DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA
[Muhammed Seif Khatib]
1.
UTANGULIZI:
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Waheshimiwa Wajumbe;
Tume ya Taifa ya Uchaguzi ndiyo Taasisi inayotakiwa
kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura,
kwa mujibu wa ibara ya 5(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
ya mwaka 1977. Kwa muda sasa Tume imekuwa ikifanya mtayarisho kwa ajili
hiyo, ikiwa ni pamoja na kuwahusisha wadau katika hatua za awali.
Tume kwa muda mrefu sasa imekuwa ikifanya maandalizi
ya kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Maandalizi hayo ni pamoja na kuhakikisha kuwepo mfumo thabiti
utakaowezesha kwa ufanisi wa hali ya juu utekelezaji wa zoezi zima ikiwa ni
pamoja na wa kisheria upatikanaji wa fedha na kutafakari ushauri wa wataalamu (consultants).
Hapo awali, Tume ilitarajia zoezi la kuanzisha
Daftari la kudumu la Wapiga Kura lingeanza mwezi Septemba, 2003. Lakini kutokana na ukosefu wa fedha, ratiba
ilipangwa upya ili zoezi lianze Januari, 2004.
Hata hivyo, uhakika wa zoezi hilo kuanza ulipatikana baada ya kiasi cha
Tshs.14.2 bilioni, hii ikiwa ni sehemu tu ya gharama zilizoidhinishwa na bunge
kwa ajili ya uanzishaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Kwa hiyo Tume ilirekebisha ratiba yake
ambapo hatimaye utekelezaji uliweza kuanza tarehe 01 Machi, 2004.
Mheshimiwa Mwenyekiti,
Waheshimiwa wajumbe,
Kama wote mnavyofahamu, uandikishaji wa Wapiga Kura
ni hatua muhimu katika uchaguzi kwani pasipo
na wapiga kura haiwezekani kuwepo na uchaguzi. Umuhimu wa hatua hiyo ndio unaotiliwa maanani katika kuanzisha
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Katika kukuza demokrasia ya vyama vingi vya siasa
nchini mwetu na kuendeleza uwazi na
utawala bora, uchaguzi ni moja kati ya nyenzo muhimu sana. Uchaguzi unaoendeshwa kwa njia za demokrasia, unahitaji kuwepo kwa utaratibu wa wazi na mzuri wa
kuandikisha raia wote wanaostahiki kupiga kura. Orodha ya wapiga kura inapokuwa inaaminika, matatizo mengi
yanaweza kupungua sana. Kutokana na
sababu hizo, uandikishaji wapiga kura ni hatua muhimu sana katika uchaguzi.
Naomba ifahamike kuwa wakati wa kuandikisha wapiga
kura, uandikishaji huo utakuwa tofauti kabisa na mfumo wa uandikishaji
tuliouzoea hapo zamani. Aidha
teknolojia itakayotumika, itakuwa tofauti kwa hivyo ni vema viongozi wa
CCM wote kujielimisha zaidi na kupata
ufahamu wa kutosha kuhusu zoezi hilo ili na sisi tushiriki kikamilifu tukiwa
wadau wa uchaguzi na kuona jinsi ya kuboresha zaidi utekelezaji wake na kuweza
kutoa elimu ya kutosha kwa ajili ya uchaguzi.
2.
GHARAMA ZA UANZISHAJI WA DAFTARI:
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Uzoefu unaonesha kuwa kila
uchaguzi unapofanyika kwa utaratibu unaotumika mpaka sasa, gharama za uandikishaji wapiga kura ni kati ya 25 – 30 asilimia ya gharama zote za uchaguzi. Kwa mfano, kabla ya uchaguzi Mkuu wa mwaka
1995 gharama za uandikishaji wapiga kura ilikuwa
Shs. 20.027 bilioni kati ya shs. 38.5 bilioni ikiwa ni 26.0 asilimia. Mwaka 2000 gharama za uandikishaji zilikuwa shs. 10.27 bilioni kati ya Shs. 39.89 bilioni
zilizotumika kwa shughuli za uchaguzi ikiwa ni 25.7 asilimia. Gharama hizo za uandikishaji tu wa wapiga
kura huigharimu fedha nyingi serikali
hasa katika chaguzi ndogo zinazofanyika kwenye majimbo yanayokuwa wazi kwa
nafasi za ubunge na udiwani gharama ya
uandikishaji hujirejea na kuwa kubwa.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi baada ya Uchaguzi Mkuu wa Kwanza chini ya
mfumo wa vyama vingi vya siasa uliofanyika mwaka 1995, ilibaini matatizo haya
na kupendekeza serikalini kwamba kuanzishwe Daftari la Kudumu la Wapiga Kura
ambalo litakuwa na kumbukumbu za wapiga
kura na kutumika katika chaguzi zote na
hivyo kupunguza gharama. Serekali yetu
ilikubali pendekezo hili na kuliingiza katika Katiba ya nchi.
