HOJA YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MUUNDO WAKE WA SERIKALI MBILI

(Omar R. Mapuri)

 

 

UTANGULIZI

 

Hoja ya Muungano wa Tanzania inasimama juu ya msingi wa sera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).  Sera ya  CCM kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kuwa Tanzania ina ncha mbili; yaani kuulinda na kuudumisha Muungano wenyewe kwa upande mmoja na muundo wa Muungano huo kuwa wa Serikali mbili kwa upande wa pili.

 

CCM inaushabikia Muungano na kupania kuulinda na kuudumisha kwa sababu kwanza inaamini kuwa Muungano huu ni wa watu wenyewe na pili, uliasisiwa na vyama wazazi wake, yaani TANU na ASP.  Zaidi ya hivyo, CCM yenyewe ni matokeo ya Muungano huo na chachu ya kuziimarisha kwani tendo la kuviunganisha vyama vya TANU na ASP kuunda CCM lilitokana na utashi wa kukamilisha hatua za kuunda Muungano.

 

CCM inaunga mkono muundo wa Muungano wa Serikali mbili kwa sababu kwanza ndio ulioamuliwa na waasisi wa Muungano, Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere na Mzee Abeid Amani Karume, na pili umezingatia vya kutosha uhalisi wa mambo wa nchi kubwa na ndogo kuungana.  Muundo huo ndio unaohakikisha umadhubuti wa Muungano wenyewe bila ya nchi ndogo (Zanzibar kwa muktadha huu) kumezwa na nchi kubwa (Tanganyika).

 

CCM inajivunia Muungano huu na muundo wake wa Serikali mbili kwani hata baada ya miaka 40 ya kuundwa kwake bado ndio mfano pekee wa Muungano uliofanikiwa wa nchi huru zilizoungana katika Bara la Afrika.  Zaidi ya yote, Muungano huu umeweza kuhimili misukosuko yote ya ndani uliyokumbana nayo ambayo ingeweza kuudhofisha au hata kuuvunja.

 

Pamoja na makelele mengi ya kisiasa yenye kuulalamikia, Muungano huu na muundo wake wa Serikali mbili unaungwa mkono na Watanzania walio wengi.  Ushahidi wa kitakwimu utatolewa katika makala haya kwamba muundo wa Serikali mbili ndio unaotakiwa na Watanzania walio wengi, na muundo wa Serikali tatu unaopigiwa debe sana na vyama vya upinzani na baadhi ya wasomi ndio unaokataliwa na Watanzania wengi kuliko muundo mwingine wowote.

 

Kabla ya kuendelea na hoja, inafaa katika hatua hii kutazama maandiko rasmi ya kisera ya CCM kuhusu Muungano na muundo wake, kama yalivyo katika Ilani za Uchaguzi za CCM za 1995 na 2000.

 

Ibara ya 47 ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 1995 inasomeka ifuatavyo:

 

47.            Sera ya Kuimarisha Muungano

Muundo wa Muungano, ambao unakubaliwa na CCM, ni Muungano wenye Serikali mbili:  Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.  Sera hii imethibitishwa mwaka 1994 wakati wanachama wetu walio wengi walioshiriki katika kura za maoni kote nchini walitaka sera hii iendelee.  Katika kipindi cha miaka mitano ijayo, CCM itaendelea kudumisha Muungano wa Tanzania katika muundo wa Serikali mbili.

 

Kwa upande wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000, ibara zinazozungumzia kuimarisha Muungano ni za 116 na 117 ambazo zinasomeka ifuatavyo:-

 

116.   Umoja wa kitaifa wa Watanzania ambao umedumu kwa kipindi kisichopungua miaka 36 unatokana na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao ulizaa Tanzania.  Katika kipindi chote hicho muundo wa muungano ambao umeendelea kukubaliwa na Chama Cha Mapinduzi ni muungano wenye Serikali mbili:  Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.  Sera hii imeendelea kuthibitishwa na wanachama wa CCM na wananchi kwa jumla.

 

117.       Katika kipindi cha miaka mitano ijayo (2000 – 2005) Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuhakikisha kuwa mafanikio yaliyorithiwa kutoka kwa Waasisi wa taifa letu Baba wa Taifa, Mwalimu J.K. Nyerere na Makamu wake wa Kwanza Sheikh Abeid Aman Karume yanaendelezwa na kulindwa kwa kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kuwa huru, Taifa lenye Umoja, Udugu na Mshikamano na nchi yenye amani na utulivu.  Aidha, muundo wa Muungano utaendelea kuwa wa Serikali mbili: yaani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

 

Hivyo ndivyo inavyosema Sera ya CCM kuhusu Muungano na muundo wake.  Ni muhimu hili kuwekwa sawa kwani wapinzani wa CCM, hasa kule Zanzibar, hupenda kujichukulia uhuru wasiopewa wa kuisemea CCM wapendavyo wao.  Hupenda sana kuipotosha sera hii kwa kuinukuu kilaghai kwamba eti “ni ya Serikali mbili kuelekea moja”.  Kauli hiyo imewahi kutoka katika vikao vya CCM kama kauli nyingi nyenginezo zilivyowahi kutoka.  Kwa mfano, Bunge, likiwa na Wabunge wa CCM watupu liliwahi kupitisha azimio la kutaka kuundwa kwa “Serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano”.  Lakini baada ya yote hayo na kauli zote zilizosemwa na/au kuandikwa, ulipofika wakati wa kutunga sera rasmi, Chama kiliamua bila ya kigugumizi kuendelea na sera ya Muungano wa Serikali mbili na kuiweka kwa uwazi na bila ubabaishaji katika Ilani za Uchaguzi.

 

NGUZO ZA MUUNGANO

 

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulijengwa juu ya msingi wa kijiografia na kihistoria uliowafanya watu wa maeneo haya kuwa wamoja, ndugu, wenye tamaduni zilizoingiliana na hata wenye utashi wa kisiasa uliofanana.

 

Juu ya msingi huo, zimesimama nguzo nne zinazouhimili Muungano huo.  Nguzo ya kwanza ambayo imejengeka kwa muda mrefu katika historia ni kwamba Muungano huu ni wa watu wenyewe.  Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kijamii na hata wa kisiasa.  Nguzo ya pili ni msukumo wa kujenga umoja wa Afrika.  Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kisiasa za kimataifa.  Nguzo ya tatu ni Hati ya Muungano ambayo iliujengea Muungano uhalali wa kisheria ambao unaendelezwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977 na Katiba ya Zanzibar ya 1984.  Nguzo ya nne inayouhimili Muungano na ambayo inaendelea kujengeka ni ya uendelevu wa Muungano wenyewe.  Muungano wa Tanzania umeshatimiza miaka 40 ukiendelea kuimarika.  Umeweza na unaendelea kuhimili misukosuko mingi, ambapo kila unapoingia kwenye tanuri la misukosuko, unaibuka ukiwa imara zaidi.  Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kisiasa za ndani.

 

Sasa tuzitazame nguzo hizi moja moja.

