UHURU 17.11.2005

 

BAADA YA UCHAGUZI MKUU KUAHIRISHWA:

  • Kitimtim cha kampeni za Urais kuanza J’mosi
  • Kikwete kuanza Jumanne wilayani Rufiji

Na Mwandishi Wetu

KITIMTIM cha kampeni za kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

kitaanza tena mwishoni mwa wiki hii ambapo mgombea mwenza wa Chama Cha Mapinduzi,

Dk. Ali Mohamed Sheni atakuwa Lushoto, Jumapili.

Mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete katika awamu hii ataanzia kampeni

zake wilayani Rufiji Jumanne ijayo.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), jana ilipitisha ratiba ya kampeni za uchaguzi za

wagombea Urais utakaofanyika Desemba 14, mwaka huu.

Mkuu wa Idara ya Elimu kwa Wapigakura wa Tume ya Uchaguzi, Eda Sanga, alisema

jana kuwa mgombea wa Urais wa CCM, Jakaya Kikwete kwa upande wake ataanza

mzunguko wa kampeni zake Jumanne ijayo wilayani Rufiji.

Ratiba hiyo ilipitishwa baada ya kikao cha vyama vyote vyenye wagombea Urais,

isipokuwa PPT-Maendeleo. Kampeni za wagombea Urais zitaanza Jumamosi kama

ilivyopangwa awali na vyama vya CUF na CCM pekee ndivyo havitakuwa na mkutano

wowote siku hiyo.

CCM inatarajia kuhitimisha kampeni zake Desemba 13, kwenye viwanja vya Jangwani,

wakati CUF itahitimisha kampeni zake kwenye uwanja huo huo, Desemba l2.

Eda alisema CUF, nayo itaanza kampeni zake Jumapili ijayo, ambapo mgombea Urais,

Profesa Ibrahim Lipumba atakuwa mjini Mwanza na Mgombea Mwenza, Juma Haji Duni,

atakuwa Morogoro Vijijini.

Ofisa wa CUF anayeshughulikia masuala ya uchaguzi, Maole Kuchilungilo, alisema

kuwa mkutano wa kampeni mjini Mwanza utarushwa moja kwa moja kupitia Radio Free

Africa na itarekodiwa na kurushwa usiku kupitia televisheni ya Star.

Kwa mujibu wa Kuchilungilo, mikutano kama hiyo huko Tabora, Mtwara na ule wa

kufunga kampeni wa Dar es Salaam nayo itaonyeshwa kwa utaratibu kama huo wa

Mwanza.

Ratiba ya kampeni ya vyama vingine ni DP itakayozindua awamu ya pili ya kampeni

jimboni Kilolo Jumamosi na kumalizia huko Chake Chake, Desemba 13. Katika siku za

karibuni mgombea Urais wa chama hicho, Mchungaji Christopher Mtikila alisema kuwa

chama chake kinawania kuiteka CUF, ngome yake ya Pemba.

Mgombea Urais wa TLP, Augustine Mrema na mgombea Mwenza wake, Rukia Kiota

wataanza Jumamosi katika majimbo ya Moshi Vijijini na Vunjo na watamalizia mkoani

Dar es Salaam siku ya mwisho wa kampeni.

Mgombea Urais wa Chadema, Freeman Mbowe atazindua awamu hiyo ya pili ya kampeni

Jumamosi huko Kinondoni na mgombea Mwenza atakuwa Visiwani Ukerewe. Kampeni hizo

zitahitimishwa kwa mgombea Urais kuwa jimboni Hai na Moshi Mjini, huku Mgombea

Mwenza, Anna Komu atakapokuwa mjini Kigoma.

Chama cha NCCR, kitaanza na mikutano ya wagombea wake, Dk. Sengondo Mvungi na

Mgombea Mwenza Naila Jiddawi Mtwara mjini na watamalizia Desemba 13 huko Ubungo,

Dar es Salaam.

Uchaguzi utafanyika Desemba 14, mwaka huu, baada ya kuahirishwa mara mbili

tofauti, kutokana na kifo cha aliyekuwa mgombea mwenza wa Chadema, Jumbe Rajab

Jumbe aliyefariki usiku wa Oktoba 26, zikiwa ni siku tatu kabla ya uchaguzi mkuu

ambao ulikuwa ufanyike Oktoba 30.

 

Mboma aomba TRC ibinafsishwe haraka

  • Asema hivi sasa linakabiliwa na hali ngumu

Na Mwandishi Wetu

SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC) linasuasua katika uendeshaji na limeiomba serikali

kulinasua kwa kuharakisha ubinafsishaji wake kutokana hali ngumu ya kiuchumi

linayolikabili shirika hilo, imeelezwa.

Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Linford Mboma alitoa kilio hicho jana kwa wajumbe wa Bodi

ya Mamlaka ya Usimamizi wa Vyombo vya Majini na Ardhini (SUMATRA), uliotembelea

vitengo mbalimbali vya shirika hilo.

Ujumbe huo uliokuwa ukiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya SUMATRA, Peter Bakilana,

ulitembelea vitengo kadhaa kikiwemo cha karakana ya TRC mjini Dar es Salaam.

Alisema kutokana na hali hiyo, safari za treni kwa reli ya kati sasa zimepungua

kutoka kila siku hadi tatu kwa wiki.

Mboma alisema tangu TRC itangazwe kubinafsishwa mapema mwaka huu, utekelezaji

wake umekuwa ukisuasua kutokana na sababu mbalimbali hatua aliyosema imekuwa

ikiathiri uendeshaji wa TRC ambayo hapo awali ilikuwa ikitegemea wafadhili kutoka

Canada na Uingereza.

Alisema kutokana na kucheleweshwa huko TRC imekuwa ikiendelea kujiendesha katika

hali ya kusuasua na kupata hasara ya wastani wa asilimia 20 kila mwaka.

Mapema mwaka huu, kampuni mbili za Great Lakes Railway Consortium (GLRC) na Rites

Consortium, zilijitokeza kuomba kukodisha miundo mbinu ya shirika hilo ambapo

katika hatua za awali za uchambuzi wa mapendekezo ya masuala ya kifedha, Rites

ilishinda, lakini iliingwa na GLRC.

Pia, GLRC ilifungua kesi dhidi ya Tume ya Rais ya Kurekebisha Mashirika ya Umma

(PSRC) katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara, ikipinga kutupwa

kwa zabuni yao hasa katika kipengele cha kiufundi. Hata hivyo, kesi hiyo

iliondolewa mahakamani bila masharti Novemba 10, mwaka huu.

