UHURU 19.11.2005

 

Wakulima Mtwara wafungia korosho ndani

  • Wagoma kupunjwa bei na wafanyabiashara
  • Wasema wanaendelea kushikamana na CCM

Na Rashid Mussa, Masasi

WAKULIMA wa korosho nchini, msimu huu wamekataa kuwauzia wafanyabiashara kwa

sababu wamekiuka makubaliano yaliyokuwa yamefikiwa ya kwamba bei ya kilo moja

isiwe chini ya sh. 600.

Makubaliano ya bei hiyo ya sh. 600 kwa kilo yalifikiwa katika mkutano wa pamoja

uliofanyika Septemba 18, mwaka huu mjini Mtwara.

Uamuzi huo wakulima kugoma kuuza korosho zao kwa wafanyabiashara ulifikiwa jana

katika mkutano wa wadau wa korosho nchini uliyofanyika mjini Masasi ambapo

wakulima hao kutoka wilaya mbalimbali walitaka matatizo yaliyojitokeza katika

ununuzi msimu huu yasihushwe na uchaguzi kwa kuishutumu serikali ama chama

chochote cha kisiasa.

Kufuatia uamuzi huo ambao ulikuja baada ya upande wa wafanyabiashara kuweka

msimamo mkali ulioonekana kuwadhalilisha wakulima wa kutotaka kujadiliana kiwango

cha bei mpya waliyoweka wao cha sh. 400 kwa kilo moja, wakulima wameiomba

serikali kupitia wizara yake ya ushirika na masoko kushughulikia tatizo hili ili

kupata ufumbuzi wa haki.

Mkutano huo uliwalaani wafanyabiashara hao kwa kutaka kuwachonganisha wananchi na

serikali ili ionekane haimjali mkulima na kutaka kutumia uwezo wao kuvuruga

uchaguzi ama kusaidia baadhi ya vyama vya siasa kwa kuwapa hoja ya kushuka kwa

bei itumike katika kampeni.

Mkulima mmoja kutoka Ruangwa, alishangiliwa na umati mkubwa wa wakulima hao

alipochangia kuwa wao watabaki na korosho zao na kwamba wanatambua kuwa suala

hilo siyo la CCM, na kwamba wataendelea kuwa na imani na chama hicho na kukipa

kura katika uchaguzi ujao.

Mkutano huo uliokuwa chini ya uenyekiti wa mkulima kutoka Tandahimba, Adinani

Bakari Mbwana na mwenza wake mfanyabiashara Arom Amar wa Kampuni ya Olam

Tanzania, wakulima walikubaliana kubaki na korosho zao majumbani kuliko kuliko

kuuza kwa bei hiyo wanayotaka wanunuzi.

Nao wafanyabiashara wakizungumza na mwandishi wa habari hii mara baada ya mkutano

kuvunjika, walisema wamefadhaishwa na msimamo mkali wa wakulima katika mkutano

huo na kwamba hawana la kufanya na kwamba wamekwishawasiliana na wanunuzi wao

waliyo kwenye vituo vya ununuzi kusimamisha na kuondoka.

Hali hii ikiwa na maana kuwa msimu wa ununuzi wa korosho mwaka huu umevurugika,

ambapo habari kutoka vijijini zinasemekana kuwa wapo baadhi ya wakulima wanaouza

korosho zao kwa kati ya sh. 150 kwa kilo hadi 400 kutokana na dhiki na matatizo

makubwa yanayowakabili wakati huu.

Wakulima waliwakilishwa katika mkutano huu na viongozi wao wa vyama vya ushirika,

na wengine binafsi waliokuja kwa malori, mabasi kutoka wilaya mbalimbali za mikoa

ya Mtwara, Ruvuma na Lindi wakiwemo viongozi wa serikali wa wilaya na mikoa,

waliwashtumu wafanyabiashara hao kwa kushusha bei kiholela bila kufuata taratibu

walizojiwekea.

Karibu wazungumzaji wote kutoka wilaya mbalimbali waliokuja kwa gharama zao

walidai kuwa wamechoka kudhalilishwa na wafanyabiashara hao kila mwaka bila

kujali shida na matatizo yanayomkabili mkulima wa korosho miaka hii ambapo

gharama za uzalishaji zinapanda kila mwaka.

Wafanyabiashara hao ambao nao kampuni zao karibu zote zilituma wawakilishi katika

mkutano huu kwa mujibu wa barua waliyoiandikia CBT na kutolewa maelezo katika

mkutano huu na mwenyekiti mwenza Amar wameshusha bei kutoka sh. 600 kwa kilo moja

hadi sh. 400 kwa madai ya bei soko la nje imeporomoka sana.

Hata hivyo, madai hayo yalishindwa kuthibitishwa katika mkutano huo kwa kukosa

vielelezo ambapo bodi ya korosho nchini CBT ilitoa vielelezo vya kuonyesha bei ya

nje ya zao hili kwa sasa imethibitika kuwa haijashuka kwa kiwango hicho

lilichokuwa kinadaiwa cha dola za Kimarekani 200 kwa tani.

Bodi ya Korosho iliwasilisha vielelezo vinavyoonyesha kuwa tani moja katika soko

la India inakouzwa ni kati ya dola za Kimarekani 800 hadi 825, wakati

wafanyabiashara hao walidai kuwa wameambiwa na wanunuzi wao huko India kuwa ni

dola za Marekani 700.