 

Nguzo Ya Umoja wa Watu Wenyewe

 

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar umejengeka kutokana na mahusiano ya dahari na karne baina ya watu wa visiwa vya Zanzibar na mwambao wa Afrika ya Mashariki, hasa Mrima ambayo ni sehemu kubwa ya Tanzania Bara ya sasa.

 

Kabla ya Kuja Kwa Wageni Toka Nje ya Afrika

 

Wanahistoria (mfano Ingrams) wakijenga hoja kutokana na maandiko ya kale ya Periplus (karne ya kwanza AD) na ngano za watu wa kale, wanakubaliana kwamba watu wa kwanza kabisa kufika katika visiwa vya Zanzibar ni Waafrika kutoka Mrima katika harakati za uvuvi.  Ushahidi wa kiakiolojia wa hivi karibuni umethibitisha usahihi wa imani hiyo.

 

Wakati wa Himaya ya Zenj

 

Lakini hata baada ya kuja kwa wageni kutoka nje ya Afrika, mahusiano ya watu wa pande hizi mbili siyo tu yaliendelea, bali yalizidi kuimarika hasa kutokana na kuongezeka kwa ubora wa teknolojia ya usafiri wa baharini.  Himaya ya Waajemi (Washirazi) katika eneo hili ambayo baadhi ya wanahistoria wanaiita Himaya ya Zenj (Zenj Empire) ilipojengeka kutokana na ujio wa wale Ndugu saba wa  El-Hasa mnamo karne ya 13 ambao walianzisha tawala katika vituo mbali mbali vya mwambao wa Afrika Mashariki (mfano Kilwa, Barawa, Lamu, Unguja, Pemba, n.k.), maingiliano ya watu wa maeneo haya yaliendelea bila ya vikwazo.

 

Wakati wa Himaya ya Biashara ya Zanzibar

 

Mnamo karne za 16 hadi katikati ya 19, ilijengeka Himaya ya Kibiashara ambayo kitovu chake kilikuwa Zanzibar.  Himaya hiyo iliyojumuisha biashara ya watumwa, vipusa na viungo, ilienea hadi maeneo ya Maziwa Makuu kwa upande wa Kaskazini Magharibi na maeneo ya Ziwa Nyasa na Mto Ruvuma kwa upande wa Kusini mwa Tanzania ya leo.  Katika kitabu chake cha Slaves, Spices & Ivory in Zanzibar Profesa Abdul Sheriff anazungumzia dhana ya Bara ya Zanzibar (The Hinterland of Zanzibar) akiwa na maana ya eneo la Bara lililokuwa chini ya ushawishi wa Zanzibar (bila shaka na Sultani wake), ambalo kwa kiasi kikubwa ni hili hili eneo la Tanzania Bara ya leo.  Dhana hiyo ilipewa methali maarufu ya: “Inapopigwa ngoma Zanzibar, wanacheza katika Maziwa Makuu”.

 

Maelezo haya yanajaribu kujenga hoja kwamba eneo ambalo leo linaitwa Tanzania, kwa kiasi kikubwa ndilo lililokuwa Himaya ya Kibiashara ya Zanzibar ya enzi hizo.  Kwa maneno mengine nchi hii ilikuwa moja toka enzi hizo ingawa yenye mipaka hafifu.  Watu wa eneo lote hili waliunganishwa na harakati za biashara.  Biashara ya utumwa iliwafanya wa huku waende kule na wa kule waje huku, ingawa katika mazingira ya uchungu.  Watumwa walichukuliwa Bara na kupelekwa visiwani Zanzibar ambako vizazi vyao vimeendelea hadi leo na kufanya sehemu kubwa ya Wazanzibari.  Kwa upande mwengine, wako wafanyabiashara ya watumwa walioanzia Zanzibar na kuhamia Bara na kufanya maskani yao huko.  Vizazi vyao vinaendelea hadi leo na wamekuwa sehemu ya jamii ya Watanzania Bara.  Hivi sasa, katika mazingira ya uhuru, watu wa kila upande kati ya pande mbili hizi wanaendelea kuhamia na kuweka maskani katika upande wa pili bila ya vikwazo.

 

Utenganishi wa Wakoloni wa Kizungu

 

Kitendo kilichowatenganisha watu wa pande hizi ni kile cha wakoloni kutoka Ulaya (Wazungu) kugawana makoloni katika Bara la Afrika, katika nusu ya pili ya karne ya 19.  Baada ya kinyang’anyiro baina yao, wakoloni hao walikutana katika Mkutano wa Berlin wa 1887 ambapo waligawana Afrika.  Katika mgao huo, sehemu ya Bara (ukiondoa ukanda wa mwambao wa pwani ulioitwa Mrima) walipewa Wajerumani.  Koloni hilo ambalo lilijumuisha Burundi na Rwanda ya sasa liliitwa Deutsche Ost Afrika (yaani Afrika Mashariki ya Wajerumani).  Sultani wa Zanzibar aliachiwa visiwa vya Unguja, Pemba na Mafia na ukanda wa Mrima.  Miaka mitatu baadae, chini ya Mkataba wa Heligoland wa 1890, Sultani alilazimishwa kuuza kwa Wajerumani ukanda wa Mrima na kisiwa  cha Mafia, na hivyo kubakiwa na visiwa vya Unguja na Pemba tu, na yeye mwenyewe kuwekwa chini ya Himaya ya Mwingereza.  Watu wa Bara na Visiwani wakawa wametenganishwa.

 

Kuanza Kurejeana

 

Baada ya Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia (1915 – 1919), majaaliwa yalianza kuwakurubisha tena watu wa pande hizi mbili.  Kufuatia kushindwa kwa Wajerumani katika vita hivyo, Rwanda na Burundi walipewa Wabelgiji na sehemu iliyobaki ya Deutsch Ost Afrika iliitwa Tanganyika Territory na kupewa Waingereza.  Kwa hivyo watu wa Zanzibar na Tanganyika ingawa waliendelea kuwa na nchi mbili tofauti, lakini angalau wakawa chini ya mkoloni mmoja.

 

Hali hiyo ilijenga mazingira ya kuweza kurejea kwa mawasiliano baina ya watu wa Bara na wa Visiwani ambayo yalikuwa yameathirika vibaya kwa kipindi cha kiasi cha miaka 30.  Mwamko wa kudai uhuru wa kijamii na baadae wa kisiasa ulipoanza kujengeka, watu wa pande hizi mbili, hususan wenyeji wa asli (yaani Waafrika) hawakusita kuitumia fursa hiyo kushirikiana na kusaidiana katika azma hiyo.

 

Mwaka 1927, Waafrika wa Dar es Salaam walianzisha jumuiya yao iliyoitwa “African Association” kwa ajili ya kupigania maslahi yao ya kijamii.  Mwaka 1934, Waafrika wa Zanzibar nao walianzisha “African Association” yao, pengine kutokana na ushawishi wa ndugu zao wa Dar es Salaam.  Nao Waafrika wa Zanzibar wakawashawishi wale wa Dodoma na kupelekea kuundwa kwa “African Association” ya Dodoma.  Jumuiya tatu hizi zilijenga umoja wa kufanya mikutano mikuu ya pamoja ya mwaka kwa zamu baina ya miji hiyo, na zilikuwa chachu ya kufunguliwa kwa matawi ya “African Association” katika miji mbali mbali Tanganyika na Zanzibar.

