YALIYOJIRI
KAMPENI ZA CCM
Kikwete
aiteka Iringa, wananchi waduwaa
Mamia
wajitokeza mikutanoni, wazuia msafara
Asema
mapinduzi katika kilimo ni muhimu
Awapasha
wanasiasa hakuna mjadala juu ya Kilolo
Mkereketwa
atoa tafsiri ya jina lake
ZIARA
ya Mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Iringa ilikuwa ya aina yake
kutokana na mapokezi makubwa aliyoyapata kila alipofika kwa ajili ya kuomba
ridhaa kwa wananchi kuichagua CCM iendelee kuongoza nchi. Mwandishi Wetu EPSON
LUHWAGO aliyekuwa kwenye ziara hiyo, anatanabaisha yaliyotokea katika makala hii.
Mgombea
Urais wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Jakaya Kikwete
alifanya ziara ya siku mbili ya kampeni mkoani Iringa Septemba 3 na 4, mwaka huu.
Kabla
ya ziara hiyo, Kikwete alihutubia mikutano ya hadhara katika wilaya ya Njombe
maeneo ya Kifanya, Njombe Mjini, Makambako na Wanging'ombe mkoani humo,
alipokuwa akipita kwenda Mbeya kwa ziara kama hiyo.
ZIARA
RASMI
Kikwete
alipokewa saa 4.30 asubuhi na viongozi wa Chama na Serikali, wakiongozwa na
Mwenyekiti wa Mkoa, Tasil Mgoda, katika Uwanja wa ndege wa Ngwazi nje kidogo ya
mji wa Mafinga.
Viongozi
wengine waliokuwepo katika mapokezi hayo ni Katibu wa Mkoa, Constantine
Malyagili, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM mkoa wa Iringa,
Joseph Mungai, Mjumbe wa NEC, William Lukuvi na Mjumbe wa Kamati Kuu Pindi Chana.
Wengine
ni Mbunge wa Viti Maalum mkoa Lediana Mng'ong'o, Mbunge wa Iringa Mjini Monica
Mbega, viongozi wa kampeni ya kanda, Peter Siyovelwa na Mustafa Songambele na
mgombea ubunge wa Mufindi Kusini, Benito Malangalila.
Baada
ya kuwasili alivalishwa skafu na vijana wa chipukizi wa CCM huku vikundi
mbalimbali vya ngoma vikitumbuiza kwa nyimbo zenye asili ya kihehe.
Msafara
wa mgombea urais uliondoka uwanjani hapo kwenda Igowole ambako alipangiwa
kufanya mkutano wa kwanza wa kampeni.
Kikwete
aliwasili Igowole saa 4.55 asubuhi na kupokewa na watu lukuki waliofika katika
viwanja vya Shule ya Msingi Igowole kwa ajili ya kumsikiliza.
Mgombea
alizunguliwa na salamu za Chama kwa lugha ya kihehe zilizosema: "CCM
Kuchanya... kuchanya, kuchanya hilo mbaka pa lunepo (maana yake CCM Juu...juu,
juu zaidi na zaidi).
Baada
ya salamu hizo, Mwenyekiti wa Chama Mkoa alimkaribisha mgombea kuzungumza na
wananchi. Kabla hajamruhusu,
aliwaambia wananchi kwamba CCM haikufanya makosa kumpitisha Kikwete kugombea
urais.
Kiwete
alisimama na kuwahutubia wananchi huku akitoa ahadi mbalimbali ambazo alisema
zitatekelezeka bila wasiwasi wowote.
Kumalizika
kwa mkutano huo kulimfanya mgombea kuendelea na safari kuelekea Mafinga mjini
ambako alifanya mkutano uliojaza umati wa watu kwenye uwanja wa Mashujaa.
Alifika
Mafinga mchana na kukutana na umati
wa watu ambao hakutarajia kutokana na mji wenyewe kuwa wa kawaida.
Msafara
wa Kikwete kuingia uwanjani hapo ulisindikizwa na pikipiki 15 na magari madogo
takriban 20 kuingia kwenye uwanja wa Mashujaa.
Mara
baada ya kufika hapo, aliduwazwa na wananchi waliokuwa wakimsubiri kwa hamu,
wengine wakiwa juu ya miti na mapaa ya nyumba zinazozunguka uwanja. Hali hiyo
ilitokana na uwanja kuwa mdogo kulinganisha na idadi ya watu.