Kufuatia malumbano hayo yalifanya kikao hicho kuvunjika kabla ya kufikia mwafaka

wa bei mpya baada ya mwenyekiti mwenza ambaye anatoka upande wa wafanyabiashara

kukataa kujadiliana ili kupata bei mpya badala hiyo ya sh. 400 ambayo wakulima

wanadai kuwa ni ya chini mno itakayoua kilimo cha zao hili kwa kulinganisha na

gharama.

 

 

Anayedaiwa jambazi sugu ajisalimisha polisi Dar

MMOJA wa watuhumiwa wa matukio ya ujambazi na uporaji kwenye mabenki, Sixtus

Alfred Ngowi (42) mkazi wa Dar es Salaam anashikiliwa na polisi baada ya

kujisalimisha jana kwenye Kituo Kikuu cha Polisi mjini Dar es Salaam.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam, Alfred Tibaigana alisema jana kuwa Ngowi

alijisalimisha jana mchana na alikuwa anahojiwa na polisi kuhusiana na matukio

mbalimbali ya ujambazi.

“Amejisalimisha leo (jana) mchana na tunaendelea kumhoji kutokana na matukio

mbalimbali ya ujambazi kwenye benki mbalimbali jijini,” alisema Tibaigana.

Novemba 11, mwaka huu, Kamanda Tibaigana alitangaza kuwatafuta watu watatu

wanaodaiwa kuwa watuhumiwa sugu wa matukio ya ujambazi ikiwemo uporaji kwenye

mabenki.

Watuhumiwa wengine waliotangazwa kutafutwa pamoja na Sixtus ni mkewe ambaye jina

lake halikutajwa, Abulkarim Mongi (37) ambaye ilidaiwa kuwa makazi yake

hayajulikani na Sadiki Fatee mkazi wa Muheza mkoani Tanga ambaye umri wake

haukufahamika.

Alisema kuwa watuhumiwa wote wanaonekana mara kwa mara Dar es Salaam, Arusha,

Nairobi na Moshi mkoani Kilimanjaro na kwamba wanahusishwa na wizi wa sh. bilioni

1.6 kutoka Kampuni ya Security Group ambayo wafanyakazi wake na watuhumiwa

wengine 18 wana kesi inayoendelea katika Mahakama ya Kisutu.

Ngowi anamiliki kituo cha vinywaji baridi kiitwacho Cold Cap kilichopo jijini Dar

es Salaam, ambapo mkewe ambaye hadi sasa amejificha, anatafutwa kwa tuhuma za

kushirikiana na mumewe baada ya nyumbani kwake kukutwa kasha la fedha lililoibwa

kwenye Kampuni ya Security Group.

Polisi inaendelea kuwatafuta Fatee na Mongi.

 

DC Chunya atoa changamoto CHUTCU kujenga sekondari

Na Mwandishi Wetu, Chunya

MKUU wa Wilaya ya Chunya, Frank Uhahula, ametoa changamoto kwa Chama Kikuu cha

Wakulima wa Tumbaku wilayani humo (CHUTCU), kujenga shule za sekondari kwa ajili

ya kuwapatia watoto wao nafasi za kuendelea na masomo ya sekondari.

Alisema hayo jana alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa chama hicho chenye

jumla ya muungano wa vyama 18.

Uhahula alisema inasikitisha kuona wakulima wamekuwa wakiuza tumbaku vizuri na

kupata fedha lakini wilaya hiyo ina shule nne tu za sekondari na watoto wamekuwa

wakihangaika kutafuta shule katika maeneo mengine au kukosa kabisa na kuwa

wazururaji.

"Katika jimbo hili la Lupa kuna shule moja tu ya sekondari... pesa tunapata

lakini hatujui kuzitumia, ni vizuri tukawekeza katika elimu kwa watoto wetu ambao

ndiyo watakuwa viongozi na wakulima wenye elimu hapo baadaye," alisema.

Alliwataka wakulima hao kuongeza mchango wao katika elimu na kuachana na sh. 10

wanayotoa katika mfuko wa maendeleo ya elimu wauzapo mazao yao ambapo alisema

kiwango hicho cha pesa ni kidogo sana kwani kilipangwa miaka 10 iliyopita.

"Mfikirie kuongeza ili kwa kusaidiana... tutakwenda haraka, kwani bado tunatambaa

hata kutembea hatujaanza," alisisizia na kusema kuwa kipato cha mauzo ya tumbaku

hivi sasa kimeongezeka lakini hakilingani na maisha halisi ya wakulima na familia

zao.

Aliwataka viongozi wa vyama hivyo kushirikiana na serikali katika kutoa elimu kwa

wakulima kwa ajili ya matumizi mazuri ya fedha wanazozipata badala ya kuishia

vilabuni huku watoto na familia zao zikikosa huduma muhimu.

Alisema siyo tu masuala ya elimu, wakulima wanapaswa kufikiria pia huduma

wanazozihitaji wilayani humo badala ya kuitegemea serikali peke yake.

Alivitaka vyama hivyo pia kuanzisha mpango na mafunzo ya utunzaji mazingira,

kwani kilimo cha tumbaku kimekuwa ni adui mkubwa wa Mazingira. Aliwataka wakulima

wa tumbaku kupanua mashamba yao ya miti ambayo imekuwa ikikatwa kila wakati kwa

ajili ya ukakushaji wa tumbaku.

