CCM BADO NI CHAMA BORA NA KINASTAHILI KUPEWA RIDHAA YA KUONGOZA TANZANIA KATIKA AWAMU HII YA NNE

 

Yapata miaka minne sasa tangu Mheshimiwa Rais Benjamin Mkapa alipotanngaza rasmi mpango wa elimu kwa wote, yaani elimu ya bure kwa watoto wa shule za msingi. Kufutwa kwa ada iliyokuwa ikitozwa kwa kila mwanafunzi ili kupata elimu ya msingi kumechochea ongezeko kubwa la idadi ya watoto walioandikishwa kuanza elimu ya msingi na hivyo kuleta matumaini makubwa kwa taifa hasa tunapozingatia ukweli kuwa watoto ni akiba na nguvu kazi ya taifa la kesho.

 

Elimu kwa wote ni sera ama mpango wa dunia nzima kufuatia makubaliano ya Jomtien huko nchini Thailand ya mwaka 1990 yaliyopitiwa na kuwekewa malengo katika mkutano wa wakuu wa nchi za Umoja wa Mataifa Septemba 2000, na kuwekwa kama lengo mojawapo na mahsusi katika malengo ya milenia.

 

Lengo la sera ama mpango huo wa elimu kwa wote ni kuwezesha hasa wale watoto wanaotoka katiaka familia zenye hali duni ya kimaisha/kiuchumi, yatima watokanao na UKIMWI watoto wa mitaani na wengine wanaoishi katika mazingira magumu kupata elimu ya msingi, ikiwa na lengo la kuwawezwesha kushiriki katika kujenga maisha yao ya baadaye na pia kujenga uchumi wa taifa letu. Hatua ya kutoa elimu ya msingi kwa wote ni hatua ya utambuzi kuwa watoto ni hazina kubwa kwa taifa linalonuiya kujenga uchumi endelevu.

 

Matarajio ya mpango huo wa elimu kwa wote ni kumwezesha kila mtoto Mtanzania kupata elimu ya msingi bila kubaguana, yaani katika hali fulani ya usawa. Japo zipo shule za msingi zenye viwango mbalimbali vya ubora, tukizingatia huduma za ziada ambazo hutolewa katika shule hizo – hasa zile za watu binafsi – bado kila mtoto wa kitanzania anaweza kupatiwa elimu nzuri na ya kuridhisha katika shule za serikali ambazo idadi yake sasa imeongezeka na zile zilizokuwepo zimepanuliwa katika mpango wa MMEM. Ikumbukwe kuwa haya yote ni kwa maendeleo endelevu ya nchi masikini duniani zikiwemo zile za Afrika: Kusini mwa Jangwa la Sahara.

 

Tanzania ni moja kati ya nchi chache sana masikini duniani, zilizofanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kutekeleza mpango wa dunia nzima wa Elimu Kwa Wote. Hapa tunaweza kutaja mipango ya MMEM na MEMKWA kama sehemu tu ya mafanikio hayo. Chini ya mpango kabambe wa MMEM, idadi ya madarasa yanayotumiwa na watoto katika shule za msing imeongezeka, kila shule ikipatiwa walao darasa moja. Pia zipo shule nyingine nyingi zilizojengwa ama zinazojengwa katika harakati nyingine za kuhakikisha kuwa kila kijiji kinakuwa na walao shule moja ya msingi na hata zaidi.

 

Takwimu zinaonyesha kuwa kufuatia mabadiliko hayo yaliyotokea ama yanayotokea katika sekta ya elimu, idadi ya watoto walioandikishwa katika shule za msingi iliongezeka kutoka watoto millioni 4.4 mwaka 2000 hadi kufikia millioni 7.5 mwaka 2004 ikiwa ni zaidi ya asilimia 94 ya watoto wote Tanzania waliofikia umri wa kuanza shule ya msingi. Sambamba na hilo idadi ya walimu wa shule za msingi imeongezeka na kusababisha tofauiti katika uwiano wa mwalimu kwa wanafunzi. Pia vyuo vya walimu vimeongezeka na mipango maalum ya kufundisha walimu imekuwepo.

