USHINDI WA JAKAYA KIKWETE NA CCM NI DHAHIRI 2005

 

Kasi inaongezeka ya mbio za wagombea wa vyama mbalimbali vya siasa katika nafasi ya urais, ubunge/uwakilishi na udiwani, kwa Uchaguzi Mkuu wa 2005 hapa nchini. Sambamba na kasi ya kuelekea ukingoni hapo tarehe 30/10/2005, ni kupanda kwa mapigo ya moyo ya wagombea wengi hususan wale wa nafasi ya urais. Hali ni shwari kabisa kwa Komredi, Ndugu yetu na Shujaa wa kitanzania, Jakaya Mrisho Kikwete. Mapigo ya Moyo ya ndugu yetu Kikwete yako barabara. Kwake, uhakika wa ushindi, uliombatana na ari mpya ya kubeba bendera ya taifa la Tanzania ili kuonesha uaminifu, uadilifu, utiifu, utayari na umahiri wa kuwatumikia watanzania vinaongeza kasi-msingi. Lengo ni kuhimili nia ya kweli ya kujenga Tanzania yenye neema tele na itakayohimili Maisha Bora kwa Kila Mtanzania.

 

Ushiriki wa Amani na Utulivu uliooneshwa na CCM katika awamu mbalimbali zinazojenga mchakato mzima wa Uchaguzi Mkuu 2005 ulipata tafsiri pogo toka kwa vyama vingi vya upinzani. Wao waliamini huo ulikuwa ni mpito kuelekea NARC kama ambavyo wapinzani hao walivyotamani iwe. Waliiombea CCM dua mbaya. Walisahau kuwa Dua za kuku hazimpati Mwewe. Kosa kubwa ni kwa Vyama hivyo vya upinzani kujifanya kusahau kwamba Amani na Utulivu ni Sera ya CCM, ambayo iliasisiwa ndani ya harakati za kudai Uhuru, ambao ndiyo kiini cha utaifa tunaojivunia. Amani na Utulivu ndiyo mzizi wa chemchem inayozaa umakini, historia ya ushindi, mshikamano, umoja wa kitaifa, muungano, sera zinazotekelezeka, mvuto wa CCM kwa wananchi, na hivyo wananchi kuipa CCM kura za Ushindi wa Kishindo.

 

Mchecheto, hekaheka, hofu na taharuki ya kushindwa ya vyama vya upinzania, imekuwa ikizua mkakati wa kampeni ulioacha wananchi makini wakijiuliza maswali yasiyo na majibu. Mfano, tumeshuhudia kampeni zilizopambwa na ufahari wa Fuso lukuki zikihama kutoka eneo hili hadi lile mithili ya wanyama jamii ya Nyumbu wa Masaimara. Hii ni hofu ya kushindwa kwani hata pale vyombo vya serikali vyenye dhamana ya kulinda raia na mali zao, vilipopiga marufuku matumizi ya Fuso kusafirisha abiria, ndugu zetu hawa walikaidi mtindo mmoja. Wananchi wanapata mashaka ya kuwapa kura ndugu hawa ambao kwao ni kawaida kukaidi sheria na taratibu za nchi za kulinda Amani na Utulivu wa nchi yetu.

 

Hofu ya kushindwa kwa Vyama vya Upinzani inavuta kasi. Sasa kampeni zinapambwa na vituko vya karne na vya kutisha. Tumeshuhudia matumizi ya mawe, mapanga, kuzusha uongo, uchokozi kwa vyombo vya Dola ati tu wapate huruma kwa mataifa ya nje. Mkakati huu kamwe siyo ustaarabu wa taifa letu, na unakiuka misingi ya ulinzi wa Amani na Utulivu wa taifa. Ni kituko kushawishi wananchi wakupigie kura kwa kuzusha vurugu ambazo zinaangamiza maisha ya wananchi hao unaodai unataka kuwatumikia. Ndugu zetu hawa kamwe siyo wenzetu na wanayo malengo mengine tofauti yale ya usajili wao kama vyama vya siasa vya Tanzania.

