UHURU 14.11.2005
KUFUATIA VIONGOZI WAKE KUZOMEWA:
Kanisa Katoliki Songea ‘lanywea’ kwa waumini
Latangaza rasmi kuachana na mahubiri ya siasa
Lilikuwa likimpigia debe mgombea wa CHADEMA
Mwandishi Wetu, Songea
KANISA Katoliki jimbo kuu la Songea limetangaza rasmi kuacha kuhubiri siasa na
kuwafanyia kampeni baadhi ya wagombea ubunge katika jimbo la Songea Mjini.
Tamko la kuacha rasmi kampeni za kisiasa kanisani lilitolewa jana wakati wa ibada
na Mwenyekiti wa Baraza la Walei la kanisa hilo, Ernest Haule ambaye alisema
uongozi wa kanisa umesikitishwa na yaliyojitokeza kutokana na mahubiri na kuwa
haitatokea tena jimboni humo.
Mwenyekiti amewataka waumini kuacha kuwazomea viongozi wa kanisa kwa yale yote
wanayoaamini kuwa yanawakwaza na badala yake watumie viongozi wao wa ngazi
mbalimbali kufikisha malalamiko yao.
Haule alisema kwa upande wao baraza limekutana na Baba Askofu Nobert Mtega na
mapadre wote na wamekubaliana kimsingi kuacha mahubiri yote yenye mwelekeo wa
kisiasa ili kulinda maadili na umoja wa kanisa hilo na kuwataka waumini kuwa
katika hali yao ya kawaida kuheshimu kanisa kama mwanzo.
Imekuwa ikidaiwa kwamba viongozi wa kanisa katika jimbo hilo, hasa mapadre na
askofu wamekuwa wakimfanyia kampeni kanisani mgombea wa ubunge wa chama kimoja
cha upinzani katika jimbo la Songea Mjini.
Wananchi wamekuwa wakililalamikia Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Songea kwamba
limekuwa likimfanyia kampeni mgombea wa Chadema hali iliyosababisha kuzomewa kwa
baadhi ya makasisi wake kanisani hapo na katika hali ya kushindana, waumini nao
wamekuwa wakivaa sare za Chama Cha Mapinduzi wakati wa ibada kanisani.
Inadaiwa Padre Noel Duwe ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo Cha Radio Maria Songea
aliwahi kuzomewa na waumini baada ya kutamka wazi kuwa wananchi wasiichague CCM
na badala yake wachague CHADEMA kwa madai CCM inatoa Khanga, fulana na kofia
ambazo zina picha za wagombea wao.
Kwa kauli yake hiyo inadaiwa ilisababisha azomewe na waumini na kuanzia hapo
waumini wakaamua kuvaa sare za CCM kanisani.
Hata hivyo, hali haikuishia hapo, kwani katika ibada siku nyingine katika kanisa
hilo hilo la kiaskofu la Mtakatifu Mathias Mulumba Kalemba inasemekana waumini
waliwahi kumzomea Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea Mhashamu Norbert Mtega
kutokana na mahubiri yake kama ya Padre Duwe na kusababisha kuamsha hasira toka
kwa waumini wa kanisa hilo.
Zomea zomea haikuishia kwa viongozi hao tu, kwani paroko wa parokia ya Songea
Mjini Padre Paulo Chiwangu ambaye anaheshimika sana kwa waumini wa kanisa hilo
naye alipata adha hiyo alipokuwa na hoja ya kuwataka waumini wa kanisa hilo
kuacha tabia ya kuwazomea na kuwatukana viongozi wao wanapowakosea na badala yake
watumie utaratibu wa kuwaona viongozi wa ngazi mbalimbali ili kutatua tatizo
hilo.
Aidha, paroko huyo alipata wakati mgumu pale alipozomewa wakati alipowataka
waumini wamwombe radhi Askofu Mkuu Mtega kutokana na kitendo chao cha kumzomea
kwa vile ni kiongozi wao mkubwa wa kanisa, na kwamba hakupaswa kuzomewa kwa
kiwango kile na kwamba ni kumkosea adabu na kukosa utii kwa Mungu.
CUF iheshimu maamuzi ya Wazanzibari - Mapuri
Na Mwandishi Wetu
KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi, Omar Ramadhan
Mapuri amewataka viongozi na wafuasi wa CUF kuheshimu uamuzi wa Wazanzibari wa
kuichagua CCM kuendelea kuiongoza Zanzibar.
