UHURU 15.11.2005
Nahodha awaasa Wawakilishi waache malumbano yasio na faida kwa wananchi
Na Khatib Suleiman,Zanzibar.
WAZIRI Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Shamsi Vuai Nahodha
amewataka Wawakilishi waliochaguliwa na wananchi kuwatumikia katika maeneo ya
majimbo ya uchaguzi na kuacha kuendeleza utashi wa kisiasa wa malumbano
yasiyokuwa na faida yeyote.
Akiliahirisha Baraza la Wawakilishi hadi Januari 18 mwakani, Shamsi alisema
Wawakilishi wanapaswa kuyafahamu vyema majukumu yao yanayowapa uhalali wa kuwa
Wawakilishi katika majimbo ya uchaguzi Unguja na Pemba.
'Huu sio wakati tena wa kuendeleza utashi wa kisiasa wa malumbano yasiyokuwa na
msingi,” alisema Shamsi na kuwa kazi kubwa inayowakabili wajumbe hao ni
kuwahudumia wananchi kwa kuwapelekea maendeleo.
Alisema tabia ya kambi ya upinzani ya chama cha CUF kususia vikao vya Baraza la
Wawakilishi pamoja na kutangaza kutomtambuwa Rais wa Zanzibar aliyechaguliwa
kutokana na ridhaa ya wananchi wa Unguja na Pemba ni kwenda kinyume na dhana
nzima ya demokrasia ya utawala bora na katiba.
Aliongeza kuwa katika dhana ya demokrasia na utawala bora, siku zote imekuwa
ikisisitiza umuhimu wa kuheshimu nguvu ya umma inayotokana na ridhaa ya wengi na
kitendo cha kukataa matokeo ya uchaguzi mkuu yanayotokana na ridhaa ya wengi ni
sawa na udikteta.
Shamsi aliwataka Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kufuatilia kwa karibu matatizo
na shida zinazowakabili wananchi katika majimbo ya uchaguzi kwa ajili ya
kuyapatia ufumbuzi.
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kutoka katika kambi ya CUF walihudhuria kikao na
walikuwepo muda wote wa hotuba hiyo ya kuahirisha kikao cha Baraza la
Wawakilishi.
Mapema Spika wa Baraza la Wawakilishi Pandu Ameir Kificho alimuapisha mjumbe wa
Baraza hilo aliyeteuliwa na Rais wa Zanzibar Amani Abeid Karume kupitia nafasi
kumi za rais ambaye ni Hasnuu Mohammed Haji kutoka Pemba.
Maofisa wa polisi mipakani wapatiwa mafunzo maalum
Ni kuhusu madhara ya mionzi
Na Mohammed Mhina wa Jeshi la Polisi, Arusha
MAOFISA wa polisi wanaofanya kazi katika maeneo ya mipakani hapa nchini wameanza
kupatiwa mafunzo maalumu juu ya madhara yatokanayo na mionzi na jinsi ya
kukabiliana na matukio yatokanayo na nguvu za Atom.
Mafunzo hayo ambayo yanafanyika mjini Arusha na kufadhiliwa na Shirika la Polisi
la Kimataifa (Interpol) na kamisheni ya nguvu za Atom ya Uingereza pia
yanawashirikisha baadhi ya waendesha mashitaka na maofisa wa Jeshi la Wananchi wa
Tanzania.
Akifungua mafunzo hayo jana, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini
Kamishna Adadi Rajabu, alisema mafunzo hayo yatawezesha wapelelezi kubaini jinsi
ya kukabiliana na matukio ya mionzi hasa katika maeneo ya mipakani.
Alisema mionzi imebainika kuwa inaweza kutumiwa na magaidi kama silaha za
maangamizi hivyo polisi imeonelea ni muhimu kutoa mafunzo kwa watendaji wake ili
kuweza kukabiliana na matukio kama hayo pindi yanapotokea.
Hii ni mara ya pili kwa mafunzo kama hayo kutolewa kwa watendaji wa vyombo vya
ulinzi na usalama hapa nchini.
Mafunzo ya awali yalifanyika Septemba mwaka huu na kuwashirikisha maofisa wa
vyombo vya ulinzi na usalama kutoka nchi za Afrika Mashariki.
Wakitoa maoni yao, baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo walisema yatawasaidia sana
kuelewa aina ya mionzi na jinsi ya kukabiliana nayo.
Washiriki wa semina hiyo ni kutoka mikoa ya Rukwa, Kigoma, Kagera, Dar e s
Salaam, Mtwara, Kilimanjaro, Tanga na Arusha.
Mbinu za kutafuta soko kikwazo kwa wafanyabiashara nchini
Na Solomon Mwansele, Rungwe
BIDHAA zinazozalishwa nchini zinakidhi mahitaji na viwango vya kuweza kushindana
katika soko la kimataifa, lakini tatizo linalowakabili
wazalishaji wa Tanzania ni ukosefu wa mbinu za kutafuta masoko.
Hayo yalisemwa na meneja wa SIDO mkoani Mbeya Tresphur Mubito, wakati wa kufunga
mafunzo ya wiki tatu ya usindikaji wa vyakula na matunda katika wilaya ya Rungwe
mkoani Mbeya.
Mubito alisema uchumi wa Tanzania hauwezi kukua kama inavyotarajiwa endapo
wazalishaji hawatapatiwa mbinu na mafunzo ya kutosha jinsi ya kuingia katika soko
la kimataifa kwa ajili ya kuuza bidhaa wanazozalisha hapa nchini.
"Zikizalishwa bidhaa bora ni rahisi kupata masoko ya uuzaji wa bidhaa hizo nje ya
nchi, wafanyabiashara wanapaswa kutengeneza bidhaa kulingana na mahitaji ya soko
katika nchi jirani," alisema Mubito.
Aliwataka wahitimu hao kuwa wabunifu wanapotengeneza bidhaa zao kulingana na
mahitaji ya soko badala ya kung'ang'ania kutengeneza aina moja ya bidhaa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Rungwe Masanga Buliga,
alisema kuwa usindikaji huo utaongeza thamani na kuhamasisha uzalishaji wa mazao
ya kilimo ambayo yatapata soko la uhakika kwa wakulima kutokana na mazao hayo
kuhitajika katika usindikaji.
Buliga alisisitiza usindikaji huo ufanyike kwa makini na kuhakikisha bidhaa hizo
zinatengenezwa kwa viwango bora kwa kuzingatia afya ili zisilete madhara kwa
watumiaji hali ambayo inaweza kuharibu soko.
Mkurugenzi huyo alisema mikopo kwa ajili ya vikundi vya vijana, wanawake, watu
wenye ulemavu na wazee inatolewa na halmashauri hiyo.
Alibainisha kuwa mikopo hiyo inatolewa kwa watu waliojiunga katika vikundi na
walio na nia ya dhati ya kuanza uzalishaji kwa lengo la kuondokana na umasikini.
Kwa upande wao, wahitimu wa mafunzo hayo walisema ukosefu wa mitaji unachangiwa
kwa kiasi kikubwa na masharti magumu ya kupata mikopo na kuwa wazalishaji wadogo
wengi wanashindwa kumudu kukopa hivyo kushindwa kuanza uzalishaji.