 

Mchecheto wa kushindwa uliovunja rekodi ya karne ni ule wa kampeni za kutumia helikopta. Hili nalo limezua maswali mengi yasiyo na majibu. Hiki ni miongoni mwa vyama vilivyolalamikia sana CCM na serikali zake, kwamba zina matumizi mabaya ya rasilmali za nchi. Ni hawahawa waliohoji kuhusu ununuzi wa ndege ya serikali “ya Rais”. Ni hawahawa wamekuwa wakilalamikia ufinyu wa ruzuku wanayopewa na serikali. Wananchi tuna haki ya kuhoji ni wapi wamepata mifedha mingi ya kununua/kukodi helikopta. Iwapo ni misaada, tunahitaji kujua mataifa au mashirika yanayohusika na undani wa mikataba na makubaliano yao. Na iwapo ni mifedha kutokana na mkopo, ni haki yetu wananchi wapiga kura, kabla ya kupiga kura tuelezwe vyanzo vya mapato na utaratibu watakaotumia kulipa deni kubwa kiasi hicho. Ni hatari kukichagua chama ambacho kitaanza kutuingiza katika madeni makubwa hata kabla chama hicho hakijaingia madarakani.

 

Helikopta hupita hewani na hivyo kumfanya mgombea kuwa mbali na uhalisia wa mazingira ya wananchi. Iwapo hivi sasa mgombea ameanza kuonesha cheche za kujiweka mbali na wananchi, ni hatari sana kumpa kura zetu, kwani mara akiingia madarakani ndiyo hataonekana kabisa. Madai kwamba helikopta inarahisisha kufanya mikutano mingi kwa wakati mmoja, ni kebehi kubwa kwa wananchi. Wananchi siyo vifaranga ambavyo mgombea anaona kuvitotoa kwa wingi kutampa faida kubwa ya ki-fedha.

 

Lakini, wananchi tunapata mashaka makubwa pale tunaposhuhudia baadhi ya wagombea, hususan wa nafasi ya urais, wakiogopa kujitambulisha na asili ya vyama vyao. Wagombea hawa kamwe hawavai Sare za Vyama vyao. Hekima zinasema, “tija huanzia nyumbani”. Iwapo wagombea hawa hawapendi kujifungamanisha na asili yao na hata kujivunia hadharani, watatushawishi namna gani tuwaamini kuwa hawatautosa u-Tanzania wetu ambao ndiyo asili na fahari  ya taifa letu?.

 

Sera za vyama vya siasa mbali na utambulisho, ni kielelezo cha uzalendo wa kweli na fungamano la uaminifu wa utaifa. Ni kutudanganya kwa ndugu zetu hawa kudai kwamba wanao uwezo wa kubeba bendera ya taifa kubwa, wakati hawana utayari wa kuvaa bendera ya vyama vyao hadharani. Wananchi wapigakura tuna haki ya kuwa na mashaka kuhusu hili. Kama nia ni kuonesha mavazi ya kimapinduzi, au kuiga mavazi ya Mwl. Nyerere wakati anadai Uhuru, hekima isiyotia shaka ingekuwa ni kujenga dhamira hiyo juu ya msingi wa kitanzania unaowakilishwa na alama halali za vyama vya siasa husika. Ni vigumu kwa wananchi kutofautisha kati ya NGOs na Vyama vya siasa. Wananchi watahofu kutoa kura zao zenye thamani kwa wagombea ambao hawana udhamini unaotambulika na unaoaminika. Mtu huyo, akichaguliwa, na itokee avuruge, kisha atoroke, wananchi watamdai nani?. Na hii dhana ya “Wakati wa Mwl. Kudai Uhuru”, ni hatari, kwani inabeza Uhuru na Utaifa wetu ulioasisiwa na Mwl. Nyerere, Baba yetu tunayemheshimu na kumthamini .

