MAHOJIANO YA RADIO UHURU NA KATIBU WA ITIKADI NA UENEZI WA
CCM MHE. OMAR R. MAPURI TAREHE 10 NOVEMBA, 2005
Swali: Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar ulifanyika tarehe
30 Oktoba, 2005 na CCM imejipatia ushindi mnono kwa Urais, Ujumbe wa Baraza la
Wawakilishi na Udiwani. Unajisikiaje
kama Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Taifa?
Jibu: Najisikia mwenye furaha kubwa sana kwani Wazanzibari
wamezizima ngebe za CUF. Aidha, katika
CCM, ushindi huo tuliutarajia na Mwenyezi Mungu ametuthibitishia matarajio yetu
hayo. Napenda kuchukua fursa hii
kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Rais Amani Abeid Karume ambaye pia ni Makamu
Mwenyekiti wa CCM (Zanzibar) kwa ushindi wa asilimia 53.2 alioupata ambao kwa
mazingira ya siasa za Zanzibar, ni mkubwa wa kishindo. Nawapongeza pia Wawakilishi na Madiwani
walioshinda kwa tiketi ya CCM.
Swali: Ndugu Mapuri umesema kwamba CCM mlikuwa
mnautarajia ushindi huo. Ni kitu gani
kilikupeni matumaini hayo.
Jibu: Ni mambo mengi yaliyotupa matumaini ya ushindi, lakini
nitataja mawili tu ambayo ndiyo ya msingi.
Kwanza, ni utekelezaji uliofanikiwa sana wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya
mwaka 2000 uliofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi
mahiri wa Mheshimiwa Rais Karume.
Maendeleo makubwa yamepatikana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita
Unguja na Pemba kutokana na utekelezaji huo wa Ilani katika nyanja za uchumi,
miundombinu, huduma za jamii na kadhalika.
Pamoja na kwamba Wazanzibari wengi hupiga kura kwa misimamo ya
ukereketwa wa vyama kama nitakavyofafanua baadaye, tuliamini kwamba wapo pia
wasiokuwa wachache ambao wangepiga kura kwa kuzingatia maendeleo yaliyopatikana
katika kipindi hicho. Jambo la pili
kubwa lililotupa uhakika wa kushinda ni zingatio la historia ya siasa za
ushindani Zanzibar. Katika chaguzi
karibu zote za kutafuta uhuru katika miaka ya 1950 na 1960, chama cha
Afro-Shirazi kilikuwa kikipata kura nyingi zaidi kuliko za chama cha Hizbu na
mshirika wake ZPPP kwa pamoja, hata pale kilipozidiwa idadi ya viti. Mfano, ni uchaguzi wa mwisho kabla ya Mapinduzi
uliofanyika mwaka 1963. Ingawa
Afro-Shirazi Party ilipata viti 13 tu vikilinganishwa na 18 vya Hizbu na ZPPP,
lakini ilipata asilimia 54.2 ya kura halali (au 53.1% ya kura zote
zilizopigwa). Hapa njama za kuinyima
ushindi Afro-Shirazi Party kwa kutumia mbinu ya ukataji wa majimbo
inadhihirika. Maeneo yaliyokuwa ngome
za Afro-Shirazi yalipatiwa majimbo machache kiidadi lakini makubwa kwa idadi ya
watu lakini yale yaliyokuwa ngome za Hizbu na ZPPP yalipatiwa majimbo mengi
lakini madogo madogo. Halafu ikawekwa
sheria kwamba anayepata majimbo mengi ndiye mshindi. Haya ni miongoni mwa mazingira yaliyoifanya Afro-Shirazi inyimwe
haki ya kuunda Serikali pamoja na kuwa ndiyo iliyokuwa na watu wengi
zaidi. Hii ndiyo maana ule uhuru wa
Zanzibar wa 1963 uliokabidhiwa kwa vyama vya wachache waliokuwa vibaraka wa
Sultani tunauita kule Zanzibar kuwa wa bandia.
