Umahiri wa CCM
na Sera ya Ajira
Katika mchakato wa uchanguzi wa
mwaka 2005, kuna ukweli usiopingika kwamba katika vyama vyote, Chama cha mapinduzi (CCM) kimeonesha
umahiri mkubwa katika kunadi ilani inayotoa majibu sahihi ya kuwawezesha watanzania
kusimamia uchumi kwa kuwa na ajira za uhakika .
Kwa kupima matamshi ya mgombea
urais wa chama hicho, ni wazi kabisa kuwa mazingira ya ajira zaidi ya milioni
moja zitakuwa wazi na zitafikiwa na kila mtanzania ambaye anao utayari wa
kufanya kazi.
Katika hilo hakuna shaka yoyote
kwani maandalizi na mazingira ya ajira hizo kwa watanzania wa jinsi zote, na wa
rika mbalimbali yameshawekwa tayari, kinachotakiwa ni watanzania kukiweka chama
hicho madarakani ili kiweze kutimiza ahadi zake, na hasa kutekeleza yale
yaliyoko katika ilani ya uchaguzi ya
chama hicho.Yote yatawezekana pale watanzania wote watakapoamua kutoa
kura zao za ndiyo kwa wagombea wa kiti cha uraisi wa Jamhuri ya muungano, urais wa
Zanzibar, wabunge , wawakilishi na madiwani.
Kwa wale ambao hawakumbuki ama
hawajawahi kusikia, Serikali ya Tanu na ASP tangu uhuru na baadaye CCM, zilikuwa na sera ya
kuhakikisha kuwa kila Mtanzania anatakiwa kuwa na maisha bora.Huu ni ukweli
usiopingika. Kama mtakumbuka fika kwamba , baada ya upembuzi yakinifu uliofanywa
na waasisi wa vyama vya TANU na ASP,hasa baada ya nchi yetu kupata uhuru, Katika mwaka 1967 Serikali ilichukua hatua ya
makusudi yenye lengo la kuondoa tofauti
katika umilikaji wa njia kuu za
uchumi na kudhamiria kuondoa matabaka ya
watu ili kuhakikisha kuwa njia kuu za uchumi zina bakia mikononi mwa
wazalendo na msimamizi mkuu ikiwa ni
serikali.
Hatua hii ya kijasiri na ya
kihistoria ya kutoa ajira kwa wazalendo inakumbukwa na wengi hasa pale serikali
ilipoamua kutaifisha mabenki, mashamba, viwanda, na taasisi mbalimbali zitoazo
huduma na pia kuunda mashirika na makampuni mbali mbali ili kuwamilikisha
wananchi uchumi wao na kutoa ajira ya uhakika kupitia sera yake Siasa ya Ujamaa
na Kujitegemea.
Bado watanzania walio wengi
wanazo kumbukumbu vichwani mwao kuhusu mwitikio wa hatua hiyo.Kila kitu
kiliwezekana,ukilinganisha na uchanga wa nchi hii na mapungufu yaliyokuwa
yameachwa na watawala wa kikoloni. Lakini kuwezekana huko kulichangiwa zaidi na
uimara wa uongozi makini wa waliokuwa
madarakani kwa kuungwa mkono na watanzania wazalendo wa nchi hii. Ngonjera
mashairi na sanaa nyinginezo zilizochangia kueleza malengo makuu na madhumuni
ya Azimio la Arusha kwa kupitia vyombo vya upashanaji wa habari kama vile redio
na magazeti katika miaka hiyo ya 1967 na kuendelea na hata wale waliokuwa
mashuleni mtakumbuka nyimbo zilizoimbwa katika mchakamchaka, sherehe mbalimbali
za kitaifa na hata katika mikusanyiko mingineyo.
Lengo la serikali katika kipindi
hicho ilikuwa ni kuufanya uchumi wa Tanzania umilikiwe na watanzania kupitia
dola na kuhakikisha kuwa ajira ya kwa wazalendo waliokuwa na sifa na elimu ya
kuweza kushika madaraka na vyeo vilivyokuwa vimeachwa wazi na wakoloni , na
serikali iliwawezesha kufanya hivyo, wakati huo huo kundi lingine la wazalenzo wakiendelea kuchapa
kazi ya uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara .
Lakini katika miaka ya mwishoni
na mwa mwaka themanini na mwanzoni mwa tisini kutokana na mabadiliko ya uchumi duniani
sera ya ujamaa na kujitegemea haijabadilika ila badala ya uzalishaji mali,
usafirisha wa bidhaa nk. kuendeshwa na dola, kwa sasa uzalishaji mali, na
huduma mbalimbali za umma zinamilikiwa na wananchi kupitia ushirika, makampuni(
kwa mtindo wa kumiliki hisa) ,na vikundi mbalimbali vya wananchi vya uzalishaji
mali na utoaji huduma.Lengo ni kuwa uchumi umilikiwe na wananchi na serikali
kukusanya kodi kuelekeza nguvu zake Katika huduma za kijamii.
Katika mikakati mbalimbali ya CCM
ni kuona kwamba wananchi wa Tanzania wanamiliki na kuendesha uchumi wa nchi yao.
Sera ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi imebuniwa kama njia ya uhakika ya
kuwapa Watanzania uwezo na fursa ya kulifikia lengo hilo la kumiliki na
kuendesha uchumi wa nchi. Aidha, Sera hii ina lengo la kuona kwamba Watanzania
kwa mamilioni wanashiriki kwa ukamilifu katika harakati za kukuza uchumi wetu
na kuondoa umaskini Kupitia Mkakati wa Kuinua Uchumi na Kuondoa Umasikini (MKUKUTA).
Wakati huo huo, utekelezaji wa dhati wa sera hii ya uwezeshaji wa wananchi
kiuchumi itatuepusha na balaa la kuwa na jamii ambayo ina matajiri wachache
walionacho na wananchi walio wengi wasio nacho.
Ili utekelezaji wa Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi
Kiuchumi ifanikiwe, CCM inaamini na inawashirikisha wananchi katika mambo makuu
yanayolenga kuleta mafanikio ya Tanzania
kwa ajili ya watanzania wote wa mijini na vijijini.Kwa njia ya ushirikishwaji
huu Chama Cha Mapinduzi katika mwelekeo huu kinatoa wito kwa Watanzania
kudhamiria yafuatayo:
Kwanza
kukubali kuwa kujitegemea kwa kufanya kazi kwa bidii na maarifa ndio msingi wa maendeleo
na kutokomeza umaskini. Kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi ana wajibu wa
kujiwezesha kwa kuishi kwa jasho lake, yaani kwa kufanya kazi. Mtaji wa maskini
ni nguvu (na akili) zake mwenyewe. Uwezeshaji kutoka katika vyanzo vingine vya
misaada ni njia ya kumuunga mkono yule aliyekwishaonesha azma ya kuanza
kujikomboa mwenyewe..
Watanzania walio wengi wanayonafasi ya kuendeleza vipaji vyao au kuwa na mali au
nyenzo za kuzitumia katika kujiendeleza kimaisha. Katika miaka mitano ya Ilani
hii CCM itazielekeza Serikali kuweka mipango ya kuwawezesha wananchi kushiriki
katika shughuli mbalimbali za kiuchumi ili kujiendeleza kimaisha..
CCM inapata faraja kuu kwa kuona kwamba tayari wananchi
wamekwishaanza kuchukua hatua za maksudi katika kujikwamua na suala hili la
kila mwenye uwezo wa kubuni kazi na kufanya kazi anafanya hivyo bila hofu
yoyote .serikali ya CCM inahakikisha kuwa amani inapatikana kwa mwenye
kudhanilia kufanya kazi afanye kazi. Mifano ni mingi lakini kwa uchache kila
mtu anashuhudia namna vijana wanavyotumia vipaji vyao katika kujiajiri kwa njia
ya vikundi mbalimbali vya uzalishaji mali katika kilimo, mawasiliano ya simu,
biashara ndogo ndogo na hata katika nyanja ya burudani mbalimbali.
Inaeleweka pia kuwa watu wetu wengi wanao uwezo wa kujitegemea
na kujiendeleza kiuchumi japo kuwa wana elimu ndogo au maarifa na ujuzi mdogo.Serikali
chini ya Chama Cha Mapinduzi inaendelea kutoa Elimu ya kawaida na mafunzo ya
ufundi stadi na maarifa ya kazi ni uwezeshaji wa msingi sana kwa binadamu.