 

Ziara za Michezo

 

Sambamba na ushirikiano huo wa kijamii, wananchi wa Tanganyika na Zanzibar walianzisha utamaduni wa kubadilishana ziara za kimichezo.  Ziara hizo zilikuwa zikifanyika wakati wa mapumziko ya Pasaka, kwa utaratibu wa zamu ambapo kama mwaka huu wanamichezo wa Zanzibar wanakwenda Tanganyika, mwaka ujao wa Tanganyika watakwenda Zanzibar.  Utamaduni huo unaendelea hadi leo na umezidi kupanuka kwa kujumuisha wasanii na hata wananchi tu wa kawaida.

 

Ushirikiano wa Kisiasa

 

Upepo wa harakati za kudai uhuru kutoka kwa wakoloni ulipofika maeneo haya, watu wa Tanganyika na Zanzibar walihamasishana, kushirikiana na kusaidiana katika jukumu hilo la kudai na kupigania uhuru wa nchi zao.  Mwaka 1954, chama cha Tanganyika African National Union (TANU) kilianzishwa Tanganyika kutokana na Tanganyika African Association, kwa ajili ya kudai uhuru wa Tanganyika.  Zanzibar nako mwaka 1957 ilianzishwa Afro-Shirazi Party (ASP) kutokana na kuungana kwa African Association na Shirazi Association (iliyokuwa imeundwa 1938).  Kuundwa kwa ASP kulishuhudiwa na Rais wa TANU, Mwalimu Julius K. Nyerere.

 

Ushirikiano wa TANU na ASP katika mapambano ya kudai uhuru hadi ulipopatikana Uhuru wa Tanganyika Disemba 9, 1961 na kufanikiwa kwa Mapinduzi ya Zanzibar Januari 12, 1964 unajulikana na hauna haja ya kuufafanua hapa.  Dhamira angalau ya ASP (wakati wa kupigania uhuru) ya kuiunganisha Zanzibar na Tanganyika baada ya uhuru haikuwa siri.  Hiyo inadhihirishwa na maelezo yafuatayo ya Marehemu Sheikh Thabit Kombo kama yalivyonukuliwa na Rais Benjamin Mkapa katika hotuba yake ya kihistoria aliyoitoa Zanzibar kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2004:-

 

Mafisadi wanalalamika, kwa nini muungano umefanyika haraka haraka;  Mapinduzi Januari na Muungano Aprili, miezi mitatu tu!  Wako wanaodhani kuwa Mwalimu Nyerere ndiye aliyelazimisha Muungano.

         

Wazo la Muungano ni wazo la Afro-Shirazi tokea mwanzo.  Utakumbuka katika Manifesto yetu tulisema kuwa tukipata Uhuru azma ya ASP ni kuona kuwa Afrika yote inakuwa moja yenye nguvu.  Lakini kwa Tanganyika na Zanzibar ahadi ya muungano ni ahadi ya wanachama wenyewe waliyokuwa wanaitoa katika mikutano yao yote…  Watu wa Tanganyika na watu wa Zanzibar ni wale wale, tofauti ni sisi wa Zanzibar kutawaliwa na Sultani….  Mazungumzo yalikuwa mafupi sana, yalichukua siku moja tu; maana hakukuwa na swali kama tuungane au tusiungane.  Hoja ilikuwa tu muungano wetu uwe na sura gani…..

 

Muungano Kama Tukio la Kimantiki

 

Kutokana na ukweli huo wa kihistoria wa umoja, udugu na ushirikiano wa muda mrefu baina ya watu wa pande hizi, na kufuatia TANU na ASP kushika madaraka baada ya Uhuru na Mapinduzi, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kuwa Tanzania uliokamilishwa rasmi tarehe 26 Aprili, 1964 lilikuwa ni tukio la kimantiki na halipaswi kuwa la kushangaza.

 

Ni ukweli wa kihistoria kwamba pamoja na kwamba watu wa Tanganyika na Zanzibar wamekuwa wamoja katika zama zote za kihistoria, lakini Tanganyika na Zanzibar hazikuwa nchi tulizoziunda.  Ziliundwa na wakoloni na mipaka yake ilikuwa ikipangwa na kupanguliwa na wakoloni kwa maslahi yao.  Tanganyika na Zanzibar pamoja na mipaka yake tuliirithi tu kutoka kwa wakoloni baada ya uhuru.  Lakini Tanzania tumeiunda wenyewe..  Katika kitabu chake cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania, Mwalimu Julius K. Nyerere anasisitiza kwa fahari:  Tanzania ni lulu ya pekee kabisa katika historia ya Afrika huru.  Nchi nyingine zote ni za kurithi kutoka katika Ukoloni.  Tanzania ni ya kuundwa na sisi wenyewe, kwa hiari yetu wenyewe, baada ya kukomboa sehemu zake mbili kutoka katika Ukoloni.  (uk.57).

 

Pamoja na hayo, kama itakavyofafanuliwa baadae, wapo watu wanaoshangaa na kuhoji uhalali wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa hoja kwamba eti hayakutafutwa maoni ya wananchi kwanza.  Katika kuwabeza watu hao, Mwalimu Nyerere katika kitabu chake hicho hicho cha “Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania anasema ifuatavyo kwa kejeli:-

 

Pwani ya Tanganyika na Zanzibar ya sasa zilikuwa pamoja kwa muda mrefu sana kabla ya kutengwa na Wakoloni Waingereza na Wajerumani.  Kama zingebaki zimetengana, kwa “wazalendo” hao hiyo ingekuwa ni halali, maana zilitengwa kwa hila na mitutu ya bunduki za Mabwana.  Lakini uamuzi wa Tanganyika huru na Zanzibr huru kuungana, na hivyo kuwaunganisha tena ndugu waliokuwa wametengwa na Mabeberu, tendo hilo kuna … wanaosema kuwa halikuwa halali.  Hatukutafuta maoni ya watu kwa njia ya demokrasia wanayoijua wao.  Wajerumani na Waingereza walitafuta maoni ya wazee wetu kwa mtutu wa bunduki!  Hiyo ilikuwa halali.  Nchi walizounda kwa njia hizo zilikuwa halali.  Tunatakiwa tujivunie Utanganyika na Uzanzibari uliopatikana kwa njia hizo; lakini tuuonee haya Utanzania, tunda la uhuru wetu wenyewe.  Sikuamini kuwa Wakoloni walifaulu kiasi hiki katika kuzinywesha kasumba na kuzitawala akili za baadhi yetu!.  (uk.58).

