UHURU 16.11.2005

 

Karume atangaza baraza la mawaziri

  • Lina mawaziri 13, wakiwemo wawili wapya

Na Mwandishi Wetu

RAIS wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, ametangaza baraza lake jipya la mawaziri,

lenye mawaziri 13, wakiwemo wawili wapya ambao wanashika nafasi za uwaziri kwa

mara ya kwanza.

Katika Baraza hilo mmoja amepandishwa kuwa waziri kamili baada ya kushika wadhifa

wa Naibu Waziri katika Baraza lililopita na mawaziri wawili wamerudi tena, baada

ya kuwa nje kwa muda.

Mawaziri wapya kabisa ni Asha Abdalla Juma, ambaye anakuwa Waziri wa Maendeleo ya

Vijana, Wanawake na Watoto, na Zainab Omar Mohammed, anayekuwa Waziri wa Nchi

Ofisi ya Rais (Kazi Maalum).

Aliyepandishwa ni Sultan Mohammed Mugheiry, aliyekuwa Naibu Waziri wa Afya katika

Baraza lililopita, ambaye anakuwa waziri mpya wa wizara hiyo, ambayo sasa inaitwa

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Zanzibar jana na gazeti hili kupata nakala yake,

ilionyesha kuwa mawaziri waliyorejea katika Baraza hilo la mawaziri, ambao

waliwahi kuwa mawaziri huko nyuma, ni Ramadhan Abdalla Shaaban na Amina Salum

Ali.

Ramadhan aliwahi kuwa Waziri wa Habari, Utangazaji, Utamaduni na Televisheni na

Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais, wakati Amina Salum Ali, alikuwa

Waziri wa Fedha katika serikali ya awamu ya tano ya Dk. Salmin Amour.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Baraza la Mawaziri la sasa lina wizara 13, likiwa

limelizidi lililopita kwa wizara moja. Lilikuwa na wizara 12. Pia, imeonyesha

kuwa mawaziri watatu wa zamani wameachwa.

Waliyoachwa ni Mussa Ame Silima, aliyekuwa Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko,

Mohammed Aboud, aliyekuwa Waziri wa Kilimo na Mifugo na Salum Juma Othman,

aliyekuwa Waziri wa Afya na Utibabu.

Mawaziri saba wameendelea kushika nafasi hizo kutoka katika Baraza la Mawaziri

liliopita, ingawa baadhi wamebadilishwa wizara.

Mawaziri hao ni Ali Juma Shamuhuna, Suleiman Othman Nyanga, Mansoor Yussuf Himid,

Dk. Mwinyihaji Makame Mwadini, Burhan Saadat Haji, Samia Suluhu Hassan na Haroun

Ali Suleiman.

Baraza kamili la mawaziri lililotangazwa jana na wizara zao katika mabano ni Ali

Juma Shamuhuna (Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo);

Amina Salum Ali (Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi); Dk. Mwinyihaji Makame

Mwadini (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,

anayeshughulikia Fedha na Uchumi).

Zainab Omar Mohammed (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi Maalum); Haroun Ali

Suleiman (Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali); Sultan Mohammed Mugheiry (Waziri

wa Afya na Ustawi wa Jamii); Burhan Saadat Haji (Waziri wa Kilimo, Mifugo na

Mazingira).

Mawaziri wengine ni Brigedia Jenerali mstaafu Adam Mwakanjuki (Waziri wa

Mawasiliano na Uchukuzi); Suleiman Othman Nyanga (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,

Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ); Mansour Yussuf Himid (Waziri wa Maji, Ujenzi,

Nishati na Ardhi).

Wengine ni Ramadhan Abdalla Shaaban (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Katiba na

Utawala Bora); Samia Suluhu Hassan (Waziri wa Utalii, Biashara na Uwekezaji) na

Asha Abdalla Juma (Waziri wa Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto).

Uteuzi huo ulianza jana.

 

 

‘Wanafunzi walioanguka kwa kunywa dawa walikuwa na njaa kali’

Na El-hadji Yuusuf, Tabora

WANAFUNZI wapatao 30 walianguka na kupoteza fahamu baada ya kupewa dawa za

kichocho na minyoo kwa sababu walizidiwa nguvu kutokana na kupewa dawa hizo bila

kula.

Juzi wanafunzi wa shule mbalimbali za mjini hapa walipoteza fahamu, mara baada ya

kupatiwa dawa za kutibu minyoo na kichocho. Walizidiwa nguvu na dawa hizo

kutokana na kupatiwa dawa hizo bila ya kula chakula.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Dk. Amos Nsheha, alisema kuwa kwa mujibu wa

Mwongozo kuhusu utoaji wa dawa hizo, hazikupaswa kutolewa kwa watoto bila ya

kupatiwa lishe ya kutosha kwanza.

Dawa zilizotolewa kwa wanafunzi hao ni aina ya Mebendazole kwa ajili ya kutibu

minyoo na Praziquentel ambayo hutibu kichocho, na kwamba inaelezwa kuwa na nguvu

nyingi na ambayo inaweza kusababisha madhara iwapo mtumiaji wake atakuwa hajapata

chakula na kushiba.

Alisema kuwa katika shule ambazo zoezi hilo liliendeshwa kwa kufuata kanuni hizo

hakukuwa na athari kubwa zilizotokea, katika kampeni maalum ya kuutokomeza

ugonjwa wa kichocho na minyoo hapa nchini.

Akiongea na waandishi wa habari, mara baada ya kumalizika kwa kikao cha dharura,

kilichoitishwa hospitalini hapo kwa ajili ya kutathmini hali iliyokuwa, Dk.

