TAARIFA YA KATIBU WA ITIKADI NA UENEZI TAIFA WA CCM KUHUSU VURUGU ZILIZOFANYWA NA WAFUASI WA CUF HUKO BAGAMOYO

 

Katika taarifa yangu kwa vyombo vya habari ya tarehe 7Juni,2005, nilitoa kwa CUF siku saba (7) kulaani vitendo vilivyofanywa na wafuasi wake huko Bagamoyo tarehe 5 Juni,2005 na kuwaomba radhi waathirika wa vurugu hizo.  Nilisema bayana kwamba kama hawakufanya hivyo ndani ya kipindi hicho, basi sisi CCM tutaamini kwamba vurugu hizo zilikuwa na baraka za viongozi wakuu wa CUF na pengine walizipanga na kuziandaa kwa makusudi. Aidha, niliongeza kwamba kama tutaridhika kuwa huo ndio ukweli, basi tutafikiri upya kuhusu uhusiano na mashirikiano yetu na CUF.

 

Leo zimekamilika siku saba (7) na CUF imeshindwa kuzilaani vurugu hizo na kuwaomba radhi waathirika.  Kwa hiyo, natangaza rasmi kwamba vurugu zile za Bagamoyo zilibarikiwa na viongozi wa juu wa CUF na uwezekano ni mkubwa kwamba walizipanga na kuziandaa kwa makusudi.  Na hili si la kushangaa kwani mara nyingi viongozi wa juu wa CUF wamekuwa wakisikika hadharani wakitoa kauli za kuwachochea vijana wao kupitia kauli mbio yao ya “Wanaume mapanga shaa shaa shaa.”  Yaani wanoe mapanga.  Tukio la Bagamoyo ni matokeo ya uchochezi huo.

 

Napenda pia kutangaza rasmi kwamba tutaendelea kutafakari  juu ya uhusiano na ushirikiano wetu na CUF.  Tutaendelea  kufuatilia kauli na vitendo vyao.  Mwelekeo wa mabadiliko ya uhusiano na ushirikiano utategemea vitendo na kauli zao.

 

Tamko langu la tarehe 7 June lilikuwa na vipengele vitatu ambavyo  niliwataka viongozi wa CUF wavitolee kauli.  Vipengele hivyo ni:-

 

Katika maelezo yao ya tarehe 9 Juni, 2005, viongozi wakuu wa CUF hawakugusia chochote kuhusu vipengele viwili vya kwanza.  Kushindwa kuzilaani vurugu hizo peke yake kunatosha kuwa ushahidi wa kuhusika kwa viongozi hao katika kuzibarikia vurugu hizo.  Kukanusha kwao kuwa chanzo cha vurugu hizo ni unafiki na uzandiki mtupu, kama kweli walikuwa wakiamini walivyokuwa wanasema kwamba eti CCM ndio ilikuwa chanzo, ingekuwa rahisi kwao kuzilaani  vurugu hizo.  Lakini wameshindwa kuzilaani kwa kuchelea kuwavunja moyo wahuni waliowatuma kwenda kufanya vurugu hizo.  Kwa vyovyote vile huwezi ukakodi gari zaid ya 70 na kuyajaza wahuni, ukawamwaga kijiji kidogo cha Bagamoyo, wakafanya vurugu halafu ukajidai huhusiki na vurugu hizo.  Hakuna atakayekuamini hata ukijieleza kwa bidii kiasi gani.

 

Kwa upande wa kuyshindwa kuomba radhi, hii haitushangazi.  Hii ni kwa sababu kuomba radhi kunahitaji uungwana, na CUF haina uungwana huo. Mbaya zaidi ni pale viongozi hao wa CUF walipojaribu kujisafisha kwa kutumia uongo.  Sijapata kuona watu wenye uhodari wa kuhusika na uongo na kujieleza kwa kujiamini kama viongozi wa CUF.

 

Nilitoa mifano mitatu tu ya uongo waliousema mchana bila ya aibu.

 

 

Sina haja ya kuendelea na uongo mwingine mwingi tu walioutoa viongozi wa CUF, kwamni naamini Watanzania wamekwishaubaini.  Masuala mengine yako mahakamani, si vizuri kuyazungumzia.

 

Ni jambo la faraja kwamba Watanzania wanazidi kuielewa nia mbaya ya viongozi wa CUF, kwa amani ya nchi yetu.  Ushahidi ni jinsi chama hicho kinavyozidi kukimbiwa na watu kama ilivyotokea wiki iliyopita huko Pemba.

 

Namalizia kwa kukitahadharisha chama cha CUF kwamba kama hakitabadilisha mwenendo wake mbaya wa kutishia amani na usalama, kitaendelea kukimbiwa na Watanzania.  Narejea kauli yangu ya wiki iliyopita kwamba kisitafute mchawi, kwani mchawi ni chenyewe.