Serikali zitaimarisha mipango ya elimu ya watu wazima yenye manufaa pamoja na
mafunzo ya fani mbalimbali za stadi za kazi mijini na vijijini. Mafunzo haya
yatahusu kilimo, biashara, ufugaji, utunzaji wa vitabu, n.k. Serikali
zitaongoza shughuli hizi za kutoa elimu na maarifa ya kazi kwa wananchi
zikishirikiana na mashirika yasiyo ya kiserikali.
CCM inaamini kuwa Ushirika ndio
njia kuu ya uwezeshaji kwa wananchi walio wengi. Ushirika ni njia ya kukusanya
nguvu. Ushirika uko wa aina nyingi. Lakini ushirika wa kuweka na kukopa una
umuhimu wa kimkakati katika harakati za kukuza uchumi na kutokomeza umaskini
kwa sababu unawawezesha wanachama wa ushirika huo kuwa na chombo chao cha
kuwapatia mikopo (mitaji) kwa uhakika na kwa masharti nafuu. Aina nyingine za
ushirika ni pamoja na ushirika wa wakulima wa mazao na mifugo, ushirika wa
biashara, ushirika wa huduma kama migahawa, ushirika wa wavuvi, ushirika wa
wachimba madini, ushirika wa ujenzi, n.k. Kwa vile ushirika ndiyo njia kuu ya
uwezeshaji wa wananchi, CCM itazisisitizia Serikali juu ya umuhimu wa kuandaa
maafisa wa ushirika waadilifu, wataalamu na wenye uzalendo.
Ili kuwakomboa watanzania, Serikali ya CCM
inaendelea na utaratibu wa kuzipa uhai
wa kisheria ardhi na nyumba ambazo hadi sasa hazikutambuliwa kisheria. Kwa
utaratibu huu wenye ardhi na nyumba hizi wanaweza kupata mikopo kwa kuweka
ardhi na nyumba hizo dhamana.Utaratibu huu unaitwa MKURABITA, yaani Mkakati wa
Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania. Lengo lake ni kuwafanya wananchi
waliokuwa hawakopesheki sasa wakopesheke na hivyo kuingia katika mchakato wa
uchumi hai.
Wananchi wengi wana uwezo, maarifa na dhamira ya
kujitegemea kiuchumi. Mipango mizuri ya mikopo ya masharti nafuu inaweza
kuwafanya wengi wao wakajiajiri na hivyo kuboresha maisha yao na kutoa mchango
katika uchumi wa taifa. Shughuli za kilimo, ufugaji, uvuvi, uchimbaji madini,
biashara, n.k. zinaweza kushamiri iwapo utakuwapo utaratibu madhubuti wa mikopo
yenye masharti nafuu. Upatikanaji wa mitaji kwa njia ya mikopo ni kikwazo
kikubwa kwa watu wengi. Serikali za CCM ziwajibike katika kuweka mfumo muafaka wa
mikopo kwa wananchi.
Kuna fani za shughuli za kiuchumi ambazo Watanzania
hatuna uzoefu nazo. Fani mojawapo ni ya ujasiriamali. CCM itazishauri Serikali
kuwa na mipango ya kuwapa fursa wajasiriamali Watanzania wanaoinukia kupata
uzoefu wa wajasiriamali wa nchi nyingine za Kusini. Aidha, katika madarasa ya
ujasiriamali na biashara, mifano halisi ya mafanikio katika nchi nyingine
itatolewa kama mifano Kuwapa elimu ya ufugaji wa kisasa na kuwatanabahisha kuwa
mifugo ni mali; waitumie ili kuboresha hali ya maisha yao.
CCM inaendelea kuwa karibu na wananchi wote katika
kusikiliza na kupokea kilio cha ajira cha
wananchi, hasa vijana. CCM imelipa na itaendelea kutoa kipaumbele suala la ajira kwa kuzingatia umuhimu mkubwa wa wananchi na hasa vijana kuwa
na uhakika wa kupata ajira na kufanya kazi katika kipindi cha miaka mingi ambayo CCM
itakuwa madarakani kwa maana ya mwaka2005-2010.