Nsheha, aliyekuwa sambamba na Mganga Mkuu wa Manispaa ya Tabora, Dk. Madaraka

Luganga, alisema kuwa watoto waliolazwa kutokana na tatizo hilo wanaendelea

vizuri.

Alisema kuwa mpango huo uliendeshwa katika mazingira ya tiba ya ugonjwa huo kwa

watoto wengi ili kuweza kupunguza madhara ya minyoo kati ya aina tatu kwa watoto

na kutibu ugonjwa wa kichocho ambao una madhara makubwa kwa binadamu.

Hata hivyo, alikiri kuwepo kwa mkanganyiko kuhusu namna ya kuwapa dawa watoto

hao, kwa sababu njia kuu iliyotumika ni ile ya kuwapa dawa baada ya kupimwa

urefu, badala ya kuzingatia uzito halisi kwa watoto.

Alisema kuwa shule nyingi zilizotekeleza tiba hiyo, hazikuwa na mizani kitu

ambacho alisema kuwa wengi wao waliamua kuwapa tiba kwa kuzingatia urefu tu.

Dk. Nsheha, alisema kuwa dawa hizo hazina madhara kabisa kwa watoto iwapo

wangepatiwa baada ya kupata chakula na kushiba, na kwamba watoto waliopatiwa dawa

hizo baada ya kula hawakuwa na athari zozote.

Alisema kuwa kati ya shule 20 zilizoendesha mpango huo juzi, katika manispaa ya

Tabora, ni wanafunzi wa shule nane ndio waliopata madhara hayo na hiyo inaashiria

kuwa kulikuwa na uzembe uliofanywa na baadhi ya walimu.

Akijibu swali ni kwanini dawa hizo zilitolewa na walimu badala ya watumishi wa

Idara ya Afya, alisema kuwa hilo lilitokana na Mwongozo wa Serikali wa mwaka 2002

na kwamba lilifanyika kutokana na manispaa kuwa na watumishi wachache wa idara

hiyo.

Dk. Nsheha, hata hivyo, alisema kuwa watoto wenye magonjwa sugu, kama ukimwi,

kansa, ‘sickle cells’, kifua kikuu na mengineyo, hawakupatiwa dawa hizo, kutokana

na Mwongozo kuzuia wasipatiwe ili kuepusha madhara kwao.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Alhaji Mussa Samizi, alisema dawa hizo hazina

madhara yeyote, kama inavyovumishwa na watu mitaani, lakini alikiri kuwa madhara

yaliyotokeza yalitokana na uzembe wa dhahiri.

Alisema kuwa walimu waliobainika kufanya uzembe huo watachukuliwa hatua za

kinidhamu, kwa sababu hawakutakiwa kuwapa watoto dawa hizo bila ya kuwapa chakula

kwanza, kama Mwongozo unavyosema.

Aliwataka wazazi na walezi wa watoto wanaosoma katika shule za msingi nchini,

wasihofu kutokana na zoezi hilo, kwa sababu halina madhara na kuomba ushirikiano

wao ili kutokomeza magonjwa ya kichocho na minyoo kwa vijana ili kuwafanya wawe

na afya bora.

Kwa upande wake, Dk. Luganga, alisema kuwa dawa hizo ni za kutibu minyoo na

kichocho na siyo chanjo kama ilivyoelezwa mitaani na baadhi ya watoto waliopatiwa

dawa hizo pamoja na wazazi na walezi wao na kuripotiwa na vyombo vya habari.

Wizara ya Afya kwa upande wake, hadi jana jioni ilikuwa ikisubiri taarifa rasmi

kutoka Tabora.

Ofisa Mawasiliano wa Wizara hiyo, Nsacris Mwamwaja alisema jana kwamba Wizara ya

Afya iliposikia kupitia magazeti iliwasiliana na Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa

Tabora ili kupata taarifa zaidi na kwamba hadi jioni ilikuwa bado haijafika.

Mwamwaja alisema kwa kawaida vidonge vinavyotolewa ni salama na kwamba vipo

kwenye mpango maalum wa kupambana na magonjwa na ulizinduliwa na Waziri Mkuu

Frederick Sumaye mjini Dodoma.

 

Wataoipigia kura CUF hawaijui tabia yake - Mangula

  • Mtanzania mpenda amani kamwe hatothubutu

Na Bashir Nkoromo, Mbeya

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Philip Mangula amesema watakaoipigia kura CUF

ni wale ambao hawakijui chama hicho na tabia zake.

Mangula alisema hayo juzi wakati akihutubia mkutano wa kampeni kwa ajili ya

mgombea ubunge wa jimbo la Mbarali, Estheria Kilasi, uliofanyika katika Kata ya

Madibira mkoani hapa.

Alisema kwa Mtanzania mpenda amani anayeijua CUF na kuzifahamu fika tabia za

chama hicho, kamwe hatathubutu kupigia kura mgombea wake yeyote katika uchaguzi

utakaofanyika Desemba 14, mwaka huu.

Mangula alisema CUF ni chama kilichobobea katika kujenga uhasama, ugomvi na

hamasa za vita na umwagaji damu.

Alitoa mifano kadhaa kwamba, wafuasi wa CUF waliwahi kuchinja hadi kumuua afisa

wa polisi huko Pemba, pia wamewahi kuua kwa kumchomea katika nyumba mwanamke

mkereketwa wa CCM na watoto wanne mjini Dar es Salaam.

Mangula alisema wafuasi wa CUF wamekuwa wakifanya maandamano haramu Dar es Salaam

na kusababisha maduka kuporwa na pia tukio la hivi karibuni la waandishi wa

habari kushambuliwa na kuharibiwa vifaa vya kazi kwenye makao makuu ya CUF,

Buguruni.