 

Tarehe 5 Februari, 1977 vyama vya TANU na ASP viliungana na kufanya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika tukio ambalo lilikuwa na maana ya kuzidi kuuimarisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.  Tena kuundwa kwa CCM kulitanguliwa na mashauriano ya kutosha.  Aidha, ilifanywa kura ya maoni ya wanachama ambayo matokeo yake yalikuwa kama yanavyoonekana katika Jedwali Na. 1 na 2 hapa chini:-

 

 

JEDWALI Na. 1:   MATOKEO YA MAONI YA WANACHAMA WA TANU KUHUSU KUUNGANISHWA TANU NA ASP

Matawi

Idadi

Asilimia

Idadi ya Matawi Yote ya TANU

6,639

100.00

Yaliyokutana

6,427

96.81

Yasiyokutana

212

3.19

Yaliyokubali

5,424

99.95

Yaliyokataa

3

0.05

Idadi ya Matawi Madogo ya TANU

38

100,00

Yaliyokutana

38

100.00

Yaliyokubali

38

100.00

Yaliyokataa

0

0.00

Chanzo:       Tathmini ya Miaka 20 ya CCM, 1977 – 1997

 

JEDWALI Na. 2:    MATOKEO YA VIKAO NA WANACHAMA WA ASP KUHUSU MAONI YA KUUNGANISHWA TANU NA ASP

Matawi

Idadi

Asilimia

Idadi ya Matawi ya ASP

257

100.00

Yaliyokubali

257

100.00

Yaliyokataa

0

0.00

Idadi ya Wanachama Wote Walioshiriki

103,983

100.00

Waliokubali

103,574

99.06

Waliokataa

409

0.04

Chanzo:       Tathmini ya Miaka 20 ya CCM, 1977 – 1997.

 

Yaani wanachama wa TANU katika katika 99.95 ya matawi yao  yaliyotoa maoni na matawi yote madogo waliafiki chama chao kuunganishwa na ASP.  Kwa upande wa Zanzibar, wanachama wa ASP katika matawi yao yote waliafiki chama chao kiunganishwe na TANU.  Na kwa wanachama mmoja mmoja walioshiriki katika kura hiyo ya maoni, ni 409 tu kati ya wote 103,983, yaani sawa na asilimia 0.04 tu ndio waliokataa.

 

Huu ulikuwa ni ushahidi madhubuti usio shaka wa kitakwimu wa imani ya wananchi kwa Muungano.  Kwa kura hiyo, watu wa Tanganyika na Zanzibar kupitia vyama vyao vya TANU na ASP ambavyo vilikuwa pekee wakati huo, waliuthibitishia Ulimwengu kwamba Muungano ni wao na haukuwa wa viongozi tu kama inavyodaiwa na wapinzani wachache wa Muungano.

 

Kabla ya kuunganishwa kwa TANU na ASP, Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar iliitaja Jamhuri hiyo kuwa ni ya mfumo wa chama kimoja ambapo kwa Tanganyika Chama hicho ni TANU na kwa Zanzibar chama hicho ni ASP.  Kwa maneno mengine, Jamhuri ilikuwa chini ya chama kimoja kwa viwili, jambo ambalo lilileta dosari kubwa katika uimara wa Muungano.  Baada ya TANU na ASP kuungana na kuwa CCM, dosari hiyo iliondolewa na hivyo kikawa ni kitendo cha kuimarisha Muungano.  Zaidi ya yote, tukio hilo ndilo lililochochea kutungwa rasmi kwa Katiba ya Kudumu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977.

 

Kwa hivyo, kwa majumuisho, inasisitizwa tena kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni wa watu wenyewe.  Waasisi wa Muungano huo, yaani Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Abeid Amani Karume kupitia Serikali zao, waliwezesha tu kufikiwa kwa matarajio ya wananchi wenyewe.  Mzee Karume alilielezea tukio hilo kwa maneno yafuatayo kama alivyonukuliwa na Rais Benjamin Mkapa katika hotuba yake ya tarehe 26 Aprili, 2004:-

 

Napenda mfahamu wananchi wote, kazi hii si kazi ya Abeid Karume.  Jambo hili, jambo la wenyewe Waafrika wote.  Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Karume wao ni watumishi wa wenyewe wana wa nchi, na sisi tumekubali kuwatumikia wenyewe wananchi.  Tunawatumikia wananchi kwa utumishi wao maalum, ule walioona wao wenyewe bora.  Basi jambo hili la kufanya Union, Tanganyika na Zanzibar, ni jambo ambalo lililofikiriwa na wenyewe wananchi wa Tanganyika na Zanzibar

 

Hatimaye, mwaka 1977, watu wenyewe, kupitia vyama vyao waliithibitisha hatua ya Waasisi ya kuunganisha Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.

 

Hiki ni kielelezo cha wazi cha umadhubuti wa nguzo hii ya Muungano ya kwamba Muungano ni wa watu wenyewe, na jinsi nguzo hii inavyoupa uhalali wa kijamii na hata wa kisiasa Muungano wetu.

 

Nguzo Ya Msukumo wa Kujenga Umoja wa Afrika

 

Nguzo ya pili inayouhimili Muungano ni utashi wa kujenga umoja wa Afrika.  Manifesto (Ilani za Uchaguzi) za TANU na ASP toka enzi za mapambano ya kudai uhuru zilikuwa na vipengele vya kutaka umoja wa Afrika.  Aidha, vyama vyote vilishiriki kikamilifu katika majukwaa yote yaliyowaunganisha Waafrika wa nchi mbali mbali katika kudai uhuru kwa lengo la kuja kuziunganisha nchi hizo baada ya uhuru.  Kwa mfano, TANU na ASP zilikuwa wanachama wa PAFMECA na baadae PAFMECSA, vyombo ambavyo viliviweka pamoja vyama vilivyokuwa vikidai uhuru kutoka nchi mbali mbali za eneo la Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.  Katika hili, hata Chama cha Hizbu (ZNP) cha Zanzibar kilikuwa kikishiriki.

 

Katika jitihada za kufikia ndoto hiyo ya umoja wa Afrika, nchi za Afrika Mashariki (yaani Kenya, Uganda, Tanganyika na Zanzibar) zilijaribu kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki baada ya uhuru wa nchi hizo.  Baada ya kuona dalili za kukawia kufikiwa kwa lengo hilo katika upeo wa Afrika Mashariki, Rais Nyerere wa Jamhuri ya Tanganyika na Rais Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar walikubaliana zianze Tanganyika na Zanzibar ili kuonyesha njia na kuendeleza shauku ya kutafuta umoja wa Afrika.  Dhamira hiyo inajieleza katika maneno ya Mwalimu Nyerere katika hotuba yake katika Mkutano Maalumu wa Bunge la Tanganyika, tarehe 25 Aprili, 1964, lililoitishwa kujadili na kuridhia Hati ya Muungano.  Mwalimu anajinukuu katika kitabu chake cha “Uhuru na Umoja kama ifuatavyo:-

 

Ikiwa, basi, nchi ambazo ni marafiki na ni jirani, na hasa zile ambazo zilipata kuwa moja bali zikagawanywa na wakoloni wapya; ikiwa hizo zitashindwa kuungana, kushindwa huko kunaweza kukaleta wasi wasi katika bara letu la Afrika na shauku yake ya Umoja.  Bali ikiwa nchi hizo zaweza kuungana, muungano huo waweza ukawa ni thibitisho la vitendo kwamba matumaini ya bara letu si ya bure. (uk.292).

