UHURU 18.11.2005

 

 

Nimekwenda Kyela kuwakabili maadui watatu, asema Dk. Mwakyembe

  • Akana kwenda kupambana na Mwakipesile

Na Bashir Nkoromo, Kyela

MGOMBEA wa Ubunge wa jimbo la Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe amesema hakwenda katika jimbo hilo kupambana na mbunge wa zamani, John Mwakipesile ila kupambana

na maadui watatu wa taifa, yaani ujinga, maradhi na umasikini.

Dk. Mwakyembe alitamka hayo alipokuwa akisalimia wananchi kwenye mkutano wa

hadhara uliohutubiwa na Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula katika Kata ya

Ipinda, Kyela juzi.

“Ndugu wananchi mimi nilikuja Kyela si kwa nia ya kupambana na Mwakipesile.

Hapana. Nilikuja kwa ajili nisaidiane nanyi katika kupambana na ujinga, umasikini

na maradhi,” alisema Dk. Mwakyembe na

kumtaka Mwakipesile ampatie ushirikiano kila mahali katika kampeni.

Dk. Mwakyembe aliwaambia wananchi wa jimbo hilo kwamba ahadi yake kwao ni kwamba

miaka mitano ya uongozi wake

akiwa Mbunge, itakuwa si ya starehe ila ya kila mwanajimbo kufunga kibwebwe na

kuchapa kazi kwa uwezo wake ili kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya 2005.

Akihutubia mkutano huo, Mangula alisema, baada ya kura za maoni na baadaye

kuteuliwa kwa mgombea katika jimbo

sasa kazi iliyobaki kwa kila mwana-CCM ni kuungana na wenzake kumpigia kura

mgombea wa Chama bila kujali tofauti zilizojitokeza wakati wa kura za maoni.

Mangula alisema, wale wote walioshiriki katika mchakato ili kupitishwa kugombea

majimboni, lakini kwa mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM wakaachwa

hawana sababu ya kuingiwa na kwikwi isiyoisha kwa sababu ikiwa ni wanachama safi

wa CCM ni lazima wazingatie nidhamu ya Chama ambayo ni pamoja na kukubali na

kutekeleza maamuzi ya juu ya Chama.

Alimpongeza mbunge za zamani wa jimbo la Kyela, Mwakipesile kwa kutotetereka

baada ya kuachwa katika kura za maoni na badala yake akaendelea kumpa ushirikiano

Mwakyembe ambaye alipitishwa.

Mangula akishangiliwa na wananchi katika mkutano huo aliwaita jukwaani Dk.

Mwakyembe na Mwakipesile na kuwataka wakumbatiane mbele ya hadhara kudhihirisha

mshikamano wao ambapo walipanda jukwaani na kufanya hivyo.

Alizungumzia haja ya wananchi kuchagua wagombea wa CCM katika ngazi zote ikiwemo

ya Urais, Mangula alisema,

watanzania hawana budi kuwachagua wagombea hao kwa tiketi ya CCM kwa kuwa ni

wagombea wa Chama kinachoaminika na chenye sera inayotekelezeka.

 

Umeme katikati ya Jiji kuwa ahueni J’tatu

  • Ni baada ya kukamilika kwa njia mpya

Na Mwandishi Wetu

HALI ya upatikanaji umeme katika maeneo ya katikati ya jiji na wilaya ya Ilala

kwa jumla itakuwa ahueni kuanzia Jumatatu baada ya kukamilika ujenzi wa njia mpya

kutoka Ubungo.

Meneja wa Usambazaji Umeme Hans Lotterine aliyosema hayo mbele ya Naibu Waziri wa

Nishati na Madini, Dk.Ibrahim Msabaha kwamba ujenzi wa njia nyingine ya umeme

kwenye njia kuu kati ya Ubungo na Ilala unatarajiwa kumalizika Jumatatu na kwamba

umeme katika wilaya ya Ilala utarejea katika hali ya kawaida, lakini Temeke

itaendelea kuwa na matatizo sehemu chache.

Lotterine alisema uwekaji nyaya za umeme kwenye njia kuu yenye urefu wa kilometa

10 kati ya Ubungo na Ilala, ulianza Novemba 8, na ulitarajiwa kukamilika Novemba

26, lakini sasa utakamilika Jumatatu ijayo kwa gharama ya karibu sh. milioni 200

na kwamba msongo wa umeme huo ni 132 Kv.

Katika hatua nyingine, Meneja huyo alimweleza Naibu Waziri kwamba Shirika lake

linao mpango wa kununua transfoma mpya kutoka India kwa gharama ya zaidi ya sh.

bilioni 1.5 na kwamba watalaamu walitarajiwa kuondoka jana kwenda India ili

kupanga zaidi juu manunuzi hayo.

Alisema transfoma hiyo itasaidia kupunguza matatizo ya umeme maeneo ya katikati

ya jiji yakiwemo Kariakoo, Sokoine, Temeke na baadhi ya maeneo ya Kipawa.