Aliwataka wananchi wa Mbarali na Watanzania kwa jumla kuipigia kura CCM kwa

sababu ndicho Chama chenye tabia makini na ujenzi wa amani na utulivu tangu nchi

kupata uhuru.

Mangula alisema kutokana na umakini wake CCM imeweza kuweka mazingira bora ya

wananchi kujiletea maendeleo ambapo sasa yanaonekana kila kona ya Tanzania.

“Kazi ya serikali si kuleta maendeleo. Maendeleo yanaletwa na wananchi huku kazi

ya serikali ikiwa ni kuwajengea mazingira bora ya kufanya hivyo,” alisema

Mangula.

Alisema miongoni mwa mazingira bora ni pamoja na hali ya utulivu na amani ambavyo

vinawawezesha Watanzania kufanya shughuli zao bila wasiwasi na kukumbusha kuwa

mahali penye vurugu na vita hakuna maendeleo yanayoweza kupatikana.

Mangula alisema mazingira mengine ni uboreshaji wa miundombinu kama vile

barabara, mawasiliano ya simu na huduma nyingine za kijamii.

Mapema kabla ya mkutano huo, Mangula alizungumza na kamati ya wilaya ya Mbarali

ambapo ilimweleza kuwa ina matumaini makubwa ya kupata ushindi katika uchaguzi wa

Desemba 14.

Baadaye alikwenda kata ya Chimala ambako alihutubia mkutano wa ndani na kumpokea

muasisi wa TLP na Katibu Kata wa chama hicho Kata ya Chimala, Isaya Mwakihwaya

ambaye alirejea CCM na mkewe na wanachama wengine zaidi ya 20.

 

 

Maofisa Uhusiano Mamlaka za maji watakiwa wawe kiungo

Na Mwandishi Wetu

MAOFISA Uhusiano wa Mamlaka za Majisafi na Majitaka nchini wametakiwa kuwa kiungo

kati ya mamlaka na umma katika kuhakikisha malengo ya mamlaka hizo yanafikiwa

ikiwa ni pamoja na kuyatangaza kwa wadau wengine.

Wito huo ulitolewa jana na Waziri wa Maji na Maendeleo ya Mifugo, Edward Lowassa,

katika hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa nne na uzinduzi wa Umoja wa

Waelimishaji na Uhamasishaji Umma Sekta ya Maji (WEMMA).

WEMMA unaundwa na maofisa uhusiano wa mamlaka za Majisafi na Majitaka nchini.

Uzinduzi huo ulifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Millenium Tower mjini Dar es

Salaam na kuhudhuriwa na maofisa kadhaa wa mamlaka hizo.

Waziri Lowassa alisema hilo linatokana na ukweli kwamba kupitia maofisa hao,

mamlaka hizo zimeweza kuwasogeza karibu wadau mbalimbali wakiwemo wateja.

Alisema hilo lilikwenda sambamba na kuongeza mwitikio wa wateja kwa mamlaka za

maji ikiwa ni pamoja na kuwahamasisha kulipia ankara za maji na kuwashirikisha

katika upanuzi wa huduma za majisafi na majitaka.

Waziri Lowassa aliyataja mafanikio mengine ya sekta ya maji kuwa ni ongezeko la

makusanyo ya mapato ya Mamlaka za Maji Mijini kutoka sh. milioni 400 mwaka 1995

hadi sh. bilioni 17.9 kufikia mwaka jana.

Alisema ongezeko hilo kwa kiwango kikubwa limeziwezesha mamlaka hizo kujiendesha

kwa sehemu kubwa.

Pia alisema hadi kufikia Juni mwaka huu, kamati za maji 9,283 ziliundwa katika

vijiji na kati hizo kamati 8,099 zilikuwa zimeanzisha mifuko ya maji yenye

thamani ya sh. bilioni 1.07.

Mapema akitoa maelezo ya WEMMA, Katibu wa umoja huo, Sebastian Warioba alisema

malengo ya uanzishaji wa WEMMA umelenga katika kuelimisha na kuhamasisha umma

kuhusu masuala yanayohusu usambazaji wa maji na uondoshaji wa majitaka katika

mazingira yaliyo safi, salama na endelevu.

Pia umelenga katika kujenga na kuendeleza mahusiano kati ya wadau wa sekta ya

maji ndani na nje ya nchi.

 

Mkenya akamatwa Arusha kwa wizi wa gari

Na Mohammed Mhina, wa Jeshi la Polisi – Arusha

MKENYA anashilikiwa na polisi mjini Arusha kwa tuhuma za kujihusisha na wizi wa

magari.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha James Kombe, alisema jana kuwa mtuhumiwa huyo

Paulo Osumba Kaserah (41) alikamatwa na Polisi akiwa na gari aina ya Toyota Hilux

iliyosajiliwa hapa nchini kwa namba TZS 3809 ambazo zilibainika kuwa zilikuwa za

bandia.

Alisema kuwa baada ya uchunguzi wa awali, Polisi ilibaini kuwa namba halali za

gari hiyo zilikuwa ni KAR. 948T iliyosajiliwa nchini Kenya ambazo pia zilikuwa

zimeandikwa katika vioo vyake na kubandikwa stika ili zisiweze kuonekana kwa

urahisi.

Kamanda Kombe alisema Polisi pia walimkuta mtuhumiwa akiwa na hati nne za

kusafiria zikiwa na majina tofauti na moja kati ya hizo ilikuwa imetolewa nchini

Tanzania na nyingine tatu zilitolewa nchini Kenya.

Alisema imebainika pia kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia hati mbili

zilizotolewa Kenya na zenye majina na picha tofauti kwa kusafiria katika nchi

mbali mbali.

Alisema katika hati nyingine mtuhumiwa Osumba, alikuwa akitumia jina la Rojers

Ochieng Okuta.