"Ni muhimu mkasimamia program ya hifadhi ya mazingira ili tusiendelee kukata

misitu yetu ovyo na kusababisha ukame hapo baadaye," alisema Uhahula na kuwataka

wakulima hao sasa kuanza kutumia teknolojia ya kisasa ya ukaushaji tumbaku badala

ya kutumia magogo ya miti.

 

 

Kanisa Katoliki Songea ‘laiangukia’ serikali

  • Ni kutokana na kuhubiri siasa kanisani

Na Mwandishi Wetu

Kanisa Katoliki jimbo la Songea, limeiangukia serikali ya mkoa wa Ruvuma na

kuomba radhi kufuatia kujiingiza kwenye siasa, kwa kuonekana likimfanyia kampeni

waziwazi mmoja wa wagombea wa vyama vya upinzani.

Hali hiyo ilionekana hapa kuhatarisha amani katika kanisa hilo kutokana na

waumini kuwazomea viongozi wake, hususan mapadre wakati wa ibada.

Akiomba radhi kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Meja Jenerali mstaafu Saidi Kalembo,

ofisini kwake jana, Mwenyekiti wa Baraza la Walei la Kanisa hilo, Ernest Haule,

alisema Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Songea, halitarudia tena kuhubiri siasa

kanisani na kwamba litaendelea na mahubiri ya kiroho kwa misingi ya haki na

kulinda heshima ya kanisa hilo.

Mwenyekiti wa baraza hilo ambaye aliongozana na

wajumbe wawili, alikutana na mkuu wa mkoa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa

wa Ruvuma, ambao kwa pamoja walisisitiza kanisa hilo kuacha siasa na kuwaachia

wanasiasa wenyewe huku kanisa likiwa katikati ya wote.

Jumapili iliyopita kanisa hilo liliwaomba radhi

waumini wake kutokana na mtafaruku uliolikumba kwa muda wote tangu kampeni zianze

kutokana na kanisa kujitumbukiza kwenye mahubiri ya kisiasa hali iliyosababisha

amani kanisani hapo ivunjike.

Pia, hali hiyo ilisababisha katika ibada zote waumini kusali chini ya ulinzi

mkali wa polisi wa sare na wasiovaa sare.

Akijibu, Mkuu wa Mkoa, Jenerali mstaafu Kalembo alisema Kamati ya Ulinzi na

Usalama ya Mkoa imefurahishwa na hatua hiyo ya Baraza la Walei kupiga marufuku

mahubiri ya kisiasa katika makanisa yote ya katoliki ambayo ndiyo yanalalamikiwa

na wananchi na waumini na kwamba serikali haina tatizo na madhehebu yoyote ya

dini ilimradi yafuate sheria.

Alionya kuwa serikali haitavumilia kuona amani

Inavunjika, hasa kutokana na wanaosababisha ni viongozi wa dini, badala yake

hatua kali zitachukuliwa endapo hali hiyo itaendelea tena kwa vile madhara yake

ni makubwa kama serikali itakaa kimya.

Jumapili iliyopita waumini wa kanisa hilo walisali chini ya ulinzi mkali wa

Polisi huku wengine wasiovaa sare waliingia ndani ya kanisa na wale waliovaa sare

walikaa nje ya kanisa na waliondoka baada ya ibada kumalizika.

Waumini wa kanisa hilo wamekuwa wakiwatuhumu viongozi wa kanisa hilo kwa

kumfanyia kampeni mgombea ubunge wa CHADEMA, Edson Mbogoro, dhidi ya wagombea wa

vyama vingine vikiwemo CCM, TLP, CUF na NCCR-Mageuzi.

Ujumbe wa kanisa hilo baada ya kumaliza kuomba radhi kwa Mkuu wa Mkoa uliendelea

kuomba radhi Chama cha Mapinduzi, ambapo walipokewa na Katibu wa CCM mkoa wa

Ruvuma, Sarah Oiso, na kamati ya siasa ya mkoa katika ofisi Chama ya mkoa mjini

hapa.

 

Viongozi wa dini ya Kiislamu wampongeza Rais Karume

Na Mwandishi Maalum, Zanzibar

Kadhi Mkuu, Mufti Mkuu na Makadhi wa wilaya za Zanzibar, wamempongeza Rais wa

Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Amani Abeid Karume, kwa

kuchaguliwa tena kuendelea kuiongoza Zanzibar kwa kipindi cha pili cha miaka

mitano.

Pongezi za viongozi hao wakuu wa dini nchini zilitolewa jana wakati walipofanya

mazungumzo na Rais Karume, Ikulu mjini hapa.

Viongozi hao wa dini walieleza kuwa wameridhishwa na kufarajika kutokana na

matokeo ya uchaguzi mkuu wa Zanzibar, ambao uliendeshwa katika mazingira ya amani

na utulivu jambo ambalo wamesema ni kiini cha maadili mema ya dini.

“Katika kipindi hiki kinachofuatia uchaguzi mkuu wa Oktoba 30, wananchi hawana

budi kuzingatia umuhimu wa amani na kutokana na msingi imara wa maelewano na

ushirikiano uliotandikwa kwa kushirikiano na serikali iliyopo madarakani, ni

hatua njema itakayowahakikishia wananchi kuishi kwa maendeleo na mafanikio

makubwa zaidi,” walieleza viongozi hao wa dini katika salamu zao za pongezi.

Ujumbe huo wa watu wanane, uliyoongozwa na Kadhi Mkuu ulimtakia heri na mafanikio

Rais Karume katika juhudi zake za kuwapatia maendeleo wananchi wa Zanzibar.

