifa wa UTPC kwa kuungana na wanachama wake nchi
nzima kwa uchungu na masikitiko makubwa unapokea kilio cha waandishi wa habari
wote kwa huzuni kubwa.
Wanadaiwa kuhusika na matukio ya ujambazi kwenye benki
Na Mwandishi Wetu
POLISI imewatangaza watu watatu kama watuhumiwa sugu wa matukio ya kijambazi,
ikiwemo kwenye benki na sasa inawasaka kwa udi na uvumba.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Alfred Tibaigana, amewataja watuhumiwa hao kuwa ni
Sixtus Alfred Ngowi (42), mkazi wa Dar es Salalaam, Abulkarim Mongi (37) ambaye
makazi yake hayajulikani na Sadik Fatee, mkazi wa Muheza ambaye umri wake
haujajulikana.
Alisema watuhumiwa hao wote wanaonekana mara kwa mara katika miji ya Dar es
Salaam, Arusha, Nairobi na Moshi, wanahusishwa na wizi wa pesa sh. bilioni 1.6
kutoka kampuni ya Security Group, ambayo wafanyakazi wake na watuhumiwa wengine
jumla yao 18 wana kesi inayoendelea katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu.
Polisi pia inamsaka mke wa Ngowi, ambaye hakutaja jina lake, kutokana na
kuhusishwa ma tuhuma za mumewe. Tibaigana alisema kuwa, mtuhumiwa Ngowi,
anamiliki kiwanda cha kutengeneza vinywaji baridi kiitwacho Cold Cap cha jijini
Dar es Salaam.
Alifafanua kuwa, mwanamke huyo anahusishwa na kesi hiyo, kwani kasha la fedha
lililoibwa kwenye kampuni ya Security Group, lilikutwa nyumbani kwake na mwanamke
huyo amejificha pasipojulikana na amekuwa akitoa taarifa kwenye ofisi mbalimbali
kwamba anatishiwa kuuawa. Hakufafanua.
Kamanda Tibaigana, alitoa wito kwa wananchi kuvifahamisha vyombo vya dola ili
watuhumiwa hao ambao kwa kiasi kikubwa wanahusishwa na matukio ya wizi kwenye
benki mbalimbali jijini Dar es Salaam, wakamatwe na kufikishwa mwenye vyombo vya
sheria.
Wakati huo huo, juzi jioni saa 1.30 majambazi manne yakiwa na silaha mbali
yalivamia na kujeruhi, pia kupora pesa na mali zenye thamani ya zaidi ya sh.
milioni mbili huko Tabata Segerea, Dar es Salaam, eneo la Ugombolwa.
Tukio hilo ni mwendelezo wa mikasa ya kijambazi, Tabata kwani ni siku moja tu
kabla ya hilo, kulifanyika uporaji wa namna hiyo katika eneo jirani la
Kilimanjaro, huko Tabata Chang'ombe majira ya saa 2.30. Tukio la Tabata Segerea,
lilitokea saa 1.30.
Kamanda Tibaigana amethibitisha kutokea kwa tukio hilo kati ya saa 1.30 na saa
2.00 na kusema uchunguzi mkali unaendelea kuwasaka watuhumiwa hao, huku mtu
mmoja, amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili akiuguza majeraha ya
kichwa.
Kwa mujibu wa Tibaigana, majeruhi aliyelazwa na Charles Batenga. Mwingine, Faiza
Batenga (30), alitibiwa majeraha na kuruhusiwa.
Mwandishi wa habari hizi aliyekuwepo katika eneo la tukio, alishuhudia maduka
yote huko Tabata Segerea yakiwa yamefungwa saa 2.30, tofauti na kawaida ambapo
baadhi huwa wazi hadi zaidi ya saa 5.00 usiku.
Akisimulia mkasa huo wa juzi, Tibaigana alisema kuwa majira kati ya saa 1.00
usiku na saa 2.00 usiku majambazi hayo manane yakiwa na panga na nyundo yalianza
kuvamia dukani kwa Faiza na yakampora pesa taslimu sh. 300,000 na kadi za simu
zenye thamani hiyo hiyo.
