HOJA YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MUUNDO WAKE WA SERIKALI
MBILI
(Omar R. Mapuri)
UTANGULIZI
Hoja
ya Muungano wa Tanzania
inasimama juu ya msingi wa sera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Sera ya
CCM kuhusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kuwa Tanzania ina ncha
mbili; yaani kuulinda na kuudumisha Muungano wenyewe kwa upande mmoja na muundo
wa Muungano huo kuwa wa Serikali mbili kwa upande wa pili.
CCM
inaushabikia Muungano na kupania kuulinda na kuudumisha kwa sababu kwanza
inaamini kuwa Muungano huu ni wa watu wenyewe na pili, uliasisiwa na vyama
wazazi wake, yaani TANU na ASP. Zaidi ya
hivyo, CCM yenyewe ni matokeo ya Muungano huo na chachu ya kuziimarisha kwani
tendo la kuviunganisha vyama vya TANU na ASP kuunda CCM lilitokana na utashi wa
kukamilisha hatua za kuunda Muungano.
CCM
inaunga mkono muundo wa Muungano wa Serikali mbili kwa sababu kwanza ndio
ulioamuliwa na waasisi wa Muungano, Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius K.
Nyerere na Mzee Abeid Amani Karume, na pili umezingatia vya kutosha uhalisi wa
mambo wa nchi kubwa na ndogo kuungana.
Muundo huo ndio unaohakikisha umadhubuti wa Muungano wenyewe bila ya
nchi ndogo (Zanzibar kwa muktadha huu) kumezwa
na nchi kubwa (Tanganyika).
CCM
inajivunia Muungano huu na muundo wake wa Serikali mbili kwani hata baada ya
miaka 40 ya kuundwa kwake bado ndio mfano pekee wa Muungano uliofanikiwa wa
nchi huru zilizoungana katika Bara la Afrika.
Zaidi ya yote, Muungano huu umeweza kuhimili misukosuko yote ya ndani
uliyokumbana nayo ambayo ingeweza kuudhofisha au hata kuuvunja.
Pamoja
na makelele mengi ya kisiasa yenye kuulalamikia, Muungano huu na muundo wake wa
Serikali mbili unaungwa mkono na Watanzania walio wengi. Ushahidi wa kitakwimu utatolewa katika makala
haya kwamba muundo wa Serikali mbili ndio unaotakiwa na Watanzania walio wengi,
na muundo wa Serikali tatu unaopigiwa debe sana na vyama vya upinzani na baadhi
ya wasomi ndio unaokataliwa na Watanzania wengi kuliko muundo mwingine wowote.
Kabla
ya kuendelea na hoja, inafaa katika hatua hii kutazama maandiko rasmi ya kisera
ya CCM kuhusu Muungano na muundo wake, kama
yalivyo katika Ilani za Uchaguzi za CCM za 1995 na 2000.
Ibara
ya 47 ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 1995 inasomeka ifuatavyo:
47.
Sera ya
Kuimarisha Muungano
Muundo wa
Muungano, ambao unakubaliwa na CCM, ni Muungano wenye Serikali mbili: Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Sera hii imethibitishwa mwaka 1994 wakati
wanachama wetu walio wengi walioshiriki katika kura za maoni kote nchini
walitaka sera hii iendelee. Katika
kipindi cha miaka mitano ijayo, CCM itaendelea kudumisha Muungano wa Tanzania katika
muundo wa Serikali mbili.
Kwa
upande wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000, ibara zinazozungumzia
kuimarisha Muungano ni za 116 na 117 ambazo zinasomeka ifuatavyo:-
116. Umoja wa kitaifa wa Watanzania ambao umedumu
kwa kipindi kisichopungua miaka 36 unatokana na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
ambao ulizaa Tanzania. Katika kipindi chote hicho muundo wa muungano
ambao umeendelea kukubaliwa na Chama Cha Mapinduzi ni muungano wenye Serikali
mbili: Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania
na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Sera
hii imeendelea kuthibitishwa na wanachama wa CCM na wananchi kwa jumla.
117.
Katika kipindi cha miaka mitano ijayo (2000 – 2005)
Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuhakikisha kuwa mafanikio yaliyorithiwa kutoka
kwa Waasisi wa taifa letu Baba wa Taifa, Mwalimu J.K. Nyerere na Makamu wake wa
Kwanza Sheikh Abeid Aman Karume yanaendelezwa na kulindwa kwa kuhakikisha kuwa
Tanzania inaendelea kuwa huru, Taifa lenye Umoja, Udugu na Mshikamano na nchi
yenye amani na utulivu. Aidha, muundo wa
Muungano utaendelea kuwa wa Serikali mbili: yaani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Hivyo
ndivyo inavyosema Sera ya CCM kuhusu Muungano na muundo wake. Ni muhimu hili kuwekwa sawa kwani wapinzani
wa CCM, hasa kule Zanzibar,
hupenda kujichukulia uhuru wasiopewa wa kuisemea CCM wapendavyo wao. Hupenda sana
kuipotosha sera hii kwa kuinukuu kilaghai kwamba eti “ni ya Serikali mbili
kuelekea moja”. Kauli hiyo imewahi
kutoka katika vikao vya CCM kama kauli nyingi
nyenginezo zilivyowahi kutoka. Kwa
mfano, Bunge, likiwa na Wabunge wa CCM watupu liliwahi kupitisha azimio la
kutaka kuundwa kwa “Serikali ya Tanganyika
ndani ya Muungano”. Lakini baada ya yote
hayo na kauli zote zilizosemwa na/au kuandikwa, ulipofika wakati wa kutunga
sera rasmi, Chama kiliamua bila ya kigugumizi kuendelea na sera ya Muungano wa
Serikali mbili na kuiweka kwa uwazi na bila ubabaishaji katika Ilani za
Uchaguzi.
NGUZO ZA MUUNGANO
Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar ulijengwa juu ya
msingi wa kijiografia na kihistoria uliowafanya watu wa maeneo haya kuwa
wamoja, ndugu, wenye tamaduni zilizoingiliana na hata wenye utashi wa kisiasa
uliofanana.
Juu
ya msingi huo, zimesimama nguzo nne zinazouhimili Muungano huo. Nguzo ya kwanza ambayo imejengeka kwa muda
mrefu katika historia ni kwamba Muungano huu ni wa watu wenyewe. Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kijamii
na hata wa kisiasa. Nguzo ya pili ni
msukumo wa kujenga umoja wa Afrika.
Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kisiasa za kimataifa. Nguzo ya tatu ni Hati ya Muungano ambayo
iliujengea Muungano uhalali wa kisheria ambao unaendelezwa na Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ya
1977 na Katiba ya Zanzibar
ya 1984. Nguzo ya nne inayouhimili
Muungano na ambayo inaendelea kujengeka ni ya uendelevu wa Muungano
wenyewe. Muungano wa Tanzania
umeshatimiza miaka 40 ukiendelea kuimarika.
Umeweza na unaendelea kuhimili misukosuko mingi, ambapo kila unapoingia
kwenye tanuri la misukosuko, unaibuka ukiwa imara zaidi. Nguzo hii inaupa Muungano uhalali wa kisiasa
za ndani.