Katika zoezi la kuanzisha
Daftari la Kudumu la Wapiga kura kwa
sasa linatarajiwa kugharimu shs. 36.6
bilioni. Sehemu kubwa ya gharama
hizo ni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hasa Kamera,
filimu, fomu za OMR na vifuko vya kadi za Wapiga Kura
(Lamination pouches). Aidha gharama za
malipo ya Waandishi Wasaidizi zinahusika katika jumla ya gharama hizo.
3.
MISINGI YA SHERIA (LEGAL
FRAMEWORK):
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ibara ya 5 (3) ya Katiba
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 na Kifungu
cha 12 cha Sheria ya Uchaguzi Na. 1 ya
mwaka 1985 vilifanyiwa marekebisho mwezi Januari, 2000 kwa madhumuni ya
kuwezesha kuanzishwa Daftari la Kudumu la Wapiga kura lakini kutokana na muda kuwa mfupi na uhaba wa fedha na nyenzo
muhimu, Daftari hili halikuweza kuanzishwa kwa ajili ya kutumika katika
chaguzi za mwaka 2000.
Baada ya Tume ya Taifa ya
Uchaguzi kuchagua mfumo na teknolojia inayofaa katika kuanzisha Daftari hili
iliviangalia tena Vifungu vya Sheria ya
Uchaguzi Na. 1 ya 1985 na ile ya
Uchaguzi wa Madiwani Na. 4 ya mwaka 1979, vinavyohusu utaratibu wa
uandikishaji Wapiga Kura na kutoa mapendekezo ya Sheria. Mapendekezo hayo yana
lengo la kuwezesha Tume kutekeleza na kusimamia ipasavyo zoezi la uanzishwaji wa utumiaji wa Daftari la
Wapiga Kura, Marekebisho hayo tayari na
yameoanishwa kwenye wa sheria
uliopitishwa na Bunge tarehe 9 Juni, 2004.
Baadhi ya mapendekezo hayo
yanahusu:-
(i)
Kutoa mamlaka kwa tume ya Taifa ya Uchaguzi kuandaa na kutunza Daftari hilo
kikamilifu.
(ii)
Kuiwezesha Tume kuandikisha wapiga kura wote watakaokuwa wamefikia umri wa
miaka 18 ifikapo Oktoba, 2005.
(iii)
Kuwa na Daftari la awali
(Provisional Voters’ Register).
(iv)
Kuweka utaratibu wa kukagua Daftari la awali na kuweka pingamizi na kukata
rufaa mahakamani kwa wasioridhika.
(v)
Kuwapatia kadi yenye picha ya mpiga
kura waliojiandikisha badala ya shahada.
(vi)
Kutoa madaraka kwa Tume kusimamia na kuratibu utoaji wa Elimu ya Mpiga
Kura.
4.
FAIDA ZA KUWA NA DAFTARI
LA KUDUMU LA WAPIGA KURA:
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura litahifadhi majina yote ya watu waliojiandikisha
kuwa wapiga kura. Daftari hilo
litaandaliwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa na kuwezesha kumbukumbu za wapiga
kura kuhifadhiwa katika kompyuta
(Central Database).
Faida za
kutumia utaratibu huu ni hizo
zifuatazo:-
(i)
Utawezesha kupungua kwa gharama za Uchaguzi kama ilivyoelezwa hapo awali,
kwa kuwa hatutarudia rudia uandikishaji kama ilivyo utaratibu wa sasa.
(ii)
Utawezesha kuwepo kwa orodha sahihi ya kudumu ya Wapiga Kura kwa majimbo na
Kata zote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itakayotumika katika chaguzi
kadhaa bila mtu kulazimika kujiandikisha tena kila uchaguzi unapofanyika. Usahihi wa Orodha ya Wapiga kura utatokana
pia na kuwa na utaratibu wa kuboresha Daftari, kwa kuwaondosha wasiostahiki
kuwamo na kuingiza wanaostahiki kuwemo.
