MKUTANO MKUU WA CCM 2006

HOTUBA YA MWENYEKITI YA KUNG’ATUKA NA KUAGA CHIMWAGA 25 JUNI, 2006

 

Waheshimiwa Makamu wa Mwenyekiti,

Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tz,

Mheshimiwa Mwenyekiti na Rais Mstaafu,

Mheshimiwa Katibu Mkuu,

Mheshimiwa Katibu Mkuu na Waziri Mkuu Mstaafu,

Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati Kuu,

Waheshimiwa Wajumbe wa Halmashauri Kuu,

Waheshimiwa Wajumbe wa Mkutano Mkuu,

Waheshimiwa Waasisi na Wazee wa Chama,

Waheshimiwa Wageni Waalikwa,

Mabibi na Mabwana.

 

Salaam Aleikum!

 

Awali ya yote napenda kujumuika nanyi kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia afya njema na kutukutanisha hapa leo hii. Binafsi sina budi nitoe shukurani nyingi sana kwa wingi wa fadhila na upendo wake ambao umeniwezesha kuhitimisha miaka kumi ya kuongoza dola na sasa Chama Cha Mapinduzi, kwa amani na usalama. Mwenyezi Mungu atuongezee baraka zake, abariki mkutano wetu, na aendelee kuibariki nchi yetu, Amin.

 

Kwa Nini Nang’atuka

Ndugu Wajumbe:

            Huu ni Mkutano Mkuu wa kwanza tangu nihitimishe kazi mliyonipa mwaka 1995 ya kuongoza nchi yetu katika mkutano kama huo.  Bado nakumbuka sana siku ile hapa Chimwaga nilipochaguliwa kuwa mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi. Leo narudia shukrani zangu kwa Chama changu kwa imani kubwa mliyonipa, na ushirikiano mkubwa mlionipa tangu wakati wa kampeni za 1995 na zile za 2000. Aidha narudia shukrani zangu kwa wote waliojitokeza kugombea Urais mwaka 1995, hususan wale watatu tuliofika hapa Chimwaga kwenye fainali ya mbio za kutafuta kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi. Ahsante sana, tena sana, Mheshimiwa Cleopa David Msuya na Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

 Wale mliokuwa hapa mwaka 1995 mtakumbuka mazingira ya uchaguzi ule. Lakini mtakumbuka pia hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Kikwete siku ile. Ilihitaji ujasiri mkubwa kutoa hotuba kama ile. Ilihitaji uwezo mkubwa wa kudhibiti hisia za kibinadamu. Ilihitaji busara na upendo mkubwa kwa Chama. Ilihitaji uwezo mkubwa wa kufikiri na kushawishi waliokuwa wakimuunga mkono wakubali matokeo ya kura na waniunge mkono. Na nyote ni mashahidi kuwa alitimiza ahadi zake alizozitoa siku ile hapa Chimwaga. Zote hizo ni sifa muhimu za kiongozi, ambazo nyote mtakuwa tayari mmeziona kwenye uongozi wake wa Taifa katika miezi sita iliyopita. Kwa hakika hatukukosea. Narudia. Nani kama CCM?

            Naona fahari kubwa zaidi kumwachia Rais Kikwete uongozi wa Taifa. Sina wasiwasi hata kidogo. Na leo naona fahari kubwa zaidi na sina wasiwasi kumwachia uongozi wa Chama Cha Mapinduzi ninapowaomba mridhie mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya Taifa.

 

Ndugu Wajumbe:

            Chama Cha Mapinduzi kina utaratibu mzuri wa kupishana uongozi wa Serikali na uongozi wa Chama. Utaratibu huu pia unamwezesha Rais anayeondoka madarakani kuendelea kuwa Mwenyekiti wa Chama kwa miaka miwili baada ya kuacha Urais. Utaratibu huu unampa nafasi Rais mpya kuunda Serikali na kuweka vipaumbele vyake bila wakati huo huo kubeba mzigo wa Uenyekiti wa Chama.

 Lakini ni vema  mapema iwezekanavyo, akishaunda Serikali na kuweka vipaumbele vyake, tumkabidhi pia Uenyekiti wa Chama ili mikono yake isifungwe na kasi yake isipunguzwe, anapotekeleza kazi za Serikali kwa niaba ya Chama.

Mimi ninaridhika kabisa kuwa wakati wa kumuachia Rais Jakaya Mrisho Kikwete Uenyekiti wa Chama sasa umefika. Nimeshauriana naye. Yuko tayari, kama ilivyokuwa maisha yake yote, kukitumikia Chama. Kwa uzoefu wake na uwezo wake mkubwa sina shaka ametosha kabisa kuwa Mwenyekiti wetu. Naomba Ndugu Wajumbe leo mkubali kwa kauli moja ya kishindo mapendekezo kwenu ya Halmashauri Kuu ya Taifa kumchagua Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete awe Mwenyekiti wetu.