 

Kufuatia mafanikio makubwa yanayoonekana dhahiri kutokana na mipango ya MMEM na MEMKWA, wananchi wamehamasika na wamekuwa na mwamko chanya wa elimu. Hilo linathibitika katika juhudi mbalimbali za wananchi, katika sehemu mbalimbali hapa nchini, kuamua kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tatu chini ya utawala wa Chama Cha Mapinduzi, kwa kuweka mipango ya kujenga shule za Sekondari za Kata. Ama kweli aliye na macho haambiwi tazama. Shule za Sekondari (za kata) zinamea kote nchini kwa juhudi za wananchi. HEKO CCM kwa kujenga mazingira mazuri ya kuwawezesha wananchi kutambua na kuchukua jukumu lao la kuendeleaza elimu hapa nchini.

 

Ikumbukwe kuwa elimu bora ni silaha mbadala ya kupambana siyo tu na umasikini uliokithiri kwenye nchi zilizoko kusini mwa Jangwa la Sahara, Tanzania ikiwa mojawapo, bali ni ngao mahsusi ya kuliwezesha taifa lolote (mataifa masikini na hata mataifa tajiri) kupambana na wimbi la utandawazi. Ndani ya utandawazi sera ni ushindani, na hilo linawezekana pale ambapo taifa husika limejiandaa vilivyo, likiwa na wasomi wa kutosha katika fani mbalimbali, zikiwemo zile za sayansi na teknolojia, biashara, sanaa, sheria na nyinginezo.

 

Inafaa tukumbuke kuwa haya yote hayatawezekana pasipokuwa na msingi imara katika sekta ya elimu na katika serikali kwa ujumla. Tunapokaribia uchaguzi mkuu ni vizuri tukajiuliza maswali machache yanayohusiana na maendeleo ya taifa letu. Je sisi tupo wapi tukijilinganisha na wenzetu katika nchi zilizoendelea? Tunaelekea wapi? Tutafika? Kama tutafika,tuzingatie mambo gani? Nani anaweza kutufikisha lengo hilo, yaani kule ambako matarajio yetu yameelekea?

 

Hivi sasa Watanzania tupo katika hatua muhimu sana ya kujiandaa kufanya uchaguzi hapo tarehe 30 mwezi Oktoba 2005 . Tusipokuwa makini tutatumbukia katika shimo la nyoka hatari wenye sumu kali, ambao bila shaka watatuangamiza. Tuufananishe huu wakati kama vile tupo ufukweni tukisuburi chombo tuende upande mwingine wa ziwa. Tunahitaji kufanya maamuzi makubwa na tusipokuwa makini ama tusipotumia busara, tutaweza kujikuta tumepanda meli mbovu isiyokuwa na nahodha mahiri na hivyo kujiweka katika hatari kubwa ya kuangamiza maisha yetu. Tukumbuke kwamba tusipofanya maamuzi ya busara, ambayo hadi siku ya kupiga kura yatakuwa ya hiari, tutalazimika kuteseka kwa kipindi kirefu, pengine kisichopungua miaka mitano. Nani ana uwezo wa kutuongoza na kutufikisha tuendako? Pia ni nani ama chama gani zaidi ya CCM kinachoweza kuendeleza mafanikio makubwa ambayo tayari yameshapatikana katiaka sekta mbalimbali hapa nchini ikiwemo ile ya elimu? Ikiwa Chama Cha Mapinduzi kimesimamia na Kuwezesha mafanikio makubwa namna hii kwa kipindi kifupi cha miaka kumi kilipokuwa madarakani tangu kuanzishwa vyama vingi vya siasa hapa nchini, ni kwa sababu gani tusiamini kuwa CCM inaweza kufanya mengi na makubwa zaidi kwa kipindi kijacho?

 

Itambulike wazi kuwa suala la maendeleo si la mzaha hata kidogo. Maendeleo hayaji kwa kusema tu katika majukwaa kama wanavyofanya wanasiasa mbalimbali katika kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi mkuu wa rais na wabunge. Mabadiliko katika maendeleo hayaji kwa muda mfupi kama ambavyo wapinzani mbalimali wamekuwa wakiahidi. Labda watuhakikishie uwezo wao wa kufanya miujiza, na ikiwa hivyo wafanye michache tuione kabla ya kuwapigia kura katika uchguzi mkuu unaokaribia. Ni jambo la busara tukatilia maanani kuwa taifa kubwa na lenye heshima kama hili la Tanzania, haliwezi kugeuzwa kuwa uwanja wa majaribio na wanasiasa ambao hawajakomaa.