Kabla
ya kupanda jukwaa maalum lililoandaliwa kwa wageni mashuhuri, Kikwete alikagua
ngoma za asili kama vile livangala pamoja na kwaya kutoka vikundi mbalimbali
vilivyokuwa vimejipanga sawia kupamba mandhari ya eneo la mkutano.
Kama
ilivyo ada Kikwete alipanda jukwaani kuwahutubia wananchi waliofurika uwanjani
hapo huku wakishangilia kwa kila aina mambo aliyokuwa akiwaeleza wananchi hao.
APEWA
TAFSIRI YA JINA
Licha
ya kuhutubia wananchi kuomba kura, Kikwete alipewa maana ya jina lake. Maana ya
jina hilo ni
K-
King (Mfalme)
I-
Intelligent (Mwenye Akili)
K-
Kind (Mwema)
W-
Wise (Mwenye Busara)
E-
Educated (Mwenye Elimu)
T-
Trusted (Anayeaminika) na,
E-
Employer (Mwajiri)
Tafsiri
ya jina hilo ilitolewa na aliyekuwa Katibu wa NCCR- Mageuzi, jimbo la Mufindi,
Boniface Mliga alipokuwa akitangaza rasmi kujiunga na CCM baada ya
kuchoshwa na ahadi hewa za kambi ya upinzani.
Baada
ya mkutano wa Mafinga, Kikwete aliendelea na safari ya kuomba wananchi kuichagua
CCM kuongoza nchi kwa kwenda Iringa.
Katika
safari ya kuelekea Iringa, alifika Ifunda katika eneo la Kibaoni, jimbo la
Kalenga ambao ulikuwa na watu wengi wa marika yote.
Tofauti
na maeneo mengine, mbali na viongozi, Kikwete alipokewa na wazee wanne waliokuwa
wamevalia rasmi kichifu. Ifunda iko katika jimbo la kalenga ambalo ni asili ya
Chifu wa zamani wa Wahehe, Mkwawa.
Kwenye
mkutano huo pia, alimnadi mgombea Ubunge wa Kalenga, Stephen Galinoma na
wagombea udiwani wa wilaya ya Iringa Vijijini.
Mkutano
wa Ifunda ulikuwa hitimisho kwa siku ya kwanza ya kampeni za mgombea urais.
Aliondoka Ifunda kwenda Iringa mjini kwa mapumziko.
HODI
IRINGA
Msafara
wa Kikwete ulipokewa katika kijiji cha Uyole, manispaa ya Iringa ambapo kulikuwa
na wananchi waliojazana kwa shauku ya kumwona mgombea huyo.
Kama
ilivyo ada aliwashukuru wananchi wa Iringa kwa mapokezi
makubwa na hatimaye kueleza nia hasa ya CCM kutaka kuendelea kuongoza
nchi.
Baada
ya maneno hayo, msafara rasmi ulianza ukisindikizwa na magari ya wakereketwa,
teksi na pikipiki zilizokuwa na bendera za CCM.
Msafara
huo ulikuwa mkubwa na pengine ulivunja rekodi ya mapokezi yaliyokuwepo awali
kwenye miji mikuu ya mikoa aliyotangulia.
Kwa
wanaoijua manispaa ya Iringa, wakati gari la kwanza likiwa limeshamaliza mlima
kuingia eneo la Mshindo, magari mengine yalikuwa bado hayajaingia hata Ipogoro.
Kuanzia
eneo la Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora hadi Gangilonga kulikuwa na umati wa watu
waliokuwa wamejipanga kando ya barabara kuulaki msafara huo.
Mgombea
mwenyewe baada ya kuona umati wa watu kuanzia Samora, aliamua kutokeza juu ya
gari na kuwapungia mkono, hali iliyoamsha bashasha na shamrashamra za aina yake.
SARAFI
YA KILOLO
Siku
iliyofuata (Septemba 4), Kikwete alikwenda Kilolo alikofanya mkutano wa hadhara
katika jimbo hilo kijijini Boma la Ng'ombe.
Safari
ya kutoka Iringa mjini kwenda huko, ilianza saa 3.15 asubuhi kupitia vijiji vya
Tagamenda, Igula, Nyabula, Kitayawa, Ndiwili na Utengule hatimaye Kilolo.
Aliwasili
Kilolo saa 4.00 asubuhi na kusalimiana na viongozi wa Chama Wilaya wakiongozwa
na Mwenyekiti Valentine Msuva, Mbunge Venance Mwamoto na Mgombea Ubunge wa jimbo
hilo, Profesa Peter Msolla.