Na hiyo ndiyo miongoni mwa sababu kuu zilizohalalisha Mapinduzi matukufu
ya 1964. Sasa nikirudi kwenye hoja
yangu ya kwa nini tulikuwa na uhakika wa kushinda; ni kwamba baada ya chama cha
CUF kuundwa mwaka 1992 kufuatia kuruhusiwa tena kwa mfumo wa vyama vingi baada
ya miaka 28 ya mfumo wa chama kimoja, wale waliokuwa wafuasi wa vyama vya
zamani vya Hizbu na ZPPP waliona (kwa kuambiwa na waanzilishi wa CUF) kwamba
vyama vyao vilivyokuwa vimepigwa marufuku vimerudi kwa jina la CUF. Afro-Shirazi nao wakaganda kwa CCM. Pamoja na kwamba ipo mifano michache ya
Hizbu na ZPPP wa zamani kuingia CCM na Afro-Shirazi wa zamani kujiunga na CUF,
mwelekeo wa jumla unabaki kwa kiasi kikubwa kuwa ule ule wa Hizbu/ZPPP kuwa CUF
na Afro-Shirazi kuwa CCM. Na wazee wa
pande zote mbili hufanya bidii kubwa kuwarithisha watoto wao mitazamo
hiyo. Sasa kwa vile Afro-Shirazi
walikuwa wengi zaidi, tuliamini kwamba CCM ni wengi zaidi pia. Na matokeo ya uchaguzi wa mwaka huu ya CCM
kupitia Rais Karume kupata ushindi wa asilimia 53.2 yamethibitisha usahihi wa
utabiri wetu.
Swali: Ndugu Katibu wa Itikadi na Uenezi, wakati
nyinyi CCM mnafurahia ushindi wenu, Seif Sharrif Hamad alijitangazia ushindi wa
asilimia 61 usiku wa tarehe 30 Oktoba, 2005 na kusababisha maandamano ya
kusherehekea ushindi huo yaliyofanywa na baadhi ya wafuasi wa CUF mjini Dar es
Salaam tarehe 31 Oktoba, 2005. Aidha,
baada ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar kutangaza rasmi matokeo ya Uchaguzi Mkuu
wa Zanzibar vilionekana vipeperushi mjini Dar es Salaam vikionyesha kwamba Seif
Sharrif Hamad alipata ushindi wa asilimia 50.63 na Ndugu Karume alipata
asilimia 49.37 tu. Unawaambia nini
wananchi kuhusu madai haya?
Jibu: Madai hayo yote ni upuuzi na ubabaishaji mtupu. Kwanza kabisa, kwa mujibu wa sheria za nchi,
chombo pekee chenye mamlaka ya kumtangaza mshindi wa uchaguzi wa Rais,
Wawakilishi na Madiwani Zanzibar ni Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar. Kwa hivyo kitendo cha Maalim Seif kutangaza
matokeo yake na kujitangaza mshindi kilikuwa cha kukiuka sheria na hivyo
kilikuwa haramu. Kwa hivyo na matokeo
yenyewe aliyoyatangaza yalikuwa haramu.
Pia ni dhahiri kabisa matokeo hayo hayakuwa sahihi. Tukianza na yale matokeo ya awali
aliyoyatangaza Maalim Seif tarehe 30 Oktoba, 2005. Matokeo hayo yalitangazwa wakati zoezi la kuhesabu kura
likiendelea. La kujiuliza hapa ni Maalim Seif aliyapata wapi matokeo hayo kama
si kuyabuni tu? Na alifanya hivyo kwa
makusudi kujenga mazingira ya kukataa matokeo sahihi na halali baada ya kutangazwa rasmi na Tume ya Uchaguzi kama
yangeonyesha kuwa ameshindwa, kwa madai ya kubuni kuwa ameibiwa kura au
amenyang’anywa ushindi. Aidha, yalikuwa
pia maandalizi ya vurugu kwani alijua kuwa akishawajenga watu wake na hisia za
ushindi wasingekubali matokeo ambayo yangeonyesha kuwa wameshindwa, na hivyo,
kujiingiza katika vurugu. Na hivyo
ndivyo ilivyotokea. Huu umekuwa mtindo
wa kawaida wa Maalim Seif ambao aliutumia mwaka 1995 na hata 2000.
Kwa
yale matokeo waliyoyatoa kwa
vipeperushi baada ya matokeo rasmi kutangazwa na Tume, CUF walidhihirisha
kutapatapa kwao pale waliposahau kuwa safari ni wagombea sita ndio walioshiriki
uchaguzi wa Rais, na siyo mawili tu.