Hata hivyo, Naibu Waziri alishauri kwamba pamoja na mipango hiyo, Shirika halina

budi kuweka utaratibu maalum wa kuhakikisha mitambo yake haiharibiki ovyo.

Alisema serikali kwa upande wake itaendelea kutekeleza majukumu yake ikiwa ni

pamoja na kuhakikisha uzalishaji wa umeme wa Megawati 510 unaendelea kama kawaida

kutoka vyanzo vya IPTL, Songas na kwenye mabwawa

Matatizo ya umeme wilayani Ilala na Temeke yanasababisha hasara ya wastani wa sh.

milioni 50 kila siku.

Dk. Msabaha amewataka wafanyakazi wa TANESCO kuongeza kasi ya kuzuia mapema

uharibifu wa miundombinu iliyopo ili kuepusha tatizo la kuwakosesha umeme wateja

kwa muda mrefu.

Naibu Waziri alitoa wito huo baada ya kumaliza ziara yake ya kujionea jitihada za

Tanesco katika kutengeneza nyaya za umeme zitakazotoa umeme Ubungo hadi Ilala ili

kupunguza matatizo ya umeme katika wilaya za Ilala na Temeke.

Machi, mwaka huu, Transfoma moja iliyopo Ilala iliharibika, lakini TANESCO

hawakushtuka hadi Oktoba 18, zilipoharibika Transfoma zingine mbili kwa mpigo na

kusababisha upungufu mkubwa wa umeme katika wilaya hizo.

Baada ya kuharibika kwa transfoma hizo, Wilaya ya Ilala inayohitaji Megawati kati

ya 80 na 100 iliweza kupata megawati 40 tu, wakati Temeke inayotumia megawati 50

ilifanikiwa kubaki na megawati 26 tu.

 

 

 

Misri, India, Nigeria zampongeza Rais Karume kwa ushindi

Na Mwandishi Maalum, Zanzibar

RAIS Hosni Mubarak wa Misri, Makamu wa Rais wa India, Bhairon Singh Shehawat na

Serikali ya Nigeria, watuma salamu za pongezi kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti

wa Baraza la Mapinduzi, Amani Abeid Karume, kwa kuchaguliwa kuendelea tena

kuiongoza Zanzibar kwa kipindi cha pili cha miaka mitano.

Pongezi kutoka kwa viongozi hao ziliwasilishwa kwa njia ya maandishi kupitia

ofisi za balozi zao nchini Tanzania.

Katika salamu kutoka kwa Rais Mubarak ambazo ziliwasilishwa na Balozi Mdogo wa

Misri nchini Tanzania, Amdi Mourad Kamel, zieleza kuwa Misri imefarajika na

matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar.

Taarifa hizo zilimpongeza Rais Karume kwa ushindi mkubwa alioupata kufuatia

mafanikio makubwa ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar, ulioendeshwa katika mazingira ya

amani na utulivu jambo ambalo lilitoa fursa kwa wananchi kupiga kura kuchagua

viongozi wanaowataka.

Rais Mubarak alimtakia heri na mafanikio Rais Karume katika juhudi zake za

kuwapatia maendeleo wananchi wa Zanzibar.

Salamu za Makamu wa Rais wa India, Shakhawat ambazo zilitumwa kwa niaba ya

serikali na wananchi wa India, zimeeleza kwamba uhusiano wa karibu baina ya India

na Zanzibar uliodumu kwa muda mrefu, unafurahiwa na wananchi wa pande zote mbili.

Alisema ana imani kuwa uhusiano huo utaendelezwa zaidi katika kipindi chote cha

uongozi wa Rais Karume, ambaye ameshinda uchaguzi mkuu wa Zanzibar kwa kupata

ridhaa ya wananchi wa Zanzibar walio wengi.

Salamu kutoka Nigeria, zilieleza kuwa kuchaguliwa kwa Rais Karume kwa kipindi cha

pili, kunaashiria heshima na imani kubwa waliyonayo wananchi wa Zanzibar na

kukubalika kwa juhudi na sera zake za maendeleo.

Pia taarifa hiyo ilielezea juu ya matarajio makubwa ya Serikali ya Nigeria katika

kuendeleza ushirikiano kati ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Wakati huo huo, Balozi mdogo wa Misri, Kamel alifanya mazungumzo na Rais Karume

na katika mazungumzo yao walitilia mkazo umuhimu wa kuimarisha uhusiano.

Rais Karume alieleza kuwa Zanzibar itaendelea kuimarisha taasisi zake za

demokrasia kwa lengo la kudumisha umoja, amani, utulivu na mshikamano nchini.

Alisema Zanzibar ina dhamira ya kujenga mfumo wa utawala wa demokrasia na

maandalizi ya uchaguzi pamoja na juhudi za kujenga misingi ya amani na utulivu

nchini ikiwemo utekelezaji wa muafaka wa pili ni uthibitisho wa dhamira ya

Serikali ya Mapinduzi katika kuimarisha utawala wa demokrasia nchini.

Rais Karume alichaguliwa tena kuiongoza Zanzibar kwa kipindi cha pili cha miaka

mitano katika uchaguzi uliyofanyika Oktoba 30, mwaka huu.