Sasa
tuzitazame nguzo hizi moja moja.
Nguzo Ya Umoja wa Watu Wenyewe
Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar umejengeka kutokana na mahusiano ya dahari na
karne baina ya watu wa visiwa vya Zanzibar
na mwambao wa Afrika ya Mashariki, hasa Mrima ambayo ni sehemu kubwa ya
Tanzania Bara ya sasa.
Kabla
ya Kuja Kwa Wageni Toka Nje ya Afrika
Wanahistoria
(mfano Ingrams) wakijenga hoja kutokana na maandiko ya kale ya Periplus (karne ya kwanza AD) na ngano
za watu wa kale, wanakubaliana kwamba watu wa kwanza kabisa kufika katika
visiwa vya Zanzibar
ni Waafrika kutoka Mrima katika harakati za uvuvi. Ushahidi wa kiakiolojia wa hivi karibuni
umethibitisha usahihi wa imani hiyo.
Wakati
wa Himaya ya Zenj
Lakini
hata baada ya kuja kwa wageni kutoka nje ya Afrika, mahusiano ya watu wa pande
hizi mbili siyo tu yaliendelea, bali yalizidi kuimarika hasa kutokana na
kuongezeka kwa ubora wa teknolojia ya usafiri wa baharini. Himaya ya Waajemi (Washirazi) katika eneo
hili ambayo baadhi ya wanahistoria wanaiita Himaya ya Zenj (Zenj Empire) ilipojengeka kutokana na ujio wa wale Ndugu saba
wa El-Hasa mnamo karne ya 13 ambao
walianzisha tawala katika vituo mbali mbali vya mwambao wa Afrika Mashariki
(mfano Kilwa, Barawa, Lamu, Unguja, Pemba,
n.k.), maingiliano ya watu wa maeneo haya yaliendelea bila ya vikwazo.
Wakati
wa Himaya ya Biashara ya Zanzibar
Mnamo
karne za 16 hadi katikati ya 19, ilijengeka Himaya ya Kibiashara ambayo kitovu
chake kilikuwa Zanzibar. Himaya hiyo iliyojumuisha biashara ya
watumwa, vipusa na viungo, ilienea hadi maeneo ya Maziwa Makuu kwa upande wa
Kaskazini Magharibi na maeneo ya Ziwa Nyasa na Mto Ruvuma kwa upande wa Kusini
mwa Tanzania
ya leo. Katika kitabu chake cha “Slaves,
Spices & Ivory in Zanzibar” Profesa Abdul Sheriff anazungumzia dhana
ya Bara ya Zanzibar (The Hinterland of Zanzibar) akiwa na maana ya eneo la Bara lililokuwa chini ya
ushawishi wa Zanzibar
(bila shaka na Sultani wake), ambalo kwa kiasi kikubwa ni hili hili eneo la
Tanzania Bara ya leo. Dhana hiyo ilipewa
methali maarufu ya: “Inapopigwa ngoma Zanzibar,
wanacheza katika Maziwa Makuu”.
Maelezo
haya yanajaribu kujenga hoja kwamba eneo ambalo leo linaitwa Tanzania, kwa kiasi kikubwa ndilo lililokuwa
Himaya ya Kibiashara ya Zanzibar
ya enzi hizo. Kwa maneno mengine nchi
hii ilikuwa moja toka enzi hizo ingawa yenye mipaka hafifu. Watu wa eneo lote hili waliunganishwa na
harakati za biashara. Biashara ya utumwa
iliwafanya wa huku waende kule na wa kule waje huku, ingawa katika mazingira ya
uchungu. Watumwa walichukuliwa Bara na
kupelekwa visiwani Zanzibar
ambako vizazi vyao vimeendelea hadi leo na kufanya sehemu kubwa ya
Wazanzibari. Kwa upande mwengine, wako
wafanyabiashara ya watumwa walioanzia Zanzibar
na kuhamia Bara na kufanya maskani yao
huko. Vizazi vyao vinaendelea hadi leo
na wamekuwa sehemu ya jamii ya Watanzania Bara.
Hivi sasa, katika mazingira ya uhuru, watu wa kila upande kati ya pande
mbili hizi wanaendelea kuhamia na kuweka maskani katika upande wa pili bila ya
vikwazo.
Utenganishi
wa Wakoloni wa Kizungu
Kitendo
kilichowatenganisha watu wa pande hizi ni kile cha wakoloni kutoka Ulaya
(Wazungu) kugawana makoloni katika Bara la Afrika, katika nusu ya pili ya karne
ya 19. Baada ya kinyang’anyiro baina yao, wakoloni hao walikutana katika Mkutano wa Berlin wa 1887 ambapo
waligawana Afrika. Katika mgao huo, sehemu
ya Bara (ukiondoa ukanda wa mwambao wa pwani ulioitwa Mrima) walipewa
Wajerumani. Koloni hilo
ambalo lilijumuisha Burundi
na Rwanda
ya sasa liliitwa Deutsche Ost Afrika (yaani
Afrika Mashariki ya Wajerumani). Sultani
wa Zanzibar aliachiwa visiwa vya Unguja, Pemba na Mafia na ukanda wa Mrima. Miaka mitatu baadae, chini ya Mkataba wa Heligoland wa 1890, Sultani alilazimishwa kuuza kwa Wajerumani ukanda wa Mrima na
kisiwa cha Mafia, na hivyo kubakiwa na
visiwa vya Unguja na Pemba tu, na yeye mwenyewe kuwekwa chini ya Himaya ya
Mwingereza. Watu wa Bara na Visiwani
wakawa wametenganishwa.
Kuanza
Kurejeana
Baada
ya Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia (1915 –
1919), majaaliwa yalianza kuwakurubisha tena watu wa pande hizi mbili. Kufuatia kushindwa kwa Wajerumani katika vita
hivyo, Rwanda na Burundi walipewa Wabelgiji na sehemu iliyobaki
ya Deutsch Ost Afrika iliitwa Tanganyika Territory
na kupewa Waingereza. Kwa hivyo watu wa Zanzibar na Tanganyika ingawa waliendelea kuwa
na nchi mbili tofauti, lakini angalau wakawa chini ya mkoloni mmoja.
Hali
hiyo ilijenga mazingira ya kuweza kurejea kwa mawasiliano baina ya watu wa Bara
na wa Visiwani ambayo yalikuwa yameathirika vibaya kwa kipindi cha kiasi cha
miaka 30. Mwamko wa kudai uhuru wa
kijamii na baadae wa kisiasa ulipoanza kujengeka, watu wa pande hizi mbili,
hususan wenyeji wa asli (yaani Waafrika) hawakusita kuitumia fursa hiyo
kushirikiana na kusaidiana katika azma hiyo.
Mwaka
1927, Waafrika wa Dar es Salaam walianzisha
jumuiya yao iliyoitwa “African Association” kwa ajili ya kupigania maslahi yao ya kijamii. Mwaka 1934, Waafrika wa Zanzibar
nao walianzisha “African Association”
yao, pengine kutokana na ushawishi wa ndugu zao
wa Dar es Salaam. Nao Waafrika wa Zanzibar
wakawashawishi wale wa Dodoma na kupelekea
kuundwa kwa “African Association” ya Dodoma. Jumuiya tatu hizi zilijenga umoja wa kufanya
mikutano mikuu ya pamoja ya mwaka kwa zamu baina ya miji hiyo, na zilikuwa
chachu ya kufunguliwa kwa matawi ya “African
Association” katika miji mbali mbali Tanganyika
na Zanzibar.