Lengo la CCM ni kuhakikisha kwamba ajira mpya zaidi ya milioni moja
zinapatikana katika miaka mitano ijayo. Ajira ziko za aina mbili: Ajira katika
maana ya kazi ya kulipwa mshahara katika sekta ya umma (Serikali na vyombo
vyake) na katika sekta binafsi (iliyo rasmi na isiyo rasmi). Ajira katika maana
ya kujiajiri binafsi katika kilimo,
ufugaji, uvuvi, viwanda, biashara, kuchimba madini, udereva, ufundi, ualimu,
uhasibu, kuendesha mgahawa, ushonaji, uandishi, uanasheria, uhandisi,
ukandarasi n.k.
Nafasi za mpya ajira katika sekta ya umma zitakuwa
nyingi kwenye sekta ya ualimu kutokana na upanuzi wa shule za msingi, sekondari
na vyuo vikuu unaoendelea. Sekta ya afya pia itatoa ajira mpya nyingi kwa
upande wa waganga na wauguzi kwa vile sekta hii lazima ipanuke kukidhi mahitaji
ya wananchi. Sekta ya ujenzi vile vile ina nafasi ya kutoa ajira mpya nyingi.
Serikali za CCM
itaendela kuhimiza na kuvutia wawekezaji katika viwanda, migodi, kilimo,
n.k. ili nafasi za ajira ziendelee kuongezeka. Mkakati mpya wa Serikali wa
kuanzisha maeneo maalum ya uchumi (SEZs) umekusudiwa kuibua nafasi nyingi mpya
za ajira. Eneo la kujiajiri ndilo lenye nafasi tele za ajira katika nchi yetu.
Katika kipindi cha Ilani hii, CCM itazihimiza Serikali zielekeze nguvu zake
kwenye kuwawezesha wananchi, hasa vijana na wanawake, kwenye shughuli za
kujiajiri vijijini na mijini. CCM inatoa wito kwa wananchi wajitokeze kuitikia
wito wa kujiajiri na pia wakubali kutobagua kazi maana wahenga wamesema mchagua
jembe si mkulima.
CCM itaendeleza jitihada zakena Serikali
kuona kwamba mipango ya uwezeshaji wananchi kiuchumi inaandaliwa kwenye kila
Wilaya. Kila Wilaya ina rasilimali za kutosha, mradi tu watu wanaamua kuibua
maendeleo yao. Mchango wa fedha (kwa ajili ya mikopo) kutoka Serikali Kuu na wa
taasisi zisizo za Kiserikali inakusudiwa upelekwe Wilayani huko huko.Serikali zitatakiwa
kuzielekeza Ofisi za Halmashauri za Manispaa, Miji na Wilaya na Ofisi za CCM za
Wilaya (Idara ya Uchumi na Fedha) zijijengee uwezo wa kuwashauri wananchi
wanaoomba mikopo kuhusu maandalizi ya michanganuo ya miradi inayokubalika.
CCM inaamini kuwa pamoja na suala la kukaribisha
wawekezaji nchini ili kukuza uchumi na kuongeza ajira, itautumia uwezo mkubwa
wa fedha uliopo katika mashirika ya hifadhi za jamii (pensheni) yaani NSSF,
PPF, LAPF na Mfuko wa Pensheni ya Serikali. Tayari NSSF na PPF wameweza
kuwekeza katika miradi ya nyumba (k.m. NSSF wamejenga mabweni ya wanafunzi wa
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mabibo) na kusaidia kutatua matatizo makubwa ya
kijamii.
CCM kwa kushirikiana na wawekezaji inahakikisha
kwamba Serikali inafanya mashauriano ya msingi na uongozi wa mifuko hii ili
kupata njia muafaka za kuifanya mifuko hii ishiriki katika uwekezaji na hivyo
kuliongezea nguvu taifa ya kukuza uchumi wake kwa kasi zaidi. Utaratibu wa
kuitumia mifuko ya hifadhi ya jamii kuchangia katika ukuzaji wa uchumi wa nchi
unatumika sana katika nchi za Magharibi ikiwemo Uingereza. Kwa maelezo haya
mafupi, tumewapa mwanga juu ya dhamira
ya CCM kuweka mazingiza bora ya ajira -Tanzania.
Abiyani Nguvu Ya Hoja
Chuo Kikuu Cha Dar Es Salaam