            Nawashukuru sana wenzangu kwenye Kamati Kuu na kwenye Halmashauri ya Taifa kwa kunikubalia ning'atuke Uenyekiti kabla ya muda wangu kikatiba kwisha.  Si wote walinikubalia kwa urahisi, lakini baada ya kusikia hoja zangu na rai yangu wote kwa kauli moja walikubali. Nataka nanyi mjue sababu nyingine, zaidi ya hizi nilizozitaja hivi punde, zilizonifanya nifikie uamuzi huu wa kung’atuka.

 

Ndugu Wajumbe:

            Ninazo sababu tano za nyongeza kwa nini nimefikia uamuzi huu ambazo ni vema ninyi, wanachama wenzetu, na wananchi kwa ujumla, wakazijua:

 

  1. Ninaamini kuwa ni vema yule tunayemkabidhi kazi ya kuongoza utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi awe huyo huyo ndiye kiongozi mkuu wa Chama. Mikono yake isifungwe, na akija kutoa taarifa na kuwajibika kwa kazi hiyo awe na madaraka kamili. Tumejaribu hivyo wakati wangu, na tukaona ni jambo jema. Hatuna sababu ya kufanya vinginevyo sasa.

 

  1. Nyote mlisikia hotuba nzuri sana ya ufunguzi wa Bunge aliyoitoa Rais wetu. Anayo mapendekezo mahsusi ya kushughulikia matatizo ya kisiasa nchini, na mahusiano baina ya Vyama vya Siasa. Mapendekezo hayo mazuri yanahitaji mawasiliano na mashauriano baina ya viongozi wa vyama vya kisiasa. Ni vema Rais akafanya hivyo akiwa amevaa kofia ya Mwenyekiti wa Chama.

 

  1. Wakati wangu tumefanya kazi naye na viongozi wengine wa Afrika Mashariki kurejesha Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mwelekeo sasa ni kwenye kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki. Na tumekubaliana kuwa hatua tuliyofikia inahitaji kuwashirikisha wananchi wa kila nchi ya Afrika Mashariki. Hiyo ni kazi ya kisiasa ambayo ni vema ikafanywa na Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama.

 

  1. Nchi yetu bado ina matatizo makubwa ya kimaendeleo. Hatua inayofuata baada ya mageuzi ya uchumi aliyoyaanzisha Mzee Mwinyi, nikayaendeleza mimi, ni kwa Awamu ya Nne kusaidia kuyafanya mageuzi hayo yawe chachu ya kubadili maisha ya wananchi wengi zaidi. Hivyo ni sahihi kabisa kuwa tuliyemkabidhi Ilani ya Uchaguzi inayodai kutoka Serikalini Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya, apewe gea nyingine ya kuhakikisha kuwa kweli kasi hiyo mpya inafikiwa.

 

5.      Na mwisho, lakini muhimu sana, ni kuwa tangu nimeacha uongozi wa Serikali nimepewa majukumu mengi sana ya kimataifa yanayonichukulia muda mwingi sana kiasi kwamba nahisi sitakitendea Chama changu haki nikiendelea kuwa Mwenyekiti hasa kwa kuzingatia kuwa wa kurithi kazi hiyo ya Chama yupo na anazo sifa za kutosha. Kwa wale ambao hamjui, miongoni mwa mambo mengine, mimi ni Mwenyekiti Mwenza wa Mfuko wa Kuboresha Mazingira ya Uwekezaji Barani Afrika. Mimi ni mjumbe wa Tume iliyoundwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Kuhuisha kazi za Umoja huo kwenye maeneo ya maendeleo, haki za binadamu, na mazingira, na tunatakiwa kukamilisha kazi hiyo kabla ya mwezi Septemba mwaka huu. Kwa kuwa wapo walio hodari wa kuzua hisia potofu ni vizuri niweke wazi kuwa ushiriki wangu katika Tume hizi hauna mshahara wala mrahaba!!  Ni kazi ya kujitolea.  Mimi ni mjumbe wa Tume ya Kimataifa kuhusu Uwezeshaji Wanyonge Kisheria, yaani MKURABITA ngazi ya kimataifa. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Umoja wa Mataifa ya kuangalia Hatma ya Shirika la Biashara na Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNCTAD). Mimi ni Mwanachama wa Chama kinachoitwa Club of Madrid ambacho ni Chama kinachowakusanya baadhi ya viongozi wanaoheshimika, waliochaguliwa kidemokrasia na kuondoka madarakani kidemokrasia, walio tayari kutumia uzoefu wao kwa manufaa ya dunia yetu, ambayo kwa kweli ni sifa kwa Chama chetu. Katika mazingira haya naamini nitakitendea Chama changu haki zaidi kwa kumkabidhi Rais wetu Uenyekiti, na ninaomba mridhie iwe hivyo leo.