Mapuri aliyasema hayo juzi baada ya kuzindua shina la Wazee wakereketwa wa CCM,
Gongolamboto, kata ya Ukonga, Dar es Salaam na kuongeza kuwa baada ya matokeo ya
uchaguzi huo kila Mzanzibar na Mtanzania kwa jumla kuyaheshimu.
Alisema baada ya kauli ya Wazanzibar waliyoitoa kwa kupiga kura Oktoba 30, mwaka
huu, katika Uchaguzi Mkuu ambapo waliichagua CCM kuendelea kuunda dola, CUF haina
budi kuheshimu kauli hiyo.
Katika uchaguzi huo, wananchi wa Zanzibar walimchagua Rais Amani Abeid Karume
kuendelea kuiongoza Zanzibar kwa kipindi kingine cha miaka mitano ijayo, pia
waliwachagua wagombea wa CCM katika majimbo 30 kati ya 49 kuwa Wajumbe wa Baraza
la Wawakilishi na Madiwani.
Huku akishangiliwa na wana-CCM na wananchi waliofurika katika viwanja vya shina
hilo, Mapuri alisema mtu yeyote kukataa matakwa ya Wazanzibari walio wengi siyo
tu ni kuwanyima haki wananchi, pia ni uvunjaji wa sheria za nchi.
Mapuri ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani, aliwatahadharisha wana-CCM na
wananchi kwa jumla wanaoitakia mema Tanzania wasibweteke na ushindi walioupata
katika Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar, Oktoba 30, mwaka huu.
Badala yake, aliwataka wajipange upya kuhakikisha CCM inashinda kwa ushindi wa
kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliopangwa
kufanyika Desemba 14, mwaka huu.
Alisema uamuzi uliofanywa na Wazanzibari wa kuichagua CCM kuendelea kuiongoza
Zanzibar uwe changamoto kwa wana-CCM na wananchi kwa jumla kuhakikisha wanaweka
mikakati madhubuti itakayohakikisha CCM inaibuka na ushindi wa kishindo katika
uchaguzi huo.
Katika Uchaguzi Mkuu wa Desemba 14, mwaka huu, Watanzania wote wa Bara na
Zanzibar watapata fursa ya kuwachagua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Wabunge na kwa Bara watawachagua pia Madiwani.
CCM haina shaka na jimbo lolote Iringa
Ni kauli ya Katibu Mkuu Mangula
Na Bashir Nkoromo, Njombe
CHAMA Cha Mapinduzi kimesema kwa sasa hakuna jimbo hata moja la uchaguzi mkoani
Iringa ambalo lina shaka nalo kwamba italikosa.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula katika mikutano yake ya
ndani na viongozi wa CCM aliyoifanya mwishoni mwa wiki kwa nyakati tofauti katika
maeneo ya Ilembula na Wanging'ombe katika jimbo la Njombe Kusini.
Alisema, hata hivyo, hali imekuwa nzuri baada ya kuwa baadhi ya majimbo kulikuwa
na shaka zilizosababishwa na tofauti baina ya wanachama zilizotokana na mchakato
wa kura za maoni wakati wa kupata wagombea.
Mangula alisema, baada ya migawanyiko hiyo ambayo ni ya kawaida kutokea wakati
kama huo, sasa mshikamano umerejea na wana CCM wamekuwa kitu kimoja.
Aliwataka wana CCM ambao bado wanazing'ang'ania tofauti hizo mkoani humo na
nchini kote kwa jumla sasa kuachana nazo kabisa kwa kuwa waliokuwa wakiwashabikia
sasa si wagombea ila waliobaki baada ya kuteuliwa na vikao vyenye maamuzi ya
mwisho ya Chama ndiyo wagombea.
Mangula alisema, mgawanyiko uliokuwepo si katika ngazi za ubunge tu na udiwani
ila hadi katika ngazi ya mgombea Urais.
Alisema, baada ya michakato kupita hatimaye alipopatikana mgombea mmoja
aliyetakiwa, migawanyiko sasa haipo na wale 10 wote ambao hawakupita wameungana
na wana-CCM wote kumpigia debe mgombea wa kiti hicho, Jakaya Kikwete.