Vile vile utaratibu utawekwa wa kurekebisha taarifa za watu ambao wamebadilisha makazi yao au wanaotaka
baadhi ya taarifa zao zibadilishwe.
(iii)
Utawezesha kuondoa malalamiko ambayo yamekuwa yakijitokeza ya kudai kwamba
baadhi ya watu wanajiandikisha zaidi ya
mara moja au kuuza shahada kwa
watu ambao hawastahiki kupiga kura.
Kuwepo kwa Daftari la Kudumu kutazuia hali hiyo kutokea kwa sababu:
·
Kadi zitakazotolewa zitakuwa na picha
ya Mpiga Kura
·
Daftari (database) litakuwa na picha,
saini na alama ya dole gumba ya
Mpiga Kura.
·
Database itakuwa na programu maalumu
ya kutambua na kulinganisha alama za dole gumba ili kutambua wapiga kura wote
waliojiandikisha zaidi ya mara moja.
Aidha, Wapiga Kura watakaogundulika
kufanya hivyo kujiandikisha zaidi ya mara (moja) wataondolewa katika database na hivyo kupoteza haki ya kupiga
kura na pia wanaweza kushitakiwa mahakamani.
(iv)
Utawezesha Tume kupanga mipango na kufanya maandalizi ya Uchaguzi mapema na
kwa uhakika zaidi kwani Tume itakuwa tayari na idadi ya Wapiga Kura ambayo
ndiyo chanzo muhimu cha kuwezesha kufahamu mahitaji halisi katika utekelezaji
wa hatua mbalimbali za uchaguzi ikiwa ni pamoja na mahitaji ya vifaa na fedha
za uchaguzi.
(v)
Utampatia Mpiga kura kitambulisho ambacho kinachoweza kumsaidia katika shughuli nyingine.
(vi)
Utamwondolea mpiga kura usumbufu wa
kulazimika kujiandikisha kila uchaguzi unapofanyika.
(vii)
Utatumia utaratibu mzuri wa teknolojia ya kisasa kwa ajili ya kuandikisha
wapiga kura na utunzaji wa kumbukumbu
zinazohusika.
5.
MFUMO WA TEKNOLOJIA
ITAKAYOTUMIKA KUANDIKISHA WAPIGA KURA:
Mheshimiwa Mwenyekiti;
(i)
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura litakaloanzishwa litakuwa katika mfumo wa
kompyuta “computerized” na kumbukumbu zake zitakuwa zikirekebishwa mara kwa
mara na kutumika katika chaguzi zingine.
(ii)
Teknolojia itakayotumika kuchukua taarifa za Wapiga Kura ni Kujaza fomu
maalum za OMR (Opitical Mark Recognition).
Ni teknolojia iliyotumika wakati
wa zoezi la sensa ya watu na makazi iliyofanyika Agosti, 2002 na itatumiwa pia na Tume ya Uchaguzi ya Zanzíbar (ZEC).
6. KANDA
ZA KUANDIKISHA NA TAREHE ZAKE
Tume imeamua kuwa uandikishaji
wa Wapiga Kura utafanyika kwa Kanda kwa
siku 21 katika kila kanda badala ya
kufanyika wakati mmoja nchi nzima kwa siku 21. Uandikishaji huo unatarajiwa kuanza Septemba, 2004 katika Kanda
saba. Utaratibu mzima utakuwa kama
ifuatavyo:-
|
Na. |
Kanda |
Mikoa inayohusika |
Wakati |
|
1. |
Kanda ya Kusini |
1. Lindi 2. Mtwara |
20/09/2004 - 10/10/2004 |
|
2. |
Kanda ya Nyanda za Juu Kusini |
1. Iringa 2. Mbeya 3. Rukwa 4. Ruvuma |
28/10/2004 – 17/11/2004 |
|
3. |
Kanda ya Kati |
1. Kigoma 2. Tabora 3. Singida 4. Dodoma |
05/12/2004 – 25/12/2004 |
|
4. |
Kanda ya Ziwa |
1. Mwanza 2. Kagera 3. Mara 4. Shinyanga |
12/01/2005 – 01.02.2005 |
|
5. |
Kanda ya Kaskazini |
1. Tanga 2. Kilimanjaro 3. Manyara 4. Arusha |
19/02/2005 – 11/03/2005 |
|
6. |
Kanda ya Pwani |
1. Pwani 2. Dar es Salaam 3. Morogoro |
29/03/2005 – 18/04/2005 |
|
7. |
Kanda ya Zanzíbar |
Mikoa yote ya Zanzíbar |
Itafuata ratiba ya uandikishaji ya ZEC |
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Zoezi la uandikishaji wapiga kura kwa ajili ya
uchaguzi wa mwaka 2005 likikamilika hakutakuwepo na uandikishaji mwingine kwa
ajili hiyo. Hapa inasisitizwa kuwa mtu yeyote ambaye
hataandikishwa kwa wakati kwa kuzingatia ratiba iliyooneshwa hapo juu, hataruhusiwa kupiga kura. Sisi viongozi tuhakikishe tunahimiza wananchi kwenda kujiandikisha ndani ya
siku 21 kama zinavyoonekana katika ratiba za Kanda.