Walisema inahitajika elimu ili waweze kuzithamini na kununua bidhaa za ndani ili
kukuza na kuinua pato la mwananchi wa kawaida na hatimaye taifa.
Katika mafunzo hayo ya wiki tatu,baadhi ya mambo yaliyofundishwa ni pamoja na
ujasiliamali, makundi ya vyakula, usindikaji wa unga wa lishe, sosi ya pilipili
pamoja na afya na ubora wa vyakula.
Mafunzo hayo yalikuwa na washiriki 25 kutoka kata za Bulyaga, Bagamoyo, Katumba,
Mpuguso, Masoko na Kandete.
Karume: SMZ kuwa makini katika utekelezaji wa Ilani ya CCM
Na Mwandishi Wetu
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (Zanzibar) Rais Amani Abeid Karume
amesisitiza kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) itakuwa makini katika
utendaji na utekelezaji wa sera na Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kipindi cha miaka
mitano ijayo kuanzia mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu mjini Zanzibar ilisema Rais Karume ameeleza hayo
jana alipofanya mazungumzo na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa CCM Zanzibar,
huko Ikulu.
"Utendaji wa majukumu ya viongozi serikalini pamoja na utekelezaji wa sera na
Ilani ya Uchaguzi ya 2005-2010 ya CCM ni changamoto kubwa ilinayokabili Serikali
hivi sasa," alisema Makamu Mwenyekiti huyo.
Alikumbusha kuwa wawakilishi wana dhamana kubwa waliyokabidhiwa na wananchi
ambapo wanatakiwa kutekeleza Ilani iliyotokana kwa mujibu wa mkataba kati ya CCM
na wananchi.
Akihimiza suala hilo katika mkutano huo, Rais Karume alisema: " Tuna dhamana
kubwa tuliyopewa na wananchi... kila mmoja mkiwa katika nafasi za uongozi, ndani
au nje ya baraza tujitahidi kama inavyowezekana kusimamia utekelezaji wa sera na
Ilani ya CCM."
Alisisitiza kuwa wajumbe wa baraza wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kuwafunza
na kuwaelimisha wajumbe wa kambi ya upinzani kutokana na udhaifu wao katika
baraza hilo ambapo upinzani unaendeleza tabia ya kususia vikao jambo ambalo
linapingana na taratibu na misingi ya demokrasia.
Karume alisema ni muhimu kuelewa kuwa nguvu kubwa ya ushindi na uimara wa CCM
unatokana na utekelezaji wa sera za umoja, mshikamano, amani na utulivu, pamoja
na ushirikiano kati ya wananchi na viongozi na kwamba hiyo ndiyo sababu kubwa ya
ushindi wa CCM kwa miaka yote.
"Tuchukue dhamana ya kuwasomesha wapinzani wetu na kuwafahamisha taratibu za
demokrasia kwa kutumia busara na hekima bila ya malumbano na kuweza kuimarisha
ushirikiano ndani ya baraza," alisisitiza Karume.
"Katika utawala wa demokrasia mambo muhimu ya kuyadumisha ni utekelezaji wa
shughuli za serikali kwa mujibu wa Katiba, sheria za nchi na kuheshimu dhamana ya
taasisi za demokrasia zilizoanzishwa nchini, aliongeza Rais Karume.
Alieleza kuwa pamoja na juhudi zilizochukuliwa na chama tawala za kuanzisha
mazungumzo ya Muafaka wa kwanza na wapili, bado upinzani haujabadilika na
unaendelea na tabia ile ile ya kususia na kukiuka taratibu za msingi za mfumo wa
demokrasia.
Mgombea Mwenza wa CHADEMA atambulishwa rasmi
Ni Anna Valeria Komu
Na Mwandishi Wetu
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) jana kilimtambulisha rasmi mgombea
mwenza wake, Anna Valeria Komu kwa waandishi wa habari.
Utambulisho huo ulifanyika mbele ya viongozi wa chama akiwemo Mwenyekiti na
Mgombea Urais, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk. Wilbrod Slaa, katika makao makuu
ya chama hicho, Kinondoni Dar es Salaam.
Anna ni mzaliwa wa Kwabijokha Zanzibar, mwaka 1950 na jina lake la awali lilikuwa
ni Maulida Abubakary. Alibadili dini na jina na kuwa Anna, baada ya kuolewa na
Valerian Komu, mwenyeji wa Mkoa wa Kilimanjaro.
Kwa mujibu wa muhtasari wa wasifu wake, Anna ni miongoni mwa waasisi wa chama
hicho na alianza na uongozi katika ngazi ya chini kabisa, akiwa katibu wa tawi
huko Mawela, Uru Moshi.
Baadaye alipanda na kuwa katibu wa wilaya ya Moshi na kukwea ngazi hadi Katibu wa
mkoa wa Kilimanjaro na akateuliwa kuwa Kaimu Katibu Mwenezi wa CHADEMA Taifa.
Ameshashika vyeo vya Naibu Mkurugenzi wa Wanawake, pia kukaimu nafasi hiyo mwaka
jana.
Akizungumzia malengo yake iwapo atabahatika kuingia Ikulu kama Makamu wa Rais,
Anna alisema lengo lake ni kuona mapinduzi makubwa katika suala la maendeleo ya
wanawake.
Pamoja na malengo hayo, ameeleza kuridhika na hatua iliyofikiwa sasa hivi, ambapo
wanawake wengine wamejitokeza katika kuwania nafasi za uongozi wa kisiasa.
Mgombea mwenza huyo anayesubiri kuthibitishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC),
alisema hali ya wanawake wa kawaida bado wana maisha magumu mno na kuna haja ya
kuwepo kwa mikakati ya kuwainua.
Kabla ya kujiunga na CHADEMA alikuwa mwana CCM mwanzilishi na kabla ya hapo,
harakati za siasa alianza akiwa katika kundi la vijana chipukizi wa chama cha ASP
na baadaye akawa mwanachama kamili.
Ameolewa na ana watoto wanane. Alisema mumewe ni mwajiriwa katika ofisi moja huko
Visiwani, lakini si mwanasiasa.
TACAIDS yashauriwa Kushirikisha halmashauri
Na Pendo Mangala, Dodoma
TUME ya Kudhibiti Ukimwi nchini (TACAIDS) imetakiwa kuwashirikisha watumishi wa
halmashauri za wilaya katika mapambano dhidi ya ukimwi ili kusaidiana nao katika
kupunguza kasi ya maambukizi mapya ya ugonjwa huo.
Hayo yalisemwa jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na
Watoto Hilda Gondwe alipokuwa akifungua warsha kuhusu ukimwi kwa waratibu wa
kamati za kudhibiti ukimwi iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Veta mjini
hapa.
Gondwe alisema TACAIDS inatakiwa ishirikiane na watumishi wa halmashauri za
wilaya katika mapambano dhidi ya ukimwi ili kusaidiana nao katika kupunguza kasi
ya maambukizi mapya ya ugonjwa huo.
Alisema Tume imekuwa ikiwasahau watumishi wa halmashauri hizo za wilaya katika
kuwashirikisha kwenye mapambano dhidi ya ukimwi na hivyo kushindwa kufikia
malengo waliyoyaweka.
Katibu Mkuu alisema watumishi wa halmashauri za wilaya nchini ni moja ya sehemu
kubwa katika TACAIDS kwani ni wahusika wakubwa katika kutekeleza mapambano ya
udhibiti wa ukimwi katika jamii na nchi kwa ujumla.