Akifafanua, Mboma alisema kutokana na hali hiyo TRC imekuwa ikijiendesha katika

mazingira magumu na hasa ikizingatiwa uchakavu wa injini za treni, mabehewa na

reli kwa jumla.

Kwa mujibu wa Mboma, mbali na uchakavu, TRC pia imekuwa ikiwajibika moja kwa moja

katika kufanya matengenezo ya reli pindi inapoharibika.

Pia, TRC imekuwa ikiendelea kulipa kodi kutokana na mafuta inayonunua na

kuendelea kusafirisha abiria wa daraja la tatu kwa bei ya chini licha ya matatizo

yaliyopo.

Kulingana na Mboma, TRC imekuwa ikitoa wastani wa sh. bilioni 2 kwa mwaka kwa

ajili ya kulipia kodi ya mafuta na pia imekuwa ikipoteza mapato ya wastani wa sh.

bilioni 3 kwa mwaka kwa ajili ya kuendelea kutoa huduma za usafiri wa daraja la

tatu.

Hata hivyo, Mboma alisema pamoja na matatizo hayo, TRC imekuwa ikipiga hatua

katika baadhi ya maeneo yakiwemo ya ufuatiliaji wa safari za treni ambapo kwa

sasa taarifa za treni zilizoko safari zinakuwa zimefika makao makuu katika muda

wa saa mbili tangu ilipoanza safari.

Chini ya utaratibu huo unaendeshwa kwa kutumia mtandao wa kompyuta, taarifa za

treni zinazohusiana na mizigo na abiria walioko safarini zinakuwa ziko kwenye

mtandao na hivyo kurahisisha ufuatiliaji wa safari hizo.

Kuhusu suala la ulinzi wa mizigo na miundombinu ya reli, Mboma alisema TRC

imeingia mkataba na vijiji 55 katika baadhi ya maeneo ambavyo vimekuwa

vikishiriki katika kutoa ulinzi.

Pia, alisema shirika hilo limeanzisha utaratibu wa wateja kushirikishwa katika

kufuatilia mizigo yao kutoka inapopakiwa hadi inaposhushwa, hatua aliyosema

imepunguza tatizo la wizi wa mizigo.

Alisema hilo lilikwenda sambamba na TRC kukabidhi vituo vyake vya mafuta kwa

kampuni ya GAPOIL na kwamba TRC inawajibika tu pale mafuta yanapoingizwa kwenye

mabehewa na kwenye injini.

Kimsingi, alisema huduma za reli zina umuhimu wa pekee na hasa ikizingatiwa

kwamba zinachangia katika kukuza uchumi sambamba na kufanikisha shughuli za

kilimo na viwandani.

Alisema kuyumba kwa TRC kwa kiwango kikubwa kutaathiri shughuli za Mamlaka ya

Bandari Tanzania (THA) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambazo zimekuwa

zikiitegemea katika usafirishaji wa mizigo.

Pia, alisema iwapo uwekezaji huo, utachelewa kuna uwezekano wa soko la TRC kwa

nchi ambazo hazina mlango bahari likachukuliwa na nchi zingine za jirani.

Mboma alisema injini kumi zilizoko Tabora zilizokodishwa kutoka India ziko

hatarini kuchukiliwa kufuatia deni la sh. bilioni 3 ambazo TRC inadaiwa. Alisema

fedha hizo ni hadi kufikia Desemba, mwaka 2002.

 

Majambazi yamtwanga mwanamke risasi kichwani na kupora gari

MWANAMKE mmoja ameuawa kwa kupigwa risasi kichwani na watu wanaohisiwa kuwa ni

majambazi baada ya kuvamia na kuliteka gari aina ya Hiace.

Shirika la habari la PST mjini Shinyanga limemkariri Kamanda wa Polisi Mkoa

Abdalah Mssika alisema tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita saa 12

jioni katika kijiji cha Ibelambogo kwenye barabara itokayo Runzewe kwenda Bwanga

katika kata ya Uyovu mpakani mwa wilaya za Bukombe na Biharamulo.

Mssika alimtaja mama huyo aliyeuawa kwa jina la Imelda Francis (40) mkazi wa

kijiji cha Nyakahala wilaya ya Biharamulo mkoa wa Kagera.

Alisema gari aina ya Hiace lenye namba za usajili T 288 AMM likiwa linatoka

Runzewe kwenda wilayani Biharamulo lilivamiwa na majambazi yenye silaha aina ya

SMG ambayo haikuweza kufahamika namba zake kwa lengo la kutaka kufanya uporaji.

Alisema majambazi hayo yalipoanza uporaji yalimfikia Imelda ambapo alikataa kutii

amri yao na ndipo yalipomfyatulia risasi katika mkono wa kulia na kichwani na

kumpora sh. 50,000.

Alisema mara baada ya uvamizi huo watu hao walitoweka na kukimbilia katika pori

la Bwanga.

Kamanda Mssika alisema polisi bado inaendelea kuwasaka majambazi hao ili kuwaweka

katika mkono wa sheria na kujibu shitaka la mauaji.

Katika tukio lingine, mkazi wa kijiji cha Kitongo kata ya Igwamanoni wilayani

Kahama Sofia Mpangala (55) alikutwa amekufa nyumbani kwake kwa kukatwakatwa

mapanga kichwani na watu wasiofahamika.

Tukio hilo lilitokea Jumatatu usiku kijijini humo baada ya watu wasiofahamika

kuvamia katika nyumba hiyo na kumshambulia kwa kumkatakata mapanga hadi kumuua na

kwamba mauaji hayo yanahusishwa imani za kichawi.

Katika tukio la tatu mkazi wa kijiji cha Ibelasula kata ya Ushetu wilayani Kahama

aliyetambuliwa kwa jina la Manyasura Bundala (60) amekutwa amekufa na mwili wake

kutupwa porini.

Mjini Morogoro Latifa Ganzel anaripoti kuwa, Kamanda wa Polisi mkoa Steven Ngowi

aliwaambia waandishi wa habari jana ofisini kwake kuwa Atanas Edward (20) mkazi

wa Ludewa Peapea wilayani Kilosa alifariki dunia baada ya kupigwa na kundi la

watu wanane akituhuhiwa kuiba baiskeli na radio.

Kamanda Ngowi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Jumanne jioni ambapo Edward

anadaiwa kuiba baiskeli, radio na fedha taslimu sh. 5,000 mali ya Donald Kayombo.