Kwa mujibu wa matokeo hayo, Maalim Seif eti alipata ushindi wa asilimia
50.63 na Rais Karume eti asilimia 49.37.
Ukijumlisha tarakimu hizi unatapata asilimia 100. Inafaa CUF waulizwe, je wale wagombea
wengine wanne wa vyama vya Jahari Asilia, DP, NRA na SAU hawakupata hata kura
moja? Inadhihirisha wazi wazi kuwa
takwimu zote hizo ni za kubuni. Zaidi
ya hivyo, kitendo chenyewe cha
kutangaza matokeo mawili yaliyo tofauti
kinadhihirisha kutapatapa kwa Maalim Seif na CUF yake na kinawashushia hadhi na
kuwa kuwafanya wasiaminike.
Swali: Ndugu Mapuri uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa
mwaka huu umeshuhudiwa na waangalizi wengi mno wa kimataifa na wa ndani
isivyokuwa kawaida. Ulipoahirishwa
uchaguzi mkuu wa Jamhuri ya Muungano, hata waangalizi wa kimataifa waliokuwa awali wamepangiwa maeneo ya Bara
walikwenda Zanzibar. Aidha, tofauti na
ilivyokuwa katika chaguzi mbili zilizopita
za miaka ya 1995 na 2000, safari hii vikundi vingi vya waangalizi
vimeutangaza uchaguzi wa mwaka huu kuwa ulikuwa huru na wa haki. Hata hivyo, vipo vikundi vichache ambavyo bado
vinasita kutamka kama uchaguzi ulikuwa huru na wa haki mpaka mamlaka husika
zifanye uchunguzi juu ya dosari
vinavyodai kuziona vikundi hivyo ili kuondoa shaka. Nini tathmini na maoni yako kuhusu hali hii?
Jibu: Kimsingi mtazamo wangu ni kwamba kwa uchaguzi wetu kuwa huru
na wa haki, si lazima upate baraka za waangalizi wa kimataifa au wa ndani. Mimi niliziona chaguzi za 1995 na 2000 kuwa
huru na za haki pamoja na kwamba waangalizi wengi walikuwa na mawazo tofauti. Hata hivyo, lazima nikiri kwamba nimefarijika
sana kuwa wengi wa waangalizi waliotazama uchaguzi wetu mwaka huu wameuona kuwa
huru na wa haki. Jambo moja
limenibainikia. Nalo ni kwamba makundi
makubwa ya waangalizi yaliyokuwa na mitandao mipana iliyoenea nchi nzima ndiyo
yaliyotoa tathmini ya kuaminika ya upeo wa nchi nzima. Makundi hayo aghlabu ndiyo yaliyouona
uchaguzi wa mwaka huu kwa ujumla wake kuwa ulikuwa mzuri, huru na wa haki,
pamoja na kuwapo kwa dosari ndogo ndogo za hapa na pale. Mifano ya makundi kama hayo ya waangalizi ni
yale ya SADC, Jumuiya ya Madola, TEMCO, EISA, Jumuiya ya Afrika Mashariki,
Umoja wa Nchi Huru za Afrika na kundi la waangalizi lililowakilisha makanisa
mbalimbali ya Afrika. Kwa upande
mwingine, ni vikundi vidogo vidogo vya waangalizi vilivyokuwa na mitandao finyu
ndivyo vinavyoonekana kuwa na shaka juu ya hadhi ya uchaguzi huo kuwa ulikuwa
huru na wa haki. Hii inaelekea ni kwa
sababu tathmini za vikundi kama hivyo zilijengwa juu ya msingi wa viliyoyaona
katika eneo dogo tu, hususani la Mji Mkongwe na kuzifanya tathmini hizo
zionekane kana kwamba ni za nchi nzima.