Baada ya hapo, yalihamia nyumbani kwa mkazi mwingine aitwaye Daudi Mboneka ambapo
walimkuta mkewe ambaye hakutajwa jina na kupora sanduku dogo (briefcase) yenye
nyaraka mbalimbali na simu ya mkononi.
Kwa mujibu wa Tibaigana, safari ya majambazi hayo ilihamia nyumbani kwa Leticia
Mwijage, aliyeporwa pesa taslimu sh. milioni 1.7. Safari ya uporaji iliishia
dukani kwa Ashery Kazimoto ambako dukani kwake, wateja waliokuwa wakiburudika kwa
kinywaji waliporwa pesa taslimu sh. 80,000 na simu ya mkononi.
Aidha, katika hatua nyingine jana asubuhi watu wenye hasira walimuua na kumchoma
moto kijana mmoja wa kiume anayetuhumiwa kuwa kibaka, huko Tabata Segerea, jirani
na kituo kipya cha polisi.
Kwa mujibu wa habari kutoka eneo la tukio, mkasa huo ulitokea saa 4.00 asubuhi
baada ya kijana huyo kukurupushwa akiiba nguo zilizoanikwa nyumbani kwa mtu mmoja
Mzungu, mkazi wa eneo hilo. Maiti iliendelewa kubakia mahali hapo hadi saa saa
7.40 mchana polisi walipofika kuichukua.
Katika tukio la Alhamisi usiku, majambazi yalipora pesa sh. 70,000 eneo Tabata,
Kilimanjaro wakitishia kuvunja chupa iliyotoa mlio kama bunduki na kufanikisha
uporaji wao.
Asema kususia Baraza ni utovu wa nidhamu
Asisitiza huwezi kumtenganisha Rais na Baraza
Na Khatibu Suleiman, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, amesema kitendo cha wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi kutoka chama cha CUF kususia uzinduzi wa Baraza hilo pamoja na
kutomtambua yeye ni uvunjaji wa Katiba ya nchi.
Alisema mbali ya kuvunja Katiba, lakini pia ni tabia ya chama hicho kuendelea na
kuonyesha vitendo vya utovu wa nidhamu.
Rais Karume alisema hayo jana alipolihutubia Baraza jipya la Wawakilishi,
lililochaguliwa katika uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa Oktoba 30 mwaka huu. Alikuwa
akilizindua Baraza hilo.
Katika uchaguzi huo Rais Karume alishinda kiti cha urais, wakati chama chake cha
CCM kilishinda viti 30 katika Baraza hilo.
Chama cha CUF ambacho kinadai hakitambui matokeo ya uchaguzi huo, kilishinda viti
19 na mgombea wake wa urais, Seif Shariff Hamad, alishindwa na Karume.
Rais alisema kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha tano
A(1), kinaeleza kwamba kutakuwa na mamlaka ya nchi ambayo ni serikali pamoja na
Baraza la Wawakilishi, ambapo yeye rais ni sehemu ya Baraza hilo.
"Rais wa Zanzibar ni sehemu ya Baraza la Wawakilishi hivyo huwezi kumtenganisha
na Baraza la Wawakilishi," alisema Karume ambapo alionesha kushangazwa na tabia
ya wajumbe wa CUF kususia Baraza hilo ambapo juzi waliapa kulinda na kuitetea
Katiba ya Zanzibar, pamoja na ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Karume alisema kitendo cha wajumbe wa chama cha CUF kususia kuingia katika Baraza
la Wawakilishi kinaonesha kwamba CUF hawapo tayari kujiheshimu wala kuheshimiwa,
na kuwaheshimu watu wengine.
Alisema wakati umefika kwa viongozi wa chama cha wananchi CUF kujenga tabia ya
kuheshimu maamuzi ya wengi, kwani ndio mfumo unaokubalika katika nchi zinazofuata
utawala wa kidemokrasia na Katiba ikiwemo Zanzibar.