7. UTARATIBU
WA KUANDIKISHA WAPIGA KURA
Mheshimiwa Mwenyekiti;
(iii)
Kutakuwepo na vituo vya kuandikisha wapiga kura (Registration Centres).
Vituo hivi vitapangwa na vitakuwa katika majengo ya umma kama mashule na vyuo.
(iv)
Kila kituo cha kuandikisha wapiga kura, kitakuwa na Mwandishi Msaidizi
atakayehusika na uandikishaji wapiga kura.
(v)
Wanaojiandikisha kwa ajili ya kupiga kura watapigwa picha mbili bure na zitakabidhiwa kwa Waandishi Wasaidizi
katika vituo vya kuandikisha wapiga kura.
(vi)
Fomu maalum ya OMR itatumika katika
kuandikisha wapiga kura. Picha moja
itabandikwa katika fomu ya OMR na nyingine itawekwa katika kadi ya Mpiga kura. Mpiga kura aliyeandikishwa atakabidhiwa kadi
yake yenye picha hapo hapo
kituoni. Kadi itatunzwa ili itumike
katika chaguzi zitakazofuata.
(vii)
Vyama vya Siasa vyenye usajili wa kudumu vitakuwa na wawakilishi
watakaoshuhudia uandikishaji huo unafanywa kwa mujibu wa sheria na taratibu
zilizowekwa.
8. DAFTARI LA AWALI LA WAPIGA KURA
- Uandikishwaji ukikamilika, fomu
maalumu za OMR zenye taarifa za
waliojiandikisha zote zitakusanywa na
kupelekwa makao makuu ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya kuingizwa
kwenye “computer” kwa kutumia mashine maalumu zinazoaitwa
“SCANNERS” na kutengeneza Daftari la Wapiga Kura (Database). Hatua inayofuata ni orodha ya awali ya
wapiga kura (Provisional voters’ Register) itachapishwa na kupelekwa kwenye
Majimbo na Kata zote nchini.
9. UKAGUZI WA
DAFTARI LA AWALI, PINGAMIZI, RUFAA NA MAREKEBISHO
Mheshimiwa
Mwenyekiti;
Orodha ya wapiga kura itawekwa
katika ofisi ya Afisa Mwandikishaji Msaidizi kwa muda wa siku saba, katika tarehe zitakazopangwa na Tume. Lengo la zoezi hili ni kuwapatia fursa
Wapiga Kura kukagua majina ya wote
waliojiandikisha kuwa wapiga kura katika kata.
Wakati huo, mtu yeyote
aliyejiandikisha kuwa mpiga kura katika jimbo au kata, anaweza kumwekea
pingamizi mtu yeyote aliyejiandikisha kuwa mpiga kura kwa maandishi, kwa
kutumia fomu maalum zitakazotolewa na Tume yenyewe. Maafisa waandikishaji watatoa
maamuzi ya pingamizi hizo kwa mujibu wa sheria. Yeyote asiyeridhika na maamuzi hayo, anayo haki ya kukata rufaa mahakamani.
Iwapo yatahitajika marekebisho kutokana na maamuzi
yanayotokana na pingamizi, marekebisho hayo yatafikishwa Tume kwa kutumia fomu
maalum zilizoandaliwa na Tume kwa ajili ya kazi hiyo. Baada ya kuzipokea fomu hizo, Tume itazifanyia “scanning” na
kurekebisha (Daftari) Database. Baada
ya marekebisho hayo sasa Daftari litakuwa tayari. Daftari la mwisho
likichapishwa, Daftari la awali litakuwa limemaliza kazi yake na halitatumika
tena.
Orodha ya mwisho ya wapiga kura itachapishwa na kutumwa
kwa Wasimamizi wote wa uchaguzi.