 

Miaka miwili baadae, wakati wa sherehe za Muungano kutimiza miaka miwili zilizofanyika Dar es Salaam mwaka 1966, Mzee Karume naye aliithibitisha dhamira hiyo.  Kama alivyonukuliwa na Rais Benjamin Mkapa katika hotuba yake ya kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2004 mjini Zanzibar, Mzee Karume alisema yafuatayo:-

 

Muungano wa Tanzania unaonyesha mithali katika Afrika.  Mithali yenyewe (ni) kuthibitisha nini viongozi wa Kiafrika kabla ya hawajapata independence walikuwa wakisema.  Neno lililokuwa likisemwa ni hili hapa – Tanzania (Muungano).  Ya kwamba kila mmoja akijitapa, “mara tu nikipata Serikali yangu katika nchi yangu lazima nilete uhusiano na Muungano wa Uafrika, tuzidi kuendelea kwa maendeleo yaliyo bora.”  Lakini si bahati mbaya (kuwa hawajatekeleza).  Watanzania mjue kuwa si bahati mbaya.  Bahati nzuri, Muungano ndiyo huu hapa.  Watanzania tena mnataka nini? …

Muungano wa Tanzania ndiyo hatua ya mwanzo. Na msife moyo wananchi wa Tanzania.  Wenzetu wako jirani watakuja unga.

 

Muungano wa Tanzania ni kani inayoendeleza uhai wa dhamira ya kuwaunganisha Waafrika na hivyo umeijengea heshima kubwa nchi yetu.  Uhai wa dhamira hiyo inayopata msukumo kutokana na Muungano wetu, unajidhihirisha katika kuingia hatua ya kuanzishwa kwa Umoja wa Afrika (African Union) wenye nguvu zaidi kutoka hatua ya uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU).  Na katika eneo letu la Afrika Mashariki, hatua za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki zimefufuliwa kutokana na uhai wa dhamira hiyo.

 

Kwa hivyo, nguzo hii ya msukumo wa kujenga umoja wa Afrika imeupa pia Muungano wetu uhalali wa siasa za kimataifa, hasa Barani Afrika.  Watanzania wanajivunia heshima hii na wanapenda iendelee.  Heshima hiyo itaendelea tu kwa kuudumisha Muungano na kamwe si kwa kuudhofisha au kuuvunja.

 

Nguzo ya Kisheria

 

Nguzo ya tatu inayouhimili na kuupa uhalali Muungano wa Tanzania ni ukweli kwamba Muungano huo umesimama juu ya msingi wa sheria za nchi na za kimataifa.  Ulijadiliwa, ukatungiwa mkataba wa kimataifa (Hati ya Muungano) ambao ulitiwa saini tarehe 22 Aprili, 1964 na Wakuu wa Nchi (Marais Nyerere na Karume) na hatimae kuridhiwa na Mabaraza ya kutunga sheria ya nchi zote mbili (yaani Bunge la Tanganyika na Baraza la Mapinduzi la Zanzibar) kwa niaba ya wananchi wao.

 

Kama itavyoonekana baadae, wapo waliowahi kudhani kwamba kwa upande wa Zanzibar, hatua za kuuhalalisha Muungano kisheria hazikutimia kwa madai eti kwamba Hati ya Muungano haikuridhiwa na baraza la kutunga sheria kwa niaba ya wananchi.  Lakini hoja yao ilinyauka pale walipozinduliwa kwamba wasilitazame Baraza la Mapinduzi kwa sura yake ya Baraza la Mawaziri tu, bali walione pia katika sura yake ya pili liliyokuwa nayo wakati huo ya Baraza la Kutunga Sheria.

 

 

 

 

Nguzo ya Uendelevu

 

Nguzo ya nne inayouhimili na kuupa uhalali wa kisiasa Muungano wa Tanzania na ambayo inaendelea kuimarika kila kukicha, ni uendelevu wa Muungano wenyewe.  Hadi sasa, miaka arobaini baada ya kuasisiwa kwake, Muungano huu unabaki kuwa mfano pekee Barani Afrika wa muungano wa nchi zilizo huru uliodumu.  Kama ilivyokwishagusiwa kabla, juhudi za kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki mara tu baada ya uhuru, zilivia.  Ulijaribiwa pia Muungano wa Misri, Libya na Syria (ulioitwa Jamhuri ya Umoja wa Kiarabu) katika miaka ya sitini, lakini haukufika mbali.  Senegal na Gambia nazo zilijaribu Senegambia katika miaka ya themanini lakini bila ya mafanikio.

 

Kama itavyofafanuliwa baadae, Muungano wa Tanzania umefaulu majaribu mengi.  Badala ya kuudhofisha, majaribu hayo yamekuwa yakiuimarisha zaidi. Muungano ulianza na mambo 11 tu katika orodha ya mambo ya Muungano, lakini hivi sasa yamefikia 22.  Wasioutakia mema Muungano wamekuwa wakidai kwamba eti mambo yaliyoongezwa yaliingizwa kinyemela na kwa kuiburuza Zanzibar.  Lakini madai kama hayo ambayo hayana chembe ya ukweli, mara nyingine yamekuwa yakiambatana na unafiki.  Kwa mfano, waliosimamia na kuhakikisha Usalama wa Taifa wa Zanzibar unawekwa chini ya Serikali ya Muungano mwaka 1984, ndio hao hao sasa wanaoongoza kampeni ya kutaka Watanzania na hasa Wazanzibari waamini kwamba eti mambo yanaingizwa kiholela tu na kwa kuwaburuza Wabunge wa Zanzibar kutokana na uchache wao Bungeni.

 

Ukweli ni kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayalinda vya kutosha maslahi ya Zanzibar kwani inatamka wazi kwamba hakuna jambo litaloongezwa au kupunguzwa katika orodha ya mambo ya Zanzibar ila kwa thuluthi mbili ya kura za Wabunge wanaotoka Zanzibar na thuluthi mbili za Wabunge kutoka Bara.  Kwa hivyo, wingi wa Wabunge wa Bara hauna nafasi ya kuwaburuza wenzao wa Zanzibar.

 

Itoshe tu kusisitiza kwamba uendelevu wa Muungano ni nguzo madhubuti ya kuuhimili Muungano huu ambayo pia inaupa uhalali wa kisiasa za ndani.