Ziara
za Michezo
Sambamba
na ushirikiano huo wa kijamii, wananchi wa Tanganyika
na Zanzibar
walianzisha utamaduni wa kubadilishana ziara za kimichezo. Ziara hizo zilikuwa zikifanyika wakati wa
mapumziko ya Pasaka, kwa utaratibu wa zamu ambapo kama mwaka huu wanamichezo wa
Zanzibar wanakwenda Tanganyika,
mwaka ujao wa Tanganyika
watakwenda Zanzibar. Utamaduni huo unaendelea hadi leo na umezidi
kupanuka kwa kujumuisha wasanii na hata wananchi tu wa kawaida.
Ushirikiano
wa Kisiasa
Upepo
wa harakati za kudai uhuru kutoka kwa wakoloni ulipofika maeneo haya, watu wa Tanganyika na Zanzibar
walihamasishana, kushirikiana na kusaidiana katika jukumu hilo la kudai na kupigania uhuru wa nchi
zao. Mwaka 1954, chama cha Tanganyika African National Union (TANU) kilianzishwa Tanganyika
kutokana na Tanganyika African
Association, kwa ajili ya kudai uhuru wa Tanganyika. Zanzibar
nako mwaka 1957 ilianzishwa Afro-Shirazi
Party (ASP) kutokana na kuungana kwa African
Association na Shirazi Association
(iliyokuwa imeundwa 1938). Kuundwa kwa
ASP kulishuhudiwa na Rais wa TANU, Mwalimu Julius K. Nyerere.
Ushirikiano
wa TANU na ASP katika mapambano ya kudai uhuru hadi ulipopatikana Uhuru wa
Tanganyika Disemba 9, 1961 na kufanikiwa kwa Mapinduzi ya Zanzibar Januari 12,
1964 unajulikana na hauna haja ya kuufafanua hapa. Dhamira angalau ya ASP (wakati wa kupigania
uhuru) ya kuiunganisha Zanzibar na Tanganyika
baada ya uhuru haikuwa siri. Hiyo
inadhihirishwa na maelezo yafuatayo ya Marehemu Sheikh Thabit Kombo kama
yalivyonukuliwa na Rais Benjamin Mkapa katika hotuba yake ya kihistoria
aliyoitoa Zanzibar
kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2004:-
Mafisadi
wanalalamika, kwa nini muungano umefanyika haraka haraka; Mapinduzi Januari na Muungano Aprili, miezi
mitatu tu! Wako wanaodhani kuwa Mwalimu
Nyerere ndiye aliyelazimisha Muungano.
Wazo la
Muungano ni wazo la Afro-Shirazi tokea mwanzo.
Utakumbuka katika Manifesto yetu tulisema kuwa tukipata Uhuru azma ya
ASP ni kuona kuwa Afrika yote inakuwa moja yenye nguvu. Lakini kwa Tanganyika
na Zanzibar ahadi ya muungano ni ahadi ya
wanachama wenyewe waliyokuwa wanaitoa katika mikutano yao yote…
Watu wa Tanganyika na watu wa Zanzibar ni wale wale, tofauti ni sisi wa Zanzibar kutawaliwa na
Sultani…. Mazungumzo yalikuwa mafupi
sana, yalichukua siku moja tu; maana hakukuwa na swali kama
tuungane au tusiungane. Hoja ilikuwa tu
muungano wetu uwe na sura gani…..
Muungano
Kama Tukio la Kimantiki
Kutokana
na ukweli huo wa kihistoria wa umoja, udugu na ushirikiano wa muda mrefu baina
ya watu wa pande hizi, na kufuatia TANU na ASP kushika madaraka baada ya Uhuru
na Mapinduzi, Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kuwa Tanzania uliokamilishwa
rasmi tarehe 26 Aprili, 1964 lilikuwa ni tukio la kimantiki na halipaswi kuwa
la kushangaza.
Ni
ukweli wa kihistoria kwamba pamoja na kwamba watu wa Tanganyika
na Zanzibar wamekuwa wamoja katika zama zote za
kihistoria, lakini Tanganyika
na Zanzibar
hazikuwa nchi tulizoziunda. Ziliundwa na
wakoloni na mipaka yake ilikuwa ikipangwa na kupanguliwa na wakoloni kwa
maslahi yao. Tanganyika
na Zanzibar
pamoja na mipaka yake tuliirithi tu kutoka kwa wakoloni baada ya uhuru. Lakini Tanzania tumeiunda wenyewe.. Katika kitabu chake cha “Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania”, Mwalimu Julius K. Nyerere
anasisitiza kwa fahari: Tanzania ni lulu ya pekee kabisa katika historia ya
Afrika huru. Nchi nyingine zote ni za
kurithi kutoka katika Ukoloni. Tanzania
ni ya kuundwa na sisi wenyewe, kwa hiari yetu wenyewe, baada ya kukomboa sehemu
zake mbili kutoka katika Ukoloni.
(uk.57).
Pamoja
na hayo, kama itakavyofafanuliwa baadae, wapo watu wanaoshangaa na kuhoji
uhalali wa Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar kwa
hoja kwamba eti hayakutafutwa maoni ya wananchi kwanza. Katika kuwabeza watu hao, Mwalimu Nyerere
katika kitabu chake hicho hicho cha “Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania”
anasema ifuatavyo kwa kejeli:-
Pwani ya Tanganyika na Zanzibar
ya sasa zilikuwa pamoja kwa muda mrefu sana
kabla ya kutengwa na Wakoloni Waingereza na Wajerumani. Kama zingebaki zimetengana, kwa “wazalendo”
hao hiyo ingekuwa ni halali, maana zilitengwa kwa hila na mitutu ya bunduki za
Mabwana. Lakini uamuzi wa Tanganyika
huru na Zanzibr huru kuungana, na hivyo kuwaunganisha tena ndugu waliokuwa
wametengwa na Mabeberu, tendo hilo
kuna … wanaosema kuwa halikuwa halali.
Hatukutafuta maoni ya watu kwa njia ya demokrasia wanayoijua wao. Wajerumani na Waingereza walitafuta maoni ya
wazee wetu kwa mtutu wa bunduki! Hiyo
ilikuwa halali. Nchi walizounda kwa njia
hizo zilikuwa halali. Tunatakiwa
tujivunie Utanganyika na Uzanzibari uliopatikana kwa njia hizo; lakini tuuonee
haya Utanzania, tunda la uhuru wetu wenyewe.
Sikuamini kuwa Wakoloni walifaulu kiasi hiki katika kuzinywesha kasumba
na kuzitawala akili za baadhi yetu!.
(uk.58).