Rais Karume aliwaeleza viongozi hao wa dini kuwa Serikali ya Mapinduzi ya

Zanzibar siku zote itakuwa tayari kushirikiana na wananchi ili kuimarisha amani

na utulivu.

“Serikali itaendelea kwa hali na mali kusaidia na kushirikiana na viongozi wa

dini ili kuiwezesha jamii kuishi katika maadili mema katika azma yake ya

kuiendeleza kimaisha,” alisisitiza Rais Karume.

Rais Karume aliwapongeza viongozi wote wa kidini nchini kwa kazi kubwa

waliyoifanya na wanayoendelea kuitekeleza katika kuisaidia jamii kuishi kwa

maelewano.

“Mafanikio makubwa yameonekana kutokana na uwezo wenu mkubwa na nia zenu njema

katika kuiongoza jamii kufuata maadili mema, na kusaidia kupata suluhu ya

matatizo mengi ya wananchi katika jamii,” alisema.

Aliendelea kusema kuwa serikali imeridhishwa na kazi inayofanywa na viongozi hao

wa dini na aliwashauri waendele kwa moyo huo huo katika kuwasaidia wananchi

kutatua matatizo yao mbali mbali ya kimaisha. “Tusichoke kupeleka ujumbe wa mambo

mema katika jamii, kwani jambo jema siku zote huzaa mafanikio,” alisema Rais

Karume.

Ujumbe huo uliwakilishwa na Kadhi Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Mussa Makungu Ali,

Mufti Mkuu Sheikh Harith Bin Khelef Bin Khamis, Naibu Kadhi wa Zanzibar, Sheikh

Ali Khatib Mranzi, na Makadhi wa wilaya ambao ni Sheikh Omar Said Omar, Sheikh

Said Mahmood Abdulrahman, Sheikh Omar Mussa Makungu, Sheikh Nyange Omar Ali na

Sheikh Ali Zubeir.

 

Mahitaji ya wananchi muhimu katika kutekeleza MKUKUTA

Na Pendo Mangala, Dodoma

SERIKALI imeshauriwa kwamba ili iweze kutekeleza mkakati wa kukuza uchumi na

kupunguza umaskini nchini (MKUKUTA) kwa wananchi ni lazima ijue mahitaji husika

ya wananchi na namna ya kuyatekeleza.

Ushauri huo ulitolewa jana na Mwenyekiti Mtendaji wa TACAIDS, Meja Jenerali

mstaafu Herman Lupogo, alipokuwa akizungumza na kamati shirikishi za kudhibiti

ukimwi mjini hapa.

Lupogo alisema ni lazima serikali itambue mahitaji muhimu ya wananchi pamoja na

jinsi ya kuyatekeleza ndipo itaweza kwenda sawa na mkakati huo.

Alisema Serikali kupitia viongozi husika ndiyo yenye jukumu la kuyatambua

mahitaji ya wanachi hivyo haina budi kufanya hivyo.

Alisema endapo Serikali itafanya hivyo itaweza pia kutekeleza masuala mbalimbali

ya wananchi ikiwa ni pamoja na kuleta maendeleo ya nchi kwa ujumla.

Alisema viongozi wanatakiwa kujua mahitaji ya jamii kwanza ndipo waanze

kuwaelezea masuala mengine yaliyopo katika jamii husika.

Alisema kiongozi ama mtu yeyote mwenye madaraka ya uongozi anapokwenda kwa

wanachi na kuwakuta hawana mahitaji muhimu ya kijamii ambayo ni maji,afya na

nyinginezo inabidi awasikilize na kujua namna ya kutekeleza matatizo hayo na si

kuanza kuelezea masuala yake ambayo yatawafanya wasiyazingatie.

Aliipongeza Serikali kwakuanzisha mkakati huo wa kukuza uchumi na kupunguza

umaskini (MKUKUTA), kwani ukitumiwa vizuri utasaidia kupunguza umaskini miongoni

mwa jamii na nchi kwa ujumla hasa katika dunia iliyopo ambayo ni ya utandawazi.

 

 

Makamba akemea umwagiliaji wa matofali kwa maji safi

Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Luteni Yusuf Makamba, amelaani tabia ya baadhi ya

wakazi wa jiji hilo, kufuja maji kwa kumwagilia matofali huku kukiwa na idadi

kubwa ya watu wanaokosa huduma hiyo.

Makamba aliyasema hayo jana wakati akifunga mkutano wa Umoja wa Uelimishaji na

Uhamasishaji Umma Sekta ya Maji Tanzania (WEMMA), uliofanyika katika ukumbi wa

mikutano wa Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO) jijini Dar es

Salaam.

Alisema mbali ya kitendo hicho kuwa si cha kiungwana, lakini pia kinakwenda

kinyume na sheria zinazosimamia utoaji wa huduma za maji safi.

Kwa mujibu wa Makamba tabia hiyo haipaswi kufumbiwa macho, hasa ikizingatiwa

kwamba maji hayo yanazalishwa kwa gharama kubwa na hivyo ni vyema yangetumika

kama yalivyokusudiwa.

Alisema gharama za uwekaji wa dawa katika maji na usambazaji wake ni kubwa na

kiwango kidogo kilichopo kinapaswa kutumiwa vyema badala ya kumwagilia matofali

na bustani.

