TAARIFA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI, MHESHIMIWA OMAR R. MAPURI JUU YA KAULI ZA UCHOCHEZI ZA VIONGOZI WA CUF ALIYOITOA TAREHE 28/1/2004 MJINI DAR ES SALAAM

 

Ninalaani vikali kauli za uchochezi na za kujenga chuki na uhasama zilizoripotiwa na vyombo vya habari kutolewa na viongozi mbalimbali wa CUF tarehe 26/1/2004 mjini Dar es Salaam na 27/1/2004 mjini Zanzibar.

 

Kauli kama zile za kuwataka wafuasi wao wajiandae kupambana na polisi, kupiga wake wa polisi au kufanya vurugu nchini siyo tu ni za kujenga chuki, bali pia ni za kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, jambo ambalo ni kinyume kabisa na dhamira za mfumo wa vyama vingi.  Aidha kauli za kuwataka wafuasi wao wawe tayari kuwa vizuka na vilema si za kuwatakia mema wafuasi wao.

 

Kauli hizo zimeripotiwa kutolewa na viongozi hao katika mikutano ya hadhara eti ya kuadhimisha matukio ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001.  Nikiyatazama katika muktadha wa Muafaka Baina ya CCM na CUF ambao Wizara yangu ina nafasi yake mahsusi katika utekelezaji wake, nayaona maadhimisho hayo kuwa yanakwenda kinyume kabisa na dhamira ya Muafaka huo.

 

Viongozi wa CUF husikika sana wakilaumu Serikali na CCM kuwa tunavunja Muafaka.  Lakini kumbe lawama hizo ni za kuficha tu uvunjaji wa Muafaka unaofanywa na wao wenyewe CUF.  Katika maelezo yake ya utangulizi, Muafaka unasema ifuatavyo miongoni mwa mengine:

 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Wananchi (CUF) vinakubaliana kimsingi:

 

KWAMBA lengo na madhumuni makubwa ya kufikia Muafaka huu ni kusahau yaliyopita na kutekeleza, kwa makusudi kabisa, makubaliano yetu ili kujenga demokrasia ya kweli na kwa hivyo kuleta maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa jamii katika nchi yetu.”

 

Kitendo cha kuadhimisha matukio ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001 ambayo yalikuwa ni miongoni mwa agenda zilizofikiwa maelewano katika Muafaka, si cha kusahau yaliyopita, bali ni cha kuyakumbusha.  Hiyo siyo dhamira ya Muafaka.  Mbaya zaidi ni kwamba viongozi wa CUF wanasisitiza kwamba hawasahau kwa kauli yao ya kilaghai kwamba “wanasamehe lakini hawasahau”.  Huo ni uvunjaji wa wazi wazi na wa makusudi wa Muafaka ambao unatutaka tusahau.

 

Kipengele kingine cha Muafaka ambacho kwa maoni yangu naona kinakiukwa sana na CUF ni ibara ndogo ya 1(i) ambayo inasema:

 

“Vyama vya siasa kuheshimu Katiba na Sheria za nchi na kuepuka kutumia lugha zinazochochea chuki baina ya vyama vya siasa, ukabila, uhasama na kutovumiliana”.

 

CUF wanaonekana kushindwa kabisa kuepuka kutumia lugha hizo.

 

Hayo ya Muafaka niyaachie hapo, lakini nataka umma wa Watanzania uelewe kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haitoruhusu kisingizio chochote kutumiwa na wanasiasa wenye kiu ya damu ya Watanzania kuvuruga amani na kuhatarisha usalama wa Watanzania.

 

Serikali hii na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar ziko madarakani kihalali kwa ridhaa ya wananchi kwa mujibu wa sheria za nchi.  SMT iko madarakani baada ya Rais Benjamin Mkapa  kuzoa kura 5,863,201 sawa na asilimia 71.7 ya kura halali zilizopigwa, dhidi ya kura 1,329,077 tu za Lupumba sawa na aslimia 16.3.  SMZ iko madarakani baada ya Rais Amani Abeid Karume kupata kura 248,095 sawa na aslimia 67 ya kura halali zilizopigwa dhidi ya 122,000 tu za Seif Sharif sawa na aslimia 33.  Serikali hizi zina heshima kubwa ndani na nje ya Tanzania.