 

 

Wastaafu wa EAC wakana kutayarisha maandamano

Na Mwandishi Wetu

CHAMA cha wastaafu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kimesema hakina

habari na maandamano ya wastaafu hao yaliyopangwa kufanyika kushinikiza malipo

yao, kwani ni kinyume na makubaliano waliongia na serikali mahakamani.

Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo, Vitus Lyamkuyu, alisisitiza chama chake hakiwezi

kushawishi wastaafu waandamane kwa lolote, kwani licha ya kukiuka sheria, pia ni

ukiukwaji wa maadili kutokana na ukweli kwamba serikali tayari imeshaonyesha

dhamira ya kutekekeza matakwa yao.

Mapema wiki hii, kundi moja la wastaafu hao walitamka wataenda Ikulu kuonana na

Rais Benjamin Mkapa kushinikiza malipo yao, ambapo wanadai ni pungufu ya kile

kinachostahili na wengine hawajalipwa kabisa.

Pia kundi hilo wamemtuhumu wakili wao Deusdedit Bishota, ambaye pia ndiye

mwenyekiti kuwa amewapotosha kisheria.

Hata hivyo, Lyamkuyu alikiri kiasi walicholipwa hivi karibuni kipo kwa wastani wa

asilimia 10 ya kile wanachokidai, lakini hawatatumia njia ya mabavu kama

maandamano kudai haki hiyo pia kwa mujibu wa makubaliano ya kisheria waliongia na

serikalini.

Alisema kauli rasmi ya wastaafu inatoka katika chama hicho ambacho hakijawahi

kufikiria hata siku moja kushurutisha serikali, ikiwa ni pamoja na kupanga

maandamano, kauli hizo zimekuwa zikitolewa na baadhi ya wastaafu walio nje ya

uongozi wake.

Lyamkuyu alionyesha nakala ya makubaliano ya kisheria baina ya wastaafu na

serikali kattika kesi ya madai namba 95 ya mwaka 2005, ambapo ilikubaliwa

serikali baada ya kuwalipa wastaafu kama kuna madai yoyote yale halali,

itayafanyia kazi ndani ya miezi sita, kuanzia Oktoba 28 mwaka huu na kwa maana

hiyo kipindi hicho kinaishia Aprili 28 mwakani.

Alisema ofisi yake inaendelea kupokea madai na malalamiko mbalimbali ya

wasioridhika na malipo au kusahauliwa katika ili wahakikishe haki yao

inapatikana, vivyo hivyo kwa warithi wa wastaafu waliofariki dunia.

Lyakumyu alitupia lawama Hazina na mashrikia yaliyorithi shughuli za iliyokuwa

Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwamba wamepotosha kumbukumbu na wapo ambao baadhi

ya nyaraka katika majalada yao yamepotezwa.

Pia ameshangazwa na hatua ya Hazina kuchukua mafaili ya wastaafu kutoka mashirika

waliokuwa na kuyalundika katika ofisi zake, kitu kitakacholeta ugumu katika

kushughulikia madai ya wastaafu husika.

Katibu Mkuu huyo, alisema licha ya hazina kulipa kiasi cha sh. bilioni 117 lakini

wana imani watalipwa kiasi kingine kumalizia madai yao kama serikali iliyoahidi

lakini ilitamka kuwa uwezo wake ni mdogo hivyo itafanya kwa awamu.

Alisema kwa mujibu wa makubaliano yaliyofikiwa ya mgawanyo wa mali ya EAC,

wastaafu hao walitakiwa kulipwa kwa thamani ya dola ya Marekani tarehe hiyo ya

mwaka 1977, ambapo dola moja ilikuwa na thamani ya sh. nane na riba ya asilimia

saba kwa mwaka kila zitakapochelewa.

Licha ya kanuni hiyo, serikali iliwalipa kwa kanuni ya riba ya asilimia 17.5 ya

sh. ya Kitanzania kwa mwaka jambo linaloleta tofauti, juu ya kiasi halisi

wanachokidai.

Kuhusu mkanganyiko ulioibuka kuhusiana na uongozi wa chama hichi cha wastaafu wa

EAC, alisema hadi sasa Mwenyekiti wao ni Bishota na amekuwa akishikilia wadhifa

huo tangu mwaka 2000, lakini mwaka juzi aliugua na kufanya nafasi yake ishikiliwe

na viongozi wengine kwa muda.

Lyamuya, aliwataja waliokuwa wakikaimu nafasi hiyo tangu Bishota augue ni

wafuatao na miaka husika katika mabano: Jafari Kibwana (2003), Nicolas Kimaro

(2003), Vitus Lyamuya (2003), Curthbert Zuberi (2004), Afree Kinyondo (2004) na

Alfred Karere ambaye ndiye kiongozi hadi sasa.

Alisema wakati wanaingia katika vikao vya mwafaka mnamo Juni mwaka jana,

mwenyekiti wao alikuwa Kinyondo ambaye aliondoka madarakani mapema mwaka huu.