Baada
ya kutia saini kitabu cha wageni, aliwahutubia wananchi waliofika kwenye ofisi
za CCM Kilolo zilizoko Luganga, juu ya azma ya Chama kuomba ridhaa kwa wananchi.
Kumalizika
kwa hotuba hiyo, kuliashiria kuiva kwa safari ya kwenda Boma la Ng'ombe kupitia
Lusinga, Ilamba, Kidabaga, Ng'ang'ange na hatimaye kituo cha mkutano.
Katika
maeneo yote aliyopita, Kikwete alilakiwa na umati wa watu uliokuwa ukimsubiri
kwa hamu kumwona na hatimaye kusikia neno la matumaini kwa maisha yao.
Wananchi
katika vijiji vya Ilamba, Kidabaga na Ng'ang'ange, walizuia msafara wake kwa nia ya kutaka awape neno. Hakusita
kusimama na kuwasalimia, kuwapa neno na hatimaye kuomba wafunge njia ili
aendelee na safari.
UMATI
BOMA LA NG'OMBE
Baada
ya kuwasili Boma la Ng'ombe asubuhi
hiyo hiyo, Kikwete aliduwazwa na umati wa watu kutoka kata mbalimbali za wilaya
ya Kilolo waliofika kuhudhuria mkutano wa kampeni.
Mkutano
wa Boma la Ng'ombe ulipambizwa na kila aina ya ngoma za wahehe kama vile
livangala na kiduo ambazo huchezwa na wananchi wa wilaya hiyo- wadzungwa na
wahehe.
Kama
ilivyo ada, Kikwete alisimama na kuwafanya wananchi 'kupagawa' baada ya kumwona
alipotambulishwa na kukaribishwa kuzungumza nao.
Bila
kusita alisimama juu ya gari lake lililokuwa na spika na kuanza kuwamwagia sera
wananchi, ambazo kwa hakika, walionekana
kuzikubali.
Katika
mkutano huo Kikwete alimnadi mgombea Ubunge wa Kilolo, Profesa Peter Msolla na
kuwaomba wananchi kumchagua kwa kuwa ni msomi, kiongozi shupavu na tegemeo
katika utekelezaji wa ahadi za CCM katika serikali ijayo.
"Wana-Kilolo
mmempata Profesa Msolla mtaalam katika kilimo. Ni raha iliyoje kumpata mtu kama
profesa ambaye ndiye bingwa katika kilimo ambacho tunakitilia mkazo,"
alisema huku akishangiliwa na umati wa watu waliokuwepo katika mkutano huo.
Baada
ya kumaliza mkutano huo, mgombea na msafara wake walirejea Iringa kwa mapumziko
mafupi na baadaye mkutano
uliofanyika jioni kwenye uwanja wa Samora.
MSAFARA
SAMORA
Msafara
wa mgombea kwenda uwanja wa Samora ulianza saa 9.05 Chuo Kikuu Kishiriki cha
Ruaha (zamani Chuo cha Benki) na kuwasili uwanjani dakika saba baadaye.
Baada
ya kuingia Samora, alitokeza juu ya gari lake na kuwapungia mkono wananchi ambao
walijawa na furaha kumwona mgombea huyo.
Alipewa
mapokezi na heshima zote, alipanda jukwaani na kuwahutubia wananchi waliofika
hapo pamoja na kumnadi mgombea Ubunge wa Iringa Mjini Monica Mbega na wagombea
udiwani.
MUNGAI
KUVUTIO
Waziri
wa Elimu na Utamaduni, Joseph Mungai ambaye ni Mjumbe wa NEC mkoa wa Iringa,
alikuwa kivutio cha aina yake katika mikutano ya kampeni mkoani Iringa hasa
katika wilaya za Mufindi, Kilolo na Iringa Mjini.
Mungai
ambaye ni Mbunge wa Mufindi Kaskazini, alikuwa akivutia kutokana na uchezaji
wake hodari wa ngoma ya Livangala iliyokuwa ikichezwa maeneo mbalimbali wakati
wa kampeni hizo.
Kiongozi
huyo wa siku nyingi, alianza kuonyesha manjonjo yake Igowole alipojiunga na
kikundi kilichokuwa kikicheza ngoma ya Livangala.