Tarehe
5 Februari, 1977 vyama vya TANU na ASP viliungana na kufanya Chama Cha
Mapinduzi (CCM) katika tukio ambalo lilikuwa na maana ya kuzidi kuuimarisha
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Tena kuundwa kwa CCM kulitanguliwa na
mashauriano ya kutosha. Aidha, ilifanywa
kura ya maoni ya wanachama ambayo matokeo yake yalikuwa kama
yanavyoonekana katika Jedwali Na. 1 na 2 hapa chini:-
JEDWALI Na. 1: MATOKEO YA MAONI YA WANACHAMA WA TANU KUHUSU
KUUNGANISHWA TANU NA ASP
|
Matawi
|
Idadi
|
Asilimia
|
|
Idadi
ya Matawi Yote ya TANU
|
6,639
|
100.00
|
|
Yaliyokutana
|
6,427
|
96.81
|
|
Yasiyokutana
|
212
|
3.19
|
|
Yaliyokubali
|
5,424
|
99.95
|
|
Yaliyokataa
|
3
|
0.05
|
|
Idadi
ya Matawi Madogo ya TANU
|
38
|
100,00
|
|
Yaliyokutana
|
38
|
100.00
|
|
Yaliyokubali
|
38
|
100.00
|
|
Yaliyokataa
|
0
|
0.00
|
Chanzo: Tathmini ya Miaka 20 ya CCM, 1977 – 1997
JEDWALI Na. 2: MATOKEO YA VIKAO NA WANACHAMA WA ASP KUHUSU
MAONI YA KUUNGANISHWA TANU NA ASP
|
Matawi
|
Idadi
|
Asilimia
|
|
Idadi
ya Matawi ya ASP
|
257
|
100.00
|
|
Yaliyokubali
|
257
|
100.00
|
|
Yaliyokataa
|
0
|
0.00
|
|
Idadi
ya Wanachama Wote Walioshiriki
|
103,983
|
100.00
|
|
Waliokubali
|
103,574
|
99.06
|
|
Waliokataa
|
409
|
0.04
|
Chanzo: Tathmini ya Miaka 20 ya CCM, 1977 – 1997.
Yaani
wanachama wa TANU katika katika 99.95 ya matawi yao
yaliyotoa maoni na matawi yote madogo waliafiki chama chao kuunganishwa
na ASP. Kwa upande wa Zanzibar,
wanachama wa ASP katika matawi yao
yote waliafiki chama chao kiunganishwe na TANU.
Na kwa wanachama mmoja mmoja walioshiriki katika kura hiyo ya maoni, ni
409 tu kati ya wote 103,983, yaani sawa na asilimia 0.04 tu ndio waliokataa.
Huu
ulikuwa ni ushahidi madhubuti usio shaka wa kitakwimu wa imani ya wananchi kwa
Muungano. Kwa kura hiyo, watu wa
Tanganyika na Zanzibar kupitia vyama vyao vya TANU na ASP ambavyo vilikuwa
pekee wakati huo, waliuthibitishia Ulimwengu kwamba Muungano ni wao na haukuwa
wa viongozi tu kama inavyodaiwa na wapinzani wachache wa Muungano.
Kabla
ya kuunganishwa kwa TANU na ASP, Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanganyika na Zanzibar iliitaja Jamhuri hiyo kuwa ni ya mfumo wa chama kimoja
ambapo kwa Tanganyika Chama hicho ni TANU na kwa Zanzibar chama hicho ni
ASP. Kwa maneno mengine, Jamhuri ilikuwa
chini ya chama kimoja kwa viwili, jambo ambalo lilileta dosari kubwa katika
uimara wa Muungano. Baada ya TANU na ASP
kuungana na kuwa CCM, dosari hiyo iliondolewa na hivyo kikawa ni kitendo cha
kuimarisha Muungano. Zaidi ya yote,
tukio hilo ndilo lililochochea kutungwa rasmi
kwa Katiba ya Kudumu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977.
Kwa
hivyo, kwa majumuisho, inasisitizwa tena kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni wa watu wenyewe. Waasisi wa Muungano huo, yaani Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere na Mzee Abeid Amani Karume kupitia Serikali zao, waliwezesha
tu kufikiwa kwa matarajio ya wananchi wenyewe.
Mzee Karume alilielezea tukio hilo kwa maneno
yafuatayo kama alivyonukuliwa na Rais Benjamin
Mkapa katika hotuba yake ya tarehe 26 Aprili, 2004:-
Napenda
mfahamu wananchi wote, kazi hii si kazi ya Abeid Karume. Jambo hili, jambo la wenyewe Waafrika
wote. Mwalimu Julius Nyerere na Abeid
Karume wao ni watumishi wa wenyewe wana wa nchi, na sisi tumekubali kuwatumikia
wenyewe wananchi. Tunawatumikia wananchi
kwa utumishi wao maalum, ule walioona wao wenyewe bora. Basi jambo hili la kufanya Union, Tanganyika
na Zanzibar, ni jambo ambalo lililofikiriwa na wenyewe wananchi wa Tanganyika na Zanzibar …
Hatimaye,
mwaka 1977, watu wenyewe, kupitia vyama vyao waliithibitisha hatua ya Waasisi
ya kuunganisha Tanganyika na
Zanzibar mwaka
1964.
Hiki
ni kielelezo cha wazi cha umadhubuti wa nguzo hii ya Muungano ya kwamba
Muungano ni wa watu wenyewe, na jinsi nguzo hii inavyoupa uhalali wa kijamii na
hata wa kisiasa Muungano wetu.
Nguzo Ya Msukumo wa Kujenga Umoja wa
Afrika
Nguzo
ya pili inayouhimili Muungano ni utashi wa kujenga umoja wa Afrika. Manifesto (Ilani za Uchaguzi) za TANU na ASP
toka enzi za mapambano ya kudai uhuru zilikuwa na vipengele vya kutaka umoja wa
Afrika. Aidha, vyama vyote vilishiriki
kikamilifu katika majukwaa yote yaliyowaunganisha Waafrika wa nchi mbali mbali
katika kudai uhuru kwa lengo la kuja kuziunganisha nchi hizo baada ya
uhuru. Kwa mfano, TANU na ASP zilikuwa
wanachama wa PAFMECA na baadae PAFMECSA, vyombo ambavyo viliviweka
pamoja vyama vilivyokuwa vikidai uhuru kutoka nchi mbali mbali za eneo la
Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.
Katika hili, hata Chama cha Hizbu (ZNP) cha Zanzibar kilikuwa kikishiriki.
Katika
jitihada za kufikia ndoto hiyo ya umoja wa Afrika, nchi za Afrika Mashariki
(yaani Kenya, Uganda, Tanganyika
na Zanzibar)
zilijaribu kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki baada ya uhuru wa nchi
hizo. Baada ya kuona dalili za kukawia
kufikiwa kwa lengo hilo katika upeo wa Afrika Mashariki, Rais Nyerere wa
Jamhuri ya Tanganyika na Rais Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar walikubaliana
zianze Tanganyika na Zanzibar ili kuonyesha njia na kuendeleza shauku ya
kutafuta umoja wa Afrika. Dhamira hiyo
inajieleza katika maneno ya Mwalimu Nyerere katika hotuba yake katika Mkutano
Maalumu wa Bunge la Tanganyika,
tarehe 25 Aprili, 1964, lililoitishwa kujadili na kuridhia Hati ya
Muungano. Mwalimu anajinukuu katika
kitabu chake cha “Uhuru na Umoja” kama ifuatavyo:-
Ikiwa, basi,
nchi ambazo ni marafiki na ni jirani, na hasa zile ambazo zilipata kuwa moja
bali zikagawanywa na wakoloni wapya; ikiwa hizo zitashindwa kuungana, kushindwa
huko kunaweza kukaleta wasi wasi katika bara letu la Afrika na shauku yake ya
Umoja. Bali ikiwa nchi hizo zaweza
kuungana, muungano huo waweza ukawa ni thibitisho la vitendo kwamba matumaini
ya bara letu si ya bure. (uk.292).
