[Omar R. Mapuri]
UTANGULIZI:
Rushwa ni miongoni mwa matatizo ya awali
kabisa katika historia ya binadamu.
Katika hisotira yote hiyo hadi leo, rushwa katika majina na aina zake
nyingi sana ipo kila pahala; katika kila jamii ya binadamu na katika kila nchi,
maskini na tajiri. Jamii za binadamu na
nchi zinatofautiana tu katika viwango vya rushwa, lakini hakuna inayoweza
kujigamba kwa dhati kuwa haina rushwa kabisa kabisa hata angalau katika upande
wa utoaji kama si wa upokeaji.
Tanzania ikiwa ni sehemu ya jamii kubwa ya kimataifa, inalo tatizo kubwa la rushwa, na kama ilivyo kwa jamii zingine ulimwenguni, imo katika mapambano ya kudumu dhidi ya sarakani hiyo. Miongoni mwa hatua za msingi zilizochukuliwa katika hatua mbali mbali za mapambano hayo baada ya Uhuru mwaka 1961 ni kuanzishwa kwa Tume ya Kudumu ya Uchunguzi (1966), kutungwa kwa Sheria ya Kuzuia Rushwa (1971), kuanzishwa kwa Kikosi cha Kuzuia Rushwa (1975) ambacho hivi sasa ni Taasisi ya Kuzuia Rushwa, kutungwa kwa Sheria ya Uhujumu Uchumi (1983) na marekebisho yake yaliyoleta Sheria ya Kudhibiti Uhalifu wa Kiuchumi na Ulioandaliwa (1984). Pamoja na hatua hizo, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kikiwa Chama tawala kilichoshika hatamu katika mfumo wa chama kimoja, mwaka 1989 kiliunda Kamati iliyochunguza tatizo la Rushwa na ukiukwaji wa maadili ya uongozi. Kamati hiyo iligundua kwamba tatizo hilo lilikuwa limefikia viwango vya kutisha.
Katika Uchaguzi Mkuu wa 1995 ambao
ulikuwa wa kwanza chini ya mfumo wa vyama vingi, suala la rushwa lilikuwa
miongoni mwa vipengele vya msingi vya kampeni za vyama vilivyokuwa vikigombea,
kikiwemo CCM. Baada ya ushindi wa CCM,
Rais Benjamin Mkapa aliunda Tume ya Uchunguzi Dhidi ya Rushwa (maarufu Tume ya
Warioba). Tume hiyo ilibaini aina mbali
mbali za mianya ya rushwa na kupendekeza hatua za kuiziba na kupambana na
tatizo zima la rushwa kwa jumla.
Mapendekezo hayo yalifanyiwa kazi na Serikali kwa njia ya hatua mbali
mbali zilizochukuliwa ambazo zitabainishwa baadae katika makala hii.
Wakati huu tukielekea Uchaguzi Mkuu wa
Oktoba 2005, mjadala umeshamiri miongoni mwa Watanzania kama kiwango cha rushwa
nchini kimepungua, kimebaki pale pale au kimeongezeka. Kutokana na kutotumika kwa vigezo vinavyopimika
kwa uhakika, mjadala huo umegubikwa zaidi na hisia na dhana tu. Wanaodai kuwa rushwa imeongezeka,
hawaonyeshi vigezo vinavyopimika kuthibitisha madai yao. Hivyo hivyo kwa wanaodai kuwa rushwa
imepungua au iko pale pale.
Kwa bahati nzuri, Taasisi ya Uwazi
Duniani (Transparency International) ambayo inafuatilia mwelekeo wa
rushwa duniani na jitihada za kupmbana nayo, imebuni kipimo cha rushwa
ilichokiita Corruption Perception Index (CPI). Kiswahili labda ni
Fahirisi ya Rushwa. Kipimo hicho kina
upeo wa alama kuanzia 0 hadi 10 ambapo 0 inaonyesha kukithiri kwa rushwa (yaani
hakuna hata chembe ya uadilifu) na 10 maana yake hakuna kabisa rushwa (yaani
uadilifu uliokamilika). Hata hivyo, kwa
lengo la kumrahisishia tafsiri Mtanzania wa kawaida, kipimo hicho tutakiita Fahirisi
ya Uadilifu kwa maana ya kwamba inapokuwa ndogo inaashiria upungufu wa uadilifu
(au ukubwa wa rushwa) na inapokuwa kubwa ni kinyume chake.