Alisema endapo viongozi husika wa Tume hiyo watawashirikisha watumishi hao
wataweza kufikia malengo waliyoyaweka.
Hata hivyo alifafanua kwamba masuala ya udhibiti ugonjwa huo wa ukimwi ni magumu
kutokana na kuambatana na matatizo mbalimbali katika jamii.
Alisema matatizo hayo ambayo yamekuwa yakichangia udhibiti wa ukimwi kuwa mgumu
ni matatizo ya usiri, ukimya, unyanyapaa, aibu na kulinda haki za binadamu.
Warsha hiyo ya wiki moja imeandaliwa na TACAIDS na kuwashirikisha waratibu wa
Halmashauri za Tanzania bara.
TRA Mbeya yakamata sukari ya magendo
Na Solomon Mwansele, Mbeya
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Mbeya imekamata sukari ya magendo tani
nne yenye thamani ya sh. milioni 2.2 iliyokuwa imeingizwa nchini kutoka nchi
jirani ya Malawi bila ya kulipiwa ushuru.
Sukari hiyo imekamatwa na maofisa wa TRA eneo la Simambwe ikiwa imepakiwa katika
gari lenye namba za usajili T 765 ABX aina ya Fuso, likiendeshwa na Charles
Hilary baada ya raia wema kutoa taarifa juu ya
kuingizwa kwa sukari hiyo nchini. Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini
kwake, Kaimu Meneja wa TRA mkoa Alphonce Mahende alisema mhusika wa sukari hiyo
hajakamatwa, lakini TRA inamshikilia dereva ili amtaje mfanyabiashara aliyemkodi
kubeba sukari hiyo.
Mahende alisema baada ya TRA kupewa taarifa hiyo, ilituma maofisa wake
kulifuatilia gari hilo na walikutana nalo eneo hilo la Simambwe lakini
walipolisimamisha dereva alikaidi na kuligeuza kurudi lilikokuwa linatoka.
"Walikaidi kusimama na kurudi kuelekea njia ya Tukuyu na walijaribu kuwazuia
maofisa wetu
wasifanye kitu kutokana na eneo hilo kutokuwa na mawasiliano na walijua kuwa
hawataweza kupiga simu kuomba msaada," alisema Mahende.
Aliongeza kuwa maofisa hao wa TRA walipoachiwa baada ya gari hilo kutoweka ndipo
walipoweza kutafuta eneo ambalo walifanikiwa kuwasiliana nao na kuwaeleza hali
halisi iliyotokea.
Kaimu Meneja huyo alisema kabla ya kuondoka waliomba msaada wa askari watatu
kutoka kituo kidogo cha polisi Uyole na kuelekea eneo hilo na walipolifuatilia,
walilikuta likiwa limewekwa kando ya barabara mpya ya kuelekea Inyala huku sukari
ikipakuliwa.
Alibainisha kuwa vijana waliokuwemo katika gari hilo walijaribu kuwazuia maofisa
hao bila ya kuwaogopa
askari ambao hawakuwa wameenda na silaha na kuendelea kupakua sukari kutoka
katika gari hilo na kwenda kuificha katika nyumba za majirani.
"Kuona hivyo ilitubidi tuombe tena msaada wa askari kutoka kituo cha Inyala ambao
walikuja na silaha kitu
kilichopelekea vijana wale wakimbie na kuliacha gari, dereva na utingo wake,"
alisema Mahende.
Mahende alisema hawakuweza kujua gari hilo lilikuwa na sukari tani ngapi, kwani
sukari nyingine
iliyoshushwa ilikutwa ikiwa imefichwa katika migomba.
Sukari iliyofanikiwa kufikishwa ofisi za TRA mkoa ni katoni 200 za kilo 20 kila
moja ambayo ni sawa na tani
4 yenye thamani ya sh. milioni 2.2.
Sh. milioni 463 zatumika kwa ujenzi kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Dodoma
Na Pendo Mangala, Dodoma
Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere
JUMLA ya sh. milioni 463.8 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa awamu ya kwanza wa
jengo la kumbukumbu ya Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere (Nyerere
Square) lililopo mjini hapa.
Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu
(CDA) Abdullahaman Mbwambo alipokuwa akiongea na waandishi wa habari mjini hapa.
Mbwambo alisema fedha hizo zimetolewa na Serikali Kuu kwa mamlaka hiyo kwa ajili
ya ujenzi wa jengo la kumbukumbu hiyo.
Alisema jengo hilo litakuwa ni moja ya kumbukumbu katika kumuenzi hayati Baba wa
Taifa kwani ni jengo la kihistoria katika vizazi vijavyo kuweza kujua umuhimu wa
Mwalimu Nyerere pamoja na shuguli alizofanya katika nchi hiyo .
Hata hivyo alisema Nyerere ni mtu ambaye amefanya mambo mengi mbalimbali na yenye
manufaa kwa umma na kwa nchi ya Tanzania kwa ujumla na kwamba ndiye mwasisi wa
kutoa wazo la Makao Makuu ya nchi kuhamia Dodoma.
Alisema mji wa Dodoma ndiyo kitovu cha nchi hivyo wazo hilo la hayati Baba wa
Taifa liko sahihi na halina budi kutekelezwa na viongozi wa Serikali.
Aliwataka wananchi kumuenzi Baba wa Taifa kwa kwa yale yote mema aliyoyafanya
enzi za uhai wake ili kuweza kuyaendeleza na kukuza sifa ya nchi kama alivyokuwa
akifanya
Pia alisema kampuni ya simu za mikononi Vodacom nchini kwa kushirikiana na
serikali imejitolea kujenga bango kubwa ndani ya jengo hilo ambalo litakuwa
likirusha hotuba mbalimbali katika redio na kuonyesha picha za mwalimu kwenye
televisheni tofauti za hapa nchini kwa lengo la kumuenzi.
Mbwambo alisema kampuni hiyo imesema inatambua mchango mkubwa uliotolewa na
hayati baba wa Taifa enzi za uhai wake hivyo wao kama kampuni ya simu hawana budi
kuyaendeleza yale yote aliyoyafanya kwa kuyaenzi.
Alisema kampuni hiyo ya Vodacom imeahidi kuwa bega kwa bega na serikali
kuhakikisha wanajenga bango hilo kubwa ndani ya jengo hilo la kumbukumbu ili
kuwezesha wananchi kuangalia na kusikiliza matangazo ambayo yatakuwa yakirushwa
ndani ya jengo hilo.
Ujenzi wa jengo la kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere unatarajiwa kukamilika Septemba
mwakani.
Wadau wa bonde la Wami Ruvu kukutana
Na Prosper Kulita,Morogoro
WADAU wa maji zaidi ya 45 katika Bonde la Wami Ruvu (WRBWO) linalojumuisha wilaya
19 za mikoa mitano ya Tanzania bara wanatarajia kukutana mjini hapa ili kujadili
usimamizi wa pamoja wa rasilimali za maji zilizoko katika bonde hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari, Ofisa wa maji wa bonde hilo, Julius Sarmett
alisema katika warsha hiyo inayotarajiwa kufanyika leo na kesho na kuwahusisha
wadau wa maji kutoka wizara za serikali, watoaji huduma za maji safi na taka
mijini na vijijini, taasisi za utafiti, halmashauri za miji na wilaya, taasisi
zisizo za kiserikali, viwanda na wamwagiliaji.