 

Wote tunatambua kuwa iIli kuleta maendeleo endelevu, katika taifa lolote lile tunahitaji sera ambazo zitaliongoza taifa katika sekta zote, Mbili kuwepo na viongozi wenye uzalendo na wanaojituma kwa moyo wao wote katika shughuli mbalimbali za ujenzi wa taifa, wasio na ubinafsi na wenye utayari wa kuwatumikia wapiga kura. Tatu:- Kuwepo na demokrasia ya kweli yenye kuheshimu haki na utu wa binadamu, na utawala wa sheria. Haya yote lazima yaanze ama yaonekane dhariri kwenye chama chochote husika. Nne:- Kuwepo kwa dhamira na mchakato wa kupambana na rushwa. Tano: -kuwepo na viongozi mahiri na wenye uzoefu wa kutosha kuliongoza taifa.

 

Wakati sifa zilizoanishwa hapo juu ni mhimili wa maendeleo ya taifa katika nyanja mbalilimbali, wote tunakiri kwamba sifa hizo hazipatikani katika vyama vingine vya siasa isipokuwa Cha Mapinduzi (CCM). Kwa mantiki hiyo inakuwa vigumu kuona ni kwa namna gani maemdeleo tuliyokwisha kuyapata yatakuwa endelevu ikiwa tutawachagua wapinzani kukamata Dola.

 

Wananchi tujihadhari na ahadi za uongo zinazogubika karibia katika majukwaa yote ya vyama vya upinzani wakati huu wa kampeni. Ahadi kama zile za kuwajengea wananchi wote wa sehemu fulani nyumba bora na za kisasa ili waepukane na adha ya kuishi katika nyumba za nyasi, kufuta umasikini kwa asilimia mia moja kwa muda mfupi mara tu wakiingia madarakani, na nyingine zinazofanana na hizo ni bora zikafanyiwa utafiti na wananchi kabla ya kuaminika. Hapa yafaa ikumbukwe kuwa kusema jambo ni kitu kimoja na kulitimiza ni kitu kingine. Wananchi tujiulize, ni kwa namna gani viongozi wa namna hiyo watatimiza ahadi hizo bila ya kuwa na sera na matayarisho ya kutosha. Tujiepushe na wanasiasa wanaohahidi kujenga madaraja hata katika sehemu ambazo hazina mito.

 

Pengine ni jambo la ukweli kabisa kwamba vyama vyote vya siasa vya upinzani vimekuwa ni sehemu ya maisha ya wananchi wengi wa taifa la Tanzania. Ingekuwa vyema vyama vya upinzani wakaliambia taifa hili ni kwa namna gani wao kama sehemu ya uhai wa taifa hili wamejaribu kutatua matatizo hayo wanayoyahubiri katika majukwaa ya kisiasa na sio tu kungojea hadi watakapoingia madarakani. Tukumbuke kuwa wapinzani siyo tu kwamba nao ni sehemu ya jamii hii ya watanzania bali wengine wengi kati yao wamewahi kushikilia nafasi mbalimbali katika kuliongoza taifa hili. Ikiwa walishindwa kuwatumikia wapiga kura wakati ule wa uongozi wao, leo hii ni lipi jipya watakalolifanya? Labda lile la kufoji pasi za kusafiria kwenda ngambo kulidhalilisha taifa. Kama kweli wapinzani wameguswa na wana uchungu na hali duni za baadhi ya wanachi, basi waonyeshe kwa vitendo wakati wote na sio tu kuyazunguzia hayo katika majukwaa hasa wakati uchaguzi mkuu unapokaribia. Inasikitisha sana na pia inakera kuona kuwa wapinzani hugundua matatizo ya wananchi pale tu uchaguzi mkuu unapokaribia. Kwa maneno mengine bado tunasisitiza kuwa Chama Cha Mapinduzi bado kina kila sababu ya kuendelea kuaminiwa na wananchi na hivyo kupewa ridhaa ya kuongoza Tanzania, kwani CCM imekuwa inaishi kila siku na kila wakati sambamba na maisha ya Watanzania. Tofauti na Vyama vya Upinzani ambavyo vinakuwa hai na uwezo wao wa kuwaona wananchi hutokea wakati wa uchaguzi pekee. Ndugu Watanzania Kura zote za NDIYO tuipe CCM. Hapo tarehe 30 Oktoba 2005.

 

 

 

Nguvu ya Hoja,

Abiyani Chuo Kuu.