Transparency International (TI) hukikokotoa kipimo hicho kutokana na
taarifa za utafiti inazozikusanya katika nchi.
Katika tafiti (surveys) hizo za kisayansi, TI hutaka tathmini na
maoni ya watu wanaoathirika sana na tatizo la rushwa (kama vile wafanyabiashara
wa ndani na nje ya nchi inayotathminiwa) kuhusu tatizo la rushwa na ukubwa wake
katika nchi, kwa kutumia njia ya sampuli nasibu. Ufafanuzi wa Fahirisi ya Uadilifu inavyopatikana uko nje ya upeo
wa madhumuni ya makala hii, lakini itoshe tu kukiri kwamba kipimo hicho
kinaheshimika sana duniani.
Toka mwaka 1995, TI imekuwa ikifanya
tafiti na kuchapisha taarifa za kila mwaka zinazoonyesha viwango vya rushwa vya
nchi mbali mbali duniani kwa kutumia kipimo cha Fahirisi ya Uadilifu. Tanzania ilianza kuingizwa katika tafiti
hizo mwaka 1998 na imeendelea kuwamo mfululizo hadi sasa. Katika kipindi hicho, Fahirisi ya Uadilifu
ya Tanzania imeongezeka kutoka 1.9 mwaka 1998 hadi 2.9 mwaka 2005. Ni dhahiri kwa hivyo kwamba kwa kipimo
hicho, kiwango cha uadilifu nchini Tanzania kimeongezeka kwa kima cha asilimia 52.6
katika kipindi hicho. Kwa maneno
mengine, kiwango cha rushwa kimepungua kwa kima hicho hicho cha asilimia 52.6.
Katika makala hii, zaidi ya kubainisha
hatua mbali mbali zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tatu chini ya Rais
Benjamin Mkapa kupambana na rushwa, tutaonyesha kwa ufafanuzi jinsi Tanzania inavyopiga
hatua katika mapambano hayo kwa ulinganisho na nchi jirani za Afrika Mashariki
na nyinginezo za Afrika zinazotafitiwa na TI.
CCM iliingia katika Chaguzi Kuu za 1995 na 2000 na ahadi ya kupambana na rushwa, miongoni mwa ahadi zake kuu za uchaguzi.
Katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 1995,
ahadi ya kupiga vita rushwa iliwekwa katika ibara ya 29 na ilisomeka
ifuatavyo:-
“29. Rushwa ni tatizo kubwa katika jamii yetu
hivi sasa na ni tishio kwa usalama, utulivu na heshima kwa taifa letu. Katika miaka mitano ijayo, Serikali za CCM zitapiga vita
kwa nguvu zaidi rushwa nchini kwa njia zifuatazo:-
(a)
Kuhakikisha
kwamba Serikali za CCM zinazingatia kwa dhati sheria za utawala Bora na Maadili
ya Viongozi, pamoja na kutakasa safu za uongozi ndani ya Serikali zote mbili na
vyombo vyao vyote.
(b)
Kuendeleza
kwa nguvu zote vita vilivyokwishaanzishwa dhidi ya rushwa ndani ya vyombo vyote
vya utoaji haki ili haki isiuzwe wala kununuliwa.
(c)
Kuwalinda
wananchi wanaowafichua wapokeaji na watoa rushwa.
(d)
Kuona
kwamba Serikali inakuwa wazi zaidi katika kuwekeana mikataba, tenda na
kandarasi mbali mbali ili kulinda maslahi ya umma wa wakulima na wafanyakazi wa
nchi yetu.