 

Ngawaiya: Kukumbatia upinzani ni kurudisha nyuma kimaendele

Na Rodrick Makundi, Vunjo

MPIGA debe maarufu wa CCM, Thomas Ngawaiya amewaambia wananchi wa jimbo la Vunjo

kuwa kuendelea kukumbatia upinzani kutachelewesha shughuli za maendeleo na

kuwasababishia kuendelea kuishi katika mazingira magumu kwa kukosa huduma muhimu.

Akitolea mfano, Ngawaiya alisema wakati akiwa TLP alishindwa kutekeleza majukumu

yake ya kuwatumikia wananchi kwani alitofautina na mwenyekiti wake wakati wa

kufanya mipango ya kuhudumia waliompigia kura.

Akaongeza kuwa yeye na Mrema walipanga mambo mengi ambayo utekelezaji wake

ulikuwa mgumu kwani hawakuwa na serikali, huku kukiwa na mikingamo mingi

iliyojitokeza baina ya viongozi hao wawili hivyo kuishia kwenye migogoro huku

wananchi waliomchagua wakisahaulika.

Alisema wanaong'ang'ania upinzani ni kwa maslahi yao binafsi na sio kwa maslahi

ya wananchi: "Mimi nilipokuwa mbunge nasema kabisa mshahara wangu nilikuwa napata

lakini linapofika suala la kuwahudumia wananchi niliambiwa nenda kwa baba yako

Mrema akakupe msaada huo."

"Nataka mjue huwezi kuwa mpinzani ukaleta maendeleo jimboni unapoona Serikali ni

ya CCM na kama mnataka maendeleo muipe kura CCM kwani jukumu la kusambaza huduma

za kijamii limo katika ilani yake," alisema Ngawaiya.

Hivyo aliwataka wananchi wa jimbo la Vunjo kuhakikisha kuwa wanampa kura mgombea

wa eneo hilo Aloyce Kimaro na madiwani ili washirikiane na mgombea wa Moshi

vijijini Dk. Cyril Chami waweze kusukumu mbele maendeleo yaliyokosekana katika

majimbo hayo kwa muda mrefu.

 

CCM Chunya wapongezwa kuwezesha wabunge kupita bila kupingwa

Na Bashir Nkoromo, Chunya

CHAMA Cha Mapinduzi kimeupongeza uongozi wa Chama wilayani Chunya kwa wagombea wa

majimbo yote mawili wanaowania ubunge kwa tiketi ya CCM wilayani humo, kupita

bila kupingwa.

Pongezi hizo zilitolewa kwa nyakati tofauti na Katibu Mkuu wa CCM, Philip Mangula

akihutubia mikutano ya kampeni kwa ajili ya wabunge hao waliopita bila kupingwa

katika majimbo ya Songwe na Lupa.

Victor Mwambalasa amepita bila kupingwa katika jimbo la Songwe na Dk. Gido

Singonda amepita Lupa lililokuwa la mbunge wa zamani, Njelu Kasaka ambaye baada

ya kutoteuliwa kugombea tena ametimkia CUF.

"Hii imetokana na mikakati yenu mizuri mliyoonyesha, ujenzi wa Chama na

utekelezaji wa dhati wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000 ndiyo sababu hata

vyama vya upinzani vikaridhika kuwa havina sababu ya kuweka wagombea katika

majimbo yenu," alisema Mangula na kuongeza kwamba huo ni mtaji mwingine ambao CCM

itaingia nao katika uchaguzi.

Alivipongeza na kuvishukuru vyama vya upinzani kwa busara ya kuikubali CCM na

kuamua kuipa nafasi ya kuweka wabunge wake ili iweze kuendeleza uletaji wa

maendeleo ya nchi wakati katika awamu nyingine.

Pia Mangula alimpongeza Njelu Kasaka kwa uamuzi wake wa kutangaza kujitoa CCM

baada ya kudhani ameonewa kutopewa kugombea tena jimbo la Lupa.

"Kwa hakika nampongeza Kasaka kwa uamuzi wake maana amekuwa muwazi. Maana wapo

wengine wasiporidhika na maamuzi ya ngazi za juu ya Chama huendelea kujifanya

wako nasi huku wakitusaliti ili tukose ushindi. Wanakuwa CCM mchana kumbe usiku

wapinzani," alisema.

Mangula ambaye alihutubia katika maeneo ya Tewe, Makongolosi na Mkwajuni, alisema

ni wale tu wasio na macho ndio bado wana hamu ya kuipinga CCM isiendelee kushika

dola kwa sababu tangu TANU imekwishafanya mengi katika kipindi chake cha miaka 43

ya utawala.

Alisema wananchi wasibabaike na vyama vya upinzani kwa kuwa ni timu zilizoingia

uwanjani zikiwa hazina kocha tofauti za CCM ambayo kocha wake yupo ambaye ni

Ilani ya Uchaguzi ya 2005 ambayo imeandikwa kwa makini na inatekelezeka.