"Kwa mwanachama aliyeiva na mwenye moyo thabiti na Chama anatambua kuwa kura za
maoni ni maoni si uamuzi... hivyo baada ya vikao vyenye maamuzi ya mwisho
kupitisha mgombea yeye wajibu wake hubaki ni kuunga mkono aliyepatikana," alisema
Mangula.
Katika mikutano hiyo Mangula aliwataka wananchi wa jimbo la Njombe Magharibi
kuhakikisha wanamchagua kwa kura nyingi mgombea wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM
Charles Kevela ambaye amechukua nafasi ya mbunge wa zamani Thomas Nyimbo.
Mangula kama alivyokuwa akitamka katika mikutano yake ya Lupembe na Makambako
jimbo la Njombe Kaskazini, aliwataka wana CCM kutambua kwamba kwa sasa kazi
iliyopo mbele yao ni moja tu, kuipatia ushindi mnono CCM katika uchaguzi Mkuu
utakaofanyika Desemba 14, mwaka huu.
Alisema, kila mwana-CCM hana budi kuhakikisha anapiga kampeni ya aina ya kipekee
kuhakikisha anashawishi wasio wanachama kuipigia kura CCM siku hiyo.
Katika mikutano hiyo Mangula alionya pia kwamba kusiwepo viongozi ndumilakuwili
watakaothubutu kukisaliti Chama wakati huu wa kutafuta kura ili CCM iweze kuunda
serikali tena.
Alisema kikao cha Kamati Kuu ya CCM kilichokutana hivi karibuni kimeagiza
kukusanywa kwa kumbukumbu za viongozi wasaliti ili baada ya uchaguzi watupwe nje
ya Chama.
Mangula alisema, kwa wale viongozi watakaoonekana kusaliti wazi wazi kama ni wa
kuchaguliwa wasimamishwe uongozi na kama ni wa kuteuliwa wafukuzwe.
Katibu Mkuu wa CCM ambaye anafanya ziara hiyo kwa ajili ya kukagua maendeleo ya
kampeni na hali ilivyo kuelekea uchaguzi mkuu, jana aliendelea na ziara yake
katika eneo la Wemba jimbo la Njombe Kusini kabla ya kwenda Mbeya leo.
Kanisa kuruhusu kondom kwa wanandoa tu, iwapo Mmoja ana virusi vya ukimwi
Na Pendo Mangala, Dodoma
KANISA Anglikana nchini limesema litaruhusu matumizi ya kondomu kwa waumini wake
ambao ni wanandoa tu pindi mmoja kati yao atakapokuwa ameathirika na ugonjwa wa
ukimwi ili kumlinda mwenzake asipate virusi vya ugonjwa huo.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Katibu Mkuu wa Kanisa hilo, Mchungaji Dk.
Akili Mwita alipofungua semina ya mama wachungaji juu ya ukimwi katika ukumbi wa
Furaha Hostel mjini hapa.
Mwita alisema kanisa hilo litaruhusu matumizi ya kondomu kwa waumini wake ambao
ni wanandoa tu pindi mmoja kati yao atakapokuwa ameathirika na ugonjwa huo.
Alisema kwamba mtu kupata ukimwi siyo dhambi na wala siyo adhabu toka kwa Mungu,
na kwamba mtu yeyote anaweza kupata ukimwi, kwani ugonjwa huo huambukizwa kwa
njia mbalimbali hivyo kanisa na jamii kwa jumla iachane na dhana hiyo potofu.
Katibu huyo alifafanua kwamba awali Kanisa Anglikana na jamii kwa jumla walikuwa
wakiamini kwamba mtu ambaye ameathirika na ugonjwa wa ukimwi ni mtenda dhambi,
jambo ambalo siyo kweli.
Alisema wao kama kanisa hawaruhusu matumizi ya kondomu kwa waumini wake na jamii
nzima, kwani kitendo cha kuwaruhusu kuvaa kondomu ni sawa na kuwatuma watende
dhambi na kuendeleza uzinzi na hivyo wanakuwa hawajajikinga na dhambi, bali
wanaiendeleza.
Aidha, aliwashauri wale ambao ni watumishi wa Mungu na ambao hivi sasa
wameathirika na ugonjwa huo wamgeukie Mungu kwa kutubu ili aweze kuwasaidia
kuishi kwa matumaini.
Hata hivyo, aliwataka kinamama hao kutumia uwezo waliupata katika kuwaelimisha
wananchi juu ya athari za ugonjwa wa ukimwi, ikiwa ni pamoja na kuzungumza na
familia zao bila woga kuhusiana na ugonjwa huo.