 

Waliojiriwa kinyemela kusimamishwa kazi

  • Ukaguzi kufanyika wizara nane

Na Mwandishi Wetu

TUME ya Utumishi wa Umma itakagua taratibu za ajira ya wafanyakazi wa wizara nane na idara mbili za umma ili kujua kama taratibu za ajira zinafuatwa na kwamba wakipatikana walioajiriwa kinyemela, watasimamishwa kazi,.

Katibu wa Tume hiyo, Thecla Shangali alisema hayo jana alipozungumza na wakaguzi watakaoanza kazi Novemba 22 hadi Desemba 4 mwaka huu, wakati wa hafla ya uzinduzi wa mpango huo iliyofanyika kwenye ofisi ya Tume hiyo barabara ya Samora jijini Dar es Salaam.

Wizara zitakazokaguliwa katika awamu hii ni Wizara ya Elimu na Utamaduni, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Afya, Wizara ya Kilimo na Chakula, Wizara ya Maji na maendeleo ya Mifugo, Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Elimu ya juu, Wizara ya Ardhi na maendeleo ya Makazi na Ofisi ya Rais Mipango na Ubinafsishaji.

Idara zitakazokaguliwa ni Kamishna ya zimamoto na uokoaji na Idara ya uhamiaji.

Hata hivyo lengo la Tume ya utumishi kwa mwaka 2005/2006 ni kukagua masuala ya ajira katika wizara 20, Idara 10 halmashauri 40 na ofisi za makatibu wa mikoa 10.

Kwa kipindi kirefu Tume ya ajira ilihusika katika kuajiri wafanyakazi wa umma, lakini sheria namba nane ya mwaka 2002 iliiondolea mamlaka hayo na kutoa madaraka kwa kila wizara au idara kutoa ajira kwa kufuata sheria na taratibu bila upendeleo.

Ukaguzi huo unafanyika ili kujua kama mamlaka za ajira zinafuata taratibu na sheria za ajira na kwamba kama watapatikana walioajiriwa kwa upendeleo au bila sifa watasimamishwa kazi ili kupata ufafanuzi zaidi.

Thecla alisema katika ukaguzi huo, fomu nane zitatumika ikiwemo fomu ya kwanza ambayo itahusu kutaka kujua kada husika ya ajira, idadi ya wafanyakazi walioomba, idadi ya walioitwa kwenye usaili na idadi ya waliochukuliwa kwa sifa.

Fomu ya pili itahusu kujua idadi ya watumishi waliothibitishwa kazini, idadi ya walioongezewa muda wa kuthibitishwa na idadi ya watumishi wasiothibitshwa kazini na kwamba fomu ya tatu itahusu idadi ya wafanyakazi waliopandishwa vyeo.

Alisema ukaguzi wa kutumia fomu ya nne utahusu masuala ya nidhamu kwa kuangalia idadi ya mashauri, yaliyoshughulikiwa, barua za maamuzi wakati ukaguzi wa masuala ya mafunzo ya watumishi utaangalia idadi ya wafanyakazi waliopata mafunzo, idadi ya wanaoendelea kupata mafunzo na idadi ya waliokosa.

Katika ukaguzi huo, fomu ya sita itajikita juu ya maslahi kwa kuangalia watumishi wanaoilipwa mishahara, wasiokuwepo, watumishi waliorekebishiwa mishahara, wanaodai malimbikizo ya mishahara, idadi ya watumishi walioshughulikiwa pensheni, idadi ya miradi iliyoshughulikiwa na iliyokwama.

Pia alisema , wakaguzi wataangalia fomu ya saba inayohusu upimaji na tathimini ya wazi kwa kila mfanyakazi ikiwa ni pamoja na kuangalia kama upo mpango maalum wa malengo, kuwepo kwa mkataba wa huduma kwa mteja. Kuwepo kwa mgawanyo wa kazi na kuwepo kwa mikakati ya utendaji kazi

Fomu ya nane katika ukaguzi huo itahusu masuala ya takwimu muhimu zikiwemo za watumishi wote, idadi ya watumishi waliostaafu kwa hiari, waliostaafu kwa ugonjwa, waliostaafu kwa lazima na idadi ya watumishi waliofariki.

Akifafanua juu ya umuhimu wa kukagua ajira za watumishi wa umma, Thecla alisema lengo nikutekeleza sheria na kwamba ukaguzi lazima ufanyike kwa haki na kuzingatia taratibu bila woga.

‘Fanyeni ukaguzi kwa fedha zilizoidhinishwa, zingatieni muda, fanyeni kwa uwazi na ukaguzi huo utoe matokeo bayana na kutoa ripoti ya kweli na sahihim,’’ alisema na kuongeza kwamba ni muhimu pia ripoti hizo zikaandikwa kwa wakati.

 

Mawaziri wapya Z’bar waapishwa rasmi

Na Mwandishi Wetu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Amani Abeid Karume jana aliwaapisha mawaziri 12 ambao ni wajumbe wa baraza lake jipy alilolitangaza juzi.

Walioapishwa na wizara zao kwenye mabano ni Ali Juma Shamhuna (Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo). Shamhuna pia ni Naibu Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Wengine walioapishwa kushika nafasi za uongozi katika cha pili cha 2005-2010 cha uongozi wa Rais Karume ni Amina Salum Ali (Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi) na Dk. Mwinyihaji Makame Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Fedha na Uchumi.

Zainab Omar Mohammed (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais kazi maalum), Burhan Saadat Haji (Waziri wa Kilimo, Mifugo na Mazingira) na Sultan Mohammed Mugheir (Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii).

Wengine ni Haroun Ali Suleiman (Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amani), Brigedia Jenerali Mstaafu Adam Mwakanjuki ( Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi) na Suleiman Othman Nyanga (Waziri na Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ).

Mansour Yussuf Himid (Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi), Ramadhan Abdallah Shaaban (Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Katiba na Utawala Bora), Samia Suluhu Hassan (Waziri wa Utalii, Biashara na Uwekezaji ) na Asha Abdallah Juma (Waziri wa Vijana, Wanawake na Watoto.

Hafla hiyo fupi iliyofanyika Ikulu mjini Zanzibar na ilihudhuriwa na Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha, Jaji Mkuu Hamid Mahmood, Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho pamoja na Kadhi Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Mussa Makungu.

 

Wanafunzi 28 hatimaye watoka hospitali

Na El-hadji Yuusuf, Tabora

WANAFUNZI 28 waliokuwa wamelazwa katika hospitali ya mkoa wa Tabora, kupatiwa matibabu baada ya kuanguka kutokana na kupatiwa tiba ya minyoo na kichocho, wametolewa hospitalini huku hali zao zikiendelea vizuri.