 

Katika sehemu hii, zimezungumziwa nguzo nne zinazouhimili Muungano wa Tanzania na hata kuupa sura mbali mbali za uhalali.  Ni kutokana na umadhubuti wa nguzo hizo ndiyo maana umehimili na unaendelea kuhimili misukosuko mbali mbali kama itavyofafanuliwa baadae.  Katika hotuba yake ya kuliaga Bunge tarehe 28 Julai, 1995, Rais Ali Hassan Mwinyi ambae alikuwa anastaafu wakati huo alisema kwa fahari kubwa:-

         

Katika kipindi hiki Muungano wetu umepita katika tanuri la moto na kutokea upande wa pili ukiwa bado imara na wenye nguvu.  Matatizo yaliyojitokeza yalishughulikiwa kwa ukamilifu na katika hali ya maelewano baina ya pande zote mbili.  Tumefanya pia marekebisho katika Katiba ambayo nina imani yatazidi kuimarisha Muungano wetu katika kipindi hiki cha mageuzi ya kisiasa na kiuchumi.

 

 

SABABU ZA MUUNGANO

 

Kwa kadiri CCM inavyohusika, sababu kubwa na za msingi zilizowaongoza Waasisi wa Muungano katika kuuanzisha  ni hizi tatu zifuatazo:-

1.                 Kuurejesha na kuuthitibisha umoja wa watu waliokuwa wametenganishwa.

2.                 Kutekeleza azma ya kujenga umoja wa Afrika.

3.                 Kulinda Uhuru wa Tanganyika na Mapinduzi ya Zanzibar.

 

Sababu mbili za kwanza zimekwishajadiliwa kwa kina hapo kabla na hivyo hapana haja ya kuurejea mjadala huo.  Kwa sababu ya tatu, ufafanuzi unapatikana kutokana na maelezo ya Sheikh Thabit Kombo kama alivyonukuliwa na Rais Mkapa katika hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano.  Maelezo hayo yaliyotolewa kama faida ya Muungano ni kama yafuatavyo:-

 

  Matumaini ya kudumu kwa amani na usalama yamekuwa makubwa kwa nchi zote mbili; wasiwasi mwingi wa usalama umeondoka.  Fikiri mwenyewe kusingekuwako muungano, na maadui wa Zanzibar wakazidisha vitimbi vyao, kusingekuwako usalama wala amani; si Bara wala si hapa Zanzibar.  Lakini kwa nguvu za muungano wakorofi wanasita kidogo …

Lakini usingekuwako muungano tungekuwa na hasara kubwa, kwa Tanganyika na kwa Zanzibar pia.  Zanzibar pamoja na mapinduzi yake, ingedumu katika wasiwasi kwamba mbinu zingeweza kutumika kumrudisha Sultani.  Na Tanganyika nayo pamoja na ukubwa wake, isingekuwa salama kabisa kama kungekuwako vurugu visiwani hapa.  Maadui wangeweza kuitumia Zanzibar kuihujumu Tanganyika kwa urahisi sana

 

Pamoja na kwamba kauli hiyo ya hadharani ilitoka muda mrefu baada ya Mapinduzi, ipo kila sababu ya kuamini kwamba suala la usalama wa Mapinduzi ya Zanzibar na hata Uhuru wa Tanganyika ni miongoni mwa mambo yaliyozingatiwa wakati wa mazungumzo ya Muungano.  Na pengine ndilo lililochangia katika kuharakisha Muungano hasa ikizingatiwa ukweli kwamba watawala waliopinduliwa Zanzibar walikuwa wamekimbilia nje ambako wangeweza kupanga mbinu za kujaribu kurudisha utawala wao.  Hao ni maadui wa Mapindizi ambao wasingeweza kupuuzwa.  Na hofu hiyo ilithibitishwa na majaribio 17 ya mapinduzi yaliyofanywa bila ya mafanikio na maadui wa Mapinduzi ya 1964.  Muungano bila shaka una mchango wake katika kuyaviza majaribio hayo.

 

Kumekuwa pia na hoja kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulipata msukumo kutokana na vita baridi vya wakati huo kati ya Marekani na Urusi na kambi zao.  Hoja ni kwamba eti Marekani ndiyo iliyoshawishi ufanyike Muungano kwa lengo la kuidhibiti Zanzibar eti isiwe “Cuba ya Afrika”.  Wana-CCM hawaafikiani na hoja hiyo.  Mtazamo wao ni kwamba kama kweli Wamarekani walikuwa na mawazo hayo, hawakwenda zaidi ya kuomba Mungu tu tukio hilo litokee.  Lakini wenyewe Watanganyika na Wazanzibari waliungana kwa utashi wao na kwa maslahi yao.  Hawakuwa na habari na ndoto za Marekani na maslahi yake.

 

Katika hili, Rais Mkapa alitoa msisitizo ufuatao katika hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano:-

  wapo wanaodhani Muungano wetu ulikuwa lazima wakati ule kwa sababu tu ya vita baridi duniani, na mapambano ya mataifa makubwa kutafuta himaya barani Afrika.  Swali linabaki.   Vita baridi vilikwisha, na harakati za wakubwa kujenga himaya Afrika nazo zimekwisha.  Lakini Muungano unaendelea, kwa nini?  Kwa sababu msingi wa Muungano haukuwa vita baridi, bali shauku kubwa – iliyozuiliwa na wakoloni kwa miaka mingi – ya watu wa Tanganyika na Zanzibar kuungana kama walivyokuwa zamani.

 

KWA NINI SERIKALI MBILI?

 

Muundo wa Muungano wa Tanzania ni wa Serikali mbili; yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambayo inashughulikia mambo ya Muungano na mambo yote ya Tanzania Bara (baada ya Serikali ya Tanganyika kufa) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoshughulikia mambo yasiyokuwa ya Muungano kwa upande wa Zanzibar.

 

Muundo huu umekuwa jambo la mjadala mkubwa na wenye kuendelea miongoni mwa Watanzania.  Wapo wanaouona muundo huu kuwa haufai kwa kuwa ni tofauti na miungano mingine inayojulikana duniani.  Wapo wanaoamini kuwa unasababisha kero nyingi na hivyo haukidhi matarajio ya Watanzania.  Wapo wanaoamini kuwa haupendwi na Watanzania.  Wapo pia waliojaribu kujenga hoja kwamba eti Waasisi wa Muungano walipokuwa wanaunganisha nchi hizi mbili, lengo lao la baadae lilikuwa ni muungano wa Serikali moja na kwamba huu wa  Serikali mbili ulikusudiwa uwe wa muda tu.  Wapo wengine waliojaribu kujenga hoja kwamba eti Waasisi hao walichounda ni Shirikisho la Serikali tatu ambapo Serikali ya Tanganyika “imefichwa” ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

 

CCM inatofautiana na mawazo yote hayo.  Kufaa au kutokufaa na kukubalika au kutokubalika kwa muundo huu kwa Watanzania kutajadiliwa baadae chini ya Misukosuko Iliyohimiliwa Na Muungano. 

 

Katika sehemu hii, inatazamwa dhamira halisi ya Waasisi katika kufikia uamuzi wa Muundo huu.   CCM inaamini kwamba Waasisi walikusudia muundo wa Serikali mbili na walikuwa wanakijua walichokuwa wanafanya.  Wao wenyewe ndio walioijua zaidi dhamira yao kuliko wale wanaojaribu kuitafsiri.