Alisema polisi kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji nchini Kenya na Tanzania,

inawasaka watu watatu wenye hati za kusafiria alizokutwanazo mtuhumiwa huyo.

Aliwataja watu wanaotafutwa kuwa ni Alan Zomboko Bongonya (31), mwenye pasi namba

AB 048106 iliyotolewa hapa nchini, Beatris Gaseri Muthamia (25), mwenye pasi

nambari A. 687034 na Rojers Ocheng Okuta (21), mwenye pasi nambari A. 808100 zote

zilizotolewa nchini Kenya katika vipindi tofauti.

Wakati huo huo Majeshi ya Polisi Tanzania na Rwanda yamekubaliana kudumisha

ushirikiano na uhusiano uliopo kwa nia ya kuimarisha ulinzi na usalama kwa nchi

za Maziwa Makuu.

Makubaliano hayo yamefikiwa na Wakuu wa majeshi hayo Inspakta Jenerali Omari

Mahita wa Tanzania na Kamishna Jenerali Andrew Rwigamba wa Rwanda, wakati wa

hafla fupi iliyofanyika jana usiku kwenye Bwalo la Polisi Oysterbay.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mahita alisema ushirikiano uliopo kwa nchi hizi

mbili utaziwezesha nchi hizi za Maziwa Makuu na ukanda wa Pembe ya Afrika kuweza

kudhibiti uhalifu wa Kimataifa kwa pamoja.

Kwa upande wake Kamishna Jenerali Rwigamba ambaye anaitembelea Tanzania kwa ziara

ya kikazi, amesema kuwa Rwanda itaendelea kujifunza mengi kutoka kwa Jeshi la

Polisi nchini Tanzania na kuhakikisha kuwa uhusiano na ushirikiano uliopo

unadumu.

 

Stashahada fani ya ustawi wa jamii kuanza kutolewa mwaka ujao

Na Mwandishi Wetu

TAASISI ya Ustawi wa jamii (ISW) itaanza kutoa shahada katika fani ya Ustawi wa

Jamii kuanzia mwaka kesho ikiwa ni moja ya jitihada za kuimarisha elimu ya jamii

nchini.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo Dk. Hosea Rwegoshora alisema hayo jana

alipozungumza na waandishi wa habari kuelezea maendeleo na mikakati mbalimbali ya

kuboresha taasisi yake pamoja na maandalizi ya mahafali ya 29 yanayotarajiwa

kufanyika Ijumaa ijayo.

Mgeni rasmi wakati wa mahafali atakuwa Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana na

Michezo Profesa Juma Kapuya na kwamba wahitimu 191 watapatiwa shahada za juu ,

shahada za kawaida na vyeti mbalimbali.

Dk.Rwegoshora alisema taasisi yake itaanza kutoa shahada ya ustawi mwaka

2006/2007 baada ya kukamilisha maandalizi ambayo yanasimamiwa na Baraza la

Mitihani la Taifa (NECTA).

“Tuliwaandikia NECTA nia yetu na mipango ya utekelezaji katika kuanzisha masomo

ya shahada, nayo NECTA ilipitia na kutoa ushauri wake wa mwisho ambao unafanyiwa

kazi ili kuanza kufundisha masomo ya shahada,’’ alisema.

Alisema taasisi yake itakuwa ya tatu nchini kutoa shahada maalum ambazo

zinatolewa na vyuo vya kati badala ya vyuo vikuu pekee.

Vyuo vingine ambavyo kwa sasa vinatoa shahada ni pamoja na Chuo cha Mipango

Dodoma na Chuo cha Ufundi Dar es Salaam.

Taasisi ya ustawi wa jamii ilianzishwa mwaka 1974 ikiwa na lengo la kufundisha

masuala ya ustawi wa jamii, lakini ilizidi kuongeza kozi kulingana na mahitaji

ambapo sasa zipo zaidi ya kozi saba za muda tofauti wa kusomea.

Dk. Rwegoshora alisema taasisi hiyo pamoja na kozi nyingi zinazohusu ustawi wa

jamii, kwa sasa inafundisha pia kozi juu ya masuala ya menejimenti ya rasilimali

watu ambayo pia inafundishwa kwenye Chuo Kikuu cha Mzumbe.

Alisema taasisi yake kwa sasa inao wanafunzi 900 ukilinganisha na wanafunzi 24

waliofungua chuo wakati kinaanza.

Wanafunzi 1,470 walimaliza masomo kwenye taasisi hiyo na walitunukiwa vyeti na

stashahada za fani mbalimbali. Waliotunukiwa stashahada za juu, kawaida na vyeti

ni pamoja na wanafunzi wa nje 91 kutoka Afrika Kuisni, Lesotho, Swaziland,

Burundi, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Gambia, Namibia na Sudan.

Wakati huohuo Chuo cha sayansi jamii cha Kivukoni (KASS) kinatarajia kuwa na

mahafali yake siku ya Novemba 26 mwaka huu ambapo wanafunzi 133 watatunukiwa

vyeti na stashahada katika fani ya jinsia, sayansi jamii, na maendeleo ya uchumi.

Taarifa iliyotolewa jana ilisema Rais Benjamin Mkapa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi

kwenye mahafali hayo na kwamba wahitimu saba watatunukiwa stashahada katika fani

ya uchumi wakati wengine 60 watapata stashahada za sayansi jamii na wengine 37

watatunukiwa stashahada za jinsia wakati wahitimu 29 watapatiwa vyeti vya fani ya

kazi za vijana.