 

 

 

Ndugu Wajumbe:

            Leo tumekutana tena hapa Chimwaga kuimarisha sifa nzuri na historia ya kutukuka ya Chama Cha Mapinduzi; historia, kwa ridhaa yenu, ya uongozi mithili ya mbio za vijiti, uongozi wa kupishana kwa upendo, si kwa chuki; uongozi wa kupishana kwa bashasha, si kwa kununa; uongozi wa kupishana kwa maelewano si kwa mafarakano; uongozi wa kupishana kwa heshima na taadhima, si kwa mizengwe na nongwa. Wanaongojea na wanaotamani hali iwe tofauti watangoja sana. Tuazimie basi kuwa waendelee kusubiri hivyo daima.

            Juzi juzi hapa nilisoma gazetini makala moja ya mahojiano na Waziri Mkuu mstaafu, Mzee Cleopa David Msuya ambapo, pamoja na mambo mengine, aliwahakikishia wananchi kuwa CCM inaendelea kuwa moja baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2005. Napenda nirejee kauli yake ninapohitimisha Uenyekiti wangu wa Chama. Kwa hakika ningesononeka na kusikitika sana kama ningeacha Uenyekiti wakati Chama kimegawanyika.  Na namshukuru sana kwa kuelezea, kwa uaminifu na haki, mazingira ya kazi na mafanikio ya serikali zote za CCM toka Uhuru.

            Chama Cha Mapinduzi bado ni imara sana, bado ni kimoja. Ni kweli, kama ilivyo kwa vyama vya siasa kote duniani, yanaweza kuwepo mawazo tofauti miongoni mwa viongozi na/au wanachama. Utasikia wapo wenye mrengo wa kulia, wapo wenye mrengo wa kati, na wapo wenye mrengo wa kushoto. Siku hizi wapo pia wenye mrengo wa kushoto kwa kati, na wengine kulia kwa kati. Ni jambo la kawaida.

Hatuwezi, na ni makosa makubwa, kudhani kuwa tutakuwa na Chama au Serikali ambapo watu wote wanafikiri sawa, wanasema sawa na wana maoni sawa kuhusu kila jambo. Hao watakuwa ama hawafikirii, au ni wanafiki wakubwa wanaojipendekeza badala ya kuchangia kwa uwazi kurutubisha sera, mwelekeo na utendaji kwenye Chama. Lakini tusiruhusu tofauti za mawazo na mapendekezo ziwe sababu au chanzo cha Chama kugawanyika. Kuhitilafiana, rukhsa; kugawanyika, marufuku. Na kweli ni wajibu wetu wa kihistoria kuhakikisha mirengo na mawazo tofauti ndani ya Chama inarutubisha mijadala na kupanua upeo wa hoja na misingi ya maamuzi, lakini kamwe haiwi kiini au chanzo cha kugombana au kuchukiana.

            La muhimu pia ni kujenga utayari kila upande wa kujitahidi kuelewa na kuheshimu hoja za upande mwingine. Yatakuwa makosa makubwa kumchukia mwenzako kwa vile tu anayo maoni tofauti nawe. Ndio maana nasema wanaoona tofauti ya maoni miongoni mwetu wasidanganyike wakafikiri huo ni mwanzo wa mpasuko wa CCM. Si  kweli; na wala tusiwape faida hiyo. Wao, pamoja na sisi tukubali hiyo kama ushahidi na kama sehemu muhimu ya demokrasia ndani ya Chama. Lakini sisi  wenye Chama tunao pia wajibu mkubwa wa kuwahakikishia wanachama na wananchi kuwa hatutaruhusu tofauti za maoni zitupeleke katika kudhoofisha Chama. Na Baba wa Taifa alituasa: Bila CCM madhubuti, nchi itayumba. Na wananchi wengi nao wanajua hivyo, na waiangalia CCM kwa makini sana.

 

Chama cha Mapinduzi na Mageuzi ya Kisiasa

Ndugu Wajumbe;

Chama chetu kina viongozi; lakini si Chama cha Viongozi! Chama chetu ni cha Wanachama wake. Wanachama wake ndiyo wahimili wakuu wa CCM. Nachukua fursa hii basi kuwashukuru     wanachama wote wa CCM kwa vile walivyoimarisha Chama chetu na kukifikisha kilele cha kupigiwa mfano katika nchi za SADC. Ndugu wanachama, Asanteni sana.

 

Ndugu Wajumbe,

Ninapong’atuka naamini ni wakati mwafaka vile vile tujikumbushe na kutafakari mnasaba wa Chama chetu ili tuandike vizuri historia yetu na tuimarishe mwelekeo wetu. Chama chetu kiliundwa kiwe na sifa na sura gani? Kiliundwa kiwe Chama cha Ukombozi cha Wakulima na Wafanyakazi. Azimio la Mkutano Mkuu wa Pamoja wa TANU na ASP wa l977 uliounda CCM ulitamka hivi:

 

“Chama tunachokiunda tunataka kiwe chombo madhubuti katika muundo wake na hasa katika fikra zake na vitendo vyake vya kimapinduzi vya kufutilia mbali aina zote za unyonyaji nchini, na kupambana na jaribio lolote lile la mtu kumuonea mtu au shirika au chombo cha nchi kuonea na kudhalilisha wananchi, kudhoofisha uchumi au kuzorotesha maendeleo ya Taifa;

                                                                       

Chama tunachokiunda tunataka kishike barabara hatamu za uongozi wa shughuli zote za umma kwa maslahi ya wafanyakazi na wakulima wa Taifa letu,

 

Chama tunachokiunda tunataka kiwe kiungo kati ya wanamapinduzi wa Tanzania na wanamapinduzi wenzetu kokote waliko.”