Mangula aliwataka wananchi kutochoka baada ya uchaguzi kusimamishwa kwa mujibu wa

sheria kutokana na kufariki dunia aliyekuwa mgombea mwenza wa Chadema, badala

yake waendeleze mshikamano na kujitokeza kwa wingi kuipigia kura CCM wakati wa

uchaguzi utakaofanyika Desemba 14 mwaka huu.

 

 

Mpiganaji wa JKU aliyeuawa Pemba azikwa

Na Mwandishi Wetu

MPIGANAJI wa Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU), Shariff Salim, aliyeuawa baada ya

kutekwa na wanakijiji cha Piki kisiwani Pemba amezikwa.

Kwa mujibu wa kipindi cha mawio kilichorushwa jana asubuhi na Sauti ya Tanzania

Zanzibar na kusikika jijini Dar es Salaam, mwili wa marehemu Salim ulizikwa juzi

mchana kijijini kwao, Chambani, mkoa Kusini Pemba.

Mwili wake ulikutwa eneo la Penjewani, Piki ukiwa umefukiwa kwenye tope na kisha

kufunikwa makuti juu yake huku kofia yake ikiwa imewekwa mfukoni mwa suruali yake

ya kijani ambayo ilikuwa sare ya jeshi hilo.

Kuhusu kifo hicho, uchunguzi uliofanywa kwa ushirikiano kati ya madaktari wa

hopsitali ya Wete na wenzao kutoka Tanzania Bara umebainisha askari huyo alikufa

baada ya ubongo wake kuchanganyika na damu.

Taarifa ya kipindi hicho pia ilieleza kuwa, damu hiyo ilitokana na Salum kuvunjwa

fuvu la kichwa baada ya kupigwa kwa kutumia kitu kizito kichwani. Pia alivunjika

mbavu. Marehemu ameacha mjane na watoto watano.

Salim alikufa kutokana na kipigo baada ya kutekwa na wananchi wa kijiji hicho

Novemba Mosi mwaka huu kutokana na kushindwa kukwepa vizuizi vilivyowekwa

barabarani wakati akitokea kambi ya JKU, Msaani kwenda kambi ya Chambani.

Akizungumza baada ya mazishi hayo, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Fakih Dadi

Fakih alilaani mauaji hayo na kuahidi Jeshi la Polisi litaendelea kuwasaka

wahalifu waliohusika na kifo hicho.

 

 

Sumaye awanadi wagombea wa CCM Moshi Vijijini na Vunjo

Na Rodrick Makundi, Moshi

WAZIRI Mkuu Fredrick Sumaye, amekutana na wananchi wa majimbo ya Moshi Vijijini

na Vunjo, katika ziara yake ya siku mbili mkoani hapa, ambapo alitumia nafasi

hiyo kuwanadi wagombea ubunge na udiwani kwenye kata zao alizotembelea wilayani

Moshi Vijijini.

Katika jimbo la Moshi Vijijini Sumaye ambaye pia ni mlezi wa chama mkoa wa

Kilimanjaro, aliwahutubia wananchi wa kata ya Kibosho Magharibi,eneo la Mlama,na

aliwataka wananchi wa eneo hilo kuipa CCM kura ili kutekeleza mipango ya

maendeleo ambayo yamo katika ilani ya uchaguzi ya Chama.

Alisema kuwa pamoja na kuwa na mfumo wa vyama vingi, asilimia kubwa ya Watanzania

wanaamini kuwa CCM itashinda katika nafasi ya urais kwa asilimia kubwa wakati

nafasi za wabunge na madiwani zitachukuliwa na chama hicho pia kwa asilimia kubwa

katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Katika kauli yake hiyo Waziri Mkuu Sumaye alidai kuwa wapinzani wenyewe wanaamini

kuwa rais ajaye ni wa CCM,na kwamba serikali itakayofuata itakuwa ni ya CCM,na

kwamba ilani itakayotekelezwa kwa kipindi chote hicho ni ya CCM.

“Yeyote yule kama ni mpinzani ukimuuliza rais ajaye ni nani atakuambia ni

Kikwete, na anafahamu wapinzani hawawezi kuwapata urais, hata wao wenyewe

wanaogombea wanatambua hilo,sasa sioni kwa nini wapinzani wasiipigie kura

CCM,maana Kikwete atakuwa rais tu,” alisema Sumaye.

Aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo viongozi wa serikali na Chama watatekeleza

ilani ya chama tawala, huku watendaji wake wakuu wakiwa ni viongozi kutoka ndani

ya chama kwani kwa kuweka kiongozi wa upinzani atapingana na ilani.

Hivyo akawataka wanachama wa Moshi Vijijini kumpigia kura mgombea wa CCM katika

nafasi ya ubunge ambaye atashirikiana na rais katika kuwaletea mandeleo wananchi

wa jimbo hilo.”Mtupe Dk.Chami kama tukishindwa kutekeleza haya tunayosema basi

mtusute”.

Alisema kuwa anaamini kuwa Dk. Chami atakuwa mbunge atakayetekeleza ilani ya

Chama katika jimbo hilo kwani ameonyesha hilo kwa kuweza kutoa ushauri wake

unaohusu masula ya kiuchumi kwenye serikali ya Rais Mkapa, ushauri ambao

umeonyesha mafanikio makubwa katika kukua kwake.

