ASASI ZISIZO ZA KISERIKALI- ZIWE WADAU NA SIYO KIKWAZO
KATIKA MAENDELEO
Nadharia ya asasi zisizo za kiserikali inazidi
kupata msukumo na
mtizamo mpya kwa siku za hivi karibuni katika ngazi ya dunia na nchi moja moja.
Mtizamo na msukumo juu ya asasi zisizo za kiserikali
unakwenda sambamba na ongezeko la kasi la idadi ya asasi zenyewe.
Kumekuwepo na sababu mbalimbali ambazo kwa namna
moja au nyingine zimechangia wimbi la ongezeko la asasi hizi na chache kati ya
sababu hizo ni hizi zifuatazo:- Kwanza ni mabadiliko
ya kinadharia na sera katika siasa na uchumi duniani mwanzoni mwa miaka ya
sabini kutoka sera zilizotilia mkazo nguvu ya dola katika uchumi na maendeleo
na badala yake sera zinazotoa nafasi kubwa kwa sekta binafsi ziliibuka. Sababu
ya pili iliyochangia ongezeko la kasi la asasi zisizo za kiserikali ni wimbi la demokrasia ya vyama vingi mwanzoni mwa miaka ya
1990.
Hapa Tanzania asasi zisizo na kiserikali pamoja na vyama vya kiraia idadi yake inazidi
kuongezeka. Kwa mujibu wa ripoti ya tume ya Afrika
iliyoundwa na Waziri Mkuu wa Uingereza Bwana Tony
Blair ambayo Rais Benjamini Mkapa alikuwa mmoja wa Makamishna
wake Tanzania inakadiriwa kuwa na vyama
vya kiraia zaidi ya 9000 mpaka kufikia mwaka 1999, ukilinganisha ni 168 tu
mwanzoni mwa miaka ya 1990. Ongezeko la idadi ya asasi hizi ni
tafsiri iliyo wazi ya utashi wa kisiasa uliopo kwa asasi hizi kutoka katika
serikali zote mbili za Chama cha Mapinduzi (CCM).
Kimsingi asasi zisizo za kiserikali umuhimu wake
unakubalika kwa watu wengi wa kada mbalimbali. Hata hivyo yapo maswali kadhaa tunayopaswa kujiuliza juu ya asasi
hizi. Kwa mfano, asasi hizi zinawajibika kwa
nani na kwa wakati gani? Ni masilahi ya nani yanapewa kipaombele na asasi hizi katika utekelezaji wa majukumu yake kati ya
wafadhiri na wananchi? Je kuwepo kwa asasi zisizo za
kiserikali na vyama vingine vya kiraia ni jawabu kamili la matatizo yetu kama jamii? Maswali haya na mengine yatasaidia katika kuibua hoja zitakazoboresha
utendaji kazi kati dola na vyama vya kiraia.
Kinadharia ni wajibu wa asasi zisizo za kiserikali
na vyama vya kiraia kuikumbusha serikali juu ya wajibu wake kwa
wananchi. Katika
kufanya hivyo asasi hizo zinapaswa kuzingatia kanuni, sheria na
tararibu za nchi zilizowekwa kwa mujibu wa katiba na si kinyume chake. Ikumbukwe
kwamba katika utawala
wa kisheria hakuna mtu au kikundi cha watu au taasisi iliyo juu ya sheria.
Katika maisha ya wanajamii waliostaarabika haki na
wajibu huenda kwa pamoja. Kwa
maneno mengine, asasi zisizo za kiserikali zinapaswa kwanza
kutafsiri kwa vitendo yale wanayohubiri ndani ya asasi zenyewe kabla ya kuinyooshea kidole dola.