Makamba alisema maji yana umuhimu mkubwa katika maisha ya binadamu na amewataka

wanachama wa WEMMA ambao ni Maofisa Uhusiano wa Mamlaka za Majisafi na Majitaka

Mijini Tanzania, kutumia taaluma yao katika kuielimisha jamii.

Alisema kutokana na umuhimu huo, serikali kupitia Chama Tawala imekuwa ikitoa

kipaumbele katika kuhakikisha huduma za maji zinaboreshwa siku hadi siku, juhudi

ambazo alisema zinapaswa kuungwa mkono.

Mapema akitoa maelezo ya umoja huo, Mwenyekiti wa WEMMA, Sebastian Warioba,

alisema ili kutimiza malengo ya umoja huo, WEMMA itaanzisha programu za pamoja za

elimu na uhamasishaji umma katika sekta ya maji katika masuala ya sera na sheria

zinazosimamia sekta hiyo.

Pia, WEMMA imelenga katika kuimarisha ushirikishwaji wa kinamama katika maendeleo

ya sekta ya maji nchini.

 

 

Tume yamthibitisha Anna Komu kuwa mwenza

Na Mwandishi Wetu

TUME ya Taifa ya Uchaguzi  (NEC) imemtangaza Anna Komu kuwa mgombea mwenza wa 

Freeman Mbowe, katika kusaka urais wa Jamhuri ya Muungano kwa tiketi ya CHADEMA.

Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Lewis Makame, aliwaambia waandishi wa habari jana

kwamba Tume yake imepitia vielelezo vyote vinavyomuhusu Anna na kuridhika navyo,

na kwamba ametimiza taratibu za kisheria.

Alisema pamoja na Tume yake kumtangaza jana, mtu yeyote anayo nafasi ya kupinga

uteuzi huo kisheria katika muda wa saa 24 kuanzia jana hadi leo saa 10 alasiri.

Anna anakuwa mgombea mwenza wa Mbowe kufuatia kifo cha aliyekuwa mgombea mwenza

wake wa awali, Jumbe Rajabu Jumbe, aliyefariki dunia mwishoni mwa mwezi uliopita

na kusababisha uchaguzi uahirishwe kutoka Novemba 30 hadi  Desemba  14, mwaka

huu.

Kuhusu hasara iliyotokea kutokana na kuahirishwa uchaguzi huko, Jaji  Makame 

alisema Tume yake imehitaji fedha zaidi za nyongeza.

Akifafanua zaidi Mkurugenzi wa Uchaguzi, Rajabu Kiravu, alisema gharama ya ziada

sasa itakuwa sh. bilioni 5.3 na kwamba  sh. bilioni 2.1 kati ya hizo ni kwa ajili

ya kuchapisha karatasi za kupiga kura ya Rais, wakati sh. bilioni 3.2 zitatumika

kwa mafunzo yatakayotolewa kwa wasimamizi wa uchaguzi kwa muda wa siku moja.

Wakati  huo huo, kampeni  za uchaguzi mkuu kwa wagombea urais zinaanza tena leo

ambapo vyama vinne vyenye wagombea wa urais vitajitupa kwenye viwanja mbalimbali

kuomba kura.

Chama cha NCCR-Mageuzi leo  kitatumia siku nzima kuomba kura katika mkoa wa

Mtwara, CHADEMA itahangaika kusaka kura Ukerewe na Ilala na Kinondoni mkoani Dar

es Salaam, wakati TLP kitaomba kura mkoani Kilimanjaro,  na chama cha DP kitaomba

kura wilaya ya Kilolo mkoani Iringa.

Ratiba ya kampeni iliyotolewa na Tume inaonyesha kwamba kesho, CCM itanguruma

wilayani Lushoto mkoani Tanga, wakati CUF itakuwa ikihaha mkoani Mwanza na

Morogoro, huku CHADEMA ikiendelea na kampeni wilaya za Ilala na Temeke. Chama cha

SAU kitakuwa jimbo la Ukonga.

 

Ushindi wa CCM unategemea mchango wa wazee - Mapuri

Na Dunstan Bahai, Kondoa

CHAMA Cha Mapinduzi kimesema ushindi mkubwa kinaoutarajia kuupata katika uchaguzi

mkuu utategemea ushiriki na mchango wa wazee.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa Itikati na Uenezi wa CCM Taifa Omar Ramadhan

Mapuri kwenye ziara yake ya siku tatu aliyoifanya wilayani Kondoa. Ziara hiyo

imemalizika jana.

"Wazee kama mnaitakia mema Tanzania mhakikishe CCM inashinda," alisema na

kuongeza kuwa misingi mizuri iliyopo Tanzania ni matokeo mazuri ya sera za Chama

Cha Mapinduzi.

Mapuri ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM

alisemna wazee ni dawa na kwamba kila jambo linalofanikiwa lazima wazee wametie

busara zao na kwamba CCM na serikali yake inathamini michango inayotolewa na

wazee.

Alisema endapo Watanzania watafanya makosa ya kuchagua vyama vya upinzani,

watazorotesha maendeleo ya kijamii yaliyokwishaanza kutekelezwa na CCM na kwamba

hata mipango ya baadaye ya utekelezaji iliyoandaliwa itazorota.

Mapuri alisema ushindi wa kishindo unaotarajiwa utafanikisha kuendeleza yale yote

mazuri yaliyokwisha anzishwa na serikali ya awamu ya tatu.