Mapema, Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho, alisema hana taarifa
yoyote kuhusu kutohudhuria kwa wajumbe wa kambi ya upinzani ya CUF katika kikao
cha jana, licha ya kuwapa taarifa ya ujio wa rais na shunguli za uzinduzi wa
Baraza hilo.
"Sina taarifa kwa nini wajumbe wa CUF hawakuja katika uzinduzi wa kikao hiki...
lakini nitafuatilia kwa makini kujua sababu ni zipi?" alisema Kificho, muda mfupi
kabla ya kumkaribisha Rais Karume kulizindua Baraza hilo.
Rais Karume katika hotuba yake alisema uchaguzi mkuu wa Oktoba 30 umekwisha kwa
Chama cha Mapinduzi kimekabidhiwa dola na wananchi, na sasa kazi kubwa iliopo
mbele yetu ni kuleta maendeleo, umoja na mshikamano wa wananchi.
Alisema serikali yake itaendelea na kazi kubwa ya kuleta maendeleo katika visiwa
vya Unguja na Pemba bila ya kujali itikadi za kisiasa, huku utekelezaji wa ilani
ya Chama cha Mapinduzi itakuwa ndiyo dira ya mafanikio yote hayo.
"Maendeleo ya nchi hayana itikadi ya kisiasa...wananchi wanataka maendeleo na
siyo siasa tu," alisema Karume ambapo alielezea mafanikio yake mbali mbali katika
utekelezaji wa ilani ya uchaguzi katika kipindi cha
miaka mitano iliyopita.
Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, alielezea muelekeo wa serikali yake katika
kipindi cha miaka mitano ijayo cha 2005-20010, ambapo alisema suala la
uimarishaji wa sekta binafsi utapewa kipaumbele ili kuongeza ajira kwa wananchi
wa Unguja na Pemba.
Alisema suala la kuimarisha miundo mbinu ya barabara, sekta ya nishati pamoja na
maji safi na salama Unguja na Pemba, litapewa kipaumbele ili kuona wawekezaji
wengi wanajitokeza kuwekeza katika sekta na miradi mbali
mbali ya maendeleo.
Karume alisema tayari kitengo cha uwekezaji cha ZIPA kimezidi kuimarishwa ili
kuwavutia wawekezaji zaidi kuwekeza katika maeneo mbali mbali ikiwemo kuondosha
urasimu kwa wawekezaji katika kuwekeza.
Alisema mpango wa kupunguza umasikini MKUZA unaendelea na unafanya kazi katika
visiwa vya Unguja na Pemba, ambapo wananchi wameweza kushirikishwa kikamilifu
katika utekelezaji wake bila ya kujali itikadi za kisiasa.
Alisisitiza na kuutaka upande wa upinzani wa chama cha CUF kujali na kuweka mbele
maslahi ya taifa kwa ajili ya kuleta maendeleo na sio ubinafsi wa watu wachache,
ambao hauwezi kuleta tija na maendeleo ya nchi.
Wana-CCM wote ni wagombea katika uchaguzi mkuu-Mangula
Aonya atakayethubutu kuupigia upinzani
Na Bashir Nkoromo, Makambako
KATIBU Mkuu wa CCM, Philip Mangula, amesema wanachama wa CCM wote ni wagombea na
kuonya kuwa mwana-CCM atakayethubutu kutompigia kura mgombea wa CCM atakuwa
amejinyima kura yeye mwenyewe.
Alisema hayo jana kwa nyakati tofauti katika mikutano yake ya ndani aliyofanya na
wanachama na viongozi wa CCM katika mji mdogo wa Makambako, jimbo la Njombe
Kaskazini mkoani Iringa.
"Ushindi wa mgombea urais, ubunge au udiwani kupitia CCM ni wa wanachama wote wa
CCM, hivyo kwa sasa wagombea ni ninyi wana-CCM. Ni lazima muhakikishe kila
mmoja wenu anapigia kura mgombea wetu kwa kuwa huyo mgombea ni mwakilishi tu,
wagombea hasa ni ninyi wanachama," alisema Mangula.