Miaka
miwili baadae, wakati wa sherehe za Muungano kutimiza miaka miwili
zilizofanyika Dar es Salaam
mwaka 1966, Mzee Karume naye aliithibitisha dhamira hiyo. Kama alivyonukuliwa na Rais Benjamin Mkapa
katika hotuba yake ya kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano tarehe 26
Aprili, 2004 mjini Zanzibar,
Mzee Karume alisema yafuatayo:-
Muungano wa Tanzania
unaonyesha mithali katika Afrika.
Mithali yenyewe (ni) kuthibitisha nini viongozi wa Kiafrika kabla ya
hawajapata independence walikuwa wakisema.
Neno lililokuwa likisemwa ni hili hapa – Tanzania (Muungano). Ya kwamba kila mmoja akijitapa, “mara tu
nikipata Serikali yangu katika nchi yangu lazima nilete uhusiano na Muungano wa
Uafrika, tuzidi kuendelea kwa maendeleo yaliyo bora.” Lakini si bahati mbaya (kuwa
hawajatekeleza). Watanzania mjue kuwa si
bahati mbaya. Bahati nzuri, Muungano
ndiyo huu hapa. Watanzania tena mnataka
nini? …
Muungano wa Tanzania ndiyo
hatua ya mwanzo. Na msife moyo wananchi wa Tanzania. Wenzetu wako jirani watakuja unga.
Muungano
wa Tanzania
ni kani inayoendeleza uhai wa dhamira ya kuwaunganisha Waafrika na hivyo
umeijengea heshima kubwa nchi yetu. Uhai
wa dhamira hiyo inayopata msukumo kutokana na Muungano wetu, unajidhihirisha
katika kuingia hatua ya kuanzishwa kwa Umoja wa Afrika (African Union) wenye nguvu zaidi
kutoka hatua ya uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU). Na katika eneo letu la Afrika Mashariki,
hatua za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki zimefufuliwa kutokana na uhai
wa dhamira hiyo.
Kwa
hivyo, nguzo hii ya msukumo wa kujenga umoja wa Afrika imeupa pia Muungano wetu
uhalali wa siasa za kimataifa, hasa Barani Afrika. Watanzania wanajivunia heshima hii na
wanapenda iendelee. Heshima hiyo
itaendelea tu kwa kuudumisha Muungano na kamwe si kwa kuudhofisha au kuuvunja.
Nguzo ya Kisheria
Nguzo
ya tatu inayouhimili na kuupa uhalali Muungano wa Tanzania ni ukweli kwamba Muungano
huo umesimama juu ya msingi wa sheria za nchi na za kimataifa. Ulijadiliwa, ukatungiwa mkataba wa kimataifa
(Hati ya Muungano) ambao ulitiwa saini tarehe 22 Aprili, 1964 na Wakuu wa Nchi
(Marais Nyerere na Karume) na hatimae kuridhiwa na Mabaraza ya kutunga sheria
ya nchi zote mbili (yaani Bunge la Tanganyika
na Baraza la Mapinduzi la Zanzibar)
kwa niaba ya wananchi wao.
Kama
itavyoonekana baadae, wapo waliowahi kudhani kwamba kwa upande wa Zanzibar, hatua za
kuuhalalisha Muungano kisheria hazikutimia kwa madai eti kwamba Hati ya
Muungano haikuridhiwa na baraza la kutunga sheria kwa niaba ya wananchi. Lakini hoja yao ilinyauka pale walipozinduliwa kwamba
wasilitazame Baraza la Mapinduzi kwa sura yake ya Baraza la Mawaziri tu, bali
walione pia katika sura yake ya pili liliyokuwa nayo wakati huo ya Baraza la
Kutunga Sheria.
Nguzo ya Uendelevu
Nguzo
ya nne inayouhimili na kuupa uhalali wa kisiasa Muungano wa Tanzania na
ambayo inaendelea kuimarika kila kukicha, ni uendelevu wa Muungano
wenyewe. Hadi sasa, miaka arobaini baada
ya kuasisiwa kwake, Muungano huu unabaki kuwa mfano pekee Barani Afrika wa
muungano wa nchi zilizo huru uliodumu. Kama ilivyokwishagusiwa kabla, juhudi za kuunda
Shirikisho la Afrika Mashariki mara tu baada ya uhuru, zilivia. Ulijaribiwa pia Muungano wa Misri,
Libya na Syria (ulioitwa
Jamhuri ya Umoja wa Kiarabu) katika miaka ya sitini, lakini haukufika
mbali. Senegal
na Gambia nazo zilijaribu Senegambia katika miaka ya themanini lakini bila ya
mafanikio.
Kama
itavyofafanuliwa baadae, Muungano wa Tanzania umefaulu majaribu
mengi. Badala ya kuudhofisha, majaribu
hayo yamekuwa yakiuimarisha zaidi. Muungano ulianza na mambo 11 tu katika
orodha ya mambo ya Muungano, lakini hivi sasa yamefikia 22. Wasioutakia mema Muungano wamekuwa wakidai
kwamba eti mambo yaliyoongezwa yaliingizwa kinyemela na kwa kuiburuza Zanzibar. Lakini madai kama
hayo ambayo hayana chembe ya ukweli, mara nyingine yamekuwa yakiambatana na
unafiki. Kwa mfano, waliosimamia na
kuhakikisha Usalama wa Taifa wa Zanzibar
unawekwa chini ya Serikali ya Muungano mwaka 1984, ndio hao hao sasa
wanaoongoza kampeni ya kutaka Watanzania na hasa Wazanzibari waamini kwamba eti
mambo yanaingizwa kiholela tu na kwa kuwaburuza Wabunge wa Zanzibar kutokana na uchache wao Bungeni.
Ukweli
ni kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayalinda vya kutosha maslahi ya Zanzibar kwani inatamka wazi kwamba hakuna jambo
litaloongezwa au kupunguzwa katika orodha ya mambo ya Zanzibar
ila kwa thuluthi mbili ya kura za Wabunge wanaotoka Zanzibar na thuluthi mbili za Wabunge kutoka
Bara. Kwa hivyo, wingi wa Wabunge wa
Bara hauna nafasi ya kuwaburuza wenzao wa Zanzibar.
Itoshe
tu kusisitiza kwamba uendelevu wa Muungano ni nguzo madhubuti ya kuuhimili
Muungano huu ambayo pia inaupa uhalali wa kisiasa za ndani.
Katika sehemu hii, zimezungumziwa nguzo
nne zinazouhimili Muungano wa Tanzania
na hata kuupa sura mbali mbali za uhalali.