 

Napenda viongozi wa CUF na wanasiasa wenzangu wengine wote waelewe kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haina unyonge wa aina yo yote na inaendesha shughuli zake kifua mbele.  Haiwezi kutikiswa na vitisho vya wanasiasa walioishiwa sera.

 

Wale wanaotayarishwa kupambana na Jeshi la Polisi eti kwa sababu ni dogo wasidanganyike.  Jeshi letu la Polisi lina uwezo wa kukabiliana na hali yoyote.  Ni dogo lakini lenye utaalamu wa kutosha na ari ya juu kabisa katika kutekeleza majukumu yake ya kulinda usalama wa raia kwa kutumia sheria za nchi.  Napenda kuchukua fursa hii kuwatahadharisha wanasiasa wasiliingize Jeshi la Polisi katika malumbano ya kisiasa.  Kazi ya Jeshi hilo si siasa bali ni kupambana na wahalifu.  Na katika jukumu hilo, Polisi watamwandama mhalifu yo yote kwa uhalifu wake bila ya kujali itikadi yake ya kisiasa, kabila, rangi au kitu kingine chochote.  Kwa hivyo, wanasiasa wanaotangaza mapambano na Polisi wasifikiri kuwa siasa itakuwa kinga kwao.

 

Lakini pia viongozi wa CUF watakuwa wanajidanganya na kudanganya wengine kama wataishia kutazama Jeshi la Polisi peke yake na kuisahau nguvu ya umma iliyo nyuma ya Serikali walioichagua.  Kama wanatoa mifano ya nchi ambako nguvu ya umma ilikuwa dhidi ya Serikali, wajue kwamba hapa Tanzania nguvu ya umma iko upande wa Serikali.  Na kwa bahati nzuri, kila kukicha nguvu hiyo inaongezeka kama matokeo ya uchaguzi mdogo wa madiwani wa hivi karibuni yanavyodhihirisha.

 

Nawaomba wananchi wawe watulivu.  Serikali itaendelea kutumia sheria, hekima na busara kuziviza shari zinazoandaliwa na wanasiasa wenye hulka za kiharamia.  Lakini pia nawahakikishia kwamba kama shari itazuka, Serikali inao uwezo kamili wa kuikabili na kuizima.  Lakini Tanzania ya shari na vurugu siyo tunayojitahidi kuijenga sisi wa Serikali ya CCM.

 

Kama Tanzania ya shari na vurugu ndiyo ndoto ya viongozi wa CUF na wanasiasa wengine, basi wakubali pia kwamba ndiyo inayowaponza na kuwagharimu kwa kunyimwa kura kwani Watanzania walio wengi siyo wanayoitaka.  Vinginevyo wanasiasa hao wamekwishajua kwamba hawana nafasi ya kushinda uchaguzi, kwa hivyo kama kawaida yao, wanaanza mapema kutengeneza visingizio vya kukataa matokeo wakati huo tukielekea Uchaguzi Mkuu wa 2005.

 

Kama hoja ya kauli za uchochezi zinazotolewa na wanasiasa ni kutaka uchaguzi mkuu wa 2005 usivurugwe, basi hiyo pia ndiyo dhamiri ya dhati ya Serikali.  Napenda kuwahakikishia wanasiasa hao na wananchi kwa jumla kwamba haitoruhusu mtu au kikundi chochote cha watu kuvuruga uchaguzi mkuu kwa kisingizio chochote kile.  Kwa hivyo kama hiyo ndiyo hofu ya kweli na kama wao wenyewe hawana agenda ya kuvuruga uchaguzi, basi nawasihi wanasiasa husika waondokane na hofu hiyo na badala yake wazungumzie mambo ya kuwaletea matumaini Watanzania badala ya kuhubiri maapizo ya kuwaangamiza katika vurugu na hivyo kuwakatisha tamaa.

 

Napenda kuchukua fursa hii kuwaasa wafuasi wa CUF na wananchi wengine kukataa kuswagiwa kwenye matatizo ya ulema, uzuka na mengine kwani wakipata matatizo hayo, viongozi wao hawatowasaidia bali wataielekea Serikali hii hii kwa misaada.

 

Napenda kumalizia kwa kuwaarifu wananchi kwamba kauli za uchochezi za viongozi wa CUF zinachunguzwa na Polisi kwa lengo la kuchukua hatua zipasavyo za kisheria.