Kwa mujibu wa Mapuri, CUF inayolilia kushika dola itaipeleka pabaya nchi hii

kwani sera zao ni za visasi na chuki na kwamba CCM itaendelea kudumisha amani,

utulivu, mshikamo wa kijamii na kitaifa na Muungano ambao vyama vingine sera yake

ni kuvuruga hayo.

Hata hivyo alisema kwa uhakika CCM itapata ushindi mkubwa na kwamba imeanza

Zanzibar kinachofuata ni Tanzania Bara.

"Kule Zanzibar tumewanyoa na wembe mkali sana, wamebakia na vipara wanachofanya

ni kuficha vipara hivyo kwa kofia," alisema na kufafanua kuwa uchaguazi ulikuwa

wa huru na wa haki.

 

Japan yatoa msaada kwa sekondari tano za wasichana

Na Mwandishi Wetu

JAPAN imetoa msaada wa sh. milioni 292 kwa shule tano za sekondari za wasichana

kwa ajili ya ujenzi wa mabweni, madarasa na tangi la kuvunia maji ya mvua.

Msaada huo umelenga kupunguza adha wanayoipata wanafunzi katika shule hizo

likiwemo la kupata mimba kutokana na wengi wao kupanga kwenye nyumba za watu

binafsi na wengine wanapokwenda kutafuta maji.

Hati za makubaliano ya msaada huo zilitiwa saini jana mjini Dar es Salaam

nyumbani kwa Balozi wa Japan hapa nchini, kati ya Balozi wa nchi hiyo, Katsuya

Ikeda na wawakilishi wa shule hizo.

Shule zilizonufaika na msaada huo ni za Masasi, iliyopo mjini Masasi mkoani

Mtwara, Songea iliyopo mkoani Ruvuma, Isimani ya Iringa, Myatazo na Nyarubanda

zilizopo mkoani Kigoma.

Shule ya sekondari ya wasichana Masasi imepata sh. milioni 53 kwa ajili ya

ununuzi wa samani, ujenzi wa tangi la kuvunia maji ya mvua na madarasa. Shule

hiyo iliwakilishwa na mkuu wake, Paulina Ndigeza.

Ismani ambayo katika hafla hiyo iliwakilishwa na mkuu wa shule, Dainess Myalla

akifuatana na Mjumbe wa Bodi ya shule hiyo, mbunge wa Ismani na Waziri wa nchi

Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera), William Lukuvi imepata sh. milioni 75.3 kwa ajili ya

ujenzi wa bweni na ununuzi wa samani.

Mkuu wa shule ya sekondari ya wasichana, Songea Mary Kisanji aliiwakilisha shule

hiyo iliyopata msaada wa sh.milioni 66.8 kwa ajili ya ujenzi wa bweni na ununuzi

wa samani

Shule za sekondari Myatazo na Nyarubanda ambazo ziliwakilishwa na Mkurugenzi wa

Shirika la Maendeleo la Kigoma (KDPA), Leonard Soza, mjumbe wa Bodi ya shule ya

Nyarubanda, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Arcado Ntagazwa

zimepata sh.milioni 53.2 kwa ajili ya ujenzi wa bweni moja kila shule.

Katika hali isiyokuwa ya kawaida mwalimu wa kujitolea kutoka Japan, Satomi Miura

anayefundisha katika shule ya sekondari ya Wasichana Masasi alibubujikwa na

machozi ya furaha baada ya kutiwa saini hati za makubaliano ya msaada huo.

Satomi mara baada ya kutiwa saini hati hizo alimfuata Mkuu wa shule hiyo, Paulina

na kumbatia kwa takriban dakika moja huku akibubujikwa machozi ya furaha.

Alipoulizwa na mwandishi wetu sababu iliyomfanya ububujikwe machozi, Satomi

alisema amepata matumaini mapya ya kupatikana maji kwa uhakika shuleni hapo kwa

kuwa tatizo hilo limekuwepo kwa muda mrefu na kusababisha adha kwa walimu,

wafanyakazi na wanafunzi.

Naye Mkuu wa shule ya sekondari Isman, Dainess alisema msaada huo ni ukombozi kwa

shule yake kwa kuwa utasaidia kupunguza tatizo la kupata mimba wanafunzi wake.

Alisema kwa wastani wanafunzi 12 hupata mimba kwa mwaka.

Dainess alisema hali ya taaluma katika shule hiyo ni mbaya kutokana na wanafunzi

kuishi katika nyumba za kupanga za watu binafsi hivyo imekuwa rahisi kupata

vishawishi vya kufanya ngono na kupata mamba.

 

 

Mgombea udiwani wa CHADEMA amfikisha mahakamani wa CUF

Ni kwa madai ya kumuita mchawi

Na Angela Sebastian, Bukoba

MGOMBEA udiwani kwa tiketi ya CHADEMA kata ya Kashai, Conchester Lwamulaza,

amemfikisha polisi mgombea mwenzake wa udiwani kwa tiketi ya CUF, Ramadhan

Bahati, akimlalamikia kuwa amemtukana.

Bahati alifikishwa kituo ha polisi cha mjini hapa jana, akidaiwa kumtuhumu

Conchester katika mikutano yake ya kampeni kwa kudai kuwa mgombea huyo ni mchawi.

Conchester ambaye pia alikuwa diwani wa viti maalum kupitia CHADEMA katika

kipindi kilichopita, anamlalamikia Bahati kuwa alimtuhumu hadharani katika

mkutano kuwa mama huyo ni mchawi kitendo ambacho alisema kimemdhalilisha mbele ya

watu.