 

 Nashukuru kwamba Chama kinaendelea kuwa na hulka hiyo. Wananchi wana Imani na CCM.

 

Ndugu Wajumbe,

Wapo wanaotuhumu kwamba tumewasaliti waasisi wa Chama chetu na kuwa tumekiuka maslahi ya wananchi wetu. Matokeo ya Chaguzi Kuu tatu zilizopita katika mfumo wa vyama  vingi yanawaumbua na kuwaadhiri. Katika chaguzi hizo zote CCM ilipata ushindi mkubwa. Tukumbushane.

Mwaka l995 mgombea Urais kwa tiketi ya CCM alipata ushindi wa 62% ya kura dhidi ya wapinzani watatu wa vyama vingine. Wagombea Ubunge kwa tiketi ya CCM walipata ushindi wa viti 214 dhidi ya 45 vya wapinzani wa vyama vingine. Mwaka 2000 mgombea Urais kwa tiketi ya CCM alipata ushindi wa 72% ya kura dhidi ya wapinzani wa vyama vingine watatu. Wagombea Ubunge kwa tiketi ya CCM walipata ushindi wa viti 258 dhidi ya viti 37 walivyopata wagombea ubunge wa vyama vingine. Mwaka jana, 2005, mgombea Urais kwa tiketi ya CCM alipata ushindi was 82% ya kura dhidi ya wapinzani tisa wa vyama vingine. Wagombea Ubunge nao walipata ushindi wa viti 275 dhidi ya viti 44 walivyopata wagombea ubunge wa vyama vingine!!

            Kadhalika katika Chaguzi za Zanzibar, ule wa mwaka 1995, mgombea Urais kwa tiketi ya CCM alipata ushindi wa 50.24% ya kura, na katika Baraza la wawakilishi wagombea wa CCM walipata viti 26 dhidi ya 24 za wapinzani.  Mwaka wa 2000, mgombea Urais kwa tiketi ya CCM alipata ushindi wa 67% ya kura dhidi ya 33% za mpinzani wake, na katika Baraza wagombea wa CCM walipata viti 34 dhidi ya 16 za wapinzani.  Na mwaka 2005 mgombea wa Urais alipata 53% dhidi ya 47 za wapinzani wake, na katika Baraza, wagombea wa CCM walipata viti 30 dhidi ya 19 za wapinzani.  Huu ni ushindi wa chaguzi tatu mfululizo na wa kujivunia.

            Wananchi wa Tanzania, Wakulima na Wafanyakazi wa Tanzania, si lofa, si mbumbumbu, si wajinga, si bubu. Kwa matokeo haya ya ushindi mkubwa wametamka kwa kishindo imani yao kwa Chama Cha Mapinduzi na Uwezo mkubwa wa Viongozi wa Serikali zake. Wafanyakazi wa mijini na wakulima wa vijijini wameweka bayana rekodi ya imani yao kwa sera na utekelezaji wa Chama Cha Mapinduzi. Tumepoteza dira ya Chama? Hapana!!

Jana tulipokea na kujadili Taarifa za Chama na Serikali zake. Maudhui ya taarifa hizo yametoa ushahidi tosha kwamba Chama chetu ni madhubuti na viongozi wa serikali zake wana upeo mkubwa wa utekelezaji. Wanaotaka uthibitisho zaidi kwamba hatukulegeza kamba au kupoteza dira ya Chama, nawaomba wapitie tena Ilani ya Uchaguzi wa mwaka jana ya Chama Chetu. Ilani hiyo inashinda zile za vyama vingine vyote vilivyoshiriki katika uchaguzi. Ina tathmini kamili ya hali halisi ya nchi na dunia katika nyanja mbali mbali, na hasa hasa kisiasa na kiuchumi. Imeainisha kwa kina malengo ya maendeleo ya miaka mitano ijayo na mikakati ya kuyafikia.. Ni ilani ya pekee ambayo maandalizi yake yalishirikisha kikamilifu wabia wote wa maendelo ya nchi na makundi makubwa yote ya jamii. Ye yote anayefanya mapitio ya ilani hiyo atazinduka na kukiri kwamba, kwa kigezo cha ushupavu, umakini, umahiri na uadilifu katika kuyakabili matatizo ya maendeleo ya nchi, CCM ndicho chama kinachoweza kutoa timu thabiti na murua ya kuongoza nchi!! Kilichobaki kwangu ni kurejea na kusisitiza kauli mbiu ya Ilani hiyo kama ilivyo katika Ibara ya 9, uk 9 wa Ilani hiyo: Twendeni basi tukaendeleze kazi ya kukuza uchumi na kupambana na umaskini kwa “ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya”!!