Alisema CCM inayo hazina kubwa ya wanachama hivyo jukumu alilonalo kila
mwanachama halisi ni kuhakikisha anatumia wakati huu uliobaki kuwashawishi wasio
wanachama kuipigia kura CCM, ili ipate ushindi mnono zaidi kuliko inavyotarajiwa.
Mangula aliwaasa wanachama wa CCM wasighilibike na kuamua kutompigia kura mgombea
wa CCM, eti kwa sababu ya ugomvi wa binafsi kati yake na kiongozi mmoja tu wa
chama.
"Ukigombana wewe binafsi na kiongozi mmoja wa chama usikiadhibu chama, hayo ni
makosa kwa kuwa utakuwa umejiadhibu na wewe kama mwanachama," alisema
Mangula.
Aliwataka wana-CCM kuongeza mshikamano wao katika chama badala ya wengine
kuendelea kukumbatia hadi sasa wagombea walioachwa katika kura za maoni.
Alifafanua kuwa walioachwa sasa si wagombea, wagombea ni waliopitishwa.
"Halmashauri Kuu inaheshimu sana maoni yenu mliyotoa katika kura za maoni, lakini
hailazimishwi kuyafuata kwa kuwa yenyewe ndiyo yenye uamuzi wa mwisho," Mangula
alikumbusha na kuongeza: "Sisi hufuata vigezo muhimu kuona kama mgombea anatosha
kwa kuwa taarifa za muhusika huwa tunaanza kuzikusanya mara tu anaponuia kuchukua
fomu ya kuomba".
"Mwanachama mara tu akitamka nataka kuchukua fomu kuwania nafasi fulani, basi
sisi mara moja tunafungua faili na kuanza kukusanya mambo yake yote. Kwa hiyo
hatumuonei mtu tunapomwacha hata kama alikuwa ameongoza katika kura za maoni,
wakati mwingine
tunaweza kuwa tumemwacha kutokana na sababu pengine zenye maslahi hata na
aliyeomba," alisema.
Kuhusu upinzani, Mangula alisema kwa sasa chama cha CUF kichwa chake kimeshakatwa
huko Zanzibar, huku Bara imebaki mikia tu mfano wa pweza, kwa hiyo
kilichobaki ni kumalizia tu hapo Desemba 14, mwaka huu.
Mangula alisema wananchi hata wale wasiokuwa wana-CCM hawana sababu ya kukichagua
CUF kwa kuwa tayari wamekuwa wakishuhudia au kusikia jinsi kilivyo cha
shari na chenye kutamani mauaji.
Alitoa baadhi ya mifano ya mauaji yaliyokwishatokea yakihusishwa na chama hicho
kuwa ni yale ya kuchinjwa kwa polisi huko Pemba wakati wa uchaguzi wa mwaka 2000
na mfuasi mmoja wa CCM kuuawa kwa nyumba yake kuchomwa moto Manzese na vitendo
walivyofanya hivi karibuni vya kupiga waandishi wa habari kwenye ofisi zake mjini
Dar es Salaam.
Mangula alisema, ukiacha CUF vyama vingine ndiyo hoi kabisa kwa sababu ndiyo
kwanza vinajikongoja kwa kuwa katika maeneo mengi havina hata anuani ya kuweza
kuvipata ukihitaji.
Mangula ambaye tangu juzi bado yupo katika wilaya ya Njombe alikagua hali ilivyo
katika majimbo, baada ya mkutano aliofanya mjini Makambako alifanya pia mkutano
wa ndani katika kata ya Mtwango.
Kabla ya kuzungumza na wananchi, Mangula alifungua shina la Wakereketwa la
Mtwango ambako aliwataka wana-CCM kuyatumia mashina kote nchini kutafakari
namna CCM itakavyoweza kuibuka na ushindi wa kihistoria katika uchaguzi mkuu.
Mapema, Katibu wa CCM wa mkoa wa Mbeya, Costantine Malyagira na Mwenyekiti wake
Tasili Mgoda walimwambia Mangula kwenye mikutano hiyo kwamba hali katika majimbo
hadi sasa inaashiria CCM kupata ushindi mkubwa na pia wanachama wanasubiri
uchaguzi kwa hamu.