 

Wengine wanne Wajitoa CHADEMA Moshi Vijijini

Na Rodrick Makundi,Moshi

KAMBI ya upinzani katika jimbo la uchaguzi la Moshi Vijijini imeendelea kupata

pigo baada ya wanachama wanne wa Chadema kujitoa kwenye chama hicho na kujiunga

na Chama Cha Mapinduzi.

Wanachama waliohama Chadema na kurejea CCM ni Mwenyekiti wa kitongoji cha Kifumbu

kata ya Uru Kusini na Mwenyekiti wa kitongoji cha Okaseni chini, Anthony Komu.

Aidha viongozi wa Chadema kata ya Mabogini wamerejea CCM ambapo walikabidhi kadi

za chama chao walichotoka kwa Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Moshi vijijini.

Viongozi waliorejesha fomu kutoka katika kata hiyo ni pamoja na Mwenyekiti wa

Chadema,Laurence Mbwambo,katibu wake Ally Mchomvu na katibu msaidizi Sadick

Lukware ambao walikuwa wahamasishaji wakubwa wa mgombea udiwani wa kata hiyo.

Wanachama hao kwa pamoja walirejesha kadi zao kwa Mwenyekiti wa CCM,wilaya ya

Moshi Vijijini ambaye aliwapokea na kuwakaribisha kuwa wanachama wapya wa CCM.

Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Moshi vijijini Gabriel Masenga mara baada ya

kuwapokea wanachama hao aliwataka kushirikiana kwa pamoja kwa kuwahamasisha

wanachama wengine kuendelea kujiunga na CCM ili kuharakisha utekelezaji wa ahadi

za chama.

Wakizungumzia azma yao ya kujiunga CCM,wanachama wa Mabogini waliojiengua kutoka

Chadema,walisema uamuzi wao huo umetokana na sera madhubuti za Chama ambazo

zimeonekana kulenga kutekeleza ahadi zinazotolewa na wagombea wakati wa kampeni

za awali za chama hicho kwenye kata hiyo.

“Tunafanya hivyo kwa kuwa tunatambua kuwa malengo ya wagombea wa CCM,Mheshimiwa

Kikwete,kwa ngazi ya urais,Dk.Cyril Chami kwa ngazi ya ubunge na Rodgers Mmary

kwa ngazi ya udiwani kata ya Mabogini ni ya kuwaletea maendeleo wananchi wa

Tanzania,jimbo la Moshi Vijijini na hasa katika kata yetu ya Mabogini”alisema

sehemu ya taarifa hiyo.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Chadema kitongoji cha Kifumbu alisema dhamira yake

ya kurejea CCM,inatokana na kukosa ushirikiano baina yake na chama hivyo kukosa

matumaini ya kupata ushindi katika eneo lake na hata kwa jimbo.

Kwa upande wake mgombea wa CCM,ngazi ya ubunge jimboni humo Dk.Cyril Chami

aliwapongeza wanachama hao kujiunga CCM na akawataka kueneza sera za chama.

Aliongeza kuwa wanachama waliorejea CCM,wanatarajiwa kupewa mkono wa pongezi na

Waziri Mkuu,Frederick Sumaye ambaye pia ni mlezi wa chama mkoa wa Kilimanjaro

wakati wa ziara yake kesho (leo) katika majimbo ya Moshi Vijijini na Vunjo

wilayani humo.

Waziri Mkuu anatarajiwa kufanya ziara ya siku mbili mkoani hapa

Kilimanjaro,katika majimbo ya Moshi Vijijini ambako atamnadi mgombea ubunge wa

jimbo hilo Dk. Chami na katika jimbo la Vunjo, Sumaye atamnadi mgombea ubunge wa

CCM Aloyce Kimaro wa jimboni humo.

Pia aliyekuwa mgombea ubunge kupitia CUF,Steven Nguma ambaye alijitoa kugombea na

kujiunga na CCM,wagombea udiwani wa TLP na Chadema waliojitoa watakutana na

Sumaye kwa kukaribishwa rasmi katika Chama.

 

Mchanga wenye madini ya Almasi waibwa Mwadui

Kundi la watu zaidi ya 100 lahusika

KUNDI la watu zaidi ya 100 limevamia mgodi wa almasi wa Mwadui mkoani Shinyanga

na kuiba mchanga wenye almasi unaosadikiwa kuwa na thamani ya mabilioni ya fedha.

Akizungumza na PST ofisini kwake jana Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga Abdallah

Mssika alisema kundi hilo pia limemuua mlinzi wa Kampuni ya Ulinzi ya Grey

Security Guard inayolinda mgodi huo.

Hata hivyo, Kamanda Mssika alisema katika msako uliofanyika hakuna madini

yaliyokamatwa katika mchanga ulioibwa katika uvamizi huo.

Kuhusiana na tukio hilo alisema, polisi inawashikilia watu kadhaa kwa tuhuma za

kuhusika na uvamizi huo na msako kwa watu wengine bado unaendelea.

Majina ya watu waliokamatwa yamehifadhiwa kwa sababu za uchuguzi zaidi wa

kipolisi.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi kundi hilo la watu maarufu kwa jina la "wabeshi"

lilifanya uvamizi huo saa 12.30 jioni Alhamis iliyopita eneo la New Almasi namba

10 ndani ya mgodi wa Mwadui.

Kundi la watu hao huku wakiwa wamebeba, mapanga, marungu, makombeo na machekeche

ya mchanga wa almasi lilivamia eneo hilo kwa lengo la kuiba mchanga wenye almasi.

Mssika alisema, mlinzi aliyemtaja kuwa ni Aden Rage (29) akiwa doria alipoliona

kundi hilo la wavamizi likivuka eneo la uzio wa mgodi alipiga risasi moja hewani

kuwatishia kwa ili kuwatawanya lakini waliendelea kumfuata na kumkabili mlinzi

huyo.