 

Ndiyo sababu wananchi wengi wa Tanzania na walio na mapenzi mema na nchi yao, bado wanaelekeza kura zao zote kwa CCM. Wagombea wote wa CCM, wake kwa waume daima huona fahari na kujitambulisha wazi pasipo mashaka kwa kuvaa Sare za CCM. Hii ni moja ya kiashiria cha msingi kinachotupa uhalali wa kukiri kuwa Ushindi wa Ndugu yetu Jakaya Kikwete uko wazi na hauna mashaka. Ng’ara Kikwete, Ng’ara CCM.

 

Dhana ya kufaa kuongoza nchi inayoendelea kama Tanzania haipimwi kwa uwezo wa Chama cha siasa kusimamisha mgombea urais kila inapofika wakati wa uchaguzi. Nchi siyo sawasawa na gari la mabua. Uongozi unahitaji kuwepo kwa mifumo ya kifikra, kisiasa, kiuchumi, kimwelekeo nk ambayo imetanda kama mizizi nchi nzima kwa uwiano unaohimili falsafa ya uongozi, utawala na kutumikia watu. Ni Chama Cha Mapinduzi peke yake ndicho kwa sasa kinatosheleza sifa hii. Ndiyo maana tunasema pasipo kusita kwamba ni CCM pekee inayofaa kukabidhiwa tena uongozi wa Tanzania 2005.

 

Vyama vya upinzani vina mtandao hafifu wa uhai na uongozi mithili ya madoa doa na viraka katika nchi. Kinadharia na kiutendaji mawasiliano kati ya viraka hivyo ni magumu na pingamizi/kikwazo kwa uhai na uimara wa taifa linalovuta kasi ya maendeleo ili kukabiliana na changamoto za utandawazi. Umoja, Amani, mshikamano na utulivu wa taifa vitakuwa hatarini.

 

Aidha uongozi wa nchi siyo ubingwa wa kukosoa, kuona mapungufu peke yake na kushindwa kuona mafanikio. Upofu huu wa vyama vya upinzani wa kuto kuona mafanikio ya CCM, umewafanya washindwe kujitambua kuwa hata wao wamezaliwa, wamekua ndani ya historia ya CCM. Iwapo CCM haijafanya jambo zuri hata moja, basi na viongozi wa vyama hivyo vya upinzani ni zao-mapungufu hayo wanayoyahubiri. Wananchi tuna haki ya kukataa kuwapa kura zetu, kwani tuna mashaka na umakini wa vyama hivyo.

 

Ubingwa wa kukosoa wachezaji siyo ubingwa wa kucheza. Tumeshuhudia mabingwa wa kukosoa katika soka kama wakiwekwa uwanjani kucheza, hawana stamina, wanaboronga kiasi cha kutia kichefuchefu. Wananchi wanachohitaji kusikia kutoka kwa vyama vyote vya siasa ni sera zinazotekelezeka na zinazoonesha namna wananchi watakavyoshirikishwa na kuwezeshwa katika kulijenga taifa lao na kuleta maendeleo yao binafsi na nchi nzima. Ni CCM peke yake ndiyo ina Ilani inayotosheleza kuwatambua, kuwajali, kuwathamini na kuwatumikia Watanzania. Chonde Watanzania, Chagua CCM, Chagua Kikwete.

 

Kikwete atakuwa na mahali pa kuanzia. Tofauti na vyama vya upinzani ambavyo vitakuwa vinaanza upya na hivyo kuwa na hatari ya kuvuruga kabisa misingi ya uchumi na utaifa wetu. Kikwete atakuwa anaendeleza mafaniko yote ambayo yamefanywa na CCM katika historia ya uongozi wake hapa nchini. Ni rahisi sana kwa wananchi kujua tunaeleka wapi tukiwa na uongozi wa CCM. Wananchi tumekuwa sehemu ya mabadiliko makubwa na madogo na tumeonesha ushirikiano na ushirikishwaji wa hali ya juu. Tukimchagua Kikwete, hakutakuwa na muda wa kupoteza wa kujiandaa na kuelewa mazingira, na hata kufanyia mazoezi sera. Mara tu Kikwete akishika usukani, maendeleo ya Taifa yatasonga mbele kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya. Hakika tutaokoa muda. Vyama vya upinzani, vitapoteza muda, kwani badala ya kuvuta kasi kwenda mbele, vinaweza kuvuta kasi ya kwenda nyuma, na hata ya kutukoroga, na kutuchanganya. Mfano rahisi ni namna viongozi wanavyovaa mavazi yasiyo na maana wazi kwa wananchi.