Pia aliwaambia wananchi hao kuwa madai ambayo yanatolewa dhidi ya Dk. Chami sio

ya kweli bali yamelenga kumchafua kwa lengo la kumkosesha kura wakati wa

uchaguzi.

"Hawa wanaosema kuwa Dk.Chami ni mfagiaji wa ofisi ya rais wana yao na hii ni

kukosa sera, mimi nawathibitishia kuwa ni mtu mwenye digirii mbili za uchumi na

serikali inalitambua hilo,sasa hao wanataka kuwapotosha ili muwape kura,” alisema

Waziri Mkuu.

Akatoa takwimu katika uchaguzi wa mwaka 2000,kuwa CCM ilishinda viti 202,wakati

upinzani walishinda viti 14,ushindi ambao ni wa asilimia zaidi ya 96,na

kutahadharisha kuwa huenda idadi ya viti vya upinzani bungeni ikapungua kwa mwaka

huu.

“Haya makelele yote wanayopiga hawa wapinzani na hata kufanya maandamano na fujo

ni katika kutetea viti hivyo kumi na vinne tu,na nina wasiwasi mwaka huu huenda

hata viti vitano wasipate,” aliongeza Sumaye.

Alipozungumza mara baada ya utambulisho, Dk. Chami alimhakikishia Waziri Mkuu

kuwa CCM katika jimbo la Moshi Vijijini linafanya kampeni za utulivu pamoja na

kuwa na maneno ya kashfa na kejeli yanayotolewa na wapinzani jimboni humo.

Akasema kuwa maneno kama hayo yamefanya wagombea wengi wa udiwani na hata ubunge

kuamua kuvihama vyama hivyo kwena CCM,kutokana na kejeli hizo badala ya kueleza

sera za vyama vyao wakati wa kampeni.

Hata hivyo,aliwataka wanachama wa CCM,kuendeleza ushirikiano uliofanywa wakati wa

kampeni kabla ya kuahirishwa kwake,kwa kutofanya fujo,au kujibu tuhuma za

wapinzani kwani hali hiyo inaweza kutia doa chama,hivyo kupoteza sifa kwa wapiga

kura wake.

Kwa upande wa mgombea wa Vunjo Aloyce Kimaro aliwataka wananchi na wanachama wa

CCM jimboni humo kuipigia kura CCM,ili iweze kutekeleza ahadi zake za maendeleo

na ambazo zimo kwenye ilani ya uchaguzi wa mwaka huu.

Alisema tangu upinzani kulishikilia jimbo la Vunjo kumekuwa mahitaji duni ambapo

miundombinu kama barabara,huduma za maji,afya na nyinginezo hazijaweza kuwa za

kiwango cha kumtosheleza kila mwananchi.

Alisema kuwa CCM ina nia thabiti katika kuyatekeleza mambo hayo,ambapo wananchi

wanalo jukumu kubwa la kuipigia kura ili iwe na nafasi ya kuonyesha hayo.

 

 

 

UVCCM Shinyanga Vijijini wampongeza Karume

Na Anthony Komanya, Shinyanga

UMOJA wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi, wilaya ya Shinyanga Vijijini wamempongeza

Rais Amani Abeid Karume, kwa ushindi wake mnono uliomwezesha kuendelea kushika

kiti cha Urais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Katibu wa UVCCM Shinyanga Vijijini, Richard Pambe, alisema ushindi huo wa Rais

Karume, unadhihirisha jinsi wananchi wa Tanzania kwa jumla walivyo na imani na

uongozi wa CCM.

Umoja huo pia umelaani kitendo cha wafuasi wa chama cha Cuvic United Front (CUF),

kuwashambulia na kuwadhuru waandishi wa habari mapema mwezi huu.

Novemba 5 kwenye Makao Makuu ya CUF, eneo la Buguruni, jijini Dar es salaam,

waandishi wa ITV, Chanel Ten, na Star tv, walishambuliwa na vitendea kazi vyao

kuharibiwa na watu wanaodhaniwa kuwa wafuasi wa CUF.

 

Ujenzi wa benki ya damu waanza Tabora

Na El-hadji Yuusuf, Tabora

UJENZI wa kituo cha utunzaji wa damu salama umeanza kufanyika katika hospitali ya

mkoa wa Tabora ya Kitete, ambao unatarajia kukamilika katika kipindi cha miezi

mitatu ijayo.

Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa wa Tabora, Dk. Amos Nsheha, alisema ujenzi huo

unaofanywa na Shirika la Msalaba Mwekundu Duniani utasaidia wagonjwa wanaohitaji

kupatiwa damu katika hospitali hiyo kupata damu salama.

Alisema damu itakayokuwa ikihifadhiwa katika kituo hicho, itakuwa salama kwa

sababu itaangaliwa kama haina ugonjwa wowote wa kuambukiza ambao unaweza

kusababbisha madhara kwa mgonjwa.