Hizo
zilikuwa kama salamu tu, kwani alipofika Mafinga, alikwenda moja kwa moja kwenye
kikundi kimojawapo na kuanza kucheza ngoma hiyo mkononi akiwa ameshika 'usinga'.
Kufuatia
hali hiyo, wananchi waliokuwepo mahali hapo walianza kumshangilia na hivyo kutia
nakshi ya aina yake katika mkutano.
Mungai
aliendelea na uchezaji wa ngoma hiyo na kuonyesha kuwa ni hodari kwenye mikutano
ya Boma la Ng'ombe na Iringa Mjini.
MANENO
YA KIKWETE
Katika
mikutano yote mkoani Iringa, Kikwete aliwahimiza wananchi kuenzi amani na
utulivu vilivyodumu nchini tangu kupatikana kwa uhuru wa nchi.
Alisema
vitu hivyo ni tunu kwa Watanzania na kamwe wasivichezee. Aliwataka kujifunza
nchi jirani ambazo zimekosa vitu hivyo kutokana na kupigana kila uchao.
"Amani
na utulivu vilivyopo nchini ni vina umuhimu wake kwa maendeleo ya nchi. Bila
amani na utulivu hakuna maendeleo. CCM imefanya yote haya ndiyo maana nchi
imetulia," alisema.
Kutokana
na hali hiyo, aliwataka wananchi kutokuwachagua viongozi wanaohubiri shari
katika mikutano kwani alisema kuwachagua ni sawa na kuiweka nchi reheni na
kuhatarisha amani na utulivu.
Mbali
na amani na utulivu, Kikwete alisema lengo la serikali ijayo chini ya CCM ni
kuhakikisha kunakuwepo mapinduzi ya kweli katika sekta ya kilimo.
Alisema
katika kufanya mapinduzi hayo, serikali itahakikisha wananchi wanaondokana na
matumizi ya nguvu ya damu kwa kutumia jembe la mkono na badala yake kutumia
nguvu ya mashine.
Licha
ya kilimo, alisema ukuzaji wa viwanja utapewa kipaumbele kwa kuweka mazingira
bora na endelevu ili kuwavutia wawekezaji kuwekeza katika sekta hiyo.
Pia
aliahidi kutengeneza barabara ya lami kutoka Minjingu- Babati-Dodoma hadi Iringa
kwa kiwango cha lami ili kuifanya barabara kutoka Cape Town, Afrika Kusini hadi
Cairo, Misri ijulikanayo kama 'Great North Road' iwe ya lami.
Mbali
na barabara hiyo, aliahidi kuboresha barabara zingine ikiwemo ya kutoka Iringa
hadi Dabaga ili kuwawezesha wananchi kunufaika na usafirishaji wa mazao yao hadi
kwenye masoko.
Kwa
upande wa elimu, alisema lengo la serikali ijayo ni kuendeleza elimu ya
sekondari na chuo kikuu ili kuwawezesha wananchi wengi kupata nafasi.,
"Elimu
ni nyenzo muhimu katika maendeleo ya nchi. Hata mataifa yaliyoendelea yanatilia
umuhimu katika elimu. Uingereza wakati wa kampeni chama cha Labour ajenda kuu
ilikuwa elimu.
"Na
sisi hii itakuwa kipaumbele kwa maendeleo ya nchi. Katika kufanya hivi,
tutapanua vyuo vikuu nchini ili kuwezesha vijana wengi zaidi kupata elimu kwa
ajili ya maendeleo," alisema.
Kuhusu
makao makuu ya wilaya ya Kilolo, mgombea Urais aliwapasha baadhi ya wanasiasa
wanaoeneza uvumi kuwa kuna mpango wa kuhamisha makao makuu ya wilaya kutoka
Kilolo kwenda Ilula.
Aliwaambia
wanasiasa hao kuwa hakuna mtu mwenye mamlaka ya kuhamisha makao makuu hayo na
kusisitiza kwamba uamuzi wa Rais juu ya suala hilo ni wa mwisho na hauna mjadala
tena.
Kikwete
alisema hayo kufuatia baadhi ya wanasiasa wakati wa kura za maoni kudai kwamba
Profesa Msolla alikuwa na mpango wa kuhamisha makao makuu kwenda Ilula.