Alisema washiriki mbali ya kubadilishana uzoefu pia watajifunza dhana ya
usimamizi wa pamoja wa raslimali za maji kimataifa kutoka taasisi ya In Went
yenye makao yake makuu Ujerumani.
Akifafanua, Sarmett alisema rasilimali za maji ni moja ya nyenzo muhimu katika
mpango wa serikali wa kukuza uchumi na kuondoa umaskini nchini (MKUKUTA).
Alisema kulingana na changamoto zinazojitokeza katika usimamizi wa matumizi bora
ya rasilimali za maji mfano kuongezeka kwa mahitaji ya rasilimali za maji,
serikali iliamua kuweka mfumo wa usimamizi wa rasilimali za maji kimabonde na
kuigawa nchi katika mabonde tisa likiwemo la Wami Ruvu.
Pia aliongeza kuwa kufuatana na sera ya maji (NAWAPO 2002) usimamizi wa
rasilimali za maji utatekelezwa katika ngazi tano ambazo ni ngazi za watumiaji,
mabonde madogo, halmashauri za wilaya, mabonde na Taifa.
Alisema ngazi hizo zimewekwa ili kuwezesha na kuimarisha mfumo wa usimamizi wa
pamoja wa rasilimali za maji.
Tanzania yasema kamwe ardhi yake haitatumiwa na waasi
Na Jumanne Gange, Kigoma
SERIKALI katika wilaya Kigoma imeihakikishia serikali ya Burundi kuwa haina
sababu na wala haitoruhusu chama cha waasi cha PELIPEHUTU - FNL na wakimbizi wa
nchi hiyo wanaohifadhiwa nchini kutumia ardhi na mpaka wa Tanzania kuivamia
serikali na wananchi wa Burundi.
Akizungumza katika kikao cha ujirani mwema kati ya wilaya ya Kigoma na wilaya za
Nyanza Lake na Mabanda za nchini Burundi zinazopakana na wilaya ya Kigoma, Mkuu
wa wilaya ya Kigoma, Henry Clemens alisema, kimsingi, mafanikio ya amani
yaliyofikiwa hivi sasa nchini humo ni jitihada za za kimataifa kwa mchango mkubwa
wa serikali ya Tanzania.
Alisema Tanzania inaheshimu maamuzi ya wananchi wa nchi hiyo katika kuiweka
serikali iliyopo madarakani kwa misingi ya kidemokrasia ikwa ni jitihada
zilizoasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Mkuu wa wilaya ya Kigoma alilazimika kutoa msimamo huo kutokana na tahathari
iliyotolewa na serikali ya Burundi kupitia Msaidizi wa Gavana wa mkoa wa Makamba,
katika kikao cha siku moja kilichiofanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Gombe,
mkoani Kigoma kuimarisha usalama, mahusiano ya kijamii na ya kiuchumi baina ya
pande mbili hizo
Gavana Deo Niyonzima ambaye aliongoza ujumbe wa Burundi katika mazungumzo hayo,
alikiambia kikao hicho kuwa serikali ya Burundi inayo taarifa kuwa kikundi cha
PALIPEHUTU -FNL kupitia Congo Mashariki na hatimaye ardhi ya Tanzania wilaya ya
Kigoma kimepanga kuushambulia mkoa huo wa Makamba nchini Burundi.
Niyonzima, aliongoza ujumbe wa watu 13, wakiwemo maafisa wa ngazi za juu wa jeshi
nchini humo, wakuu wa wilaya za Nyanza Lake na Mabanda, wataalamu na
wafanyabiashara wa mkoa huo.
Alisema Burundi inazo taarifa pia za kikundi hicho kutaka kuwashawishi na
kuwatumia baadhi ya wakimbizi wa nchi hiyo katika kambi za wakimbizi mkoani
Kigoma kujiunga nao katika azma yao hiyo.
Aidha, kikao hicho chini ya uenyekiti wa Clemens ambaye aliambatana na kamati ya
ulinzi na usalama na wataalamu kadha ndani ya wilaya yake, kilikubaliana kwa
kauli moja kuweka maazimio 12 kama dira mpya ya mahusiano ya kiulinzi, kiuchumi
na kijamii.
Maazimio hayo ni pamoja na kuwapo kwa vikao vya ujirani mwema kila baada ya miezi
mitatu, kuanzishwa na kuundwa kwa kamati za pamoja za ulinzi, usalama na masuala
ya kibiashara.
Vilevile, kikao hicho kiliazimia kuweka utaratibu wa kisheria wa kubadilishana
wahalifu na mali zilizoibwa baina ya pande mbili hizo.
Vyama na mabaraza ya wafanyakazi yakuze tija
Na El-hadji Yuusuf, Tabora
WAFANYAKAZI nchini wametakiwa wavitumie vizuri vyama, pamoja na mabaraza yao
katika sehemu za kazi kwa ajili ya kuleta ufanisi na siyo kuwa chanzo cha
migogoro na kuwatetea wafanyakazi wazembe.
Kauli hiyo imetolewa mjini hapa na Mkuu wa mkoa wa Tabora, Abbas Kandoro,
alipokuwa akifungua rasmi baraza la wafanyakazi wa mamlaka ya majisafi na
majitaka katika manispaa ya Tabora (TUWASA).
Alisema kuwa ni makosa kwa vyama vya wafanyakazi na mabaraza ya wafanyakazi
nchini, kuwa chanzo cha migogoro na hatimaye kusababisha ufanisi wa kiutendaji
kushuka katika sehemu zao za kazi jambo ambalo alisema kuwa linawaumiza wananchi.
Aliwataka wafanyakazi wawe makini katika utumishi na kuhakikisha kuwa wanayafikia
malengo ya ajira zao, ili kuifanya mamlaka yao iweze kutoa huduma bora za maji
hapa nchini.
Alisema kuwa kwa mujibu wa uchunguzi wake, pale ambapo kuna migogoro mingi ya
kiutendaji katika sehemu za kazi ni kwamba viongozi wa vyama vya wafanyakazi na
mabaraza ya kazi huwa na kasoro kubwa.
Alisema kuwa viongozi kama hao ndiyo wanaosababisha utendaji duni na kutofikiwa
kwa malengo katika sehemu zao za kazi na hatimaye kusababisha utendaji mbovu,
ambao huzua minong'ono na malalamiko kutoka kwa wateja ambao katu hawawezi
kulipia huduma mbovu.
Aliwataka wafanyakazi wa mamlaka hiyo kutambua kuwa mabaraza ya wafanyakazi ya
sasa yanakwenda na wakati na kwamba yenyewe ndiyo yawe kichocheo kikubwa cha
maendeleo katika sehemu za kazi kwa kuhimiza ufanisi na juhudi kwa wafanyakazi na
utawala ili kuwezesha kupatikana kwa maslahi mazuri.
Alisema kuwa hali hiyo inaweza kuepukwa iwapo kama watu wanaochaguliwa kuongoza
vyama vya wafanyakazi na mabaraza ya wafanyakazi wanakuwa na elimu bora na uwezo
wa kuongoza ikiwa ni pamoja na kuishauri menejimenti ifanye nini kuongeza tija.