 

Ilani imezingatia Dira ya Taifa

Ndugu Wajumbe,

Narudia. Hatukupoteza dira. Tukumbushane. Tulipokaribia kuanza karne ya 21, tuliona umuhimu wa kutafakari changamoto la maendeleo katika karne mpya. Matokeo ya tafakuri hiyo ni Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025. Nawaomba wajumbe muipitie tena dira hiyo. Mkifanya hivyo mtaona kwamba katika hoja ya Utaifa na maendeleo ya watu wake hatujapoteza mwelekeo wala kulegeza kamba.

Dira ya Maendeleo imetutahadharisha  kuwa karne hii itakuwa ya ushindani mkali, na itatawaliwa na wale wenye uwezo mkubwa kiteknolojia, tija kubwa katika uzalishaji, miundombinu imara na ya kisasa ya mawasiliano na uchukuzi na, zaidi ya yote, nguvu kazi yenye ustadi mkubwa na hulka ya kujituma. Inabainisha jinsi ya kuamsha, kuunganisha na kuelekeza juhudi na fikra zetu na raslimali za Taifa letu katika maeneo ya msingi ili kufikia malengo ya maendeleo yaliyoainishwa na kustahimili ushindani huo mkubwa.

 

Tulipoiandaa, tulishirikisha na kupata maoni na ridhaa ya wananchi wengi, kutoka sehemu zote za jamii:- waheshimiwa Wabunge, vyama vyote vya siasa, viongozi wa madhehebu mbali mbali ya dini, jumuiya za akina mama na vijana, vyama vya wafanyabiashara na wenye viwanda, wakulima, wasomi, watu mashuhuri katika historia ya nchi yetu na wananchi wa kawaida. Dira inaelewesha vyema tulikotoka, tulipo na kule tuendako. Inaelezea sifa za nchi yetu zinazotarajiwa kuwepo ifikapo mwaka 2025 ikiwa ni pamoja na wananchi kuwa na maisha bora na mazuri; amani utulivu na umoja; utawala na uongozi bora; jamii iliyoelimika na inayojituma katika masuala ya maendeleo; na uchumi wenye uwezo wa ushindani na wenye ukuaji wa kudumu kwa maslahi ya watu wote.

Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu imezingatia vyema Dira ya Taifa ya Maendeleo na hivyo kudhihirisha vilivyo kwamba CCM imebeba vizuri mamlaka ya kuwa Chama Tawala!! Chama gani kama CCM? Hakuna!!!

 

Kujitegemea:  Nyenzo Kuu ya Maendeleo

Ndugu Wajumbe,

Narudia. Hatukupoteza dira ya Chama chetu. Nguzo Kuu ya falsafa yetu ya maendeleo ni Kujitegemea. Baba wa Taifa alituasa: Uhuru na Kazi, na baadaye Uhuru ni Kazi! Ubora wa sera zetu za uchumi na maendeleo ya jamii ulikuwa na mvuto mkubwa kwa mataifa wahisani miaka ya 60 na 70. Matatizo ya uchumi wa dunia yaliyofuatia, hususan kupaa kwa bei ya mafuta na kuporomoka kwa bei ya mazao tunayouza nje ya nchi, kuliongezea utegemezi kwa wahisani. Lakini wakati wote shabaha yetu imekuwa  ile ile – Kujitegemea na kupunguza hisani ya utegemezi. Miaka hii 10 tumejitahidi kupunguza hisani hiyo katika bajeti ya Serikali, ikapungua toka 48% mpaka 42%. Serikali ya Awamu ya Nne imeanza kwa kuamua kupunguza hisani hiyo kwa 3% zaidi katika bajeti mpya. Ndugu Rais na Serikali yako tunawapongeza sana. Kwani kwa mujibu wa falsafa ya maendeleo yetu, ukweli unabaki pale pale: Mtaji wa maskini ni nguvu zake mwenyewe!  

            Ninaposema haya sina maana ya kupuuza mchango wa wahisani wa kimataifa kwa maendeleo yetu.  Sitaki kuwa mchoyo wa shukurani.  Nashukuru sana kwa hisani tuliyopata ya kufutiwa madeni na kuongezewa misaada katika miaka ya karibuni.  Na ninaendelea kujenga hoja katika kamisheni kadhaa za kimataifa, hoja ya mataifa kama letu kufutiwa madeni kabisa, kuongezewa misaada, na kuandaliwa mfumo wa biashara wa kimataifa utakaozipa bidhaa za nchi zao thamani na bei za haki zaidi.  Maana ni vizuri pia kuipa hisani hii tafsiri ya kiwango halisi cha matokeo yake.