Alisema Rage alipoona wanaendelea kumkabili alijaribu kufyatua tena risasi ya

pili ili kuwatanyawa lakini kwa bahati mbaya risasi hiyo ilikwama katika bunduki

yake aina ya shotgun.

Kiongozi huyo wa polisi alisema kitendo hicho kilitoa mwanya kwa kundi hilo

kumvamia na kuanza kumpiga na kumchoma na kitu chenye ncha kali kifuani upande wa

kulia na kusababisha kifo chake.

Wavamizi baada ya kumuua, alisema Mssika walivunja kitako cha bunduki yake na

kuitupa bunduki kando ya maiti na kisha kuanza kusomba mchanga unaosadikiwa kuwa

na thamani ya mabilioni ya shilingi uliokuwa katika mashine moja ya kusomba

mchanga.

Kamanda alisema wavamizi waliusomba mchanga uliokuwa katika mashine hiyo maarufu

kama kijiko" kilichokuwa kikiendeshwa na mfanyakazi wa

mgodi Aloyce Zengo (40) na kutoweka nao nje ya mgodi .

 

Serikali kuboresha maslahi ya watumishi wa umma

Na Mwandishi Maalum

SERIKALI imedhamiria kuboresha mishahara na maslahi ya watumishi wa umma kufikia

kiwango cha kuweza kujiwekea akiba kwa ajili ya maendeleo yao.

Hayo yalibainishwa na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi

wa Umma, George Yambesi, alipokuwa akifungua mafunzo ya namna ya kuandaa makisio

ya ikama na bajeti ya mishahara ya watumishi wa umma kwa maofisa utumishi wa

wizara, idara, wakala na halmashauri za miji na wilaya.

Yembesi katika mafunzo hayo yanayoendeshwa katika Chuo cha Ufundi Stadi -VETA,

mjini Morogoro alisema nia hiyo ya serikali, itaweza kutekelezeka endepo ukuaji

wa uchumi wa taifa utafikia kiwango cha juu katika kuchangia pato la taifa hivyo

kuwezesha serikali kulipa mishahara na maslahi bora zaidi kwa watumishi wa umma.

Alisema kwa kuzingatia hilo, ndio maana Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa

Umma, kupitia Programu ya Kuboresha Utumishi wa Umma, imeamua kuendesha mafunzo

hayo kwa watendaji wake ili kiasi kidogo kilichopo kiweze kutumika vizuri na

kutoa motisha kwa watumishi hivyo kuwajengea ari.

Yambesi alikiri kuwa tathmini ya hali halisi ilivyo hadi sasa imeonyesha bado

kuna baadhi ya matatizo katika utendaji wa shughuli za utumishi wa umma ikiwemo,

uwajibikaji usioridhisha katika kushughulikia maslahi ya watumishi wapya na

wanaopandishwa vyeo.

Naibu katibu mkuu huyo alisema kufuatia hali hiyo, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya

Utumishi wa Umma tayari imetoa maelekezo kwa watumishi wote wenye dhamana za

kushughulikia malipo ya mishahara kuhakikisha malipo yanafanyika bila

ucheleweshaji usio wa lazima.

Naye Naibu Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Misaada ya Kimaendeleo la Japan JICA

waliofadhili mafunzo hayo, Naoki Takahashi ameihakikishia Serikali ya Tanzania

kuendelea kufaidika na ufadhili wao katika programu mbalimbali za maendeleo

ikiwemo ya Kuboresha Utumishi wa Umma (PSRP).

Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Dk. Richard Kavura, alisema chuo

chake kimefikia kiwango cha juu katika utoaji wa mafunzo ya menejimenti na

utawala kwa kada ya kati na juu sio tu kwa watumishi wa umma, bali pia hata

taasisi binafsi.

Mafunzo hayo yatahusisha maofisa zaidi ya 400 yataendeshwa kwa awamu 4 za maofisa

100 kila awamu na yameandaliwa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

 

 

CCM Mwanza yapinga kutenguliwa wenyeviti wake

Na Eva Musiba, Mwanza

CHAMA Cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza kimesema kuwa kinapinga hukumu iliyotolewa na

Mahakama ya Hakimu Mkazi ya kutengua matokeo ya wenyeviti wake wawili wa mitaa

kata ya Mbugani Halmashauri ya jiji la Mwanza.

Katibu wa CCM mkoa wa Mwanza Mujuni Kataraia alisema kuwa chama chake

kinawasiliana na msimamizi wa uchaguzi jiji la Mwanza ili kiweze kupata ufafanuzi

kuhusiana na uamuzi huo wa mahakama.

Kataraia alisema chama hicho hakikubaliani maamuzi hayo kwa kuwa

hakikushirikishwa tangu mwanzo wa kesi na kinashangazwa kesi hiyo kuamuliwa

upande mmoja.

"Nimewasiliana na msimamizi wa uchaguzi ambaye pia ni mkurugenzi wa jiji la

Mwanza kupata ufafanuzi kuhusiana na suala hilo,naye amtueleza kuwa haelewi ni

kwa nini maamuzi hayo yalifanyika upande mmoja, ndio maana hatukubaliani na

maamuzi hayo na tunajiandaa kupigania haki yetu," alisema.

Mkurugenzi wa jiji la Mwanza Paul Baruti ambaye pia ni msimamizi wa uchaguzi

alisema kuwa ofisi yake inashangazwa na maamuzi ya mahakama ya kusikiliza kesi

hiyo upande mmoja pasipo kuishirikisha ofisi yake.

Baruti alisema ofisi yake haikuwahi kuitwa mahakamani wakati wa usikilizwaji wa

shauri hilo lililokuwa limefunguliwa na chama cha Civic United Front (CUF)

kupinga matokeo ya uchaguzi wa wenyeviti wa mitaa kata ya Mbugani.

"Baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo nilimuita mwanasheria wa jiji kumuulizia

kuhusiana na shauri hilo naye alinieleza kuwa ofisi yake haikuwahi kuitwa

mahakamani hivyo kutokana na utata huo tunafuatilia ili kuweza kuchukua hatua

zaidi," alisema msimamizi huyo wa uchaguzi.

Katika hukumu iliyotolewa, mahakam ilitengua uenyekiti wa mitaa ya Kreluu na

Serengeti kwa madai kuwa taratibu za uchaguzi zilikiukwa.

Kufuatia kutolewa kwa huku hiyo tayari msimamizi wa uchaguzi amewaandikia barua

wenyeviti wa mitaa hiyo Ezekiel Bahebe (Kreluu) na Brown Aunice (Serengeti)

kuacha kufanya shughuli za uenyekiti wa mtaa hadi pale uchaguzi utakapofanyika

tena.

 

TRA Kilimanjaro yasema haina lengo la kufilisi watu

Na Rodrick Makundi, Moshi

MAMLAKA ya Mapato (TRA) mkoa wa Kilimanjaro imesema haijalenga kufunga au

kufilisi biashara katika zoezi lake la kutoza kodi, badala yake imelenga kuwa ni

chombo cha kisasa cha ukusanyaji wa kodi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Katika mkutano kati ya TRA na wafanyabiashara wa mji wa Moshi, Meneja wa mamlaka

hiyo mkoa Patience Minga alisema wamedhamiria kujenga uhusiano mzuri na wafanya

biashara ili waondokane na kukwepa kodi bali watambue kuwa kulipa kodi ni wajibu

wao wa msingi.

Minga aliyasema hayo juzi katika moja ya semina ambazo zinaendeshwa na TRA,

kupitia idara yake ya elimu kwa walipa kodi ikiwa ni sehemu ya mkakati wa mamlaka

hiyo katika kuwaelimisha walipa kodi.

Alisema wafanyabaishara wakubwa na wadogo mkoani hapa hawana budi kuondoa fikra

potofu zinazokwamisha uhusiano mzuri kati ya mamlaka na wafanya biashara.

Aliwataka wafayabiashara hao kutokuwa na woga katika suala zima la ulipaji kodi

badala yake wawasiliane na ofisi yake ili kupata ufafanuzi juu ya taratibu sahihi

zinazomstahili mlipa kodi.

Alisema mamlaka hiyo pia imeanzisha utaratibu wa kuwa na visanduku kwa ajili ya

walipa kodi kutoa maoni yao juu ya huduma wanazopatiwa na mamlaka hiyo.

Minga alisema walipa kodi wasioridhika na huduma za TRA, ama kuridhishwa watakuwa

wanajaza maoni yao katika vikaratasi maalumu na kuviweka katika visanduku hivyo

kwa ajili ya kufanyiwa kazi na kwamba vitasambazwa katika vituo vyote vya TRA,

wilayani na mikoni.

Aliwataka wafayabishara kujenga uaminifu kwani kwa njia hiyo mamlaka hiyo

haitawaona kama maadui bali marafiki wema wanaostahili katika kuendeleza bishara

zao kwa manufaa ya Taifa.

 

Mwili wa askari aliyeuawa Pemba hatimaye wapatikana

  • Inadaiwa aliuawa na wafuasi wa CUF

Na Mwandishi Wetu

MWILI wa askari wa kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKU), Shariff Salum

aliyetekwa nyara na wananchi wa kijiji cha Piki Pemba umeokotwa ukiwa umefichwa

kwenye kichaka.

Kwa mujibu wa matangazo ya Idhaa ya Sauti ya Tanzania Zanzibar, mwili huo

uliokotwa jana kufuatia msako uliofanywa kwa ushirikiano kati ya JKU na polisi.

Salum aliuawa na watu wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa CUF baada ya kutekwa nyara

Novemba Mosi, mwaka huu, kufuatia vurugu zilizotokea Pemba, mara baada ya

uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 30.

Uchunguzi wa awali kutoka hospitali ya Wete ambako mwili wa marehemu ulipelekwa

umebainisha kuwa askari huyo aliuawa baada ya kupigwa na kitu kizito kichwani.

Mwili wa marehemu Salum ulikabidhiwa kwa familia yake ambayo wiki iliyopita

ilianua tanga baada ya kukata tamaa kufuatia kukwama kwa juhudi za kumtafuta.

Salum alikamatwa na wanakijiji hao baada ya kuziba barabara wakati akirejea

kambini katika kijiji cha Pujini, mkoa wa Kusini Pemba akitokea Utaani, Kaskazini

Pemba baada ya pikipiki aliyokuwa akiendesha kushindwa kuendelea na safari

kufuatia magogo yaliyokuwa yamewekwa barabarani.

Kutokana na kushindwa kuendelea na safari, Salum aliamua kubaki ili kulinda

pikipiki hiyo, lakini wanakijiji hao ambao walikuwa wameshikilia mapanga, magongo

na visu walimkamata na kumpakia kwenye mkokoteni hadi porini ambako inasadikiwa

walimpiga hadi kufa.

Askari mwenzake ambaye alikuwa amempakia kwenye pikipiki hiyo alifanikiwa

kutoroka na kutoa taarifa polisi kuhusu kutekwa kwake, lakini juhudi za kumpata

akiwa hai zilishindikana kwani katika msako huo polisi walifanikiwa kuukuta

mkokoteni uliotumika kumbeba ukiwa umetapakaa damu.