 

Kikwete anao uzoefu wa kulitumikia taifa hili katika nyanja na kada mbalimbali. Uzoefu uliotukuka katika ushirikiano wa kimataifa umempa uzoefu mkubwa sana wa kuongoza nchi vema na kuiepusha na athari hasi za utandawazi. Kikwete amekuwa mstari wa mbele katika kujenga suluhu kwa njia ya mazungumzo katika nchi za Maziwa makubwa. Zaidi, Kikwete anakijua vema chama chake CCM. Amekua na kuitumikia CCM katika umri wake wote. Kamwe hataiangusha CCM. Aidha, Kikwete amekua na kulelewa katika uongozi wa Mwl. Nyerere. Hivyo, atakuwa mrithi mzuri wa fikra za Baba wa Taifa. Chini ya uongozi wa Kikwete, Uhuru, Utaifa, Amani na Utulivu utasonga mbele kwa kasi mpya.

 

CCM ina historia ya kushinda. CCM itashinda tena kwa kishindo 2005. Ushindi huu unasubiriwa kwa hamu na vijana wote wa Tanzania. Zaidi, vijana wanafunzi na wale wa Vyuo vya Elimu ya Juu. Kiu ya matumaini ya Vijana hawa wa shule na vyuo inatokana na ukweli kwamba, Ndugu yetu Jakaya Kikwete na familia yake ni zao halisi la shule za hapa nchini na Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Ndugu Kikwete ni tunda halisi lenye mizizi katika harakati za Uhuru wa Tanzania na Utaifa wetu, ambavyo vilivuta kasi sambamba na majira alipozaliwa shujaa huyu. Hakika, vijana na wanazuoni wote wanayo kila sababu ya kukiri waziwazi kwamba watampa mwenzao na ndugu yao Kikwete kura zote za ndiyo. Ng’ara Kikwete, Ng’ara CCM.

 

Pamoja na ari waliyokuwanayo watanzania, hususan vijana ya kumpa kura zote Kikwete, ni vema utayari huo uwe ni mtaji-msingi wa kumuunga mkono Ndugu Kikwete kutekeleza kwa ufanisi yale yote aliyowaahidi watanzania, na ambayo yamo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM-2005. Vijana mpeni Kikwete ushirikiano, muwe tayari kufanya kazi kwa bidii, muwe na moyo wa kulipenda taifa lenu, moyo wa kujitegemea na kukataa umasikini. Aidha, vijana muwe na ubunifu, utii wa sheria na hofu ya Mungu ili kwa pamoja muweze kujenga Tanzania yenye Neema tele kwa Ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya. Ni Tanzania ambamo vijana mnaishi leo na kesho.

 

Tuendelee kuwapa vyama vya upinzani muda zaidi wa kukua na kuotesha mizizi ya uhai nchi nzima. Kinyume na hapo bado Watanzania tutaendelea kuwa na mashaka ya kuvikabidhi vyama hivi uongozi wa nchi yetu, Mama, Tanzania.

 

Watanzania tuendelee kuwa na msimamo na utulivu huku tukitunza vyote; Shahada za kupigia kura na dhamira ya kumpa ndugu yetu Jakaya Kikwete, CCM kwa ujumla, kura zetu zote za ndiyo. Chini ya uongozi wa Kikwete, Maisha Bora kwa kila Mtanzania yatapatikana.

 

Nguvu ya Hoja.

Abiyani Chuo Kikuu.