Pamoja na kutolewa hospitalini hapo jana, wanafunzi waliokuwa darasa la nne wameshindwa kufanya mtihani wa taifa baada ya kukumbwa na athari za dawa hizo.

Wanafunzi hao walilazwa kutokana na kuanguka huku wengi wao wakiwa wamekumbwa na matatizo ya kuumwa sana kichwa, kizunguzungu, kutapitika na kuharisha kiasi cha kufikia hatua ya kupoteza fahamu.

Kaimu Mganga mkuu wa hospitali ya mkoa wa Tabora, Dk. Amos Nsheha, aliwataja wanafunzi walioruhusiwa hadi kufikia jana mchana kuwa ni Fatuma Shaaban, Lucy Fussi, Johari Rajab, Tea Juma, Pili Mussa, Mwajuma Ramadhani, Tausi Ramadhani, na Gulamali Selemani.

Wengine ni Habiba Nasib, Asha mohamed, Hussein Selemani, Rashid Hamina, Mohamed Mustafa, Sudi Mussa, Cecilia Vincent,Christina Paul, Asha Mashaka, Bakari Omari, Mwanahamis Juma, na Michael Mziku.

Dk. Nsheha, aliwataja wanafunzi wengine waliotolewa jana kuwa ni Sabina Evans, Asha Athumani, Nassibu Athumani, Tausi juma, Juma Mashaka, Christopher Melkior na Athumani Mussa.

Alisema watoto hao walipatwa matibabu na kuwa hali hiyo nikutokana na sababu mbalimbali ikiwa pamoja na kushindwa kupatiwa chakula chenye lishe ya kutosha muda mfupi kabla ya kupewa dawa hizo ambazo ina nguvu kubwa ya kukabiliana na ugonjwa wa kichocho.

Alisema kuwa wanafunzi waliopatwa na mkasa huo, wanatoka katika shule 11 za manispaa hiyo kati ya shule 20.

Aliongeza kuwa wanafunzi waliokumbwa na mkasa huo wanaweza pia kuwa walikuwa na matatizo mengine ya kiafya kama kuwa na vijidudu vya malaria, kuwa dhaifu kiafya na sababu nyinginezo.

Hata hivyo, Dk Nsheha, alisema kuwa watoto hao walipatiwa tiba bure hospitalini hapo na kwamba kulikuwa na uangalizi maalum, kitu ambacho kimesaidia kuwapatia huduma bora na nzuri na hivyo kuokoa maisha yao.

Mkuu wa wilaya ya Tabora, Alhaji Mussa Samizi, alisema dawa hizo hazina madhara, lakini kuna uzembe uliofanywa na walimu baada ya kuwapa bila ya kuwapa chakula cha kutosha, tatizo ambalo alisema limetokana na walimu hao kushindwa kufuata muongozo waliopewa.

 

DAWASCO: Watakaounganisha maji kinyemela kukiona

Na Mwandishi Wetu.

SHIRIKA la Uendeshaji la majisafi na maji taka Dar es Salaam (DAWASCO)limetangaza kuwafuta uteja na kuwang'olea mabomba wateja wote ambao watabainika kwenda kinyume na taratibu za kuunganisha maji ikiwa ni pamoja na uchepushaji wa mita.

Hatua hiyo ya kuwafuta wateja katika orodha yake imewakumba wateja kadhaa waliokuwa wameingia mkataba na DAWASCO kama wateja wa majumbani, lakini wakakiuka taratibu na badala yake kufanya biashara ya kuuza maji.

Baadhi ya wateja wanaotuhumiwa kwa madai ya kuhusika na utaratibu huo mpya wa DAWASCO ni pamoja na Dismas Njau, Izadin Kazokola na Oliverturist Mwakaikamu wakazi wa Mbezi Luois.

Meneja Uhusiano wa DAWASCO, Shy-Rose Bhanji aliwaambia waandishi wa habari kwamba pamoja wateja hao kufutiwa uteja na mabomba yao kung'olewa, vilevile watatozwa faini ya malipo ya matumizi ya maji kwa miezi 24.

Shy-Rose alisema kila mteja aliyebainika kuchepusha mita na kuuza maji kwa wenye magari atatozwa faini ya sh. milioni 11.8 na sh. milioni 4.3 kwa kuuza maji kwa wenye mikokoteni la sivyo atapelekwa mahakamani.

Kwa sasa wateja wa majumbani wanatozwa kiasi cha sh. 359 kwa mita za ujazo tano za mwanzo na iwapo zitazidi basi mteja atatozwa sh. 506 kwa kila mita moja ya ujazo. Wateja wa biashara wanatozwa kiasi cha sh. 725 kwa mita ya ujazo.

Shy-Rose ametoa wito kwa wateja wote kuheshimu taratibu zote za kuunganishiwa maji kwani kuanzia sasa DAWASCO haitamvumilia mteja ambaye atakiuka taratibu.

"DAWASCO inatoa wito kwa wateja wake wote kufuata taratibu zilizowekwa kwa kweli sasa kila tukibaini kwamba mteja amechepua mita tunachofanya ni kuondoa uteja wa mteja husika na zaidi ya hapo ni kung'oa bomba na mteja huyo hatapatiwa tena huduma ya DAWASCO, " alisema meneja huyo wa uhusiano.

DAWASCO ambayo imeingia madarakani kwa takriban miezi mitano sasa, imemaliza mkakati wake wa siku 100 ulioanza mwezi Julai hadi Oktoba ambapo imeweza kufanikisha malengo iliyojiwekea chini ya mkakati uliojulikana ‘siku 100 za utekelezaji’.

Juzi Waziri wa Maji na Maendeleo ya Mifugo, Edward Lowassa alitembelea maeneo kadhaa ya jiji kujionea hatua iliyofikiwa na DAWASCO.

Baadhi ya wakazi walikiri kuboreshwa kwa huduma ya maji katika maeneo ya Sinza, Mikocheni, Kigogo, Kijitonyama Block 46/47, Mwananyamala kisiwani na Tabata. Wakazi wa Mburahati hata hivyo walisema bado huduma ya maji inahitaji kuboreshwa zaidi.

 

 

Walemavu waliogawa vibanda kwa wengine kunyang’anywa

  • Ni vile vya biashara katikati ya Jiji

Na Mwandishi Wetu

WALEMAVU waliopangisha vibanda vya biashara walivyogawiwa na Halmashauri ya Jiji

la Dar es Salaam watanyang’anywa na kugawiwa kwa wengine.