Ni kutokana na umadhubuti wa nguzo hizo ndiyo maana umehimili na
unaendelea kuhimili misukosuko mbali mbali kama
itavyofafanuliwa baadae. Katika hotuba
yake ya kuliaga Bunge tarehe 28 Julai, 1995, Rais Ali Hassan Mwinyi ambae
alikuwa anastaafu wakati huo alisema kwa fahari kubwa:-
Katika kipindi hiki Muungano wetu umepita katika
tanuri la moto na kutokea upande wa pili ukiwa bado imara na wenye nguvu. Matatizo yaliyojitokeza yalishughulikiwa kwa
ukamilifu na katika hali ya maelewano baina ya pande zote mbili. Tumefanya pia marekebisho katika Katiba
ambayo nina imani yatazidi kuimarisha Muungano wetu katika kipindi hiki cha
mageuzi ya kisiasa na kiuchumi.
SABABU ZA
MUUNGANO
Kwa
kadiri CCM inavyohusika, sababu kubwa na za msingi zilizowaongoza Waasisi wa
Muungano katika kuuanzisha ni hizi tatu
zifuatazo:-
1.
Kuurejesha na
kuuthitibisha umoja wa watu waliokuwa wametenganishwa.
2.
Kutekeleza azma
ya kujenga umoja wa Afrika.
3.
Kulinda Uhuru wa Tanganyika na Mapinduzi ya Zanzibar.
Sababu
mbili za kwanza zimekwishajadiliwa kwa kina hapo kabla na hivyo hapana haja ya
kuurejea mjadala huo. Kwa sababu ya
tatu, ufafanuzi unapatikana kutokana na maelezo ya Sheikh Thabit Kombo kama alivyonukuliwa na Rais Mkapa katika hotuba yake ya
maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano.
Maelezo hayo yaliyotolewa kama faida ya Muungano ni kama
yafuatavyo:-
… Matumaini ya kudumu kwa amani na usalama
yamekuwa makubwa kwa nchi zote mbili; wasiwasi mwingi wa usalama
umeondoka. Fikiri mwenyewe kusingekuwako
muungano, na maadui wa Zanzibar wakazidisha vitimbi vyao, kusingekuwako usalama
wala amani; si Bara wala si hapa Zanzibar. Lakini kwa nguvu za muungano wakorofi
wanasita kidogo …
Lakini
usingekuwako muungano tungekuwa na hasara kubwa, kwa Tanganyika
na kwa Zanzibar
pia. Zanzibar pamoja na mapinduzi yake,
ingedumu katika wasiwasi kwamba mbinu zingeweza kutumika kumrudisha
Sultani. Na Tanganyika nayo pamoja na
ukubwa wake, isingekuwa salama kabisa kama
kungekuwako vurugu visiwani hapa. Maadui
wangeweza kuitumia Zanzibar kuihujumu Tanganyika kwa urahisi sana…
Pamoja
na kwamba kauli hiyo ya hadharani ilitoka muda mrefu baada ya Mapinduzi, ipo
kila sababu ya kuamini kwamba suala la usalama wa Mapinduzi ya Zanzibar
na hata Uhuru wa Tanganyika
ni miongoni mwa mambo yaliyozingatiwa wakati wa mazungumzo ya Muungano. Na pengine ndilo lililochangia katika
kuharakisha Muungano hasa ikizingatiwa ukweli kwamba watawala waliopinduliwa Zanzibar walikuwa
wamekimbilia nje ambako wangeweza kupanga mbinu za kujaribu kurudisha utawala
wao. Hao ni maadui wa Mapindizi ambao
wasingeweza kupuuzwa. Na hofu hiyo
ilithibitishwa na majaribio 17 ya mapinduzi yaliyofanywa bila ya mafanikio na
maadui wa Mapinduzi ya 1964. Muungano
bila shaka una mchango wake katika kuyaviza majaribio hayo.
Kumekuwa
pia na hoja kwamba Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar
ulipata msukumo kutokana na vita baridi vya wakati huo kati ya Marekani na
Urusi na kambi zao. Hoja ni kwamba eti
Marekani ndiyo iliyoshawishi ufanyike Muungano kwa lengo la kuidhibiti Zanzibar eti isiwe “Cuba ya Afrika”. Wana-CCM hawaafikiani na hoja hiyo. Mtazamo wao ni kwamba kama kweli Wamarekani
walikuwa na mawazo hayo, hawakwenda zaidi ya kuomba Mungu tu tukio hilo litokee. Lakini wenyewe Watanganyika na Wazanzibari
waliungana kwa utashi wao na kwa maslahi yao. Hawakuwa na habari na ndoto za Marekani na
maslahi yake.
Katika
hili, Rais Mkapa alitoa msisitizo ufuatao katika hotuba yake ya maadhimisho ya
miaka 40 ya Muungano:-
… wapo wanaodhani Muungano wetu ulikuwa lazima
wakati ule kwa sababu tu ya vita baridi duniani, na mapambano ya mataifa
makubwa kutafuta himaya barani Afrika.
Swali linabaki. Vita baridi
vilikwisha, na harakati za wakubwa kujenga himaya Afrika nazo zimekwisha. Lakini Muungano unaendelea, kwa nini? Kwa sababu msingi wa Muungano haukuwa vita
baridi, bali shauku kubwa – iliyozuiliwa na wakoloni kwa miaka mingi – ya watu
wa Tanganyika na Zanzibar kuungana kama
walivyokuwa zamani.
KWA NINI SERIKALI MBILI?
Muundo
wa Muungano wa Tanzania ni
wa Serikali mbili; yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambayo inashughulikia
mambo ya Muungano na mambo yote ya Tanzania Bara (baada ya Serikali ya Tanganyika kufa) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoshughulikia mambo yasiyokuwa ya Muungano kwa
upande wa Zanzibar.
Muundo
huu umekuwa jambo la mjadala mkubwa na wenye kuendelea miongoni mwa
Watanzania. Wapo wanaouona muundo huu
kuwa haufai kwa kuwa ni tofauti na miungano mingine inayojulikana duniani. Wapo wanaoamini kuwa unasababisha kero nyingi
na hivyo haukidhi matarajio ya Watanzania.
Wapo wanaoamini kuwa haupendwi na Watanzania. Wapo pia waliojaribu kujenga hoja kwamba eti
Waasisi wa Muungano walipokuwa wanaunganisha nchi hizi mbili, lengo lao la
baadae lilikuwa ni muungano wa Serikali moja na kwamba huu wa Serikali mbili ulikusudiwa uwe wa muda
tu. Wapo wengine waliojaribu kujenga
hoja kwamba eti Waasisi hao walichounda ni Shirikisho la Serikali tatu ambapo
Serikali ya Tanganyika
“imefichwa” ndani ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
CCM
inatofautiana na mawazo yote hayo. Kufaa
au kutokufaa na kukubalika au kutokubalika kwa muundo huu kwa Watanzania
kutajadiliwa baadae chini ya Misukosuko Iliyohimiliwa Na Muungano.
Katika
sehemu hii, inatazamwa dhamira halisi ya Waasisi katika kufikia uamuzi wa
Muundo huu. CCM inaamini kwamba Waasisi
walikusudia muundo wa Serikali mbili na walikuwa wanakijua walichokuwa
wanafanya. Wao wenyewe ndio walioijua
zaidi dhamira yao
kuliko wale wanaojaribu kuitafsiri.