 

Kwa mnasaba huo, tunaanza na kuwanukuu kauli zao kama walivyosema wenyewe.

 

Katika “Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania, Mwalimu Nyerere anaifichua dhamira yao na sababu za kuamua muundo wa Serikali mbili kama ifuatavyo:-

 

Nchi mbili zinapoungana na kuwa Nchi Moja mifumo ya kawaida ya miundo ya Katiba ni miwili:  Muungano wa Serikali Moja, au Shirikisho la Serikali Tatu.  Kwa mfumo wa kwanza kila nchi itafuta Serikali yake, na Nchi mpya inayozaliwa itakuwa ni Nchi Moja yenye Serikali Moja.  Katika mfumo wa pili kila Nchi itajivua madaraka fulani ambayo yatashikwa na Serikali ya Shirikisho, na itakuwa Serikali ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo yaliyobaki….

 

Tanganyika na Zanzibar zilipoamua kuungana na kuwa Nchi Moja, tungeweza kufuata mmojawapo wa mifumo hiyo ya kawaida.  Lakini tulishindwa kufanya hivyo kwa sababu ya udogo wa Zanzibar na ukubwa wa Tanganyika.  Zanzibar ilikuwa na watu laki tatu (300,000) na Tanganyika watu milioni kumi na mbili (12,000,000).  Muungano wa Serikali Moja ungefanya ionekane kama Tanganyika imeimeza Zanzibar.  Tulikuwa tunapigania Uhuru na Umoja wa Afrika; hatukutaka tudhaniwe, hata kwa makosa, kwamba tunaanzisha ubeberu mpya1  Kwa hiyo mimi nilipinga mfumo wa Serikali Moja.  Shirikisho la Serikali Tatu lingekuwa ni gharama kubwa mno kwa Tanganyika.  Zanzibar ingeendesha Serikali yake na kuchangia gharama za kuendesha serikali ya Shirikisho; na Tanganyika ingefanya vivyo hivyo.  Lakini ni dhahiri kwamba mchango wa Tanganyika ndio hasa ungeendesha Serikali yake ya watu 12,000,000 na pia ndiyo ingetoa sehemu kubwa ya kuendesha Serikali ya Shirikisho la watu 12,300,000.  Ni watu wanaofikiri kwa ndimi zao wanaodhani kuwa gharama ya Serikali yo yote kati ya hizo ingekuwa ndogo.  Gharama ya Serikali ya Tanganyika isingekuwa ndogo, (waulizeni Wazanzibari) na wala Serikali ya Shirikisho isingekuwa ndogo, hata bila gharama za mambo yasiyo ya Shirikisho.  Na gharama zote hizo kwa kweli zingebebwa na Tanganyika.

 

Kwa hiyo ilitupasa tujiulize kwa nini tunataka kuibebesha Tanganyika gharama zote hizo; na hasa kwa nini tunataka Serikali ya Tanganyika?  Hivi tuna hofu ya kwamba Tanganyika, bila kuwa na Serikali yake, itaonekana kuwa imemezwa na Zanzibar?  Hofu yetu ni kwamba tukiwa na Serikali Moja Tanganyika itaonekana kuwa imeimeza Zanzibar.  Basi na tutafute muundo ambao utaiondolea Zanzibar hofu hii ya kumezwa, bila kuibebesha Tanganyika mzigo wa kuendesha Serikali mbili zenye uzito unaolingana.

         

Hivyo ndivyo tulivyofanya, na hiyo ndiyo asili ya muundo wa Muungano wa Serikali Mbili.  Badala ya kutungua mfumo uliopo kama wapumbavu, tulitazama hali halisi yetu ilivyokuwa na tukabuni mfumo utakaotufaa zaidi.  (uk.15 – 16).

 

Mzee Abeid Amani Karume kwa upande wake aliielezea kwa ushupavu zaidi dhamira ya kuunda Muungano kwa kutumia neno la Kiingereza la Union ili kuziba mwanya wa kubabaisha na shirikisho.  Katika hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano, Rais Mkapa alimnukuu Mzee Karume kutokana na hotuba yake maarufu aliyoitoa siku za mwanzoni za Muungano ambayo husikika sana katika redio.  Katika nukuu hiyo Mzee Karume alitamka yafuatayo:-

 

Leo tumekuja kuonana na nyinyi wananchi wote.  Na ikiwezekana kuusia mambo.  Sababu baadhi ya watu wengi, wanataka kufahamu (kuhakikishiwa kwamba) Serikali ya Unguja (kwa maana ya Zanzibar) na Serikali ya Tanganyika zimechanganyika, zimekuwa Union moja tu. …

 

Kwa hivyo, ni dhahiri kabisa kwamba walipoamua muundo huo wa Muungano walikuwa wanajua walichokuwa wanakifanya na walichokuwa wanakitaka.  Na wala haina maana kwamba labda walipoamua muundo huo walidhani hautokuwa na matatizo.  Matatizo walijua yatakuwepo lakini waliamua kwa makusudi wakabiliane nayo ndani ya Muungano badala ya kusubiri yamalizike kwanza ndio waunganishe nchi.  Ukweli huo unadhihirishwa katika kitabu cha ASP cha Maendeleo ya Mapinduzi ya Afro-Shirazi Party  1964 – 1974kama ifuatavyo:-

 

Nchi mbili huru, kama zilivyokuwa Zanzibar na Tanganyika, zinapoungana, kuna njia mbili za kuunganisha.  Njia ya kwanza ni kuungana kwa yale wanayokubaliana, hata yakiwa ni machache, madamu tu nia ipo, ni kuitekeleza ile nia na halafu zikaendelea kutanzua matatizo yao na kujenga juu ya ile nia iliyokwisha kutekelezwa.  Njia ya pili ni kukaa na kutanzua matatizo kwa makubaliano mpaka kifikilie kima cha makubaliano kiwezacho kuleta muungano.  Zote hizi njia mbili si rahisi na kila moja ina matatizo yake yanayoweza kuchukua muda mrefu kutanzuliwa.  Tanganyika na Zanzibar zilichukua njia ya kwanza, siyo kwamba ndiyo iliyokuwa rahisi, bali kwa sababu nchi mbili hizi zilikubaliana na kutekeleza nia yao ya kuungana na kutanzua matatizo yaliyosalia ya muungano huku zimo katika Muungano.  (uk.33).

 

Kwa hivyo, matatizo ambayo yamekuwa yakiukabili Muungano ambayo mengine yamefikia kuutia katika misukosuko mikubwa hayawezi yakawa ni kioja, kwani yalitabiriwa.   Hata hivyo, kuendelea kuimarika kwa Muungano ndani ya mazingira ya matatizo hayo, ni kielelezo cha udhati wa nia ya kuungana na usahihi wa uamuzi wa kuteua muundo wa Serikali mbili.