Alisema kuwa kinyume na hali hiyo ni kukaribisha ubabaishaji katika vyama hivyo,
sambamba na kuwa na vyama vibovu ambavyo viongozi wake ni wapenda majungu na
kulalamika kwa kila jambo na hivyo kuzifanya sehemu za kazi kuwa sehemu zisizo na
amani.
Alisema kuwa atarajika sana iwapo baraza hilo la wafanyakazi analolizindua leo,
litakuwa ni mfano mzuri wa utendaji kazi wa mabaraza ya wafanyakazi nchini, kwa
kusimamia vizuri wajibu wa mwajiri na wafanyakazi na kupigania maslahi ya
wafanyakazi na stahili zao kwa mujibu wa sheria.
Wananchi wawe macho na vyama vinavyowamurika mchana, watambue usiku vitawachoma vikishinda
Na Mwadini Hassan
BINAADAM ni mtu. Mtu ni kiumbe. Katika ulimwengu huu tunaoishi kuna viumbe vya
aina mbali mbali. Lakini sifa kuu ya kiumbe ni kuwa na roho kama vile binaadamu,
mnyama, ndege, samaki na wadudu.
Katika jamii hizo za viumbe, wanyama, ndege, samaki na wadudu ni viumbe
vinavyoishi bila ya kuwa na akili za kuwaza na kupambanua mambo.
Viumbe hivyo viliumbwa na kuwa na akili ya kawaida tu vinavyoweza kuitumia
kujitafutia chakula na namna ya kulea watoto wao. Maumbile yao na kwa akili
walizojaaliwa hawawezi kujua zuri na baya
Ndiyo maana wanyama kwa mfano, hawana akili ya kupambanua kuwa huyu ni mama au
baba yangu. Anakuwa na akili za kujua hayo anapokuwa mdogo tu ili aweze kulelewa
na kukua. Akishakua kwa kukosa kupambanua zuri na baya, ndiyo maana wanaweza
kuzaa na baba ama mama waliowazaa.
Kwao hakuna tofauti ama ubaya wa mtoto kuzaa na mzazi wake, ama dada kuzaa na
kaka wa kuzaliwa naye tumbo moja, au kinyume chake. Kwao vyo vyote ni sawa na
hakuna miongoni mwao atakayemshangaa mwenzake kwa kufanya hivyo. Ni jambo la
kawaida kabisa.
Kwa unyama wao, ndiyo maana kuuana ni jambo la kawaida kwao. Huyu anamuua na
kumla yule bila kimeme au aibu. Ni jambo la kawaida na wala hakuna jamii moja ya
mnyama inayoungana kupambana na ‘maonevu’ hayo.
Mnyama mmoja anamuona mwenzake wa ana ile ile anakamatwa na kuliwa na mnyama wa
aina nyingine, atakalofanya ni kukimbia kujisalimisha yeye tu, na mwenzake
akishakamatwa na kuliwa, na yeye amepona, hana habari. Yamemuishia mradi yeye leo
kanusurika.
Huo ndiyo unyama. Hawakujaaliwa kujua zuri na baya, au hili linafaa ama halifai
kutendwa katika jamii. Na kwa kweli hakuna atakewashangaa ama kuwalaumu. Na hata
Muumba wa mbingu na ardhi, hakuwawekea mipaka ama kanuni za maisha yao. Vyovyote
wanavyoishi viumbe hao ni sawa.
Lakini, hali haikuwa hivyo kwa binaadamu. Binaadamu ni tofauti na mnyama, ndege
ama wadudu. Anatakiwa aishi kwa nidhamu na utaratibu maalum katika maisha yake.
Hiyo inatokana na ukweli kwamba mwanaadamu ni kiumbe mwenye daraja la juu kabisa
kuliko viumbe vyote vilivyoumbwa na Mungu. Hiyo inatokana na kwamba binaadamu
amepewa uwezo mkubwa wa kufikiri. Ana uwezo wa kujua zuri na baya, lipi linalofaa
kutendwa na lipi halifai.
Amepewa pia uwezo wa kutawala mazingira yake na mazingira ya viumbe vingine.
Ndiyo maana basi, binaadamu amepewa uwezo wa kujifanyia mambo mbali mbali
yanayomtofautisha maisha yake na viumbe vilivyonyimwa uwezo wa kufikiri na
kuamua.
Binaadamu kwa sifa hiyo, anajijengea nyumba ya kuishi, anajiandalia chakula chake
kwa kujipikia, anavaa nguo, anachana ama kusuka nywele na mambo mengine kadhaa.
Kwa kujua zuri na baya, hawezi kuzaa na mtoto wake, baba ama mama yake. Kwa
maumbile yake ya ubinaadamu, hawezi kutembea bila kuvaa nguo, na kutokana na
uwezo huo amejitengenezea vitu kadhaa vya kumrahisishia maisha yake. Huo ndiyo
ubinaadamu na huyo ndiye binaadamu.
Inapotokea binaadamu kufanya vitu kinyume cha hivyo, huwa ni kioja. Kwa kweli
binaadamu wenzake watamshangaa, na hata kufikia hatua ya kuamua huyo kiumbe
mwenzao ni punguwani au kumpa sifa ya uwendawazimu.
Na mtu anapoitwa mwendawazimu, huwa ubinaadamu wake umepungua na unaelekea katika
sifa za unyama. Mwendawazimu huwa hajui zuri au baya. Anafanya lolote, mahala
popote na huwa hana tofauti kubwa na mnyama.
Vitendo vilivyotokea hivi karibuni katika kijiji cha Ilolangulu, mkoani Tabora
vya binaadamu kutia vinyesi kwenye visima vya maji, ni uwendawazimu unaomtoa mtu
katika ubinaadamu.
Mbaya zaidi inadaiwa waliyofanya, eti walifanya hivyo kwa sababu za kisiasa.
Sababu yao ni kuwa wao ni wafuasi wa chama cha CUF na wanaotumia visima hivyo ni
wafuasi wa Chama cha Mapinduzi!
Ni unyama gani huo? Binaadamu aliyepewa heshima na sifa zote na Mungu,
aliyekutukuza kwa kila hali na kuwa mtawala wa viumbe na vitu vyote humu duniani,
uutupe ubinaadamu wako na kutia vinyesi kwenye visima vya maji, vinavyotumiwa na
mamia ya binaadamu wenzako!
Cha ajabu wanaotenda vitendo hivyo, hivi sasa wamo katika harakati za
kuwashawishi Watanzania wawachague na kuwapa uongozi wa kata, majimbo na nchi ya
Tanzania!
Ni Mtanzania gani baada ya wafuasi wa chama hicho kufanya ujinga na unyama huo,
watakaokipa chama chao kura eti wawaongoze?
Chama hicho kimeshajidhihirisha kuwa hakifai kupewa uongozi, siyo wa nchi tu,
bali hata wa kijiji. Waswahili husema anayekumurika mchana, usiku atakuchoma.
Chama hicho kimeshaonyesha wazi kuwa kinawamurika mchana Watanzania kwa
kuwafanyia visa na vitimbi vya kuwawekea kinyeshi kwenye visima. Kikipata
madaraka wafuasi wake wanaweza hata kuweka sumu kwenye visima vya maeneo ambayo
watakuwa hawaungwi mkono.