Mlalamikiwa Bahati alipozungumza na mwandishi wa habari hizi jana, alikana

kutumia lugha za matusi katika mikutano yake na kudai mgombea mwenzake huyo

amefanya hivyo makusudi kwa lengo la kutaka kumharibia.

Bahati alisema anapanda jukwaani kunadi sera za chama chake na kuelezea yale

atakayowafanyia wananchi pindi akichaguliwa kuwa diwani wa kata hiyo, na kuwa

hawezi kupanda jukwaani kutoa lugha za matusi.

Alisema hakuwahi kutumia lugha za matusi katika mikutano yake na kuwa anazo kanda

zinazorekodiwa katika kila mkutano anaoufanya na akataka zisikilizwe kama zina

lugha yoyote ya matusi.

Alidai mama huyo alifanya hivyo kwa sababu zake binafsi ili yeye akamatwe awekwe

ndani na kupelekwa mahakamani kwa lengo la kumdhalilisha.

Alidai pia mgombea mwenzake huyo alimlalamikia kuwa aliwahi kumkaribisha chakula

akakikataa na kudai haoni sababu ya yeye kumwandalia chakula kwa kuwa hata katika

kumbukumbu zake hajui kama aliwahi kuwa na mahusiano yoyote na yeye hadi afikie

hatua ya kumwandalia chakula.

Polisi mkoani hapa imethibitisha wagombea hao kufikishana kituoni hapo na kuwa

walihojiwa na kuachiwa.

 

Sumaye awataka Moshi mjini kubadilika

Na Rodrick Makundi, Moshi

WANANCHI wa jimbo la Moshi mjini wametakiwa kuondokana na dhana potofu ya

kutotaka kuongozwa na wanawake na badala yake wawaone ni viongozi wanaoweza

kuleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi katika kuboresha maisha yao.

Kauli hiyo ilitolewa hapa na Waziri mkuu Fredrick Sumaye, alipohutubia mkutano wa

hadhara wa kumnadi mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM katika jimbo hilo, Elizabeth

Minde.

Sumaye ambaye ni mlezi wa chama mkoa wa Kilimanjaro alitoa kauli hiyo kwa kile

alichoeleza kumekuwa na dhana kuwa mwanamke hafai kuwa kiongozi bora na anayeweza

kuongoza wananchi.

Kutokana na hali hiyo alisema dhana hiyo inapaswa kufutiliwa mbali, kwani hata

sera ya CCM kwa serikali ijayo imetoa kipaumbele kwa wanawake kushika nyadhifa

mbalimbali serikalini na katika chama.

Akimnadi mgombea huyo wa ubunge jimboni humo, Waziri Mkuu alisema kutokana na

uzoefu alionao katika masuala ya sheria, anaamini Elizabeth atawawakilisha

wananchi wa Moshi mjini ipasavyo kwa kuzipanga hoja zenye ushawishi wa kutekeleza

sera na ilani ya CCM katika jimbo hilo.

"Mtu asiwadanganye eti mwanamke hawezi kuwaongoza, eleweni kuwa Minde (Elizabeth)

ni mwanasheria anayepanga hoja, sasa sisi tunaamini atakuwa mwakilishi imara na

mbunge atakayetetea wananchi watakaomchagua," alisema.

Akaongeza kuwa pamoja na kelele zinazopigwa na wagombea wa vyama vya upinzani,

hazitasaidia kumpata rais wa upinzani atakayeingia ikulu, hivyo iwapo serikali

ijayo itakuwa ya CCM sera zitakazotekelezwa zitakuwa za CCM.

Pia alisema hata wabunge wengi watatoka CCM na ndio watakaokuwa na nafasi ya

kupendekeza utekelezaji wa ilani kwa kupitisha hoja nyingi zinazotolewa na

wabunge hao wa CCM.

Sumaye aliongeza kuwa ili kutekeleza malengo hayo wananchi wanapaswa kumpigia

kura wagombea wote wa CCM kuanzia ngazi ya urais, wabunge na madiwani ili kuwa na

mzunguko wa viongozi bora wenye msukumo wa kutekeleza ahadi zinazotolewa.

"Ninyi wakazi wa Moshi mjini,napenda mfahamu iwapo mtakuwa na mbunge wa CCM, bado

pia mnalo jukumu la kuwa na madiwani wa CCM kwani hatutakiwi kuwa na halmashauri

inayoendeshwa na wapinzani, huku mbunge wake ni wa CCM," alisema na kuongeza kuwa

hiyo itapelekea kupingwa kwa kila kinachojadiliwa wakati wa vikao.

Kwa upande wake, mpiga debe wa CCM, Thomas Ngawaiya aliwaambia wananchi hao kuwa

iwapo watachagua kambi ya upinzani bado watakuwa katika wakati mgumu wa kupata

huduma zinazohitajika.

Alisema idadi kubwa ya wabunge wa chama kimoja ndiyo inayowezeshwa kupitishwa

hoja za kutekeleza ujenzi wa miundombinu katika majimbo na akaongeza kuwa

wapinzani wamekuwa wakishindwa kutekeleza majukumu yao kwa kukosa kuungwa mkono

bungeni.

Hivyo alidai wapinzani wataendelea kuwa wasindikizaji, bungeni huku CCM

ikiendelea kutekeleza majukumu yake na akatoa wito kwa wananchi wa jimbo la Moshi

mjini kuipa kura CCM.