Hivi karibuni baadhi ya asasi zisizo za kiserkali
zimeonekana waziwazi kutoposha kwa makusudi na kubeza
mafanikio ya serikali ya Chama Cha Mapinduzi katika kuwaletea maendeleo
wananchi wake hasa katika kipindi cha miaka kumi ya uongozi wa Rais Benjamin William Mkapa. Inaeleweka wazi kwamba
idadi ya wanafunzi wa shule za msingi imeongezeka kutoka milioni tatu na nusu
mwaka 1995 na kufikia zaidi ya milioni saba na nusu mwaka 2005, ukuaji wa
uchumi umeongezeka kufikia asilimia 6.7 kutoka asilimia 3.6 mwaka 1995, mfumuko
wa bei umeshuka kutoka asilimia 27 mwaka 1995 hadi asilimia 4.5 mwaka 2005, makusanyo na
mapato ya serikali yameongezeka kutoka bilioni 25 kwa mwezi mwaka 1995 hadi
kufikia zaidi ya bilioni 150 mwaka huu.
Rekodi hizi za mafanikiao ya utekelezaji wa sera makini za Chama Cha Mapinduzi si tu zinapaswa kupongezwa
na wananchi ambao bado wana imani kubwa na serikali yao lakini pia na asasi zisizo
za kiserikali ambao pia na wadau muhimu katika maendeleo endelevu ya nchi yetu.
Hatusemi kwamba serikali za Chama Cha Mapinduzi zimetekeleza yote kwa asilimia mia moja, la hasha. Bali tunachosisistiza ni kwamba rekodi hii ya utekelezaji wa sera za Chama Cha Mapinduzi kwa vitendo chini ya
uongozi shupavu wa Rais Mkapa hauwezi kubezwa na mtu
yeyote wala asasi yoyote ile.
Katika mtizamo ule ule unaolenga kuboresha maisha ya
watanzania, serikali makini ya Chama Cha Mapinduzi imebuni mikakati mbalimbali
katika kuhakikisha kwamba yale ambayo hayakutekelezwa na
serikali ya awamu ya tatu yanatekelezwa na serikali ya awamu ya nne kwa ari
mpya, nguvu mpya na kasi mpya. Mpango wa
kukuza uchumi na kupunguza umaskini Tanzania (MKUKUTA), Mkakati wa Kurasimisha
Rasilimali na Biashara Tanzania (MKURABITA) na Mpango wa Kuondoa Umaskini
Zanzibar (MKUZA) ni ishara ya wazi ya utashi wa kisiasa uliomo ndani ya Chama
Cha Mapinduzi katika kuinua maisha ya watanzania. Katika hili pia tunasema
asasi zisizo za kiserikali na vyama vingine vya kiraia
vinapaswa kuliona na kuiunga mkono serikali katika juhudi zake na si kubeza na
kupotosha juhudi hizo kama ilivyojitokeza kwa baadhi
ya asasi hizo hivi karibuni.
Upotoshaji wa makusudi wa
mafanikio ya serikali ya Chama Cha mapinduzi unapofanywa na
mtu au kikundi cha watu au taasisi yoyote ile unaacha maswali mengi bila
majibu. Lakini swali kubwa zaidi linaloibuka ni je
upotoshaji huu unafanya kwa faida ya nani? Jibu sahihi la
swali hili wanalo wapotoshaji wenyewe. Tunahisi kwamba upotoshaji huu
unalenga kuikatisha tamaa serikali lakini pia kuigombanisha serikali na watu wake jambo ambalo tunaamini kwamba halitawezekana
kwa sababu watanzania bado wana imani na Chama Cha Mapinduzi na serikali zake shupavu.
Tunapenda kuzikumbusha asasi zisizo za kiserikali
pamoja na vyama vyote vya kiraia kwamba hazikuanzishwa
ili ziwe pinzani kwa serikali au ziwe za mbadala wa dola kwa wananchi. Kwa
mantiki hii asasi hizi zinapaswa kuonyesha wajibu wao kwa
umma wa watanzania kwa kudumisha mshikamano miongoni mwao na hivyo kuwaunganisha
wananchi na kuwaleta karibu zaidi na serikali yao. Hili likifanyika kwa moyo wa dhati kabisa ni wazi kwmaba asasi zisio za
kiserikali zitakuwa ni mhimili mkubwa wa maendeleo ya nchi yetu.