Dk. Nsheha alisema katika kituo hicho kutakuwa na mashine ya kisasa za kupima

damu ili kuifanya iwe salama na kuzuia maambukizi ya magonjwa yanayoweza kutokana

na mtu kuongezewa damu.

Alisema hata hivyo benki hiyo ya damu katika siku za mwanzo itakuwa ikipokea damu

inayochunguzwa katika hospitali ya Bugando, ambayo kwa sasa ndiyo yenye kituo cha

kisasa cha uchunguzi wa magonjwa katika mikoa ya kanda ya kati, ziwa na

magharibi.

Alisema kuwa kituo hicho kinatarajia kuwahudumia wakazi wa mikoa ya Tabora,

Rukwa, Singida, Shinyanga, Kigoma na Dodoma.

Hata hivyo, Dk Nsheha, hakuweza kueleza gharama halisi zinazotumika katika ujenzi

wa kituo hicho, lakini alisema mkandarasi kwa ajili ya kuanza kazi hiyo

amekwishafika mkoani Tabora.

Wakati huo huo, hospitali ya Kalunde inatarajia kuanza kazi ya utoaji wa huduma

kwa wagonjwa Jumatatu wiki ijayo, baada ya ukarabati uliokuwa ukifanyika katika

hospitali hiyo kukamilika.

Dk. Nsheha, alisema ukarabati huo umefanyika kwa kipindi cha miezi sita,

ulifanywa baada ya hospitali hiyo kuwa katika hali mbaya, kutokana na kuwa na

majengo chakavu na kutokuwa na vifaa vya kisasa kwa ajili ya utoaji wa tiba.

 

"Hamasisheni kupata ushindi wa kishindo'

Na Eva Musiba, Mwanza

KATIBU Umoja wa Vijana Mkoa wa Mwanza Ghati Abubakar amewataka vijana wasibweteke

kwa kudhani kuwa CCM tayari imeshinda na kuwa wafanye uhamashishaji ifikapo

Desemba 14 kuhakikisha Chama kinashinda kwa kishindo.

Aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na viongozi mbalimbali wa umoja huo katika

ofisi za Chama, zilizoko uwanja ya CCM Kirumba jijini hapa.

Ghati amewaasa vijana kudumisha amani iliyoachwa na wasisi wa Taifa hili, kwani

nchi mbalimbali zinazipigana, vijana ambao ndiyo wenye nguvu wanaathirika zaidi

ikiwemo pia na wanawake, watoto na wazee.

Aliwataka vijana kuwa wadadisi na kutekeleza majukumu ya kufanya kazi za Chama

kwa uaminifu na kuhakikisha wapinzani wanarejea CCM katika hali ya utulivu na

amani.

Akizungumzia kuhusu chipukizi aliwataka viongozi kuahakikisha wanapata mafunzo ya

malezi bora, usafi na tabia njema ili kuwaandaa kuwa viongozi wema na waadilifu.

 

Kanisa Anglikana sasa kuongeza idadi ya watoto yatima inaowasomesha

Ni kutoka 92 hadi 250

Na Solomon Mwansele, Mbeya

ASKOFU wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kusini, John Mwela amesema kanisa lina

mpango wa kuongeza idadi ya watoto yatima linaowasomesha kutoka 92 hadi kufikia

250 ifikapo mwaka 2007.

Aliyasema hayo jana wakati akikabidhi msaada wa sare za shule na vyakula kwa

watoto yatima katika kata ya Ghana iliyopo jijini hapa.

Askofu Mwela alisema kwa sasa kanisa hilo linawasomesha wanafunzi 92 kuanzia

elimu ya msingi na kwamba wanafunzi watatu wanasomeshwa chuo kikuu na chuo cha

mipango na kwamba kanisa limeanzisha miradi ili liweze kuwahudumia yatima wengi

zaidi.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Moshi Chang'a akizungumza katika hafla hiyo,

alikemea tabia ya baadhi ya wanawake wasiotaka kuwajibika na waliokata tamaa na

kuwaacha watoto wao wawe ombaomba mitaani wakati wanao uwezo wa kuwalea.

Alisema Mkoa wa Mbeya unaoonekana kuwa una idadi kubwa ya watoto yatima kutokana

na kutofanyika kwa utafiti kubaini wapi kati yao ni watoto yatima wenye kuhitaji

msaada na ambao wanao walezi wenye uwezo lakini wamewatelekeza.

"Watu wengi wamewekeza katika kuchangia sherehe na mashindano yasiyo na na

manufaa kwa jamii huku wakiwaacha watoto wao wakizurura mitaani na kukosa haki

zao za msingi," alisema Chang'a.

Mkuu huyo wa wilaya alisema ni aibu kuona baadhi ya watu wanaona ni heshima kuwa

na watoto yatima na kutafuta misaada, wakati uwezo wa kuwalea wanao na kuwa

misaada kwa yatima itolewe baada ya kufanyika utafiti wa kina ili wenye shida

wasaidiwe.