            Nitoe mfano.  Kwenye mkutano wa viongozi wa nchi tajiri na kubwa nane duaniani kule Gleneagles, Scotland, mwaka jana, waliahidi kuiongeza misaada kwa $21 bilioni, sawa na 37%.  Lakini utafiti wa Shirika lisilo la Kiserikali la Oxfam umeonyesha kwamba sehemu kubwa ya fedha ilitumika kufutia madeni, na kwamba ongezeko halisi la misaada yao lilikuwa asilimia 9 tu (9%)!  Na mtaalamu mmoja wa Benki ya Dunia ameeleza kuwa, kwa wastani, asilimia 70 (70%) ya misaada inatumika katika nchi inayotoa misaada, kulipia ushauri na wataalamu!!  Mtaji wa maskini kweli ni nguvu zake mwenyewe.

            Ndugu Wajumbe na Watanzania kwa ujumla.  Kwa miaka kadhaa tumekuwa tunatumia kauli mbiu ya kuwa ili nchi iendelee inahitaji mambo manne:

                                                                                               

(a)                Watu

(b)               Ardhi

(c)                Siasa Safi, na

(d)               Uongozi bora

 

Kutokana na mabadiliko na mfumo wa uchumi duniani ulivyo sasa hatuna budi kusisitiza kuwa pia tunahitaji “mitaji” (mtaji) kama nyenzo ya tano kubwa ya msingi wa kuleta maendeleo.  Mitaji hiyo itatokana na tabia ya kujiwekea akiba, kubana matumizi yasiyo ya lazima na kukusanya na kuboresha raslimali zetu zote ili zituwezeshe kujikimu na kumiliki uchumi wetu kwa njia ya kuanzisha, kuendeleza na kuboresha biashara, uzalishaji na kurutubisha mazingira ya ujasirimali.

 

Hayo yatatuwezesha kuwa na wimbi la baadaye la Watanzania tunaoendesha na kumiliki uchumi wetu kwa mitaji yetu wenyewe.  Nilipofunga majadiliano ya Taarifa za Chama na Serikali niligusia kikao kilichopitisha mpango wa Utekelezaji wa Ilani wa Kata ya Malindi, Lushoto, katika miaka 5 ijayo.  Lengo lililonivutia sana miongoni mwa mengi, ni uamuzi wao wa kuanzisha SACCOS ya Kata.  Kwa hakika mtaji wa maskini ni nguvu na akili zake mwenyewe.

                                                                       

Mshikamano na Vyama Rafiki

Ndugu Wajumbe,

            Nimekumbusha kwamba Chama chetu kiliundwa kwa matarajio kuwa kitakuwa “kiungo kati ya wanamapinduzi wa Tanzania na wanamapinduzi wenzetu kokote waliko”.  Dira hii ya Chama nayo hatukuipoteza.  Wengi wenu mmeshuhudia jinsi wawakilishi wa vyama mbali mbali rafiki toka ndani na nje ya bara letu, walivyohudhuria mikutano mikuu yetu yote.  Tumeshirikiana na vyama rafiki kwa kufanya ziara zilizowezesha kubadilishana ujuzi na uzoefu wa kuimarisha vyama, kushinda chaguzi na kufunza makada.  Na kwa namna ya pekee tumeimarisha uhusiano wetu na vyama vya Ukombozi wa Jumuiya ya SADC, warithi wa vyama vilivyopigania uhuru wa nchi za Kusini mwa Afrika.  Hatuna budi tuushupalie ushirikiano huu, kwani Utandawazi si mtihani wa Kiuchumi tu; unaelekea pia kuwa mtihani wa kisiasa unaotishia uhuru na umoja wa nchi hizo.

 

            Ndugu Rais Kikwete umeamua kuvalia njuga mradi wa Uandishi wa kuweka kumbukumbu sahihi historia ya ukombozi wa nchi zetu hizi za SADC na kuuongezea kasi yake kwa hali na mali.  Mradi wa Utunzaji wa Kumbukumbuza Harakati za Ukombizi (Liberation Heritage Project) ni mojawapo ya nyenzo muhimu kwa maendeleo yetu.  Nakupongeza sana sana.  Ni vema kabisa kwamba historia ya ukombozi wetu iandikwe na sisi wenyewe badala ya kutegemea historia iliyo kasuku wa waliotutawala.

 

 

 

Muungano wa Tanzania

Ndugu Wajumbe,

            Kielelezo kikubwa cha Uhai wa Chama chetu ni Uendelevu wa Muungano wetu.  Muungano wa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, uliasisiwa na vyama vya TANU na ASP, ambavyo baadaye vikaamua kuungana na kuunda Chama Cha Mapidnuzi.  Ni dhahiri basi kuwa ustawi wa Muungano ni pima-joto ya uhai wa CCM.  Nawashukuru WanaCCM kwa ari yenu kubwa ya kudumisha Muungano na kustawisha wananchi wake.

            Kama Ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka jana ilivyobainisha:  “Ushirikiano baina ya pande mbili za Muungano umekuwa ukikua na maelewano baina ya serikali mbili na hasa ya wananchi yanaimarika kila kukicha.  Ushirikiano wa kiuchumi na kijamii umeanza kuimarika na mfano mzuri wa ushriikiano huo umedhihirika katika utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Jamhuri, Bara na Zanzibar”.