Vitendo vyao vinathibitisha kuwa hawafai kupewa madaraka.
Kwa nini uchaguzi wa Zanzibar ulikodolewa sana macho na wakubwa
Ulitegemewa kufuta kashfa
Ni matumaini ya matajiri wa kiarabu
WACHAMBUZI wetu wa masuala ya uchaguzi wanaendelea kutuelimisha kuhusiana na
matukio na mambo mbali mbali yaliyojitokeza katika uchaguzi mkuu wa Zanzibar na
uchambuzi kuhusiana na hali hiyo vyanzo na malengo yake, kama inavyoeleza makala
hii ya pili ya mfululizo huo.
MWANAFALSAFA mmoja aliwahi kuelezea juu ya mabadiliko ya kisiasa na udhibiti wa
biashara na uchumi chini ya mfumo wa utandawazi wa utawala wa upande mmoja au
demokrasia ya mfumo mpya . Alieleza kuwa mabadiliko haya yametoa udhibiti kwa
mataifa ya Magharibi tokea kumalizwa kwa vita baridi na kusambaratika kwa Taifa
kubwa la Kisovieti.
Nilipoisoma makala ile kwanza nilikumbuka yaliyotokea mwaka 1964
Januari 12 pale ilipotoka kauli ya kuungwa mkono na Mataifa ya Mashariki
Mapinduzi ya Zanzibar.
Mataifa hayo yaliongozwa na Urusi, Uchina, Ujerumani Mashariki na Cuba. Urusi
ilitoa onyo kali kwa Taifa lolote litakaloingilia Mapinduzi halali ya Wananchi wa
Zanzibar. Na kila mtu aliufyata. Mapinduzi baridi yaliyotaka kuletwa na wajanja
yalizimwa.
Na sasa inanikumbusha kuwepo nguvu za upande wa Magharibi zinazotawala kila kitu
kutoka siasa, hadi uchumi. Na ninakumbuka usemi wa baadhi ya viongozi na wafuasi
wa Chama cha CUF pale walipokuwa wakijipongeza na kushangilia ushindi kabla kura
katika vituo vya uchaguzi hazijamalizwa kuhesabiwa. Walituambia hata CCM
ikishinda ushindi itapewa CUF kwa nguvu za Umoja wa Mataifa.
Wachunguzi wa mambo ya kisiasa tulishindwa kuamini kauli hiyo isiyofuata nadharia
za demokrasia na utawala bora. Hadi hapo tulipoanza kuulizwa masuala ya kuwepo
Serikali ya kitaifa, na Mashirika yasiyokuwa ya kiserikali (yaani NGO) kumiminiwa
fedha kedekede za kuendesha mafunzo ya urai , tulianza kubashiri mbinu, ujanja na
mikakati inaundwa na Mataifa ya Magharibi yakiongozwa na Marekani ya kuipa CUF
madaraka ya kutawala pole pole iwapo itashindwa katika uchaguzi. Dhana ya kuwepo
serikali ya pamoja ndivyo inavyoendelezwa.
Kwa CUF kutegemea nundu, walinyamaza kimya tokea kumalizika uchaguzi kwa
kisingizio cha kusubiri mkutano wa Baraza kuu. Kumbe kulichokuwa kikisubiriwa ni
kauli ya Marekani ya kutotambua matokeo ya uchaguzi iliyotolewa katika mkesha wa
Novemba 3, 2005. Kauli hiyo nayo ikaungwa mkono na Serikali ya Norway ambayo kwa
jeuri kubwa inaitaka SMZ/Tume ya Uchaguzi kurudia uchunguzi wa madai ya CUF ya
kasoro za uchaguzi na kuyaweka hadharani matokeo ya uchaguzi.
MASWALI
Hapa wachunguzi wa kisiasa tunaanza kujiuliza Norway wamepata wapi madaraka ya
kuihoji Tume au SMZ juu ya matokeo ya uchaguzi yaliyoungwa mkono na Taasisi na
mashirika kadhaa? Norway imebainika kuiunga mkono kauli ya uchochezi ya Marekani
ya kuyakataa matokeo halali ya uchaguzi yaliyotolewa na Tume huru wakati historia
bado inatukumbusha yaliyotokea Florida, Marekani katika uchaguzi wa Rais mwaka
2000 ambapo Tume ya uchaguzi ya Marekani ilifyata mkia. Na Rais Bush akatangazwa
Urais wake na Mahakama Kuu ya Florida. Haya ni maajabu na kweli.
Hoja gani inataka kujengwa hapa? Kuleta vurugu nchini na itakapodhibitiwa
serikali ilaumiwe kutumia nguvu kubwa kwa vikosi vya ulinzi. Vurugu zizagae ili
nchi isitawalike na hatimae utawala wa nguvu mpya uchukue mkondo wake wa
kumlazimisha Rais wa Zanzibar aunde Serikali ya kitaifa. Hiyo ndiyo misingi ya
ukoloni mambo leo unaosaidiwa na hoja mpya inayoitwa "Industrial imperialism".
Turudi katika ukweli wa kutafuta mbinu za kufuta kashfa iliyowakuta Waingereza
mwaka 1963-64. Waingereza kwa kebehi, dhuluma na jeuri walitoa uhuru wa Zanzibar
kwa walowezi wenzao kupitia vyama vya Hizbu na ZPPP. Vyama hivyo kwa pamoja
vilipata aislimia 45.4 ya kura zilizopigwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1963, wa
kutafuta uhuru wa Zanzibar, Chama cha ASP cha wanyonge, wakwezi na wakulima
kilipata kura nyingi zaidi - asilimia 54.6. Waingereza waliona demokrasia sahihi
ni ile ya kuwapa wachache, makabaila, madaraka ya kuitawala nchi ya Zanzibar,
chini ya mamlaka ya Sultan Jemshid Bin Abdulla, Bin Khalifa Bin Haroub ... Huu ni
ukoo mrefu wa Ma-Busaidi kutoka Oman, wavamizi wa nchi hii katika karne ya17.
Hatua hiyo iliwanyima haki wanyonge walio wengi, waliochoka kutawaliwa,
kubaguliwa, kunyanyaswa na ambao walikuwa watumwa katika nchi yao.
Wanaume hao wenye nguvu za umma kwa asilimia 54.6 dhidi ya nguvu hafifu za
makabaila na vibaraka vyao kwa asilimia 45.4 walisubiri Muingereza akabidhi nchi
aondoke ili wanaume wachukuwe nchi yao. Wanamapinduzi hao Wazanzibari halisi
"waliuwa tembo kwa ubuwa" wakaikomboa nchi yao, na hadi leo Wazanzibari hao
wanayaona mapinduzi yao ni ya kudumu na ndiyo maana yakawa "Mapinduzi Daima".
Kitendo cha wanaume kuiondoa madarakani Serikali ya Sultani na vibaraka wake kwa
kipindi cha mwezi mmoja tu, tokea Serikali hiyo iwepo madarakani ni kashfa na
aibu kubwa kwa Serikali ya Kiingereza. Na ndiyo maana inatafuta mbinu za kuifuta
kashfa hiyo.