Katibu huyo alisema mama ndiye kitovu cha familia, hivyo ana wajibu mkubwa katika
kukaa na kuzungumza nayo juu ya maadili mema na mienedo bora ya watoto, hasa
kuwaeleza juu ya ugonjwa wa ukimwi bila woga.
Alisema baadhi ya kinamama wamekuwa wakiogopa kuongea na familia zao juu ya
mienendo mibaya waliyonayo watoto wao ikiwa ni pamoja na kuwaeleza juu ya ugonjwa
huo na hivyo kuwafanya waingie katika janga la ugonjwa huo.
Alisema madhumuni ya semina hiyo ni kuwawezesha wake za wachungaji kuelewa na
kushiriki katika huduma ya kutunza wagonjwa nyumbani pamoja na kuwapa ushauri
nasaha.
Semina hiyo iliandaliwa na Kanisa Anglikana la Tanzania ambapo liliwashirikisha
jumla ya Mama Wachungaji 35 kutoka katika wilaya za Manyoni, Kongwa, Mpwapwa na
Dodoma mjini.
Dk. Mahanga awataka wananchi kuichagua CCM
Na Nashon Maingu
WANACHAMA wa CCM na wananchi kwa ujumla wametakiwa kuiga mfano wa Wazanzibari kwa
kuwapigia kura wagombea wa CCM katika uchaguzi mkuu mwezi ujao ili kudumisha
amani.
Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na mgombea ubunge, jimbo la Ukonga, kupitia
CCM , Dk. Makongoro Mahanga, alipokuwa akihutubia mkutano wa kampeni katika
viwanja vya Kilimani.
"Kule Zanzibar wapinzani wamenyolewa kwa wembe mkali na kuwaacha vipara, basi na
sisi Tanzania bara tuwakwanguwe kabisa ngozi ili wasambaratike,"alisema Dk.
Mahanga.
Mgombea huyo amewatoa shaka wakazi wa kata ya Kitunda katika maeneo yaliyokuwa
yametengwa kwa ujenzi wa viwanda kuwa sasa serikali imekubali yawe maeneo ya
makazi na kuwa kazi ya kupima viwanja imeishaanza.
Mgeni rasmi katika mkutano huo, J. Gasaya ambaye ni Mwenyekiti wa mtaa wa Kivule,
kwa vipindi viwili mfululizo, amewaonya wana CCM ambao wanasemekana kuajiriwa na
wapinzani katika kata hiyo ili kuweka makundi.
Imebainika kuwa baadhi ya wanachama wanadanganywa na wapinzani kuwa watapelekewa
maendeleo, kama vile barabara, zahanti, shule na watapatiwa masoko ya uhakika ya
kuuza mboga na mayai.
Mwenyekiti wa mtaa aliwambia wananchi kuwa ili kuwasogezea maendeleo na pia
kuongeza ajira, serikali ya awamu ya tatu imeishaidhinisha kugawanya kata ya
Kitunda kuwa kata mbili.
Kata moja itajumuisha mitaa ya Kitunda kati na Mzinga na kata ya pili itakuwa na
mitaa ya Kivule na Kipunguni B.
Naye mgombea kiti cha udiwani Johness Kasema aliwataka wana CCM kuwa askari
mahiri wa kulinda amani na usalama uliopo.
Mwenyekiti wa CCM, wilaya ya Ilala Mikidadi Mahamud aliwakumbusha kuwa kata ya
Kitunda ilivunja rekodi ya taifa kumpigia kura Rais Benjamin Mkapa mwaka 2000 na
hivyo kuwataka mwaka huu wazidishe maradufu ya hapo na kuwapitisha wagombea wote
watatu wa CCM.
Mwenegoha: wapinzani wanaozuia uchangiaji maendeleo wapuuzwe
Na Latifa Ganzel na Prosper Kulita, Morogoro
MGOMBEA ubunge jimbo la Morogoro Kusini kupitia CCM, Hamza Mwenegoha amewataka
wananchi kuwa macho na vyama vya upinzani vyenye sera ya kuzuia kuchangia ujenzi
wa shule kwani kufanya hivyo ni kuondoa kasi ya maendeleo ya elimu.
Mwenegoha ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ujenzi alisema
hayo mwishoni mwa wiki alipokuwa akiongea na wananchi wa kijiji cha Kibangile
Morogoro vijijini juu ya uchangiaji wa ujenzi wa shule za sekondari.