10. UBORESHAJI WA DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka
2005 kukamilika, utakuwapo utaratibu utakaotumika kuboresha Daftari ambao
unaandaliwa na Tume. Uboreshaji huo
utazingatia kanuni za msingi zifuatazo:-
(i)
Kutangaza wakati na mahali pa kujiandikisha
(ii)
Kuongeza majina mapya katika daftari ya watakaokuwa wamefikia umri wa miaka 18 au kupata sifa za kuwa
wapiga kura kwa mujibu wa sheria, n.k.
(iii)
Kuondoa wale waliokufa au watakaokosa sifa kwa mujibu wa sheria.
(iv)
Kurekebisha taarifa za Wapiga Kura zilizokosewa au za wanaoomba kufanya
hivyo.
(v)
Kurekebisha kasoro zozote zitakazoonekana katika Daftari.
(vi)
Kurekebisha taarifa za wapiga kura watakaohama kutoka Kata/Jimbo kwenda
Kata/Jimbo lingine
(vii)
Kutoa nafasi kwa walioandikishwa kukagua taarifa zilizopo katika Daftari au
zinazokusudiwa kuboreshwa
(viii)
Kuwaruhusu wawakilishi wa vyama vya siasa kuangalia zoezi la uboreshaji wa
Daftari la Wapiga Kura.
Uboreshaji huu utafanyika kila
mara baada ya uchaguzi mkuu kufanyika.
11. ELIMU YA
MPIGA KURA
Utaratibu wa kuandikisha wapiga kura
katika Daftari la Kudumu la Wapiga
Kura ni mpya na wananchi
hawajauzoea. Tume inaandaa programu ya.
kuwaelimisha wapiga kura na itatekelezwa
kwa kushirikisha wadau
mbalimbali ili kuwahamasisha
wananchi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Kazi hii isiachiwe Tume peke yake;
sisi viongozi tuliopo hapa ni wadau, kwa hiyo ni lazima tushiriki
kikamilifu.
12. MWISHO
Wote tuliopo hapa leo tuliitwa
ili tushiriki katika semina hii muhimu kwetu wengi wetu tukiwa karibu sana na
wapiga Kura wanachama wa Chama cha Mapinduzi.
Ni jukumu letu kwenda kuwahamasisha kwa nguvu zetu zote wana CCM na
wapenzi wa CCM kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kuwa wapiga kura katika
tarehe zilizopangwa na Tume ya Uchaguzi ndani ya Kanda zetu.
Bila kujiandikisha yeyote
anayestahiki kupiga kura, siku ya kupiga kura itapofika hatoruhusiwa kupiga kura.
Tukiwa wadau katika uchaguzi ni lazima tushiriki kikamilifu katika
kuhamasisha wananchi kujiandikisha kuwa wapiga Kura.
Ni matumaini ya Serikali ya
Chama cha Mapinduzi kwamba sote tutachukua nafasi zetu na kutekeleza wajibu
katika kufanikisha zoezi la kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Zoezi hili likiimarika litasaidia sana
kuendesha chaguzi za kuaminika, kukubalika na za uhakika na hivyo
kuimarisha zaidi demokrasia nchini
mwetu!
13. HITIMISHO:
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kuwepo kwa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kutakuwa na faida zifuatazo:
(i)
Daftari linapunguza gharama kubwa za kifedha za uandikishaji wapiga kura
kila mara uchaguzi unapofanyika au kurudiwa.
(ii)
Daftari linaimarisha uwazi katika zoezi zima la uchaguzi.
(iii)
Daftari linaimarisha demokrasia nchini mwetu katika uchaguzi unaendeshwa
ndani ya mfumo wa vyama vingi vya siasa.
(iv)
Daftari linajenga heshima ndani na nje ya nchi yetu kwa kuendesha uchaguzi
ulio huru na wa haki.
(v)
Daftari linawaondolea usumbufu wananchi kwa kutotumia muda mwingi katika
kujiandikisha kila unapoitishwa uchaguzi na kuutumia muda huo kwa shughuli
mbalimbali za maendeleo.
(vi)
Daftari linahifadhi kumbukumbu muhimu za wananchi ambazo zinaweza kutumiwa
kwa mambo mengine muhimu kama vile kutengeneza vitambulisho vya uraia.
(vii)
Daftari litazuia wapiga kura wanaopandikizwa kutoka sehemu nyingine.
(viii)
Daftari litazuia wapiga kura wanaonunua shahada za kupiga kura.
(ix)
Daftari litazuia watu kupiga kura zaidi ya moja.