(e)
Kuona
kwamba Serikali inadhibiti kwa makini zaidi masuala ya uhamiaji, huduma za
Bandari na Ushuru wa Forodha ili kupambana kwa ukamilifu na watoaji na
wapokeaji rushwa na wakwepaji kulipa ushuru na kodi nyingine katika maeneo
hayo.
(f)
Kuona
kwamba Serikali zote mbili zinahakikisha kuwa mifumo ya utendaji kazi
inapunguza fursa (mianya) ya kutoa na kupokea rushwa”.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000, CCM ilikuwa tena na kauli ya ahadi ya vita dhidi ya rushwa na hujuma za kiuchumi. Ahadi hiyo imo katika ibara za 92 na 93 za Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka wa 2000, na inasomeka kwa sehemu kama ifuatavyo:-
“92. Mapambano dhidi ya rushwa ni ahadi na sera
ya TANU, ASP na sasa CCM. Serikali ya
Awamu ya Tatu imechukua hatua madhubuti kupambana na rushwa ndani ya CCM,
katika vyombo vya umma na jamii kwa jumla ……….”
“93. Baada ya mafanikio makubwa yaliyopatikana
katika kupambana na rushwa katika kipindi cha uongozi kilichopita, CCM katika
kipindi cha miaka mitano ijayo itafanya yafuatayo:-
(i)
Serikali
zitaendelea kuchukua hatua za kisheria, kiutawala na kinidhamu kwa wale wote
waliobainika walihusika na vitendo vya rushwa. Katika kipindi hiki, Serikali zitahakikisha haya yote
yanaendelezwa ili kufikia lengo linalohitajika, yaani kutokomeza rushwa.
(ii)
Serikali
zitaimarisha uwezo na nguvu za wananchi kuwawezesha kuzidisha vita dhidi ya
rushwa. Wananchi wataelimishwa na
kuhamasishwa juu ya haki zao, asili na aina ya rushwa, mbinu za kutambua na
kukabiliana na vitendo vya rushwa, mbinu za kutoa taarifa za rushwa kwenye
vyombo vya dola na namna ya kujikinga dhidi ya athari zinazotokana na kuwaumbua
wala rushwa.
(iii)
Serikali
zitaendelea kusisitiza kwamba viongozi na watendaji waheshimu utawala wa sheria
na utawala bora, na kuzingatia maadili na uadilifu wakati wote wa kuwahudumia
wananchi. Aidha, Serikali zitaendelea
kusafisha safu za uongozi na utendaji Serikalini watakaobainika kujihusisha na
vitendo vya rushwa na kuwachukulia hatua zinazostahili.
(iv)
Serikali
zitaelekeza mapambano dhidi ya rushwa kwenye vyombo vya haki kwa nguvu na kasi
kubwa zaidi. Vyombo vya fedha, hususan,
sekta ya ukusanyaji mapato na mabenki vitaangaliwa kwa umuhimu wa pekee ili
mapato yanayopaswa kukusanywa na matumizi yake yadhibitiwe.
(v)
Katika
kuimarisha uchumi, Serikali zitaendelea kuweka na kusimamia misingi ya uwazi na
uwajibikaji katika mikataba, tenda, ununuzi na udhibiti wa viwango vya
utekelezaji wake. Pia Serikali
zitachukua hatua za kuhuisha au hata kuvunja mikataba yo yote itakayoonekana
utekelezaji wake umegubikwa na vitendo vya rushwa.
(vi)
Serikali
zitaendelea kuboresha na kurahisisha taratibu za uwekezaji ili kuondoa vishawishi
vya rushwa. Aidha, Serikali
zitafuatilia mtiririko wa uwekezaji kuhakikisha kwamba wawekezaji nao wanafuata
sheria, taratibu na maadili ya uwazi na uwajibikaji.”