Hii ni mara ya pili kwa wananchi kisiwani Pemba kumwua askari, ambapo mwaka 2001,

askari mwingine Muslim Mussa alikufa kwa kupigwa panga kichwani katika maandamano

haramu ya CUF Januari 26, 2001

 

CCM yakana kuorodhesha shahada za wapigakura

  • Yasema huo ni woga na dalili za kushindwa kwa CHADEMA

Na Lilian Mamushu wa PST, Shinyanga

CHAMA cha Mapinduzi wilaya ya Shinyanga Mjini, kimesema wajumbe wake wa mashina

hawaorodheshi shahada za wapiga kura wilayani humo.

Chama cha Demokrasi na Maendeleo (CHADEMA), kimetoa shutuma hizo kikiwatuhumu

wajumbe hao wa CCM kwa kudai wamekuwa wakipita nyumba hadi nyumba wakiorodhesha

shahada hizo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, Katibu wa CCM wilaya, Kilumbe

Ngenda, alisema madai hayo ya CHADEMA ni uongo mtupu na hayana ukweli wowote.

Alisema chama chake hakina sababu zozote za kuwafanya wajumbe wake wa mashina

kupita nyumba hadi nyumba kuorodhesha shahada za wapiga kura.

Pia, alikanusha madai ya kuwashawishi wafuasi wa vyama vya upinzani kuuza shahada

zao kwa lengo la kupunguza kura za wagombea kutoka katika kambi hiyo ya upinzani.

Alisema jimbo la Shinyanga Mjini lina zaidi ya wapiga kura 70,000

walioandikishwa, ambapo CCM katika jimbo hilo ina wanachama 18,000 na kuhoji ni

kiasi gani cha fedha ambacho kitatumika kununua shahada hizo kutoka kwa

wapinzani.

Hata hivyo, alisema chama kwa upande wake kiliwaagiza wenyeviti wake wa mashina

kufanya kampeni za nyumba hadi nyumba kwa ajili ya kumtambulisha mgombea wao wa

ubunge, Dk. Charles Mlingwa, ambaye hafahamiki kwa wakazi wengi wa jimbo hilo.

"Mimi nafahamu kuwepo kwa zoezi la wenyeviti wetu wa mashina kupita nyumba hadi

nyumba kumtambulisha mgombea ubunge wetu ambaye kwa kweli hafahamiki vizuri na

wapiga kura, hiyo ndiyo kazi inayofanyika mitaani na si kuorodhesha shahada za

wapiga kura," alieleza Ngenda.

Kuhusu uzushi wa kununua shahada, alisema CCM haiwezi kufanya upuuzi huo na kama

kweli CHADEMA ina ushahidi, basi inapaswa kutoa taarifa polisi ili wahusika

wakamatwe na kufikishwa mahakamani.

Alisema malalamiko hayo ni dalili za kushindwa ambazo tayari CHADEMA imeshaziona,

hivyo inatafuta visingizio ambavyo havina msingi.

"Sisi hatuwezi kununua shahada za wapiga kura Tunanunua ili iweje? Tunao

wanachama wa kutosha na mtandao wa uongozi kuanzia chini ambao unatuwezesha

kupata ushindi bila shida. Labda wao CHADEMA ndiyo wanaonunua shahada, tunao

ushahidi, kwani mmoja wa viongozi wao alikamatwa hivi karibuni na shahada za

wapiga kura," alisema Ngenda.

Mapema wiki iliyopita, CHADEMA mjini hapa kiliandika barua kwa msimamizi wa

uchaguzi jimbo la Shinyanga Mjini, kikilalamikia ilichodai wajumbe wa mashina wa

CCM kupita nyumba hadi nyumba wakiorodhesha shahada za wapiga kura.

 

NLD Mara yaiomba serikali iifute CUF

  • Yadai imepoteza sifa za kuwa chama cha siasa

Na Joseph Manyonyi, Bunda

KATIBU wa chama cha NLD mkoani Mara, Ascetic Malagila, ameiomba serikali ikifute

chama cha CUF kwa sababu kimepoteza sifa ya kuwa chama cha siasa kwa kuvunja

amani ya Tanzania.

Malagila alisema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari nyumbani

kwake mtaa wa Nyasura mjini hapa.

Alisema viongozi na wanachama wa CUF wanataka kuiingiza Tanzania katika dimbwi la

damu, kutokana na vitendo viovu vya chama hicho vya kuwapiga waandishi wa habari,

maandamano ya mara kwa mara, fujo na jazba za kidini.

Malagila ambaye ni mwanasiasa machachari, alieleza kuwa vitendo vya CUF ni kama

bomu linaloweza kuiangamizi Tanzania ikiwa serikali haitakifuta chama hicho kwa

siasa za ubabe na chuki.

Akizungumzia uchaguzi wa Zanzibar uliomalizika hivi karibuni, alisema ulikuwa

huru na wa haki.

Amevitaka vyama vya siasa visiingizwe katika serikali ya mseto, kwani kufanya

hivyo ni kupata madaraka bila ridhaa ya wananchi.

Alipinga wazo la kuwepo kwa mazungumzo kati ya CCM na CUF, kwani ni kupoteza muda

na fedha za wananchi, ambazo zinatakiwa kuleta maendeleo hapa nchini.

Katika mkutano huo, Malagila alijitangaza kugombea uspika wa Bunge la Jamhuri ya

Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya NLD, na kueleza kuwa tayari amekwishapata

baraka za Kamati Kuu ya chama chake.

 

 

Wananchi wainyime kura CUF kutokana na sera za mabavu

Na Prosper Kulita, Morogoro

CHAMA cha Mapinduzi wilaya ya Morogoro, kimewataka wakazi wa mkoa huo

kutowachagua wagombea wa chama cha CUF kwa kuwa chama hicho hakil