Lakini Mji Mkongwe ni jimbo moja tu kati ya majimbo 50 yaliyofanya
uchaguzi. Aidha, hata katika hilo jimbo
la Mji Mkongwe, ni vituo vitatu tu ndivyo viliyvoripotiwa sana kukumbwa na hizo
dosari zinazotajwa katika ripoti za waangalizi na kupigiwa chapuo na vyombo vya
habari hasa vile vya nje. Vituo hivyo
ni Kiwanda cha Madawa, Forodhani na Bwawani ambavyo ni kati ya jumla ya vituo
1,617 vilivyokuwapo nchi nzima. Kwa
hivyo si sahihi, si haki na ni upotoshaji mkubwa kuzikuza dosari ndogo ndogo
zilizoonekana katika eneo dogo sana kama hilo na kuzifanya zionekane kuwa ni za
nchi nzima. Lakini naamini pia kwamba
miongoni mwa hao waangalizi wanaosita kutamka kuwa uchaguzi ulikuwa huru na wa
haki, wapo waliokuja na mitazamo ya jumla kwamba uchaguzi hauwezi kuwa huru na
wa haki Barani Afrika kama haukiondoi madarakani chama tawala hasa kama ndicho
kilichopigania uhuru na kuung’oa ukoloni.
Swali: Ndugu Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM
miongoni mwa dosari zilizotajwa sana katika ripoti za waangalizi na kutangazwa
sana na vyombo vya habari hasa vya nje, ni kwamba ulinzi ulikuwa mkali mno
kiasi cha kuwatisha wapiga kura. Wewe
mwenyewe ulikuwako Zanzibar siku ya uchaguzi.
Hili unalielezea vipi?
Jibu: Mimi Ndugu Mtangazaji naliona dai hili la watu kutishika na
ulinzi uliokuwapo kuwa ni upuuzi mtupu.
Kama wapiga kura wangetishika kweli wasingejitokeza kwa wingi wa kiwango
cha zaidi ya asilimia 90 ambacho ni adimu kufikiwa hasa katika hizo nchi za
Magharibi zinazojifanya kuwa walimu wa demokrasia. Ukweli ni kwamba ulinzi mkali uliokuwepo ambao ulikwishaahidiwa
kabla na Serikali, ulikuwa faraja kwa wapiga kura waliokuwa wametishwa sana na
viongozi na wafuasi wa CUF wakati wa kampeni.
Ni ulinzi huo ambao uliwahakikishia usalama wao ndio uliowapa imani
wapiga kura kujitokeza kwa wingi kwenda kupiga kura kwa uhuru. Ulinzi ulioonekana kuwa mkali sana katika
eneo la Mji Mkongwe mnamo nyakati za jioni, ulikuwa umeimarishwa baada ya
kuongezeka kwa matukio ya kupigwa watu (hususan waliodhaniwa kuwa ni wana CCM)
na kuondolewa kwenye mistari ya kwenda kupiga kura. Kama matukio hayo yangeachiwa kuendelea, ilikuwapo hatari ya
uchaguzi kuvurugika kweli katika jimbo hilo.
Swali: Dosari nyingine iliyotajwa na Seif Sharrif
Hamad ni kuwa wapiga kura zaidi ya 80,000 walizuiliwa kupiga kura kutokana na
kutoonekana majina yao kwenye dafari la wapiga kura. Hii nayo unaielezea vipi?
Jibu: Hili nalo dhahiri ni dai la kubuni. Kwa bahati nzuri hata Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la CUF
kupitia Tamko lake la tarehe 5 Novemba, 2005 lilimsahihisha Maalim Seif kwa
kiasi fulani. Katika Tamko hilo, CUF
inadai kuwa ni watu 47,000 ndio eti waliozuiliwa kupiga kura. Lakini ukweli kwa mujibu wa takwimu rasmi za
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni kwamba kati ya watu 507,225 waliothibitishwa
kuwa wapiga kura halali baada ya uhakiki wa daftari la kudumu la wapiga kura,
460,581 sawa na asilimia 90.8 walipiga kura zao. Ni watu 46,644 tu (au 47,000 kama walivyotajwa na CUF katika
Tamko lao) ndio ambao hawakupiga kura.