            Hapana shaka kwamba katika mchakato wa ushirikiano kuna kero kadhaa.  Napongeza kwa dhati ari na kasi mpya ambayo kwayo Serikali zetu sasa zimewania kushughulikia kero hizo.  Rai yangu ni kwamba wakati huo huo tusichoke kuelezea, kutetea na kushangilia mafanikio ya Muungano.  Mimi naamini kuwa katika mizani ya maendeleo ya Muungano, mafanikio yanazidi kero zake.

 

Tumsaidie Rais na Mwenyekiti Mpya

Ndugu Wajumbe,

Kwa usahihi mkubwa, Rais wetu, Ndugu Kikwete, amefananisha mtiririko wa kumpata kiongozi wa mbio za kijiti. Naamini kwa dhati kwamba huu ni wakati muafaka wa kumkabidhi yeye kijiti cha uongozi wa Chama chetu. Katika chama chetu, kijiti hiki ni Mwenge. Naamini pia kwamba niliupokea mwenge huo ukiwaka; sikuuzima; na ninaukabidhi ukiwaka.

 

Ndugu Wajumbe:

            Ombi langu kwenu leo ni kuwa tumsaidie sana Rais wetu ambaye sasa atakuwa pia Mwenyekiti wetu wa CCM. Anayo kazi kubwa sana tunayomtwisha. Tusikae pembeni na kumtazama. Tuwe naye bega kwa bega katika kuimarisha Chama na kutekeleza sera na Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu. Nguvu yake ni sisi, tukimwacha pekee tutakuwa tunahujumu juhudi zake na Chama chetu. Na tusimtwishe mno matarajio yetu binafsi kwa uongozi wake. Nasema hivyo kwa uzoefu wangu, na kwa vile ni jambo la kawaida kwa binadamu kuwa na mategemeo fulani wakati yanapotokea mabadiliko ya uongozi.  Yapo matarajio ya ngazi ya mtu binafsi. Yapo pia matarajio ya Chama, na yale ya wananchi wengine na Taifa kwa jumla.  Si rahisi kwa kiongozi kukidhi matarajio binafsi ya kila mwanachama au kila kiongozi mwingine. Ahadi niliyotoa mimi mliponichagua Mwenyekiti na ambayo natarajia ndiyo atakayoitoa Rais kwenu leo ni kuwa atatumia uwezo wake wote kutimiza matarajio ya Chama na ya Taifa.

 

Shukrani

Ndugu Wajumbe:

            Naomba nimalizie kwa kurudia kutoa shukrani. Miaka kumi iliyopita hapa Chimwaga mlinichagua kuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi. Leo, baada ya haya niliyoyasema, sina la kuongeza ila kutoa shukrani zangu za dhati kwa heshima kubwa mliyonipa, na kwa ushirikiano mlionipa katika miaka hiyo kumi iliyopita. Kwa msaada wenu nimefanya nilichoweza kwa bidii zangu zote, na leo nakabidhi kijiti kwa mkimbiaji mwingine wa CCM. Kama mlivyonisaidia naomba ninyi na mimi tumsaidie na kushirikiana naye kwa upendo na kwa moyo mmoja.

            Nawashukuru waasisi wa Chama chetu kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuanzisha TANU na ASP, na hatimaye kuviunganisha na kuanzisha CCM. Leo sisi tunasimama juu ya mabega yao, na tunajenga juu ya msingi imara walioujenga.

            Namshukuru sana Mwenyekiti aliyenitangulia, Mzee wetu Ali Hassan Mwinyi kwa busara zake na kwa upendo wake kwangu. Namshukuru kwa kuniachia Uenyekiti wa CCM mwaka 1996 kabla ya muda wake kikatiba kwisha. Namshukuru kwa kunisaidia katika uongozi wangu. Sasa nami niko tayari kuungana naye katika kumpenda na kumsaidia Mwenyekiti wetu mpya tukiwa wastaafu.

            Nawashukuru sana Makamu Wenyeviti niliofanya kazi nao, Mheshimiwa Dkt Salmin Amour, Mheshimiwa Dkt John Samwel Malecela na Mheshimiwa Rais Amani Abeid Karume. Walinisaidia sana na tulifanya kazi za Chama pamoja kwa maelewano na ushirikiano mkubwa. Ahsanteni sana.

            Mheshimiwa Dkt. Salmin, maarufu kama “Komandoo”, ukomandoo wako daima umesisimua fikra juu ya saa zetu za ukombozi, ustawi wa jamii na utawala wa haki na hivyo kuhuisha mustakabali wa Taifa.  Nakushukuru sana.