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Luteni Yusuf Makamba alitangaza azma hiyo jana

alipokuwa akizungumza wakati wa hafla ya kuwakabidhi walemavu baiskeli.

“Nataka niwahakikishie kuwa serikali hii na hata hiyo ijayo inawapenda na ndiyo

sababu imefanya juhudi kadhaa za kuwasaidia, ikiwemo ya kuwapatia vibanda vya

biashara ingawa wengi wenu mmevipangisha badala ya kuvitumia kujiendeleza,”

alisema.

Alisema uamuzi wa walemavu hao kupangisha vibanda hivyo kwa wafanyabiashara

wengine ni ukiukwaji wa mikataba ya umilikaji ambayo lengo lake ni kuwahudumia

watu wenye ulemavu kwa kuwapatia nafasi za uhakika za kufanya biashara katika

maeneo yanayokubalika kisheria.

Luteni Makamba alibainisha kuwa uchunguzi wake kuhusu umilikaji wa vibanda hivyo

umebaini kuwa kwa sasa asilimia kubwa vinatumiwa na wafanyabiashara wengine na

walemavu wamebakia kuwa ‘maboya’ tu.

“Unapotembelea vibanda hivyo, kweli utaona vinamilikiwa na walemavu kwa vile vina

maandishi yanayoonyesha hivyo, lakini ukivisogelea utapokewa na kukaribishwa na

wafanyabiashara ambao sio walemavu na unapohoji zaidi, wanakosa hata jibu,”

alisema na kuongeza kuwa hali hiyo inatia shaka kuhusu wamilikaji halali wa

vibanda hivyo.

Utaratibu wa kuhakikisha vibanda hivyo vinarejea na kumilikiwa kwa walengwa

unaanza mara moja ambapo Makamba amewaagiza walemavu waliovipangisha kuwaondoa

wapangaji wao.

Sambamba na hatua hiyo, pia ameiagiza Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam

kufanya tathmini ili kupata takwimu sahihi kuhusu idadi kamili ya vibanda

vilivyokodishwa kinyume cha sheria ili waliokodisha waweze kuchukuliwa hatua

ambazo ni pamoja na kunyang’anywa.

Uamuzi wa kuwanyang’anya walemavu vibanda hivyo umekuja kutokana na wengi wao

kuingia mitaani na kuwa omba omba baada ya kukodisha vibanda hivyo, kazi ambayo

Makamba alisema ni aibu kwao, familia zao pamoja na taifa.

Akizungumza katika halfa hiyo, Askofu Mkuu wa Kanisa la International Evangelism,

Eliud Issangya aliwashauri walengwa waliopatiwa baiskeli hizo kuzitumia kwa

shuhguli za kimaendeleo zaidi ili ziweze kuwanufaisha.

“Ni vema mkatumia msaada huu kama nyenzo ya kuwapeleka kwenye nyumba za ibada,

sambamba na katika shughuli za kibiashara badala ya kwenda kwenye vilabu vya

pombe,” alisema.

Baiskeli hizo 100 zenye thamani ya sh. milioni 35 zimetolewa na kanisa hilo baada

ya kuzipokea kutoka kwa wasamaria wema nchini Marekani.

 

Viongozi wa TLP wilayani Arusha wafikishana kortini

  • Mmoja anaaiwa kwa wizi wa kuaminiwa

Na Omari Shaaban, Arusha

CHAMA cha Tanzania Labour (TLP) wilayani Arusha kipo katika mgogoro mzito

kufuatia kutofautiana kwa viongozi wake na hivyo kukifanya kishindwe kuendesha

kampeni zake.

Mgogoro huo umezidi kuota mizizi ambapo hivi sasa mwenyekiti wa wilaya wa chama

hicho, Calist Lazaro, anadaiwa kumshtaki mgombea udiwani wa kata ya Ngarenaro

kupitia TLP, Raphael Mwaisambule, kwa tuhuma za wizi wa kuaminiwa.

Katika tuhuma hizo, mwenyekiti huyo wa wilaya, anamtuhumu mgombea huyo, kuiba

vifaa vya umeme vyenye thamani ya sh. milioni moja ambavyo ni seti nzima ya vifaa

vya kutangazia vya kampeni, spika, vipaza sauti na vinginevyo.

Mgombea udiwani huyo, anashatakiwa kwa wizi wa kuaminiwa wa vifaa hivyo ambavyo

ni mali ta TLP.

Imeelezwa na watu kutoka ndani ya TLP Arusha, kwamba kufunguliwa kwa mashataka

kwa mgombea udiwani huyo ni maagizo kutoka ngazi za juu za chama hicho, ingawa

hawakuwa tayari kuelezea suala hilo.

Hata hivyo, hadi kufikia jana asubuhi mgombea udiwani huyo alikuwa bado

hajafikishwa mahakamani kutokana na tuhuma hizo, na hakuwa amepatiwa dhamana kwa

siku mbili tangu awekwe rumande ya polisi kwa uchunguzi wa tuhuma hizo.

Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoa, James Kombe alisema kuwa

mgombea udiwani huyo anatuhumiwa kuiba spika, kipaza sauti na kifaa maalumu cha

kuongeza mwangwi wa sauti, ambavyo vyote ni mali ya TLP.

Alisema kuwa uchunguzi wa madai hayo unaendelea vizuri na kwamba mtuhumiwa huyo

ambaye amefunguliwa mashtaka hayo na mwenyekiti wake wa wilaya atafikishwa

mahakamani leo.

Habari za uhakika kutoka TLP zimeeleza pia kuwa, tangu kukamatwa na kuweka ‘selo’

kwa mgombea huyo, inadaiwa kuwa mgombea ubunge wake, kupitia chama hicho,

Godbless Lema hajawahi hata kukanyaga eneo hilo la polisi ambalo kwake lilikuwa

kama mazoea kabla ya tukio hilo na wananchi kujiuliza maswali mengi kuhusiana na

tukio hilo.

 

CCM Moro yateua kaimu katibu wa wilaya K’mbero

Na Igamba Libonge, Kilombero

CHAMA cha Mapinduzi mkoani Morogoro kimemteua Juma Ndekanye (52) kuwa kaimu

katibu wa wilaya ya Kilombero kukaimu nafasi ya katibu ambaye hivi sasa

anakabiliwa na matatizo ya kuumwa.