Seif Sharif Hamad alikuwa (na bado anaendelea) mkereketwa mkubwa wa muungano wa
ZNP/ZPPP tokea awe mwanafunzi wa King George VI katika miaka ya 1960. Hivyo ni
muathirika mkubwa wa mapinduzi matukufu ya Zanzibar, ingawa ni mmoja
aliyesomeshwa na kupewa vyeo kadhaa hadi kufikia Waziri Kiongozi (1984 -88).
Kutumiwa muathirika wa mapinduzi kama Seif Sharif Hamad kuifuta kashfa ya
Muingereza sio ajabu hata kidogo. Lengo kuu ni kufuta historia ya Mapinduzi na
kuurejesha utawala wa Zanzibar kwa "mabwanyenye"chini ya nguvu za ukoloni mambo
leo. Historia kweli hujirudia, lakini penye haki sio penye batili.
UKOLONI MAMBOLEO
Mbinu za kurudisha nguvu za ukoloni mamboleo zilianza kupamba moto tokea pale
vilipomalizika vita baridi na kusambaratika kwa Taifa la Kirusi, kama
nilivyoeleza hapo awali. Sera mpya za utanuzi wa demokrasia kuheshimu haki za
binadamu, utawala bora na mbinu za kupunguza nguvu za utawala wa serikali
zikatawaliwa kwa kuanzisha taasisi zisizokuwa za kiserikali yaani (NGO). Hii ni
mikakati maalum iliyoandaliwa na Mataifa ya Magharibi ambayo yalipoteza makoloni
yao yaliyodai uhuru sasa katika miaka ya 1960, ikiwemo Zanzibar.
Makoloni hayo yaliyopata uhuru katika miaka ya 1960 ndiyo yaliyokuwa yakiimarisha
uchumi wa viwanda wa nchi za Magharibi kwa kutoa malighafi na nguvu kazi. Hivyo
kwa kupata uhuru wao ni kujitegemea kwa nguvu kazi zao na malighafi zao na
kuimarisha uchumi wa nchi za Magharibi.
Ndiyo maana sasa juhudi zinafanywa na nchi hizo kuirejesha hali hiyo kwa kupitia
mlango wa nyuma chini ya misingi ya utawala wa nguvu za upande mmoja. Katika
kutekeleza nguvu hizo juhudi zinafanywa za kuondoa madarakani uongozi wote
uliofanikisha ukombozi wa nchi zao, wanamapiduzi washupavu, na badala yake
kuuweka uongozi utakaoshinda maslahi yao.
Na kwa upande wa Zanzibar (na hata Zimbabwe) kuuondosha uongozi wa kimapinduzi na
badala yake kuweka uongozi utakaolinda sera za kikabaila, na kufuta kashfa
iliyowakuta watawala wawili, kwa mpigo, Muingereza na Sultani Jemshid na vibaraka
wake.
Kutokana na maelezo haya, wasomaji sasa watafahamu kwa nini uchaguzi wa Zanzibar
ukawa na mvuto mkubwa kwa Mataifa Makubwa, na hasa nchi marafiki za Magharibi
zikiongozwa na Marekani, Uingereza na nchi ya Norway.
Zanzibar ina historia ya ukombozi iliyojengeka kwa misingi imara sana. Haibomoki
mpaka ifutwe na historia ya Mapinduzi. Inaonekana wazi kuwa atakayeweza kuifuta
historia hiyo sio Karume, mwana Mapinduzi lakini Seif Sharif Hamad muathirika wa
Mapinduzi hayo.
Wakati Karume na watu wake wanasema "Mapinduzi Daima", Seif na wafuasi wake
wanasema "Mapinduzi Dhulma". Hizi ni tofauti mbili za msingi zinazosababisha CCM
kushinda Zanzibar. Kwani wanaoyaunga mkono Mapinduzi bado ni wengi na wataendelea
kukiunga mkono chama cha sasa kinachoheshimu mapinduzi na kuyalinda mapinduzi
hayo.
Itaendelea..
NGAWAIYA: Rais Mkapa amefanya mengi ya neema kwa Tanzania
Ni katika miundombinu, elimu na huduma za afya
KUTOKANA na mafanikio mengi yaliyofanywa na Serikali ya awamu ya tatu, aliyekuwa
Mbunge wa Moshi Vijijini (TLP) Thomas Ngawaiya ambaye sasa ni mwana-CCM, amekiri
kwamba Rais Benjamin Mkapa amefanya mengi mazuri kwa wananchi. Katika makala hii
Mwandishi GABRIEL JOHN anaelezea zaidi.
Thomas Ngawaiya anaeleza kushangazwa kwake na ‘kelele’ zinazopigwa na viongozi wa
vyama vya upinzani kwamba tangu Chama Cha Mapinduzi kishike hatamu za uongozi
uongozi kutoka vyama vya TANU na ASP, kasi ya maendeleo ya nchi yetu imesimama na
kwamba hakuna wananchi wanachofaidi zadi ya kuonezeka kwa shida na kero
mbalimbali.
Katika kupinga kauli hiyo, Ngawaiya anasema kwamba mafanikio mengi yamepatikana
baada ya CCM kushika dola tofauti na hali ilivyokuwa miaka iliyopita ambapo sasa
huduma nyingi za jamii zimepatikana na zilizokuwepo kuboreshwa.
Akieleza zaidi kuhusu mafanikio ya serikali hiyo, Ngawaiya anataja kuboreshwa kwa
utoaji wa elimu kuanzia ngazi ya awali hadi chuo kikuu. Anasema miaka mingi
Tanzania ilikuwa ikijivunia kuwa na chuo kikuu kimoja tu cha Dar es Salaam,
lakini sasa vipo vyuo zaidi ya 10.
Mbali na elimu, mbunge huyo wa zamani wa kambiya upinzania anasifu jitihada za
serikali ya Rais Mkapa katika kuboresha miundombinu, huduma za afya na maji ikiwa
ni sambamba na upatikanaji wa nishati ya umeme katika maeneo mengi ya Tanzania.
ELIMU
Ngawaiya anasema katika kuhakikisha kwamba elimu inakuwa bora na kwamba kila
mwenye sifa anafika hatua ya juu ya elimu hiyo, serikali imeweka mikakati ya
kuhakikisha kila mtoto mwenye sifa za kujiunga na elimu ya msingi anafanya hivyo.
Katika kusisitiza hilo, serikali ilipitisha sheria kali kwa wazazi ambao
watashindwa kuwaandikisha watoto wao wenye sifa za kujiunga na darasa la kwanza.
Hali hiyo imesaidia mno kuongeza idadi ya watoto hao hasa ikizingatiwa kwamba ada
na michango yote kwa kiwango hicho cha elimu imefutwa.
“Kuna mipango mingi kwenye sekta ya elimu ambayo yote ina lengo la kuiarisha
utoaji na upatikanaji wa elimu wa watoto wetu,” anasema.
Serikali ilibuni mpango mahsusi wa kuhakikisha kwamba elimu ya msingi inakuwa
boora kuanzia walimu, majengo na vifaa vya kufundishia, mpango ambao mafanikio
yake yanaonekana kuwa na faida kubwa. Mpango huo maarufu kwa jina la MMEM (Mpango
wa Maendeleo kwa Elimu ya Msingi).