Lakini hata hao, haiwezekani kuwa wote hawakupiga kura kwa sababu ya kuzuiliwa
kutokana na kutoonekana majina yao katika daftari au kuwa wote ni wafuasi wa
CUF. Wapo waliokwishafariki dunia, wapo
waliokuwa safarini nje ya nchi na wapo wengi wengine waliokuwa na dharura mbali
mbali zilizowafanya washindwe kwenda vituoni kupiga kura. Hakuna uchaguzi
popote duniani ambao wote waliojiandikisha wanapiga kura. Uhakika ni kwamba Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar ilikuwa imetoa taarifa mapema kabla ya siku ya uchaguzi kwamba watu
2,007 waliondolewa katika daftari wakati wa uhakiki wa mwisho kutokana na
kubainika kuwa walijiandikisha zaidi ya mara moja. Naamini ni miongoni mwa hawa ndio waliokwenda vituoni na kugundua
kuwa majina yao hayakuwamo kwenye daftari.
Siyo watu 80,000 aliodai Maalim Seif.
Watu 80,000 ni wengi mno kwa mazingira ya Zanzibar kiasi kwamba kama
wote wangekwenda vituoni na majina yasionekane, kungekuwa na fadhaa kubwa
vituoni ambayo ingeathiri zoezi lote la upigaji kura.
Swali: Kuna madai pia kwamba watu wengi wakiwemo maaskari walipiga
kura zaidi ya mara moja. Unasemaje
kuhusu hili?
Jibu: Hata dai hilo nina matatizo nalo kwani maelezo yote
kuhusiana nalo hayajathibitishwa angalau hata kwa mfano mmoja halisi wa mtu
aliyekamatwa au angalau wa jitihada za kusaidia vyombo vya dola vimkamate na
kumfikisha mbele ya sheria. Dai hili si
cho chote zaidi ya uvumi na simulizi za kufikirika.
Swali: Ndugu Mapuri
tupe maoni yako kuhusu madai mengine ya CUF na baadhi ya waangalizi kwamba fomu
za matokeo hazikupelekwa katika baadhi ya vituo na kwamba matokeo
hayakubandikwa vituoni.
Jibu: Swali hili linapaswa kujibiwa na Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar. Lakini niliwahi kumsikia
Mwenyekiti wa Tume hiyo, Mzee Masauni Yussuf akihojiwa na BBC ambapo
alizikanusha tuhuma zote hizo. Lakini
mimi nawastaajabu hawa CUF. Upande
mmoja wanasema hawakupewa fomu za matokeo lakini wakati huo huo wanajitangaza
washindi. Huu tuuiteje kama si unafiki?
Swali: Zimeelezewa pia fujo nyingi kutokea katika
maeneo ya Darajani, Mtendeni na maeneo kadha ya Kaskazini Pemba ambako wameuawa
watu wawili – mmoja raia na mwingine askari.
Kwa maoni yako huoni kama fujo hizo ziliingilia zoezi la uchaguzi?
Jibu: Ni kweli zilitokea vurugu za hapa na pale katika maeneo hayo
zilizosababishwa na wafuasi wa CUF ama wakishangilia ushindi hewa au wakipinga
matokeo yaliyotangazwa na Tume.
Navipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuzidhibiti fujo hizo kabla
ya kuleta madhara makubwa zaidi. Lakini
kwa kujibu swali lako, fujo na vurugu zote hizo zilitokea baada ya zoezi lote
la uchaguzi kukamilika. Kwa hivyo
hazikuathiri kwa aina yo yote mwenendo wa zoezi la uchaguzi.
Swali: Ndugu Katibu wa Itikadi na Uenezi huoni kama
wingi wa dosari zilizotajwa unaweza kuwa umeathiri uchaguzi mzima na hivyo hata
matokeo yake?
Jibu: Katika suala hili, wingi si hoja. Hoja ni usahihi na uzito wa dosari zenyewe. Lakini kama nilivyojibu kuhusu dosari moja
moja, mimi naziona nyingi ya dosari zinazotajwa kuwa si za kweli na chache
zenye ukweli fulani hazina msingi wala uzito wo wote wa kuathiri matokeo ya
uchaguzi. Katika hatua hii ningependa
kuelezea masikitiko yangu kwa kundi la waangalizi la NDI la Marekani kusita
kutamka kuwa uchaguzi wa Zanzibar ulikuwa huru na wa haki. Nasikitika kwa sababu wote tunajua
yaliyotokea katika uchaguzi mkuu wa Marekani wa mwaka 2000, hasa katika Jimbo
la Florida. Uchaguzi huo ulikumbwa na
madosari makubwa na ya msingi ambapo hata mashine za kuhesabia kura zilishindwa
na ikabidi itumike mikono. Tulisikia
mabunda ya kura zilizokuwa zimefichwa vyooni.