Taarifa iliyotolewa jana na Katibu wa CCM Mkoa wa Morogoro Catherine Ndahani

katika kikao cha kamati ya siasa wilaya kilichofanyika makao makuu ya chama

wilaya mjini Ifakara.

Ndekanye ambaye pia ni Katibu wa Wazazi wilaya Kilombero amekaimu nafasi hiyo

baada ya katibu wa wilaya, Luteni Makame Makame kuugua na kulazwa katika

Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Catherine alisema Sekretarieti ya CCM mkoa Morogoro imeamua kumteua Ndekanye

baada ya kuona wilaya haina kiongozi mkuu, hasa katika kipindi hiki kigumu cha

uchaguzi.

Alisema kwa sasa wilaya ilikuwa inaongozwa na wasaidizi, kwani mapema mwezi

uliopita mwenyekiti wa Chama, Kassimu Kulolela alifariki dunia ghafla nyumbani

kwake huko Mang’ula na sasa katibu wake anaumwa hivyo ofisi iko wazi.

Katibu huyo wa mkoa alisema Ndekanye atashikilia wadhifa huo hadi hapo hali ya

Makame itakapokuwa njema au makao makuu ya Chama kumteua katibu mwingine.

 

Maregesi achangia sh. milioni 3.6 sekondari za WAZAZI

Na Mussa Homera, Songea

MWENYEKITI wa Jumuia ya Wazazi Tanzania, Abiud Maregesi amechangia jumla ya sh.

milioni 3.6 kuimarisha shule za sekondari za Wazazi mkoani Ruvuma.

Alitoa mchango huo mwanzoni mwa wiki alipokuwa ziarani mkoani Ruvuma kukagua

maendeleo ya elimu na malezi, majukumu yanayosimamiwa na Jumuia hiyo ya CCM.

Katika Shule ya Sekondari Mkinga iliyoko wilayani Mbinga Maregesi aliipatia shule

hiyo sh. 600,000 ili kukarabati majengo ya shule yaliyopo, wakati katika Shule ya

Sekondari Namtumbo aliipa sh. milioni moja ili kuanzisha ujenzi wa madarasa ya

kidato cha tano na sita.

Mchango wa aina hiyo aliutoa wilayani Tunduru ambako jumla ya sh. milioni mbili

alizitoa kwa ajili ya kusaidia kuokoa matofali laki tatu yaliyofyatuliwa na

wananchi ili kuanzisha ujenzi wa shule ya sekondari Muhuwesi, itakayomilikiwa na

Jumuia ya Wazazi.

Mbali ya kukagua maendeleo ya elimu na malezi, mwenyekiti huyo pia alihutubia

mikutano ya hadhara iliyoambatana na kampeni za uchaguzi mkuu wa taifa ambapo

aliwataka wananchi kuipa ridhaa CCM kuunda serikali kwa mara nyingine tena ili

kuendeleza mafanikio yaliyopo.

Aliwaonya wananchi kutofanya majaribio katika kuweka viongozi ndani ya dola kwa

kuwakumbusha kuwa vyama vya upinzani havijajenga mwelekeo wa kuweza kuiongoza

nchi.

Alitoa mfano wa baadhi ya vyama kuwa vimekuwa vikigombania ruzuku kila kukicha na

kushangaa iwapo vitapewa kasiki la umma watafanyaje kama siyo kuuvuruga uchumi

uliojengeka na serikali ya CCM katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Katika ziara hiyo, Maregesi pia alitoa baiskeli nane kwa Jumuia za Wazazi na

mbili kwa UWT wilaya ya Tunduru ili zisaidie kurahisisha utendaji kazi katika

matawi ya jirani.

 

 

Watakiwa kujitokeza kuchukua mafunzo ya ufundi

Na Hussein Semdoe, Handeni

WANANCHI wilayani Handeni wametakiwa kujitokeza kwa wingi kujifunza ufundi katika

fani mbali mbali katika Chuo cha maendeleo ya wananchi FDC kilichopo mjini

Chanika.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Chuo hicho Barnaba Majili alipokuwa akiongea na

mwaandishi wa habari hii Ofisini kwake.

''Natoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kwa kusoma ufundi katika chuo chao

hiki ili waweze kujiajiri wenyewe na kuacha tabia iliojengeka kwa vijana ya kukaa

vijiweni, ''alisema.

Majili alsema mafunzo yanayotolewa na chuo ni pamoja na

ufundi magari,umeme,ushonaji,uselemara,upishi na kompyuta biashara,kilimo na

mifugo .

Alisema hivi sasa kuna wanafunzi 80 wakiwemo wanawake 30wanaofanya mitihani ya

kitaifa ya VETA iliyoanza juzi katika masomo ya ufundi mbalimbali.

Majili aliwaomba wafadhili kama Halmashauri ya Wilaya, Serikali,mashirika ya

Serikali na yasiyo ya kiserikali kuwadhamini walemavu kwa kuwalipia ada za masomo

ambazo alizitaja kuwa ni kati ya Sh.70,000 na sh 130,000 kutegemea na fani ya

ufundi mwanafunzi atakayochukua.

 

China yatoa misaada ya vifaa vya kilimo

Na Furaha Omary na Njumai Ngota

UBALOZI wa China umeipatia Wizara ya Kilimo na Chakula, vifaa vya kilimo vyenye

thamani ya sh. 141,119,813 (Dola za Marekani 123,615).

Vifaa hivyo ambavyo ni pamoja na pampu za umwagiliaji (2), mashine za kusaga (3),

mashine kulimia (7) na trekta (3) zilikabidhiwa na Balozi wa China nchini, Yu

Quing Tai, kwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Wilfred Ngirwa.

Sherehe za makabidhano zilifanyika juzi kwenye maghala ya wizara Chang'ombe, Dar

es Salaam ambapo katibu mkuu huyo alisema itasaidia nchi kuingia katika kilimo

cha kisasa.

"Msaada huo umekuja katika wakati mwafaka, ambapo wananchi wetu wanauhitaji kwa

kiasi kikubwa teknolojia ya kisasa katika uzalishaji wa kilimo," alisema Ngirwa.

Alisema Serikali imejitahidi kuwa na uzalishaji wa kisasa na wa kibiashara katika

sekta ya kilimo na hivyo pampu hizo zitatumika kwenye miradi iliyoanzishwa ya

umwagiliaji.

Kwa mujibu Ngirwa, katika siku za karibuni kulikuwa na vituo 55 vya maksai

kusaidia kilimo na wananchi sasa wameanza kubadilishwa, ili waondokane na jembe

la mkono na kuingia kwenye kilimo cha maksai.