Mara tu baada ya ushindi wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 1995, Rais Benjamin Mkapa aliunda Tume ya Uchunguzi Dhidi ya Rushwa, maarufu kwa jina la Tume ya Warioba kutokana na Mwenyekiti wake, Jaji Joseph Sinde Warioba, Waziri Mkuu Mstaafu. Katika ripoti yake yenye uchambuzi wa kina kuhusu hali ya rushwa nchini wakati huo, Tume hiyo ilibaini mianya mingi ya rushwa. Tume iligundua pia kwamba rushwa ilifikia viwango vya juu kiasi kwamba ilichangia sana katika kudumaza uchumi wa nchi na ilikuwa kikwazo kikubwa katika ufanisi wa utendaji Serikalini ambapo malengo ya kiuchumi na kijamii yalikuwa hayafikiwi. Mapato ya Serikali yalikuwa yakiingia mifukoni mwa wajanja badala ya kuelekezwa kwenye kukuza uchumi wa nchi. Hali hiyo iliathiri vibaya imani ya wananchi kwa Serikali.
Tume ilipendekeza hatua mbali mbali za
kupambana na rushwa zilizogawika katika maeneo mawili makuu ya kimkakati. Maeneo hayo ni kwanza kuziba mianya ya
rushwa na pili kuwafichua na kuwachukulia hatua za kisheria, kiutawala na
kinidhamu wanaobainika kujihusisha na vitendo vya rushwa.
Mara tu baada ya kukabidhiwa Ripoti ya Tume ya Warioba, Rais Mkapa alichukua hatua zifuatazo:-
Hatua hizi zilifungua milango
kwa hatua nyingi mahususi zilizokoleza vita dhidi ya rushwa.
Kwa upande wa kuziba mianya ya rushwa, hatua zifuatazo ni baadhi ya
zilizochukuliwa katika hatua mbali mbali za mapambano dhidi ya rushwa kuanzia
1996 hadi 2004:-
Kwa upande wa kukabiliana na watuhumiwa
wa rushwa, hatua
zifuatazo zimechukuliwa katika hatua mbali mbali za mapambano:-
Hatua hizo za kuziba mianya ya rushwa na kuwakabili wala rushwa, zimechangia kwa kiasi kikubwa katika mafanikio ya kiuchumi na kijamii yafuatayo miongoni mwa mengine:-
Hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa kupiga vita rushwa toka 1995 hadi sasa ni ushahidi tosha wa dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tatu chini ya CCM kupambana na rushwa. Matokeo ya hatua hizo ni kukua kwa uchumi na unafuu katika upatikanaji wa huduma mbali mbali za elimu, hali ambayo inaashiria dalili za kupungua kwa rushwa.
Hata hivyo, kutokana na tathmini za
kihisia ambazo aghlabu zinaathiriwa na mitazamo na misimamo ya kisiasa,
Watanzania wamegawanyika. Wapo
Watanzania wanaoamini kuwa kiwango cha rushwa kimeongezeka katika kipindi cha
1995-2005. Wapo wanaooamini kuwa
haikuongezeka wala kupungua. Lakini pia
wapo wanaoamini kuwa imepungua. Lakini
wote hao huwa hawatoi vielelezo vya kuthibitisha madai yao.
Kutokana na ukweli kwamba dhana ya rushwa
imesimama juu ya msingi wa hisia kutokana na ugumu wa kuithibitisha, pengine
mjadala juu ya kuongezeka au kupungua kwa kiwango cha rushwa si rahisi kutoa
jawabu linaloweza kukubalika kwa wote katika jamii. Kwa maana hiyo, mjadala utaendelea tu wakati wote. La muhimu kuzingatia ni kwamba mijadala hiyo
ndiyo inayochochea mapambano dhidi ya rushwa kwa maslahi ya jamii.
Hata hivyo, pamoja na ukweli huo,
wanasayansi hawajapumzika katika kutafuta vigezo vya kitarakimu vya kupimia
kiwango cha rushwa katika jamii. Ndipo
TI walipokuja na kigezo cha Fahirisi ya Uadilifu, kilichofafanuliwa katika
Utangulizi. Kipimo hicho kinawezesha
kubaini kwa uhakika zaidi kuongezeka au kupungua kwa kiwango cha rushwa katika
nchi na kulinganisha viwango vya rushwa baina ya nchi na nchi. Kwa bahati nzuri, toka 1998, Tanzania imo katika
tathmini ya kimataifa ya viwango vya rushwa inayofanywa kila mwaka na TI. Matokeo ya tathmini hii yanawapa fursa
Watanzania kufuatilia mabadiliko (kuongezeka au kupungua) ya viwango vya rushwa
nchini na pia kujua nafasi yao katika upeo wa kimataifa. Makala hii imekusudiwa pia kuwaarifu
Watanzania kuwepo kwa kigezo hiki ili nacho wakitumie katika mjadala wa rushwa
kwa uelewa na utulivu zaidi.