Mimi naamini kwamba dosari zilizoukumba uchaguzi huo katika Jimbo la
Florida zilikuwa kubwa zaidi kuliko za Mji Mkongwe. Isitoshe, matokeo ya Florida yalikuwa na taathira kubwa kwa
matokeo ya mwisho ya uchaguzi mzima wa Marekani kwani hatimaye ndiyo yaliyoamua
mshindi. Lakini yale ya Mji Mkongwe
hayakuwa na taathira ya kiasi hicho kwani hata kama kura zote halali 9,485
zilizopigwa katika jimbo hilo angepewa Maalim Seif, bado matokeo yangebaki yale
yale ya Rais Karume kuwa mshindi. Kama
NDI waliuona uchaguzi wa Marekani kuwa huru na wa haki pamoja na mazonge yote
ya Florida, iweje wauone wetu si huru na wa haki kama hawana agenda ya siri? Nimesoma makala kwenye gazeti la Uhuru la
leo tarehe 10 Novemba, 2005 inayoonyesha kwamba hata uchaguzi wa 2004 wa
Marekani ulikumbwa na dosari nyingi, lakini hatusikii lugha ya kuutilia shaka.
Swali: Ndugu Mapuri nini mtazamo wako kuhusu uamuzi wa CUF kuyakataa
matokeo ya Urais lakini kuyakubali yale ya Uwakilishi na Udiwani?
Jibu: Ni dalili ya kuchanganyikiwa. Niliwahi kuwasikia hata baadhi ya wafuasi wa CUF wakisema kuwa
hawawaelewi viongozi wao kwa uamuzi huo.
Hata mimi siwaelewi. Chaguzi za Urais, Uwakilishi na Udiwani zilifanywa
wakati mmoja, katika mazingira yale yale na wapiga kura walioshiriki ni wale
wale. Kama kweli wanaamini kuwa
uchaguzi mzima ulivurugika, vipi iwe kwa Urais tu? Hususani tutazame jimbo la Mji Mkongwe ambalo ndilo linasemwa
sana kukumbwa na dosari. Kama dosari
hizo hazikuathiri matokeo ya Uwakilishi, iweje ziathiri ya Urais? Mimi ningewaelewa kama wangeyakataa kwanza
matokeo ya Uwakilishi na Udiwani kabla ya kuyakataa ya Urais. Kwa sababu hawakufanya hivyo, ni dhahiri
kwamba wameyakataa matokeo ya Urais kwa shinikizo tu la Maalim Seif ambaye kwake
hulka ya kukataa kushindwa imekwishaota mizizi. Napenda kuwashauri CUF waanze kukomaa kisiasa. Wapone uchungu wa kushindwa na wautazame
upya uamuzi wao wa kuyakataa matokeo ya uchaguzi wa Urais kwa manufaa ya Taifa. Napenda kuwakumbusha kwamba katika Muafaka,
walipewa karibu kila kitu walichokitaka.
Mifano ni daftari la kudumu la wapiga kura, kushirikishwa katika uteuzi
wa wajumbe wa Tume ya Uchaguzi, na kushirikishwa kupitia Tume ya Muafaka katika
marekebisho ya Katiba, Sheria ya Uchaguzi na sheria nyingine mbali mbali. Watanzania wamechoshwa na hulka ya kukataa
kushindwa.
Swali: Mwisho, uchaguzi wa Zanzibar umekwisha na
washindi wamepatikana ambao ni CCM.
Nini matarajio yako na ya CCM
kuhusu uchaguzi mkuu ujao wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wabunge
na Madiwani wa Bara?
Jibu: Matarajio yetu ni ushindi tu, tena mkubwa sana wa
kishindo. Ushindi wetu wa Zanzibar
umezidi kutufyagilia njia yetu ya ushindi katika uchaguzi utakaofanyika tarehe
14 Disemba, 2005. Naamini Watanzania
hawatopenda kuharibu kura zao kwa kuwapigia wapinzani ambao ni hakika
watashindwa vibaya sana. Kwa nini
ujiunge na kambi ya washindwa wakati ya washindi ipo?