 

Katika hotuba yake ya kihistoria iliyoimarisha hoja ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2004 kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano, Rais Mkapa alitoa majumuisho mazuri ya suala hili kama ifuatavyo:-

 

Muungano wetu umefikisha miaka 40, na upo imara.  Nguvu yake ni Watanzania wenyewe, wengi wao – asilimia 84.8 – wakiwa hawajui uraia mwingine isipokuwa Utanzania.  Watanzania hawa waliozaliwa mwaka 1964 na kuendelea, ambao leo wana umri wa miaka 40 au chini zaidi, hawana uzoefu wa kuwa kitu kingine isipokuwa kuwa Watanzania.

 

Na hawajui mfumo mwingine wa Muungano isipokuwa mfumo wa Serikali mbili, wenye manufaa mawili makubwa ambayo ni sehemu ya msingi wa Muungano wetu.  Kwanza, mfumo huu unadhihirisha kuwa kweli sisi tumeungana,  serikali yetu ni muungano, si shirikisho.  Na, muungano ni imara kuliko shirikisho.

 

Msingi wa pili ni madaraka kamili ya Zanzibar kwa mambo ambayo si ya muungano.  Madaraka hayo yanasaidia kuhakikisha kuwa Zanzibar inahifadhi utambulisho wake na haimezwi na Tanzania Bara.  Wapo wanaoamini kuwa mfumo huu hauna haiba nzuri; ati haupendezi.  Kwao napenda kusema kuwa jambo muhimu kuliko yote katika msingi wa nyumba si sura yake, muhimu zaidi ni uimara wake.  Na mimi nakuhakikishieni, Ndugu Wananchi, kuwa mfumo wa Serikali mbili ndicho chombo imara kilichotuvusha salama katika bahari ya miaka 40 iliyopita, na Inshallah, ndicho kitatuvusha salama katika miaka ijayo.

MISUKOSUKO ILIYOHIMILIWA NA MUUNGANO

 

Kama ilivyokwishaelezewa, Muungano umeweza na unaendelea kuhimili misukosuko mingi.  Misukosuko hiyo imekuwa ni changamoto inayouwezesha kujidhatiti zaidi, kwani kila unapoishinda changamoto moja, unaibuka imara zaidi.  Hii ni kwa sababu changamoto hizo huwafanya wahusika, hasa Serikali zote mbili, kutoa ufafanuzi kusafisha upotoshaji unaotolewa au kuyafanyia kazi na kuyapatia ufumbuzi matatizo yanayojitokeza ambayo hutumiwa kuutia misukosuko Muungano.

 

Awali, misukosuko ilijikita zaidi katika kuhoji uhalali wa Muungano wenyewe.  Baadae, baada ya shaka kuondolewa kuhusu uhalali wake, misukosuko imeelekea zaidi katika kuhoji muundo wa Serikali mbili.

 

Kuhoji Muungano Wenyewe

 

Hoja ya kwamba Muungano haukuwa halali kwa sababu eti haukupata ridhaa ya wananchi na haukukamilisha taratibu za kisheria zilianza kusikika hadharani Zanzibar mwanzoni mwa miaka ya themanini.  Seif Sharif Hamad na wenzake ambao baadae walikiri kuwa walikuwa wapinzani ndani ya CCM na Serikali, waliitumia fursa iliyotolewa kwa nia njema na CCM ya kuanzisha mjadala wa kitaifa wa marekebisho ya Katiba kutaka kuudhofisha au hata kuuvunja Muungano.  Watu hao hao ni wale wale ambao baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi waliunda chama chao cha CUF katika miaka ya tisini. 

 

Kipindi hicho cha msukosuko wa kwanza mkubwa kuutikisa Muungano kilikuwa baina ya 1983 na 1984 na kinajulikana kwa umaarufu wa kuchafuka kwa hali ya hewa ya kisiasa Zanzibar.  Madai yaliyokuwa yameshika nguvu wakati huo ni ya kudai kura ya maoni ya wananchi ili eti kuupa uhalali Muungano huo na kukamilisha hatua za kisheria.

 

Imekwishaelezewa kwa kina katika sehemu ya Nguzo za Muungano jinsi Muungano ulivyo na uhalali unaotokana na watu wenyewe, na kwamba umekidhi matakwa ya sheria.

 

Mtazamo wa CCM kuhusu kura za maoni ni kwamba si jambo la lazima na wala si njia pekee ya kupima utashi wa wananchi.  Hadi wakati Tanganyika na Zanzibar zinaungana hakukuwa na nchi duniani zilizokuwa zimeungana baada ya kuitishwa kura za maoni.  Miungano mikubwa mikubwa iliyodumu na iliyo madhubuti kabisa kama ile ya Marekani (USA) na Uingereza (UK) haikuanzishwa kwa kura za maoni.  Na wala hadi leo haikupigiwa kura za maoni za kuithibitisha.  Kinyume chake,Marekani iliwahi kuingia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kuulinda Muungano baada ya majimbo ya Kusini kutaka kujitoa.  Wanaolalamikia Muungano hupenda kutaja mifano ya nje kuzipa nguvu hoja zao, lakini mifano hii ya Marekani na Uingereza hawaitaji katika muktadha huu.  Kwa mazingira ya wakati ule na hasa kuzingatia usalama wa Mapinduzi ya Zanzibar, isingeweza kutumika njia nyengine zaidi ya iliyotumika.  Hata hivyo, suala hili la kura ya maoni lilikuwa agenda kuu ya uchaguzi katika Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa 1990 ambapo Dr. Salmin Amour alichaguliwa kuwa Rais wa tano wa Zanzibar.  Uchaguzi huo uliambatana na kampeni kubwa ya chini kwa chini iliyowataka watu waususie hadi kwanza itapoitishwa kura ya maoni.   Inasadikiwa katika CCM kwamba kampeni hiyo iliongozwa na kundi la wanasiasa chini ya uongozi wa Seif Sharif Hamad waliokuwa wamefukuzwa kutoka CCM kwa sababu za usaliti.  Ni watu hao hao ndio wanasadikiwa pia kuongoza kampeni ya chini kwa chini ya kutaka Sheikh Idris Abdul-Wakil apigiwe kura za HAPANA wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 1985.

 

Kampeni zote hizo hazikufanikiwa.  Kushindwa kwa kampeni ya 1990 iliyotaka kura za maoni kuliidhoofisha kwa kiasi kikubwa hoja ya kwamba Muungano eti Wazanzibari hawakuwa wameuridhia.  Kujitokeza kwa wingi kwa wananchi kupiga kura na kumchagua Dr. Salmin Amour ambae kampeni yake na ya CCM ilikuwa ya kupinga kura za maoni ulikuwa ushahidi wa kutosha kwamba Wazanzibari hawakuwa na tatizo na Muungano.

 

Kwa upande wa uhalali wa kisheria, kitendawili kiliteguliwa na Tume ya Chama Kimoja au Vyama Vingi (maarufu Tume ya Nyalali) katika miaka ya tisini.  Tume hiyo  ilijiridhisha kwamba Baraza la Mapinduzi la Zanzibar likikaa kama Baraza la