Kama ilivyokwishaelezwa, Fahirisi ya Uadilifu ya Taasisi ya Uwawazi Ulimwenguni (TI) ni kipimo kinachowezesha kufuatilia mabadiliko ya viwango vya rushwa na kulinganisha baina ya nchi na nchi. Katika sehemu hii ya makala hii tutaitumia fursa hiyo kuilinganisha Tanzania na nchi jirani na washiriki wake katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, yaani Uganda na Kenya.
Jedwali Na. 1 linaonyesha Fahirisi za Uadilifu za Tanzania, Uganda na Kenya kwa miaka 8 toka 1998 hadi 2005.
|
Jedwali Na. 1: Fahirisi za Uadilifu za Tanzania kwa
Ulinganisho na za Uganda na Kenya, 1998-2005
|
|||
MWAKA |
FAHIRISI ZA UADILIFU (KATIKA 10) (Corruption Perception Index) |
||
|
|
Tanzania |
Uganda |
Kenya |
|
1998 |
1.9 |
2.6 |
2.5 |
|
1999 |
1.9 |
2.2 |
2.0 |
|
2000 |
2.5 |
2.3 |
2.1 |
|
2001 |
2.2 |
1.9 |
2.0 |
|
2002 |
2.7 |
2.1 |
1.9 |
|
2003 |
2.5 |
2.2 |
1.8 |
|
2004 |
2.8 |
2.6 |
2.1 |
|
2005 |
2.9 |
2.5 |
2.1 |
|
Ongezeko baina ya 1998 na 2004 |
1.0 |
-0.1 |
-0.4 |
|
Ongezeko kiasilimia |
52.6% |
-4.0% |
-19.0% |
|
Chanzo: www.transparency.org |
|||
Inaonekana kwamba Fahirisi ya Uadilifu ya
Tanzania imeongezeka kutoka 1.9 mwaka 1998 hadi 2.9 mwaka 2005, likiwa ni
ongezeko la asilimia 52.6. Kwa maana
nyingine, kiwango cha rushwa nchini Tanzania kilipungua kwa asilimia 52.6
katika kipindi hicho.
Kwa ulinganisho na Uganda na Kenya,
Tanzania ilipitwa na nchi hizo kwa uadilifu katika miaka ya 1998 na 1999. Lakini kuanzia mwaka wa 2000 imezipita
mfululizo. Aidha, wakati Fahirisi ya
Uadilifu ya Tanzania iliongezeka kwa asilimia 52.6 baina ya 1998 na 2005, ile
ya Uganda imepungua kwa asilimia 4.0 na ile ya Kenya imepungua kwa asilimia 19.0.
Ni dhahiri kwa hivyo kwamba Tanzania
ina kiwango cha chini kabisa cha rushwa katika nchi za Afrika Mashariki na
inafanya vizuri zaidi kuliko zote katika mapambano dhidi ya rushwa.
Tanzania iemonyesha mwelekeo wa kuongezeka ufanisi hata katika upeo wa Afrika. Jedwali Na. 2 linaonyesha nafasi ya Tanzania katika orodha ya nchi za Afrika zilizotathminiwa na AI kwa kila mwaka, hadi kufikia mwaka 2004.