CCM
na mikakati ya ushindi Temeke
KATIKA
kipindi hiki cha kampeni kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu ujao, watu wasiojua siasa za
Temeke, 'wanaropoka' kwamba miongoni mwa majimbo yanayotajwa kuwa huenda
yakaangukia kwa wapinzani ni pamoja na lile la Temeke, mkoani Dar es Salaam kwa
madai kwamba limekuwa na historia
fupi ya kuongozwa na wapinzani. Hata hivyo wenye mwelekeo huo wanasahau kuwa
kuna nafasi kubwa ya jimbo hilo kwenda CCM kutokana na siri iliyofichika. Ni
siri gani hiyo? Mwandishi THOMAS MTINGE, anafafanua katika makala hii.
JIMBO
la Uchaguzi la Temeke mkoani Dar es Salaam katika nafasi ya ubunge kabla ya
Uchaguzi Mkuu wa sasa lilikuwa chini ya CCM ambapo mbunge wake alikuwa Khadija
Kusaga.
Mgombea
huyo wa CCM katika uchaguzi wa kura za maoni hakupata nafasi ya kuteuliwa
kutetea kiti chake na badala yake nafasi hiyo imechukuliwa na Abbas Mtemvu
ambaye anapeperusha bendera ya CCM katika kinyang'anyiro cha ubunge.
Wakati
joto la kuwania nafasi hiyo likizidi kupanda kwa kuwa siku nazo zinakaribia
kuchagua viongozi, kumejitokeza baadhi ya wanaojiita watabiri wa masuala ya
siasa na watu wengine kwa ajili ya kutoa maoni mbalimbali huku wakielezea kuwa
jimbo hilo linaweza kuchukuliwa na upinzani na hasa chama cha CUF.
'Watabiri'
hao wanataja sababu nyingi mbalimbali lakini baadhi ni kuwa mgombea wa CUF
Tambwe Hizza ambaye amewania nafasi hiyo mara tatu sasa lakini bila mafanikio,
amepata ukomavu na uelewa mkubwa wa kisiasa hivyo kuwa rahisi kushinda.
Wanasema
kuwa kitendo cha Tambwe kupata nafasi hiyo tena, kinampa fursa ya kuibuka na
ushindi dhidi ya mgombea wa CCM.
Sababu
nyingine inayotajwa ni kuwa wananchi wa jimbo hilo wameshawahi kuwapa wapinzani
ushindi kama ilivyokuwa kwa Mwenyekiti wa sasa wa TLP Augustine Mrema ambaye
alipata kuongoza jimbo hilo akiwa NCCR-Mageuzi.
Mrema
alikuwa mbunge wa Temeke hadi alipotangaza kujiengua kutoka NCCR-Mageuzi na
kujiunga na Tanzania Labour ambapo kisheria alikuwa amepoteza wadhifa wake wa
ubunge.
Lakini
jingine linalotajwa kuwa litachangia ushindi kwa CUF ni kuwa jimbo hilo eti lina
wanachama wengi wa CUF kuliko majimbo mengine katika jiji la Dar es Salaam.
Kwa
mujibu wa taratibu za uchaguzi, Wilaya ya Temeke ina majimbo mawili ya Kigamboni
na Temeke.
Baada
ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000, katika mkoa mzima wa Dar es Salaam, jimbo pekee
lililochukuliwa na wapinzani ni lile la Kigamboni tu ambalo mbunge wake alikuwa
Frank Magoba. Kwa sasa Magoba amerejea CCM.
Majimbo
mengine kama vile Kawe, alikuwa Ritha Mlaki ambaye amepata nafasi ya kutetea
kiti chake, Kinondoni alikuwa Peter Kabissa ambaye safari hii naye hakuteliwa
ambapo nafasi hiyo inatetewa na Iddi Azan, Ubungo alikuwa Charles
Keenja,anatetea kiti chake, Ukonga alikuwa Dk. Makongoro Mahanga, anatetea tena
kiti chake na Ilala alikuwa Idd Simba ambaye ameamua kupumzika na kuiacha
bendera ya CCM katika jimbo hilo ikipeperushwa na Mussa Azzan 'Zungu'.
UTABIRI
HAUNA NGUVU
Lakini
utabiri huo unaotolewa na baadhi ya watu katika jimbo hilo unatofautiana kabisa
na mtazamo wa kamanda wa Umoja wa Vijana wa CCM Kata ya 14, wilayani Temeke Fard
Bazar.
Akieleza
mtazamo wake, Bazar anasema utabiri huo kwa sasa hauna nafasi tena katika
jimbo hilo kutokana na jinsi CCM ilivyojiimarisha pande zote.