Akizungumzia suala la jinsia katika uongozi Ngawaiya aliwataka wananchi kutambua

mchango mkubwa,wa aliyekuwa mbunge wa zamani Moshi Lucy Lamecki ambaye alileta

maendeleo makubwa na ambayo hakuna kiongozi yeyote aliyefikia hatua ya mbunge

huyo.

Aliainisha baadhi ya miundo mbinu hioyo kuwa ni pamoja na barabara, huduma za

afya, upatikanaji wa maji safi, ambapo alidai kuwa bado mwanamke anayo nafasi

kubwa na uwezo wa kuweza kuleta maendeleo kinyume na mtazmo wa watu wanaodai

mwanamke hawezi kuongoza.

Mgombea ubunge wa jimbo hilo Elizabeth Minde aliwaambia wananchi katika mkutano

huo kuwa iwapo watamchagua kuwa mbunge wao atahakikisha utekelezaji wa sera

zinazoelezwa na CCM unafanikishwa katika jimbo lake ili kuleta imani kuwa CCM

inao uwezo mkubwa wa kuwaangalia wananchi wake.

 

Mgodi wa Kiwira Mbeya kuongeza uzalishaji

Na Nico Mwaibale wa PST, Mbeya

MGODI wa makaa ya mawe Kiwira (KCM) mkoani Mbeya, unatarajia kuongeza uzalishaji

wa makaa kutoka wastani wa tani 150,000 kwa mwaka hadi zaidi ya tani 500,000

kuanzia mwaka ujao baada ya kupata mwekezaji mzalendo.

Mwekezaji huyo amekwisha tenga zaidi ya sh. bilioni mbili kwa ajili ya kufanyia

matengenezo na ukarabati wa mitambo, miundombinu na kununua vifaa vipya vya

kisasa vya mgodi huo.

Meneja mkuu wa mgodi huo, Abdul Adam, alisema jana kuwa mwekezaji huyo ameingia

ubia na serikali tangu Agosti mwaka huu, ambapo amechukua asilimia 88 ya umiliki

na serikali imebakiwa na asilimia 12, na kuwa tayari amekwishaanza kazi ya

ukarabati na matengenezo katika mgodi huo.

Hata hivyo, Meneja Mkuu huyo hakuwa tayari kutaja kiasi cha fedha kilichowekezwa

na mwekezaji huyo, lakini habari zilizopatikana mgodini hapo zilieleza kuwa mbia

huyo amenunua mgodi huo kwa kiasi cha sh. bilioni tano.

Mkurugenzi Mtendaji huyo, Balozi Evans Mapundi ambaye ndiye mwekezaji, alisema

baada ya kukamilisha matengenezo na ukarabati unaoendelea hivi sasa, mgodi

utakuwa na uwezo wa kuzalisha zaidi ya tani 500,000 za makaa ya mawe kwa mwaka

kutoka wastani wa tani 150,000 zilizokuwa zinazalishwa.

Mapundi alisema lengo ni kuuwezesha mgodi huo kuzalisha wastani wa tani milioni

moja ya nishati hiyo kwa mwaka na kwamba hilo linawezekana katika kipindi kifupi

kijacho kutokana na kuweka vifaa vya kisasa na kufanyiwa ukarabati na matengenezo

ya mitambo iliyopo.

Alisema kampuni hiyo ya makaa ya mawe Kiwira hivi sasa inazalisha umeme wa

megawati sita ambao megawati moja inatumika mgodini hapo, 0.5 zinatumika katika

wilaya ya Kyela, na megawati mbili zinatumika wilaya ya Rungwe kupitia gridi ya

Taifa kwa mkataba na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Aliongeza kuwa hata hivyo, kampuni hiyo inakifanyia matengenezo kituo cha

kuzalisha umeme ili kuongeza uzalishaji kutoka megawati sita zinazozalishwa sasa

hadi megawati 50 ifikapo Januari 2007, kiwango ambacho kitazidi mahitaji kwani

mkoa wote wa Mbeya unatumia megawati 20 sasa.

Alisema umeme unaozalishwa mgodini hapo ni wa uhakika katika kipindi chote, kwani

hauathiriwi na hali ya hewa kama ule wa Tanesco ambao uzalishaji wake unategemea

hali ya hewa na ujazo wa maji katika mabwawa ya Mtera na Kidatu.

Balozi Mapundi alisema ana uhakika wa soko la makaa ya mawe katika kiwanda cha

Saruji cha Songwe Mbeya, Wazo Tanga, kiwanda cha SPM, viwanda vya chai, kiwanda

cha nguo cha New Mbeya Textile na wateja wengine wadogo kama hospitali, jeshini

na vyuoni, na kwamba wanatarajia pia kutengeneza makaa ya kiwango cha chini

kitakachowezesha kutumika majumbani.

Habari zaidi zimeeleza kuwa uboreshaji wa mgodi huo unakwenda sambamba na maslahi

ya wafanyakazi, ambapo kuanzia Januari mwaka ujao kiwango cha mshahara

kinatarajia kuongezwa kutoka sh. 50,000 hadi sh. 100,000 kwa mwezi kulingana na

mfanyakazi anavyozalisha.

Alisema katika kuboresha maslahi pia watoto watatu wa kila mfanyakazi

watagharamiwa masomo hadi ngazi ya chuo kikuu.

Mgodi huo una wafanyakazi 500 kutoka zaidi ya 1,500 waliokuwepo zamani, ambapo

wafanyakazi 300 kati yao wameajiriwa na 200 ni wa muda.