|
Jedwali Na. 2: Nafasi ya Tanzania Miongoni mwa Nchi za
Afrika katika Uadilifu |
|||||
|
Mwaka |
Nafasi ya Tanzania |
Idadi ya Nchi Zilizoshiriki |
Idadi ya Nchi Ilizogawana Nazo Nafasi |
Idadi ya Nchi Ziliyoipita |
Idadi ya Nchi Ilizozipita |
|
1998 |
14 |
17 |
1 |
14 |
1 |
|
1999 |
12 |
18 |
0 |
15 |
2 |
|
2000 |
12 |
21 |
0 |
14 |
6 |
|
2001 |
11 |
16 |
0 |
11 |
4 |
|
2002 |
11 |
20 |
2 |
10 |
7 |
|
2003 |
11 |
27 |
3 |
12 |
11 |
|
2004 |
9 |
36 |
3 |
13 |
19 |
|
Chanzo: www.transparency.org ANGALIZO:
Wakati makala hii
inaandikwa uchambuzi wa takwimu hizi kwa mwaka 2005 haukuweza kufanyika
kutokana na kukosekana kwa takwimu za msingi. |
|||||
Inaonekana kwamba pamoja na kuongezeka
kwa idadi ya nchi za Afrika zilizotathminiwa na AI kutoka 17 mwaka 1998 hadi 36
mwaka 2004, nafasi ya Tanzania katika Fahirisi ya Uadilifu iliongezeka kwa
ubora kutoka 14 hadi 9 katika kipindi hicho.
Aidha, wakati mwaka 1998, Tanzania iliipita nchi moja tu, mwaka 2004
ilizipita nchi 19. Zaidi, mwaka 2004,
kwa mara ya kwanza kabisa Tanzania ilizipita nchi nyingi zaidi kuliko
ziliyoipita. Miongoni mwa nchi ambazo
awali zilikuwa na Fahirisi ya Uadilifu kubwa zaidi kuliko Tanzania lakini sasa
inazipita au iko sawa nazo ni Kenya, Uganda, Ivory Coast, Zambia, Msumbiji,
Zimbabwe, Malawi, Algeria na Ethiopia.
Miongoni mwa nchi ambazo wakati wote Tanzania imezipita ni Nigeria,
Cameroun, Angola, Chad, Sudan, Sierra Leone, Congo Brazzaville, Niger, Libya na
Eritrea.
Kwa upande mwingine, nchi za Afrika
ambazo wakati wote zimeipita Tanzania kwa uadilifu ni Botswana, Namibia,
Mauritius, Afrika Kusini, Misri, Ghana, Senagal na Morocco.
HITIMISHO:
Kutokana na tathmini hii kwa kutumia vigezo vya ndani na vya Kimataifa, ni maoni yetu kwamba kiwango cha rushwa kimepungua nchini Tanzania kutoka mwaka 1995 hadi 2005. Hayo ni matokeo ya hatua mbali mbali zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tatu chini ya Rais Benjamin Mkapa zilizolengwa mahsusi katika kupambana na rushwa. Rais Mkapa anastahili sifa za pekee katika mafanikio haya kwa jinsi anavyoongoza mapambano haya kisayansi na kwa ujasiri mkubwa. Aidha, kwa vile hatua zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa ni za utekelezaji wa Ilani za Uchaguzi za CCM za 1995 na 2000, CCM inayo haki ya kujisifu kwa matokeo mazuri ya hatua hizo.
Tathmini hii haionyeshi na wala sisi
hatudai kwamba rushwa imekwisha nchini Tanzania. Rushwa bado ipo, tena katika viwango vya juu. Lakini inapigwa vita ipasavyo na inapungua;
tena kwa uendelevu. Hata CCM haikuahidi
katika Ilani zake kwamba itaimaliza rushwa katika kipindi hiki. Kutokana na ukubwa na ugumu wa vita dhidi ya
rushwa, CCM ingeahidi hivyo ingeuhadaa umma wa Watanzania. CCM iliahidi kwamba Serikali zake
zitapambana vikali na rushwa. Serikali
zimetekeleza na zinaendelea kutekeleza hilo kwa ufanisi mkubwa. Mara nyingi Rais Mkapa amekuwa akitukumbusha
msemo wa wahenga kwamba: ada ya mja hunena, uungwana ni vitendo. CCM na Serikali zake imedhihirisha
uungwana huo katika utekelezaji wa kauli yake ya kupambana na rushwa.