Wapinzani,
alisema hawana nafasi tena ya kulitawala jimbo hilo kwa sababu
walichezea bahati waliyoipata katika uchaguzi wa mwaka 1995 ambapo Mrema
alichaguliwa kuwa mbunge.
Pamoja
na wananchi kutupa karata yao katika kambi ya upinzani wakitarajia kupata
mabadiliko ya maendeleo, bado ikaonekana kama ndoto kwao baada ya Mrema
kuwatelekeza kwa kujiuzulu ghafla bila kutoa sababu za msingi.
Kitendo
cha Mrema kujiuzulu wadhifa huo bila sababu za msingi, kimewachukiza wananchi na
kuwafanya wasiwe na imani tena na kambi hiyo, anasema Bazar.
Akifafanua,alisema
kuwa kutokana na imani hiyo iliyojengeka kwa wananchi, kambi ya upinzani
sasa imekuwa haiaminiki tena.
"
Samaki mmoja akioza wote wameoza'. Hivyo kitendo alichokifanya Mrema kinaweza
kufanywa pia na wagombea wengine kutoka kambi ya upinzani endapo watapewa ridhaa
ya wananchi kushika nafasi za uongozi."
Kutokana
na kulitambua hilo, ndio maana ulipofanyika uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi
iliyoachwa wazi na Mrema, wananchi wakaamua kuichagua CCM.
Kamanda
Bazar anasema wameamua kuichagua CCM si kwa
kubahatisha, bali wakiwa na
matumaini kwamba ni Chama chenye sera nzuri na kinachoweza kuwaletea maendeleo.
Kwa
mujibu wa Bazar, katika uchaguzi huo mdogo ambapo CCM ilimsimamisha John Kibaso
kuwa mgombea wake, iliibuka na ushindi wa kishindo dhidi ya wapinzani.
Ushindi
huo wa CCM, ndio ikawa mwanzo wa kuzika ndoto za wapinzani kuliongoza tena jimbo
hilo.
Kwa
kuthibitisha hilo, wapinzani
walisambaratishwa tena katika Uchaguzi Mkuu uliyofanyika mwaka 2000.
.CCM
haiwezi kubishana na vyama ambavyo havina sera wala mwelekeo ambavyo hata
wananchi tayari wameonyesha hali ya kutovikubali.
"
kama ni mchezo wa mpira wa miguu basi naweza kusema kwa sasa CCM ndio timu ya
Simba na wapinzani ni Yanga.kwahiyo hawa ni wateja wetu na wataendelea kuwa
wateja wetu hadi hapo tukapoamua vinginevyo," anasema kamanda Bazar.
Litakuwa
ni jambo la ajabu kwa wananchi wa jimbo hilo kuthubutu kurudia makosa
waliyoyafanya mwaka 1995 kwa kuchagua mgombea kutoka kambi ya upinzani.
Endapo
wananchi wataamua kuchagua wagombea waliosimamishwa na vyama vya upinzani katika
uchaguzi mkuu ujao, watakuwa wamejifunga kitanzi cha kujiletea maendeleo katika
maeneo yao husika.
Hii
ni kwa sababu kambi hiyo haijajiimarisha kisera na hivyo haina uwezo wa
kuwaletea maendeleo wananchi.
UONGOZI
SI MAJARIBIO
Wanachokifanya
sasa kuhusu kushiriki kwao katika uchaguzi huo, Bazar anasema
ni kutaka kujaribu kama wanakubalika kiasi gani.
Anashauri
wana-CCM na wananchi kwa ujumla wao kutofanya makosa ya majaribio ya uongozi kwa
kuwachagua wapinzani.
"Uongozi
kamwe haujaribiwi hata siku moja kwani kufanya hivyo ni sawa na kuchezea
shilingi katika tundu la choo ambapo ikidumbukia haitapatikana tena.
"
Kuwapa uongozi wapinzani kwa majaribio ni sawa na kumpa panga mwenda wazimu
ambaye anaweza kulitumia vibaya wakati wote na baadaye ukajutia uamizu wako
uliyoufanya," anasema.
CCM,
anasema imejiandaa vema
kukabiliana na hali ya upinzani katika uchaguzi mkuu ujao. "Tuko
imara kukabiliana na hali yoyote ile kwani tuna silaha za kutosha za kupambana
nao na lazima CCM itashinda tu na si vinginevyo.