Kwa
mnasaba huo, tunaanza na kuwanukuu kauli zao kama
walivyosema wenyewe.
Katika
“Uongozi
Wetu na Hatima ya Tanzania”,
Mwalimu Nyerere anaifichua dhamira yao na sababu
za kuamua muundo wa Serikali mbili kama
ifuatavyo:-
Nchi mbili
zinapoungana na kuwa Nchi Moja mifumo ya kawaida ya miundo ya Katiba ni
miwili: Muungano wa Serikali Moja, au
Shirikisho la Serikali Tatu. Kwa mfumo
wa kwanza kila nchi itafuta Serikali yake, na Nchi mpya inayozaliwa itakuwa ni
Nchi Moja yenye Serikali Moja. Katika
mfumo wa pili kila Nchi itajivua madaraka fulani ambayo yatashikwa na Serikali
ya Shirikisho, na itakuwa Serikali ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo
yaliyobaki….
Tanganyika na
Zanzibar zilipoamua kuungana na kuwa Nchi Moja, tungeweza kufuata mmojawapo wa
mifumo hiyo ya kawaida. Lakini
tulishindwa kufanya hivyo kwa sababu ya udogo wa Zanzibar
na ukubwa wa Tanganyika. Zanzibar
ilikuwa na watu laki tatu (300,000) na Tanganyika watu milioni kumi na
mbili (12,000,000). Muungano wa Serikali
Moja ungefanya ionekane kama Tanganyika
imeimeza Zanzibar. Tulikuwa tunapigania Uhuru na Umoja wa
Afrika; hatukutaka tudhaniwe, hata kwa makosa, kwamba tunaanzisha ubeberu
mpya1 Kwa hiyo mimi nilipinga mfumo wa
Serikali Moja. Shirikisho la Serikali
Tatu lingekuwa ni gharama kubwa mno kwa Tanganyika. Zanzibar
ingeendesha Serikali yake na kuchangia gharama za kuendesha serikali ya
Shirikisho; na Tanganyika
ingefanya vivyo hivyo. Lakini ni dhahiri
kwamba mchango wa Tanganyika
ndio hasa ungeendesha Serikali yake ya watu 12,000,000 na pia ndiyo ingetoa
sehemu kubwa ya kuendesha Serikali ya Shirikisho la watu 12,300,000. Ni watu wanaofikiri kwa ndimi zao wanaodhani
kuwa gharama ya Serikali yo yote kati ya hizo ingekuwa ndogo. Gharama ya Serikali ya Tanganyika isingekuwa
ndogo, (waulizeni Wazanzibari) na wala Serikali ya Shirikisho isingekuwa ndogo,
hata bila gharama za mambo yasiyo ya Shirikisho. Na gharama zote hizo kwa kweli zingebebwa na Tanganyika.
Kwa hiyo
ilitupasa tujiulize kwa nini tunataka kuibebesha Tanganyika
gharama zote hizo; na hasa kwa nini tunataka Serikali ya Tanganyika? Hivi tuna hofu ya kwamba Tanganyika, bila
kuwa na Serikali yake, itaonekana kuwa imemezwa na Zanzibar?
Hofu yetu ni kwamba tukiwa na Serikali Moja Tanganyika
itaonekana kuwa imeimeza Zanzibar. Basi na tutafute muundo ambao utaiondolea
Zanzibar hofu hii ya kumezwa, bila kuibebesha Tanganyika mzigo wa kuendesha
Serikali mbili zenye uzito unaolingana.
Hivyo ndivyo
tulivyofanya, na hiyo ndiyo asili ya muundo wa Muungano wa Serikali Mbili. Badala ya kutungua mfumo uliopo kama
wapumbavu, tulitazama hali halisi yetu ilivyokuwa na tukabuni mfumo utakaotufaa
zaidi. (uk.15 – 16).
Mzee
Abeid Amani Karume kwa upande wake aliielezea kwa ushupavu zaidi dhamira ya
kuunda Muungano kwa kutumia neno la Kiingereza la Union ili kuziba mwanya
wa kubabaisha na shirikisho. Katika
hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano, Rais Mkapa alimnukuu Mzee
Karume kutokana na hotuba yake maarufu aliyoitoa siku za mwanzoni za Muungano
ambayo husikika sana
katika redio. Katika nukuu hiyo Mzee
Karume alitamka yafuatayo:-
Leo tumekuja
kuonana na nyinyi wananchi wote. Na
ikiwezekana kuusia mambo. Sababu baadhi
ya watu wengi, wanataka kufahamu (kuhakikishiwa kwamba) Serikali ya Unguja (kwa
maana ya Zanzibar) na Serikali ya Tanganyika
zimechanganyika, zimekuwa Union moja
tu. …
Kwa
hivyo, ni dhahiri kabisa kwamba walipoamua muundo huo wa Muungano walikuwa
wanajua walichokuwa wanakifanya na walichokuwa wanakitaka. Na wala haina maana kwamba labda walipoamua
muundo huo walidhani hautokuwa na matatizo.
Matatizo walijua yatakuwepo lakini waliamua kwa makusudi wakabiliane
nayo ndani ya Muungano badala ya kusubiri yamalizike kwanza ndio waunganishe
nchi. Ukweli huo unadhihirishwa katika
kitabu cha ASP cha “Maendeleo ya Mapinduzi ya Afro-Shirazi Party 1964 – 1974” kama
ifuatavyo:-
Nchi mbili
huru, kama zilivyokuwa Zanzibar na Tanganyika, zinapoungana, kuna njia mbili za
kuunganisha. Njia ya kwanza ni kuungana
kwa yale wanayokubaliana, hata yakiwa ni machache, madamu tu nia ipo, ni
kuitekeleza ile nia na halafu zikaendelea kutanzua matatizo yao na kujenga juu ya ile nia iliyokwisha
kutekelezwa. Njia ya pili ni kukaa na
kutanzua matatizo kwa makubaliano mpaka kifikilie kima cha makubaliano kiwezacho
kuleta muungano. Zote hizi njia mbili si
rahisi na kila moja ina matatizo yake yanayoweza kuchukua muda mrefu
kutanzuliwa. Tanganyika na Zanzibar
zilichukua njia ya kwanza, siyo kwamba ndiyo iliyokuwa rahisi, bali kwa sababu
nchi mbili hizi zilikubaliana na kutekeleza nia yao ya kuungana na kutanzua matatizo
yaliyosalia ya muungano huku zimo katika Muungano. (uk.33).
Kwa
hivyo, matatizo ambayo yamekuwa yakiukabili Muungano ambayo mengine yamefikia
kuutia katika misukosuko mikubwa hayawezi yakawa ni kioja, kwani
yalitabiriwa. Hata hivyo, kuendelea
kuimarika kwa Muungano ndani ya mazingira ya matatizo hayo, ni kielelezo cha
udhati wa nia ya kuungana na usahihi wa uamuzi wa kuteua muundo wa Serikali
mbili.