 

Wito kwa wana-Korogwe kuungana na kuunda klabu

Na Esther Katua

WANANCHI wa Wilaya ya Korogwe waishio maeneo mengine ya nchi wametakiwa kuungana

na kuunda klabu kwa lengo la kuchangia maendeleo ya wilaya hiyo.

Hayo yalisemwa jana na Makamu Mwenyekiti wa Klabu ya wanananchi wa Korogwe

waishio Dar es Salaam Luteni Kanali Iddi Kipingu alipokuwa akizungumza na

waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) mjini Dar es

Salaam

Kipingu ambaye alizungumza kwa niaba ya mlezi wa klabu hiyo, Luteni mstaafu Yusuf

Makamba alisema wanachama waliokutana hivi karibuni wamechagua viongozi wa muda

kwa ajili ya kuongoza klabu hiyo.

Aliwataja viongozi wa muda waliochaguliwa na nafasi zao kwenye makano kuwa ni

Makamba (Mlezi), Martin Mvaa (Mwenyekiti), Kipingu ( Makamu Mwenyekiti), Nicholas

Kingazi ( Katibu) na Issa Lupatu (Mhazini).

Wengine ni wajumbe watano, Profesa Maurice Mbago, Christopher Shekiondo, Ayubu

Mbegha, Hemed Kimea na Maurice Sapanjo.

Alisema kuwa klabu inaandaa katiba rasmi kwa ajili kuisajili kwa mujibu wa

taratibu za kisheria.

Kipingu alisema wanananchi wa Korogwe waishio mikoa mbalimbali nchini hawana budi

kuanzisha klabu kama iliyoanzishwa Dar es Salaam kwenye mikoa wanayoishi na

kuchangisha fedha kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya wilaya ikiwa ni pamoja na

ujenzi wa shule na hospitali.

Alisema wana-Korogwe waishio Dar es Salaam wameamua kuanzisha klabu hiyo kwa

lengo la kuendeleza vitu mbalimbali vilivyokufa wilayani humo ikiwemo mazao ya

biashara.

"Kwenye klabu hii iliyoanzishwa juzi, tumeazimia kumalizia ujenzi wa madarasa

manne kwenye shule ya Sekondari ya Chifu Kimweri ili kuokoa wanafunzi wanaokosa

nafasi ya kujiunga na sekondari pamoja kuwa wamefaulu," alisema Kipingu.

Alisema mbali na ujenzi wa madarasa hayo manne, wanachama waliazimia kukarabati

jiko la hospitali ya wilaya ya Magunga ambalo ni bovu.

" Pamoja na uchache tuliokuwa nao lakini kwa kuwa tulikuwa na malengo,

tulifanikiwa kuchangishana sh. 5,580,000 na hii ni kwa ajili ya kumalizia ujenzi

wa madarasa manne na tunawaomba wenzetu wengine wajitokeze hasa wa mikoa mingine

kwa ajili ya kufanikisha lengo letu," alisema Kipingu.

Alisema shule hiyo ya Chifu Kimweri, iliyoanza kujengwa mwaka jana ina madarasa

mawili ambayo yana wanafunzi wanaopaswa kuingia kidato cha pili mwakani, hivyo

inawalazimu kujengwa madarasa mengine mawili ili wanafunzi hao wapate madarasa ya

kuhamia na kuwapisha wanafunzi wapya wa kidato cha kwanza mwakani.

Kipingu alisema ili shule ikamilike zinahitajika jumla ya sh. milioni 25.

 

Mgodi wa Kiwira mfano bora wa uwekezaji - Mangula

Na Bashir Nkoromo, Mbeya

KATIBU Mkuu wa CCM, Philip Mangula amesema mgodi wa Mawe wa Kiwira mkoani Mbeya

hapa ni kielelezo cha mfano bora wa uwekezaji.

Mangula alisema hayo juzi alipotembelea mgodi huo wakati akielekea wilaya ya

Rungwe kuhutubia mikutano ya kampeni katika majimbo ya Rungwe Magharibi na Rungwe

Mashariki .

Alisema tangu mgodi huo uwe chini ya mwekezaji kampuni ya Tanpower Resources

Limited, umekuwa na mafanikio.

Akipatiwa maelezo kuhusu mgodi huo, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Evans Mapundi

alisema sasa una wafanyakazi zaidi ya 4,000 na ndio unaoipatia gridi ya Taifa

umeme unaokwenda Tukuyu, Mbeya na Kyela.

Akieleza mipango ya baadaye Mapundi alisema, mgodi una mpango wa kuanzisha

uzalishaji wa gesi mwakani au mwaka 2007.

Alisema, awali mgodi ulikuwa ukimilikiwa na

STAMICO lakini baadaye ukabinafsishwa kwa Wachina ambao nao wameuza hisa na

kujindoa na sasa unaendeshwa na kampuni yake kwa ushirikiano wa kampuni nyingine

tatu.

Alisema, binafsi anaona fahari mgodi huo kupiga hatua kwa sababu ni sehemu ya

utekelezaji wa Ilani ya CCM ambapo sehemu kubwa ya hisa na wafanyakazi ni

wazalendo wa hapa nchini.