Alisema, mauzo ya trekta kitaifa yameongezeka maradufu, akitroa mfano wa mwaka

1996 kulikuwepo na trekta 49 mwaka 1996 na sasa kiwango hicho kimefikia 350 kwa

mwaka, ilipofika mwaka jana.

Ngirwa alisema, hali hiyo imewezekana zaidi pia kutokana na msamaha wa kodi

katiia ununzi wa nyenzo hizo za kilimo.

Pia kumekuwepo na mfuko wa kuendeleza kilimo ambacho kimewezesha kukarabati

matrekta yaliyoharibika, kununua mapya na wananchi kukodi, yote hiyo ikiwa na

maana kubwa kwa maendeleo ya kilimo.

Ngirwa alisema, licha msaada katika sekta hiyo ya kilimo na chakula, pia nchi

hiyo imekuwa ikiisaidia Tanzania katika sekta za afya, pia usafiri na

mawasiliano.

Kwa upande wake Balozi Tai, alisema lengo la msaada huo ni kuwafanya wafikie

lengo la kujitegemea kwa chakula, na kuwa na uhakika wa upatikanaji wa chakula.

 

Mafunzo yatolewa kuuelewa Mkukuta

Na Rodrick Makundi,Moshi

SERIKALI imesema mafanikio ya uelewa wa kutosha juu ya mkakati wa kukuza uchumi

na kupunguza umaskini, Mkukuta, utafanikisha kutoa elimu kwa Watanzania ambao

watakuwa na mbinu za kutosha juu ya kukuza uchumi wao hususani uchumi wa

mwananchi moja mmoja.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Mary Mushi, wakati

alipokuwa akifungua juzi mafunzo ya Mkukuta ambayo yamewashirikisha wadau wa

mpango huo kutoka mikoa ya Arusha,Tanga na Kilimanjaro.

Washiriki wa mafunzo hayo ni wataalamu wa sekretarieti za mikoa na mamlaka za

serikali za mitaa,ambapo pia mafunzo yanatolewa katika kanda sita,zinazojumuisha

mikoa yote nchini.

Katika hotuba yake katibu huyo alisema matarajio makubwa ni kwamba iwapo

wataalamu wataufahamu Mkukuta watakuwa na nafasi kubwa ya kuelimisha wengine

katika ngazi ya mikoa, halmashauri hadi kufikia ngazi za jamii.

"Ili kufikia malengo ni jukumu la kila mmoja kusimamia na kufuatilia utekelezaji

wa mikakati ya kisekta ya kupambana na umaskini na kutumia vizuri fedha za

serikali na rasilimali katika kuandaa mipango bora," alisema katibu huyo.

Pia aliongeza kuwa mafunzo juu ya Mkukuta kwa wataalamu kutoka katika ngazi zote

za utawala ndani ya serikali yamelenga kuzifahamisha sekretarieti za mikoa na

mamlaka za serikali za mitaa juu ya mfumo wa ufuatiliaji unaofanywa katika

kuboresha ili kufuatilia utekelezaji wa mpango huo.

Akitoa maelezo mafupi juu ya mafunzo hayo Mkurugenzi Msaidizi wa mpango huo,

Marry Mwasha, alisema kuwa serikali imeweka mkazo mkubwa katika kuhakikisha kuwa

bajeti ya serikali inalenga kuutekeleza mpango huo kulingana na bajeti ya mwaka

wa fedha 2005/06.

Alisema kuwa hivi sasa mtazamo wa serikali ni kuhakikisha kuwa utekelezaji wa

mpango huo unafanywa kama ilivyopangwa, ili kufikia malengo ya uanzishwaji

wake,ambapo Ofisi ya Makamu wa Rais imepewa jukumu la kutoa elimu kwa

sekretarieti za mikoa na mamlaka za serikali za mitaa kuhusu mpango huo.

Mpango wa kukuza uchumi na kupunguza umaskini Mkukuta,ni awamu ya pili ya

utekelezaji wa mkakati wa kupunguza umaskini ulioandaliwa mwaka 2000,chini ya

mpango wa msamaha wa madeni kwa nchi masikini sana duniani.

Mkakati huo umefanyiwa mapitio,kufuatia utekelezaji wake katika kipindi cha miaka

mitatu,lengo la mapitio hayo likiwa ni kubaini mapungufu na kuboresha mkakati ili

uweze kuleta mafanikio zaidi kwa wananchi na kuhakikisha kuwa uchumi unakuwa

zaidi kwa kasi na hivyo kuiwezesha Tanzania kufikia malengo yaliyobainishwa

kwenye dira ya taifa ya maendeleo ya 2025.

Mapitio hayo yalifanywa kwa ushirikiano kati ya serikali na wadau katika ngazi

mbali mbali kwa njia ya mahojiano,ukusanyaji wa maoni na majadiliano,maoni

yaliyokusanywa na uzoefu uliopatikana katika utekelezaji wa awamu ya kwanza

ulifanyiwa uchambuzi wa kina na kufanikisha maandalizi ya MKUKUTA.

Tofauti na mkakati Mkukuta unatambua mchango wa sekta zote katika kukuza uchumi

na kuondoa umaskini wakati mkakati ulitoa kipaumbele kwa sekta sita ambazo ni

kilimo,elimu,afya,maji na barabara vijijini.

 

 

 

Plan International kutumia sh. milioni 300 mpango wa HISA

SHIRIKA la Plan International la hapa nchini limesema litatumia jumla ya sh.

milioni 300 kusambaza mpango wa akiba ya kuweka na kukopa vijijini maarufu kama

HISA katika wilaya tatu nchini, inaripoti PST mjini Mwanza.

Wilaya ambazo zinatarajiwa kufikishiwa huduma ya mpango huo hivi karibuni na

shirika hilo ni pamoja na Geita mkoani Mwanza, Ifakara mkoani Morogoro na Kibaha

mkoani Pwani.

Hayo yalielezwa na Mkurugenzi wa Plan Internation nchini Heather Borquez wakati

wa ufunguzi wa warsha ya kuutangaza mpango huo kwa wadau wake kutoka katika nchi

mbalimbali za kusini na mashariki mwa bara la Afrika.

Alisema hatua hiyo inatokana na mafanikia makubwa yaliyopatikana katika mradi wa

majaribio wa wilayani Kisarawe mkoani Pwani, ambao walifanya kwa kushirikiana na

Shirika la Care International.