Katika
hotuba yake ya kihistoria iliyoimarisha hoja ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2004
kwenye kilele cha maadhimisho ya miaka 40 ya Muungano, Rais Mkapa alitoa
majumuisho mazuri ya suala hili kama
ifuatavyo:-
Muungano wetu
umefikisha miaka 40, na upo imara. Nguvu
yake ni Watanzania wenyewe, wengi wao – asilimia 84.8 – wakiwa hawajui uraia
mwingine isipokuwa Utanzania. Watanzania
hawa waliozaliwa mwaka 1964 na kuendelea, ambao leo wana umri wa miaka 40 au
chini zaidi, hawana uzoefu wa kuwa kitu kingine isipokuwa kuwa Watanzania.
Na hawajui mfumo
mwingine wa Muungano isipokuwa mfumo wa Serikali mbili, wenye manufaa mawili
makubwa ambayo ni sehemu ya msingi wa Muungano wetu. Kwanza, mfumo
huu unadhihirisha kuwa kweli sisi tumeungana,
serikali yetu ni muungano, si shirikisho. Na, muungano ni imara kuliko shirikisho.
Msingi wa
pili ni madaraka kamili ya Zanzibar
kwa mambo ambayo si ya muungano.
Madaraka hayo yanasaidia kuhakikisha kuwa Zanzibar inahifadhi utambulisho wake na haimezwi na
Tanzania
Bara. Wapo wanaoamini kuwa mfumo huu
hauna haiba nzuri; ati haupendezi. Kwao
napenda kusema kuwa jambo muhimu kuliko yote katika msingi wa nyumba si sura
yake, muhimu zaidi ni uimara wake. Na
mimi nakuhakikishieni, Ndugu Wananchi, kuwa mfumo wa Serikali mbili ndicho
chombo imara kilichotuvusha salama katika bahari ya miaka 40 iliyopita, na
Inshallah, ndicho kitatuvusha salama katika miaka ijayo.
MISUKOSUKO ILIYOHIMILIWA NA MUUNGANO
Kama
ilivyokwishaelezewa, Muungano umeweza na unaendelea kuhimili misukosuko
mingi. Misukosuko hiyo imekuwa ni
changamoto inayouwezesha kujidhatiti zaidi, kwani kila unapoishinda changamoto
moja, unaibuka imara zaidi. Hii ni kwa
sababu changamoto hizo huwafanya wahusika, hasa Serikali zote mbili, kutoa
ufafanuzi kusafisha upotoshaji unaotolewa au kuyafanyia kazi na kuyapatia
ufumbuzi matatizo yanayojitokeza ambayo hutumiwa kuutia misukosuko Muungano.
Awali,
misukosuko ilijikita zaidi katika kuhoji uhalali wa Muungano wenyewe. Baadae, baada ya shaka kuondolewa kuhusu
uhalali wake, misukosuko imeelekea zaidi katika kuhoji muundo wa Serikali
mbili.
Kuhoji Muungano Wenyewe
Hoja
ya kwamba Muungano haukuwa halali kwa sababu eti haukupata ridhaa ya wananchi
na haukukamilisha taratibu za kisheria zilianza kusikika hadharani Zanzibar mwanzoni mwa
miaka ya themanini. Seif Sharif Hamad na
wenzake ambao baadae walikiri kuwa walikuwa wapinzani ndani ya CCM na Serikali,
waliitumia fursa iliyotolewa kwa nia njema na CCM ya kuanzisha mjadala wa
kitaifa wa marekebisho ya Katiba kutaka kuudhofisha au hata kuuvunja
Muungano. Watu hao hao ni wale wale
ambao baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi waliunda chama chao cha CUF
katika miaka ya tisini.
Kipindi
hicho cha msukosuko wa kwanza mkubwa kuutikisa Muungano kilikuwa baina ya 1983
na 1984 na kinajulikana kwa umaarufu wa kuchafuka
kwa hali ya hewa ya kisiasa Zanzibar. Madai yaliyokuwa yameshika nguvu wakati huo
ni ya kudai kura ya maoni ya wananchi ili eti kuupa uhalali Muungano huo na
kukamilisha hatua za kisheria.
Imekwishaelezewa
kwa kina katika sehemu ya Nguzo za Muungano jinsi Muungano ulivyo na uhalali
unaotokana na watu wenyewe, na kwamba umekidhi matakwa ya sheria.
Mtazamo
wa CCM kuhusu kura za maoni ni kwamba si jambo la lazima na wala si njia pekee
ya kupima utashi wa wananchi. Hadi wakati
Tanganyika na Zanzibar zinaungana
hakukuwa na nchi duniani zilizokuwa zimeungana baada ya kuitishwa kura za
maoni. Miungano mikubwa mikubwa
iliyodumu na iliyo madhubuti kabisa kama ile
ya Marekani (USA) na Uingereza (UK) haikuanzishwa kwa kura za maoni. Na wala hadi leo haikupigiwa kura za maoni za
kuithibitisha. Kinyume chake,Marekani
iliwahi kuingia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kuulinda Muungano baada ya
majimbo ya Kusini kutaka kujitoa.
Wanaolalamikia Muungano hupenda kutaja mifano ya nje kuzipa nguvu hoja
zao, lakini mifano hii ya Marekani na Uingereza hawaitaji katika muktadha
huu. Kwa mazingira ya wakati ule na hasa
kuzingatia usalama wa Mapinduzi ya Zanzibar,
isingeweza kutumika njia nyengine zaidi ya iliyotumika. Hata hivyo, suala hili la kura ya maoni
lilikuwa agenda kuu ya uchaguzi katika Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar
wa 1990 ambapo Dr. Salmin Amour alichaguliwa kuwa Rais wa tano wa Zanzibar. Uchaguzi huo uliambatana na kampeni kubwa ya
chini kwa chini iliyowataka watu waususie hadi kwanza itapoitishwa kura ya
maoni. Inasadikiwa katika CCM kwamba
kampeni hiyo iliongozwa na kundi la wanasiasa chini ya uongozi wa Seif Sharif
Hamad waliokuwa wamefukuzwa kutoka CCM kwa sababu za usaliti. Ni watu hao hao ndio wanasadikiwa pia
kuongoza kampeni ya chini kwa chini ya kutaka Sheikh Idris Abdul-Wakil apigiwe
kura za HAPANA wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 1985.
Kampeni
zote hizo hazikufanikiwa. Kushindwa kwa
kampeni ya 1990 iliyotaka kura za maoni kuliidhoofisha kwa kiasi kikubwa hoja
ya kwamba Muungano eti Wazanzibari hawakuwa wameuridhia. Kujitokeza kwa wingi kwa wananchi kupiga kura
na kumchagua Dr. Salmin Amour ambae kampeni yake na ya CCM ilikuwa ya kupinga
kura za maoni ulikuwa ushahidi wa kutosha kwamba Wazanzibari hawakuwa na tatizo
na Muungano.
Kwa
upande wa uhalali wa kisheria, kitendawili kiliteguliwa na Tume ya Chama Kimoja
au Vyama Vingi (maarufu Tume ya Nyalali) katika miaka ya tisini. Tume hiyo
ilijiridhisha kwamba Baraza la Mapinduzi la Zanzibar
likikaa kama Baraza la