Alisema kumekuwa na tabia ya baadhi wa vyama vya upinzani kuwarubuni wananchi
wasichangie ujenzi huo hali ambayo inarudisha nyuma maendeleo ya elimu.
Aliongeza kuwa tangu kuanza kwa mpango wa kuchangia ujenzi wa shule za msingi na
sekondari hali ya elimu imepanda tofauti na awali.
Wakati huo huo, imeelezwa kuwa sera za CCM zilizowekwa katika kutafuta maendeleo
hazipo kuwabagua wanachama wa vyama vya wapinzani wala wagombea wa vyama hivyo
badala yake zitafanya kazi kwa malengo ya kuwatafutia maendeleo Watanzania wote
bila kujali itikadi zao.
Hayo yamesemwa na msemaji mkuu wa CCM jimbo la Morogoro Mjini ambaye pia ni kaka
wa mgombea ubunge kupitia CUF, Mbarala Mharagande, Mahiku Maharagande alipokuwa
akielezea sera za CCM katika uzinduzi wa kampeni za ubunge na udiwani awamu ya
pili zilizofanyika katika kata ya mji mkuu manispaa ya Morogoro mwishoni mwa
wiki.
Alisema baadhi ya wapinzani wakiwemo vijana ambao wanavishabikia vyama hivyo wana
mtazamo wa kubaguliwa iwapo CCM itashika madaraka na kuwa sera za CCM hazibagui
wala kuweka matabaka.
Mharagande alisema wafuasi wa vyama vya upinzani pamoja na viongozi wao lazima
watambue kuwa sera za kuwaneemesha Watanzania kiuchumi hazitalenga mwana CCM ama
shabiki wa CCM badala yake zitaangalia watu wote.
Wahimizwa kujenga mabweni katika shule za sekondari
Na El-hadji Yuusuf, Tabora
SERIKALI imewataka wakazi wa mkoa wa Tabora waanze sasa kujenga mabweni katika
shule za sekondari za kata kwa ajili ya kulala wanafunzi wanaoishi mbali na shule
hizo, ili kuwaepusha na vishawishi vinavyosababisha washindwe kuendelea na
masomo.
Wito huo, umetolewa na Mkuu wa mkoa wa Tabora, Abbas Kandoro, wakati akihutubia
wananchi katika mkutano wa hadhara, uliofanyika kijiji cha Goweko, wilaya ya
Uyui.
Mkuu mkoa, aliwaambia wananchi kuwa, sekondari zinazoendelea kujengwa katika kila
kata ni vyema zikawa na mabweni ya kulala wanafunzi, hususan wa kike
ili kuwaepusha na vishawishi, ambavyo husababishia wengi kushindwa kuendelea na
masomo.
“Mwanafunzi anayelala bwenini ana muda mwingi wa kujisomea tofauti na yule
anayelala nyumbani, kwa kuwa ana muda mwingi wa kujifunza na kupata msaada wa
walimu wakati wote, hivyo kuwa na maendeleo mazuri ya masomo tofauti na yule
anayesoma na kurudi nyumbani kwao jioni,” alisema Kandoro.
Mkuu wa mkoa ambaye alikuwa katika ziara ya kukagua shughuli za maendeleo,
aliwataka wananchi hao kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa shule ya sekondari ya
kata hiyo ili watoto wao waanze kuitumia katika muhula wa kidato cha kwanza
mwakani.
Alieleza kwamba jitihada za serikali za ujenzi wa shule za sekondari katika kila
kata zitafanikiwa haraka iwapo wananchi katika kata hizo watahamasika na
kuchangia ujenzi wa shule hizo kwa kutumia nguvu zao.
Katika ziara hiyo ya kukagua miradi ya maendeleo, mkuu wa mkoa aliweka jiwe la
msingi katika jengo la vyumba vinne na ofisi ya shule ya sekondari ya kata ya
Goweko na nyumba ya mwalimu ambapo majengo hayo yanatarajia kukamilika kati ya
mwezi ujao ili yaanze kutumika mwakani.
Katika hatua nyingine, mkuu huyo wa mkoa amewaagiza watendaji kuwa ifikapo
Januari mwakani, watoto wote waliokusudiwa kuandikishwa kwenda shule, wawe
wameandikishwa, vinginevyo wazazi au walezi wakamatwe na kuwajibishwa kwa mujibu
wa sheria.