Baada ya kuonekana mafanikio hayo kwa elimu ya msingi, serikali pia inaendelea
kuweka nguvu zake katika kuiboresha elimu ya sekondari kupitia mpango wake wa
MMES.
Katika mpango huu, serikali imedhamiria kuona kwamba kila kata inakuwa na shule,
walau moja ya sekondari ili kukidhi mahitaji ya upatikanaji wa kiwango hicho cha
elimu.
Mbali na jitihada hizo, serikali pia kwa kutambua kuwepo kwa idadi ya watoto
waliokosa elimu ya sekondari kutokana na sababu mbalimbali, ilibuni mpango wa
kuwapatia elimu vijana walioikosa wa MEMKWA.
Katika mpango huo, watoto hao wanapatiwa elimu kuanzia ya msingi na baadaye wenye
uwezo kuendelea na sekondari na hata elimu ya juu.
Akitoe mifano halisi juu ya mafanikio ya elimu, Ngawaiya anasema kwamba katika
jimbo la Moshi Vijijini, kata nyingi zimejengwa shule za sekondari na hiyo n
kuonyesha kwamba Ilani ya CCM ya Uchaguzi inatekelezeka.
Ngawaiya anasema kwamba kata ya Kibosho Mashariki, ina shule za sekondari zaidi
ya tano, miongoni mwa shule hizo ni Old Moshi, Kibosho Girls, Nsoo na Sungu.
Anazitaja shule nyingine kuwa ni Sahoni, Mbokomu, Meli Nane ambazo ni miongoni
mwa shule zilijengwa katika kipindi cha awamu ya tatu ya uongozi.
BARABARA
Ngawaiya anasema serikali ya awamu ya tatu imejenga barabara nyingi kwa kiwango
cha lami na zingine kuwekwa changarawe ili kuzifanya kupitika kwa mwaka mzima,
bila kujali mabadiliko ya hali ya hewa.
Anasema miongoni mwa barabara zilizowekwa ‘mkeka’ na kuondoa kabisa mashimo
kwenye barabra hizo ni barabara toka Rombo hadi Takeya (Kenya) ambapo awali
zilikuwa hazifai kutokana na kuharibika mara kwa mara, huku ziishindwa kabisa
kupitika wakati wa masika.
Barabara nyingine ni Oriri kuelekea Dar es Salaam ambazo zimewekwa lami jambo
ambalo hurahisisha mawasiliano katika kusafirisha bidhaa na abiria baina ya Kenya
na Tanzania.
Pia anasema kwamba si barabara hizo tu zinazounganisha Tanzania na Kenya, bali
barabara za mikoani zimeboreshwa na zinajengwa katika kuhakikisha kuwa
mawasiliano yanakuwa rahisi kutoka eneo moja hadi jingine.
Ngawaiya anasema kwamba yote hayo ni maendeleo makubwa yanayofanywa na Serikali
ambayo inamaliza muda wake baadaye mwaka huu.
HUDUMA YA AFYA
Serikali ya awamu ya tatu imewajibika ipasavyo katika kuhakikisha kuwa huduma za
afya zinakuwa bora zaidi na kwamba zinapatikana jirani zaidi na makazi ya
wananchi.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, zahanati nyingi zimejengwa, dawa
zinapatikana huku wataalamu wa afya wakiongezeka katika zahanati, vituo vya afya
na hospitali.
Ngawaiya anasema kwamba kutokana na hali hiyo, anaamini kwamba vifo vingi
vimepungua ikilinganishwa na wakati ambapo hapakuwa na huduma za afya jirani
zaidi na makazi ya watu, hasa wa vijijini.
“Nina amini kwamba idadi ya akinamama wajawazito ambao walikuwa wakipoteza maisha
kutokana na umbali wa vituo vya afya, sasa imepungua kwa kiasi kikubwa,”
anaongeza mbunge huyo wa zamani.
Mbali na kuwa baadhi ya maeneo bado yana umbali mkubwa kufia hospitali kubwa,
lakini kuimarishwa kwa miundombinu, limekuwa jambo jingine lenye faida kubwa
kwani wagonjwa wanaweza kusaidiwa kufika mapema kunakopatikana huduma hizo za
afya.
USHINDI KWA CCM
Ngawaiya anasema kuwa baada ya kupokea matokeo ya ushindi wa ‘Tsunami’ kwa CCM
Zanzibar, ushindi kwa upande wa Tanzania Bara utakuwa wa kishindo zaidi na kwamba
vyama vya upinzani havitaambulia matarajio yao.
Anasema ushindi wa CCM Zanzibar ni ishara ya mvua ya kubwa ya masika
inayotarajiwa bada ya wananchi uwa wamepiga kura Desemba 14, mwaka huu.
“Kutokana na ushindi huo wa Zanzibar, niliamua kufanya tambiko kwa kuchinja mbuzi
ikiwa ni ishara ya kuondoa mikosi niliyokumbana nayo nilipokuwa TLP kwa kipindi
cha zaidi ya miaka kumi…
Nina imani kwamba sasa yote yaliyokuwa yakijitokeza kuishambulia CCM na maendeleo
yake kwa wananchi yamefutika, nimekuwa mtu mpya kabisa,” anaongeza.
WAPINZANI
Ngawaiya anasema kwamba kwa sasa vyama vya upinzani havina nguvu na vinavurugwa
zaidi na chama cha CUF kwa kuendelea kutomtambua Rais Amani Abeid Karume ambaye
alipata ridhaa ya wananchi kuongoza kwa kipindi kingine cha miaka mitano.
Anasema ni jambo la kushangaza kwa CUF kuendelea kudai kuwa uchaguzi haukuwa wa
huru huku watu wengi wa ndani na nje walioshuhudia uchaguzi huo wakieleza kuwa
huru na kwamba ulifuata misingi yote ya kidemokrasia.
Hivyo, anawataka viongozi wa CUF na wote wasiokubalina na matokeo hayo, kuacha
kuchochea vurugu Zanzibar.
MATARAJIO
Anasema kwamba kukosa ubunge siyo mwisho wa kushirikiana na wananchi wa Moshi
Vijijini kuleta maendeleo.
Ngawaiya anaeleza kuwa ataendelea kushirikiana na wananchi wa jimbo hilo
kuhakikisha kwamba maendeleo yanaendelea kuimarishwa kwa kuwa anatarajia CCM
kushinda katika jimbo hilo.
Mbunge huyo wa zamani anabainisha kwamba kurejea CCM siyo jambo la kushangaza,
kwani kabla ya vyama vingi alikuwa mwanachama na kiongozi ndani ya Chama na
kwamba amerejea tu nyumbani baada ya kutangatanga pembeni.
“Kama madaraka nimekaa ndani ya CCM tangu mwaka 1977 nikiwa Mwenyekiti wa
Serikali ya Mtaa Mlangede, Iringa kabla ya kuingia kwa mfumo wa vyama, anasema
Ngawaiya.
Ngawaiya anasema kuwa CCM haina mpinzani katika uchaguzi ujao, kwa kuwa itaibuka
na ushindi utakaowahakikishia wapinzani kwamba hawana chao.
Amewataka wananchi kuhakikisha kwamba kadi zao za kupiga kura wanazitunza hadi
siku ya upigaji kura wa rais, wabunge na madiwani ili wasipoteze haki yao ya
kupiga kura na kuhakikisha maendeleo ya Tanzania.