Borquez alisema mpango wa HISA ni rahisi kuuendesha, hauhitaji mtaji, unamilikiwa

na wananchi wenyewe ambao wanaweka mitaji yao kwa kuweka fedha na baadaye

kuzikopa.

Alisema HISA inamnufaisha mwanajamii moja kwa moja kwa kuwa anao uwezo wa kukopa

fedha bila ya masharti magumu na urasimu, ili mradi awe mwanakikundi na

alishaweka akiba kupitia katika mpango huo.

Warsha hiyo imehudhuriwa na washiriki kutoka Sudan, Burkina Faso, Kenya, Uganda,

Niger, Zambia, Zimbabwe, Ujerumani, Marekani na Uingereza ambayo ni makao makuu

ya Shirika hilo na wenyeji Tanzania.

 

TOUCH laokoa waliojiingiza kwenye ukahaba

WASICHANA kadhaa waliokuwa wakifanya biashara ya ukahaba katika mji wa Kigoma

wameokolewa na kurudishwa kwao na shirika linashughulika na kutetea haki za

watoto la Tanzania Outreach For Children (TOUCH) lenye makao yake makuu mjini

Kigoma.

Kwa mujibu wa PST hayo yalisemwa juzi na Mkurugenzi wa shirika hilo Shilinde

Filbert wakati wa tamasha la watoto lililofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri mjini

Dodoma na kuwashirikisha watoto kutoka katika baadhi ya shule zilizopo katika

manispaa ya Dodoma.

Filbert alisema watoto hao waliwaokoa katika kipindi cha mwaka huu na wengi wao

walikuwa na umri wa chini ya miaka 15 ambapo baada ya kuwaokoa waliwauliza

wanatoka wapi na wote waliwasafirisha hadi kwenye maeneo wanayotoka.

Alisema watoto hao walikuwa wakifanya biashara ya ukahaba katika maeneo

mbalimbali ya mji wa Kigoma na wateja wao wakubwa wanadaiwa kuwa ni wavuvi wa

dagaa na samaki.

Filbert alisema kuwa shirika lake lilifanya utafiti na kugundua kuwa biashara ya

ukahaba katika mji wa Kigoma inafanywa na watoto wadogo, ndipo walipoamua

kuwakusanya na kuwarudisha kwao.

Alisema japo ilikuwa ni kazi ngumu kuwashawishi ili warudi kwao lakini kwa juhudi

walizozifanya walifanikiwa kuwarudisha na hadi sasa wanafuatilia kuhakikisha kuwa

hawarudi tena mjini.

TOUCH bado linaendelea na kazi ya kuwakusanya watoto ambao wapo katika ajira

mbaya na kuwarudisha kwao na vilevile kuwatetea watoto.

 

Williamson Diamonds yawapa tuzo mameneja wastaafu

KAMPUNI ya mgodi wa machimbo ya almasi ya Williamson Diamonds Limited ya Mwadui

mkoani Shinyanga imewatunuku mameneja wake wastaafu sita tuzo ya utumishi bora

ikiwa ni moja ya maadhimisho ya kutimiza miaka 65 ya mgodi, inaripoti PST.

Tuzo hizo zilikabidhiwa kwa wastaafu hao juzi katika sherehe za maadhimisho ya

kutimiza miaka 65 tangu mgodi huo ulipoasisiwa nchini katika sherehe

zilizofanyika ukumbi wa Recreation Club uliopo mgodini humo na kuhudhuriwa na

viongozi mbalimbali wakiwemo wajumbe wa bodi ya wakurugenzi kutoka Afrika ya

kusini.

Mameneja wastaafu waliotunukiwa tuzo hizo hiyo juzi ni pamoja na William Manning

(1976-1979), John Kiwia (1979 - 1982), Erasto Ndanguzi (1982 - 1983) Samwel

Lwakatare (1973 - 1976) Robin Crawford (1958 - 1973) na Sylivanus Mipawa (1984 -

1994).

Pia tuzo hiyo ya utumishi bora ilitolewa kwa wafanyakazi wengine walioonyesha

juhudi katika utendaji kazi wao akiwemo mshauri wa kampuni kuhusu masuala ya

mazingira Bertus Stoker.

Akikabidhi tuzo hizo kwa mameneja hao, Mwenyekiti wa kampuni tanzu inayomiliki

mgodi huo ya De Beers yenye makao yake nchini Afrika Kusini Jonathan Oppenheimer

alisema utendaji kazi wa wastaafu hao ndio uliochangia kwa kiasi kikubwa

kuendelea kuwepo kwa mgodi huo hadi hivi leo.

Oppenheimer aliwapongeza mameneja hao kwa uhodari wao na uvumilivu waliouonyesha

wakati wa utendaji kazi licha ya kufanya hivyo katika mazingira magumu.

Hata hivyo, alisema changamoto ilinayoukabili mgodi huo kwa sasa ni kuongeza

uboreshaji pamoja na tija, hali bora ya maslahi ya watumishi na familia ili nao

wapate mafanikio sambamba na kampuni yenyewe.

Alisema pamoja na mafanikio ambayo mgodi umepata kwa bado wafanyakazi

wanalojukumu la kuhakikisha hali hiyo inaendelea katika kipindi cha miaka 35

ijayo ambapo mgodi utatimiza miaka 100.

"Ni nadra mno kampuni kufikisha umri wa miaka 65 bila kuanguka mfano barani

Amerika kampuni nyingi huishia miaka 13 au zaidi kidogo kwetu sisi huo ni fahari

na tunajivunia kwa hilo," alisema Oppenheimer.

Mgodi wa Williamson Diamonds Limited ulianzishwa na mtaalamu wa madini kutoka

Canada John Williamson mwaka 1940 ambao umeendelea kuchimba almasi katika eneo

hilo la Mwadui na kwa hivi sasa ndiyo mgodi mkubwa nchini na eneo la Afrika

Mashariki.

 

Morogoro yateuliwa mfano wa kuboresha maduka ya dawa baridi

Na Mwandishi Wetu

MKOA wa Morogoro umeteuliwa kuwa miongoni mwa mikoa mitatu nchini itakayoshiriki

awamu ya kwanza ya usambazaji wa mpango wa kuboresha maduka ya dawa baridi, mikoa

mingine ikiwa ni Rukwa na Mtwara.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Magreth Ndomondo juzi wakati wa

warsha ya uhamasishaji kwa wadau wa ngazi ya mkoa kuhusu mpango huo ambao mara

baada ya kuboreshwa kwa maduka hayo yataitwa maduka ya dawa muhimu.

Alisema mpango hu