Akihutubia wananchi kwenye mkutano wa hadhara, Kandoro amewataka viongozi wa
serikali za vijiji kutumia sheria kuwabana wazazi wasiotaka kupeleka watoto wao
wakaandikishwe kwa ajili ya kuanza darasa la kwanza mwakani.
Agizo hilo lilitolewa kufuatia risala ya wakazi wa kata hiyo kwa mkuu wa mkoa,
ambayo ilieleza kuwa hadi kufikia mwezi huu, wazazi na walezi katika kata hiyo
wameandikisha watoto 200 tu, wakati lengo la kata ni kuandikisha watoto zaidi ya
1,000.
Kamati za ujenzi wa shule zatakakiwa kumaliza kazi
Na Bahati Alex, Iringa
SERIKALI wilayani Njombe imezitaka kamati za ujenzi wa shule za msingi na
sekondari, kumaliza ujenzi wa vyumba vya madarasa, vyoo na nyumba za walimu kabla
ya Desemba 15, mwaka huu.
Mkuu wa wilaya ya Njombe, Halima Kihemba aliyasema hayo wakati wa ziara ya wiki
mja ya ukaguzi wa shule za sekondari na kuzungumza na kamati za ujenzi.
Aliziambia kamati hizo kuwa, kushirikisha wananchi na serikali kwa ukaribu
kunaweza kuweka mipango madhubuti na mikakati itakayowezesha watoto watakaofaulu
kuanza kidato cha kwanza mwakani kuendelea na masomo.
Shule zilizochelewa kupokea wanafunzi mwaka jana ni Jackson Makweta, iliyopo kata
ya Igongolo na shule ya sekondari Uliwa iliyopo kata ya Iwungilo.
Jumla ya shule za sekondari mpya 13 zimefunguliwa mwaka huu wilayani Njombe, kati
ya shule 28, zilizofunguliwa mkoani Iringa.
Wakati huo huo, jumla ya viwanja 6,000 vya ujenzi wa nyumba bora vinatarajiwa
kupimwa katika kata ya Makambako wilayani Njombe mkoani hapa ili kukamilisha
ujenzi wa mji mdogo utakaojengwa kufuatia sheria za mipango miji.
Ofisa Mtendaji wa mji mdogo wa Makambako, Godwin Beeny alisema upimaji wa viwanja
hivyo utauweka mji huo katika ramani ya mji wa kisasa kuliko ulivyo hivi sasa.
Alisema Makambako inayokadiriwa kuwa na wakazi zaidi ya 52,000 umepitishwa kuwa
mji mdogo, lakini nyumba nyingi zimejengwa holela bila kufuata utaratibu
unaotakiwa kufuatwa.
Katika hatua nyingine wakazi wa wilaya ya Makete mkoani hapa wametakiwa
kuwasaidia watoto yatima na waathirika wa ukimwi, kwani wanapata shida sana
kutokana na mazingira wanayoishi.
Wito huo umetolewa na Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania
(KKKT) Dayosisi ya Kusini-Kati, Shadrack Manyeiwa wakati akiongea na wakazi wa
tarafa ya Bulongwa, wilayani Makete, ili kuwahamasisha wawe na moyo wa kujitolea
katika kuwasaidia walio na shida.
Tupigwe na wafuasi wa CUF, kisha tulipwe fidia, hapana…!
Na Dunia Mzobora
BILA shaka, nitatofautiana kwa kiasi kikubwa na wanataaluma wenzangu wa habari
kutokana na hili la kupigwa, kisha tukubali kulipwa fidia.
Nitatofautiana na wengi kwa sababu yapo masuala ya mtu kupigwa na baadaye
mahakama au wazee wakaketi na kisha wakamwamuru muhusika alipe fidia na
aliyepigwa au kuumizwa kuipokea fidia hiyo.
Hili kwa namna fulani linakubalika na kwa kiasi kikubwa, fidia aliyolipa muhusika
huyo huweza kumpa fundisho la kutorudia makosa yake, na wakati huo huo kumpoza
aliyefidiwa kwa namna moja.
Kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyochapishwa na Taasisi ya Uchunguzi
wa Kiswahili (TUKI) mwaka 1981, Uk. wa 55, fidia ni malipo kwa ajili ya hasara au
maumivu yaliyofanywa.