            Katika ushindani wa siasa ndani na nje ya Chama, hapakosi kuwa na mashambulio, na mara kadhaa yamemlenga Dkt. John Malecela.  Licha ya mashambulio hayo, mara ya moto, mara ya baridi, mara ya uzushi, daima amedhihirisha msimamo thabiti na mkali, wa MUUMINI WA CCM.  Nakushukuru sana.

            Nawashukuru viongozi wengine waasisi na wastaafu walionisaidia sana, kwa hekima na busara, akiwemo Mzee wetu Rashidi Mfaume Kawawa.  Pamoja na umri wake Mkubwa na matatizo ya afya, Mzee Kawawa hakukosa vikao vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu, na hakusita kutoa ushauri kwa uaminifu na uwazi.  Nakushukuru sana.

Aidha nawashukuru Mawaziri Wakuu wastaafu, akiwemo Mzee Cleopa David Msuya, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba na Dkt. Salim Ahmed Salim na Waziri Mkuu wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa F. T. Sumaye.  

Waziri Mkuu Sumaye ndio aliyeshika kamandi ya askari wa miavuli wa Serikali ya Awamu ya Tatu.  Amefanya kazi nami kwa uaminifu na kwa taadhima kubwa kwa Chama.  Nakushukuru sana.

Wote hawa na wengine wanaendelea kuwa hazina kubwa ya Chama Cha Mapinduzi.  Nawashukuru wote niliofanya nao kazi kwenye Kamati  Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa kwa msaada wao na ushirikiano mkubwa. Naomba kila mmoja ajue kuwa natambua mchango wake na ajisikie kuwa nimemshukuru sana.

            Nawashukuru Makatibu Wakuu wa CCM, Dkt Lawrence Gama na Philip Mangula, pamoja na Sekretarieti walizoziongoza katika miaka kumi iliyopita.

            Nawashukuru wana-CCM wote kuanzia Wenyeviti wa Mikoa, Wenyeviti wa Wilaya, Makatibu wao na watendaji wote wa Chama.

            Nawashukuru kwa njia ya pekee wananchi wa Dodoma. Siku zote nilijisikia nipo nyumbani kila nilipokuja hapa, kwa vile ambavyo wamekuwa wananipokea mimi na wajumbe wote wa mikutano ya Chama kwa upendo mkubwa. Ahsanteni sana. Na katika shukrani hizo, zipo pia maalumu kwa wanakijiji wa Chamwino walionipokea kama mwana-kijiji mwenzao kwa miaka kumi, na kunionyesha upendo na ukarimu mkubwa sana.

Ndugu Wajumbe:

            Ipo methali ya Wahabeshi inayosema, “Usimlaumu Mungu kwa kuumba chui. Mshukuru kwamba hakumuumba chui mwenye mbawa.”

Nami ninapotazama nyuma katika miaka kumi iliyopita yapo mambo ambayo ningeshukuru kama Mwenyezi Mungu angetuepusha nayo. Lakini namshukuru sana kwamba hakututwisha mzigo uliotushinda kwa umoja wetu. Ninapoagana nanyi namwomba kuwa katika kipindi cha uongozi wa Serikali na Chama tunaomkabidhi ndugu yetu Jakaya Mrisho Kikwete yasitokee yatakayomshinda yeye akishirikiana nasi. Naamini kwa rehema zake hivyo ndivyo itakavyokuwa, na CCM itadumu, na itazidi kutoa uongozi bora kwa nchi yetu na watu wake daima.

Wachangiaji wote katika mjadala wa jana wamenimwagia sifa kwa maendeleo ya miaka 10 hii.  Wengi wamediriki kusema mafanikio ya Uongozi wangu.  Ndugu Wajumbe, nawasihi mzingatie ukweli huu.  Mafanikio hayo ni mafanikio ya Uongozi wa pamoja.  Mafanikio hayo ni matokeo ya utekelezaji.  Na zaidi ya yote, mafanikio hayo ni matunda ya KAZI YA CHAMA!!

Kuna msanii mmoja maarufu ambaye daima alikuwa anatamba na kuona fahari kwa kuwa hakuwa mwanasiasa.  Alipoulizwa kwa nini aliona fahari hiyo, alijibu ni kwa sababu asingeweze kuhimili mzigo wa kuwa sahihi wakati wote.  Nilipokabidhiwa madaraka nilisema ningaliongozwa na hoja ya Uwazi na Ukweli.  Najua sikuwa sahihi wakati wote.  Wapo ambao niliwakosea; nawaomba radhi.  Wapo ambao sikutimiza matarajio yao; nao pia nawaomba radhi.  Lakini kwa wote nathubutu kusema: nimefanya bidii yangu yote kuingoza nchi kwa haki.  Sasa namaliza ngwe yangu.  Nimeitunza Imani ya Chama.  Nashukuru kwa zawadi nyingi toka mikoani mlizotupa mimi na Mama Mkapa.  Katika maisha yetu yaliyobaki tutazihesabu zawadi hizo kama tuzo kwa maisha ya Utumishi na Uadilifu.

 

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI!!

MAPINDUZI DAIMA           

Ahsanteni kwa kunisikiliza.