Kinadharia asasi zisizo za kiserikali zinapaswa
kuendeshwa kwa uwazi na ukweli hii ikiwa ni pamoja na
kuweka wazi mapato na matumizi ya pesa wanazopata toka kwa wafadhili wawe wa
ndani au wa nje. Lakini pia mikataba ambayo asasi hizi inaingia na washirika wao mbalimbali inapaswa kuwa wazi ili wananchi
wajue ukweli na undani wa mikataba hii. Kama tulivyokwisha kusema hapo awali, Tanzania inakadiriwa kuwa na zaidi
ya vyama vya kiraia na asasi zisizo za kiserikali zipatazo 9000. Tunaamini
kwamba kwa idadi kubwa kama hii ya asasi zikiachwa
kuendesha mambo yake bila utaratibu itakuwa ni hatari kubwa kwa usalama wa nchi
yetu. Ni katika msinig huu tunazidi kusisitiza kwamba asasi hizi ni lazima ziwe ni mfano bora kwa kuheshimu taratibu, kanuni
na sheria za nchi ili dhana ya utawala wa kisheria iweze kutamalaki.
Hivi karibuni hapa nchini kumekua na
mazoea kwa baadhi ya asasi zisizo za kiserikali kujikita katika kutoa sura
mbaya tu ya utekelezaji wa sera za Chama Cha Mapinduzi kana kwamba hakuna mazuri
yaliyofanywa na serikali. Hili limefanyika kwa nguvu zote ikiwa ni pamoja na kubuni
matangazo mbalimbali yanayoonekana katika vyombo mbalimbali vya habari. Sekta
ya elimu kwa mfano imekuwa ni mhanga mkubwa katika
kubeza mafanikio yake. Hatuna uhakika na nia ya dhati
ya asasi kama hizi lakini jambo moja ni dhahiri kuwa kwa kufanya
hivyo wanavutia ufadhiri hasa kutoka nje.
Katika jamii ya watu waliostaarabika kuwa tayari
kukosolewa ni jambo la kawaida. Lakini kukosoa tu bila
kutoa njia mbadala nako hakuna maana sana. Tunahisi kwamba ni wajibu wa mkosoaji kueleza
bayana nini kifanyike ili kuboresha kile ambacho anaona ni tatizo. Kwa
kushindwa kueleza njia mbadala, tafsiri yake ni kwamba
weww ni sehemu ya huo uozo unaodai kuona. Kwa mfano kama unazungumzia kushuka kwa
ubora wa elimu au mfumo mbovu wa utoaji elimu bila kugusia juu ya nini
kifanyike kuboresha elimu yetu maana yake ni kwamba mfumo huo mbovu wa elimu
wewe ni tunda lake ndiyo maana umeshidwa kujenga
hoja ya kuboresha kero hiyo.
Lakini
sisi tunaamini elimu yetu kwa mfano haijashuka na wala
si mbovu kama jinsi ambavyo baadhi ya watu wanataka tuamini.
Katika hili mifano iko mingi tu. Hivi sasa kuna
wataalamu wengi sana kutoka Tanzania wanaofanya kazi ndani ya
nchi na nje ya nchi hasa katika nchi za kusini mwa Afrika. Sisi tunajiuiza na tunapenda kuwauliza wakosoaji kwamba hivi kama elimu yetu ingekuwa duni
wataalamu hawa ambao tunaamini ni kielelezo cha ubora wa elimu yetu tungewapata
wapi?
Tunapenda kuhitimisha kwa kutoa wito kwa asasi
zisizo za kiserikali kushirikiana zaidi na serikali yetu katika harakati
za kuwaletea watanzania maisha bora badala ya kuonekana kikwazo kwa maendeleo
ya nchi. Na hili linawezekana ili mradi kila upande
utimize wajibu wake.
Nguvu ya Hoja,
Abiyani Chuo Kikuu.