Ni kweli wanataaluma wenzetu wamepigwa, wameumizwa, na hivi sasa wanaugulia
maumivu makali mwilini mwao… vyombo vyao vya kazi, zikiwemo kamera na magari
navyo viliharibiwa vibaya.
Si hivyo tu, heshima na utu wa wanataaluma wenzetu umeporomoka mbele ya jamii
kutokana na kipigo kile cha ‘mbwa mwizi’, na mbaya zaidi ni kwamba wameathirika
kisaikoliojia.
Kwa namna yoyote ile, hili la kupigwa na wafuasi wa chama cha CUF na kisha
‘tupozwe machungu’ kwa kupokea fidia itakayolipwa na chama hicho ni jambo ambalo
halikubaliki.
Kama ni kulipwa, fidia hiyo italipwa na waajiri wao kwa sababu wanataaluma hawa
walipatwa na madhila hayo wakiwa kazini, na sheria za kazi zinaweka bayana kuhusu
suala hilo.
Vinginevyo, wanataaluma ya habari kupitia ‘majukwaa’ yetu mbalimbali tunaweza
kukutana na kuchangishana kidogo kidogo na kisha tukawapa ‘pole’ wenzetu hawa,
John Maxmillian na Salehe Masoud.
Kuikubali fidia ya CUF ni kukubali ‘kujiua’ kwa kisu chetu wenyewe. Kwamba,
watakuwa wakitupiga kwa makusudi kwa kutambua kwamba kesho yake watalipa fidia.
Kamwe tusikubali mchezo wa mume ‘mshenzi’ anayempiga mkewe kila mara kwa kutambua
kuwa kesho yake atamwangukia kwa doti ya khanga au kitenge cha Wax! Huu ni
upuuzi.
Tangu tukio la awali la kupigwa kwa ‘mdogo wangu’ Khalfan Said na mwenzake na
wafuasi wa chama hicho, CUF ilikaa kimya kabisa kana kwamba hakuna kilichotokea.
Hata baada ya kutokea hili la kupigwa kwa kina Maxmillian, CUF haikujali mpaka
vyombo vyenyewe vya habari vilipoichachamalia, ndipo zikaanza kujitokeza kauli za
‘kujikosha’.
Kimsingi, siandiki hivi kwa kuwa ni mwandishi na mhariri katika gazeti la Chama
tawala, la hasha, naandika kama mwanataaluma wa habari, ambaye ningeweza kuandika
haya katika chombo na mahali popote duniani.
Ninaomba nieleweka vyema kwamba, hapa sisukumwi na itikadi ya chama au
ukereketwa, bali misingi na kanuni zinazoongoza taaluma ya habari, ambayo
nimeisomea ndani na nje ya nchi.
Hivi mbona tukio la kupigwa kwa kina Mpoki Bukuku na Christopher Kidanka na
askari magereza na wafungwa wao, vyombo vya habari havikusita kuchukua hatua
dhidi ya wakubwa wa taasisi hizo?
Kila mmoja ameshuhudia jinsi Waziri wa Mambo ya Ndani, Omar Ramadhani Mapuri na
Kamishna Mkuu wa Magereza, Nicas Banzi ‘walivyosuswa’ na baadhi ya vyombo vya
habari vya hapa nchini.
Kumbe ni kitu gani, kama wanataaluma ya habari kinachotufanya tushindwe kuiadhibu
CUF kwa kususia habari zake, japo kwa kipindi fulani cha mwaka mpaka uongozi wake
utakapoheshimu taaluma na wanataaluma ya habari.
Kama chenyewe katika moja ya kauli mbiu yake ni ‘haki sawa kwa wote’, iweje chama
hicho kishindwe kuheshimu uhuru na haki ya wanahabari kuandika na kupasha habari
jamii?
Kwa heshima na taadhima, ninawaomba wanahabari tuache unafiki na tufuate kanuni
za msumeno, ambao unakata huku na huku kwa kuiadhibu CUF kwa kuacha kuandika au
kutangaza habari zao, achilia mbali ati kupokea fidia!
Vinginevyo, kuendelea kuandika na kutangaza habari za CUF tena kwa kuona kama
matukio yale yalifanywa kwa bahati mbaya, tunakifanya chama hicho kizidi kuwa
‘nunda’, na tusije tukashangaa ya baadaye, kwani ‘mchelea mwana kulia hulia
yeye’!
Alamsiki!