Silaha
hizo ni utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM ambayo Bazar anasema
imetekelezeka kwa asilimia kubwa katika serikali ya awamu tatu.
Lengo
la CCM, ni kupata tena ridhaa ya wananchi katika uchaguzi mkuu ujao, ili
kuendeleza mafanikio iliyoyafanya na kuongeza mengine zaidi ili kuondoa kero
zinazowakabili wananchi wake.
CCM
ina uwezo wa kutekeleza ahadi zake inazozitoa kwa wananchi hususan katika
kipindi hiki cha uchaguzi mkuu tofauti na sera za wapinzani ambazo
hazitekelezeki hata kidogo.
Ushindi
huo kwa CCM, Bazar anakiri hauwezi kupatikana hivi hivi bali utapatikana kwa
kunadi mafanikio yaliyopatikana kupitia ilani yake ya uchaguzi kwa wananchi.
Akiwa
kama kamanda wa UVCCM, alisema atahakikisha kwamba vijana wake wanashiriki
kikamilifu katika kunadi sera za CCM kwa wanchi.
Bazar
anasema kushiriki kikamilifu kwa vijana katika kunadi sera za CCM ni sehemu ya
wajibu wao lakini pia kutawafanya wananchi walio wengi kutambua nini
ilichokifanya CCM.
Alifafanuwa
kwamba kumekuwa na taarifa za
upotoshaji zinazosambazwa na wapinzani mitaani eti CCM katika kipindi cha
utawala wake haijafanya kitu chochote huku wakitembelea barabara nzuri, kupata
maji safi, afya, elimu na maendeleo mengine mengi.
"Vijana
ndio nguzo ya CCM hivyo lazima washiriki kikamilifu katika uchaguzi huo kwa
kuwaelimisha wananchi waachane na vyama 'uchwara' ambavyo havina sera madhubuti
na badala yake waichague CCM iendelee kuleta maendeleo," anasema.
Katika
kipindi hiki cha uchaguzi, Bazar alisema atahakikisha
kwamba kauli ya Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Benjamin William Mkapa ya kuwataka
makamanda wa UVCCM washirikiane na vijana badala ya kuvaa majoho tu inatekelezwa
ipasavyo kwa kuipatia ushindi CCM katika jimbo hilo.
Akielezea
alivyoawaandaa vijana, alisema tayari
amekaa na vijana kupanga nao mikakati ya kuipatia CCM ushindi ukiacha ile ya
kujiletea maendeleo endelevu ambayo pia ishakamilika.
Kwa
mujibu wa Bazar, anakusudia
kukutana na makamanda wenzake wa UVCCM waliomo katika jimbo la Temeke ili
kujenga nguvu na mawazo ya pamoja ya jinsi ya kuwahimiza vijana ili wajitokeze
kwa wingi wakati wa kupigakura kuchagua viongozi na waichague CCM.
Kuna
haja ya makusudi kabisa kila mwana-CCM kuunga mkono kauli ya mgombea wa CCM wa
kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete ya kuweka
serikali yenye mafiga matatu, alibainisha.
Kauli
hiyo, aliongeza imejaa ukweli tupu
kwamba wananchi hawawezi kupata maendeleo safi endapo serikali ijayo itakuwa na
upungufu wa mafiga matatu kama alivyosema Kikwete kwa maana ya kwamba rais,
wabunge na madiwani lazima watokane na CCM.
"
Ilani za vyama zinatofautiana hivyo unapochagua Rais kutoka CCM na kisha
ukachagua mbunge kutoka CUF, ujuwe wazi kwamba hapo maendelo yake ni sawa na 'ziro'
kwa sababu kila kiongozi atataka kutekeleza sera ya ilani yake," anasema
kamanda Bazar.
Kwa
vyovyote vile, aliongeza Kikwete
atashinda katika uchaguzi ujao na kuwataka wananchi wamchagulie wabunge na
madiwani kutoka CCM ili waweze kuchapa kazi na kuzungumza lugha moja ya
kuwaletea maendeleo ya haraka.
Kamanda
Bazar anaongeza kuwa serikali ijayo ya CCM inauhakika wa kuongoza nchi kwa
kipindi cha miaka kumi ijao kutokana na ukweli kwamba sera zake zinakubalika na
wananchi.
"Ari
mpya, nguvu mpya. Kasi mpya 2015,"
anasema Bazar akimaanisha kwamba CCM itaendelea na kasi hiyo kwa kipindi chote
hicho.